Winamp Logo
Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu Cover
Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu Profile

Habari za UN - Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu

Swahili, News, 1 season, 603 episodes, 17 hours, 5 minutes
About
Mtazamo wa Kimataifa Habari za kiutu
Episode Artwork

Muunganisho wa kijamii huondoa upweke na kuboresha afya kwa jamii – WHO

Mwezi Novemba mwaka jana shirika la Umoja wa Mataifa la Afya duniani, WHO lilizindua Kamisheni  ya kuchochea Muunganisho wa Kijamii au Social Connection kwa lengo la kuondokana na tatizo la upweke ambalo limetambuliwa kuwa moja ya tishio kubwa la afya duniani. WHO inasema kutengwa na jamii na kuishi maisha ya upweke ni jambo hatari, chungu, na zaidi hatari kwa afya ya binadamu. Upweke  unaweza kuathiri mtu yeyote, wa hali yeyote mahali popote. Kamisheni hiyo sasa kupitia video za Muunganisho wa Kijamii hufikia watu kote ulimwenguni wanaoishi pekee yao lengo kuu likiwa ni kuwapatanisha na kuwashirikisha na jamii pamoja na marafiki ili waondokane na msongo wa mawazo na kuboresha afya yao. Tayari msusururu wa video hizo umeanza kuchapishwa mitandaoni ambapo Selina Jerobon wa Idhaa hii amefuatilia simulizi ya Maria Ondosia Mawero, mama mzee anayeishi katika eneo la mabanda la Kibera jijini Nairobi, nchini Kenya akitueleza ni kwa nini uhusiano wa kijamii ni muhimu kwa afya yetu, ustawi na ubinadamu wetu.
2/2/20244 minutes, 6 seconds
Episode Artwork

Hakikisha usalama zaidi ili wahudumu wa kibinadamu waweze kusambaza chakula Sudan - WFP

Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP limezitaka pande zinazohasimiana nchini Sudan kutoa hakikisho zaidi la usalama kwa shirika hilo ili liweze kusambaza msaada wa chakula kwa wananchi waliokimbia makazi yao na waliokwama katikati ya mapigano ili kuwanusuru watu hao kutokufa njaa. Akizungumza na waandishi wa habari kwa njia ya mtandao huko Geneva Uswisi, Msemaji wa WFP nchini Sudan, Leonie Kinsley amesema hali ya chakula nchini humo ni mbaya sana, licha ya juhudi zinazofanywa na shirika lao kutoa Msaada kwa watu milioni 6.5,  bado watu milioni 18 wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula.Kinsley amesema “WFP kwa sasa ina uwezo wa kutoa msaada wa haraka wa chakula kwa mtu mmoja kati ya 10 ambao wanakabiliwa na hali ya dharura ya njaa nchini Sudan. Ikimaanisha asilimia 90 ya watu ambao ni wenye njaa zaidi hawapati msaada.”Maeneo yaliyoathirika zaidi ni Khartoum, Darfur and Kordofan na sasa jimbo la Jazeera, ambako mzozo ulisambaa mwezi Desemba mwaka jana.WFP imeeleza kuwa chakula kipo nchini humo lakini inawawia vigumu kukisambaza na wanakabiliwa na changamoto lukuki ikiwemo kuporwa kwa chakula katika ghala lao la chakula huko jimboni Jazeera.“Ili Msaada uweze kuwafikia wananchi, misafara ya misaada ya kibinadamu lazima iruhusiwe kuvuka katika eneo lenye mapigano. Hata hivyo imekuwa vigumu hilo kufanyika kutokana na vitisho vya usalama, mapigano yanayoendelea na kulazimishwa kuwekewa vizuizi barabarani wakidai ada na ushuru. Hali nchini Sudan leo ni janga. Mamilioni ya watu wameathiriwa na mzozo huo.”Angalau juhudi za WFP kusaka hakikisho la usalama ili kusambaza chakula zimezaa matunda wiki iliyopita, na sasa usambazaji wa misaada unaendelea huko Kassala, Gadhafi na jimbo la Blue Nile.Hata hivyo malori mengine 31 ya WFP, ambayo yalipaswa kupeleka misaada ya mara kwa mara huko Kordofan na White Madani, yameegeshwa tupu yakishindwa kuondoka.Hata hivyo malori mengine 31 ya WFP, ambayo yalipaswa kupeleka misaada ya mara kwa mara huko Kordofan na White Madani, yameegeshwa tupu yakishindwa kuondoka. 
2/2/20242 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

02 FEBRUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia mizozo nchini Sudan, na uvutaji wa cigara. Makala inatupeleka nchini Kenya kumulika madhara ya upweke na programu ya Muunganisho wa Kijamii inayosaidia watu kuondokana na upweke. Mashinani tunakuletea ujumbe kuhusu saratani. Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP limezitaka pande zinazo hasimiana nchini Sudan kutoa hakikisho la usalama kwa shirika hilo ili liweze kusambaza msaada wa chakula kwa wananchi waliokimbia makazi yao na waliokwama katikati ya mapigano ili kuwanusuru watu hao kutokufa njaa. Nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, simulizi ya mtu aliyeanza kuvuta sigara akiwa kijana balehe na sasa ameamua kuacha inamulika ni kwa nini shirika la Umoja wa Mataifa la afya duniani, WHO linasisitiza umuhimu wa kampeni za kuacha tumbaku kwani ni miongoni mwa visababishi vikubwa vya maambukizi ya saratani ya mapafu inayooongoza kwa kuua zaidi vifo miongoni mwa wanaume duniani. Makala inaangazia madhara ya upweke, na tunakutana na mama mzee ambaye ameishi pekee yake kwa muda mrefu katika eneo la mabanda la Kibera jijini Nairobi, Kenya, lakini programu ya Muunganisho wa Kijamii (Social Connection) unaofanikishwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO imemuondolewa upweke.Mashinani tunaelekea mkoani Mwanza kaskazini magharibi mwa Tanzania, kusikia ujumbe wa matibabu ya saratari ya shingo ya kizazi.      Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
2/2/202411 minutes, 27 seconds
Episode Artwork

Acheni sigara haina maana - Thierry

Nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, simulizi ya mtu aliyeanza kuvuta sigara akiwa kijana balehe na sasa ameamua kuacha inamulika ni kwa nini shirika la Umoja wa Mataifa la afya duniani, WHO linasisitiza umuhimu wa kampeni za kuacha tumbaku kwani ni miongoni mwa visababishi vikubwa vya maambukizi ya saratani ya mapafu inayooongoza kwa kuua zaidi vifo miongoni mwa wanaume duniani. WHO inasema katika ukanda wa  Afrika kuna wavuta sigara milioni 73, na kijana balehe 1 kati ya 10 anavuta sigara. Thierry Anatole kutoka Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR sasa mtu mzima alikuwa miongoni mwa takwimu hizo.Anasema “nilivuta sigara kwa miaka 30. Nilianza miaka ya 1980 na nilikuwa na umri wa kati ya miaka 11 na 12. Kwa siku nilikuwa navuta pakiti 4.”Kwa mujibu wa WHO, nusu ya watu wanaotumia tumbaku, hufariki dunia. Na Tumbaku husababisha aina lukuki za saratani ikiwemo ya mapafu na njia ya hewa.“Unaweza kuwa na kikohozi mfululizo kwa miezi mitatu, anaendelea Thierry watu wanaweza kukosea na kudhania ni Kifua Kikuu, kumbe ni kikohozi sugu. Na madhara yake ni makubwa.”Thierry akaendelea kuelezea madhara ya uvutaji kiuchumi akisema “hata wakati wa ukata, huwezi kuacha kuvuta sigara. Hata kama ni fedha ya kununulia dawa, unanunulia sigara.”Sasa Thierry yuko uwanjani anafanya mazoezi kwani miaka 7 iliyopita aliamua kuacha kuvuta sigara. Ari ya kulinda watoto wake dhidi ya moshi wa sigara ikaongezeka, “Nilikuwa ninawaumiza bila kutambua.”WHO inasema moshi kutoka kwa mvutaji sigara husababisha vifo vya zaidi ya watu milioni 1 kila mwaka kwani huathiri afya ya walio karibu nae.Hapo ndipo akili ilinirudia na kuanzia Aprili 2016 hadi leo sijavuta tena sigara. Nimetoka kwenye kifungo cha sigara, Niko huru! Sasa niña fedha kwenye mifuko yangu. Ninaweza kufanya michezo, nakimbia, na ninapumua vizuri.”Thierry akatamatisha na ujumbe.“Kwa wavutaji, na wanaotaka kuvuta, kwa waanzao na wanaovuta mara moja moja, wasikilize sauti ndani ya roho yao inayosema acha kuvuta sigara, usisubiri hadi ukachelewa kwani uvutaji unaua kila siku.”
2/2/20242 minutes, 26 seconds
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili: Ufafanuzi wa neno “MITONGO.”

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii lleo fursa ni yake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “MITONGO.”         
2/1/20241 minute
Episode Artwork

01 FEBRUARI 2024

Hii leo jaridani tumekuandalia mada kwa kina ambayo  leo inatupeleka katika kijijini Lokujo wilayani Koboko Kusini mwa Uganda kusikia simulizi ya mnufaika wa msaada wa mafunzo, fecda, na pembejeo wa WFP, Pia tunakuletea habari kwa ufipi na uchambuzi wa methali.Kufuatia uamuzi wa nchi 16 wafadhili kusitisha utoaji fedha kwa shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia wakimbizi wa kipalestina UNRWA baada ya Israel kulishutumu shirika hilo kuwa wafanyakazi wake 12 walihusika katika shambulio lililotokea tarehe 7 Oktoba mwaka jana, Mkuu wa UNRWA Philipe Lazzarini amesema kuwa iwapo fedha zitaendelea kuzuiliwa, watalazimika kufunga operesheni zao ifikapo mwishoni mwa mwezi huu wa Februari.     Wataalamu wa Haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa wameeleza kusitikishwa na kulaani vitendo vya waandishi wa habari kuuawa, kushambuliwa, kujeruhiwa na kuwekwa vizuizini huko katika eneo la palestina linalokaliwa kwa mabavu na kutoa wito kwa pande zote kwenye mzozo kuhakikisha wanalinda waandishi wa habari.Tumalizie na masuala ya afya ambapo Shirika la kimataifa la utafiti wa saratani, IARC ambalo ni shirika tanzu la WHO hii leo limetangaza matokeo ya utafiti wake uliofanyika katika nchi 115 wakiangazia mzigo wa kimataifa wa saratani ambapo wamebaini kuwa nchi nyingi hazitoi kipaumbele na kufadhili ipasavyo huduma za matibabu ya saratani kama sehemu ya mpango wa afya kwa wote.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii lleo fursa ni yake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “MITONGO.”          Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
2/1/202411 minutes, 39 seconds
Episode Artwork

Mwanafunzi Msumbiji: Iwe mvua iwe upepo mkali madarasa yetu ni salama

Kila mwaka, Msumbiji hukabiliwa na matukio ya hali mbaya za hewa kupindukia kama vile vimbunga na mafuriko, matukio ambayo husababisha uharibifu wa shule na hatimaye watoto kushindwa kujifunza. Hata hivyo, ujenzi wa madarasa yanayohimili matukio kama vile pepo kali na mafuriko umeleta nuru na matumiani kwa watoto, wazazi na walimu. Madarasa haya yanawezesha watoto kubakia salama hata wakati wa mvua na upepo mkali. Hali hii ni uwekezaji wa kudumu kwani ni  hakikisho kwa watoto kuendelea kupata elimu na mustakabali wao kuwa bora. Selina Jerobon wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anamulika ni kwa vipi hilo limefanyika kupitia mradi uliofadhiliwa na Benki ya Dunia.
1/31/20244 minutes, 11 seconds
Episode Artwork

Kamishna Mkuu wa UNHCR akiwa ziarani Ethiopia anasihi wasisahaulike wanaoikimbia Sudan

Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), Filippo Grandi akihitimisha ziara ya siku tatu nchini Ethiopia ametoa wito kwa ulimwengu kuwasaidia watu wa Sudan wanaoikimbia nchi yao na kuingia Ethiopia ambayo ni moja ya nchi wenyeji wa wakimbizi na wakimbizi wa ndani wengi zaidi ulimwenguni. “Kuna majanga mengine kote duniani. Mengine makali zaidi na mengine yanaongelewa zaidi. Tusiwasahau watu ambao nimezungumza nao waliokimbia vita Sudan. Hawa wanateseka kila siku na wanahitaji msaada.”Grandi amesafiri hadi magharibi mwa Ethiopia katika mji wa Assosa, ambao ni mji mkuu wa eneo la Benishangul-Gumuz karibu na mpaka wa Sudan, ambako amekutana na baadhi ya wakimbizi na waomba hifadhi zaidi ya 20,000 waliopo katika kituo cha usafiri cha Kurmuk.“Waafrika kamwe hawatupani, wanashikana mkono na ni watu wakarimu kwa walio katika madhila. Hili ni ombi pia kwa jumuiya ya kimataifa. Nchi zote hizo ikiwemo Ethiopia sio nchi tajiri, sio nchi zenye raslimali nyingi, zinahitaji usaidizi wa kimataifa, zinahitaji kugawana uzito wa mzigo na isivyo bahati janga la wakimbizi wa Sudan, janga la kufurushwa, janga la kibinadamu ni moja ya majanga yenye ufadhili mdogo zaidi duniani leo.”
1/31/20241 minute, 31 seconds
Episode Artwork

31 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunafuatilia ziara ya Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), Filippo Grandi nchini Ethiopia na wakimbizi wa ndani nchini Sudan. Makala tunakupeleka nchini Msumbiji na mashinani nchini Kenya. Kulikoni?Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR), Filippo Grandi akihitimisha ziara ya siku tatu nchini Ethiopia ametoa wito kwa ulimwengu kuwasaidia watu wa Sudan wanaoikimbia nchi yao na kuingia Ethiopia ambayo ni moja ya nchi wenyeji wa wakimbizi na wakimbizi wa ndani wengi zaidi ulimwenguni. Islam Mubarak, msichana mwenye umri wa miaka 21 ambaye vita mpya iliyozuka Sudan Aprili mwaka jana ilimlazimisha kufungasha virago na familia yake na kuukimbia mji mkuu Khartoum na sasa amekwama katika kambi ya wakimbizi wa ndani katika jimbo la El-Gedarif, lakini ndoto yake ni kurejea nyumbani siku moja.Makala tunakwenda nchini Msumbiji ambako Selina Jerobon wa Idhaa hii anamulika kabla na baada ya ujenzi wa madarasa yanayohimili hali mbaya za hewa ikiwemo vimbunga vinavyong’oa mapaa.Mashinani tutaelekea katika kambi ya wakimbizi ya Kakuma, Kaunti ya Turkana, nchini Kenya kusikia ni kwa jinsi gani wazazi wenye ujuzi Chanya wa malezi wanapewa Usaidizi wa Kisaikolojia ili kuwapa watoto msingi muhimu katika ukuaji wao.      Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
1/31/202411 minutes, 18 seconds
Episode Artwork

Simulizi ya Islam Mubarak: Ndoto yangu ni kurejea nyumbani na kuishi kwa amani

Kutana na Islam Mubarak msichana mwenye umri wa miaka 21 ambaye vita mpya iliyozuka Sudan Aprili mwaka jana ilimlazimisha kufungasha virago na familia yake na kuukimbia mji mkuu Khartoum na sasa amekwama katika kambi ya wakimbizi wa ndani katika jimbo la El-Gedarif, lakini ndoto yake ni kurejea nyumbani siku moja.Katika kambi ya wakimbizi wa ndani inayosimamiwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR ni Islam akiwa amekata tamaa kwa kutouona au kuelezea mustakbali wake .Kabla ya kuzuka mapigano na kukimbia Khartoum Islam alikuwa akisomemea masuala ya fasihi ya Kiingereza, kisha maisha yake yakapinduliwa na ndoto yake kubadilika,“Kama ungeniuliza hapo awali ningekueleza mustakbali wangu utakuwaje , ningemaliza masomo na kisha kwenda zangu Korea Kusini kukutana na kundi la muziki wa pop la BTS, lakini sasa siwezi kusema hivyo.”Kama mmoja wa mashambiki wakubwa Islam anapata faraja kupitia muziki wa kundi maarufu la BTS na kwa kusoma taarifa zao.“Niliingia kwenye Google nikarambaza na kusoma kuhusu maisha yao na ninaweza kulinganisha na maisha yangu kwa kiasi fulani, kwani walipitia changamoto kubwa kabla ya kuwa maarufu. Wanatoka Korea Kusini na walijisukuma sana kujifunza kuongea Kiingereza na hilo ndilo linaloniunganisha mimi na wao.”Kwa mujibu wa UNHCR Islam ni miongoni mwa Wasudan zaidi ya milioni 7 waliofurushwa makwao hadi sasa na kulazimika kuwa wakimbizi ndani ya Sudan na katika nchi jirani na vita bado inaendelea. Islam anasema kambini maisha magumu.“Hali hapa ni ngumu sana kwa wakimbizi wa ndani, ni vigumu kuielezea mtu anahitaji kuishi hapa na kuishuhudia , sijui cha kusema.”Hata hivyo Islam ana matumaini kwamba vita itakwisha hivi karibuni ili akaendelee na masomo na kutimiza ndoto yake.“Maisha yetu Khartoum yalikuwa mazuri, nahisi mambo yatakuwa bora kwangu, hivyo hakuna shida kusubiri kidogo kabla ya kurejea Khartoum “Na hilo ndilo UNHCR inalitaka kwa wakimbizo wote kutoka Sudan kama Islam.
1/31/20242 minutes, 30 seconds
Episode Artwork

30 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na inatupeleka kwa wataalam wa afya katika mataifa mbalimbali ikiwemo Tanzania ambao wamekuwa wakitoa elimu ya ugonjwa huo katika jamii na kuhamasisha wanawake kujitokeza katika vituo vya afya vinavyotoa huduma hiyo ili kupima afya zao ili wafahamu iwapo wameambukizwa ugonjwa huo au la. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na sauti za mashinani.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres anakutana na wafadhili wakuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA ili kuwafahamisha jinsi Umoja wa Mataifa unavyoshughulikia madai ya hivi karibuni dhidi ya UNRWA kuhusika katika mashambulizi ya Oktoba 7 mwaka jana Kusini mwa Israel na pia kuwasihi kuendelea kufadhili misaada ya kibinadamu ya shirika hilo. Leo ni siku ni siku ya magonjwa ya kitropiki yaliyopuuzwa duniani. Katika ujumbe wake wa siku hii Mkurugenzi mkuu wa shirika la afya duniani WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus amesema “Magonjwa ya kitropic yaliyopuuzwa au NTDs yanaathiri zaidi ya watu bilioni moja duniani kote hususani katika jamii masikini na zilizotengwa, lakini magonjwa ya NTDs yanazuilika na mara nyingi yanaweza kutokomezwa kabisa katika nchi.Na Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk leo mjini Geneva Uswisi ametoa ombi la dola milioni 500 kufadhili shughuli za ofisi hiyo kwa mwaka 2024 akionya kwamba ofisi yake inakabiliwa na upungufu mkubwa wa fedha zinazohitajika ili kusongesha mbele haki za binadamu duniani.Mashinani tutasalia papa hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa, jijini New York, Marekani, kusikia kauli ya Mahakama ya Kimataifa ya uhalifu, ICC kuhusu Sudan.      Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
1/30/202411 minutes, 17 seconds
Episode Artwork

Angola: Mradi wa IFAD umeniheshimisha Kijiji kwetu- Albertina

Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo, IFAD ni taasisi ya fedha ya kimataifa na pia shirika la Umoja wa Maitafa lililojikita katika kutokomeza umaskini na njaa kwenye maeneo ya vijijini yaliyoko katika nchi zinazoendelea. Miongoni mwa maeneo ambako Mfuko huo unafanya kazi ni nchini Angola barani Afrika ambako huko takwimu zinaonesha ongezeko la vijana wanaohamia mijini kutoka vijijini kwa sababu ya umaskini wa vijijini. Kwa kutambua hilo, na kwa kusaka kuchagiza ufanikishaji wa lengo namba 1 la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs kuhusu kutokomeza umaskini, Mfuko huo ukachukua hatua ya kuanzisha mradi wa kuepusha vijana kukimbilia mijini kwani vijijini nao kuna fursa. Ili kufahamu mradi huo ulioleta matokeo chanya, ungana na Assumpta Massoi kwenye makala hii iliyofanikishwa na IFAD.
1/29/20244 minutes, 36 seconds
Episode Artwork

Mashamba darasa yaliyoandaliwa na FAO Syria yainua wanawake wafugaji

Na sasa tuelekee Mashariki ya Kati, Leah Mushi anatueleza jinsi mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Chakula na Kilimo FAO na la Mpango wa chakula duniani WFP yanavyosaidia kuinua maisha ya wananchi katika nchi ya Syria.Mashariki mwa Syria katika mji wa Deir ez-Zor ulioko umbali wa km 450 kutoka mji mkuu wa nchi hiyo Damascus, mashirika ya UN lile la FAO na WFP yanafanya kila juhudi kuwajengea uwezo na kubadili maisha ya wananchi kupitia miradi mbalimbali.Katika Kijiji cha Al Masrab FAO ilianzisha mafunzo ya mashamba ya wakulima, na wanakijiji wakapewa mafunzo mbalimbali ikiwemo ya ufugaji wa kondoo kwa faida.Bi. Wafaa Al Sydyan anasema mara baada ya kuhitimu mafunzo hayo WFP ikampa mtaji wa zizi la kondoo. “Chanzo changu kikuu cha mapato kinatokana na ufugaji kondoo, na kipato changu kiliongezeka baada ya kupata uzoefu kutoka kwenye mafunzo mbalimbali ambayo yaliniwezesha mimi na familia yangu kumudu gharama za maisha. Nauza maziwa katika kituo cha ushindikaji cha hapa kijijini kwetu Al Masrab.”Video ya WFP inamuonesha Bi. Baraa Nadal mnufaika wa WFP akiwa na wanawake wenzake wanne katika kituo cha usindikaji maziwa, wakichemsha maziwa na kisha kuchakata mazao yatokanayo na maziwa katika mashine maalum ili kujipatia mazao mbalimbali na anasema si haba biashara inaenda vyema.“Tunauza baadhi ya mazao hapa kijijini kwetu na baadhi tunauza katika soko la Shmatieh. Tunamshukuru Mungu, mapato yetu yamekuwa bora kwa sababu ya kitengo cha usindikaji tulichowezeshwa na WFP.”Miradi hii ya WFP na FAO imepata ufadhili kutoka kwa wadau mbalimbali ikiwemo Muungano wa Ulaya, Wizara ya mambo ya nje ya Norway na Idara ya maendeleo ya serikali ya Italia.
1/29/20241 minute, 42 seconds
Episode Artwork

Nchi 5 zapokea vyeti kutoka WHO kwa kuchukua hatua kutokomeza vambato hatari kwenye vyakula

Kwa mara ya kwanza leo shirika la Umoja wa Mataifa la afya duniani, WHO, limezitunukia vyeti nchi tano kwa hatua kubwa zilizopiga katika kutokomeza viambato vya mafuta katika vyakula vinavyosindikwa viwandani kwa ajili ya kuongeza ladha au Trans Fats. Flora Nducha na maelezo zaidi.Kwa nmujibu wa WHO nchi hizo tano zilizopokea vyeti leo mjini Geneva Uswisi ni Denmark, Lithuania, Poland, Saudi Arabia na Thailand na zimepongezwa kwa kuwa na será bora kwa ajili ya kutokomeza viambato hivyo vya mafuta kwa vyuakula vinavyosindikwa viwandani au iTFA na pia mfumo wa kufuatilia utekelezaji wa serra hizo.Ingawa lengo la WHO lililowekwa mwaka 2018 la kutokomeza viambato vya mafuta y kuongeza ladha katika vyakula vinavyosindikwa viwandani ifikapo mwisho wa mwaka 2023 halikutimia shirika hilo linasema kuna hatua kubwa zimepigwa kuelekea utimizaji wa lengo hilo katika kila kanda duniani.Mathalani limesema mwaka jana pekee nchi saba ziliweka na kuanza kutekeleza será za kutokomeza viambato hivyo vya mafuta ambazo ni Misri, Mexico, Moldova, Nigeria, North Macedonia, Ufilipino na Ukraine.Viambato vya mafuta katika chakula vinahusishwa na athari nyingi za kiafya zikiwa ni pamoja na ongezeko la magonjwa ya kiharusi, shinikizo la damu na vifo vitokanavyo na magonjwa ya moyo.Baadhi ya vyakula vyenye kiwango kikubwa cha viambato hivyo vya mafuta WHO inasema ni vuakula vya kukaangwa, keki na miliambayo imeshatayarishwa na kufungashwa viwandani ambavyo vina viwango vya juu vya sukati, mafuta na chumvi.Akikabidhi vyeti hivyo mkuruhenzi mkuu wa WHO Dkt. Tedros Adhanon Ghebreyesus amesema “ Viambato vya mafuta havina faida yoyote mwilini isipokuwa hatari kubwa. Tunafuraha kwamba kuna nchi nyingi zimeweka será za kutokomeza au kupunguza viambato vya mafuta katika chakula. Lakini kuweka será ni suala moja na kuzitekeleza ni suala lingine. Nazipongeza Denmark, Lithuania, Poland, Saudi Arabia na Thailand kwa kuingoza Dunia katika kufuatilia na kutekeleza será dhidi ya viambato vya mafuta katika chakula, tunazichagiza nchi zingine kufuata nyayo zao.”Hivi sasa shirika hilo linasema kuna jumla ya nchi 53 zimeweka será na kuanza kuzitekeleza dhidi ya viambato vya mafuta katika chakula na hivyo kuboresha lishe ya watu bilioni 3.7 sawa na asilimia 46 ya watu wote duniani ikilinganishwa na asilimia 6 tu ya watu miaka mitano iliyopita.   
1/29/20242 minutes, 38 seconds
Episode Artwork

29 JANUARI 2024

Hii leo kwenye Jarida la Habari la Umoja wa Mataifa Anold Kayanda anaanzia na masuala ya afya, hususan viambato vya mafuta vinavyohatarisha afya ya mwili, kisha miradi ya UN ilivyosaidia wanawake huko Syria .Makala inakupeleka Angola kuona jinsi Umoja wa Mataifa umenusuru wanawake wa vijijini kwa hohehahe na mashinani atakupeleka katika kambi ya wakimbizi ya Kakuma iliyoko Kaunti ya Turkana, nchini Kenya kupata ujumbe kuhusu elimu hasa kwa wasichana.Kwa mara ya kwanza leo shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO, limezitunukia vyeti nchi tano kwa hatua kubwa zilizopiga katika kutokomeza viambato vya mafuta katika vyakula vinavyosindikwa viwandani kwa ajili ya kuongeza Ladha au Trans Fats. Flora Nducha amefuatilia taarifa hiyo na anatujuza zaidi.Mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Chakula na Kilimo FAO na la Mpango wa chakula duniani WFP yanasaidia kuinua maisha ya wananchi katika nchi ya Syria kwa kuwapatia miradi mbali mbali ikiwemo ya ufugaji wa kondoo. Leah Mushi anakusimulia kilichofanyikaMakala Assumpta Massoi anakupeleka Angola, kusini mwa Afrika kusikia ni vipi mradi wa Umoja wa Mataifa umeheshimisha wanawake wa vijijini akiwemo mmoja wao aitwaye Albertina.Mashinani: Igiraneza Mixella, msichana mkimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambaye amesajiliwa kusoma kwa ufadhili wa Mpesa Foundation Academy ambayo huelemisha wanafunzi mahiri na wenye vipaji lakini wasiojiweza kiuchumi, akielezea jinsi alivyo na furaha isiyo na kifani kwa kutimiza ndoto zake za kuendelea na masomo yake ya sekondari katika shule hiyo.Karibu! 
1/29/202411 minutes, 44 seconds
Episode Artwork

Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ yaitaka Israeli iepushe mauaji ya kimbari Gaza

Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ hii leo imeamua kuwa Israel lazima ichukue hatua zote za kuzuia vitendo vya mauaji ya kimbari katika mashambulizi yake dhidi ya wapalestina huko, Gaza, uamuzi unaofuatia shauri lililowasilishwa na Afrika Kusini la kutaka Mahakama hiyo ya Umoja wa Mataifa ichukue hatua za awali kwa mujibu wa Mkataba wa kimataifa wa kuepusha mauaji ya kimbari wa mwaka 1948. Hakika Leah! Kama unavyofahamu Afrika Kusini katika shauri lake iliyowasilisha tarehe 29 mwezi Desemba mwaka jana wa 2023, Afrika Kusini ilidai kuwa Israeli inakiuka wajibu wake wa kuzingatia Mkataba wa Kimataifa wa Kuzuia mauaji ya Kimbari kuhusiana na wapalestina huko Ukanda wa Gaza na hivyo kutaka ICJ ichukue hatua za awali kuepusha kinachoendelea. Hatua ni pamoja na Israel isitishe mara moja operesheni zake za kijeshi ndani na dhidi ya Gaza, ichukue hatua za kimsingi kuepusha mauaji ya kimbari na pia ichukue hatua zote ndani ya uwezo wake kufuta amri zinazohusiana na mashambulizi ikiwemo za kuzuia au kufukuza na kufurusha watu kutoka makazi yao, halikdhalika watu kunyimwa fursa ya kupata chakula cha kutosha na maji.   Hukumu ya ICJ yenye kurasa 29 iliyosomwa na Jaji Phillipe Gautier inasema masharti yote ya kuwezesha kuchukua hatua za dharura yako wakati uamuzi wake wa mwisho ukisubiri wa kutangaza hatua za kulinda haki zinazodaiwa na Afrika Kusini.  Ingawa hivyo Mahakama imesema kwa mazingira ya kesi husika, hatua zitakazochukuliwa si lazima zifanane na zile zilizoombwa na Afrika Kusini. Kwa hivyo basi Israeli inapaswa, kwa mujibu wa Mkataba wa kuzuia mauaji ya kimbari ambayo taifa hilo ni mwanachama, itumie uwezo wake wote izuie vitendo vyote kwa mujibu wa ibara ya pili ya mkataba huo ikiwemo mauaji ya kundi hilo yaani wapalestina. Israeli izuie na iadhibu mauaji yoyote ya wapalestina Ukanda wa Gaza na ichukue hatua zote kuwezesha ufikishaji wa misaada ya kibinadamu eneo hilo. Mahakama imetaka Israel iwasilishe ripoti ya utekelezaji wa uamuzi huu wa Mahakama ndani ya mwezi mmoja kuanzia tarehe ya leo ya hukumu, ripoti ambayo itawasilishwa pia kwa Afrika Kusini ili nayo iweze kutoa maoni yake kuhusu utekelezaji.  Suala hili lilikuwa miongoni mwa maombi ya Afrika Kusini ya kwamba ripoti ya utekelezaji iwasilishwe. Kwa mujibu wa Mkataba ulioanzisha ICJ, uamuzi unaotolewa na Mahakama hii huwa haukatiwi rufani. 
1/26/20242 minutes, 13 seconds
Episode Artwork

26 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia maamuzi wa Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ vitendo vya mauaji ya kimbari katika mashambulizi ya Israel dhidi ya wapalestina huko Gaza. Pia tunamulika viwanda vya nishati safi ulimwenguni, makala ikitupeleka nchini India. Mashinani tnakuletea ujumbe wa mhamiaji ambaye ni mchezaji wa musiki, mwalimu na rafiki nchini Burundi.Mahakama ya Kimataifa ya Haki, ICJ hii leo imeamua kuwa Israel lazima ichukue hatua zote za kuzuia vitendo vya mauaji ya kimbari katika mashambulizi yake dhidi ya wapalestina huko, Gaza, uamuzi unaofuatia shauri lililowasilishwa na Afrika Kusini la kutaka Mahakama hiyo ya Umoja wa Mataifa ichukue hatua za awali kwa mujibu wa Mkataba wa kimataifa wa kuepusha mauaji ya kimbari wa mwaka 1948. Assumpta Massoi amefuatilia na kuandaa taarifa ifuatayo.     Kilimo ni moja ya shughuli za kibinadamu zinazochangia katika uchafuzi wa hewa. Kwa kulitambua hilo, FAO kote ulimwenguni inachagiza kile inachokiita kwa lugha ya kiingereza Bioeconomy yaani uchumi ambao msingi wake unatokana na matumizi ya rasilimali za kibayolojia zinazopatikana kwenye mazingira; kwa mfano kurejesha taka katika uzalishaji wa nishati safi, mbadala wa mafuta ya kisukuku. Kupitia harakati hizo, FAO inasaidia wakulima kuongeza mapato, kupunguza uzalishaji wa hewa chafuzi na kuchangia kupunguza taka ulimwenguni kwa kubadilisha mifumo ya zamani ya kilimo ambayo ilikuwa inachangia kuharibu mazingira.Na makala ikiwa leo ni maadhimisho ya kwanza kabisa ya siku ya kimataifa ya nishati safi nakupeleka Tanzania kuangazia juhudi zinazofanyika kuhamasisha umma kuhamia kwenye nishati safi au jadidifu kutimiza lengo namba 7 la maendeleo endelevu SDGs. Vijana wako msitari wa mbele katika harakati hizo na miongoni mwao ni Nuzulack Dausen mwanzilishi wa Jukwaa la kidijitali la Jiko point linaloendesha kipindi cha mwanaume jikoni kupitia mtandao wa Youtube. Amezungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam na Stella Vuzo afisa habari wa Umoja wa Mataifa na kumfafanulia wanavyochangia katika kufanikisha lengo la maendeleo endelevu la Umoja wa Mataifa      kuhusu nishati safi . Mashinani tutaelekea katika Jiji la Bujumbura nchini Burundi kumsikia mhamiaji ambaye ni mchezaji wa musiki, mwalimu na rafiki.      Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
1/26/202412 minutes, 7 seconds
Episode Artwork

FAO: Kuna nishati safi na fedha katika kinachoonekana kuwa ni takataka

Kilimo ni moja ya shughuli za kibinadamu zinazochangia katika uchafuzi wa hewa. Kwa kulitambua hilo, FAO kote ulimwenguni inachagiza kile inachokiita kwa lugha ya kiingereza Bioeconomy yaani uchumi ambao msingi wake unatokana na matumizi ya rasilimali za kibayolojia zinazopatikana kwenye mazingira; kwa mfano kurejesha taka katika uzalishaji wa nishati safi, mbadala wa mafuta ya kisukuku. Kupitia harakati hizo, FAO inasaidia wakulima kuongeza mapato, kupunguza uzalishaji wa hewa chafuzi na kuchangia kupunguza taka ulimwenguni kwa kubadilisha mifumo ya zamani ya kilimo ambayo ilikuwa inachangia kuharibu mazingira. FAO iliwatembelea wakulima wa mpunga katika eneo moja nchini India. Kama walivyo wakulima wengine katika maeneo mengine duniani, hawa nao walikuwa wanachoma moto mabaki ya mimea baada ya mavuno ili kuandaa shamba kwa ajili ya msimu mwingine. Njia hiyo isiyofaa ilimaanisha kuwa wakulima hawakufaidika na mabaki ya mimea ya mpunga lakini sasa wakulima na kampuni za biashara wanavuna pia kutoka katika mabaki hayo kwa kuzalisha nishati mbadala ya mafuta ya kuendeshea mitambo na pia vumbi la mabaki linatumika kutengeneza nishati, mbadala wa mkaa wa miti.Profesa Ramesh Chand ambaye ni mmoja wa jopo la fikra la Serikali ya India linalohusika na sera za umma za kuchochea maendeleo ya kiuchumi, anasema, “kwa kuchoma moto tu mabaki ya mazao bila kuyatafutia shughuli mbadala sio tu unaharibu mazingira na afya bali pia kwa namna fulani unachoma moto utajiri.”
1/26/20241 minute, 42 seconds
Episode Artwork

Nuzulack Dausen: Nishati safi inanusuru mazingira na kuinua kipato katika jamii

Leo ni siku ya kimataifa ya nishati safi ambayo lengo lake ni kuzihimiza jamii kote duniani kutekeleza lengo la 7 la maendeleo la Umoja wa Mataifa la kuhakikisha kila mtu anahamia kwenye matumizi ya nishati hiyo ifikapo mwaka 2030. Nchini Tanzania wako msitari wa mbele katika harakati za utekelezaji wa lengo hilo na miongoni mwao ni Nuzulack Dausen mwanzilishi wa Jukwaa la kidijitali la Jiko point linaloendesha kipindi cha mwanaume jikoni kupitia mtandao wa Youtube. Amezungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam na Stella Vuzo afisa habari wa Umoja wa Mataifa na kumfafanulia wanavyochangia katika kufanikisha lengo la maendeleo endelevu la Umoja wa Mataifa kuhusu nishati safi. 
1/26/20245 minutes, 1 second
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili: Ufafanuzi wa neno “KUWEKUA.”

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili  leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KUWEKUA.”
1/25/20241 minute, 8 seconds
Episode Artwork

25 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambayo inamulika hali ya kibinadamu na ya kiafya katika ukanda wa Gaza. Pia tunakuletea habari kwa ufupi tukisalia huko huko Gaza, machafuko nchini Sudan na ya siku ya kimataifa ya wanawake katika ushirikiano wa kimataifa. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili tunakuletea ufafanuzi wa neno “KUWEKUA”.Mashambulizi makubwa dhidi ya majengo Gaza ambayo raia wenye hofu wanakimbilia kupata hifadhi ni "ya kuchukiza na lazima yakome mara moja", amesisitiza Thomas White naibu mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa katika eneo hilo linalokaliwa la Gaza baada ya leo, kombora kuanguka katika kituo cha mafunzo cha Umoja wa Mataifa.. Sudan inakaribia kuwa moja ya janga baya zaidi la elimu duniani ameonya mwakilishi wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF nchini humo Mandeep O’Brien. Katika mahojiano maalum na UN News kwa njia ya mtandao Bi. O’Brien amesema Sudan inakabiliwa na janga la kibinadamu lisiloelezeka na ni jinamizi kwa watoto kwani  watoto "Milioni 14 wanahitaji haraka msaada wa kuokoa maisha wa afya, lishe, elimu, maji na ulinzi. Pili, tunapozungumza, tunajua kwamba zaidi ya watoto milioni 3.5 wamelazimika kukimbia makazi yao tangu vita hii ianze na hii inaifanya Sudan kuwa taifa lenye idadi kubwa zaidi ya watoto waliokimbia makazi yao duniani”. Sudan ina watoto milioni 19 wenye umri wa kwenda shule ambao sasa hawasomi.Na leo ni siku ya kimataifa ya wanawake katika ushirikiano wa kimataifa. Mwaka huu 2024 inaadhimishwa chini ya kaulimbiu “Usawa wa kijinsia katika kutatua dharura ya mabadiliko ya tabianchi.” Shirika la Umoja wa Mataifa la elimu, sayansi na utamaduni UNESCO ambalo linasimamia siku hii, limesema lengo lake ni kutambua wanawake viongozi katika mfumo wa kushirikiano wa kimataifa ili kuchagiza mazungumzo kuhusu suluhu za kimataifa dhidi ya ubaguzi wa kijinsia ambao unakwamisha hatua dhidi ya dharura ya mabadiliko ya tabianchi. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili  leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KUWEKUA”.      Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
1/25/202413 minutes, 10 seconds
Episode Artwork

Wakazi wa Ituri, DRC, wazungumzia usaidizi wa MONUSCO kwenye eneo lao

Katika jimbo la Ituri, mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, watu waliokimbia makazi yao wanaishi katika takribani kambi 38, ambapo miongoni mwao ni Drodro, Roe, Lodha, Jaiba na Gina. Zaidi ya wakimbizi Laki Nne (400,000) wanafaidika na ulinzi wa moja kwa moja wa ujumbe wa walinda amani wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO.  Walinda amani hao wakiwemo wale wa kutoka Nepal hulinda kambi za watu waliohamishwa kwa kufanya doria za usiku na mchana. Na zaidi ya yote MONUSCO imeweka miundombinu ya kuhakikishia raia usalama wao, moja ya majukumu ya ujumbe huo ambao kwa sasa unaanza kufunga virago taratibu kwa mujibu wa azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kufuatia ombi la serikali ya DRC. Katika makla hii mwandishi wetu wa habari mashariki mwa DRC George Musubao alifuatilia mtazamo wa wananchi kuhusu usaidizi wa MONUSCO.   
1/24/20244 minutes, 24 seconds
Episode Artwork

Siku ya Elimu Duliani 2024 yatumika kukabiliana na kauli za chuki

Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limeyatumia maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Kimataifa ya Elimu kuangazia jukumu muhimu la elimu na walimu katika kukabiliana na kauli za chuki, jambo ambalo limekithiri katika miaka ya hivi karibuni kutokana na matumizi ya mitandao ya kijamii na hivyo kuharibu muundo wa jamii kote duniani. UNESCO ambalo ndilo shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika moja kwa moja na jukumu la kuratibu maadhimisho ya siku hii ya kimataifa ya elimu inayodhimishwa kila mwaka tarehe 24 Januari, linasema ulimwengu unashuhudia ongezeko la migogoro inayoambatana na ongezeko la kutisha la ubaguzi, ubaguzi wa rangi, chuki dhidi ya wageni, na kauli za chuki. Na kwa kuwa madhara yanavuka mipaka yoyote ya kijiografia, jinsia, rangi, dini, siasa, nje ya mtandao na mtandaoni elimu ni msingi wa kufanikisha kupambana na hali hiyo.Audrey Azoulay ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa UNESCO kupitia ujumbe wake mahususi kwa siku hii akifafanua kauli mbiu ya mwaka huu ambayo ni ‘Elimu kwa ajili ya amani ya kudumu’ amesema, “kwa sababu kama chuki inaanza kwa maneno, basi amani inaanza na elimu. Tunachojifunza hubadilisha jinsi tunavyouona ulimwengu na huathiri jinsi tunavyowatendea wengine. Kwa hivyo elimu lazima iwe kiini cha juhudi zetu za kufikia na kudumisha amani ya ulimwengu.” Anasisitiza kwamba, katika siku hii, kujitolea kwako kutetea haki ya elimu bora ambayo inatambua haki za binadamu za kila mtu inamaanisha kujitolea kwa mustakabali wa amani kwa wote, ambapo kila mtu anaweza kuishi maisha ya utu, kwa kuelewana na heshima.Ili mawazo haya yawafikie watu wengi zaidi ulimwenguni, UNESCO hii leo kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa mjini New York, Marekani imewakutanisha wadau wa elimu kutoka kote ulimwenguni ili kujadili mchango muhimu wa elimu katika kufikia amani endelevu duniani. Pia imefanya mafunzo ya mtandaoni ya siku moja kwa maelfu ya walimu kutoka kote ulimwenguni kuhusu utatuzi wa kauli za chuki, ambayo yamewapa zana za kutambua vyema, kukabiliana na kuzuia matukio ya kauli za chuki. Mafunzo haya ni sehemu ya hatua ya UNESCO kusaidia Nchi Wanachama na wataalamu wake wa elimu kushughulikia kauli za chuki kupitia elimu.
1/24/20242 minutes, 10 seconds
Episode Artwork

24 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya kimataifa ya elimu duniani mada kuu ikiwa ni elimu na mchango wake wa kuleta amani ulimwenguni. Makala tunakupeleka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na mashinani nchini Kenya, kulikoni?Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni (UNESCO) limeyatumia maadhimisho ya mwaka huu ya Siku ya Kimataifa ya Elimu kuangazia jukumu muhimu la elimu na walimu katika kukabiliana na kauli za chuki, jambo ambalo limekithiri katika miaka ya hivi karibuni kutokana na matumizi ya mitandao ya kijamii na hivyo kuharibu muundo wa jamii kote duniani.     Nchini Uganda katika makazi ya wakimbizi ya Kyangwali wilaya ya Kikuube magharibi mwa taifa hilo, suala la mchango wa elimu kwenye amani liko dhahiri kwani tulipotembelea katika makazi hayo, Yahya Kato ambaye ni Mwalimu Mkuu katika Shule ya msingi Kasonga kwenye makazi hayo ya wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Sudan aliteueleza kile wanachofanya.Makala inatupeleka huko Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC hususan jimboni Ituri mashariki mwa nchi hiyo ambako wakazi wanazungumzia mchango wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO wakati huu ambapo ujumbe huo umeanza kufungasha virago. Mashinani tutaelekea katika kaunti ya Garissa nchini Kenya ambapo mvua kubwa inayohusiana na El Niño, imesababisha maelfu ya watu kuyahama makazi yao, kuharibu miundombinu na kusababisha kipindupindu na magonjwa mengine yatokanayo na maji yasiyo safi na salama, Mohammed Saidi, Chifu wa kambi ya waislamu waliopoteza makazi yao katika kaunti ya Garissa anasimulia kinachojiri.      Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
1/24/20249 minutes, 57 seconds
Episode Artwork

Uganda: Makazi ya wakimbizi yatumia elimu kusongesha amani miongoni mwa wakimbizi

Nchini Uganda katika makazi ya wakimbizi ya Kyangwali wilaya ya Kikuube magharibi mwa taifa hilo, suala la mchango wa elimu kwenye amani liko dhahiri kwani tulipotembelea katika makazi hayo, Yahya Kato ambaye ni Mwalimu Mkuu katika Shule ya msingi Kasonga kwenye makazi hayo ya wakimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na Sudan aliteueleza kile wanachofanya. 
1/24/20241 minute, 15 seconds
Episode Artwork

23 JANUARI 2024

Hii leo jaridani mada kwa kina, ambapo katika mchakato wa kuleta mabadiliko kwa kuwezesha wanaojifunza kupata ufahamu muhimu, maadili, mienendo, stadi na tabia na hivyo wawe wachagizaji wa amani kwenye jamii zao, tnakupeleka katika makazi ya wakimbizi nchini Uganda kuona ni kwa vipi mchakato huo unafanyika. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limeonya kwamba watu 570,000 wanakabiliwa na janga kubwa la njaa kutokana na kuendelea kwa mapigano makali, wahudumu wa misaada kunyimwa fursa ya kuwafikia wenye uhitaji na kukatwa kwa mawasiliano, sababu ambazo pia zimeathiri uwezo wa shirika hilo kufikisha na kusambaza msaada kwa usalama kwa maelfu ya watu. Hivyo limetoa wito wa kuongezwa haraka fursa za usambazaji na ufikishaji wa misaada ya kibinadamu. Kwingineko wito wa kuchukuliwa hatua za haraka kushughulikia ongezeko kubwa la vifo vya wakimbizi wa Rohingya baharini umetolewa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR. Kwa mujibu wa shirika hilo wakimbizi wa Rohngya 569 walipoteza maisha au kupotea walipotumia safari hatari za boti katika bahari ya Andaman na Ghuba ya Bengal mwaka 2023, hiyo ikiwa ni idadi kubwa zaidi ya waliopoteza Maisha tangu mwaka 2014.Na huko Ukraine Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu wa nchi hiyo Denise Brown amelaani vikali wimbi jipya la mashambulizi ya anga ya Urusi dhidi ya miji iliyo na watu wengi nchini Ukraine. Mashinani tutaelekea katika ukanda wa Gaza kusikia ujumbe kuhusu harakati za chanjo kwa watoto ambao tayari wamekumbwa na changamoto ya vita.      Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
1/23/202412 minutes, 37 seconds
Episode Artwork

Hata mimi mwenyewe nilikuwa sijiamini hadi nilipopata mafunzo ya RLabs - Mariam

Mkakati wa Afya ya Uzazi kwa Wasichana, Haki, na Uwezeshaji nchini Tanzania (GRREAT) unaoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa kushirikiana na wadau likiwemo shirika lisilo la kiserikali la RLabs Tanzania na serikali ya Canada ni mpango wa miaka mitano (2019-2024) ili kuisaidia Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar katika kuboresha ustawi wa wasichana balehe katika mikoa ya Mbeya na Songwe, pamoja na Zanzibar. Kupitia mpango huu wasichana wamepata zana na ujuzi wanaohitaji ili kuboresha maisha yao, familia na jamii zao. Mmoja wao ni Mariam wa Nyanda za juu kusini mwa Tanzania. 
1/22/20243 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

UN: Raia 25, 000 wamepoteza maisha katika vita Gaza na mahitaji ya kibinadamu yanazidi kuongezeka

Mashambulizi makubwa ya mabomu yanayofanywa na Israel Gaza yameendelea tena leo sanjari na maroketi yanayovurumushwa na makundi yenye silaha ya Kipalestina kuelekea Israel, wakati wahudumu wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa wakiripoti kuuawa kwa watu zaidi ya 25,000 Gaza tangu kuanza kwa machafuko hayo mapya Oktoba 7 mwaka jana na mahitaji ya kibinadamu yakiongezeka kila uchao. Hali inazidi kubwa mbaya na hakuna dalili ya kukomesha uhasama Gaza limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA. Likinukuu takwimu za wizara ya afya ya Gaza mbali ya watu waliopoteza maisha Wapalestina zaidi ya elfu 62 wamejeruhiwa, wakati serikali ya Israel kwa upande wake ikisema tangu mwishoni mwa wiki askari wake wawili wameuawa na kufanya jumla ya askari wa Israel waliopoteza Maisha tangu kuanza kwa operesheni ya vita vya ardhini kufikia 193 na majeruhi zaidi ya 1200.Leo mawaziri wa mambo ya nje wa Israel na Palestina wanajiandaa kukutana na wenzao wa Ulaya kwenye mazungumzo ya faragha mjini Brussels Ubeligiji, na hatua hii imekuja baada ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres mwishoni mwa wiki kwenye mkutano wa G-77 na China uliofanyika Kampala Uganda kulaani vikali umwagaji damu unaoendelea Gaza akisema ni unasikitisha na haukubaliki akisisitiza kufanyika kila linalowezekana kuzuia mgogoro huo kusambaa zaidi kikanda.Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa mahitaji ya kibinadamu ni makubwa sana na yanaongezeka kila siku, hivi sasa ni maduka 15 pekee ya kuoka mikate ndio yanayofanya kazi sita Rafah na tisa Deir al Balah na hakuna hata moja Kaskazini mwa Wadi Gaza.Nalo shirika la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema kuendelea kutokuwepo kwa mawasiliano kwa siku ya saba sasa kunavuruga usambazaji wa misaada na watu kupata huduma muhimu zikiwemo za matibabu hasa ukizingatia kwamba watu milioni 1.7 wametawanywa na miongoni mwa raia waliouawa 335 walikuwa katika makazi ya UNRWA na wafanyakazi wa shirika hilo waliopoteza Maisha hadi sasa ni 151.
1/22/20242 minutes, 22 seconds
Episode Artwork

22 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia msaada wa kibinadamu katika ukanda wa Gaza, na mradi wa ufugaji nyuki nchini Zimbabwe. Makala tunamuika mkakati wa Afya ya Uzazi kwa Wasichana, Haki, na Uwezeshaji nchini Tanzania na mashinani tunasalia na mada ya elimu bora na tunakupeleka nchini Uganda.Mashambulizi makubwa ya mabomu yanayofanywa na Israel dhidi ya Gaza yameendelea tena leo sanjari na maroketi yanayovurumushwa na makundi yaliyojihami ya kipalestina kuelekea Israel, wakati wahudumu wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa wakiripoti kuuawa kwa watu zaidi ya 25,000 huko Gaza tangu kuanza kwa machafuko hayo mapya Oktoba 7 mwaka jana na mahitaji ya kibinadamu yakiongezeka kila uchao. Nchini Zimbabwe, mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, FAO, wa kusongesha ajira rafiki kwa mazingira umeanzisha mashamba darasa ya ufugaji wa nyuki na hivyo kuandaa vijana kuwa wakulima wajasiriamali vijijini. Mradi huo unatekelezwa kwa ubia na shirika la Korea Kusini la Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa, KOICA.Makala inatupeleka nchini Tanzania kuangazia Mkakati wa Afya ya Uzazi kwa Wasichana, Haki, na Uwezeshaji nchini Tanzania (GRREAT) unaoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa kushirikiana na wadau likiwemo shirika lisilo la kiserikali la RLabs Tanzania na serikali ya Canada. Kupitia mpango huu wasichana wamepata zana na ujuzi wanaohitaji ili kuboresha maisha yao, familia na jamii zao. Mmoja wao ni Mariam wa Nyanda za juu kusini mwa Tanzania. Mashinani tunakupeleka makazi ya wakimbizi ya Kyangwali magharibi mwa Uganda kupata ujumbe wa uhusiano wa elimu na amani.      Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
1/22/202410 minutes, 18 seconds
Episode Artwork

Ufugaji nyuki ‘waua’ ndege zaidi ya mmoja, yasema FAO - Zimbabwe

Nchini Zimbabwe, mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, FAO, wa kusongesha ajira rafiki kwa mazingira umeanzisha mashamba darasa ya ufugaji wa nyuki na hivyo kuandaa vijana kuwa wakulima wajasiriamali vijijini. Mradi huo unatekelezwa kwa ubia na shirika la Korea Kusini la Ushirikiano wa Maendeleo ya Kimataifa, KOICA. Pasi shaka Assumpta, naanza na Angelina Manhanzva, kijana wa kike akiwa shambani akihudumia mzinga wa nyuki anatanabaisha kuwa…(Nats) fursa inapokufikia usiipuuze kwani inaweza kubadili maisha yako katika fumba na kufumbua.  Mjasiriamali kijana huyu kutoka wilaya ya Chegutu jimboni Mashonaland kaskazini-kati mwa Zimbabwe anakiri kuwa baada ya kushiriki kwenye ufugaji wa nyuki kwa miezi kadha wameshuhudia maisha yao  yakibadilika.  Barnabas Mawire, mtaalamu wa maliasili wa FAO nchini Zimbabwe anasema, “Wazo ni kwamba, eneo moja lenye mizinga ya nyuki linaweza kugeuzwa kuwa shamba darasa  ambako vijana kutoka wilaya au kata tofauti wanaweza kuja kujifunza kama waendavvyo shuleni .”  FAO inasema kuwa kupatia vijana wa vijijini ajira zisizoharibu au kuchafua mazingira kunaweza kukabili madhara ya mabadiliko ya tabianchi, kuondoa umaskini na kutokomeza umaskini wa vijijini. Mkulima mjasiriamali kijana Evelyne Mutuda naye anakiri faida inapatikana na kwamba, "Tunatarajia kuongeza mizinga mingine ya nyuki kwa kutumia faida  ya fedha tuliyopata baada ya kuuza asali.  Na pia tutapanda mijakaranda .”   Akitamatisha afisa wa FAO, Bwana Mawire anadhihirisha uhusiano wa ufugaji nyuki na ulinzi wa bayonuai.  “Nyuki wanafaa sana kwa ajira zisizoharibu mazingira kwa mantiki kwamba wanahitaji aina mbali mbali za mimea . Kwa hiyo nyuki wanasongesha uhifadhi wa bayonuai. Unapotunza miti, unatunza tabianchi yetu,  chakula chetu na uhai wetu.  Hivyo ufugaji nyuki unanufaisha kwa juhudi kidogo.”  
1/22/20242 minutes, 12 seconds
Episode Artwork

EmpowerU Cash+; yabadilisha maisha katika Wilaya ya Lamwo nchini Uganda

Kutokana na ushirikiano kati ya serikali ya Uganda na ya Uholanzi, Mradi wa Maendeleo wa Kukabiliana na Athari za Ufurushwaji (DRDIP), Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa kutumia mfumo wa fedha taslimu wa EmpowerU Cash+.limewasaidia walengwa waliochaguliwa katika Wilaya ya Lamwo ambapo mpango uliwalenga wakimbizi na jamii zilizowapokea.  Mpango huo wa EmpowerU Cash+ ulikuwa unalenga idadi ya juu ya watoto kufikia wanne kwa kila kaya na kila mtoto kila mwezi alipewa Shilingi 45,000 za Uganda sawa na takribani  dola 11 za kimarekani hiyo ikimaainisha kila kaya ilipata jumla ya Shilingi za Uganda 180,000 sawa na takribani dola 47 za kimarekani kwa mwezi. Huduma hiyo ilikuwa kwa muda wa miezi sita katika wilaya za Lamwo, Adjumani, Yumbe, na Obongi lakini hapa ninaangazia wilaya moja tu, Lamwo. 
1/19/20244 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

19 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia vita katika ukanda wa Gaza, na tukielekea siku ya elimu duniani tunabisha hodi nchini Burundi ambako UNICEF inahakikisha watoto wakimbizi wanaorejea nchini humo wanaweza kuendelea na elimu. Makala na mashinani tunasalia na mada ya elimu bora na tunakupeleka nchini Uganda, kulikoni?.Mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa leo yameeielezea hali inayoendelea Gaza siku 105 baada ya kuzuka vita mpya baina ya wapiganaji wa Hamas na vikosi vya Israel, kuwa ni zahma juu ya zahma. Watu zaidi ya milioni 1.7 wametawanywa huku hofu ya milipuko ya magonjwa, janga la njaa na vifo zaidi likitawala. Nchini Burundi shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limechukua hatua kuhakikisha watoto wakimbizi wanaorejea nchini humo wanaweza kuendelea na elimu bila uoga na jakamoyo hasa pale wanapokumbana na vizuizi vya tofauti ya lugha waliyotumia ukimbizini na ile inayotumika nyumbani walikorejea.Makala inatupeleka kaskazini mwa Uganda katika wilaya ya Lamwo ambako Kutokana na ushirikiano kati ya serikali ya Uganda na ya Uholanzi, Mradi wa Maendeleo wa Kukabiliana na Athari za Ufurushwaji (DRDIP), Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa kutumia mpango wa fedha taslimu wa EmpowerU Cash+ limewasaidia wananchi kuboresha hali yao ya maisha. Mashinani Mashinani ttunasalia huko huko Uganda katika makazi ya wakimbizi ya Kyangwali magharibi mwa Uganda kupata ujumbe wa uhusiano wa elimu.      Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
1/19/202412 minutes, 24 seconds
Episode Artwork

Methali: "Aliye na hamu ya kupanda juu hukesha"

Leo katika kujifunza lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Aliye na hamu ya kupanda juu hukesha.”
1/19/20241 minute, 11 seconds
Episode Artwork

Nchini Burundi mbinu ya mashangazi na baba wa shuleni yaepusha watoto na kejeli kutoka kwa wenzao

Nchini Burundi shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF limechukua hatua kuhakikisha watoto wakimbizi wanaorejea nchini humo wanaweza kuendelea na elimu bila uoga na jakamoyo hasa pale wanapokumbana na vizuizi vya tofauti ya lugha waliyotumia ukimbizini na ile inayotumika nyumbani walikorejea. Hebu fikiria baada ya machungu ya ukimbizini, unarejea nyumbani nako shuleni unakumbwa na kejeli kisa tu matamshi ya lugha utumiayo ni tofauti na yale ya wenzako darasani. Pelouse Nibitanga huyu, ambaye amerejea Burundi kutokea Rwanda ni mwanafunzi wa darasa la saba katika shule ya msingi Kamena iliyoko mkoa wa Kirundo kaskazini mwa Burundi barani Afrika anathibitisha.  Anasema niliporejea hapa kutangamana hakukuwa rahisi. Kwani wanafunzi wengine walinicheka na kunikejeli kwa matamshi yake ya lugha darasani. Katika mazingira hayo kufaulu ilikuwa ni changamoto. Kupitia mradi wa kuweko kwa mashangazi na wababa wa shuleni, wanafunzi kama Pelouse na wale waliokuweko walipatiwa msaada sio tu wa kielimu bali pia kisaikolojia wa kuwawezesha kuishi na kusoma kwa utangamano. Mwalimu Sandrine Kamutako ni miongoni mwa washauri nasaha na mashangazi wa shuleni. “Usaidizi wa kisaikolojia na kijamii unaongeza zaidi imani ya mtoto kwa mwalimu na mnasihi wake. Mbinu hii ni nzuri kwani inasaidia wanafunzi kuwa na tabia nzuri. Na pia hujenga kuaminiana kati ya mwalimu na mwanafunzi.” Pelouse anathibitisha hilo akisema “shukrani sana kwa ushauri nasaha kwani nilianza kufuatilia masomo vizuri sana na nilimaliza darasa la 6 na sasa nimejiunga na darasa la 7. Sina tena aibu na ninafurahia masomo na wanafunzi wengine. Utangamano wangu unastawi vizuri. Inafurahisha mno.” Mafunzo hayo ya kuleta utangamano yamekuwa na manufaa kwa wanafunzi zaidi ya 18, wakiwemo zaidi ya 7,000 waliorejea Burundi kutoka ukimbizini. Shule nufaika na mafunzo hayo pia zimenufaika na miradi mingine kama ya ujenzi wa miundombinu ya kuvuna maji ya mvua, madarasa na mafunzo kwa walimu zaidi ya 1,500, UNICEF Burundi ikisema yote yamewezekana kufuatia ufadhili kutoka Muungano wa Ulaya, EU. 
1/19/20242 minutes, 21 seconds
Episode Artwork

Hali katika ukanda wa Gaza ni zahma juu ya zahma: Mashirika ya UN 

Mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa leo yameeielezea hali inayoendelea Gaza siku 105 baada ya kuzuka vita mpya baina ya wapiganaji wa Hamas na vikosi vya Israel, kuwa ni zahma juu ya zahma. Watu zaidi ya milioni 1.7 wametawanywa huku hofu ya milipuko ya magonjwa, janga la njaa na vifo zaidi likitawala. Asante Anold, nikianza na shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO linaonya juu ya mlipuko wa magonjwa ya kuambukiza Gaza watu zaidi ya milioni 1.7 waliotawanywa hivi sasa wanaishi katika makazi ya dharura yaliyofurika pomoni na kwa wastani watu 500 wanatumia choo kimoja huku watu zaidi ya 2000 wakitumia bafu moja kuoga na wakati mwingine kwenye baadhi ya makazi ya dharura hakuna choo kabisa.Hivyo shirika hilo linasema ukosefu wa vyoo na huduma za usafi vimewalazimisha watu kujisaidia haja kubwa kwenye maeneo ya wazi na kuongeza hatari kubwa ya kusambaa kwa magonjwa ya kuambukiza. Tangu katikati ya kwezi Oktoba mwaka jana WHO inasema kumekuwa na makali ya wagonjwa wa kuhara, matatizo ya njia ya mfumo wa hewa, chawa, upele, tetekuanga, homa ya manjano na hata homa ya ini aina ya E.Osisi ya Haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa OHCHR inasema ukiukwaji mkubwa wa haki unaendelea katika ukanda huo mkuu wa ofisi ya haki za binadamu kwenye eneo linalokaliwa la Gaza Ajith Sunghay mbaye yuko Gaza tangu Jumatatu anasema “Nimewaona wanaume na watoto wakifukua vifusi kupata matofali ya kujengea mahema ya mifuko ya plastiki, huli ni janga kubwa la haki za binadamu na janga kubwa lililosababishwa na binadamu. Gaza inahitaji ongezeko la misaada ya kibinadamu ikiwemo ulinzi.”Kwa upande wake shirika la kuhudumia watoto UNICEF linaangazia watoto wanaozaliwa wakati vita hii ikiendelea, ikiwa ni sikua ya 105 leo shirika hilo linasema karibu watoto 20,000 wamezaliwa katika hali ya jehanamu ikimaanisha mtoto 1 amezaliwa kila baada ya dakika 10 likionya kwamba wengi huenda wakafariki dunia kutokana na vita na hali mbayá ya Maisha na huduma Gaza.Nahitimisha na Shirika la kuratibu misaada ya kibinadamu OCHA ambalo linasema leo ni siku ya tano mfululizo huduma za mawasiliano zimekatwa Gaza na hali hii inazuia maelfu ya watu kupata tarifa za kuokoa maisha, kukosa fursa ya kuwapigia wahudumu wa afya kupata msaada na inaendelea kuathiri usambasaji wa msaada wa kibinadamu unaohitajika sana.Hadi kufikia sasa kwa mujibu wa takwimu za wizara ya afya ya Gaza takriban watu 25,000 wameuawa tangu Oktoba 7 mwaka jana.
1/19/20242 minutes
Episode Artwork

18 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Imesalia miaka 6 kufikia ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yaliyopitishwa na nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa mwaka 2015. Dkt. Venance Shillingi Mhadhiri Mwandamizi kutoka Chuo Kikuu Mzumbe nchini Tanzania aliwasilisha pendekezo la utafiti wake utakaoweza kuwa moja ya majawabu ya changamoto barani Afrika.  Pia tunakuletea habari kwa ufupi na uchambuzi wa methali.Mashirika ya Umoja wa Mataifa yamerejea kupaza sauti kuhusu misaada muhimu ya kibinadamu kuendelea kuruhusiwa kuingia Gaza, lile la kuratibu Misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA likisema kwa mara ya kwanza dawa kwa ajili ya mateka wa Israel zimeripotiwa kuruhusiwa kuingia leo sanjari na msaada kwa ajili ya Wapalestina kwa makubaliano maalum yaliyowezeshwa na serikali za Qatar na Ufaransa. Kwingineko ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kutafuta ukweli nchini Sudan umeanza kazi yake kwa ujumbe wa awali kuwasili mjini Geneva wiki hii, ukizitaka pande zinazozozana Sudan kumaliza vita, kutekeleza wajibu wao wa kulinda raia na kuhakikisha kwamba wahusika wa ukiukaji mkubwa wa haki za binadamu na uhalifu wanawajibishwa.Na barani Ulaya ambako ripoti mpya iliyochapishwa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF inasema takriban watoto nusu milioni kote barani Ulaya na Asia ya Kati wanaishi katika vituo vya makazi ya kulelea watoto pamoja na katika taasisi kubwa. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Aliye na hamu ya kupanda juu hukesha.”.  Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
1/18/202411 minutes, 50 seconds
Episode Artwork

Mbinu 3 za kuhakikisha watoto wanapata chanjo

Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto ulimwenguni UNICEF linatumia njia mbalimbali kuhakikisha watoto na familia zao wanapata chanjo stahili hili kuwaepusha kuugua magonjwa ambayo mengine yanaweza kuzuilika kwa kupata chango. Katika Makala hii Leah Mushi anatujuza mbinu tatu zinazotumiwa na UNICEF kuhakikisha jamii inapata chanjo. 
1/17/20243 minutes, 8 seconds
Episode Artwork

Guterres: Vita, mabadiliko ya tabianchi na AI ni changamoto tunazopaswa kuzishughulikia haraka

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo amehutubia jukwaa la uchumi duniani mjini Davos Uswis akigusia changamoto mbalimbali zinazpoikabili dunia hivi sasa kuanzia vita inayoendelea Gaza na kwingineko, hali ya kutochukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na maendeleo ya akili mnemba au AI. Asante Evarist katika hotuba yake Bwana Guterres alianza kwa kuelezea wasiwasi kuhusu changamoto ya tabianchi na ongezeko la joto duniani akisema nchi zimekumbwa na tabia ya kutochukua hatua na ubinafsi katia masuala ya maendeleo na matumizi ya mafuta kisikuku yameifanya dunia kushindwa kushikamana kushughulikia mabadiliko ya tabianchi na hivyo kuchochea ongezeko la joto duniani “ Nchi zinaendelea kuzalisha hewa chafuzi, sayari yetu inazidi kuchemka kuelekea nyuzi joto 3celisius, ukame, vimbunga, moto wa nyika na mafuriko winaathiri nchi na jamii.”Hotuba hiyo pia imegusa kwa kirefu hofu ya ukiukwaji wa sheria za kimataifa na majanga ya kibinadamu hususan katika mizozo inayoendelea kama vile Gaza na Ukraine akisema kuanzia uvamizi wa Urusi Ukraine hadi Sudan na hivi karibuni kabisa Gaza, pande husika katika mizozo hiyo zinapuuza sheria za kimataifa, zinakiuka mikataba ya Geneva na hata kukiuka katiba ya Umoja wa Mataifa.“Dunia imesismama ikiangangalia raia hususani wanawake na watoto wakiuawa, kulemazwa, kushambuliwa kwa mabonmu, kufurushwa makwao na kunyimwa haki ya misaada ya kibinadamu.”Kwa Gaza mathalani amerejea wito wa usitishwaji mapigano mara moja na kuwa na mchakato ambao utaelekea kuleta amani ya kudmu kwa Israel na Palestina  kwa misingi ya kuwa na mataifa mawili akisistiza kwamba “Hii ndio njia pekee ya kukata shina la madhila na kuzuia mzozo huo kusambaa hali ambayo itawasha moto katika ukanda mzima.”Na kuhusu suala la Akili mnemba Katibu Mkuu amezungumzia hatari yake na uwezekano wa kuongeza pengo la usawa na tabia isiyofaa ya makampuni makubwa ya teknolojia "Teknolojia hii ina uwezo mkubwa wa maendeleo endelevu lakini kama Shirika la Fedha Duniani lilivyotuonya hivi karibuni, kuna uwezekano mkubwa wa kuzidisha ukosefu wa usawa duniani. Na baadhi ya makampuni yenye nguvu ya teknolojia tayari yanafuata faida kwa kutozingatia haki za binadamu, faragha kibinafsi na athari za kijamii,"Amehitimisha hotuba yake kwa kwa kusisitiza hali muhimu na inayowezekana ya kujenga upya imani kwa ajili ya dunia iliyo salama na imara zaidi.
1/17/20242 minutes, 37 seconds
Episode Artwork

17 JANUARI 2024

Jaridani leo tunamulika jukwaa la uchumi duniani mjini Davos Uswis, na suala la kilimo endelevu. Makala tnakuletea mbinu tatu zinazotumika kuhakikisha watoto na familia zao wanapata chanjo na mashinani tutabisha hodi mkoani Mbeya nchini Tanzania kusikia ujumbe kuhusu ujuzi unaohitajika ili kufundisha wanafunzi kwa ufanisi.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres leo amehutubia jukwaa la uchumi duniani mjini Davos Uswis akigusia changamoto mbalimbali zinazoikabili dunia hivi sasa kuanzia vita inayoendelea Gaza na kwingineko, hali ya kutochukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na maendeleo ya akili mnemba au AI. Kilimo kinaweza kuchukua jukumu kuu katika hatua dhidi ya tabianchi wakati huo huo kikihakikisha uhakika wa chakula duniani, ni maoni ya Mkurugenzi wa Ofisi ya Mabadiliko ya Tabianchi, Bayonuai na Mazingira katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) Kaveh Zahedi kufuatia hivi majuzi mwaka 2023 kuthibitishwa kuwa mwaka wa joto zaidi katika rekodi za dunia.Makala hii leo Leah Mushi kupitia video ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF anatujuza mbinu tatu zinazotumika kuhakikisha watoto na familia zao wanapata chanjo.  Na katika mashinani Mwalimu Upendo Mwakapala kutoka Shule ya Msingi ya Uhuru iliyoko mkoani Mbeya Tanzania anatujuza mbinu bunifu za kufundisha ili kusaidia kuboresha elimu kwa watoto kupitia Mpango wa Mafunzo ya Ualimu wa Shule za Msingi unaofanikishwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF na wadau wake.   Mwenyeji wako ni Evarist Mapesa, karibu!
1/17/202410 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

Kaveh Zahedi wa FAO: Hatuwezi kuwa tu watazamaji wa mabadiliko ya tabianchi, kilimo kina jukumu

Kilimo kinaweza kuchukua jukumu kuu katika hatua dhidi ya tabianchi wakati huo huo kikihakikisha uhakika wa chakula duniani, ni maoni ya Mkurugenzi wa Ofisi ya Mabadiliko ya Tabianchi, Bayonuai na Mazingira katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) Kaveh Zahedi kufuatia hivi majuzi mwaka 2023 kuthibitishwa kuwa mwaka wa joto zaidi katika rekodi za dunia. “Kwa hivyo, rekodi hizi ni muhimu. Sasa tunahitajika kuchukua hatua sasa. Hatuwezi tu kuwa aina ya watazamaji tu wa mabadiliko ya tabianchi, na kilimo kina jukumu kuu la kutekeleza". Bwana Zahedi anaongeza kusema kwamba kilimo endelevu kinaweza kuchangia katika kufikia uzalishaji sifuri wa hewa chafuzi.“Mashamba hayapaswi tu kuwa wazalishaji wa chakula. Yanaweza kuwa vyanzo vya nishati mbadala. Nishati inaweza kutumika katika shamashamba ya ndani, kwa ajili ya kusukuma maji, kwa ajili ya umwagiliaji, au nishati ambayo inaweza kugawanywa katika gridi ya taifa, au taka za kilimo kugeuzwa kuwa nishati au nishati ya mimea. Hizi zote ni suluhisho za kilimo bora kwa nishati, na hiyo ndiyo aina ya kazi ambayo sisi FAO tumekuwa tukifanya na nchi." 
1/17/20241 minute, 18 seconds
Episode Artwork

16 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina inayomulika uhakika wa chakula, ambapo FAO imekuwa msitari wa mbele kwa miradi mbali mbali ya kuwasaidia wakulima na wafugaji kwenye mizozo ili kuhakikisha wanapunguza mzigo wa kuwa tegemezi wa msaada wa chakula. Pia tunakuletea muhtasari wa habari zikiwemo mauaji wa mlinda amani nchini CAR na sauti za jamii mashinani kama zifuatazo.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelaani mauaji ya jana Januari 15 ambapo aliuawa mlinda amani mmoja wa kutoka Cameroon aliyekuwa anahudumu katika Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati (MINUSCA) na kujeruhiwa kwa watu wengine watano, wawili kati yao wakiwa wamejeruhiwa mno kutokana na mlipuko huko Mbindali, katika Mkoa wa Ouham-Pendé, kaskazini-magharibi mwa Paoua. Huku visa vya kipindupindu vikizidi kuongezeka katika maeneo ya Kusini mwa Afrika, Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) linataka kuzingatiwa zaidi kwa watoto katika kukabiliana na kipindupindu. Janga la kipindupindu ambalo liliathiri nchi nyingi za Mashariki na Kusini mwa Afrika mwaka 2023 linaendelea kuathiri eneo hilo, na kuweka matatizo ya ziada kwa jamii na vituo vya afya.Na matumizi ya tumbaku yanaoekana kupungua licha ya juhudi za sekta ya tumbaku kuhatarisha maendeleo, imeeleza ripoti mpya iliyotolewa leo na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO. WHO inaeleza kwamba mienendo ya kuanzia mwaka 2022 inaonesha takriban mtu mzima 1 kati ya 5 duniani kote anatumia tumbaku ikilinganishwa na ilivyokuwa mwaka 2000 ambapo ilikuwa ni mtu 1 kati ya 3.  Mashinani tunakutana na Bora Meto, mkimbizi na muathirika wa unyanyasaji wa kijinsia nchini DRC akisema amepata usalama na matumaini kupitia mfuko wa dharura wa Umoja wa Mataifa CERF na ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu na Afya ya Uazi, UNFPA ambao umehakikisha usaidizi wa kimatibabu na kisaikolojia, na mafunzo ya stadi za maisha.   Mwenyeji wako ni Evarist Mapesa, karibu!
1/16/202411 minutes, 13 seconds
Episode Artwork

Wahudumu wa afya: Hali katika Hospital ya El-Najar Gaza iko nje ya uwezo wetu

Mashambulio makubwa ya mabomu, vizuizi vya kutembea, na mawasiliano yaliyovurugwa vinafanya iwe karibu kutowezekana kuwasilisha vifaa tiba mara kwa mara na kwa usalama kote Gaza, hasa kaskazini. Kupitia video iliyoratibiwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO) huko Rafar, Anold Kayanda anasimulia.
1/15/20243 minutes, 23 seconds
Episode Artwork

15 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko katika ukanda wa Gaza na Ufugaji nyukinchini Uganda. Makala tunarejea Gaza na mashinani tunakupeleka nchini Rwanda, kulikoni?Zikiwa ni zaidi ya siku 100 tangu kuibuka upya kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo wametoa taarifa inayoeleza kuongezeka kwa hatari ya baa la njaa na milipuko ya magonjwa ya kuambukiza huku yakisisitiza muarobaini pekee kwa sasa ni kuruhusu njia mpya za kuingiza misaada ya kwenda kutatua changamoto zinazowakabili wananchi walioko Gaza.Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO limewapiga jeki wafugaji wa nyuki na usindikaji wa mazao ya asali wilayani NAKAPIRIPIRIT katika jimbo la Karamoja nchini Uganda. Kwa msaada wa vifaa na mafunzo kutoka kwa shirika hilo maisha ya wafuga nyuki wa eneo hilo na familia zao yamebadilika.Makala inatupeleka Gaza ambako mashambulio makubwa ya mabomu, vizuizi vya kutembea, na mawasiliano yaliyovurugwa vinafanya iwe karibu kutowezekana kuwasilisha vifaa tiba mara kwa mara na kwa usalama kote Gaza, hasa kaskazini. Mashinani tutaelekea nchini Rwanda kusikia kuhusu usajili wa watoto wachanga punde wanapozaliwa katika kambi za wakimbizi.   Mwenyeji wako ni Evarist Mapesa, karibu!
1/15/202412 minutes, 41 seconds
Episode Artwork

UN yaomba kufunguliwe njia nyingine ya kufikisha misaada Gaza

Zikiwa ni zaidi ya siku 100 tangu kuibuka upya kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo wametoa taarifa inayoeleza kuongezeka kwa hatari ya baa la njaa na milipuko ya magonjwa ya kuambukiza huku yakisisitiza muarobaini pekee kwa sasa ni kuruhusu njia mpya za kuingiza misaada ya kwenda kutatua changamoto zinazowakabili wananchi walioko Gaza. Hii leo kutoka Geneva Uswisi na New York Marekani Mashariki manne ya UN ambayo  ni lile la Mpango wa chakula duniani WFP, Afya ulimwenguni WHO, linalohusika na masuala ya watoto UNICEF na  la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina UNRWA wametoa taarifa ya pamoja inayoeleza zahma zinazowakumba wakazi wa Gaza na nini kifanyike kuwasaidia.  WFP, ambao tangu tarehe 7 wamekuwa wakitoa Msaada wa chakula na kuweza kuwafikia zaidi ya wananchi 900,000 mpaka sasa, wanaeleza kuwa wananchi wengi wanakabiliwa na uhaba mkubwa wa chakula ambapo watu wazima wanapitisha hata siku nzima bila kula chochote ili angalau watoto waweze kuweka chochote tumboni. “Wananchi wa Gaza wapo hatarini kufa njaa wakati maili chache tu toka walipu kuna msururu wa malori yaliyojaa chakula” amesema Mkurugenzi Mkuu wa WFP Cindy McCaini ambaye pia ametoa suluhu akisema “Kila saa inayopotea tunaweka maisha mengi hatarini. Tunaweza kuzuia njaa lakini ikiwa tu tunaweza kutoa vifaa vya kutosha na pia kufikisha misaada hiyo kwa njia zilizo salama ili kula mwenye uhitaji popote alipo afikiwe.”UNICEF, Mkurugenzi Mkuu wake anasema Bi. Catherine Russell anasema watoto huko Gaza mbali na kiwewe cha milipuko na kutakiwa kuhama huku kisha kule na kujeruhiwa na kuuawa wengi wanakabiliwa na utapiamlo mkali na wengine wana uzito mdogo ikilinganishwa na urefu wao. “Watoto walio katika hatari kubwa ya kufa kutokana na utapiamlo na magonjwa wanahitaji sana matibabu, maji safi na huduma za usafi wa mazingira, lakini hali haituruhusu kuwafikia watoto na familia zao, baadhi ya misaada inayohitaji sana kuwasaidia imezuiliwa kuingia Gaza. Maisha ya watoto na familia zao yananing'inia kwenye mizani.”Mkurugenzi wa WHO Dkt.Tedros Adhanom Ghebreyesus anasema mbali na kutoa misaada ya vifaa tiba na kusaidia sekta ya afya iliyohemewa na wingi wa wagonjwa lakini wamelazimika kufungua majiko mawili katika hospital maana watu wanaumwa na wana njaa. “Watu huko Gaza wanateseka kutokana na ukosefu wa chakula, maji, dawa na ukosefu wa  huduma za afya za kutosha. Njaa itafanya hali mbaya ambayo ipo tayari kuwa janga kwa sababu wagonjwa wana uwezekano mkubwa wa kufa na njaa na watu wenye njaa wana hatari zaidi ya magonjwa. Tunahitaji ufikishaji misaada usiozuiliwa, salama wa kutoa misaada na usitishaji mapigano kwa sababu za kibinadamu ili kuzuia vifo na mateso zaidi.”Mkuu wa UNRWA Phillip Lazzarini amehitimisha taarifa hiyo ya pamoja kwa kusema misaada inayoingia Gaza ni tone la maji katika baharí ya misaada inayohitajika , ombi ni kuwa Israel iruhusu bandari ya Ashdod ambayo ipo umbali wa Km 40 tu kutoka Gaza kaskazini itumike kupitisha misaada ili waweze kuwafikia wananchi wengi wenye uhitaji. 
1/15/20243 minutes, 34 seconds
Episode Artwork

Wafugaji wa nyuki Karamoja wasema mafunzo ya FAO yamewakomboa wao na familia zao

Shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO limewapiga jeki wafugaji wa nyuki na usindikaji wa mazao ya asali wilayani Nakapiripirit katika jimbo la Karamoja nchini Uganda. Kwa  msaada wa vifaa na mafunzo kutoka kwa shirika hilo maisha ya wakulima wa asali wa eneo hilo na familia zao yamebadilika. Wilaya ya Nakapiripirit ina mamia ya wakulima wa asali wengi wakiwa katika vikundi vya kijamii na wengine wafugaji nyuki binafsi. FAO ilitambua thamani ya mazao ya asli kwa watu wa Kramoja na ikaanza kuwapa mafunzo kupitia mradi maalum wa ufugaji wa nyuki, kuanzia utundikaji mizinga, urinaji, usindikaji wa mazao ya asali na hata kuwasidia kutafuta masoko. Miongoni mwa waliokumbatia fursa hiyo ni John Lopetangor ingawa anasema si kazi rahisi, “Kuna kazi nyingi katika kuezeka mizinga ya nyuki sio watu wote wanaiweza. Kuna wadudu wanapenda kuingia katika mizinga ya nyuki na wakiingia tu hbasi nyuki wanakimbia. Na cha pili ukiwa na mizinginga ni lazima uitembelee kama vile unatembelea ng’ombe na katika mizinga ambayo haina nyuki lazima uhakikishe unajua tatizo ni nini na ufukishe moto hadi uone nyuki wameingia mzingani, usiache tu ukitegemea nyuki wataingia hapo hutopata asali. Na wakati wa ukame mizinga inapaswa kumwagiliwa maji.”Licha ya changamoto hizo John anaipenda kazi hii, “Hii kazi ni kazi ya maana kwa sababu sasa siuzi ng’ombe , siuzi mbuzi kazi yangu sasa hivi ni kuanzia mwezi wa nne mi nashika pesa mkononi tu hadi mwezi wa tisa, nasomesha sasa watoto wangu vizuri kwa sababu ya asali.”Na faida hiyo si kwa John peke yake Susan Chepsugul naye ni mfugaji binasi wa nyuki aliingia katika mradi na sasa matunda ameyaona, “Nilipouza hiyo asali nilipata fedha kidogo ikanisaidia kuweka akiba nikaenda kuongeza mizinga miwili sasa nikapata mizinga mitatu. Na ninapouza hiyo asali pia inanisaidia kulisha watoto, kulima shamba na kununulia watoto nguo. Wakati nilipolima shamba kwa kutumia hela za asali nilipata gunia moja nikaongeza mzinga mwingine nilionunua.”Kwa mujibu wa FAO mradi huu sio tu wa kuwainua kiuchumi wanajamii hawa bali pia kuhakikisha wanakuwa na mnepo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.
1/15/20242 minutes, 28 seconds
Episode Artwork

Olga muathirika wa vita Ukraine anasema bila UNHCR sijui ningekaa wapi

Kutana na Olga mwathirika wa vita inayoendelea nchini Ukraine ambaye baada ya nyumba yake kushambuliwa na kombora mjini Borodyanka alikataa tamaa ya Maisha lakini sasa mradi wa UNHCR wa kukarabati nyumba zilizoharibiwa na vita Ukraine umemfufulia matumaini ya Maisha yeye na mwanaye.  Kwa undani zaidi ungana na Flora Nducha kwa makala hii.
1/12/20243 minutes, 9 seconds
Episode Artwork

Israel yaiambia mahakama ya ICJ kwamba vita dhidi ya Hamas huko Gaza ni kitendo cha kujilinda

Israel imekanusha vikali shutuma kuwa ina nia ya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina na kusisitiza kuwa ipo katika vita ambayo wao hawakuianzisha na wala hawakuitaka kufuatia hapo jana nchi ya Afrika kusini kuwasilisha kesi mbele ya mahakama ya Umoja wa Mataifa ya kimataifa ya haki ICJ wakitaka kukomesha mauaji ya raia huko Gaza.Leo ijumaa ya tarehe 12 Januari ni siku ya pili na ya mwisho ya kusikilizwa kwa kesi ya awali katika Mahakama ICJ ambapo baada ya jana Afrika Kusini kutoa maeleo yale leo timu ya wanasheria wa Israel imesisitiza kwamba wana malengo mawili ambayo mosi ni kutokomeza tishio lililokuwepo la wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas na Pili ni kuwaachilia huru mateka 136 ambao bado wanashikiliwa katika vita inayoendelea huko mashariki ya Kati. kamanda wa Israel Tal Becker aliwaambia majaji wa ICJ huko The Hague nchini Uholanzi kuwa “Israel iko katika vita dhidi ya Hamas, sio dhidi ya watu wa Palestina” kufuatia mashambulizi ya kigaidi yaliyoongozwa na Hamas tarehe 7 Oktoba mwaka 2023. Akisoma jumbe za mwisho zilizotumwa na baba wa moja ya familia za wakulima ambao nyumba zao zilichomwa moto na watu wanaodhaniwa kuwa ni Hamas, Bwana Becker amesema “kumekuwa na mateso ya kiraia "ya kutisha" na "ya kuhuzunisha moyo" "katika vita hivi, kama katika vita vyovyote vile.”Becker pia amekataa ombi la Afrika Kusini kwa mahakama chini ya vifungu vya Mkataba wa Mauaji ya Kimbari la kutoa "hatua za muda" ili kuiamuru Israel kusimamisha mara moja shughuli zake za kijeshi huko Gaza akisema kuwa hatua hiyo ni “jaribio la kuinyima Israel uwezo wake wa kutimiza wajibu wake wa kuwalinda raia wake, mateka, na zaidi ya Waisraeli 110,000 waliokimbia makazi yao ambao hawakuweza kurejea kwa usalama makwao,”Wanasheria wa Israel wamewaeleza majaji wa ICJ kuwa nchi inaposhambuliwa, ina haki ya kujilinda yenyewe na raia wake, “Hakuna nia ya mauaji ya kimbari hapa, haya sio mauaji ya halaiki,” wakili wa Israel Malcolm Shaw aliiambia mahakama hiyo akisisitiza kuwa ukatili uliofanywa na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas “hauhalalishi ukiukwaji wa sheria katika wakujibu mashambulizi na bado ni chini ya mauaji ya halaiki - lakini unahalalisha...utekelezaji wa haki halali na ya asili ya Nchi kujilinda kama ilivyoainishwa katika Mkataba wa Umoja wa Mataifa”.Timu ya wanasheria wa Israel pia imekataa maelezo yaliyowasilishwa hapo jana na timu ya wanasheria ya Afrika kusini ikisema yana “upotoshaji sana” na kwamba wanatumia neno “Mauaji ya kimbari” kama silaha ambapo Wakili Galit Raguan aliiambia mahakama hiyo kuwa “Vita vya mijini daima vitasababisha vifo vya kusikitisha, madhara na uharibifu, lakini huko Gaza matokeo haya yasiyotakikana yanazidishwa kwa sababu ni matokeo yanayotarajiwa ya Hamas.”
1/12/20243 minutes, 4 seconds
Episode Artwork

12 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia kesi mbele ya mahakama ya Umoja wa Mataifa ya kimataifa ya haki ICJ inayotaka Israeli kukomesha mauaji ya raia huko Gaza, na haki za wanawake za unyonyeshaji. Makala tunakupeleka nchini Ukraine na mashinani nchini Kenya, kulikoni?Israel imekanusha vikali shutuma kuwa ina nia ya mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina na kusisitiza kuwa ipo katika vita ambayo wao hawakuianzisha na wala hawakuitaka kufuatia hapo jana nchi ya Afrika kusini kuwasilisha kesi mbele ya mahakama ya Umoja wa Mataifa ya kimataifa ya haki ICJ wakitaka kukomesha mauaji ya raia huko Gaza.Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto UNICEF Rwanda kwa kushirikiana na wadau kama Shirika la Taifa la Maendeleo ya Mtoto nchini humo, NCDA, wanatoa wito kwa sekta binafsi, taasisi za serikali, washirika, asasi za kiraia kuweka mazingira rafiki ya unyonyeshaji mahali pa kazi. Evarist Mapesa anaangazia faida ya moja ya vyumba vya kunyonyeshea mahali pa kazi jijini Kigali Rwanda.Makala leo inakukutanisha na Olga mwathirika wa vita inayoendelea nchini Ukraine ambaye baada ya nyumba yake kushambuliwa na kombora mjini Borodyanka alikataa tamaa ya maisha lakini sasa mradi wa UNHCR wa kukarabati nyumba zilizoharibiwa na vita Ukraine umemfufulia matumaini ya Maisha yeye na mwanaye. Mashinani inatupeleka Kakuma nchini Kenya ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula WFP limejenga ustahimilivu na uwezo wa kujitegemea miongoni mwa wakimbizi na jamii zinazowapokea, kupitia uzalishaji wa mazao na ufugaji unaohimili mabadiliko ya tabianchi”.   Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
1/12/202412 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

Wanawake Rwanda: Tunapaswa tufanye kunyonyesha mahali pa kazi kufanye kazi!

Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto UNICEF Rwanda kwa kushirikiana na wadau kama Shirika la Taifa la Maendeleo ya Mtoto nchini humo, NCDA, wanatoa wito kwa sekta binafsi, taasisi za serikali, washirika, asasi za kiraia kuweka mazingira rafiki ya unyonyeshaji mahali pa kazi. Katika moja ya maeneo tulivu ya jiji lenye shughuli nyingi za jiji la Kigali-Rwanda kumetengwa chumba eneo maalumu lenye mazingira yote yanayofaa kwa akina mama kuwanyonyesha Watoto wao au hata kukamua maziwa na kuyahifadhi. Banamwana Yvette Mfanyakazi wa Ofisi za Jiji na Kigali anasema alikuwa anapoteza muda mwingi njiani kutoka kazini kwenda kumnyonyesha mtoto na kurudi kazini.  Kayitesi Sophie mwajiriwa wa Benki ya Kigali anasema, “tulikuwa tunakamua maziwa maliwatoni na baadaye kuyamwaga kwa kuwa hatukuwa na pa kuyatunzia.” Vick Mujiji, yeye ni mfanyakazi wa kampuni ya Africa Improved Foods anaeleza kwamba kukitumia chumba cha kunyonyeshea kumeongeza tija kazini kwake kwani ofisi yake haiko mbali na hapa na kwa hivyo anaweza kuja muda wowote akakamua maziwa yake na kurejea kazini. Ingabire Assumpta ni Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Taifa la Maendeleo ya Mtoto Rwanda (NCDA) anasema, “Wengi wa watoto wanaonyonyeshwa katika saa ya kwanza mara tu baada ya kuzaliwa ni watoto wa vijijini kuliko wa mjini. Kwa hiyo ndio hiyo ilifanya tuwawezeshe wazazi kunyonyesha katika maeneo yao ya kazi. Ninawahamasisha mashirika mbalimbali ambao hawajaanzisha vyumba hivi kuanza kwani ni kwa faida yao pindi mama anapokuwa na uhakika kwamba mtoto wake amenyonya vizuri, ana afya na yuko karibu naye, atafanya kazi vizuri na tija inaongezeka.”   Baada ya mafanikio haya ya mfano, Mwakilishi wa UNICEF nchini Rwanda, Julianna Lindsey ana ujumbe, “Ujumbe wangu kwetu sote ni kwamba wanawake hawapaswi kuchagua kati ya kazi yao na kuchangia katika uchumi wa Rwanda na utimilifu wa taaluma zao dhidi ya kuhakikisha mtoto anapata lishe muhimu.” 
1/12/20242 minutes, 34 seconds
Episode Artwork

METHALI: “MSIBA WA MWENZIO NI KANDA LA USUFI”

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo Dkt. Mwanahija Ally Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA anatufafanulia maana ya methali “MSIBA WA MWENZIO NI KANDA LA USUFI”. 
1/11/20240
Episode Artwork

11 JANUARI 2024

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo mwezi Desemba mwaka jana nilihudhuria Kongamano la 8 la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU) nchini Tanzania na walifanya warsha kuhusu ChatGPT kwa wafundishaji wa lugha ya kiswahili. Dkt. Fillipo Lubua anaeleza zaidi kuhusu jambo hilo. Pia tunakuletea muhtasari wa habari na uchambuzi wa methali. Leo Afrika Kusini imezungumza mbele ya mahakama ya Umoja wa Mataifa ya kimataifa ya haki ICJ baada ya kuwasilisha kesi katika jitihada za kukomesha mauaji ya raia huko Gaza, ikiishutumu Israel kutekeleza mauaji ya kimbari dhidi ya Wapalestina madai ambayo Israel imekanusha vikali ikisema kuwa hayana msingi.Shirika la Kimataifa la Uhamiaji IOM leo limezindua mpango mkakati wake wa kimataifa wa miaka mitano mjini, N'Djamena Chad unaolenga kutimiza ahadi ya usalama, utaratibu na uhamiaji wa mara kwa mara huku ukisaidia watu walio hatarini zaidi duniani.Na Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa Misaada nchini Afghanistan UNAMA leo umesema una wasiwasi mkubwa kuhusu kukamatwa kiholela na kuzuiliwa kwa wanawake na wasichana kunakofanywa na maafisa wa serikali ya Afghanistan kwa sababu ya madai ya kutofuata kanuni za mavazi ya Kiislamu. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili nampisha Dkt. Mwanahija Ally Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA akitufafanulia maana ya methali “MSIBA WA MWENZIO NI KANDA LA USUFI”.   Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
1/11/202410 minutes
Episode Artwork

MINUSCA yachukua hatua kukabili habari potofu n aza uongo CAR

Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR kwa muda mrefu imegubikwa na mizozo ya wenyewe kwa wenyewe hususuan maeneo ya kaskazini mwa nchi. Umoja wa Mataifa umekuwa na juhudi mbalimbali za kuleta amani hadi kuwezesha kufanyika kwa uchaguzi mwaka 2016 uliomwezesha Rais wa sasa Faustin Archange Touadera kuwa madarakani. Ingawa hivyo kumekuweko na changamoto za mivutano huku kuenea kwa habari potofu na za uongo kuwa moja ya kichocheo. Kwa kutambua hilo ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MINUSCA umechukua hatua. Je ni zipi hizo? Ungana na Assumpta Massoi kwenye makala hii.  
1/10/20243 minutes, 56 seconds
Episode Artwork

10 JANUARI 2024

Jaridani leo tunaangazizia ripoti ya ajira ulimwenguni kote, na masuala ya afya nchini Botswana. Makala tunakupeleka nchini Jamhuri ya Afrika Kati, CAR. Mashinani tunaelekea Zanzibar nchini Tanzania, kulikoni?Ripoti mpya iliyotolewa leo na shirika la kazi la Umoja wa Mataifa ILO kuhusu mtazamo wa ajira na kujamii imeonya juu ya kuongezeka kwa ukosefu wa ajira kimataifa kwa mwaka huu wa 2024, sanjari na pengo la usawa na kudumaa kwa kiwango cha uzalishaji hali ambayo inaibua wasiwasi.Botswana iko njiani kutokomeza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI - VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, shukrani kwa msaada kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya WHO kanda ya Afrika wakishirikiana na mashirika ya kiraia.Makala inakupeleka Jamhuri ya Afrika Kati, CAR ambako huko Umoja wa Mataifa umechukua hatua ya kukabiliana na habari potofu, za uongo na chuki kupitia redio. Mashinani tunakuletea ujumbe wa mkulima wa mwani kutoka zanzibar nchini Tanzania kuhusu jinsi ufadhili wa Benki ya Dunia unavyoboresha ukulima wake.   Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
1/10/202411 minutes, 49 seconds
Episode Artwork

Botswana wako mstari wa mbele kutokomeza maambukizi ya VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto

Botswana iko njiani kutokomeza maambukizi ya Virusi vya UKIMWI - VVU kutoka kwa mama kwenda kwa mtoto, shukrani kwa msaada kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya WHO kanda ya Afrika wakishirikiana na mashirika ya kiraia. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi. Botswana ni moja ya nchi zinazokuwa na changamoto ya maambukizi ya VVU, mwaka 2022 wizara ya afya ya Botwasana wakishirikiana na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kanda ya Afrika na mashirika ya kiraia waliunganisha nguvu kushughulikia changamoto hiyo ambayo ilikuwa ikiwaathiri wajawazito wanaoishi na VVU kwani walikuwa hawajui mengi kuhusu haki zao ikiwemo haki ya faragha, usiri na ruhusa ya kutoa taarifa zao.WHO na wadau wengine walitoa mafunzo kwa wawakilishi 27 wa vikundi vya msaada kwa watu wanaoishi na VVU, wahudumu wa afya katika ngazi ya jamii na watu waliojitolea, na wote hawa walipewa jukumu la kuelimisha wenzao juu ya haki za binadamu, kutoa ridhaa baada ya kuarifiwa na usawa wa kijinsia kama anavyoeleza Layeza Maraya Mbulawa, Muuguzi mkuu katika Kliniki ya Thini iliyoko Tutuma nchini Botswana. “Tumepewa mafunzo ya haki za binadamu, ambayo tunayatekeleza katika ngazi ya wilaya ambapo safari hii kuna mabadiliko makubwa. Watu wanajua haki ya binadamu.”Na sasa wanawake wanaoishi na VVU wanajua zaidi kuhusu haki zao hususan kwenye masuala ya afya kama anavyoeleza mmoja wa wanufaika ambaye jina lake hatutalitaja. “Siku hizi mambo yamekuwa bora sana kwa sababu sasa najua kuhusu haki zangu na hakuna anayefanya maamuzi kwa niaba yangu na mtu unaweza kuamua unachotaka.”Kuimarisha haki ya afya ni kusaidia kuimarisha huduma bora. Afya kwa wote ni kitovu cha mapambano dhidi ya VVU nchini Bostwana.
1/10/20242 minutes, 1 second
Episode Artwork

Ripoti ya ILO: Ukosefu wa ajira duniani kuongezeka 2024 sanjari na pengo la usawa

Ripoti mpya iliyotolewa leo na shirika la kazi la Umoja wa Mataifa ILO kuhusu mtazamo wa ajira na kujamii imeonya juu ya kuongezeka kwa ukosefu wa ajira kimataifa kwa mwaka huu wa 2024, sanjari na pengo la usawa na kudumaa kwa kiwango cha uzalishaji hali ambayo inaibua wasiwasi. Ripoti hii ya mwaka 2024  iliyopewa jina Mienendo ya mtazamo wa Dunia wa ajira na kijamii 2024 imegawanyika katika sehemu kuu 4, mosi ni hali halisi ya mtazamo wa ajira duniani kote ambapo inasema ingawa kiwango cha ukosefu wa ajira na pengo katika kusaka ajira vilishuka kidogo chini ya kiwango cha kabla ya COVID-19  kutokana na mnepo uliojitokeza licha ya kuzororta kwa hali ya uchumi lakini matarajio ya kimataifa ndio yanayotia hofu kubwa.Pili ripoti hiyo ya ILO imetaja nini kinachangia hofu hii kwa mwaka 2024, kwanza ni ongezeko la migogoro mipya ambayo mingi inapunguza matarajio ya kijamii ya kupata haki za kijamii ikiwemo ajira ikisema “Mwaka huu wa 2024 wafanyikazi milioni mbili zaidi wanatarajiwa kutafuta kazi, na hivyo kuongeza kiwango cha ukosefu wa ajira duniani kutoka asilimia 5.1 mwaka 2023 hadi asilimia 5.2. Mapato yanayoweza kutumika yamepungua katika nchi nyingi Tajiri duniani za G20 na, kwa ujumla, kuporomoka kwa viwango vya maisha kunaotokana na mfumuko wa bei ambao hauna uwezekano wa kutengamaa haraka".Na pili ripoti inasema ni uwekezaji ambapo tofauti muhimu zinaendelea kati ya nchi za kipato cha juu na cha chini. Sehemu ya tatu ya ripoti ni nani waathirika wakumbwa ambapo imebainisha kuwa “Wakati kiwango cha pengo la ajira mwaka 2023 kilikuwa asilimia 8.2 katika nchi zenye kipato cha juu, kilisimama kwa asilimia 20.5 katika kundi la watu wenye kipato cha chini. Vile vile, wakati kiwango cha ukosefu wa ajira cha 2023 kiliendelea kuwa asilimia 4.5 katika nchi za kipato cha juu, kilikuwa asilimia 5.7 katika nchi za kipato cha chini.”Mwisho ripoti imeongelea kuendelea kwa umasikini hususani katika nchi za kipato cha chini kutokana na ushiriki katika soko la ajira na pengo la usawa ikisema imesema idadi ya wafanyakazi wanaoishi katika umaskini uliokithiri  ambao wanapata chini ya dola 2.15 kwa kila mtu kwa siku iliongezeka kwa takriban watu milioni 1 mwaka 2023.Pia idadi ya wafanyakazi wanaoishi katika umaskini wa wastani wakipata chini ya dola 3.65 kwa siku kwa kila mtu iliongezeka kwa watu milioni 8.4 mwaka 2023. Imeonya kwamba ukosefu wa usawa wa mapato umeongezeka, na hii "vinaashiria hali mbaya kwa mahitaji ya jumla na kujikwamua kuliko uendelevu zaidi kiuchumi.” Na katika ushiriki imesema ukosefu wa ajira kwa vijana umeendelea kuwa mtihani mkubwa hasa kwa wasichana na licha ya maendeleo ya teknolojia bado hakuna ongezeko lenye tija la ajira.Mkurugenzi mkuu wa ILO Gilbert F. Houngbo amesema “Inaanza kuonekana kana kwamba kukosekana kwa usawa huku si sehemu tu ya kujikwamua na janga la COVID-19 bali ni suala la kimuundo. Changamoto za wafanyakazi inazotambua ni tishio kwa maisha ya watu binafsi na biashara na ni muhimu kuzishughulikia kwa ufanisi na haraka.”Amesisitiza kuwa “Na bila uadilifu mkubwa wa kijamii kamwe hatutakuwa na ahueni endelevu”.
1/10/20242 minutes, 47 seconds
Episode Artwork

Kiswahili kuanza kutumika EAC rasmi mwaka 2024

Lengo namba 17 la Malengo ya Maendeleo Endelevu SDGs linataka uwepo wa Ushirikiano katika kufanikisha malengo. Ushirikiano huo unaweza kuwa baina ya nchi na nchi, wananchi na ushirikiano wa kikanda. Mwezi Desemba mwaka jana 2023 nilifunga safari hadi jijini Arusha nchini Tanzania na kuzungumza na Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt. Peter Mathuki kutaka kufahamu namna wanavyoshirikiana na Umoja wa Mataifa katika maeneo mbalimbali ikiwemo ulinzi na usalama pamoja na kukuza lugha ya Kiswahili. Karibu usikilize mazungumzo yetu. 
1/9/20247 minutes, 40 seconds
Episode Artwork

09 JANUARI 2024

Hii leo jaridani mada kwa kina tukimulika lengo namba 17 la Malengo ya Maendeleo Endelevu SDGs linataka uwepo wa Ushirikiano katika kufanikisha malengo. Ushirikiano huo unaweza kuwa baina ya nchi na nchi, wananchi na ushirikiano wa kikanda. Pia tunaangazia mzizo katika ukanda wa Gaza na Ukraine, na ripoi ya uchumi.Kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO na timu yake iliyoko huko idadi ya vifo na majeruhi Gaza kutokana na mzozo unaoendelea baina ya Israel na kundi la Hamas inaongezeka kila uchao na waathirika wakubwa ni wanawake na watoto.Ni karibu miaka miwili sasa tangu Urusi kuivamia Ukraine shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR linasema wakimbizi zaidi ya milioni sita wamefurushwa kutoka makwao nchini Ukraine ambapo Zaidi ya wakimbizi milioni 5.9 wako katika nchi mbalimbali za Ulaya.Na ripoti ya Benki ya Dunia ya matarajio ya uchumi kwa mwaka huu iliyotolewa leo ambapo takwimu zinaonyesha kuwa huu ni nusu muongo uliodorora saana katika ukuaji wa pato la taifa au GDP kwa takribani miaka 30, huku matarajio yakionyesha kushuka kwa ukuaji wa uchumi duniani kwa mwaka wa tatu mfululizo kutoka asilimia 2.6 mwaka jana hadi asilimia 2.4 mwaka huu. Mashinani tunarejea katika ukanda wa Gaza kusikiliza simulizi ya manusura wa vita baina ya Israel na kundi la Hamas.   Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
1/9/202410 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

Mradi wa IFAD umenisaidia baada ya kuathiriwa na mabadiliko ya tabianchi – Mkulima Kenya

Mradi wa kilimo endelevu unaofadhiliwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya Kilimo, IFAD na Serikali ya Kenya ambao unalenga kukuza miche ya miti na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi umeleta manufaa kwa wakulima wadogo kutoka eneo la Kaunti ya Kiambu nchini Kenya na kuboresha ukulima wao. Mkulima mdogo Francis Njoroge ni mmoja wa mamilioni ya wakulima wadogo wanaokabiliwa na athari za mabadiliko ya tabianchi lakini kwa bahati nzuri, amefaidika na Mfuko wa Upper Tana Nairobi Water Fund unaolenga kukuza miche ya miti na kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Kupitia video iliyoandaliwa na IFAD, Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anasimulia zaidi.  
1/8/20244 minutes, 4 seconds
Episode Artwork

08 JANUARI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia vita katika ukanda wa Gaza, na huduma za afya na umaskini nchini Nigeria. Makala na mashinani tunamulika ukulima bunifu na wa umwagiliaji unaosaidia wakulima wadogo kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi nchini Kenya.Ikiwa leo ni siku ya 93 tangu mapigano yaanze huko Ukanda wa Gaza kati ya jeshi la Israel na wanamgambo wa kipalestina waliojihami, likiwemo kundi la Hamas, mashirika ya Umoja wa Mataifa ya usaidizi wa kiutu yanazungumzia uwepo wa idadi kubwa ya vifo miongoni mwa wanawake na watoto huku yakisihi timu za madaktari ziruhusiwe kuingia eneo la Gaza ili ziendelee na jukumu la kuokoa maisha. Assumpta Massoi amefuatilia na kutuandalia ripoti hii.Nchini Nigeria katika Jimbo la Anambra shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kanda ya Afrika kwakushirikiana na mpango wa Bima ya Afya ya Serikali wanabadilisha maisha ya wananchi kwa kulipia sehemu kubwa ya gharama za matibabu ili kuhakikisha kila mtu anaweza kupata huduma za afya bila kudumbukia katika umaskini.Makala leo tunabisha hodi eneo la Murang’a katika kaunti ya Kiambu, nchini Kenya ambapo tunakutana na Francis Njoroge, mkulima mdogo mmoja wa mamilioni ya wakulima wadogo walioathiriwa na mabadiliko ya tabianchi lakini kupitia ufadhili wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Maendeleo ya kilimo, IFAD, anasimulia jinsi ukulima wake umeimarika. Na mashinani tunasalia nchini Kenya mada huo wa ukulima na tunakwenda Kibera, kusikia ujumbe kuhusu mbinu bunifu ya kilimo inayoleta tija kwa wakaazi.   Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
1/8/202410 minutes, 50 seconds
Episode Artwork

Hospitali zazidi kuzidiwa uwezo, wagonjwa sakafuni katika hospitali - Mzozo Gaza

Ikiwa leo ni siku ya 93 tangu mapigano yaanze huko Ukanda wa Gaza kati ya jeshi la Israel na wanamgambo wa kipalestina waliojihami, likiwemo kundi la Hamas, mashirika ya Umoja wa Mataifa ya usaidizi wa kiutu yanazungumzia uwepo wa idadi kubwa ya vifo miongoni mwa wanawake na watoto huku yakisihi timu za madaktari ziruhusiwe kuingia eneo la Gaza ili ziendelee na jukumu la kuokoa maisha.  Naanzia eneo la kati mwa Gaza ambako huko shirika la Umoja wa Mataifa la Afya, WHO limeonya kuwa madaktari katika hospitali pekee inayotoa huduma kwenye jimbo la Deir al Balah ilibidi jana Jumapili waache kutoa huduma baada ya kupokea amri ya kutakiwa kuondoka eneo hilo kutokana na mashambulizi yanayoendelea kufanywa na jeshi la Israel.  Na kwenye hospital ya Al-Aqsa ambako timu ya WHO ilipeleka vifaa vya matibabu kusaidia wagonjwa 4,500 wanaohitaji huduma ya kusafisha figo na wengine 500 wanaokabiliwa na kiwewe, idadi ya madaktari waliosalia ni watano pekee.  Kupitia mtandao wa X, Afisa wa WHO anayehusika na masuala ya dharura ya afya Sean Casey alichapisha video inayoonesha heka heka kwenye hospitali hiyo ya Al- Aqsa, wagonjwa wakiwa wamefurika sakafuni, madaktari wakiwapatia tiba hapo hapo, huku damu imetapakaa, na mamia ya wagonjwa wengine wakifikishwa hapo kwa ajili ya matibabu.  Dkt, Tedros Ghebreyesus ambaye ni Mkurugenzi Mkuu wa WHO naye kupitia mtandao wa X akasema hospitali ina mahitaij makubwa, kama vile wahudumu wa afya, vitanda lakini wafanyakazi wa Al- Aqsa wanasema jambo muhimu zaidi kwao, wagonjwa na familia ni kulindwa dhidi ya mashambulizi ya makombora na uhasama ukome.  Huku mashambulizi yakiendelea shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoot, UNICEF linasema magonjwa nayo yanashamiri kwani kila siku kuna wagonjwa wapya 3,200 wa kuhara miongoi mwa watoto wenye umri wa chini ya miaka mitano.  Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA imenukuu takwimu mpya kutoka Wizara ya Afya ya Gaza zikionesha kuwa kati ya Ijumaa na jana Jumapili wapalestina 225 wameuawa na 300 wamejeruhiwa  huku jeshi la Israel likiripotikuwa tangu lianze operesheni za ardhini, askari wake 174 wameuawa na wengine zaidi ya 1,000 wamejeruhiwa. 
1/8/20242 minutes, 16 seconds
Episode Artwork

Wananchi wa jimboni Anambra, Nigeria wapata bima ya afya kwa bei nafuu kwa usaidizi wa WHO

Nchini Nigeria katika Jimbo la Anambra shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kanda ya Afrika kwakushirikiana na mpango wa Bima ya Afya ya Serikali wanabadilisha maisha ya wananchi kwa kulipia sehemu kubwa ya gharama za matibabu ili kuhakikisha kila mtu anaweza kupata huduma za afya bila kudumbukia katika umaskini. Anambra ni jimbo la nane lenye wakazi wengi nchini Nigeria na jimbo la pili kwa idadi kubwa ya watu baada ya jimbo la Lagos. Wananchi wa jimbo hili wanachangamkia kujiandikisha katika mpango wa jimbo hilo wa bima ya afya ambapo WHO inatoa usaidizi kupitia mafunzo na miongozo ya kimkakati.Zaidi ya wananchi 225,000 wameshakata bima ya afya na Mkurugenzi Mkuu wa shirika la Bima ya Afya la jimbo la Anambra Dokta. Simeon Onyemaechi anaeleza malengo yao.“Hakuna mtu anayepaswa kuwa maskini kwa sababu anahitaji huduma ya afya. Tumewapa  wananchi ulinzi wa hatari za kifedha ili kuwaokoa kutokana na matumizi makubwa ya afya kwa njia ambayo hakuna hata mtu mmoja anayepaswa kukabiliwa na ugumu wa kifedha au kuwa maskini kwa sababu alilazimika kulipa bili kubwa za hospitali.”Mpango huu unawashirikisha viongozi wa kimila, mmoja wao ni Mfalme Ben Emeka, wa himaya ya Umueri.“Bima ya Afya ni jambo la ajabu ambalo limekuja jimbo la Anambra na limefika kwa watu wangu, watu wa Umueri, kwa sababu kabla ya sasa walikuwa wakilipa kiasi kikubwa sana.”Sio tu Mfalme Emeka anahamasisha wananchi wake kukata bima za afya lakini pia amekatia wananchi wake 300 bima ya afya na anatoa wito kwa watu wenye uwezo wa kifedha na ushawishi kufanya kama yeye.“Matajiri sasa wanaweza kuwasaidia masikini kwa kuwakatia bima za afya. Na masikini pia wanaweza kujilipia wenyewe bima za afya kwakuwa bei imekuwa nafuu.”
1/8/20242 minutes, 9 seconds
Episode Artwork

Ukiweka bidii na kuzingatia mwongozo hakuna linaloshindikana: Mary Keitany 

Mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira duniani UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya ivi karibuni yalizindua kampeni ya kuhimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora.   Kampeni hiyo maalum ilifanyika jijini Nairobi kwa kuwaalika wanaridha kadhaa wa Kenya wa zamani na wa sasa kwenye ofisi za Umoja wa mataifa. Lengo lilikuwa ni kuzungumza na wanariadha hao kuhusu uhusiano uliopo baina ya mazingira na afya bora ili wawe mabalozi wa kuchagiza hilo katika tasnia yao ambayo mara nyingi hufanyika katika maeneo ya wazi na hewa safi ni muhimu.   Miongoni wa wanariadha hao ni Mary Jepkosgei Keitany anayeshikilia rekodi kadhaa za mbio ndefu au marathoni. Amezungumza na Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi UNIS akianza kwa kutoa historia fupi ya safari yake ya riadha.
1/5/20243 minutes, 56 seconds
Episode Artwork

05 JANAURI 2024

Hii leo jaridani tunaangazia msaada wa kibinadamu na hali ya watototo katika ukanda wa Gaza, na ugonjwa wa Saratani ya shingo ya Kizazi na jinsi ambavyo inawezatibika ikigunduliwa mapema. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani tutaelekea huko Lopit nchini Sudan Kusini, kulikoni?Watoa huduma za misaada ya kibinadamu wanatoa wito wa kupatiwa fursa ya kufikisha misaada kwa haraka, kwa usalama, kiendelevu na bila vikwazo huko Kaskazini mwa Gaza, Mashariki ya Kati kwani hali ya kibinadamu inazidi kuwa tete.Mwezi huu wa januari umetangazwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Afya WHO kuwa ni mwezi wa kujenga ufahamu kuhusu ugonjwa wa Saratani ya shingo ya Kizazi.Makala inatupeleka Nairobi Kenya ambako hivi karibuni mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya yalizindua kampeni ya kuhimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora kwa kushirikisha baadhi ya wanariadha nyota wa zamani na wa sasa nchini humo. Na hapo baadaye ni mashinani na tutaelekea huko Lopit nchini Sudan Kusini kwa mnufaika wa mradi wa Umoja wa Mataifa wa kukabiliana na athari za mabadiliko tabianchi.   Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
1/5/202410 minutes, 40 seconds
Episode Artwork

Saratani ya shingo ya kizazi inatibika ikigundulika mapema – WHO

Mwezi huu wa januari umetangazwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Afya WHO kuwa ni mwezi wa kujenga ufahamu kuhusu ugonjwa wa Saratani ya shingo ya Kizazi, nami nimemualika mwenzangu Leah Mushi hapa studio ambaye amefuatilia kwa kina suala hilo kupitia wavuti wa WHO.Swali: Leah kwanza tueleze lipi hasa WHO wanalotaka wadau wafanye?Jibu: WHO inahamasisha mambo makuu 3 mosi, kutoa taarifa kuwa kuna ugonjwa huo, pili kuhimiza uchunguzi na tatu kuhamasisha chanjo. Swali: Tuanze na hilo la kwanza taarifa za ugonjwa huo?Jibu: Assumpta ningependwa kuwajuza wasikilizaji wetu kuwa 90% ya wanaougua saratani ya shingo ya kizazi ni kutoka nchi masikini na viwango vya juu vya vifo ni kutoka Afrika, Kusini mwa Jangwa la Sahara, Amerika ya Kati na Kusini-Mashariki mwa Asia. Swali: Mtu anapataje saratani hii?Jibu: WHO inasema virusi aina ya Human Papiloma (HPV) ambayo huambukizwa kwa njia ya zinaa ndio chanzo, mgonjwa asipopata matibabu au maambukizi ya mara kwa mara ya virusi hivyo vya HPV yanaweza kusababisha seli zisizo za kawaida kukua, ambazo zitaendelea kukua na kuwa saratani.Lakini pia wagonjwa wa UKIMWI wapo katika hatari mara 6 zaidi ya kupata saratani ya shingo ya kizazi. Swali: Mtu anawezaje kujikinga?Jibu: Kubwa ni kupata chanjo ya HPV na inaanza kutolewa kwa wasichana katika umri ambao bado hawajaanza kujamiiaa ndio maana inahimizwa kutolewa kuanzia umri wa miaka 9 mpaka 14.Pia kufanya uchunguzi wa kizazi, mwanamke kuanzia umri wa miaka 35 na kuendelea anapaswa angalau mara 2 kwa mwaka kwenda kufanya uchunguzi. Swali: Tiba sasa ni nini?Jibu: ukigundulika tiba ni zile za wagonjwa wa saratani kama vile upasuaji, tiba ya mionzi na tibakemikali ili kutoa huduma pamoja na udhibiti wa maumivu.
1/5/20241 minute, 59 seconds
Episode Artwork

Uwasilishaji misaada kaskazini mwa Gaza umezuiliwa na vizingiti vya kufikisha misaada ya kibinadamu

Wasaidizi wa kibinadamu wanatoa wito wa fursa ya ufikishaji misaada kwa haraka, salama, endelevu na usiozuiliwa kaskazini mwa Gaza kwani hali ya binadamu inazidi kuwa tete. Umoja wa Mataifa na wadau wengine wa misaada ya kibinadamu wameshindwa kutoa msaada unaohitajika haraka wa kuokoa maisha kaskazini mwa Wadi Gaza kwa siku nne kutokana na ucheleweshaji na kukataliwa, pamoja na migogoro inayoendelea imeeleza Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura OCHA katika taarifa yake iliyokusanya takwimu za hadi jana Jan 4 na kuchapishwa leo Jan 5.  Hii ni pamoja na dawa ambazo zingetoa msaada muhimu kwa zaidi ya watu 100,000 kwa siku 30, pamoja na lori nane za chakula kwa watu ambao kwa sasa wanakabiliwa na uhaba wa chakula unaohatarisha maisha.  Kwa upande wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF), linasema maelfu ya watoto tayari wamekufariki dunia kutokana na ukatili huo unaoendelea, huku hali ya maisha kwa watoto ikiendelea kuzorota kwa kasi. "Watoto huko Gaza wanakumbwa na jinamizi ambalo linazidi kuwa baya kila kukicha," anasema Catherine Russell, Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF na kuongeza kuwa, “Watoto na familia katika Ukanda wa Gaza wanaendelea kuuawa na kujeruhiwa katika mapigano, na maisha yao yanazidi kuwa hatarini kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuilika na ukosefu wa chakula na maji.” Anatoa wito kwamba watoto na raia wote lazima walindwe dhidi ya unyanyasaji na kupata huduma za kimsingi. Nalo Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) linaeleza kamba tangu tarehe 24 Desemba 2023, limethibitisha mashambulizi manane kwenye hospitali ya Al-Amal, mashambulizi yaliyoua watu 7 na kujeruhi 11. Mashambulizi ya karibu zaidi ni ya jana Januari 4. Tangu Oktoba 7 mwaka jana, WHO imethibitisha mashambulio 590 dhidi ya huduma za afya katika ardhi ya Palestina inayokaliwa kwa mabavu.  Pamoja na hali hii ngumu, wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa wanaendelea kusaidia watu katika kila hali inavyowezekana ijapokuwa ni katika hali hatarishi. Kufikia juzi tarehe 3 Januari, jumla ya wafanyakazi 142 wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina (UNRWA) wameuawa tangu kuanza kwa mapigano hapo Oktoba 7.  
1/5/20241 minute, 50 seconds
Episode Artwork

Methali: Mla mbegu huvuna vya wenyewe

Karibu kujifunza Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mla mbegu huvuna vya wenyewe.”
1/4/20241 minute, 41 seconds
Episode Artwork

04 JANUARI 2024

Karibu kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa, miongoni wa tuliyokuandalia  ni pamoja na mada kwa kina itakayokupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kumsikia manusura wa ukatili wa kingono. Lakini kabla ya hiyo utasikia Muhtasari wa Habari na kama ilivyo ada ya kila alhamisi tunajifuza lugha ya kiswahili na leo mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mla mbegu huvuna vya wenyewe.” Mwenyeji wako ni Leah Mushi
1/4/202411 minutes, 7 seconds
Episode Artwork

Kipaji cha sarakasi chamwezesha mkimbizi kutoka DRC kupata elimu bora Uganda

Umoja wa Mataifa unapazia sauti suala la vijana kutumia vipaji vyao ili kuweza kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu .SDGs. Mmoja wa walioitikia wito huo ni mkimbizi kutoka mjini Bukavu jimboni Kivu Kusini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambaye baada ya kuwasili ukimbizini nchini Uganda, kipaji chake cha kucheza sarakasi kimemwezesha kupata elimu bora na hivyo kuwa na uhakika wa ustawi wake na familia yake. Ni kwa vipi kipaji hicho kimemsaidia? John Kibego wa Redio washirika Kazi Njema FM iliyoko Hoima nchini Uganda amezungumza na kijana huyo.  
1/3/20244 minutes, 7 seconds
Episode Artwork

Si haki kutumia gesi ya Nitrojeni Hypoxia kumuua Kenneth - Wasema wataalam wa UN

Wataalamu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa akiwemo Alice Jill Edwards, anayeshughulikia masuala yanayohusu mateso, na Adhabu nyingine za Kikatili, za kinyume cha utu au za Kushusha hadhi, leo Januari 3 mjini Geneva-Uswisi wameelezea wasiwasi wao kuhusu kukaribia kutekelezwa kwa hukumu ya kifo kwa kutumia gesi ya nitrojeni hypoxia dhidi ya Kenneth Eugene Smith hapa nchini Marekani. Mwenzangu Anold Kayanda amekifuatilia kisa hicho kwa kina… ASSUMPTA: Anold hukumu ya kifo bado inatekelezwa katika maeneo kadha duniani, ni kwa nini hii ya sasa inafuatiliwa zaidi? ANOLD: Assumpta hilo ni swali muhimu hasa na jibu ni kuwa utekelezaji huu wa hukumu ya kifo umepangwa kufanyika kwa kutumia gesi ya Nitrojeni hypoxia ambapo huyu Kenneth Eugine Smith atanyimwa hewa ya Oksijeni lakini atapewa nafasi ya kuvuta hiyo gesi ambayo ndiyo itamuua. Sasa wataalamu hawa wa haki za binadamu wanasema kwa kuwa jambo hili halijawahi kujaribiwa  hapo awali, kwa hivyo utekelezaji unaweza kumfanya anayeuawa atendewe ukatili, unyama au udhalilishaji au hata kuteswa na kwamba hakuna ushahidi wa kisayansi wa kuthibitisha vinginevyo. ASSUMPTA: Nikikurudisha nyuma kidogo, huyu anayetarajiwa kuuawa kwa njia hii alifanya kosa gani? Smith alipatikana na hatia ya kuua kwa kukodiwa mwaka wa 1988 na kuhukumiwa kifungo cha maisha bila msamaha kwa kura 11 za kukubali na 1 ya kupinga. Hata hivyo, hakimu aliyetoa hukumu alipuuza pendekezo la jopo la mahakama la kifungo cha maisha na akamhukumu kifo. ASSUMPTA: Na mwisho ikiwa hukumu hii itatekelezwa, ni lini? ANOLD: Kenneth Smith, ambaye amekuwa akisubiri kunyongwa kwa zaidi ya miaka thelathini, amepangwa kunyongwa Januari hii tarehe 25, 2024, katika Jimbo la Alabama hapa Marekani. Mamlaka huko Alabama hapo awali zilijaribu kumuua Smith mnamo Novemba mwaka juzi 2022 kwa kutumia sindano ya sumu, lakini jaribio hilo lilishindikana kwa hiyo na hili ni la kusubiri kuona.   
1/3/20242 minutes, 1 second
Episode Artwork

UN yasema inashikamana na Japan wakati huu taifa hilo limekumbwa na tetemeko kubwa la ardhi

Harakati zikiendelea za kunasua watu waliokwama kwenye vifusi kufuatia tetemeko kubwa la ardhi lililokumba eneo la kati mwa Japan Jumatatu alasiri kwa saa za huko na kusababisha vifo vya watu 62, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameelezea masikitiko yake kufuatia tetemeko hilo lililokuwa na ukubwa wa 7.6 katika kipimo cha Richa. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah MushiMsemaji wa Umoja wa Mataifa Florencia Soto Nino aliwaambia waandishi wa habari mjini New York, Marekani kwamba, “Katibu mkuu amehuzunishwa sana na taarifa za vifo na uharibifu wa mali uliosababishwa na tetemeko. Na ameelezea mshikamano wake na serikali ya Japan na watu wa Japan. Ametuma pia salamu za rambirambi kwa familia za waliopoteza maisha na kutakia ahueni ya haraka majeruhi.” Vyombo vya  habari vinaripoti ya kuwa zaidi ya waokoaji 3,000 wamefika eneo la tukio ambalo ni katikati mwa Japan kwa ajili ya kunasua watu waliokwama kwenye vifusi huku moto ukiripotiwa kulipuka kwenye eneo hilo. Kitovu cha tetemeko hilo ni rasi ya Noto, katikati mwa Honshu ambacho ndio kisiwa kikubwa nchini Japan kinachojumuisha maeneo kama vile Tokyo, Kyoto, Osaka na Hiroshima. Bi. Soto Nino amezungumzia pia ajali ya ndege ya shirika la ndege la Japan na ndege iliyokuwa inaelekea kutoa msaada eneo la tetemeko la ardhi ambapo abiria wote kwenye ndege walinusurika ilhali wafanyakazi watano wa ndege ya misaada wamepoteza maisha. “Mawazo yetu kwa sasa yako na wananchi wa Japan na tunatumai kuwa wataweza kujikwamua kwenye hili.” 
1/3/20241 minute, 36 seconds
Episode Artwork

03 JANUARI 2024

Hii leo kwenye jarida la Habari za Umoja wa Mataifa tunamulika tetemeko la ardhi nchini Japan; Matumizi ya gesi aina ya Naitrojeni Hypoxia kuua mfungwa; Makala ni jinsi sarakasi ilivyomwezesha kijana mkimbizi kupata unafuu wa malipo na mashinani tunakwenda Afar nchini Ethiopia.Harakati zikiendelea za kunasua watu waliokwama kwenye vifusi kufuatia tetemeko kubwa la ardhi lililokumba eneo la kati mwa Japan Jumatatu alasiri kwa saa za huko na kusababisha vifo vya watu 62, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameelezea masikitiko yake kufuatia tetemeko hilo lililokuwa na ukubwa wa 7.6 katika kipimo cha Richa. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi.Wataalamu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa akiwemo Alice Jill Edwards, anayeshughulikia masuala yanayohusu mateso, na Adhabu nyingine za Kikatili, za kinyume cha utu au za Kushusha hadhi, leo Januari 3 mjini Geneva-Uswisi wameelezea wasiwasi wao kuhusu kukaribia kutekelezwa kwa hukumu ya kifo kwa kutumia gesi ya nitrojeni hypoxia dhidi ya Kenneth Eugene Smith hapa nchini Marekani. Mwenzangu Anold Kayanda amekifuatilia kisa hicho kwa kinaMakala: John Kibego, mwandishi wa redio washirika Kazi Njema FM huko Hoima nchini Uganda anazungumza na mkimbizi kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, ambaye kipaji chake cha kucheza sarakasi kimwezesha kupata elimu bora. Mashinani: Mama Fatuma, kutoka eneo la Afar, nchini Ethiopia ambaye mwanaye Fatuma ni mnufaika wa huduma za afya ya msingi ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia watoto, UNICEF, kwa jamii za wafugaji kuipitia kliniki tembezi ambayo inahakikisha kumfikia kila mama na kila mtoto popote alipo. 
1/3/20249 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

02 JANUARI 2024

Heir ya mwaka mpya 2024 na leo katika jarida letu la kwanza kabisa kwa mwaka huu tunakuletea Habari kwa Ufupi, Mada kwa Kina ikielelea Tanzania na Mashinani tunajikita Kenya. Mwenyeji wako ni Leah Mushi.Habari kwa ufupi: Tetemeko la ardhi Japan; Mashambulizi Ukraine; Mwezi wa Januari kuhamasisha kuhusu saratani ya shingo ya kizazi.Mada Kwa kina: Jinsi gani Umoja wa Mataifa kupitia mfuko wake wa maendeleo ya kilimo, IFAD imesaidia watu wa jamii ya wahadzabe nchini Tanzania kuhimili madhara ya mabadiliko ya tabianchi.Mashinani: Mratibu wa shirika lisilo la Kiserikali la Center for the Study of Adolescents, linaloendesha programu ya She Leads, lengo lao likiwa ni kuongeza ushawishi endelevu kwa wasichana na wanawake vijana katika kufanya maamuzi na mabadiliko ya kanuni za kijinsia katika kusongesha lengo namba 5 la Umoja wa Mataifa la usawa wa kijinsia.. 
1/2/20249 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

Mfumo wa AFCAFIM unaoratibiwa na IFAD wawezesha wakulima Kenya kuhimili mabadiliko ya tabianchi

Kwa miaka 45, mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo , IFAD umekuwa ukifadhili wakulima wadogo wadogo na maendeleo vijijini. IFAD inakuwa kama mratibu kwa kushirikiana na benki binafsi na sasa kuna mfumo wa fedha wa kuwezesha wakulima Afrika kukabiliana na kuhimili madhara ya mabadiliko ya tabianchi au ARCAFIM. Mfumo huo umewezesha kupatikana kwa dola milioni 700 za uwekezaji kutoka sekta binafsi kwenye kwa wakulima wadogo huko Kenya, Rwanda, Tanzania na Uganda, ili kutokomeza umaskini na njaa katika maeneo ya vijijini ya nchi zinazoendelea. Je, ni kwa jinsi gani wameweza kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi? Kupitia video iliyoandaliwa na IFAD, Pamela Awuori wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amefuatilia  mafanikio ya wakulima wadogo wadogo nchini Kenya, ungana naye. 
12/29/20232 minutes, 40 seconds
Episode Artwork

Nchini Niger ILO yanusuru wanawake na mfumo wa utumwa

12/29/20232 minutes, 16 seconds
Episode Artwork

Ili kusaidia kukabili mapigano mashariki mwa nchi, kikosi cha kwanza cha SADC chawasili DRC

12/29/20231 minute, 37 seconds
Episode Artwork

29 DESEMBA 2023

Miongoni mwa yaliyomo kwenye Jarida la Habar iza UN:Kikosi cha kwanza cha SADC chawasili DRC.ILO yanusuru wanawake na mfumo wa utumwa nchini Niger.Makala leo tunakwenda Kenya kumulika jinsi mfumo wa fedha wa kuwezesha wakulima kukabiliana na kuhimili madhara ya mabadiliko ya tabianchi.Na mashinani na fursa ni yake Agnes Abisa, Afisa Habari na Mawasiliano wa YUNA ambayo ni Jumuiya ya Vijana ya Umoja wa Mataifa nchini Tanzania.
12/29/20239 minutes, 59 seconds
Episode Artwork

28 DESEMBA 2023

Hujambo na karibu kusikiliza jarida kutoka Idhaa ya Kiswahili  ya Umoja wa Mataifa ikiwa ni Alhamisi ya tarehe 28  ya  mwezi Desemba takribani siku 4 panapo majaliwa kuumaliza mwaka huu wa 2023. Mimi ni ASSUMPTA MASSOI ninakukaribisha kusikiliza mkusanyiko wa matukio machache kati ya mengi yaliyojiri katika mwaka huu ambapo Umoja wa Mataifa ulikuwa na jukumu zito kuhakikisha pamoja na yote bado dunia inasalia kuwa mahali salama pa kuishi. 
12/28/202314 minutes, 9 seconds
Episode Artwork

Zaidi ya wakazi 500 Beni, DRC wanufaika na matibabu bure kutoka MONUSCO

Mjini Beni jimboni Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC takribani watu 500 wamenufaika na matibabu ya bure yanayotolewa na walinda aman iwa Umoja wa Mataifa kutoka India, wanaohudumu kwenye ujumbe wa umoja huo wa kulinda amani nchini humo MONUSCO.  Evarist Mapesa na taarifa zaidi.Miongoni mwa wanufaika hao ni Samson Muvu, Mkuu wa kitongoji cha Paida hapa mjini Beni, akizungumza kupitia video ya MONUSCO akiwa kwenye kituo cha matibabu kinachoendeshwa na walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka India anaelezea vile ambavyo waliagizwa na mkuu wa kitongoji cha Ruwenzori kwenda kuhamasisha watu kufika hapa kupata matibabu ya bure.Bwana Muvu anasema, "nikaona na mimi kama kiongozi nije nipate dawa kwa sababu mwili hauko vizuri. »Mwingine ni Kamate Masika ambaye anasema, "mimi ni mkimbizi kutoka Mbao Oicha, Niko hapa Beni. Tangu ile vita ya kila siku wanachinja watu, mimi nasikia mwili unachoka, na mishipa yote inauma. Sina amani. Wakati Niko hapa mwili unaendelea kuuma ndio jirani yangu akanionesha jinsi ya usaidizi wa dawa iko MONUSCO kwani yeye amepata yake. Na ndio niliamua kuja ili nitunzwe.”Kamate alipata pia msongo wa mawazo na kiwewe kwani alishuhudia jamaa zake pia wakichinjwa.Anne- Marie Kave anasema ni mara ya pili amefika hapa. Awali alikwenda kwingineko na kulipa jumla ya dola 180. Anasema jambo jema ni kwamba “nilipofika hapa dawa ya bure ya askari. Naamini nitalima. Nitafanya kazi ya shamba. Sikufanya kazi ya shamba kutokana na maumivu ya kiuno.”Dkt. Kowsalya mlinda amani huyu wa MONUSCO kutoka India ni mshauri mtabibu na anasema “watu wanakuja hapa na magonjwa ya kawaida kama vile Mafua, Malaria, homa ya matumbo, maumivu ya mgongo, kichwa, kisukari na moyo. Tunawapatia matibabu na wanaridhika pian a matibabu.”
12/27/20232 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

Fahamu jinsi Nukta Fakti ilivyosaidia lishe bora kwa watoto kupitia mtandao

Leo katika makala tunakwenda Tanzania kuzungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya habari na teknolojia ya Nukta Afrika Nuzulack Dausen  ambaye pia mwanzilishi wa Jiko point inayojihusisha zaidi na utoaji habari sahihi kuhusu uhakika wa chakula na lishe, jambo ambalo linapigiwa upatu kila uchao na Umoja wa Mataifa. Amezungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam na Stella Vuzo afisa habari wa Umoja wa Mataifa kufahamu kwa undani wanachokifanya katika kutimiza azma hiyo na anaanza kwa kueleza Jiko point ni nini hasa?
12/27/20233 minutes, 22 seconds
Episode Artwork

DRC: Asante MONUSCO kwa kuniepusha kuwa mpiganaji msituni

Bila MONUSCO ningalikuwa bado msituni – Mpiganaji wa zamani DRCNchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, kazi ya kuhesabu kura za Rais kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 20 na kuendelea katika maeneo mengine siku zilizofuata, inaendelea huku nao wanufaka wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO ambao umeanza kufunga virago, wakitoa shukrani zao. Ufafanuzi zaidi anakupataia Anold Kayanda.Tume ya Huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini DRC, CENI, inaendelea kutangaza matokeo ya Urais halikadhalika matokeo ya magavana, wabunge na madiwani, huku mshindi wa kiti cha Urais akitarajiwa kutangazwa tarehe 31 mwezi huu wa Desemba.Kwingineko nchini humo hususan jimboni Kivu Kaskazini, MONUSCO inaanza kufunga ofisi zake kwa mujibu wa azimio la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kufuatia ombi la serikali.Ofisi ya hivi karibuni zaidi kufungwa ni ile ya Lubero jimboni humo ambako Gentil Kakule Kombi alishukuru uwepo wa MONUSCO kwenye eneo hilo kwa miaka 21.Amesema ni kwa msaada wa MONUSCO nilitoka porini, nikasalimisha silaha na sasa nimetulia vema kabisa kwenye jamii yangu na ninashikiri kwenye harkati za ujenzi wa amani.”Anakumbuka MONUSCO kumpokea Rutshuru na kisha kusafirishwa kwa basi na kukabidhiwa kwa serikali ambako walipatiwa program ya kujumuishwa tena kwenye jamii.Gentil alijisalimisha mwaka 2015 na sasa ni mwanachama wa klabu ya soka ya Lubero inayocheza kwenye ligi ya jimbo la Kivu Kaskazini. 
12/27/20231 minute, 31 seconds
Episode Artwork

27 DESEMBA 2023

Hii leo jarida linajikita barani Afrika likianzia Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kuangazia uchaguzi, wapiganaji wa zamani na MONUSCO, halikdhalika Jiko Point na mashinani ni nchini Kenya.Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, kazi ya kuhesabu kura za Rais kufuatia uchaguzi mkuu uliofanyika tarehe 20 na kuendelea katika maeneo mengine siku zilizofuata, inaendelea huku nao wanufaka wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO ambao umeanza kufunga virago, wakitoa shukrani zao. Ufafanuzi zaidi anakupataia Anold Kayanda.Mjini Beni jimboni Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC takribani watu 500 wamenufaika na matibabu ya bure yanayotolewa na walinda aman iwa Umoja wa Mataifa kutoka India, wanaohudumu kwenye ujumbe wa umoja huo wa kulinda amani nchini humo MONUSCO. Evarist Mapesa anafafanua zaidi.Makala: Leo inatupeleka Tanzania kuzungumza na Mkurugenzi Mtendaji wa kampuni ya habari na teknolojia ya Nukta Afrika Nuzulack Dausen  ambaye pia mwanzilishi wa Jiko point inayojihusisha zaidi na utoaji habari sahihi kuhusu uhakika wa chakula na lishe, jambo ambalo linapigiwa upatu kila uchao na Umoja wa Mataifa. Amezungumza hivi karibuni jijini Dar es Salaam na Stella Vuzo afisa habari wa Umoja wa Mataifa kufahamu kwa undani wanachokifanya katika kutimiza azma hiyo na anaanza kwa kueleza Jiko point ni nini hasa?Mashinani: Tutaelekea katika Kaunti ya Turkana nchini Kenya, kumsikia mvuvi ambaye ameweza kuongeza kipato chake na kupunguza upotevu wa chakula kwa msaada wa Umoja wa Mataifa 
12/27/20239 minutes, 57 seconds
Episode Artwork

Baada ya mashambulizi kutoka CODECO maisha yarejea hali ya kawaida huko Fataki, Ituri

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kazi ya kuhesabu kura inaendelea baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatano na kuendelea katika baadhi ya maeneo jana Alhamisi, huku ikielezwa kwamba jimboni Ituri, maisha  yamerejea katika hali ya kawaida kwenye eneo la Fataki baada ya mwaka mmoja wa mashambulizi kutoka kwa wanamgambo waliojihami wa kundi la CODECO. Radio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO imegusia zaidi kituo cha biashara cha FATAKI kilichoko mji mkuu wa Ituri, Bunia ambako CODECO kwa mwaka mzima walikuwa wakishambulia mara kwa mara. Mathalani mwezi Mei mwaka huu, CODECO walishambulia eneo la Djugu na kuua raia 38, hali iliyosababisha wakazi wengine kukimbilia eneo la Djahiba lililoko kilometa 5 kutoka kituo cha MONUSCO. Sababu ya maisha kurejea kwenye hali ya kawaida ni doria za magari na za miguu zinazofanywa na askari wa jeshi la serikali, FARDC na walinda amani wa MONUSCO kwenye eneo hilo. Usalama umeimarika, wakazi wanaendelea na biashara sambamba na ukulima mashambani. Wakati huo huo, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini DRC, CENI imesema kazi ya kupiga kura kwenye maeneo yaliyoshindwa kufanya hivyo imekamilika jana Alhamisi na kwamba hakuna eneo lolote lile lililopiga kura leo Ijumaa. Matokeo rasmi ya uchaguzi wa Rais yanatarajiwa kutangazwa tarehe 31 mwezi huu na kisha Rais mteule ataapishwa tarehe 24 Januari mwaka 2024. 
12/22/20230
Episode Artwork

Baada ya mashambulizi kutoka CODECO maisha yarejea hali ya kawaida huko Fataki, Ituri

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kazi ya kuhesabu kura inaendelea baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatano na kuendelea katika baadhi ya maeneo jana Alhamisi, huku ikielezwa kwamba jimboni Ituri, maisha  yamerejea katika hali ya kawaida kwenye eneo la Fataki baada ya mwaka mmoja wa mashambulizi kutoka kwa wanamgambo waliojihami wa kundi la CODECO. Radio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO imegusia zaidi kituo cha biashara cha FATAKI kilichoko mji mkuu wa Ituri, Bunia ambako CODECO kwa mwaka mzima walikuwa wakishambulia mara kwa mara. Mathalani mwezi Mei mwaka huu, CODECO walishambulia eneo la Djugu na kuua raia 38, hali iliyosababisha wakazi wengine kukimbilia eneo la Djahiba lililoko kilometa 5 kutoka kituo cha MONUSCO. Sababu ya maisha kurejea kwenye hali ya kawaida ni doria za magari na za miguu zinazofanywa na askari wa jeshi la serikali, FARDC na walinda amani wa MONUSCO kwenye eneo hilo. Usalama umeimarika, wakazi wanaendelea na biashara sambamba na ukulima mashambani. Wakati huo huo, Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini DRC, CENI imesema kazi ya kupiga kura kwenye maeneo yaliyoshindwa kufanya hivyo imekamilika jana Alhamisi na kwamba hakuna eneo lolote lile lililopiga kura leo Ijumaa. Matokeo rasmi ya uchaguzi wa Rais yanatarajiwa kutangazwa tarehe 31 mwezi huu na kisha Rais mteule ataapishwa tarehe 24 Januari mwaka 2024. 
12/22/20231 minute, 20 seconds
Episode Artwork

22 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia uchaguzi mkuu nchini DRC na hali ya usalama katika ukanda wa Gaza.  Makala tuankuletea ujumbe wa mwanariadha Violah Cheptoo kutoka Kenya na mashinani tuankupeleka nchini Tanzania kusikia ujumbe kuhusu mazingira na haki za watoto. Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kazi ya kuhesabu kura inaendelea baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatano na kuendelea katika baadhi ya maeneo jana Alhamisi, huku ikielezwa kwamba jimboni Ituri, maisha  yamerejea katika hali ya kawaida kwenye eneo la Fataki baada ya mwaka mmoja wa mashambulizi kutoka kwa wanamgambo waliojihami wa kundi la CODECO.Njaa imeukumba Ukanda wa Gaza kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO na hivyo kutishia ongezeko la magonjwa hususan miongoni mwa watoto, kina mama wajawazito na wanaonyonyesha na makundi mengine yaliyo hatarini na nishati ya kupikia nayo imeota mbawa.Katika makala Assumpta Massoi anazungumza na mwanariadha wa kimataifa kutoka Kenya wakati alipotembelea hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani mwezi Novemba mwaka huu kwani Umoja wa Mataifa unapigia chepuo michezo kwa afya, ustawi na amani. Mashinani tutaelekea nchini Tanzania kusikia ujumbe kuhusu haki za Watoto.   Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/22/20230
Episode Artwork

22 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia uchaguzi mkuu nchini DRC na hali ya usalama katika ukanda wa Gaza.  Makala tuankuletea ujumbe wa mwanariadha Violah Cheptoo kutoka Kenya na mashinani tuankupeleka nchini Tanzania kusikia ujumbe kuhusu mazingira na haki za watoto. Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kazi ya kuhesabu kura inaendelea baada ya uchaguzi mkuu uliofanyika Jumatano na kuendelea katika baadhi ya maeneo jana Alhamisi, huku ikielezwa kwamba jimboni Ituri, maisha  yamerejea katika hali ya kawaida kwenye eneo la Fataki baada ya mwaka mmoja wa mashambulizi kutoka kwa wanamgambo waliojihami wa kundi la CODECO.Njaa imeukumba Ukanda wa Gaza kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO na hivyo kutishia ongezeko la magonjwa hususan miongoni mwa watoto, kina mama wajawazito na wanaonyonyesha na makundi mengine yaliyo hatarini na nishati ya kupikia nayo imeota mbawa.Katika makala Assumpta Massoi anazungumza na mwanariadha wa kimataifa kutoka Kenya wakati alipotembelea hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani mwezi Novemba mwaka huu kwani Umoja wa Mataifa unapigia chepuo michezo kwa afya, ustawi na amani. Mashinani tutaelekea nchini Tanzania kusikia ujumbe kuhusu haki za Watoto.   Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/22/20239 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

WHO inaonya kwamba njaa inaongezeka Gaza hakuna chakula wala nishati ya kupikia na kukaribisha magonjwa zaidi

Njaa imeukumba Ukanda wa Gaza kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO na hivyo kutishia ongezeko la magonjwa hususan miongoni mwa watoto, kina mama wajawazito na wanaonyonyesha na makundi mengine yaliyo hatarini na nishati ya kupikia nayo imeota mbawa. Majira ya mchana mlo unandaliwa katika eneo la Rafah kwa ajili ya wakimbizi wa ndani wakishuhudia kwa hamu kubwa na zana zao mikononi mabakuli , vikombe na hata masufuria. Mlo wenyewe ni uji unaopikwa katika masufuria makubwa na kwa ukosefu wa gesi unapikwa kwenye kuni ambazo sasa ni adimu na ndio nishati pekee inayotegemewa.WHO inaonya kwamba Gaza inakabiliwa na viwango vikubwa vya ukosefu wa chakula na kila siku kuwa hatarini kukumbwa na baa la njaa. Watu hawa hawana chochote kama anavyoema mmoja wa wapishi ambaye pia ni mkimbizi wa ndani,“Vita hii imetudhalilisha kwa kiwango kisichoelezeka, Tunataabika na kudhalilika ili tu tupate mmlo wa mchana. Maisha hapa yamekuwa ghali sana hatuwezi kumudu, hatuli, hatunywi wala kulala vizuri na hakuna kinachopatikana.”Uji sasa tayari na unaanza kugawiwa, mwenye kikombe, mwenye bakuli haya ili mradi kila mtu anagombea maana huenda huu ndio mlo pekee atakaoupata kwa siku hii watu ni wengi. Mpishi huyu anaongeza, “Inachukua dadika 45 kwenda kwa mguu kufuata chakula hii na dakika 45 zingine kurudi ili nipike na kuwagawia , sijui nisema nini zaidi , hali ni ngumu sana.”Katika baadhi ya mitaa ya Rafah kuna vitu vichache vinavyouzwa kama vile vyakula vya makopo na barabarani kina mama na baba lishe wanajitahidi kupika wakipatacho na kuuza. Mkimbizi huyu wa ndani aliyekuja kununua chakula hicho anasema “Leo hii tuko katika hali mbya sana kwenye makazi ya muda, kuna vurugu, machafuko na mambo yasiyowezekana, sisi si watu wabaya , hata msaada wa chakula unaotolewa na UNRWA na mashirika mengine ni gharama kuuandaa na kupika kuliko hata thamani yake. Watu hawawezi kununua au kuandaa chakula kutokana na ukosefu wa gesi.”Wakimbizi hawa wa ndani wanasema watoto wao wengi sasa ni wagonjwa wana mafua, kukohoa matatizo ya tumbo na huduma ni haba. Mafuta pia hayapatikani  wenye magari sasa wakilazimika kujaza matanki yao kwa mabaki ya mafuta ya kupikia  na si salama kwa afya zao.Kwa mujibu wa WHO kuna wagonjwa zaidi ya 100,000 wa kuhara Gaza tangu katikati ya Oktoba na nusu yao ni watoto wa umri wa chini ya miaka 5 na pia kuna wagonjwa zaidi ya 150,000 wa magonjwa ya mfumo wa hewa, lakini pia uti wa mgongo, upele, wenye chawa na tetekuanga.
12/22/20230
Episode Artwork

WHO inaonya kwamba njaa inaongezeka Gaza hakuna chakula wala nishati ya kupikia na kukaribisha magonjwa zaidi

Njaa imeukumba Ukanda wa Gaza kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO na hivyo kutishia ongezeko la magonjwa hususan miongoni mwa watoto, kina mama wajawazito na wanaonyonyesha na makundi mengine yaliyo hatarini na nishati ya kupikia nayo imeota mbawa. Majira ya mchana mlo unandaliwa katika eneo la Rafah kwa ajili ya wakimbizi wa ndani wakishuhudia kwa hamu kubwa na zana zao mikononi mabakuli , vikombe na hata masufuria. Mlo wenyewe ni uji unaopikwa katika masufuria makubwa na kwa ukosefu wa gesi unapikwa kwenye kuni ambazo sasa ni adimu na ndio nishati pekee inayotegemewa.WHO inaonya kwamba Gaza inakabiliwa na viwango vikubwa vya ukosefu wa chakula na kila siku kuwa hatarini kukumbwa na baa la njaa. Watu hawa hawana chochote kama anavyoema mmoja wa wapishi ambaye pia ni mkimbizi wa ndani,“Vita hii imetudhalilisha kwa kiwango kisichoelezeka, Tunataabika na kudhalilika ili tu tupate mmlo wa mchana. Maisha hapa yamekuwa ghali sana hatuwezi kumudu, hatuli, hatunywi wala kulala vizuri na hakuna kinachopatikana.”Uji sasa tayari na unaanza kugawiwa, mwenye kikombe, mwenye bakuli haya ili mradi kila mtu anagombea maana huenda huu ndio mlo pekee atakaoupata kwa siku hii watu ni wengi. Mpishi huyu anaongeza, “Inachukua dadika 45 kwenda kwa mguu kufuata chakula hii na dakika 45 zingine kurudi ili nipike na kuwagawia , sijui nisema nini zaidi , hali ni ngumu sana.”Katika baadhi ya mitaa ya Rafah kuna vitu vichache vinavyouzwa kama vile vyakula vya makopo na barabarani kina mama na baba lishe wanajitahidi kupika wakipatacho na kuuza. Mkimbizi huyu wa ndani aliyekuja kununua chakula hicho anasema “Leo hii tuko katika hali mbya sana kwenye makazi ya muda, kuna vurugu, machafuko na mambo yasiyowezekana, sisi si watu wabaya , hata msaada wa chakula unaotolewa na UNRWA na mashirika mengine ni gharama kuuandaa na kupika kuliko hata thamani yake. Watu hawawezi kununua au kuandaa chakula kutokana na ukosefu wa gesi.”Wakimbizi hawa wa ndani wanasema watoto wao wengi sasa ni wagonjwa wana mafua, kukohoa matatizo ya tumbo na huduma ni haba. Mafuta pia hayapatikani  wenye magari sasa wakilazimika kujaza matanki yao kwa mabaki ya mafuta ya kupikia  na si salama kwa afya zao.Kwa mujibu wa WHO kuna wagonjwa zaidi ya 100,000 wa kuhara Gaza tangu katikati ya Oktoba na nusu yao ni watoto wa umri wa chini ya miaka 5 na pia kuna wagonjwa zaidi ya 150,000 wa magonjwa ya mfumo wa hewa, lakini pia uti wa mgongo, upele, wenye chawa na tetekuanga.
12/22/20231 minute, 56 seconds
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili: Tofouti ya matumizi ya "Habari kwa ufupi na Muhtasari wa habari"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua tofauti ya maneno “HABARI KWA UFUPI NA MUHTASARI WA HABARI”
12/21/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili: Tofouti ya matumizi ya "Habari kwa ufupi na Muhtasari wa habari"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua tofauti ya maneno “HABARI KWA UFUPI NA MUHTASARI WA HABARI”
12/21/20231 minute, 2 seconds
Episode Artwork

21 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo mwezi Agosti mwaka huu wa 2023, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kutangaza tarehe 21 mwezi Desemba kila mwaka kuwa siku ya mpira wa kikapu duniani. Hii ni kwa kutambua nafasi ya mchezo huu katika kuleta amani, maendeleo na ustawi wa jamii. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na ufafanuzi wa tofouti ya maneno. Mashirika ya Umoja wa Mataifa leo yameendelea kusisitiza wito wa usitishwaji mapigano Gaza kwani hali inazidi kuwa mbaya kila uchao, lile la afya duniani WHO limesema timu yake ilifanikiwa kufika katika hospitali za Al Ahil Arab na Al Shifa Gaza kaskasini na uharibifu walioushuhudia hauelezeki. Dkt. Richard Peeperkorn akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswisi hii leo amesema “Wafanyikazi wetu wanakosa maneno ya kuelezea hali mbaya zaidi inayowakabili wagonjwa na wahudumu wa afya waliobaki katika hospitali hizo..Takriban watu 300,000 wamefungasha virago na kukimbia katika mji wa pili kwa ukubwa nchini Sudan wa Wad Madani kwenye jimbo la Aj Jazirah kwa mujibu wa shirika la umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM kufuatia wimbi jipya la mapigano ambayo pia yametawanya maelfu ya watu ndani ya jimbo hilo.Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC hapo jana watu wapatao milioni 44 walijitokeza kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na wawakilishi wa serikali za mitaa. Rais wa tume ya uchaguzi nchini humo CENI Denis Kadima amesema wale wote walioshindwa kupiga kura jana kwa sababu mbalimbali ikiwemo mvua leo wamepiga kura zao na matokeo ya awali yameanza kubandikwa katika baadhi ya vituo huku zoezi la kuhesabu kura likiendelea nchi nzima.. Katika kujifunza Kiswahili leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua tofauti ya maneno. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/21/20230
Episode Artwork

21 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo mwezi Agosti mwaka huu wa 2023, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio la kutangaza tarehe 21 mwezi Desemba kila mwaka kuwa siku ya mpira wa kikapu duniani. Hii ni kwa kutambua nafasi ya mchezo huu katika kuleta amani, maendeleo na ustawi wa jamii. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na ufafanuzi wa tofouti ya maneno. Mashirika ya Umoja wa Mataifa leo yameendelea kusisitiza wito wa usitishwaji mapigano Gaza kwani hali inazidi kuwa mbaya kila uchao, lile la afya duniani WHO limesema timu yake ilifanikiwa kufika katika hospitali za Al Ahil Arab na Al Shifa Gaza kaskasini na uharibifu walioushuhudia hauelezeki. Dkt. Richard Peeperkorn akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswisi hii leo amesema “Wafanyikazi wetu wanakosa maneno ya kuelezea hali mbaya zaidi inayowakabili wagonjwa na wahudumu wa afya waliobaki katika hospitali hizo..Takriban watu 300,000 wamefungasha virago na kukimbia katika mji wa pili kwa ukubwa nchini Sudan wa Wad Madani kwenye jimbo la Aj Jazirah kwa mujibu wa shirika la umoja wa Mataifa la uhamiaji IOM kufuatia wimbi jipya la mapigano ambayo pia yametawanya maelfu ya watu ndani ya jimbo hilo.Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC hapo jana watu wapatao milioni 44 walijitokeza kupiga kura katika uchaguzi mkuu wa Rais, wabunge na wawakilishi wa serikali za mitaa. Rais wa tume ya uchaguzi nchini humo CENI Denis Kadima amesema wale wote walioshindwa kupiga kura jana kwa sababu mbalimbali ikiwemo mvua leo wamepiga kura zao na matokeo ya awali yameanza kubandikwa katika baadhi ya vituo huku zoezi la kuhesabu kura likiendelea nchi nzima.. Katika kujifunza Kiswahili leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua tofauti ya maneno. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/21/202310 minutes, 59 seconds
Episode Artwork

UN: Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Binadamu ni kusherehekea Umoja wetu katika tofauti zetu

DAFI, Mfuko wa Ufadhili wa Kimasomo kwa Wakimbizi, kwa kushirikiana na UNHCR wanawasaidia wakimbizi kutimiza ndoto zao za kupata elimu ya juu katika nchi ya kwanza wanakopata hifadhi baada ya kuzikimbia nchi zao. Idadi ya waliokwisha kunufaika na ufadhili wa DAFI inazidi kuongezeka lakini takwimu za hivi karibuni zinaonesha angalau hadi kufikia mwaka jana 2022 DAFI ilipotimiza miaka 30 tangu kuanziswa kwake, chini ya serikali ya Ujerumani na wadau wengine, tayari imewafadhili wakimbizi zaidi ya 24,000 kusoma elimu za juu iwe vyuo vikuu au vyuo vingine vya ujuzi.Kwa leo tuchukue mfano mdogo tu wa nchini Rwanda. DAFI imewasaidia zaidi ya wanafunzi wakimbizi 500 tangu mwaka 2010 nchini humo. Wanafunzi 154 kati yao hivi sasa wanasoma katika ngazi ya chuo kikuu. Tuchukue wawili tu kuwawakilisha wengine mmoja anamalizia na mwingine ameshahitimu.Eric Nshizirungu, mkimbizi kutoka DR Congo mkazi wa Kambi ya wakimbizi Kiziba nchini Rwanda yuko katika mwaka wake wa mwisho wa masomo akisoma Ufamasia katika Chuo Kikuu cha Rwanda, kampasi ya Remera, "Nia yangu katika masomo yanayohusiana na afya ni kwa sababu kadhaa kama vile kukulia katika kambi ya wakimbizi, kukabiliwa na changamoto nyingi ambapo afya inafunikwa na majanga mengine ya kibinadamu kama vile chakula, malazi na mengine. Kwa hiyo, niliendeleza azma hiyo kwamba siku moja hata kama sitafanikiwa nikiwa kambini, labda nitafanikiwa nikiwa sehemu nyingine, lakini nitaisaidia jamii katika masuala ya afya.”Francois Mbyirukira, naye kutoka DRC, mkazi wa Kigali lakini mwenyeji wa Kambi ya wakimbizi ya Kigeme, kusini mwa Rwanda. Baada ya kuhitimu masomo, akaanzisha biashara yake ya samani: Viti, makochi, meza, masofa mazuri, vyote unapata kwake, “Nilichagua kusomea manunuzi kwa sababu yanaendana na kile ambacho nimekuwa nikifanya kuanzia zabuni hadi ugavi. Yote ni kuhusu kufanya biashara. Kwa maoni yangu, udhamini wa DAFI umefanya kazi kubwa sana. DAFI ilinijengea kujiamini. Leo ninafanya biashara mjini Kigali. Biashara yangu imepanuka sana.”Naam hayo ni matunda ya wanadamu walio katika hali nzuri walioamua kushikamana na walio katika shida kama inavyokumbusha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Kibinadamu kuwa ni siku ya kusherehekea umoja wetu katika utofauti wetu. Mnamo mwaka 2005, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa azimio namba 60/209 lilitambua mshikamano kama moja ya tunu za kimsingi na za ulimwengu ambazo zinapaswa kuwa msingi wa uhusiano kati ya watu katika karne ya 21 na kwa maana hiyo Baraza likaamua kuitangaza tarehe 20 Desemba ya kila mwaka kuwa ya Mshikamano wa Binadamu.
12/20/20230
Episode Artwork

UN: Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Binadamu ni kusherehekea Umoja wetu katika tofauti zetu

DAFI, Mfuko wa Ufadhili wa Kimasomo kwa Wakimbizi, kwa kushirikiana na UNHCR wanawasaidia wakimbizi kutimiza ndoto zao za kupata elimu ya juu katika nchi ya kwanza wanakopata hifadhi baada ya kuzikimbia nchi zao. Idadi ya waliokwisha kunufaika na ufadhili wa DAFI inazidi kuongezeka lakini takwimu za hivi karibuni zinaonesha angalau hadi kufikia mwaka jana 2022 DAFI ilipotimiza miaka 30 tangu kuanziswa kwake, chini ya serikali ya Ujerumani na wadau wengine, tayari imewafadhili wakimbizi zaidi ya 24,000 kusoma elimu za juu iwe vyuo vikuu au vyuo vingine vya ujuzi.Kwa leo tuchukue mfano mdogo tu wa nchini Rwanda. DAFI imewasaidia zaidi ya wanafunzi wakimbizi 500 tangu mwaka 2010 nchini humo. Wanafunzi 154 kati yao hivi sasa wanasoma katika ngazi ya chuo kikuu. Tuchukue wawili tu kuwawakilisha wengine mmoja anamalizia na mwingine ameshahitimu.Eric Nshizirungu, mkimbizi kutoka DR Congo mkazi wa Kambi ya wakimbizi Kiziba nchini Rwanda yuko katika mwaka wake wa mwisho wa masomo akisoma Ufamasia katika Chuo Kikuu cha Rwanda, kampasi ya Remera, "Nia yangu katika masomo yanayohusiana na afya ni kwa sababu kadhaa kama vile kukulia katika kambi ya wakimbizi, kukabiliwa na changamoto nyingi ambapo afya inafunikwa na majanga mengine ya kibinadamu kama vile chakula, malazi na mengine. Kwa hiyo, niliendeleza azma hiyo kwamba siku moja hata kama sitafanikiwa nikiwa kambini, labda nitafanikiwa nikiwa sehemu nyingine, lakini nitaisaidia jamii katika masuala ya afya.”Francois Mbyirukira, naye kutoka DRC, mkazi wa Kigali lakini mwenyeji wa Kambi ya wakimbizi ya Kigeme, kusini mwa Rwanda. Baada ya kuhitimu masomo, akaanzisha biashara yake ya samani: Viti, makochi, meza, masofa mazuri, vyote unapata kwake, “Nilichagua kusomea manunuzi kwa sababu yanaendana na kile ambacho nimekuwa nikifanya kuanzia zabuni hadi ugavi. Yote ni kuhusu kufanya biashara. Kwa maoni yangu, udhamini wa DAFI umefanya kazi kubwa sana. DAFI ilinijengea kujiamini. Leo ninafanya biashara mjini Kigali. Biashara yangu imepanuka sana.”Naam hayo ni matunda ya wanadamu walio katika hali nzuri walioamua kushikamana na walio katika shida kama inavyokumbusha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Kibinadamu kuwa ni siku ya kusherehekea umoja wetu katika utofauti wetu. Mnamo mwaka 2005, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kwa azimio namba 60/209 lilitambua mshikamano kama moja ya tunu za kimsingi na za ulimwengu ambazo zinapaswa kuwa msingi wa uhusiano kati ya watu katika karne ya 21 na kwa maana hiyo Baraza likaamua kuitangaza tarehe 20 Desemba ya kila mwaka kuwa ya Mshikamano wa Binadamu.
12/20/20233 minutes, 22 seconds
Episode Artwork

UNICEF Tanzania: Chanjo ya polio sio tu inamlinda mtoto bali inaokoa maisha

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linahimiza kila nchi kuhakikisha watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wanapatiwa chanjo dhidi ya polio ugonjwa ambao sio tu unasababisha ulemavu kwa watoto lakini pia ukakatili maisha yao. Kwa msaada kutoka wakfu wa Bill na Melinda gates hivi karibuni UNICEF na shirika la afya duniani WHO nchini Tanzania walizindua kampeni kubwa ya chanjo dhidi ya ugonjwa huo iliyowafikia watoto zaidi ya milioni 4. Kutana na Therezia Kaminda muhudumu wa afya ya jamii miongoni mwa wahudu wengi walioshiriki kampeni hii chanjo ya nchi nzima mjini Sumbawanga mkoani Rukwa Magharibi mwa Tanzania na anapita nyumba kwa nyumba kutoa chanjo hiyo, "Kitu kinachonifurahisha kabisa ni uelewa walio nao wananchi wangu wameelewa vizuri na wameipokea chanjo hii kwa furaha”.Kwa mujibu wa WHO kila ambukizi 1 kati ya 200 ya polio husababisha ugonjwa wa kupooza ambao hauwezi kubadilishwa na asilimia 5-10 miongoni mwa waliopooza hupoteza maisha. Pascal ni mzazi ameelimika kuhusu ugonjwa huu na amewapeleka mwanawe kupata chanjo sasa anataka elimu zaidi itolewe, “Polio ni ugonjwa unaowapata watoto wa umri wa miaka 15 kushuka chini na una athari kubwa sana, kwa hiyo ni lazima watu waendelee kuelemishwa ili wawapeleke watoto ili wapatiwe chanjo. Watoto wangu wote chanjo walipata hata kuna wakati walitoa kwa watu wazima na hata chanjo ya Corona mimi nilipata”Lengo la kampeni hii ya siku nne ni kumlinda kila mtoto na kwa Terezia uelewa kuhusu chanjo ni kitu cha msingi zaidi, “Kabla ya hata ya kuwapa chanjo kwanza huwa nataka nifahamu wanafahamu nini kuhusu chanjo hii, lakini pia nawapa elimu kwa sababu siwezi kujua kama wote wameshapata tarifa au nini.”Katika kampeni hiyo ya kuhakikisha kila mtoto anafikiwa na chanjo, watoto zaidi ya milioni 4.2 walipokea chanjo ya matone dhidi ya polio.
12/20/20230
Episode Artwork

UNICEF Tanzania: Chanjo ya polio sio tu inamlinda mtoto bali inaokoa maisha

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linahimiza kila nchi kuhakikisha watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wanapatiwa chanjo dhidi ya polio ugonjwa ambao sio tu unasababisha ulemavu kwa watoto lakini pia ukakatili maisha yao. Kwa msaada kutoka wakfu wa Bill na Melinda gates hivi karibuni UNICEF na shirika la afya duniani WHO nchini Tanzania walizindua kampeni kubwa ya chanjo dhidi ya ugonjwa huo iliyowafikia watoto zaidi ya milioni 4. Kutana na Therezia Kaminda muhudumu wa afya ya jamii miongoni mwa wahudu wengi walioshiriki kampeni hii chanjo ya nchi nzima mjini Sumbawanga mkoani Rukwa Magharibi mwa Tanzania na anapita nyumba kwa nyumba kutoa chanjo hiyo, "Kitu kinachonifurahisha kabisa ni uelewa walio nao wananchi wangu wameelewa vizuri na wameipokea chanjo hii kwa furaha”.Kwa mujibu wa WHO kila ambukizi 1 kati ya 200 ya polio husababisha ugonjwa wa kupooza ambao hauwezi kubadilishwa na asilimia 5-10 miongoni mwa waliopooza hupoteza maisha. Pascal ni mzazi ameelimika kuhusu ugonjwa huu na amewapeleka mwanawe kupata chanjo sasa anataka elimu zaidi itolewe, “Polio ni ugonjwa unaowapata watoto wa umri wa miaka 15 kushuka chini na una athari kubwa sana, kwa hiyo ni lazima watu waendelee kuelemishwa ili wawapeleke watoto ili wapatiwe chanjo. Watoto wangu wote chanjo walipata hata kuna wakati walitoa kwa watu wazima na hata chanjo ya Corona mimi nilipata”Lengo la kampeni hii ya siku nne ni kumlinda kila mtoto na kwa Terezia uelewa kuhusu chanjo ni kitu cha msingi zaidi, “Kabla ya hata ya kuwapa chanjo kwanza huwa nataka nifahamu wanafahamu nini kuhusu chanjo hii, lakini pia nawapa elimu kwa sababu siwezi kujua kama wote wameshapata tarifa au nini.”Katika kampeni hiyo ya kuhakikisha kila mtoto anafikiwa na chanjo, watoto zaidi ya milioni 4.2 walipokea chanjo ya matone dhidi ya polio.
12/20/20232 minutes, 17 seconds
Episode Artwork

Uchaguzi mkuu mwaka 2023 nchini DRC wafanyika kama ilivopangwa

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, uchaguzi mkuu wa Rais, Magavana, wabunge na madiwani umefanyika hii leo kama ilivyopangwa licha ya changamoto zilizojitokeza katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. Asante Flora. Ni kweli uchaguzi umefanyika kama ilivyopangwa kwani Radio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO imesema vituo vya kupigia kura vilifunguliwa saa 12 asubuhi kama ilivyopangwa, ingawa kwingine vilichelewa kufunguliwa kwa dakika kadhaa kwa sababu tofauti tofauti.  Mathalani kwenye mji mkuu Kinshasa baadhi ya vituo hadi leo asubuhi kwa saa za DRC havikuwa vimepokea vifaa vya uchaguzi.  Katika vituo vya Somba ne Lutulu huko Tshikapa, jimbo la Kasaï, upigaji kura ulianza kama ilivyopangwa licha ya mvua kubwa iliyoanza kunyesha saa moja asubuhi kwa saa za huko.  Mvua imeripotiwa kusababisha upelekaji vifaa vya upigaji kura kuanza asubuhi huko eneo la Mbuji-Mayi.  Huko jimboni Ituri, wakimbizi wa ndani walioko Mudzipela mjini Bunia, walivamia kituo cha kupigia kura na kuharibu vifaa vya kwa kuchukizwa na uamuzi wa CENi wa kuwataka wakapigie kura kwenye makazi yao huko Djugu.  Wapiga kura milioni 44 walijiandikisha kupiga kura kuchagua viongozi wao ambapo wagombea wa nafasi ya urais ni 20 akiwemo rais wa sasa Felix Tshisekedi anayesaka awamu ya pili.  Mchakato wa uchaguzi umekuwa na changamoto ikiwemo usafirishaji wa vifaa kwenye maeneo ya mashariki mwa nchi ambako jeshi la serikali linakabiliana na vikundi vilivyojihami.  Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini DRC, CENI iliomba MONUSCO isaidie usafirishaji wa vifaa na ombi liliitikiwa huku Katibu Mkuu wa UN Antonio Guterres akisihi mazingira yawe rafiki ili kila mwenye haki ya kupiga au kupigiwa kura afanye hivyo bila vitisho vyovyote.  Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi iliyotolewa CENI, matokeo yatatangazwa tarehe 31 mwezi huu wa Desemba na Rais mteule ataapishwa tarehe tarehe 24 mwezi Januari 2024. 
12/20/20230
Episode Artwork

Uchaguzi mkuu mwaka 2023 nchini DRC wafanyika kama ilivopangwa

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, uchaguzi mkuu wa Rais, Magavana, wabunge na madiwani umefanyika hii leo kama ilivyopangwa licha ya changamoto zilizojitokeza katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. Asante Flora. Ni kweli uchaguzi umefanyika kama ilivyopangwa kwani Radio Okapi ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini DRC, MONUSCO imesema vituo vya kupigia kura vilifunguliwa saa 12 asubuhi kama ilivyopangwa, ingawa kwingine vilichelewa kufunguliwa kwa dakika kadhaa kwa sababu tofauti tofauti.  Mathalani kwenye mji mkuu Kinshasa baadhi ya vituo hadi leo asubuhi kwa saa za DRC havikuwa vimepokea vifaa vya uchaguzi.  Katika vituo vya Somba ne Lutulu huko Tshikapa, jimbo la Kasaï, upigaji kura ulianza kama ilivyopangwa licha ya mvua kubwa iliyoanza kunyesha saa moja asubuhi kwa saa za huko.  Mvua imeripotiwa kusababisha upelekaji vifaa vya upigaji kura kuanza asubuhi huko eneo la Mbuji-Mayi.  Huko jimboni Ituri, wakimbizi wa ndani walioko Mudzipela mjini Bunia, walivamia kituo cha kupigia kura na kuharibu vifaa vya kwa kuchukizwa na uamuzi wa CENi wa kuwataka wakapigie kura kwenye makazi yao huko Djugu.  Wapiga kura milioni 44 walijiandikisha kupiga kura kuchagua viongozi wao ambapo wagombea wa nafasi ya urais ni 20 akiwemo rais wa sasa Felix Tshisekedi anayesaka awamu ya pili.  Mchakato wa uchaguzi umekuwa na changamoto ikiwemo usafirishaji wa vifaa kwenye maeneo ya mashariki mwa nchi ambako jeshi la serikali linakabiliana na vikundi vilivyojihami.  Tume Huru ya Taifa ya Uchaguzi nchini DRC, CENI iliomba MONUSCO isaidie usafirishaji wa vifaa na ombi liliitikiwa huku Katibu Mkuu wa UN Antonio Guterres akisihi mazingira yawe rafiki ili kila mwenye haki ya kupiga au kupigiwa kura afanye hivyo bila vitisho vyovyote.  Kwa mujibu wa ratiba ya uchaguzi iliyotolewa CENI, matokeo yatatangazwa tarehe 31 mwezi huu wa Desemba na Rais mteule ataapishwa tarehe tarehe 24 mwezi Januari 2024. 
12/20/20231 minute, 47 seconds
Episode Artwork

20 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia uchaguzi mkuu nchini DRC, na kampeni ya chanjo ya polio nchini Tanzania. Makala tunamulika DAFI Scholarship Programme nchini Rwanda na mashinani tutaelekea Mkoani Kigoma, nchini Tanzania kumsikia kijina mbunifu wa majiko yanayopunguza hewa ukaa.Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, uchaguzi mkuu wa Rais, Magavana, wabunge na madiwani umefanyika hii leo kama ilivyopangwa licha ya changamoto zilizojitokeza katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. Assumpta Massoi amefuatiliana na kutuandalia ripoti hii.Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linahimiza kila nchi kuhakikisha watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wanapatiwa chanjo dhidi ya polio ugonjwa ambao sio tu unasababisha ulemavu kwa watoto lakini pia ukakatili maisha yao.Katika makala ambayo kwa kuzingatia kuwa leo ni Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Binadamu, Anold Kayanda anaangazia ‘DAFI Scholarship Programme’ ambao ni Mfuko wa Ufadhili wa Kimasomo kwa ajili ya wakimbizi unaopewa nguvu na Serikali ya Ujerumani kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR). Mashinani tunakupeleka Mkoani Kigoma, nchini Tanzania kumsikia kijina mbunifu wa majiko yanayopunguza hewa ukaa.  Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
12/20/20230
Episode Artwork

20 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia uchaguzi mkuu nchini DRC, na kampeni ya chanjo ya polio nchini Tanzania. Makala tunamulika DAFI Scholarship Programme nchini Rwanda na mashinani tutaelekea Mkoani Kigoma, nchini Tanzania kumsikia kijina mbunifu wa majiko yanayopunguza hewa ukaa.Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, uchaguzi mkuu wa Rais, Magavana, wabunge na madiwani umefanyika hii leo kama ilivyopangwa licha ya changamoto zilizojitokeza katika maeneo mbalimbali ya nchi hiyo. Assumpta Massoi amefuatiliana na kutuandalia ripoti hii.Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linahimiza kila nchi kuhakikisha watoto wote wenye umri wa chini ya miaka 5 wanapatiwa chanjo dhidi ya polio ugonjwa ambao sio tu unasababisha ulemavu kwa watoto lakini pia ukakatili maisha yao.Katika makala ambayo kwa kuzingatia kuwa leo ni Siku ya Kimataifa ya Mshikamano wa Binadamu, Anold Kayanda anaangazia ‘DAFI Scholarship Programme’ ambao ni Mfuko wa Ufadhili wa Kimasomo kwa ajili ya wakimbizi unaopewa nguvu na Serikali ya Ujerumani kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR). Mashinani tunakupeleka Mkoani Kigoma, nchini Tanzania kumsikia kijina mbunifu wa majiko yanayopunguza hewa ukaa.  Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
12/20/202311 minutes, 5 seconds
Episode Artwork

19 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo kesho nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ni uchaguzi mkuu ikiwa ni tamati ya kampeni huku Umoja wa Mataifa kupitia ujumbe wake wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO umeshiriki kwa kusafirisha sio tu vifaa vya uchaguzi lakini pia kuelimisha wananchi jinsi ya kukabili na kuzia habari potofu na za uongo kwani ni tisho la amani na usalama. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Leo Umoja wa Mataifa umeonya kwamba Gaza ni mahali hatari zaidi kuishi kwa watoto. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, James Elder amesema, “Siku baada ya siku ukatili wa hali ya juu unadhihirika. Katika saa 48 zilizopita hospitali kubwa Zaidi iliyobaki inafanyakazi imeshambuliwa mara mbili...Nchini Sudan shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR leo limesema linatiwa wasiwasi kubwa na kiwango cha janga la watu wanaoendelea kulazimika kutawanywa ndani ya Sudan na katika nchi Jirani.Na ripoti mpya "Hali ya mifumo ya chakula duniani kote katika kuelekea mwaka  2030", iliyochapishwa leo na mradi wa shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa FAO unaoangia mifumo hiyo kuelekea ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu ifikapo mwaka 2030 (FSCI), inatoa tathimini ya kwanza ya ufuatiliaji wa kisayansi ili kuwaongoza watoa maamuzi wanapotaka kufanya mabadiliko ya jumla ya kilimo cha kimataifa na mifumo ya chakula. Mashinani tunakupeleka nchini Somalia kusikia ujumbe kuhusu uwezo wa filamu katika simulizi ya hadithi za utamaduni na haki za binadamu.  Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/19/20230
Episode Artwork

19 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo kesho nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ni uchaguzi mkuu ikiwa ni tamati ya kampeni huku Umoja wa Mataifa kupitia ujumbe wake wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO umeshiriki kwa kusafirisha sio tu vifaa vya uchaguzi lakini pia kuelimisha wananchi jinsi ya kukabili na kuzia habari potofu na za uongo kwani ni tisho la amani na usalama. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Leo Umoja wa Mataifa umeonya kwamba Gaza ni mahali hatari zaidi kuishi kwa watoto. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF, James Elder amesema, “Siku baada ya siku ukatili wa hali ya juu unadhihirika. Katika saa 48 zilizopita hospitali kubwa Zaidi iliyobaki inafanyakazi imeshambuliwa mara mbili...Nchini Sudan shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR leo limesema linatiwa wasiwasi kubwa na kiwango cha janga la watu wanaoendelea kulazimika kutawanywa ndani ya Sudan na katika nchi Jirani.Na ripoti mpya "Hali ya mifumo ya chakula duniani kote katika kuelekea mwaka  2030", iliyochapishwa leo na mradi wa shirika la chakula na kilimo la Umoja wa Mataifa FAO unaoangia mifumo hiyo kuelekea ukomo wa malengo ya maendeleo endelevu ifikapo mwaka 2030 (FSCI), inatoa tathimini ya kwanza ya ufuatiliaji wa kisayansi ili kuwaongoza watoa maamuzi wanapotaka kufanya mabadiliko ya jumla ya kilimo cha kimataifa na mifumo ya chakula. Mashinani tunakupeleka nchini Somalia kusikia ujumbe kuhusu uwezo wa filamu katika simulizi ya hadithi za utamaduni na haki za binadamu.  Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/19/202311 minutes, 15 seconds
Episode Artwork

Wanazuoni waanza utafiti wa kupunguza maneno ya kigeni katika lugha ya kiswahili

Wakati wadau wa lugha ya kiswahili wakikuna vichwa namna ya kuhakikisha lugha hiyo adhimu inasambaa na kuzungumzwa duniani kote, wengine wanaendelea na utafiti kuhakikisha lugha hiyo inakuwa na maneno ya kiswahili fasaha na kupunguza mchanganyiko wa maneno ya kigeni katika lugha hiyo. Leah Mushi aliyehudhuria Kongamano la Kimataifa la Kiswahili lililoandaliwa na Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili duniani – CHAUKIDU huko jijini Arusha nchini Tanzania ameketi chini na mwanazuoni huyo na kutuandalia makala haya. 
12/18/20230
Episode Artwork

Wanazuoni waanza utafiti wa kupunguza maneno ya kigeni katika lugha ya kiswahili

Wakati wadau wa lugha ya kiswahili wakikuna vichwa namna ya kuhakikisha lugha hiyo adhimu inasambaa na kuzungumzwa duniani kote, wengine wanaendelea na utafiti kuhakikisha lugha hiyo inakuwa na maneno ya kiswahili fasaha na kupunguza mchanganyiko wa maneno ya kigeni katika lugha hiyo. Leah Mushi aliyehudhuria Kongamano la Kimataifa la Kiswahili lililoandaliwa na Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili duniani – CHAUKIDU huko jijini Arusha nchini Tanzania ameketi chini na mwanazuoni huyo na kutuandalia makala haya. 
12/18/20234 minutes, 36 seconds
Episode Artwork

18 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia vita katika ukanda wa Gaza, na mradi wa UNHC kwa wakimbizi Kigoma Tanzania.  Makala tunakuletea mahojiano ya Wanazuoni na wataalamu wa lugha ya Kiswahili na mashinani leo ikiwa ni siku ya wahamiaji duniani tunakupeleka nchini Uganda kupata ujumbe mahsusi.Hali ya kibinadamu inazidi kuwa mbayá katika Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati, huku hospitali zilizosalia zikiendelea kushambuliwa na kukatili maisha ya watu na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet vikizidisha adha yameonya leo mashirika ya Umoja wa Mataifa..Nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kushirikiana na wadau wamewezesha kaya zinazopakana na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma kujitengenezea mkaa mbadala na hivyo kusaidia kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na ukataji miti kwa ajili ya mkaa.Makala tunakwenda mkoani Arusha kaskazini mwa Tanzania kunakofanyika kongamano la kimataifa la Kiswahili. Wanazuoni na wataalamu wa lugha ya Kiswahili ambayo ni moja kati ya lugha 10 zinazo zungumzwa zaidi duniani wameanza kufanya utafiti wa kupunguza maneno ya kigeni katika lugha hiyo.. Mashinani leo ikiwa ni siku ya wahamiaji duniani tunakupeleka nchini Uganda kupata ujumbe mahsusi.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/18/20230
Episode Artwork

18 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia vita katika ukanda wa Gaza, na mradi wa UNHC kwa wakimbizi Kigoma Tanzania.  Makala tunakuletea mahojiano ya Wanazuoni na wataalamu wa lugha ya Kiswahili na mashinani leo ikiwa ni siku ya wahamiaji duniani tunakupeleka nchini Uganda kupata ujumbe mahsusi.Hali ya kibinadamu inazidi kuwa mbayá katika Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati, huku hospitali zilizosalia zikiendelea kushambuliwa na kukatili maisha ya watu na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet vikizidisha adha yameonya leo mashirika ya Umoja wa Mataifa..Nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kushirikiana na wadau wamewezesha kaya zinazopakana na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma kujitengenezea mkaa mbadala na hivyo kusaidia kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na ukataji miti kwa ajili ya mkaa.Makala tunakwenda mkoani Arusha kaskazini mwa Tanzania kunakofanyika kongamano la kimataifa la Kiswahili. Wanazuoni na wataalamu wa lugha ya Kiswahili ambayo ni moja kati ya lugha 10 zinazo zungumzwa zaidi duniani wameanza kufanya utafiti wa kupunguza maneno ya kigeni katika lugha hiyo.. Mashinani leo ikiwa ni siku ya wahamiaji duniani tunakupeleka nchini Uganda kupata ujumbe mahsusi.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/18/202313 minutes, 16 seconds
Episode Artwork

Kaya Kigoma wameweza kuinua kipato na pia kutunza mazingira kupitia Mradi wa UNHCR

Nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kushirikiana na wadau wamewezesha kaya zinazopakana na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma kujitengenezea mkaa mbadala na hivyo kusaidia kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na ukataji miti kwa ajili ya mkaa. Mkoani Kigoma, kaskazini magharibi mwa Tanzania, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kupitia shirika la Denmark la kuhudumia wakimbizi, DRC wamefanikisha mradi wa kusaidia jamii kutengeneza mkaa kwa kutumia mabaki ya mahindi, maranda, mihogo na mawese.  Wanufaika wa mafunzo yaliyotolewa na DRC ni Kikundi cha Tubadilike kinachojihusisha na uchakati wa malighafi za kutengeneza mkaa kilichoko kijiji cha Mvugwe, wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.  Ayoub Juma Shaban, ni Mwenyekiti wa kikundi hicho ambaye amesema walipatiwa mafunzo ya kutengeneza mkaa huo ambapo wanachanganya maranda ya mbao, magunzi ya mahindi na hutumia mabaki ya unga wa muhogo wa ajili ya kugandisha mkaa huo.  Amesema wanatumia mkaa mbadala kama njia ya kuhifadhi mazingira. Badala ya kukata miti sasa wanatumia mabaki kutengeneza mkaa.  Mkaa huo wanauza ujazo wa ndoo ya lita 10 kwa shilingi 1,500 sawa na dola senti 65.  Bwana Iyege anasema walipatiwa mashine ya kutengeneza mkaa huo mbadala na kutokana na mauzo wanaweza kutunza familia ikiwa ni pamoja na kununulia watoto wao sare za shule.  
12/18/20230
Episode Artwork

Kaya Kigoma wameweza kuinua kipato na pia kutunza mazingira kupitia Mradi wa UNHCR

Nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kushirikiana na wadau wamewezesha kaya zinazopakana na kambi ya wakimbizi ya Nyarugusu mkoani Kigoma kujitengenezea mkaa mbadala na hivyo kusaidia kupunguza uharibifu wa mazingira unaosababishwa na ukataji miti kwa ajili ya mkaa. Mkoani Kigoma, kaskazini magharibi mwa Tanzania, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kupitia shirika la Denmark la kuhudumia wakimbizi, DRC wamefanikisha mradi wa kusaidia jamii kutengeneza mkaa kwa kutumia mabaki ya mahindi, maranda, mihogo na mawese.  Wanufaika wa mafunzo yaliyotolewa na DRC ni Kikundi cha Tubadilike kinachojihusisha na uchakati wa malighafi za kutengeneza mkaa kilichoko kijiji cha Mvugwe, wilaya ya Kasulu mkoani Kigoma.  Ayoub Juma Shaban, ni Mwenyekiti wa kikundi hicho ambaye amesema walipatiwa mafunzo ya kutengeneza mkaa huo ambapo wanachanganya maranda ya mbao, magunzi ya mahindi na hutumia mabaki ya unga wa muhogo wa ajili ya kugandisha mkaa huo.  Amesema wanatumia mkaa mbadala kama njia ya kuhifadhi mazingira. Badala ya kukata miti sasa wanatumia mabaki kutengeneza mkaa.  Mkaa huo wanauza ujazo wa ndoo ya lita 10 kwa shilingi 1,500 sawa na dola senti 65.  Bwana Iyege anasema walipatiwa mashine ya kutengeneza mkaa huo mbadala na kutokana na mauzo wanaweza kutunza familia ikiwa ni pamoja na kununulia watoto wao sare za shule.  
12/18/20232 minutes, 43 seconds
Episode Artwork

UN: Kushambuliwa kwa hospitali na kukatwa kwa mawasiliano ni pigo kubwa kwa mfumo wa afya na raia Gaza

Hali ya kibinadamu inazidi kuwa mbayá katika Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati, huku hospitali zilizosalia zikiendelea kushambuliwa na kukatili maisha ya watu na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet vikizidisha adha yameonya leo mashirika ya Umoja wa Mataifa. Asante Anold kama ulivyosema hali si hali Gaza Maisha ya watu yanaendelea kupotea kila siku kwanza kutokana na mashambulizi lakini pia kwa kukosa huduma muhimu za afya kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus ambaye kupitia ukurasa wake wa X hii leo amesisitiza kwamba “Mashambulizi dhidi ya hospitali , wahudumu wa afya na wagonjwa lazima yakome na usitishwaji mapigano ufanyike sasa”Dkt. Tedros pia amelaani vikali uharibifu mkubwa uliofanyika katika hospitali ya Kamal Adwan Kaskazini mwa Gaza baada ya kuvamiwa na vikosi vya Israel mwishoni mwa wiki  ambapo wagonjwa wanane wameuawa akiwemo mtoto wa miaka 9.Ameongeza kuwa wiki iliyopita vikosi vya Israel kwa siku nne viliivamia hospitali hiyo na kuipekua ndani nje huku kukiwa na taarifa za wahudumu wengi wa afya kushikiliwa.Dkt. Tedros ameonya kwamba “Mfumo wa afya wa Gaza ambao tayari ulikuwa taaban sasa kupoteza hospitali nyingine hata kama inafanya kazi kwa kiasi kidogo ni pigo kubwa kwa watu wa Gaza.”Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema “Kutokana na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet Gaza nzima sasa hakuna taarifa mpya zinazopatikana za vifo na majeruhi.”Limeongeza kuwa katika Ukingo wa Magharibi tangu kuanza kwa mzozo huu mpya Wapalestina 268 wameuawa na vikosi vya Israel wakiwemo watoto 70 ikiwa ni idadi kubwa Zaidi ya vifo vya Wapalestina kwa mwaka.Shirika hilo limeonya kwamba kuendelesha kwa mashambulizi kwenye Ukanda wa Gaza kunasababisha ugumu mkubwa wa kuafikia wenye uhitaji na hivyo kuwafanya watu waendelee kuwa katikati ya vita, kuzingirwa na kukosa mahitaji.Nimalizie na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF ambalo linasema ushitishwaji haraka wa mapigano wa muda mrefu kwa minajili ya kibinadamu ni lazima kwani sasa eneo zima la Gaza ambako Watoto walikuwa wakicheza na Kwenda shuleni kufurahia utoto wao limegeuka kifusi na kuwaacha njiapanda watoto hao. 
12/18/20230
Episode Artwork

UN: Kushambuliwa kwa hospitali na kukatwa kwa mawasiliano ni pigo kubwa kwa mfumo wa afya na raia Gaza

Hali ya kibinadamu inazidi kuwa mbayá katika Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati, huku hospitali zilizosalia zikiendelea kushambuliwa na kukatili maisha ya watu na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet vikizidisha adha yameonya leo mashirika ya Umoja wa Mataifa. Asante Anold kama ulivyosema hali si hali Gaza Maisha ya watu yanaendelea kupotea kila siku kwanza kutokana na mashambulizi lakini pia kwa kukosa huduma muhimu za afya kwa mujibu wa mkurugenzi mkuu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus ambaye kupitia ukurasa wake wa X hii leo amesisitiza kwamba “Mashambulizi dhidi ya hospitali , wahudumu wa afya na wagonjwa lazima yakome na usitishwaji mapigano ufanyike sasa”Dkt. Tedros pia amelaani vikali uharibifu mkubwa uliofanyika katika hospitali ya Kamal Adwan Kaskazini mwa Gaza baada ya kuvamiwa na vikosi vya Israel mwishoni mwa wiki  ambapo wagonjwa wanane wameuawa akiwemo mtoto wa miaka 9.Ameongeza kuwa wiki iliyopita vikosi vya Israel kwa siku nne viliivamia hospitali hiyo na kuipekua ndani nje huku kukiwa na taarifa za wahudumu wengi wa afya kushikiliwa.Dkt. Tedros ameonya kwamba “Mfumo wa afya wa Gaza ambao tayari ulikuwa taaban sasa kupoteza hospitali nyingine hata kama inafanya kazi kwa kiasi kidogo ni pigo kubwa kwa watu wa Gaza.”Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema “Kutokana na kufungwa kwa mawasiliano ya simu na mtandao wa intanet Gaza nzima sasa hakuna taarifa mpya zinazopatikana za vifo na majeruhi.”Limeongeza kuwa katika Ukingo wa Magharibi tangu kuanza kwa mzozo huu mpya Wapalestina 268 wameuawa na vikosi vya Israel wakiwemo watoto 70 ikiwa ni idadi kubwa Zaidi ya vifo vya Wapalestina kwa mwaka.Shirika hilo limeonya kwamba kuendelesha kwa mashambulizi kwenye Ukanda wa Gaza kunasababisha ugumu mkubwa wa kuafikia wenye uhitaji na hivyo kuwafanya watu waendelee kuwa katikati ya vita, kuzingirwa na kukosa mahitaji.Nimalizie na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF ambalo linasema ushitishwaji haraka wa mapigano wa muda mrefu kwa minajili ya kibinadamu ni lazima kwani sasa eneo zima la Gaza ambako Watoto walikuwa wakicheza na Kwenda shuleni kufurahia utoto wao limegeuka kifusi na kuwaacha njiapanda watoto hao. 
12/18/20232 minutes, 32 seconds
Episode Artwork

Siri ya kuwa sehemu ya tuzo hii ni ushirikiano wetu - Fr. Benedict Ayodi

Hii leo kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika hafla la kupatia tuzo washindi wa Tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, tuzo inayotolewa kwa mtu mmoja mmoja au kundi kwa kuzingatia mchango wao kwenye kusongesha haki za binadamu. Miongoni mwa washindi wa watano ni Ushirikiano wa kimataifa wa mashirika ya kijamii, watu wa asili, harakati za kijamii na jamii za mashinani. Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la Wafransiskani wakapuchini ni sehemu ya ushirikiano huo. Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya  Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Father Benedict Ayodi kutoka shirika hili kufahamu pamoja na mambo mengina sababu ya Ushindi wao. Lakini kwanza anaanza kwa kuelezea jinsi walivyopokea tuzo hii. 
12/15/20230
Episode Artwork

Siri ya kuwa sehemu ya tuzo hii ni ushirikiano wetu - Fr. Benedict Ayodi

Hii leo kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika hafla la kupatia tuzo washindi wa Tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, tuzo inayotolewa kwa mtu mmoja mmoja au kundi kwa kuzingatia mchango wao kwenye kusongesha haki za binadamu. Miongoni mwa washindi wa watano ni Ushirikiano wa kimataifa wa mashirika ya kijamii, watu wa asili, harakati za kijamii na jamii za mashinani. Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la Wafransiskani wakapuchini ni sehemu ya ushirikiano huo. Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya  Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Father Benedict Ayodi kutoka shirika hili kufahamu pamoja na mambo mengina sababu ya Ushindi wao. Lakini kwanza anaanza kwa kuelezea jinsi walivyopokea tuzo hii. 
12/15/20237 minutes, 46 seconds
Episode Artwork

Ushirikiano wetu ndio siri ya kuwa sehemu ya tuzo hii – Fr. Ayodi

Hii leo kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika hafla la kupatia tuzo washindi wa Tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, tuzo inayotolewa kwa mtu mmoja mmoja au kundi kwa kuzingatia mchango wao kwenye kusongesha haki za binadamu. Miongoni mwa washindi wa watano ni Ushirikiano wa kimataifa wa mashirika ya kijamii, watu wa asili, harakati za kijamii na jamii za mashinani. Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la Wafransiskani wakapuchini ni sehemu ya ushirikiano huo. Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya  Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Father Benedict Ayodi kutoka shirika hili kufahamu pamoja na mambo mengina sababu ya Ushindi wao. Lakini kwanza anaanza kwa kuelezea jinsi walivyopokea tuzo hii. 
12/15/20230
Episode Artwork

Ushirikiano wetu ndio siri ya kuwa sehemu ya tuzo hii – Fr. Ayodi

Hii leo kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika hafla la kupatia tuzo washindi wa Tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu, tuzo inayotolewa kwa mtu mmoja mmoja au kundi kwa kuzingatia mchango wao kwenye kusongesha haki za binadamu. Miongoni mwa washindi wa watano ni Ushirikiano wa kimataifa wa mashirika ya kijamii, watu wa asili, harakati za kijamii na jamii za mashinani. Shirika lisilo la kiserikali la kimataifa la Wafransiskani wakapuchini ni sehemu ya ushirikiano huo. Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya  Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Father Benedict Ayodi kutoka shirika hili kufahamu pamoja na mambo mengina sababu ya Ushindi wao. Lakini kwanza anaanza kwa kuelezea jinsi walivyopokea tuzo hii. 
12/15/20233 minutes, 48 seconds
Episode Artwork

15 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tnaangazia ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania, na wanariadha mashujaa wa mazingira nchini Kenya. Makala tunasalia hapa makao makuu na mashinani tunakupeleka nchini Zimbabwe, kulikoni?.Baada ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO kuitambua lugha ya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha za kimataifa, sasa Tanzania imetangaza kwamba kwa kushirikiana na nchi nyingine wataanza kutoa Tuzo za Kimataifa za Kiswahili. Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo wa Tanzania Dkt. Damas Ndumbaro amemweleza hayo mwandishi wa Idhaa hii Leah Mushi aliyehudhuria ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania.Mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira duniani UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya yamehimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora katika kampeni maalum iliyofanyika jana Alhamisi walipowaalika wanaridha kadhaa wa Kenya kwenye ofisi za Umoja wa mataifa jijini Nairobi.Miongoni wa wanariadha hao ni Francis Kipkoech Bowen ambaye kwa takriban miaka 20 amekuwa mkibiaji wa mbio za kawaida na marathon. Amezungumza na Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi UNIS kwanza akishukuru Umoja wa Mataifa kumjumuisha. Mashinani tnakuleta ujumbe wa mmoja wa wakimbizi nchini Zimbabwe kuhusu mchango wao katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.  Mwenyeji wako ni Flora, karibu!
12/15/20230
Episode Artwork

15 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tnaangazia ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania, na wanariadha mashujaa wa mazingira nchini Kenya. Makala tunasalia hapa makao makuu na mashinani tunakupeleka nchini Zimbabwe, kulikoni?.Baada ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO kuitambua lugha ya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha za kimataifa, sasa Tanzania imetangaza kwamba kwa kushirikiana na nchi nyingine wataanza kutoa Tuzo za Kimataifa za Kiswahili. Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo wa Tanzania Dkt. Damas Ndumbaro amemweleza hayo mwandishi wa Idhaa hii Leah Mushi aliyehudhuria ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania.Mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira duniani UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya yamehimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora katika kampeni maalum iliyofanyika jana Alhamisi walipowaalika wanaridha kadhaa wa Kenya kwenye ofisi za Umoja wa mataifa jijini Nairobi.Miongoni wa wanariadha hao ni Francis Kipkoech Bowen ambaye kwa takriban miaka 20 amekuwa mkibiaji wa mbio za kawaida na marathon. Amezungumza na Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi UNIS kwanza akishukuru Umoja wa Mataifa kumjumuisha. Mashinani tnakuleta ujumbe wa mmoja wa wakimbizi nchini Zimbabwe kuhusu mchango wao katika kukabiliana na changamoto za mabadiliko ya tabianchi.  Mwenyeji wako ni Flora, karibu!
12/15/202311 minutes, 2 seconds
Episode Artwork

CHAUKIDU: Ujio wa Tuzo ya Kiswahili ya Mwalimu Nyerere watangazwa

Baada ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO kuitambua lugha ya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha za kimataifa, sasa Tanzania imetangaza kwamba kwa kushirikiana na nchi nyingine wataanza kutoa Tuzo za Kimataifa za Kiswahili. Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo wa Tanzania Dkt. Damas Ndumbaro amemweleza hayo mwandishi wa Idhaa hii Leah Mushi aliyehudhuria ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania.“Mwakani 2024 katika kusherehekea siku ya Kiswahili duniani ambayo inatambulika na UNESCO, Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau wengine tutazindua rasmi ‘Tuzo ya kimataifa ya Kiswahili ya Mwalimu Nyerere’ ili kuenzi Kiswahili pamoja na mchango wa mwalimu Nyerere katika kuikuza lugha ya Kiswahili Tanzania, Afrika na duniani kote.”Waziri Ndumbaro amesema katika tuzo hiyo watu mbalimbali ambao wametoa mchango katika kukuza na kueneza Kiswahili duniani watatambulika nawatapewa tuzo hiyo kwa heshima ya Mwalimu Nyerere. Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni Rais wa kwanza wa taifa la Tanzania ambaye mara baada ya nchi hiyo kupata uhuru alihakikisha Kiswahili kinakuwa lugha rasmi ya mawasiliano ya taifa lake na pia kuendelea kukitangaza katika nchi jirani katika ukanda wa Afrika Mashariki. Akiulizwa kwanini tuzo hizo hazitolewi Afrika Mashariki na badala yake zinaenda kutolewa nchini Ufaransa, Waziri huyo wa Utamaduni Sanaa na michezo wa Tanzania amesema “Tuzo hizo zinatolewa Paris kwenye ofisi za UNESCO kwa heshima ya UNESCO kutambua Kiswahili duniani lakini pia kuchagua tarehe 7 ya mwezi wa Saba kila mwaka kuwa siku ya Kiswahili duniani.” Kongamano hilo lililozinduliwa leo tarehe 15 Desemba jijini Arusha, litaendelea mpaka tarehe 17 na linahudhuriwa na washiriki kutoka katika nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Comorrow, India, Nigeria, Italia, Marekani na Uingereza.Wahudhuriaji wa kongamano hilo ni pamoja na wawakilishi wa vyama na taasisi zinazokuza lugha za Kiswahili, wakalimani pamoja na walimu wa Kiswahili. Rais wa CHAUKIDU Dkt. Fillipo Lubua akizungumza katika uzinduzi huo amewasihi washiriki wa kongamano hilo kuzingatia maendeleo ya kidigitali katika ufundishaji wa lugha ya Kiswahili. Dkt. Lubua ambaye pia ni mhadhiri katika chuo kikuu cha Pittsburg cha nchini Marekani ametoa mafunzo kwa washiriki wa kongamano hili juu ya kutumia Akili unde (AI) ambapo aliwafundisha matumizi bora na yenye maadili ya ChatGPT pamoja na Adobe Express ambao ni mfumo wa kutengeneza picha.
12/15/20230
Episode Artwork

CHAUKIDU: Ujio wa Tuzo ya Kiswahili ya Mwalimu Nyerere watangazwa

Baada ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO kuitambua lugha ya Kiswahili kuwa miongoni mwa lugha za kimataifa, sasa Tanzania imetangaza kwamba kwa kushirikiana na nchi nyingine wataanza kutoa Tuzo za Kimataifa za Kiswahili. Waziri wa Utamaduni Sanaa na Michezo wa Tanzania Dkt. Damas Ndumbaro amemweleza hayo mwandishi wa Idhaa hii Leah Mushi aliyehudhuria ufunguzi wa Kongamano la nane la Kimataifa la Chama cha Ukuzaji wa Kiswahili Duniani (CHAUKIDU), uliofanyika leo jijini Arusha kaskazini mwa Tanzania.“Mwakani 2024 katika kusherehekea siku ya Kiswahili duniani ambayo inatambulika na UNESCO, Serikali ya Tanzania kwa kushirikiana na wadau wengine tutazindua rasmi ‘Tuzo ya kimataifa ya Kiswahili ya Mwalimu Nyerere’ ili kuenzi Kiswahili pamoja na mchango wa mwalimu Nyerere katika kuikuza lugha ya Kiswahili Tanzania, Afrika na duniani kote.”Waziri Ndumbaro amesema katika tuzo hiyo watu mbalimbali ambao wametoa mchango katika kukuza na kueneza Kiswahili duniani watatambulika nawatapewa tuzo hiyo kwa heshima ya Mwalimu Nyerere. Hayati Mwalimu Julius Kambarage Nyerere ni Rais wa kwanza wa taifa la Tanzania ambaye mara baada ya nchi hiyo kupata uhuru alihakikisha Kiswahili kinakuwa lugha rasmi ya mawasiliano ya taifa lake na pia kuendelea kukitangaza katika nchi jirani katika ukanda wa Afrika Mashariki. Akiulizwa kwanini tuzo hizo hazitolewi Afrika Mashariki na badala yake zinaenda kutolewa nchini Ufaransa, Waziri huyo wa Utamaduni Sanaa na michezo wa Tanzania amesema “Tuzo hizo zinatolewa Paris kwenye ofisi za UNESCO kwa heshima ya UNESCO kutambua Kiswahili duniani lakini pia kuchagua tarehe 7 ya mwezi wa Saba kila mwaka kuwa siku ya Kiswahili duniani.” Kongamano hilo lililozinduliwa leo tarehe 15 Desemba jijini Arusha, litaendelea mpaka tarehe 17 na linahudhuriwa na washiriki kutoka katika nchi za Tanzania, Kenya, Uganda, Rwanda, Burundi, Comorrow, India, Nigeria, Italia, Marekani na Uingereza.Wahudhuriaji wa kongamano hilo ni pamoja na wawakilishi wa vyama na taasisi zinazokuza lugha za Kiswahili, wakalimani pamoja na walimu wa Kiswahili. Rais wa CHAUKIDU Dkt. Fillipo Lubua akizungumza katika uzinduzi huo amewasihi washiriki wa kongamano hilo kuzingatia maendeleo ya kidigitali katika ufundishaji wa lugha ya Kiswahili. Dkt. Lubua ambaye pia ni mhadhiri katika chuo kikuu cha Pittsburg cha nchini Marekani ametoa mafunzo kwa washiriki wa kongamano hili juu ya kutumia Akili unde (AI) ambapo aliwafundisha matumizi bora na yenye maadili ya ChatGPT pamoja na Adobe Express ambao ni mfumo wa kutengeneza picha.
12/15/20231 minute, 35 seconds
Episode Artwork

UNEP/WHO: Afya na mazingira ni lila la fila havitengamani

Mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira duniani UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya yamehimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora katika kampeni maalum iliyofanyika jana Alhamisi walipowaalika wanaridha kadhaa wa Kenya kwenye ofisi za Umoja wa mataifa jijini Nairobi. Lengo ni kuzungumza na wanariadha hao kuhusu uhusiano uliopo baina ya mazingira na afya bora ili watambue na kuwa msitari wa mbele kuchagiza hilo katika tasnia yao ambayo mara nyingi hufanyika katika maeneo ya wazi na hewa safi ni muhimu. Miongoni wa wanariadha hao ni Francis Kipkoech Bowen ambaye kwa takriban miaka 20 amekuwa mkibiaji wa mbio za kawaida na marathon. Amezungumza na Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi UNIS kwanza akishukuru Umoja wa Mataifa kumjumuisha.“ Nimefurahia sana kuwa hapa UN, kuwa hapa UNEP wakishirikiana na WHO , nimefurahia kmakaribisho, nimeona wanatumikia watu kwa njia nzuri.”Ni kipi ulichojifunza kutokana na mazungumzo yenu na WHOP na UNEP,“Mambo ya hali ya hewa na afya vinaambatana pamoja na kitu kizuri kufundisha hata kizazi kijacho ili tuwe na afya bora wakati wote.”Kitu gani hasa kilichokugusa?“Haswa mambo ya maji na hewa safi “Kama mkimbiaji  unafikiri hewa safi ni muhimu sana kwako?“Ni muhimu kwa sababu ile hewa unayovuta ni muhimu nzuri na muhimu kwa afya ya kila mtu na hasa yale mazingira unayoishi kuwa mazuri.”Kwa mujibu wa UNEP na WHO mazingira na afya ni lila na fila havitengamani.
12/15/20230
Episode Artwork

UNEP/WHO: Afya na mazingira ni lila la fila havitengamani

Mashirika ya umoja wa Mataifa lile mazingira duniani UNEP na lile la afya WHO nchini Kenya yamehimiza umuhimu wa kuhakikisha mazingira safi kwa ajili ya afya bora katika kampeni maalum iliyofanyika jana Alhamisi walipowaalika wanaridha kadhaa wa Kenya kwenye ofisi za Umoja wa mataifa jijini Nairobi. Lengo ni kuzungumza na wanariadha hao kuhusu uhusiano uliopo baina ya mazingira na afya bora ili watambue na kuwa msitari wa mbele kuchagiza hilo katika tasnia yao ambayo mara nyingi hufanyika katika maeneo ya wazi na hewa safi ni muhimu. Miongoni wa wanariadha hao ni Francis Kipkoech Bowen ambaye kwa takriban miaka 20 amekuwa mkibiaji wa mbio za kawaida na marathon. Amezungumza na Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi UNIS kwanza akishukuru Umoja wa Mataifa kumjumuisha.“ Nimefurahia sana kuwa hapa UN, kuwa hapa UNEP wakishirikiana na WHO , nimefurahia kmakaribisho, nimeona wanatumikia watu kwa njia nzuri.”Ni kipi ulichojifunza kutokana na mazungumzo yenu na WHOP na UNEP,“Mambo ya hali ya hewa na afya vinaambatana pamoja na kitu kizuri kufundisha hata kizazi kijacho ili tuwe na afya bora wakati wote.”Kitu gani hasa kilichokugusa?“Haswa mambo ya maji na hewa safi “Kama mkimbiaji  unafikiri hewa safi ni muhimu sana kwako?“Ni muhimu kwa sababu ile hewa unayovuta ni muhimu nzuri na muhimu kwa afya ya kila mtu na hasa yale mazingira unayoishi kuwa mazuri.”Kwa mujibu wa UNEP na WHO mazingira na afya ni lila na fila havitengamani.
12/15/20231 minute, 48 seconds
Episode Artwork

METHALI: MSASI HAOGOPI MIIBA

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo mtaalamu wetu Nicholus Makanji, Mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya anatufafanulia maana ya methali MSASI HAOGOPI MIIBA.
12/14/20230
Episode Artwork

METHALI: MSASI HAOGOPI MIIBA

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo mtaalamu wetu Nicholus Makanji, Mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya anatufafanulia maana ya methali MSASI HAOGOPI MIIBA.
12/14/20230
Episode Artwork

14 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo tunamulika kazi za mshindi wa tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu Julienne Lusenge kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambaye shirika aliloanzisha la SOFEPADI limenasua wanawake kutoka kwenye ukatili wa kijinsia na kingono, sambamba na utumikishwaji, Mashariki mwa nchi hiyo. Tumekuandalia pia habari kwa ufupi na uchmbuzi wa methali.Mvua kubwa imesababisha maafa mapya huko Gaza huku wasaidizi wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa wakirudia kueleza wasiwasi wao kuhusu kuzorota kwa hali ya afya katika Ukanda huo,wakati kukiwa bado na mashambulizi yanayoendelea kati ya Israel na makundi yenye silaha ya Palestina. Ofisi ya Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura (OCHA) imesema kuwa maeneo mengi katika eneo hilo yamefurika, "na kuzidisha mahangaiko ya Wapalestina waliokimbia makazi yao.Jukwaa la pili la kimataifa la wakimbizi, GRF, linalowakutanisha takribani watu 4000 kutoka nchi 165 limeingia siku yake ya pili leo huko Geneva, Uswisi ambapo washiriki wanatoa ahadi zao kuhusu namna bora ya kushughulikia suala la wakimbizi. Katika tamko la Kenya lililochapishwa kwenye ukurasa rasmi wa mkutano huo, Kenya imeeleza namna ilivyotekeleza ahadi yake iliyotoa kwenye mkutano wa kwanza miaka minne iliyopita kwa kuwapa uraia Washona, Wamakonde na Wapemba. Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO, ili kuwalinda watoto limetoa wito wa kutaka serikali kote duniani zichukue hatua za haraka dhidi ya sigara za kisasa zilizoundwa kwa mfumo wa umeme yaani e-cigarettes. Kupitia wito huo, WHO imeonesha watoto wenye umri wa miaka 13-15 wanatumia sigara za kielektroniki kwa viwango vya juu kuliko watu wazima kote duniani. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalamu wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali « MSASI HAOGOPI MIIBA». Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/14/20230
Episode Artwork

14 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo tunamulika kazi za mshindi wa tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu Julienne Lusenge kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambaye shirika aliloanzisha la SOFEPADI limenasua wanawake kutoka kwenye ukatili wa kijinsia na kingono, sambamba na utumikishwaji, Mashariki mwa nchi hiyo. Tumekuandalia pia habari kwa ufupi na uchmbuzi wa methali.Mvua kubwa imesababisha maafa mapya huko Gaza huku wasaidizi wa kibinadamu wa Umoja wa Mataifa wakirudia kueleza wasiwasi wao kuhusu kuzorota kwa hali ya afya katika Ukanda huo,wakati kukiwa bado na mashambulizi yanayoendelea kati ya Israel na makundi yenye silaha ya Palestina. Ofisi ya Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura (OCHA) imesema kuwa maeneo mengi katika eneo hilo yamefurika, "na kuzidisha mahangaiko ya Wapalestina waliokimbia makazi yao.Jukwaa la pili la kimataifa la wakimbizi, GRF, linalowakutanisha takribani watu 4000 kutoka nchi 165 limeingia siku yake ya pili leo huko Geneva, Uswisi ambapo washiriki wanatoa ahadi zao kuhusu namna bora ya kushughulikia suala la wakimbizi. Katika tamko la Kenya lililochapishwa kwenye ukurasa rasmi wa mkutano huo, Kenya imeeleza namna ilivyotekeleza ahadi yake iliyotoa kwenye mkutano wa kwanza miaka minne iliyopita kwa kuwapa uraia Washona, Wamakonde na Wapemba. Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani, WHO, ili kuwalinda watoto limetoa wito wa kutaka serikali kote duniani zichukue hatua za haraka dhidi ya sigara za kisasa zilizoundwa kwa mfumo wa umeme yaani e-cigarettes. Kupitia wito huo, WHO imeonesha watoto wenye umri wa miaka 13-15 wanatumia sigara za kielektroniki kwa viwango vya juu kuliko watu wazima kote duniani. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalamu wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali « MSASI HAOGOPI MIIBA». Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/14/20239 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

Heko Marynsia kwa ushindi wa tuzo COP28

Marynsia Mangu, mmoja wa washiriki wa COP28 au mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC uliofanyika huko Dubai, Falme za Kiarabu, ambaye ameondoka akiwa amebeba tuzo. Tuzo inayodhihirisha utendaji wake yeye kama Afisa Mtendaji Mkuu wa shirika lisilo la kiserikali la Success Hands Tanzania.  Shirika hili linahusika na kuwajengea watoto tabia ya kupenda kusoma vitabu, tena tangu wakiwa tumboni mwa mama zao. Idhaa ya Umoja wa Mataifa ilitaka kufahamu mengi kutoka kwake ikiwemo ni tuzo gani ameshinda. Ezzat El Feri wa Idhaa ya Umoja wa Mataifa alizungumza naye huko Dubai na kisha Assumpta Massoi akandaa makala hii. Marynsia anaanza kwa kuelezea tuzo aliyonyakua. 
12/13/20230
Episode Artwork

Heko Marynsia kwa ushindi wa tuzo COP28

Marynsia Mangu, mmoja wa washiriki wa COP28 au mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC uliofanyika huko Dubai, Falme za Kiarabu, ambaye ameondoka akiwa amebeba tuzo. Tuzo inayodhihirisha utendaji wake yeye kama Afisa Mtendaji Mkuu wa shirika lisilo la kiserikali la Success Hands Tanzania.  Shirika hili linahusika na kuwajengea watoto tabia ya kupenda kusoma vitabu, tena tangu wakiwa tumboni mwa mama zao. Idhaa ya Umoja wa Mataifa ilitaka kufahamu mengi kutoka kwake ikiwemo ni tuzo gani ameshinda. Ezzat El Feri wa Idhaa ya Umoja wa Mataifa alizungumza naye huko Dubai na kisha Assumpta Massoi akandaa makala hii. Marynsia anaanza kwa kuelezea tuzo aliyonyakua. 
12/13/20233 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

13 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mkutano wa COP28 ambao unafunga pazia leo. Pia tunamulika Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi. Makala tunasalia huko huko Duabai kwenye mkutano wa COP28 na mashinani inamulika afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana walio katika mazingira magumu.Hatimaye mkutano wa 28 wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28, leo umekunja jamvi mjini Dubai Falme za nchi za Kiarabu kwa muafaka ambao Umoja wa Mataifa unasema unatoa ishara ya kuanza kutokomezwa kwa mafuta kisukuku au fosil fuel ingawa baadhi ya nchi za visiwa vidogo vinavyoendelea ikiwemo Samoa zinaona muafaka huo hautoshelezi kuwalinda kikamilifu dhidi ya tabianchi.Ikiwa leo Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi ambalo hufanyika kila baada ya miaka minne linaanza huko Geneva, Uswisi na kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wakiwemo wakimbizi kutafuta suluhu na kuahidi hatua kwa ajili ya wakimbizi duniani na nchi na jamii zinazowahifadhi, nikepeleke sasa nchini Zimbabwe ambako kuna mfano wa wazi namna wakimbizi wanavyoweza kuwa na mchango chanya katika jamii zinazowahifadhi. Makala inatupeleka Dubai, Falme za Kiarabu kwenye  mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ambako  huko Marynsia Mangu, Afisa Mtendaji Mkuu wa shirika la kiraia la Success Hands la nchini Tanzania linalohusika na kuwajengea watoto tabia ya kupenda kusoma vitabu ameshinda tuzo. Amezungumza na Idhaa ya Umoja wa Mataifa baada ya kupokea tuzo na hapa anaelezea mengi ikiwemo alivyoipokea. Mashinani itamulika afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana walio katika mazingira magumu.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/13/20230
Episode Artwork

13 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mkutano wa COP28 ambao unafunga pazia leo. Pia tunamulika Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi. Makala tunasalia huko huko Duabai kwenye mkutano wa COP28 na mashinani inamulika afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana walio katika mazingira magumu.Hatimaye mkutano wa 28 wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28, leo umekunja jamvi mjini Dubai Falme za nchi za Kiarabu kwa muafaka ambao Umoja wa Mataifa unasema unatoa ishara ya kuanza kutokomezwa kwa mafuta kisukuku au fosil fuel ingawa baadhi ya nchi za visiwa vidogo vinavyoendelea ikiwemo Samoa zinaona muafaka huo hautoshelezi kuwalinda kikamilifu dhidi ya tabianchi.Ikiwa leo Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi ambalo hufanyika kila baada ya miaka minne linaanza huko Geneva, Uswisi na kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wakiwemo wakimbizi kutafuta suluhu na kuahidi hatua kwa ajili ya wakimbizi duniani na nchi na jamii zinazowahifadhi, nikepeleke sasa nchini Zimbabwe ambako kuna mfano wa wazi namna wakimbizi wanavyoweza kuwa na mchango chanya katika jamii zinazowahifadhi. Makala inatupeleka Dubai, Falme za Kiarabu kwenye  mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ambako  huko Marynsia Mangu, Afisa Mtendaji Mkuu wa shirika la kiraia la Success Hands la nchini Tanzania linalohusika na kuwajengea watoto tabia ya kupenda kusoma vitabu ameshinda tuzo. Amezungumza na Idhaa ya Umoja wa Mataifa baada ya kupokea tuzo na hapa anaelezea mengi ikiwemo alivyoipokea. Mashinani itamulika afya ya uzazi na haki za wanawake na wasichana walio katika mazingira magumu.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/13/202312 minutes, 16 seconds
Episode Artwork

Wakimbizi vijana dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kambini Tongogara nchini Zimbabwe

Ikiwa leo Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi ambalo hufanyika kila baada ya miaka minne linaanza huko Geneva, Uswisi na kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wakiwemo wakimbizi kutafuta suluhu na kuahidi hatua kwa ajili ya wakimbizi duniani na nchi na jamii zinazowahifadhi, nikepeleke sasa nchini Zimbabwe ambako kuna mfano wa wazi namna wakimbizi wanavyoweza kuwa na mchango chanya katika jamii zinazowahifadhi.Kundi la wakimbizi vijana katika Kambi ya Wakimbizi ya Tongogara nchini Zimbabwe wanaongoza juhudi za kurejesha mazingira yao katika hali nzuri wakiungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR. EKambi ya wakimbizi ya Tongogara iliyoko kusini mwa Zimbabwe ni makazi ya wakimbizi 16,000, hasa kutoka Burundi, Msumbiji, Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC. “Miti ina faida nyingi, inavutia mvua, inatupatia kivuli, inakinga vumbi.”  Faida alizozitaja Mugisha Everiste, mtoto huyu mkimbizi kutoka Burundi zisingepatikana kambini Tongogara kama si juhudi za vijana wakimbizi kupitia taasisi yao ya Refugee Coalition for Climate Action (RCCA). Elie Nsala Tshikuna, Mkimbizi kutoka DR Congo anaeleza akisema kwamba (Nats)…walianza kupanda miti mwaka 2020. Na kuanzia mwaka huo hadi sasa wamepanda miti zaidi ya 2,000 kambini. Hili limeleta mabadiliko makubwa kwa sababu wameona kwamba jukumu ambalo jamii sasa inalo la kulinda miti limekuwa bora zaidi.  Jeanne Muhimundu, yeye ni mkimbizi kutoka Rwanda, mshiriki wa harakati hizi za utunzaji mazingira kambini, ana matumaini makubwa na hatua waliyoichukua,   "Natumai kuona miti zaidi. Natumai kuona watu wanachukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.” 
12/13/20230
Episode Artwork

Wakimbizi vijana dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kambini Tongogara nchini Zimbabwe

Ikiwa leo Kongamano la Kimataifa la Wakimbizi ambalo hufanyika kila baada ya miaka minne linaanza huko Geneva, Uswisi na kuwaleta pamoja wadau mbalimbali wakiwemo wakimbizi kutafuta suluhu na kuahidi hatua kwa ajili ya wakimbizi duniani na nchi na jamii zinazowahifadhi, nikepeleke sasa nchini Zimbabwe ambako kuna mfano wa wazi namna wakimbizi wanavyoweza kuwa na mchango chanya katika jamii zinazowahifadhi.Kundi la wakimbizi vijana katika Kambi ya Wakimbizi ya Tongogara nchini Zimbabwe wanaongoza juhudi za kurejesha mazingira yao katika hali nzuri wakiungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi, UNHCR. EKambi ya wakimbizi ya Tongogara iliyoko kusini mwa Zimbabwe ni makazi ya wakimbizi 16,000, hasa kutoka Burundi, Msumbiji, Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC. “Miti ina faida nyingi, inavutia mvua, inatupatia kivuli, inakinga vumbi.”  Faida alizozitaja Mugisha Everiste, mtoto huyu mkimbizi kutoka Burundi zisingepatikana kambini Tongogara kama si juhudi za vijana wakimbizi kupitia taasisi yao ya Refugee Coalition for Climate Action (RCCA). Elie Nsala Tshikuna, Mkimbizi kutoka DR Congo anaeleza akisema kwamba (Nats)…walianza kupanda miti mwaka 2020. Na kuanzia mwaka huo hadi sasa wamepanda miti zaidi ya 2,000 kambini. Hili limeleta mabadiliko makubwa kwa sababu wameona kwamba jukumu ambalo jamii sasa inalo la kulinda miti limekuwa bora zaidi.  Jeanne Muhimundu, yeye ni mkimbizi kutoka Rwanda, mshiriki wa harakati hizi za utunzaji mazingira kambini, ana matumaini makubwa na hatua waliyoichukua,   "Natumai kuona miti zaidi. Natumai kuona watu wanachukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.” 
12/13/20232 minutes
Episode Artwork

UN: COP28 yafunga pazia kwa muafaka wa kuanza kutokomeza mafuta kisuskuku

Hatimaye mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28, leo umekunja jamvi mjini Dubai huko Umoja w Falme za Kiarabu (UAE) kwa muafaka ambao Umoja wa Mataifa unasema unatoa ishara ya kuanza kutokomezwa kwa mafuta kisukuku au Fossil Fuels, ingawa baadhi ya nchi za visiwa vidogo vinavyoendelea ikiwemo Samoa zinaona muafaka huo hautoshelezi kuwalinda kikamilifu dhidi ya tabianchi.Ni Katibu Mtendaji wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi Simon Stiell akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya makubaliano kufikiwa akisema ingawa hawafungua ukurasa mpya kabisa wa kutokomeza mafuta kisukuku Dubai lakini makubaliano hayo yanatoa ishara ya kuanza utokomezaji wa mafuta hayo ambayo ni kichocheo kikubwa cha mabadiliko ya tabianchi. Stiel amesema “makubaliano hayo  yameweka msingi wa mpito wa haraka, wa haki na usawa, unaounga mkono kupunguzwa kwa kiasi kikubwa kwa uzalishaji wa hewa chafuzi na kuongezwa kwa ufadhili.”Amesisitiza kuwa “sasa serikali na sekta ya biashara wanahitaji kugeuza ahadi hizi kuwa matokeo halisi ya ya uchumi, bila kuchelewa.Akitoa kauli yake baada matokeo ya mkutano huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema "licha ya tofauti nyingi, ulimwengu unaweza kuungana na kukabiliana na changamoto ya janga la mabadiliko ya tabianchi. Ushirikiano wa kimataifa unasalia kuwa tumaini bora la ubinadamu." Kwa wale waliopinga kuainisha wazi utokomezaji wa nishati ya mafuta kisukuku katika waraka wa COP28, amesema "utokomezaji wa mafuta kisukuku haiwezi kuepukika watake wasitake. Hebu tutumaini kwamba hautachelewa sana. "Na mgawanyiko wa matokeo hayo ulikuwa bayana hususan kwa visiwa vidogo vinavyoendelea kama Samoa ambayo haikuficha hisia zake kuhusu matokeo na Stiel amekiri hilo akisema, tumesikia wasiwasi wa Samoa na mataifa yote ya visiwa ambayo yameweka wazi kwamba muafaka huu hautoshelezi kulinda watu wao na sayari. Ukweli kwamba ndio walioshangiliwa zaidi ni ishara tosha kwamba hisia zao zinaungwa mkono na wengi.”Washiriki kutoka nchi 199 na takriban pande 200 wamejadiliana Dubai kwa wiki mbili kwa lengo la kudhibiti athari za madiliko ya tabianchi na hasa kuhakikisha joto la duniani haliongezeki zaidi ya nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi.
12/13/20230
Episode Artwork

UN: COP28 yafunga pazia kwa muafaka wa kuanza kutokomeza mafuta kisuskuku

Hatimaye mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28, leo umekunja jamvi mjini Dubai huko Umoja w Falme za Kiarabu (UAE) kwa muafaka ambao Umoja wa Mataifa unasema unatoa ishara ya kuanza kutokomezwa kwa mafuta kisukuku au Fossil Fuels, ingawa baadhi ya nchi za visiwa vidogo vinavyoendelea ikiwemo Samoa zinaona muafaka huo hautoshelezi kuwalinda kikamilifu dhidi ya tabianchi.Ni Katibu Mtendaji wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi Simon Stiell akizungumza na waandishi wa habari mara baada ya makubaliano kufikiwa akisema ingawa hawafungua ukurasa mpya kabisa wa kutokomeza mafuta kisukuku Dubai lakini makubaliano hayo yanatoa ishara ya kuanza utokomezaji wa mafuta hayo ambayo ni kichocheo kikubwa cha mabadiliko ya tabianchi. Stiel amesema “makubaliano hayo  yameweka msingi wa mpito wa haraka, wa haki na usawa, unaounga mkono kupunguzwa kwa kiasi kikubwa kwa uzalishaji wa hewa chafuzi na kuongezwa kwa ufadhili.”Amesisitiza kuwa “sasa serikali na sekta ya biashara wanahitaji kugeuza ahadi hizi kuwa matokeo halisi ya ya uchumi, bila kuchelewa.Akitoa kauli yake baada matokeo ya mkutano huo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema "licha ya tofauti nyingi, ulimwengu unaweza kuungana na kukabiliana na changamoto ya janga la mabadiliko ya tabianchi. Ushirikiano wa kimataifa unasalia kuwa tumaini bora la ubinadamu." Kwa wale waliopinga kuainisha wazi utokomezaji wa nishati ya mafuta kisukuku katika waraka wa COP28, amesema "utokomezaji wa mafuta kisukuku haiwezi kuepukika watake wasitake. Hebu tutumaini kwamba hautachelewa sana. "Na mgawanyiko wa matokeo hayo ulikuwa bayana hususan kwa visiwa vidogo vinavyoendelea kama Samoa ambayo haikuficha hisia zake kuhusu matokeo na Stiel amekiri hilo akisema, tumesikia wasiwasi wa Samoa na mataifa yote ya visiwa ambayo yameweka wazi kwamba muafaka huu hautoshelezi kulinda watu wao na sayari. Ukweli kwamba ndio walioshangiliwa zaidi ni ishara tosha kwamba hisia zao zinaungwa mkono na wengi.”Washiriki kutoka nchi 199 na takriban pande 200 wamejadiliana Dubai kwa wiki mbili kwa lengo la kudhibiti athari za madiliko ya tabianchi na hasa kuhakikisha joto la duniani haliongezeki zaidi ya nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi.
12/13/20232 minutes, 47 seconds
Episode Artwork

12 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na tunamulika mchango wa vijana katika mkutano wa COP28.  Pia tunakuletea muhtasari wa habari zikiwemo vita Gaza, na hudam ya afya. Mashinani tunakupeleka nchini Sudan Kusini kusikia ni kwa jinsi gani mashirika ya Umoja wa Mataifa yanavyosaidia wafugaji kakabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Katika saa za mwisho za mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 majadiliano yanaendelea kwa matumaini kwamba wajumbe watatoka na makubaliano yatakayoweka ulimwengu kwenye njia ya mustakabali endelevu zaidi. Hata hivyo rasimu ya awali ya makubaliano hayo inaonyesha wito wa kuachana na nishati ya mafuta kiskuku umepewa kisogo, na kusababisha kilio kutoka kwa nchi zilizo katika mazingira magumu ya mabadiliko ya tabianchi na mashirika ya kiraia..Huko Gaza hali ya kibinadamu inazidi kudororora huku mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa yakipaza sauti ya kunusuru maisha ya watu wanaopitia adhabu ya jehanamu duniani. Lile la afya WHO linataka ulinzi na fursa ya kufikisha huduma za kibinadamu, wakati la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA likisema karibu Gaza nzima inazingirwa na kusababisha adhabu ya pamoja kwa zaidi ya watu milioni 2 ambapo nusu yake ni watoto. Na leo ni siku ya huduma za afya kwa wote mwaka huu ikibeba maudhui “Afya kwa wote, wakati wa kuchukua hatua” Mkurugenzi mkuu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO Dkt. Tedross Ghebreyesus katika ujumbe wake wa siku hii amesema “Huduma za afya kwa wote inamaanisha kwamba watu wote wanaweza kupata huduma wanazohitaji bila gharama kubwa lakini bado nusu ya watu wote duniani hawana huduma muhimu za afya. WHO ilizaliwa miaka 75 iliyopita kwa Imani kwamba afya ni haki ya binadamu na njia bora ya kutimiza haki hiyo ni huduma za afya kwa wote. Mashinani tutaelekea nchini Sudan Kusini kusikia ni kwa jinsi gani mashirika ya Umoja wa Mataifa yanavyosaidia wafugaji kakabiliana na mabadiliko ya tabianchi.  Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/12/20230
Episode Artwork

12 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na tunamulika mchango wa vijana katika mkutano wa COP28.  Pia tunakuletea muhtasari wa habari zikiwemo vita Gaza, na hudam ya afya. Mashinani tunakupeleka nchini Sudan Kusini kusikia ni kwa jinsi gani mashirika ya Umoja wa Mataifa yanavyosaidia wafugaji kakabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Katika saa za mwisho za mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 majadiliano yanaendelea kwa matumaini kwamba wajumbe watatoka na makubaliano yatakayoweka ulimwengu kwenye njia ya mustakabali endelevu zaidi. Hata hivyo rasimu ya awali ya makubaliano hayo inaonyesha wito wa kuachana na nishati ya mafuta kiskuku umepewa kisogo, na kusababisha kilio kutoka kwa nchi zilizo katika mazingira magumu ya mabadiliko ya tabianchi na mashirika ya kiraia..Huko Gaza hali ya kibinadamu inazidi kudororora huku mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa yakipaza sauti ya kunusuru maisha ya watu wanaopitia adhabu ya jehanamu duniani. Lile la afya WHO linataka ulinzi na fursa ya kufikisha huduma za kibinadamu, wakati la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA likisema karibu Gaza nzima inazingirwa na kusababisha adhabu ya pamoja kwa zaidi ya watu milioni 2 ambapo nusu yake ni watoto. Na leo ni siku ya huduma za afya kwa wote mwaka huu ikibeba maudhui “Afya kwa wote, wakati wa kuchukua hatua” Mkurugenzi mkuu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO Dkt. Tedross Ghebreyesus katika ujumbe wake wa siku hii amesema “Huduma za afya kwa wote inamaanisha kwamba watu wote wanaweza kupata huduma wanazohitaji bila gharama kubwa lakini bado nusu ya watu wote duniani hawana huduma muhimu za afya. WHO ilizaliwa miaka 75 iliyopita kwa Imani kwamba afya ni haki ya binadamu na njia bora ya kutimiza haki hiyo ni huduma za afya kwa wote. Mashinani tutaelekea nchini Sudan Kusini kusikia ni kwa jinsi gani mashirika ya Umoja wa Mataifa yanavyosaidia wafugaji kakabiliana na mabadiliko ya tabianchi.  Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/12/202311 minutes, 10 seconds
Episode Artwork

Uwekezaji katika elimu kwa watoto utawasaidia kupambana na mabadiliko ya tabianchi

Pazia la mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 likitarajiwa kufungwa hapo kesho huko Dubai Falme za kiarabu tunaangazia suala la jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri watoto hususani katika suala la Afya na kwenye elimu. Tarehe 08 Desemba ratiba ya COP28 ilijikita mahususi kujadili masuala ya vijana na watoto. Mashirika mbalimbali yalitoa takwimu zinazohusiana na madhara ya mabadiliko ya tabianchi kwa watoto na vijana moja wao ni Mfuko wa kimataifa wa elimu haiwezi kusubiri ECW. Ungana na Leah Mushi katika makala hii anayekujuza zaidi katika makala hii. 
12/11/20230
Episode Artwork

Uwekezaji katika elimu kwa watoto utawasaidia kupambana na mabadiliko ya tabianchi

Pazia la mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 likitarajiwa kufungwa hapo kesho huko Dubai Falme za kiarabu tunaangazia suala la jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri watoto hususani katika suala la Afya na kwenye elimu. Tarehe 08 Desemba ratiba ya COP28 ilijikita mahususi kujadili masuala ya vijana na watoto. Mashirika mbalimbali yalitoa takwimu zinazohusiana na madhara ya mabadiliko ya tabianchi kwa watoto na vijana moja wao ni Mfuko wa kimataifa wa elimu haiwezi kusubiri ECW. Ungana na Leah Mushi katika makala hii anayekujuza zaidi katika makala hii. 
12/11/20233 minutes, 13 seconds
Episode Artwork

Guterres kwa washiriki COP28: Epukeni majawabu ya kutia moyo bila ufanisi

Mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ukifikia ukingoni huko Dubai, Falme za Kiarabu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka washiriki waepuke msemo wa “Funika kombe mwanaharamu apite,” na badala yake waje na majawabu ya kina na ya kijasiri ili lengo la kutozidi kwa nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha selsiyasi liweze kufikiwa. Katibu Mkuu Guterres akizungumza na waandishi wa habari hii leo huko Dubai, Falme za Kiarabu amewakumbusha wasongeshaji wa majadiliano hayo kwenye COP28 kuwa mkutano unakunja jamvi kesho lakini bado kuna mapengo makubwa ya kuzibwa.  Ni wakati wa kusaka kulegeza misimamo ili kupata majawabu, anasema Guterres, akiongeza kuwa misimamo hiyo ilegezwe bila kupuuza sayansi au kupuuza umuhimu wa kuwa na matamanio makubwa. Anasema katika dunia iliyomeguka na kugawanyika, COP28 inaweza kudhihirisha kuwa ushirikiano wa kimataifa ndio tumaini letu bora la kutatua changamoto za dunia. Ndio hapo Katibu Mkuu akataja maeneo mawili ambayo anasihi pande husika kwenye mkutano huo kuyapatia kipaumbele: Mosi kupunguza utoaji wa hewa chafuzi na kuhakikisha kuna majawabu yanayopatia haki tabianchi. Katibu Mkuu anasema Uhakiki wa kimataifa lazima uwasilishe mpango wa wazi wa kuongeza nishati rejelezi, kuongeza maradufu nishati fanisi, na mpango mmoja wa kushughulikia vyanzo vya janga la tabianchi ambavyo ni uzalishaji na utumiaji wa nishati kisukuku. “Ametamatisha mkutano wake kwa kusema lazima COP28 imalizike kwa kuendeleza azma ya kudhibiti kiwango cha joto kisizidi nyuzi joto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi kama ilivyopitishwa na Mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya tabianchi mwaka 2015. 
12/11/20230
Episode Artwork

Guterres kwa washiriki COP28: Epukeni majawabu ya kutia moyo bila ufanisi

Mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ukifikia ukingoni huko Dubai, Falme za Kiarabu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka washiriki waepuke msemo wa “Funika kombe mwanaharamu apite,” na badala yake waje na majawabu ya kina na ya kijasiri ili lengo la kutozidi kwa nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha selsiyasi liweze kufikiwa. Katibu Mkuu Guterres akizungumza na waandishi wa habari hii leo huko Dubai, Falme za Kiarabu amewakumbusha wasongeshaji wa majadiliano hayo kwenye COP28 kuwa mkutano unakunja jamvi kesho lakini bado kuna mapengo makubwa ya kuzibwa.  Ni wakati wa kusaka kulegeza misimamo ili kupata majawabu, anasema Guterres, akiongeza kuwa misimamo hiyo ilegezwe bila kupuuza sayansi au kupuuza umuhimu wa kuwa na matamanio makubwa. Anasema katika dunia iliyomeguka na kugawanyika, COP28 inaweza kudhihirisha kuwa ushirikiano wa kimataifa ndio tumaini letu bora la kutatua changamoto za dunia. Ndio hapo Katibu Mkuu akataja maeneo mawili ambayo anasihi pande husika kwenye mkutano huo kuyapatia kipaumbele: Mosi kupunguza utoaji wa hewa chafuzi na kuhakikisha kuna majawabu yanayopatia haki tabianchi. Katibu Mkuu anasema Uhakiki wa kimataifa lazima uwasilishe mpango wa wazi wa kuongeza nishati rejelezi, kuongeza maradufu nishati fanisi, na mpango mmoja wa kushughulikia vyanzo vya janga la tabianchi ambavyo ni uzalishaji na utumiaji wa nishati kisukuku. “Ametamatisha mkutano wake kwa kusema lazima COP28 imalizike kwa kuendeleza azma ya kudhibiti kiwango cha joto kisizidi nyuzi joto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi kama ilivyopitishwa na Mkataba wa Paris wa Mabadiliko ya tabianchi mwaka 2015. 
12/11/20231 minute, 56 seconds
Episode Artwork

Lilly Kiden: Asante FAO kunijengea mnepo sasa najikimu mimi na familia yangu

Wakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukijiandaa kufunga pazia hapo kesho nakupeleka Sudan Kusini jimbo la Equatorial Mashariki ambako wakulima walioathirika na mabadiliko ya tabianchi sasa wanajengewa mnepo na mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO na wengi wameweza kujikwamua pamoja na familia zao. Ungana na Flora Nducha akikuletea safari ya mafanikio ya mmoja wa wanuafa wa mradi huo wa FAO. Kutana na Lilly Kiden mama mjasiriamali anayelima na kuchuza mboga za majani  katika eneo la Lopit Sudan KusiniLilly anasema ana watoto 7 na jamaa wengine 10 wa familia ambao wote wanamtegemea . Shukran kwa FAO  kwa kuwajengea wanawake mnepo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kupitia ufadhili kutoka Benki ya Maendeleo Afrika sasa wana mabwa yanayotumia pampu za sola na kumuwesha Lilly na wanawake wengine wakulima wadogo kumwagilia mashamba yao.  Kwa Lilly anasema kibarua ni kigumu kueedesha familia kubwa kama aliyonayo bila msaada mwingine.Ingawa sasa amekuwa mchumia juani anayelia kivulini, ukame wa muda mrefu Sudan umekuwa mwiba kwa wakulima hawa,“Mabadiliko ya tabianchi yametuathiri sana, na mwaka huu umekuwa mbayá zaidi, kila tulichopanda kilikauka na jua hali ikiendelea hivi wanangu hawatakuwa na chakula na wengine watashindwa kwenda shule.”Lilly mwenye umri wa miaka 38 kutokana na kuuza mbogamboga yeye na wenzake 25 wamewekeza fedha wanazopata na sasa wanapena mikopo kupitia jumuiya yao ya akiba ya kijiji. Ama kwa hakika jembe halimtupi mkulima, ”Hela ninayopata kwa kuuza mbogamboga imenisaidia sana naweza kununua chakula kwa ajili ya familia yangu, na kuweka akiba kidogo ambayo imekuwa mkombozi wangu yote ni kwa kulima na kuuza mbogamboga. Ndoto yangu ni kuongeza bidii ili watoto wangu waendelee na masomo.”FAO mbali ya kuwajengea mabwawa kwa ya umwagiliaji wakulima hawa pia inawapa mafunzo, mbegu na mikopo.
12/11/20230
Episode Artwork

Lilly Kiden: Asante FAO kunijengea mnepo sasa najikimu mimi na familia yangu

Wakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukijiandaa kufunga pazia hapo kesho nakupeleka Sudan Kusini jimbo la Equatorial Mashariki ambako wakulima walioathirika na mabadiliko ya tabianchi sasa wanajengewa mnepo na mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO na wengi wameweza kujikwamua pamoja na familia zao. Ungana na Flora Nducha akikuletea safari ya mafanikio ya mmoja wa wanuafa wa mradi huo wa FAO. Kutana na Lilly Kiden mama mjasiriamali anayelima na kuchuza mboga za majani  katika eneo la Lopit Sudan KusiniLilly anasema ana watoto 7 na jamaa wengine 10 wa familia ambao wote wanamtegemea . Shukran kwa FAO  kwa kuwajengea wanawake mnepo dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kupitia ufadhili kutoka Benki ya Maendeleo Afrika sasa wana mabwa yanayotumia pampu za sola na kumuwesha Lilly na wanawake wengine wakulima wadogo kumwagilia mashamba yao.  Kwa Lilly anasema kibarua ni kigumu kueedesha familia kubwa kama aliyonayo bila msaada mwingine.Ingawa sasa amekuwa mchumia juani anayelia kivulini, ukame wa muda mrefu Sudan umekuwa mwiba kwa wakulima hawa,“Mabadiliko ya tabianchi yametuathiri sana, na mwaka huu umekuwa mbayá zaidi, kila tulichopanda kilikauka na jua hali ikiendelea hivi wanangu hawatakuwa na chakula na wengine watashindwa kwenda shule.”Lilly mwenye umri wa miaka 38 kutokana na kuuza mbogamboga yeye na wenzake 25 wamewekeza fedha wanazopata na sasa wanapena mikopo kupitia jumuiya yao ya akiba ya kijiji. Ama kwa hakika jembe halimtupi mkulima, ”Hela ninayopata kwa kuuza mbogamboga imenisaidia sana naweza kununua chakula kwa ajili ya familia yangu, na kuweka akiba kidogo ambayo imekuwa mkombozi wangu yote ni kwa kulima na kuuza mbogamboga. Ndoto yangu ni kuongeza bidii ili watoto wangu waendelee na masomo.”FAO mbali ya kuwajengea mabwawa kwa ya umwagiliaji wakulima hawa pia inawapa mafunzo, mbegu na mikopo.
12/11/20232 minutes, 8 seconds
Episode Artwork

11 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mabadiliko ya tabianchi na wakulima nchini Sudan kusini. Makala tunamulika madhara ya mabadiliko ya tabianchi kwa watototo na mashinani tunakupeleka nchini DRC kwa mshindi wa tuzo ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa ya Haki za bindamu. Mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ukifikia ukingoni huko Dubai, Falme za Kiarabu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka washiriki waepuke msemo wa “Funika kombe mwanaharamu apite,” na badala yake waje na majawabu ya kina na ya kijasiri ili lengo la kutozidi kwa nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha selsiyasi liweze kufikiwa.Wakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukijiandaa kufunga pazia hapo kesho nakupeleka Sudan Kusini jimbo la Equatorial Mashariki ambako wakulima walioathirika na mabadiliko ya tabianchi sasa wanajengewa mnepo na mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO na wengi wameweza kujikwamua pamoja na familia zao. Katika makala wakati pazia la mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 likitarajiwa kufungwa hapo kesho huko Dubai Falme za kiarabu tunaangazia suala la jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri watoto hususani katika suala la Afya na kwenye elimu. Na mashinani tunakwenda Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, DRC kwa mshindi wa tuzo ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa ya Haki za bindamu.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/11/20230
Episode Artwork

11 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mabadiliko ya tabianchi na wakulima nchini Sudan kusini. Makala tunamulika madhara ya mabadiliko ya tabianchi kwa watototo na mashinani tunakupeleka nchini DRC kwa mshindi wa tuzo ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa ya Haki za bindamu. Mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa Mkataba wa Mabadiliko ya Tabianchi, COP28 ukifikia ukingoni huko Dubai, Falme za Kiarabu, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ametaka washiriki waepuke msemo wa “Funika kombe mwanaharamu apite,” na badala yake waje na majawabu ya kina na ya kijasiri ili lengo la kutozidi kwa nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha selsiyasi liweze kufikiwa.Wakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukijiandaa kufunga pazia hapo kesho nakupeleka Sudan Kusini jimbo la Equatorial Mashariki ambako wakulima walioathirika na mabadiliko ya tabianchi sasa wanajengewa mnepo na mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO na wengi wameweza kujikwamua pamoja na familia zao. Katika makala wakati pazia la mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 likitarajiwa kufungwa hapo kesho huko Dubai Falme za kiarabu tunaangazia suala la jinsi mabadiliko ya tabianchi yanavyoathiri watoto hususani katika suala la Afya na kwenye elimu. Na mashinani tunakwenda Jamhuri ya Kidemokrasi ya Congo, DRC kwa mshindi wa tuzo ya mwaka huu ya Umoja wa Mataifa ya Haki za bindamu.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/11/202310 minutes, 10 seconds
Episode Artwork

NENO: Kifandugu

Leo katika Jifunze Kiswahili ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua maana ya neno “KIFANDUGU”.  Anapochambua neno hili anapatia pia kisawe chake ambacho ni "KITOKONO."
12/8/20230
Episode Artwork

NENO: Kifandugu

Leo katika Jifunze Kiswahili ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua maana ya neno “KIFANDUGU”.  Anapochambua neno hili anapatia pia kisawe chake ambacho ni "KITOKONO."
12/8/20230
Episode Artwork

Mafuriko yazidi 'kutikisa' maeneo yaliyokuwa yamegubikwa na ukame Mashariki mwa Afrika

Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) linaonya kuwa mafuriko makubwa yanatishia kuongeza zaidi tatizo la kukosekana kwa uhakika wa kupatikana kwa chakula katika eneo la Mashariki mwa Afrika licha ya kwamba shirika hilo linajitahidi kusambaza misaada. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kuleta maafa katika eneo la Mashariki mwa Afrika, eneo ambalo lina uchangiaji mdogo katika uzalishaji wa hewa chafuzi lakini likiwa eneo ambalo linabeba mzigo mkubwa wa dharura ya tabanchi duniani. Baada ya ukame mkali kati ya mwaka 2020 na 2022, sasa ni mvua asilimia 140 juu ya viwango vya kawaida.Kwa mujibu wa WFP, takriban watu milioni 3 wameathiriwa, huku zaidi ya watu milioni 1.2 wakilazimika kuyahama makazi yao. Somalia, Ethiopia, na Kenya ndizo zinazobeba mzigo mkubwa wa janga hili, zikifuatiwa kwa karibu na Sudan, Sudan Kusini, Burundi, na Uganda na sasa Tanzania ambayo tukio la hivi karibuni ni maporomoko ya udongo katika Mlima Hanang, huko kaskazini mwa nchi. Kwa bahati mbaya, mvua zinatarajiwa kuendelea kote mashariki mwa Afrika hadi mapema mwaka 2024.Petroc Wilton wa WFP Somalia anasema, "El Niño na janga la tabianchi vimepeleka athari mbaya katika maeneo mengi ya Afrika Mashariki. Tumeona mfululizo wa majanga ya tabianchi. WFP hapa Somalia tunatumia boti, tunatumia helikopta kufikisha msaada wa kuokoa maisha kwa watu wenye uhitaji zaidi.”
12/8/20230
Episode Artwork

Mafuriko yazidi 'kutikisa' maeneo yaliyokuwa yamegubikwa na ukame Mashariki mwa Afrika

Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) linaonya kuwa mafuriko makubwa yanatishia kuongeza zaidi tatizo la kukosekana kwa uhakika wa kupatikana kwa chakula katika eneo la Mashariki mwa Afrika licha ya kwamba shirika hilo linajitahidi kusambaza misaada. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Mabadiliko ya tabianchi yanaendelea kuleta maafa katika eneo la Mashariki mwa Afrika, eneo ambalo lina uchangiaji mdogo katika uzalishaji wa hewa chafuzi lakini likiwa eneo ambalo linabeba mzigo mkubwa wa dharura ya tabanchi duniani. Baada ya ukame mkali kati ya mwaka 2020 na 2022, sasa ni mvua asilimia 140 juu ya viwango vya kawaida.Kwa mujibu wa WFP, takriban watu milioni 3 wameathiriwa, huku zaidi ya watu milioni 1.2 wakilazimika kuyahama makazi yao. Somalia, Ethiopia, na Kenya ndizo zinazobeba mzigo mkubwa wa janga hili, zikifuatiwa kwa karibu na Sudan, Sudan Kusini, Burundi, na Uganda na sasa Tanzania ambayo tukio la hivi karibuni ni maporomoko ya udongo katika Mlima Hanang, huko kaskazini mwa nchi. Kwa bahati mbaya, mvua zinatarajiwa kuendelea kote mashariki mwa Afrika hadi mapema mwaka 2024.Petroc Wilton wa WFP Somalia anasema, "El Niño na janga la tabianchi vimepeleka athari mbaya katika maeneo mengi ya Afrika Mashariki. Tumeona mfululizo wa majanga ya tabianchi. WFP hapa Somalia tunatumia boti, tunatumia helikopta kufikisha msaada wa kuokoa maisha kwa watu wenye uhitaji zaidi.”
12/8/20231 minute, 48 seconds
Episode Artwork

GAZA: Misaada ni haba, nyaya za simu zageuzwa kuni

Wakati mashambulizi ya Israel yakiendelea kushika kasi huko Ukanda wa Gaza na mapigano na makundi yaliyojihami ya kipalestina yakiwa kikwazo kikubwa cha kusambaza misaada ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa leo umeonya kwamba jamii inakaribia kusambaratika kabisa watu wakifikia hatua ya kukata nyaya za simu za kuzitumia kama kuni. Flora Nducha amefuatilia na anatusimulia zaidi.Asante Assumpta , Yumkini hali si hali tena Gaza kwa mujibu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswiss hii leo msemaji wa shirika la Afya la Umoja WHO Christian Lindmeier amesema “Watu Gaza wanalazimishwa kutumbukia katika janga kubwa huku kukiwa na kampeni ya kikatili ya Israel dhidi ya wakazi wa Ukanda huo kulipiza kisasi mashambulizi ya kigaidi ya Hamas tarehe 7 Oktoba.Amesisitiza kuwa “Hali ni mbayá sana na hatuwezi kumudu kupoteza hata gari linguine moja la wagonjwa au hospoitali kwani hadi sasa mashambulizi 212 yamefanyika dhidi ya huduma za afya na kuathiri vituo 56 na magari ya wagonjwa 59.”Wakati huo huo hapa mjini New York, leo mkutano wa dharura wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa unafanyika ili kujadili mzozo wa Palestina na Israel na azimio linatarajiwa kupitishwa. Katika mitaa ya Gaza shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA linasema utulivu umetoweka hivyo “ Ni muhimu kuhakikisha tunazuia kuporomoka kabisa kwa Gaza na mzozo huu kusambaa kwingineko.  Utaratibu wa kiraia unasambaratika Gaza na mitaa sasa ni mahame, haswa baada ya giza kuingia baadhi ya misafara ya misaada inaporwa na magari ya Umoja wa Mataifa kupigwa mawe. Jamii iko kwenye ukingo wa kuporomoka kabisa”.Nalo shirika la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA limeonya juu kushindwa kuwafikia watu kwa misaada ya muhimu  kama maji, chakula, dawa namingineyo likisema usambazaji wa misaada kwa sasa ni mdogo sana hasa Kusini mwa Ukanda huo na pia hakuna mahali popote palipo salama kwa raia na wahudumu wa misaada.Tangu Oktoba 7 zaidi ya asilimia 85 ya watu Gaza wametawanywa na machafuko ambapo takriban milioni 1.2 wamekuwa wakimbizi Wanjiku ndani wakipatiwa hifadhi katika vituo 151 vya UNRWA. Kwako Assumpta.
12/8/20230
Episode Artwork

GAZA: Misaada ni haba, nyaya za simu zageuzwa kuni

Wakati mashambulizi ya Israel yakiendelea kushika kasi huko Ukanda wa Gaza na mapigano na makundi yaliyojihami ya kipalestina yakiwa kikwazo kikubwa cha kusambaza misaada ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa leo umeonya kwamba jamii inakaribia kusambaratika kabisa watu wakifikia hatua ya kukata nyaya za simu za kuzitumia kama kuni. Flora Nducha amefuatilia na anatusimulia zaidi.Asante Assumpta , Yumkini hali si hali tena Gaza kwa mujibu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswiss hii leo msemaji wa shirika la Afya la Umoja WHO Christian Lindmeier amesema “Watu Gaza wanalazimishwa kutumbukia katika janga kubwa huku kukiwa na kampeni ya kikatili ya Israel dhidi ya wakazi wa Ukanda huo kulipiza kisasi mashambulizi ya kigaidi ya Hamas tarehe 7 Oktoba.Amesisitiza kuwa “Hali ni mbayá sana na hatuwezi kumudu kupoteza hata gari linguine moja la wagonjwa au hospoitali kwani hadi sasa mashambulizi 212 yamefanyika dhidi ya huduma za afya na kuathiri vituo 56 na magari ya wagonjwa 59.”Wakati huo huo hapa mjini New York, leo mkutano wa dharura wa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa unafanyika ili kujadili mzozo wa Palestina na Israel na azimio linatarajiwa kupitishwa. Katika mitaa ya Gaza shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA linasema utulivu umetoweka hivyo “ Ni muhimu kuhakikisha tunazuia kuporomoka kabisa kwa Gaza na mzozo huu kusambaa kwingineko.  Utaratibu wa kiraia unasambaratika Gaza na mitaa sasa ni mahame, haswa baada ya giza kuingia baadhi ya misafara ya misaada inaporwa na magari ya Umoja wa Mataifa kupigwa mawe. Jamii iko kwenye ukingo wa kuporomoka kabisa”.Nalo shirika la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA limeonya juu kushindwa kuwafikia watu kwa misaada ya muhimu  kama maji, chakula, dawa namingineyo likisema usambazaji wa misaada kwa sasa ni mdogo sana hasa Kusini mwa Ukanda huo na pia hakuna mahali popote palipo salama kwa raia na wahudumu wa misaada.Tangu Oktoba 7 zaidi ya asilimia 85 ya watu Gaza wametawanywa na machafuko ambapo takriban milioni 1.2 wamekuwa wakimbizi Wanjiku ndani wakipatiwa hifadhi katika vituo 151 vya UNRWA. Kwako Assumpta.
12/8/20232 minutes, 27 seconds
Episode Artwork

08 DESEMBA 2023

Hii leo kwenye jarida Assumpta Massoi anamulika mzozo Mashariki ya Kati hususan huko Gaza,  nyaya za simu zageuzwa kuni, kisha anakwenda Mashariki mwa Afrika huko baada ya ukame wa muda mrefu sasa ni mvua za kupindukia zinazosababisha maafa makubwa,; makala anakupeleka Tanzania kusikia uchambuzi wa Ibara ya 15 ya Tamko la Haki za Binadamu la UN, na mashinani utamsikia binti shujaa wa mazingira kutoka visiwani Zanzibar nchini Tanzania.Wakati mashambulizi ya Israel yakiendelea kushika kasi huko Ukanda wa Gaza na mapigano na makundi yaliyojihami ya kipalestina yakiwa kikwazo kikubwa cha kusambaza misaada ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa leo umeonya kwamba jamii inakaribia kusambaratika kabisa watu wakifikia hatua ya kukata nyaya za simu za kuzitumia kama kuni. Taarifa ni ya Flora Nducha.Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) linaonya kuwa mafuriko makubwa yanatishia kuongeza zaidi tatizo la kukosekana kwa uhakika wa kupatikana kwa chakula katika eneo la Mashariki mwa Afrika licha ya kwamba shirika hilo linajitahidi kusambaza misaada. Anold Kayanda ndiye ameandaa ripoti hii.Makala inamulika ibara ya 15 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75. Mchambuzi wetu ni Mhadhiri na mwanasheria wa Haki za Binadamu kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino SAUT mkoani Mwanza, Kaskazini-Magharibi mwa Tanzania Shukuru Paul, akihojiwa na Evarist Mapesa wa Idhaa hii.Na mashinani fursa ni yake Nasra, binti huyu shujaa wa mazingira kutoka Zanzibar nchini Tanzania, ambaye ni kiongozi mwenye shauku wa klabu yake ya shule ya upandaji miti na anatumia sauti yake kuhamasisha watu kutunza mazingira na kuhakikisha ulimwengu ulio endelevu zaidi siku za usoni.  Karibu!
12/8/20230
Episode Artwork

08 DESEMBA 2023

Hii leo kwenye jarida Assumpta Massoi anamulika mzozo Mashariki ya Kati hususan huko Gaza,  nyaya za simu zageuzwa kuni, kisha anakwenda Mashariki mwa Afrika huko baada ya ukame wa muda mrefu sasa ni mvua za kupindukia zinazosababisha maafa makubwa,; makala anakupeleka Tanzania kusikia uchambuzi wa Ibara ya 15 ya Tamko la Haki za Binadamu la UN, na mashinani utamsikia binti shujaa wa mazingira kutoka visiwani Zanzibar nchini Tanzania.Wakati mashambulizi ya Israel yakiendelea kushika kasi huko Ukanda wa Gaza na mapigano na makundi yaliyojihami ya kipalestina yakiwa kikwazo kikubwa cha kusambaza misaada ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa leo umeonya kwamba jamii inakaribia kusambaratika kabisa watu wakifikia hatua ya kukata nyaya za simu za kuzitumia kama kuni. Taarifa ni ya Flora Nducha.Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) linaonya kuwa mafuriko makubwa yanatishia kuongeza zaidi tatizo la kukosekana kwa uhakika wa kupatikana kwa chakula katika eneo la Mashariki mwa Afrika licha ya kwamba shirika hilo linajitahidi kusambaza misaada. Anold Kayanda ndiye ameandaa ripoti hii.Makala inamulika ibara ya 15 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75. Mchambuzi wetu ni Mhadhiri na mwanasheria wa Haki za Binadamu kutoka Chuo Kikuu cha Mtakatifu Agustino SAUT mkoani Mwanza, Kaskazini-Magharibi mwa Tanzania Shukuru Paul, akihojiwa na Evarist Mapesa wa Idhaa hii.Na mashinani fursa ni yake Nasra, binti huyu shujaa wa mazingira kutoka Zanzibar nchini Tanzania, ambaye ni kiongozi mwenye shauku wa klabu yake ya shule ya upandaji miti na anatumia sauti yake kuhamasisha watu kutunza mazingira na kuhakikisha ulimwengu ulio endelevu zaidi siku za usoni.  Karibu!
12/8/20239 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

07 DESEMBA 2023

Hii leo kwenye jarida Leah Mushi anakuletea Habari kwa Ufupi ikiangazia Tanzania, janga la chakula Afrika na Mkutano wa UN na wanazuoni. Katika Mada kwa Kina tunamulika mshindi wa Tuzo ya UN ya Haki za Binadamu Julienne Lusenge kutoka DRC na Jifunze Kiswahili maana ya neno, Kifandugu.Habari kwa UfupiWakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukiendelea Dubai Falme za Kiarabu, nchini Tanzania mafuriko makubwa na maporomoko yameleta janga la kibinadamu katika wilaya ya Hanang mkoani Manyara Kazkazini mwa nchi hiyo, watu zaidi ya 65 wamekufa, zaidi ya 100 kujeruhiwa na maelfu kutawanywa. Serikali imeomba msaada kwa umoja wa Mataifa ambao umesema uko tayari kusaidia.Afrika inakabiliwa na janga kubwa chakula ambao halijawahi kushuhudiwa, kwa mujibu wa ripoti mpya ya pamoja iliyozinduliwa leo na mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la chakula na kilimo FAO , la mpango wa chakula duniani WFP, Tume ya Muungano wa Afrika (AUC) na Kamisheni ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Afrika (ECA), Ripoti hiyo, ya uhakika wa chakula na lishe kanda ya Afrika 2023 inaangazia takwimu za kutisha za ukosefu wa chakula na utapiamlo ambazo zinasisitiza haja ya haraka ya hatua za kina kuepusha zahma kubwa. Takribani watu milioni 282 barani Afrika karibu asilimia 20 ya idadi ya watu wote hawana lishe bora, ikiwa ni ongezeko la watu milioni 57 tangu kuanza kwa janga la COVID-19.Na leo mkutano wa Umoja wa Mataifa na wanazuoni kutoka Vyuo Vikuu unakunja jamvi hapa New York,  Marekani na mmoja wa washiriki ni Dkt. Venance Shillingi kutoka Chuo Kikuu Mzumbe nchini Tanzania.Mada kwa Kina: Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zinaelekea ukingoni kwani kilele in tarehe 10 mwezi huu wa Desemba ambayo ni siku ya haki za binadamu duniani. Nayo Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa leo inammulika mmoja wa washindi wa tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu ambaye ameweka rehani hata maisha yake kutetea waliokumbwa na ukatili wa kijinsia nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC . Akisema SOFEPADI ni kifupi cha shirika la mshikamano wa wanawake kwa ajili ya amani na maendeleo.  Jifunze Lugha ya Kiswahili: Kiswahili  leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua maana ya neno “KIFANDUGU”. Karibu sana!
12/7/20230
Episode Artwork

07 DESEMBA 2023

Hii leo kwenye jarida Leah Mushi anakuletea Habari kwa Ufupi ikiangazia Tanzania, janga la chakula Afrika na Mkutano wa UN na wanazuoni. Katika Mada kwa Kina tunamulika mshindi wa Tuzo ya UN ya Haki za Binadamu Julienne Lusenge kutoka DRC na Jifunze Kiswahili maana ya neno, Kifandugu.Habari kwa UfupiWakati mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 ukiendelea Dubai Falme za Kiarabu, nchini Tanzania mafuriko makubwa na maporomoko yameleta janga la kibinadamu katika wilaya ya Hanang mkoani Manyara Kazkazini mwa nchi hiyo, watu zaidi ya 65 wamekufa, zaidi ya 100 kujeruhiwa na maelfu kutawanywa. Serikali imeomba msaada kwa umoja wa Mataifa ambao umesema uko tayari kusaidia.Afrika inakabiliwa na janga kubwa chakula ambao halijawahi kushuhudiwa, kwa mujibu wa ripoti mpya ya pamoja iliyozinduliwa leo na mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la chakula na kilimo FAO , la mpango wa chakula duniani WFP, Tume ya Muungano wa Afrika (AUC) na Kamisheni ya Uchumi ya Umoja wa Mataifa kwa ajili ya Afrika (ECA), Ripoti hiyo, ya uhakika wa chakula na lishe kanda ya Afrika 2023 inaangazia takwimu za kutisha za ukosefu wa chakula na utapiamlo ambazo zinasisitiza haja ya haraka ya hatua za kina kuepusha zahma kubwa. Takribani watu milioni 282 barani Afrika karibu asilimia 20 ya idadi ya watu wote hawana lishe bora, ikiwa ni ongezeko la watu milioni 57 tangu kuanza kwa janga la COVID-19.Na leo mkutano wa Umoja wa Mataifa na wanazuoni kutoka Vyuo Vikuu unakunja jamvi hapa New York,  Marekani na mmoja wa washiriki ni Dkt. Venance Shillingi kutoka Chuo Kikuu Mzumbe nchini Tanzania.Mada kwa Kina: Siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zinaelekea ukingoni kwani kilele in tarehe 10 mwezi huu wa Desemba ambayo ni siku ya haki za binadamu duniani. Nayo Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa leo inammulika mmoja wa washindi wa tuzo ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu ambaye ameweka rehani hata maisha yake kutetea waliokumbwa na ukatili wa kijinsia nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC . Akisema SOFEPADI ni kifupi cha shirika la mshikamano wa wanawake kwa ajili ya amani na maendeleo.  Jifunze Lugha ya Kiswahili: Kiswahili  leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua maana ya neno “KIFANDUGU”. Karibu sana!
12/7/202311 minutes, 41 seconds
Episode Artwork

Kituo cha afya cha Mtofaani kwa hisani ya Milele Zanzibar Foundation utekelezaji wa SDG 3

Shirika lisilo la kiserikali la Milele Zanzibar Foundation la Zanzibar Tanzania ambalo limejipambanua kujikita na utekelezaji wa malengo 12 kati ya malengo 17 ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu, limetekeleza lengo namba 3 la Afya Bora na Ustawi kwa kujenga kituo cha afya katika Shehia ya Michikichini, Unguja. Hamad Rashid wa redio washirika wetu Mviwata FM ya Morogoro - Tanzania amefika visiwani humo na kutuandalia makala hii.
12/6/20230
Episode Artwork

Kituo cha afya cha Mtofaani kwa hisani ya Milele Zanzibar Foundation utekelezaji wa SDG 3

Shirika lisilo la kiserikali la Milele Zanzibar Foundation la Zanzibar Tanzania ambalo limejipambanua kujikita na utekelezaji wa malengo 12 kati ya malengo 17 ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu, limetekeleza lengo namba 3 la Afya Bora na Ustawi kwa kujenga kituo cha afya katika Shehia ya Michikichini, Unguja. Hamad Rashid wa redio washirika wetu Mviwata FM ya Morogoro - Tanzania amefika visiwani humo na kutuandalia makala hii.
12/6/20234 minutes, 25 seconds
Episode Artwork

Solar Sister watekeleza kwa vitendo nishati safi kwa jamii za pembezoni

Kila uchao, sauti zinapazwa kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, tena hasa wakati huu ambapo wanachama wa mkataba wa Umoja wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC wakikutana Dubai, huko Falme za Kiarabu kwenye mkutano wao wa 28 au COP28. Tayari  hatua zimechukuliwa na shirika la kimataifa la Solar Sister kusaka nishati salama hasa kwa wanawake wa vijijini kama anavyoshuhudia mwanachama na mnufaika wake, Loveness Sabaya wa jamii ya kimasai kutoka Arusha nchini Tanzania kupitia video iliyochapishwa kwenye ukurasa wa X wa mkutano wa COP28. 
12/6/20230
Episode Artwork

Solar Sister watekeleza kwa vitendo nishati safi kwa jamii za pembezoni

Kila uchao, sauti zinapazwa kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, tena hasa wakati huu ambapo wanachama wa mkataba wa Umoja wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC wakikutana Dubai, huko Falme za Kiarabu kwenye mkutano wao wa 28 au COP28. Tayari  hatua zimechukuliwa na shirika la kimataifa la Solar Sister kusaka nishati salama hasa kwa wanawake wa vijijini kama anavyoshuhudia mwanachama na mnufaika wake, Loveness Sabaya wa jamii ya kimasai kutoka Arusha nchini Tanzania kupitia video iliyochapishwa kwenye ukurasa wa X wa mkutano wa COP28. 
12/6/20231 minute, 39 seconds
Episode Artwork

06 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki za binadamu Gaza na mkutano wa COP28. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani tutasalia huko huko COP28, kulikoni?Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk leo amelaani vikali ukiukaji mkubwa wa haki wa kingono dhidi ya Waisraeli unaodaiwa kutekelezwa na wanamgambo wa Hamas wakati wa mashambulizi yao ya kigaidi kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, huku wahudumu wa kibinadamu huko Gaza wakionya kuhusu hali mbaya ya raia, kutokana na kunaendelea kwa mashambulizi ya mabomu na watu kutawanywa eneo la kusini.Kila uchao, sauti zinapazwa kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, tena hasa wakati huu ambapo wanachama wa mkataba wa Umoja wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC wakikutana Dubai, huko Falme za Kiarabu kwenye mkutano wao wa 28 au COP28. Tayari  hatua zimechukuliwa na shirika la kimataifa la Solar Sister kusaka nishati salama hasa kwa wanawake wa vijijini kama anavyoshuhudia mwanachama na mnufaika wake, Loveness Sabaya wa jamii ya kimasai kutoka Arusha nchini Tanzania kupitia video iliyochapishwa kwenye ukurasa wa X wa mkutano wa COP28. Makala inakupeleka Zanzibar, Tanzania ambako Shirika lisilo la kiserikali la Milele Zanzibar Foundation limejenga kituo cha afya katika Shehia ya Michikichini - Unguja ikiwa ni utekelezaji wa lengo namba 3 la Umoja wa Mataifa la Maendeleo Endelevu linalohusu Afya Bora na Ustawi. Na mashinani tunakupeleka katika mkutano wa COP28 huko Dubai, Umoja wa Falme za kiarabu kupata ufafanuzi kuhusu hasara na uharibifu.  Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
12/6/20230
Episode Artwork

06 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki za binadamu Gaza na mkutano wa COP28. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani tutasalia huko huko COP28, kulikoni?Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk leo amelaani vikali ukiukaji mkubwa wa haki wa kingono dhidi ya Waisraeli unaodaiwa kutekelezwa na wanamgambo wa Hamas wakati wa mashambulizi yao ya kigaidi kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, huku wahudumu wa kibinadamu huko Gaza wakionya kuhusu hali mbaya ya raia, kutokana na kunaendelea kwa mashambulizi ya mabomu na watu kutawanywa eneo la kusini.Kila uchao, sauti zinapazwa kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi, tena hasa wakati huu ambapo wanachama wa mkataba wa Umoja wa Mabadiliko ya Tabianchi, UNFCCC wakikutana Dubai, huko Falme za Kiarabu kwenye mkutano wao wa 28 au COP28. Tayari  hatua zimechukuliwa na shirika la kimataifa la Solar Sister kusaka nishati salama hasa kwa wanawake wa vijijini kama anavyoshuhudia mwanachama na mnufaika wake, Loveness Sabaya wa jamii ya kimasai kutoka Arusha nchini Tanzania kupitia video iliyochapishwa kwenye ukurasa wa X wa mkutano wa COP28. Makala inakupeleka Zanzibar, Tanzania ambako Shirika lisilo la kiserikali la Milele Zanzibar Foundation limejenga kituo cha afya katika Shehia ya Michikichini - Unguja ikiwa ni utekelezaji wa lengo namba 3 la Umoja wa Mataifa la Maendeleo Endelevu linalohusu Afya Bora na Ustawi. Na mashinani tunakupeleka katika mkutano wa COP28 huko Dubai, Umoja wa Falme za kiarabu kupata ufafanuzi kuhusu hasara na uharibifu.  Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
12/6/202310 minutes
Episode Artwork

Uchunguzi ufanywe Gaza kuhusu madai ya ukatili wa kingono wakati wa shambulio la Hamas - OHCHR

Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk leo amelaani vikali ukiukaji mkubwa wa haki wa kingono dhidi ya Waisraeli unaodaiwa kutekelezwa na wanamgambo wa Hamas wakati wa mashambulizi yao ya kigaidi kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, huku wahudumu wa kibinadamu huko Gaza wakionya kuhusu hali mbaya ya raia. Kamishina mkuu Türk akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis amesisitiza kuhusu hofu yake kwa hatma ya raia akirejea wito wa kukomesha uhasama mara moja kunusuru Maisha ya raia na miundombinu yao. Na kuhusu madai ya Umoja wa Mataifa kuwa na misimamo miwili kunapokuja masuala ya ukatili Gaza amekanusha madai hayo na kubainisha kuwa amefahamishwa kuhusu madai ya unyanyasaji wa kijinsia na kingono wakati wa shambulio la Hamas kwa jamii za kusini mwa Israeli.Amesema kwa uchungu mkubwa kwamba “Ni bayana kwamba mashambulizi ya kikatili yanapaswa kuchunguzwa kikamilifu, kwa uchunguzi huru kwa sababu hilo ni deni letu kwa waathirika.”Juliette Touma, ambaye ni msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina, UNRWA, wakati wa mahojiano na vyombo vya habari yaliyochapishwa mtandaoni leo kuhusu hali mbaya ya raia Gaza amesema "Nadhani tumegonga mwamba na ni hatua ya mabadiliko katika vita hivi  hali inazidi kuwa mbaya kila dakika tunapokea simu za mara kwa mara za dharura kutoka kwa wafanyakazi wenzetu na marafiki."​Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA mapambano yameshika kasi Israel ikishambulia kila kona kwa njia ya anga, baharini na ardhinihususan Mashariki mwa mji wa Gaza kwenye na kuna tarifa za takribani watu 60,000 kuwasili katika kambi ya wakimbizi ya Jabalia na Khan Younis saa chache zilizopita na Hamas inaendelea kuvurumisha maroketi kwenda Israel kutokea Gaza.Mbali ya changamoto kubwa za kiafya kutokana na mrundikano wa watu na mazingira machafu sasa shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa WFP WFP linaonya kuhusu janga kubwa la njaa.
12/6/20230
Episode Artwork

Uchunguzi ufanywe Gaza kuhusu madai ya ukatili wa kingono wakati wa shambulio la Hamas - OHCHR

Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk leo amelaani vikali ukiukaji mkubwa wa haki wa kingono dhidi ya Waisraeli unaodaiwa kutekelezwa na wanamgambo wa Hamas wakati wa mashambulizi yao ya kigaidi kusini mwa Israel tarehe 7 Oktoba, huku wahudumu wa kibinadamu huko Gaza wakionya kuhusu hali mbaya ya raia. Kamishina mkuu Türk akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis amesisitiza kuhusu hofu yake kwa hatma ya raia akirejea wito wa kukomesha uhasama mara moja kunusuru Maisha ya raia na miundombinu yao. Na kuhusu madai ya Umoja wa Mataifa kuwa na misimamo miwili kunapokuja masuala ya ukatili Gaza amekanusha madai hayo na kubainisha kuwa amefahamishwa kuhusu madai ya unyanyasaji wa kijinsia na kingono wakati wa shambulio la Hamas kwa jamii za kusini mwa Israeli.Amesema kwa uchungu mkubwa kwamba “Ni bayana kwamba mashambulizi ya kikatili yanapaswa kuchunguzwa kikamilifu, kwa uchunguzi huru kwa sababu hilo ni deni letu kwa waathirika.”Juliette Touma, ambaye ni msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina, UNRWA, wakati wa mahojiano na vyombo vya habari yaliyochapishwa mtandaoni leo kuhusu hali mbaya ya raia Gaza amesema "Nadhani tumegonga mwamba na ni hatua ya mabadiliko katika vita hivi  hali inazidi kuwa mbaya kila dakika tunapokea simu za mara kwa mara za dharura kutoka kwa wafanyakazi wenzetu na marafiki."​Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA mapambano yameshika kasi Israel ikishambulia kila kona kwa njia ya anga, baharini na ardhinihususan Mashariki mwa mji wa Gaza kwenye na kuna tarifa za takribani watu 60,000 kuwasili katika kambi ya wakimbizi ya Jabalia na Khan Younis saa chache zilizopita na Hamas inaendelea kuvurumisha maroketi kwenda Israel kutokea Gaza.Mbali ya changamoto kubwa za kiafya kutokana na mrundikano wa watu na mazingira machafu sasa shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa WFP WFP linaonya kuhusu janga kubwa la njaa.
12/6/20231 minute, 53 seconds
Episode Artwork

Tushikamane kwa vitendo kupinga ukatili wa kijinsia - Mwanariadha

Violah Cheptoo au Violah Lagat ni maarufu sana sio tu nchini Kenya bali pia nje ya taifa hilo kutokana na umaarufu wake kwenye mbio za nyika au marathoni. Lakini zaidi ya hivyo, Viola anatambulika pia nje ya michezo kuwa mpeperushaji wa bendera ya kupinga ukatili wa kijinsia. Ni kwa mantiki hiyo katika siku hizi 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alitumia fursa ya uwepo wa mwanariadha huyo hapa Marekani wakati wa mbio za Marathoni jijini New York, Marekani mwezi ulipita wa Novemba kufahamu kwa kina usuli wa harakati hizo nje ya riadha na alianza kwa kumuuliza kuhusu taasisi aliyoanzisha mwaka 2021 inayoitwa Tirop’s Angels.
12/5/20230
Episode Artwork

Tushikamane kwa vitendo kupinga ukatili wa kijinsia - Mwanariadha

Violah Cheptoo au Violah Lagat ni maarufu sana sio tu nchini Kenya bali pia nje ya taifa hilo kutokana na umaarufu wake kwenye mbio za nyika au marathoni. Lakini zaidi ya hivyo, Viola anatambulika pia nje ya michezo kuwa mpeperushaji wa bendera ya kupinga ukatili wa kijinsia. Ni kwa mantiki hiyo katika siku hizi 16 za kupinga ukatili dhidi ya wanawake Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alitumia fursa ya uwepo wa mwanariadha huyo hapa Marekani wakati wa mbio za Marathoni jijini New York, Marekani mwezi ulipita wa Novemba kufahamu kwa kina usuli wa harakati hizo nje ya riadha na alianza kwa kumuuliza kuhusu taasisi aliyoanzisha mwaka 2021 inayoitwa Tirop’s Angels.
12/5/20235 minutes, 48 seconds
Episode Artwork

05 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alitumia fursa ya uwepo wa mwanariadha kutoka nchini Kenya hapa Marekani wakati wa mbio za Marathoni jijini New York, Marekani mwezi ulipita wa Novemba kufahamu kwa kina usuli wa harakati hizo nje ya riadha hasa kuhusu taasisi aliyoanzisha mwaka 2021 inayoitwa Tirop’s Angels. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 unaendelea huko Dubai na leo ukimulika mada mbalimbali ikiwemo kuongeza ufadhili kupambana na janga la tabianchi, kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa kujenga mnepo katika sekta ya nishati hasa mifumo ya upoozaji ambayo imeelezwa kuwa ni mzigo mara mbili na inatumia kiwango kikubwa cha nitashi ya umeme hasa kwa viyoyozi na mitambo mingine , pia mkutano huo utasikia kutoka kwa watu wa jamii za asili.Mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa leo yameonya kuhusu kuendelea kwa hali mbaya ya kibinadamu huko Gaza yakisema kati ya mchana wa tarehe 3 Desemba na tarehe 4 Desemba Gaza imeshuhudia mashambulizi makubwa Zaidi ya mabomu tangu kuanza kwa mzozo huu mpya kutoka angani, ardhini na baharini, huku maroketo yanayovurumishwa na kundi la Kipalestina la Hamas Kwenda Gaza nayo yakiendelea. Na mkutano wa Umoja wa Mataifa wa ulinzi wa Amani ulifungua pazia hii leo huko Accra Ghana ambako mawaziri na wajumbe kutoka nchi zaidi ya 85 na mashirika ya kimataifa wanakutana kwa siku mbili kwa mara ya kwanza barani Afrika, ili kuwapa fursa nchi wachangiaji wa vikosi vya ulinzi wa Amani kudhihirisha msaada wao wa kisiasa na kuahidi hatua madhubuti za kuimarisha juhudi za ulinzi wa Amani wa Umoja wa Mataifa kwenda sanjari na mahitaji na changamoto za sasa na zijazo.. Mashinani tunakuletea ujumbe wa mwanaharakati ambaye amezungumza na washirika wetu Radio Dumus katika sherehe za “SHE Leads” nchini Kenya, shirika lisilo la kiserikali linalopazia sauti  masuala ya wanawake na wasichana, na anatumia fursa ya kusikilizwa kote duniani kupitia njia ya radio kuwasilisha ujumbe wake kuhusu ukatili wa kijinsia, GBV.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/5/20230
Episode Artwork

05 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alitumia fursa ya uwepo wa mwanariadha kutoka nchini Kenya hapa Marekani wakati wa mbio za Marathoni jijini New York, Marekani mwezi ulipita wa Novemba kufahamu kwa kina usuli wa harakati hizo nje ya riadha hasa kuhusu taasisi aliyoanzisha mwaka 2021 inayoitwa Tirop’s Angels. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 unaendelea huko Dubai na leo ukimulika mada mbalimbali ikiwemo kuongeza ufadhili kupambana na janga la tabianchi, kupunguza uzalishaji wa hewa ukaa kujenga mnepo katika sekta ya nishati hasa mifumo ya upoozaji ambayo imeelezwa kuwa ni mzigo mara mbili na inatumia kiwango kikubwa cha nitashi ya umeme hasa kwa viyoyozi na mitambo mingine , pia mkutano huo utasikia kutoka kwa watu wa jamii za asili.Mashirika ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa leo yameonya kuhusu kuendelea kwa hali mbaya ya kibinadamu huko Gaza yakisema kati ya mchana wa tarehe 3 Desemba na tarehe 4 Desemba Gaza imeshuhudia mashambulizi makubwa Zaidi ya mabomu tangu kuanza kwa mzozo huu mpya kutoka angani, ardhini na baharini, huku maroketo yanayovurumishwa na kundi la Kipalestina la Hamas Kwenda Gaza nayo yakiendelea. Na mkutano wa Umoja wa Mataifa wa ulinzi wa Amani ulifungua pazia hii leo huko Accra Ghana ambako mawaziri na wajumbe kutoka nchi zaidi ya 85 na mashirika ya kimataifa wanakutana kwa siku mbili kwa mara ya kwanza barani Afrika, ili kuwapa fursa nchi wachangiaji wa vikosi vya ulinzi wa Amani kudhihirisha msaada wao wa kisiasa na kuahidi hatua madhubuti za kuimarisha juhudi za ulinzi wa Amani wa Umoja wa Mataifa kwenda sanjari na mahitaji na changamoto za sasa na zijazo.. Mashinani tunakuletea ujumbe wa mwanaharakati ambaye amezungumza na washirika wetu Radio Dumus katika sherehe za “SHE Leads” nchini Kenya, shirika lisilo la kiserikali linalopazia sauti  masuala ya wanawake na wasichana, na anatumia fursa ya kusikilizwa kote duniani kupitia njia ya radio kuwasilisha ujumbe wake kuhusu ukatili wa kijinsia, GBV.  Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
12/5/202311 minutes, 21 seconds
Episode Artwork

Walio hatarini zaidi waletwe ‘mbele ya mstari’ wa ufadhili wa tabianchi - COP28

Leo huko Dubai, UAE kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira, COP28, Akaunti ya Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi imezinduliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu na Masuala ya Dharura (OCHA) ili kutoa njia ya ziada ya kufadhili hatua za kibinadamu kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi kama vile mafuriko, ukame, dhoruba na joto kali, na kujenga uwezo wa kustahimili tabianchi. COP28 inaendelea Dubai, na ni dhahiri wadau wa mazingira na tabianchi wameshaona kuna athari mbaa za mabadiliko ya tabianchi zinazoongeza machungu kwa wanadamu ambao wengine tayari wanakabiliwa na changamoto nyingine za kibinadamu. OCHA ambayo ni mdau muhimu wa misaada ya kibinadamu, pia ni sehemu muhimu ya Mfuko Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Kukabiliana na Dharura (CERF), ambao kila mwaka, kati ya robo na theluthi ya ufadhili wake unaenda kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi. Naibu wa Mkuu wa OCHA, Joyce Msuya amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufadhili huu akisema "tunapoingia katika ulimwengu ambao mabadiliko ya tabianchi yanashikilia upanga juu ya kuongezeka kwa idadi ya watu". Jopo la serikali (duniani) kuhusu mabadiliko ya tabianchi IPCC, takribani watu bilioni 3.5, karibu nusu ya wanadamu wote duniani, wanaishi katika maeneo ambayo yanaweza kuathiriwa sana na mabadiliko ya tabianchi. Ili kusaidia nchi zilizo hatarini katika kujilinda na matokeo mabaya zaidi ya uharibifu wa tabianchi, mfuko wa hasara na uharibifu ulikubaliwa katika COP27 huko Sharm el-Sheikh mwaka jana na kuidhinishwa kuanza kutumika siku ya ufunguzi wa COP28 umesifiwa kama chombo muhimu cha haki ya tabianchi na. matokeo makubwa ya kwanza ya mkusanyiko huo unaoendelea hadi tarehe 10 mwezi huu. Zaidi ya dola milioni 650 zimeripotiwa kuahidiwa kufikia sasa na watetezi wa jamii zilizo katika mazingira magumu waliopo Dubai wamesisitiza haja ya kuhakikisha kwamba wale walioathirika zaidi wananufaika na ufadhili huo. Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi Filippo Grandi amesisitiz, "Sauti ya wale waliofurushwa na dharura hii lazima isikike, na lazima wajumuishwe katika mipango na ugawaji wa rasilimali. 
12/4/20230
Episode Artwork

Walio hatarini zaidi waletwe ‘mbele ya mstari’ wa ufadhili wa tabianchi - COP28

Leo huko Dubai, UAE kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira, COP28, Akaunti ya Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi imezinduliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu na Masuala ya Dharura (OCHA) ili kutoa njia ya ziada ya kufadhili hatua za kibinadamu kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi kama vile mafuriko, ukame, dhoruba na joto kali, na kujenga uwezo wa kustahimili tabianchi. COP28 inaendelea Dubai, na ni dhahiri wadau wa mazingira na tabianchi wameshaona kuna athari mbaa za mabadiliko ya tabianchi zinazoongeza machungu kwa wanadamu ambao wengine tayari wanakabiliwa na changamoto nyingine za kibinadamu. OCHA ambayo ni mdau muhimu wa misaada ya kibinadamu, pia ni sehemu muhimu ya Mfuko Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa Kukabiliana na Dharura (CERF), ambao kila mwaka, kati ya robo na theluthi ya ufadhili wake unaenda kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi. Naibu wa Mkuu wa OCHA, Joyce Msuya amesisitiza umuhimu wa kuongeza ufadhili huu akisema "tunapoingia katika ulimwengu ambao mabadiliko ya tabianchi yanashikilia upanga juu ya kuongezeka kwa idadi ya watu". Jopo la serikali (duniani) kuhusu mabadiliko ya tabianchi IPCC, takribani watu bilioni 3.5, karibu nusu ya wanadamu wote duniani, wanaishi katika maeneo ambayo yanaweza kuathiriwa sana na mabadiliko ya tabianchi. Ili kusaidia nchi zilizo hatarini katika kujilinda na matokeo mabaya zaidi ya uharibifu wa tabianchi, mfuko wa hasara na uharibifu ulikubaliwa katika COP27 huko Sharm el-Sheikh mwaka jana na kuidhinishwa kuanza kutumika siku ya ufunguzi wa COP28 umesifiwa kama chombo muhimu cha haki ya tabianchi na. matokeo makubwa ya kwanza ya mkusanyiko huo unaoendelea hadi tarehe 10 mwezi huu. Zaidi ya dola milioni 650 zimeripotiwa kuahidiwa kufikia sasa na watetezi wa jamii zilizo katika mazingira magumu waliopo Dubai wamesisitiza haja ya kuhakikisha kwamba wale walioathirika zaidi wananufaika na ufadhili huo. Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi Filippo Grandi amesisitiz, "Sauti ya wale waliofurushwa na dharura hii lazima isikike, na lazima wajumuishwe katika mipango na ugawaji wa rasilimali. 
12/4/20232 minutes, 6 seconds
Episode Artwork

04 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia yaliyojiri katika Mkutano wa COP28 na miradi ya Benki ya Dunia nchini Tanzania.  Makala inatupeleka nchini Kenya na mashinani tunakuletea uchambuzi wa ibara ya 14 ya tamko la haki za binadamu.Leo huko Dubai, UAE kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira, COP28, Akaunti ya Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi imezinduliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu na Masuala ya Dharura (OCHA) ili kutoa njia ya ziada ya kufadhili hatua za kibinadamu kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi kama vile mafuriko, ukame, dhoruba na joto kali, na kujenga uwezo wa kustahimili tabianchi.Tarehe 19 Desemba mwaka 2019, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio namba 74/245, ambalo liliteua tarehe 4 Desemba kuwa Siku ya Kimataifa ya Benki kwa kutambua mchango mkubwa wa benki za maendeleo za kimataifa na benki nyingine za maendeleo za kimataifa katika kuleta maendeleo endelevu na kuchangia uboreshaji wa hali za maisha za wananchi. Makala inamulika siku ya watu wenye ulemavu duniani iliyoadhimishwa jana desemba 3 ikiwa na maudhui Ushirikiano katika hatua ya kuokoa na kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, (SDGs) kwa  pamoja na watu wenye ulemavu. Na ninakupeleka nchini Kenya kummulika mchezeshaji muziki au DJ mwenye ulemavu wa kutoona John Ndichu al maaruf, DJ Ndichi Kings. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza naye akiwa eneo la Ruiru, Kaunti ya Kiambu. Na mashinani katika kuelekea siku ya haki za binadamu itakayoadhimishwa tayere 10 Desemba leo Dkt. Anna Henga mkurugenzi mtendaji wa kituo cha sheria na haki za binadamu nchini Tanzania anatufafanulia kuhusu Ibara ya 14 ya tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/4/20230
Episode Artwork

04 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia yaliyojiri katika Mkutano wa COP28 na miradi ya Benki ya Dunia nchini Tanzania.  Makala inatupeleka nchini Kenya na mashinani tunakuletea uchambuzi wa ibara ya 14 ya tamko la haki za binadamu.Leo huko Dubai, UAE kwenye Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mazingira, COP28, Akaunti ya Hatua Dhidi ya Mabadiliko ya Tabianchi imezinduliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kuratibu Misaada ya Kibinadamu na Masuala ya Dharura (OCHA) ili kutoa njia ya ziada ya kufadhili hatua za kibinadamu kwenye majanga yanayohusiana na tabianchi kama vile mafuriko, ukame, dhoruba na joto kali, na kujenga uwezo wa kustahimili tabianchi.Tarehe 19 Desemba mwaka 2019, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio namba 74/245, ambalo liliteua tarehe 4 Desemba kuwa Siku ya Kimataifa ya Benki kwa kutambua mchango mkubwa wa benki za maendeleo za kimataifa na benki nyingine za maendeleo za kimataifa katika kuleta maendeleo endelevu na kuchangia uboreshaji wa hali za maisha za wananchi. Makala inamulika siku ya watu wenye ulemavu duniani iliyoadhimishwa jana desemba 3 ikiwa na maudhui Ushirikiano katika hatua ya kuokoa na kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, (SDGs) kwa  pamoja na watu wenye ulemavu. Na ninakupeleka nchini Kenya kummulika mchezeshaji muziki au DJ mwenye ulemavu wa kutoona John Ndichu al maaruf, DJ Ndichi Kings. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza naye akiwa eneo la Ruiru, Kaunti ya Kiambu. Na mashinani katika kuelekea siku ya haki za binadamu itakayoadhimishwa tayere 10 Desemba leo Dkt. Anna Henga mkurugenzi mtendaji wa kituo cha sheria na haki za binadamu nchini Tanzania anatufafanulia kuhusu Ibara ya 14 ya tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
12/4/202311 minutes, 1 second
Episode Artwork

Siku ya ulemavu duniani: Kauli kutoka kwa mchezesha muziki mwenye ulemavu wa kutoona

Siku ya watu wenye ulemavu duniani iliadhimishwa jana desemba 3 ikiwa na maudhui Ushirikiano katika hatua ya kuokoa na kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, (SDGs) kwa  pamoja na watu wenye ulemavu, na leo inakupeleka nchini Kenya kummulika mchezeshaji muziki au DJ mwenye ulemavu wa kutoona John Ndichu al maarufu, DJ NdichiKings. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza naye akiwa eneo la Ruiru, Kaunti ya Kiambu. 
12/4/20230
Episode Artwork

Siku ya ulemavu duniani: Kauli kutoka kwa mchezesha muziki mwenye ulemavu wa kutoona

Siku ya watu wenye ulemavu duniani iliadhimishwa jana desemba 3 ikiwa na maudhui Ushirikiano katika hatua ya kuokoa na kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu, (SDGs) kwa  pamoja na watu wenye ulemavu, na leo inakupeleka nchini Kenya kummulika mchezeshaji muziki au DJ mwenye ulemavu wa kutoona John Ndichu al maarufu, DJ NdichiKings. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza naye akiwa eneo la Ruiru, Kaunti ya Kiambu. 
12/4/20233 minutes, 14 seconds
Episode Artwork

Nchini Tanzania Benki ya Dunia yasaidia ukuzaji wa rasilimali watu na maendeleo

Tarehe 19 Desemba mwaka 2019, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio namba 74/245, ambalo liliteua tarehe 4 Desemba kuwa Siku ya Kimataifa ya Benki kwa kutambua mchango mkubwa wa benki za maendeleo za kimataifa na benki nyingine za maendeleo za kimataifa katika kuleta maendeleo endelevu na kuchangia uboreshaji wa hali za maisha za wananchi. Afrika ni Bara lenye idadi kubwa ya watoto na vijana na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatafsiri maana ya takwimu hizo. “Habari hii ni nzuri na vile vile ni mbaya kwetu, Hali hii inaweza kuwa nzuri na yenye tija iwapo tutawekeza kwenye rasilimali watu kwa kuhakikisha uwepo wa afya bora, elimu bora yenye stadi za maisha.”  Benki ya Dunia, kama moja ya wadau wa Maendeleo katika nchi ya Tanzania kupitia chama chake cha maendeleo cha kimataifa IDA ikaitikia wito huo wa Rais Samia kwa kuwekeza katika nyanja mbalimbali na wanufaika wa miradi hiyo wanaeleza matunda ya uwekezaji.Dorice Msafiri wa jijini Dar es Salaam ni mnufaika wa miradi ya kuwainua wanawake “Naweza nikawashauri wanawake wengine ambao wangetamani kujiunga na na kozi za uhandisi ni mambo magumu lakini tunaweza wote. Kama ambavyo wanaweza wanaume na sisi pia tunaweza.”Mradi wau meme vijijini, Sofia Mkuya ni fundi cherehani kutoka Bahi mkoani Dodoma “Tangu umeme ulivyokuja ( katika eneo letu) ninashona mpaka usiku na ninatumia pasi ya umeme kunyoosha nguo situmii mkaa tena.” Mradi wa maji vijijini, Herman Mwendowasa mkazi wa kijiji cha Mtisi Villa mkoani Katavi, “Tumeondokana na changamoto ya maji machafu yenye tope maradhi, shida nyingi.” Na huko visiwani Zanzibar Benki ya Dunia inaendesha miradi mbalimbali ikiwemo wa nishati ya umeme wa Solar ambao utakapo kamilika unatarajiwa kutoa umeme Kilowati 132 kutoka Kilowati 32 zinazo zalisha hivi sasa. Mbali na mchango wao muhimu katika maendeleo ya Tanzania Mwakilishi mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania Nathan Belete anatoa pongezi, “Tunaipongeza serikali kwa kutoa kipaumbele kwenye elimu kwenye mkakati wao wa ukuaji kwakuzingatia idadi ya watu inaendelea kuongezeka nchini Tanzania hili ni suala muhimu kabisa.”
12/4/20230
Episode Artwork

Nchini Tanzania Benki ya Dunia yasaidia ukuzaji wa rasilimali watu na maendeleo

Tarehe 19 Desemba mwaka 2019, Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa lilipitisha azimio namba 74/245, ambalo liliteua tarehe 4 Desemba kuwa Siku ya Kimataifa ya Benki kwa kutambua mchango mkubwa wa benki za maendeleo za kimataifa na benki nyingine za maendeleo za kimataifa katika kuleta maendeleo endelevu na kuchangia uboreshaji wa hali za maisha za wananchi. Afrika ni Bara lenye idadi kubwa ya watoto na vijana na Rais wa Tanzania Samia Suluhu Hassan anatafsiri maana ya takwimu hizo. “Habari hii ni nzuri na vile vile ni mbaya kwetu, Hali hii inaweza kuwa nzuri na yenye tija iwapo tutawekeza kwenye rasilimali watu kwa kuhakikisha uwepo wa afya bora, elimu bora yenye stadi za maisha.”  Benki ya Dunia, kama moja ya wadau wa Maendeleo katika nchi ya Tanzania kupitia chama chake cha maendeleo cha kimataifa IDA ikaitikia wito huo wa Rais Samia kwa kuwekeza katika nyanja mbalimbali na wanufaika wa miradi hiyo wanaeleza matunda ya uwekezaji.Dorice Msafiri wa jijini Dar es Salaam ni mnufaika wa miradi ya kuwainua wanawake “Naweza nikawashauri wanawake wengine ambao wangetamani kujiunga na na kozi za uhandisi ni mambo magumu lakini tunaweza wote. Kama ambavyo wanaweza wanaume na sisi pia tunaweza.”Mradi wau meme vijijini, Sofia Mkuya ni fundi cherehani kutoka Bahi mkoani Dodoma “Tangu umeme ulivyokuja ( katika eneo letu) ninashona mpaka usiku na ninatumia pasi ya umeme kunyoosha nguo situmii mkaa tena.” Mradi wa maji vijijini, Herman Mwendowasa mkazi wa kijiji cha Mtisi Villa mkoani Katavi, “Tumeondokana na changamoto ya maji machafu yenye tope maradhi, shida nyingi.” Na huko visiwani Zanzibar Benki ya Dunia inaendesha miradi mbalimbali ikiwemo wa nishati ya umeme wa Solar ambao utakapo kamilika unatarajiwa kutoa umeme Kilowati 132 kutoka Kilowati 32 zinazo zalisha hivi sasa. Mbali na mchango wao muhimu katika maendeleo ya Tanzania Mwakilishi mkazi wa Benki ya Dunia nchini Tanzania Nathan Belete anatoa pongezi, “Tunaipongeza serikali kwa kutoa kipaumbele kwenye elimu kwenye mkakati wao wa ukuaji kwakuzingatia idadi ya watu inaendelea kuongezeka nchini Tanzania hili ni suala muhimu kabisa.”
12/4/20232 minutes, 5 seconds
Episode Artwork

SHDEPHA+ yatekeleza kwa vitendo kauli ya UNAIDS ya jamii zishike hatamu kutokomeza Ukimwi

Leo ni siku ya Ukimwi duniani takwimu zikionesha kupungua sio tu kwa asilimia 70 ya vifo ikilinganishwa na mwaka 2004, idadi ilipokuwa kiwango cha juu zaidi duniani, bali pia maambukizi mapya ikilinganishwa na miaka ya 1980. Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la UNAIDS linasema miongoni mwa sababu za kupungua ni ushiriki wa jamii, yaani jamii kushika hatamu za vita dhidi ya Ukimwi. Hilo ni dhahiri huko nchini Tanzania ambako mashirika ya kiraia ikiwemo mtandao wa kitaifa wa maendeleo ya afya, huduma na uegemezi wa watu waishio na Virusi Vya Ukimwi na Ukimwi, SHDEPHA+, unatekeleza kwa vitendo ujumbe wa mwaka huu wa siku ya Ukimwi duniani, wa Achia Jamii Ziongoze Harakati dhidi ya Ukimwi. Assumpta Massoi anafafanua kinagaubaga kwenye makala hii kile kinachofanyika. 
12/1/20230
Episode Artwork

SHDEPHA+ yatekeleza kwa vitendo kauli ya UNAIDS ya jamii zishike hatamu kutokomeza Ukimwi

Leo ni siku ya Ukimwi duniani takwimu zikionesha kupungua sio tu kwa asilimia 70 ya vifo ikilinganishwa na mwaka 2004, idadi ilipokuwa kiwango cha juu zaidi duniani, bali pia maambukizi mapya ikilinganishwa na miaka ya 1980. Umoja wa Mataifa kupitia shirika lake la UNAIDS linasema miongoni mwa sababu za kupungua ni ushiriki wa jamii, yaani jamii kushika hatamu za vita dhidi ya Ukimwi. Hilo ni dhahiri huko nchini Tanzania ambako mashirika ya kiraia ikiwemo mtandao wa kitaifa wa maendeleo ya afya, huduma na uegemezi wa watu waishio na Virusi Vya Ukimwi na Ukimwi, SHDEPHA+, unatekeleza kwa vitendo ujumbe wa mwaka huu wa siku ya Ukimwi duniani, wa Achia Jamii Ziongoze Harakati dhidi ya Ukimwi. Assumpta Massoi anafafanua kinagaubaga kwenye makala hii kile kinachofanyika. 
12/1/20235 minutes, 22 seconds
Episode Artwork

01 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya UKIMWI duniani na Mkutano wa COP28.  Makala inatupeleka nchini Tanzania na mashinani tunasalia hapa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kulikoni?Leo ni siku ya UKIMWI duniani ambapo mwaka huu shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili ukimwi UNAIDS limetenga maudhui kuwa “Achia Jamii Ziongoze” kwa lengo la kuzisihi serikali kote duniani kutumia ipasavyo nguvu ya jamii mashinani ili hatimaye kutokomeza ugonjwa wa Ukimwi ifikapo mwaka 2030  huku Afrika, Kusini mwa Janga la Sahara ikitajwa kuwa muathirika mkumbwa wa maambukizi mapya ya VVU. Na sasa tuangazie majanga ya asili. Mkutano wa COP28 ukiendelea Dubai, Falme za kiarabu kusaka suluhu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi, huko Somalia mafurikio makubwa yameendelea kusababisha zahma kwa wananchi ambapo Umoja wa Mataifa kupitia ofisi yake ya uratibu wa misaada ya dharura, OCHA umezungumzia hali halisi na nini kinafanyika.Makala inatupeleka mkoani Shinyanga nchini Tanzania ambako huko mtandao wa kitaifa wa maendeleo ya afya, huduma na uegemezi wa watu waishio na Virusi Vya Ukimwi na Ukimwi, SHDEPHA+, unatekeleza kwa vitendo ujumbe wa mwaka huu wa siku ya Ukimwi duniani, Jamii iongoze katika harakati za kutokomeza Ukimwi.Katika mashinani utasikia ujumbe kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kukabili Ukimwi UNAIDS. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
12/1/20230
Episode Artwork

01 DESEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya UKIMWI duniani na Mkutano wa COP28.  Makala inatupeleka nchini Tanzania na mashinani tunasalia hapa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kulikoni?Leo ni siku ya UKIMWI duniani ambapo mwaka huu shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili ukimwi UNAIDS limetenga maudhui kuwa “Achia Jamii Ziongoze” kwa lengo la kuzisihi serikali kote duniani kutumia ipasavyo nguvu ya jamii mashinani ili hatimaye kutokomeza ugonjwa wa Ukimwi ifikapo mwaka 2030  huku Afrika, Kusini mwa Janga la Sahara ikitajwa kuwa muathirika mkumbwa wa maambukizi mapya ya VVU. Na sasa tuangazie majanga ya asili. Mkutano wa COP28 ukiendelea Dubai, Falme za kiarabu kusaka suluhu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi, huko Somalia mafurikio makubwa yameendelea kusababisha zahma kwa wananchi ambapo Umoja wa Mataifa kupitia ofisi yake ya uratibu wa misaada ya dharura, OCHA umezungumzia hali halisi na nini kinafanyika.Makala inatupeleka mkoani Shinyanga nchini Tanzania ambako huko mtandao wa kitaifa wa maendeleo ya afya, huduma na uegemezi wa watu waishio na Virusi Vya Ukimwi na Ukimwi, SHDEPHA+, unatekeleza kwa vitendo ujumbe wa mwaka huu wa siku ya Ukimwi duniani, Jamii iongoze katika harakati za kutokomeza Ukimwi.Katika mashinani utasikia ujumbe kutoka kwa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kukabili Ukimwi UNAIDS. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
12/1/202313 minutes, 51 seconds
Episode Artwork

Katika kutokomeza VVU mchango wa jamii hasa vijana unahitajika sana - Jane

Leo ni siku ya ukimwi duniani ambapo mwaka huu shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili ukimwi UNAIDS limetenga maudhui kuwa “Achia Jamii Ziongoze” kwa lengo la kuzisihi serikali kote duniani kutumia ipasavyo nguvu ya jamii mashinani ili hatimaye kutokomeza ugonjwa wa Ukimwi ifikapo mwaka 2030  huku Afrika Kusini mwa Janga la Sahara ikitajwa kuwa muathirika mkumbwa wa maambukizi mapya ya VVU. Kwa mujibu wa takwimu za UNAIDS za mwaka huu 2023 wasichana vigori na vijana walichangia zaidi ya asilimia 77 ya maambukizi mapya ya VVU Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara mwaka jana 2022 miongoni mwa vijana wenye umri wa miaka 15-24.Na wasichana wana uwezekano mara tatu zaidi ya kupata VVU kuliko wenzao wa kiume. Kenya ikiwa ndani ya nchi 15 zenye maambukizi makubwa ya VVU Afrika juhudi kubwa zinafanywa kupitia serikali, asasi za kiraia na hata watu binafsi kusongesha mbele vita dhidi ya VVU kwa msaada wa wadau mbalimbali wa kitaifa na kimataifa ukiwemo Umoja wa Mataifa ambao leo katia kuadhimisha siku hii jijini Nairobi umeandaa mashindano ya riadha ya kilometa 5 na kuchangisha fedha zitakazowasaidia yatima wa ugonjwa huo kama anavyofafanua Jane Sinyei Afisa Uratibu Msaidisi wa ofisi ya Umoja wa Mataifa Nairobi UNON.“Zile fedha ambayo tutapata itaenda kusaidia watoto wale wasio na wazazi, wasio na kitu chochote hivyo tutakuwa tunafanya kazi ya kusaidia wasiojiweza. Pia tutafanya vipimo vya VVUnkwa wale ambao watakuwa na virudsi hivyo wataelimishwa jinsi ya kufika kwa madaktari, kupata dawa na kwa wale ambao hawatakuwa na virusi vya ukimwi wataelimishwa jinsi ya kuendelea kujikinga na VVU ili wazuie kupata ukimwi na kusambazia wengine ukimwi.” Jane ana ujumbe kwa vijana ambao ndio kundi kubwa la waathirika wa VVU“Vijana tunawasihi mje msitari wa mbele , nyinyini viongozi wa leo na kesho na hapa Kenya mko wengi sana kuliko sisi. Mje mjifunze jinsi mtakavyojikinga na ukimwi, Homa ya ini aina B na magonjwa ya zinaa, na kuelimisha arafiki zenu ili wajikinge na haya magonjwa, muwe na afya bora ili muongize watu wote katika hii nchi yetu.”Nchi za Afrika zinazoongoza kwa VVU kwamujibu wa UNAUDS ni Eswatini inayoshika namba moja ikifuatiwa na Lesotho, Botswana na Zimbabwe. Tanzania inashika namba 11, Kenya 12 na Uganda ya 13.
12/1/20230
Episode Artwork

Katika kutokomeza VVU mchango wa jamii hasa vijana unahitajika sana - Jane

Leo ni siku ya ukimwi duniani ambapo mwaka huu shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili ukimwi UNAIDS limetenga maudhui kuwa “Achia Jamii Ziongoze” kwa lengo la kuzisihi serikali kote duniani kutumia ipasavyo nguvu ya jamii mashinani ili hatimaye kutokomeza ugonjwa wa Ukimwi ifikapo mwaka 2030  huku Afrika Kusini mwa Janga la Sahara ikitajwa kuwa muathirika mkumbwa wa maambukizi mapya ya VVU. Kwa mujibu wa takwimu za UNAIDS za mwaka huu 2023 wasichana vigori na vijana walichangia zaidi ya asilimia 77 ya maambukizi mapya ya VVU Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara mwaka jana 2022 miongoni mwa vijana wenye umri wa miaka 15-24.Na wasichana wana uwezekano mara tatu zaidi ya kupata VVU kuliko wenzao wa kiume. Kenya ikiwa ndani ya nchi 15 zenye maambukizi makubwa ya VVU Afrika juhudi kubwa zinafanywa kupitia serikali, asasi za kiraia na hata watu binafsi kusongesha mbele vita dhidi ya VVU kwa msaada wa wadau mbalimbali wa kitaifa na kimataifa ukiwemo Umoja wa Mataifa ambao leo katia kuadhimisha siku hii jijini Nairobi umeandaa mashindano ya riadha ya kilometa 5 na kuchangisha fedha zitakazowasaidia yatima wa ugonjwa huo kama anavyofafanua Jane Sinyei Afisa Uratibu Msaidisi wa ofisi ya Umoja wa Mataifa Nairobi UNON.“Zile fedha ambayo tutapata itaenda kusaidia watoto wale wasio na wazazi, wasio na kitu chochote hivyo tutakuwa tunafanya kazi ya kusaidia wasiojiweza. Pia tutafanya vipimo vya VVUnkwa wale ambao watakuwa na virudsi hivyo wataelimishwa jinsi ya kufika kwa madaktari, kupata dawa na kwa wale ambao hawatakuwa na virusi vya ukimwi wataelimishwa jinsi ya kuendelea kujikinga na VVU ili wazuie kupata ukimwi na kusambazia wengine ukimwi.” Jane ana ujumbe kwa vijana ambao ndio kundi kubwa la waathirika wa VVU“Vijana tunawasihi mje msitari wa mbele , nyinyini viongozi wa leo na kesho na hapa Kenya mko wengi sana kuliko sisi. Mje mjifunze jinsi mtakavyojikinga na ukimwi, Homa ya ini aina B na magonjwa ya zinaa, na kuelimisha arafiki zenu ili wajikinge na haya magonjwa, muwe na afya bora ili muongize watu wote katika hii nchi yetu.”Nchi za Afrika zinazoongoza kwa VVU kwamujibu wa UNAUDS ni Eswatini inayoshika namba moja ikifuatiwa na Lesotho, Botswana na Zimbabwe. Tanzania inashika namba 11, Kenya 12 na Uganda ya 13.
12/1/20233 minutes, 17 seconds
Episode Artwork

Mafuriko makubwa yaathiri wenyeji Somalia baada ya ukame wa miaka minne mfululizo

Mkutano wa COP28 ukiendelea Dubai, Falme za kiarabu kusaka suluhu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi, huko Somalia mafurikio makubwa yameendelea kusababisha zahma kwa wananchi ambapo Umoja wa Mataifa kupitia ofisi yake ya uratibu wa misaada ya dharura, OCHA umezungumzia hali halisi na nini kinafanyika. Kwenye mkutano na waandishi wa habari uliofanyika kwa njia ya mtandao  kutokea Mogadishu,Somalia, OCHA imebainisha kuwa  Somalia inakabiliana na mafuriko yaliyoyaathiri maeneo mengi. Tangu mvua za msimu kuanza mwezi wa Oktoba,zaidi ya watu milioni 2 wameathirika.Milioni wameachwa bila makazi na wengine 100 wameuawa hasa katika maeneo ya Kusini Magharibi, Galmudug, Puntland, Hirshabelle, Banadir na Jubaland. Kwenye mkutano huo, Naibu mwakilishi maalum wa Katibu Mmkuu wa Umoja wa Mataifa,na mratibu wa misaada ya dharura, George Conway, alielezea kuwa ametiwa moyo na  mashirika ya kibinadamu yanayoshirikiana na uongozi pamoja na jamii kuokoa maisha katika mazingira magumu.  Mvua zinazoendelea na mafuriko yamesababisha mawasiliano kukatika, vijiji kuporomoka na barabara kuharibika. Kwa upande wake,Mkurugenzi wa muungano wa mashirika yasiyo ya kiserikali ya Somalia, Nimo Hassan, amebainisha kuwa uharibifu mkubwa umetokea na ipo haja ya kuwekeza katika suluhu za kudumu za kupambana na mafuriko kadhalika kutoa tahadhari ya mapema ili kuokoa maisha ya Wasomali. Takwimu rasmi zinaashiria kuwa wahudumu wa dharura wamewafikia kiasi ya watu laki Nane na Elfu Ishirini (820,000) na kuwapa usaidizi wa kuokoa maisha ila mahitaji bado yanaongezeka kwasababu ya mafuriko. Kamishna wa mamlaka ya udhibiti wa hali ya dharura nchini Somalia Mahamud Moalim anasema hatua ya muhimu kwa sasa ni kuwaokoa walionasa kwenye mafuriko na kuwapa msaada wa haraka wa kibinadamu. Duru zinaeleza kuwa zahma hiyo inatokea wakati ambapo mamilioni ya raia wa Somalia wanakabiliana na njaa na utapiamlo huku watoto kiasi ya milioni 1.5 walio na umri wa chini ya miaka 5 huenda wakatatizwa na utapiamlo sugu katika kipindi cha agosti 2023 na Julai 2024. Mpango wa usaidizi wa dharura kwa Somalia kwa mwaka huu wa 2023 unahitaji dola bilioni 2.6 kukimu mahitaji ya watu milioni 7.6. 
12/1/20230
Episode Artwork

Mafuriko makubwa yaathiri wenyeji Somalia baada ya ukame wa miaka minne mfululizo

Mkutano wa COP28 ukiendelea Dubai, Falme za kiarabu kusaka suluhu dhidi ya madhara ya mabadiliko ya tabianchi, huko Somalia mafurikio makubwa yameendelea kusababisha zahma kwa wananchi ambapo Umoja wa Mataifa kupitia ofisi yake ya uratibu wa misaada ya dharura, OCHA umezungumzia hali halisi na nini kinafanyika. Kwenye mkutano na waandishi wa habari uliofanyika kwa njia ya mtandao  kutokea Mogadishu,Somalia, OCHA imebainisha kuwa  Somalia inakabiliana na mafuriko yaliyoyaathiri maeneo mengi. Tangu mvua za msimu kuanza mwezi wa Oktoba,zaidi ya watu milioni 2 wameathirika.Milioni wameachwa bila makazi na wengine 100 wameuawa hasa katika maeneo ya Kusini Magharibi, Galmudug, Puntland, Hirshabelle, Banadir na Jubaland. Kwenye mkutano huo, Naibu mwakilishi maalum wa Katibu Mmkuu wa Umoja wa Mataifa,na mratibu wa misaada ya dharura, George Conway, alielezea kuwa ametiwa moyo na  mashirika ya kibinadamu yanayoshirikiana na uongozi pamoja na jamii kuokoa maisha katika mazingira magumu.  Mvua zinazoendelea na mafuriko yamesababisha mawasiliano kukatika, vijiji kuporomoka na barabara kuharibika. Kwa upande wake,Mkurugenzi wa muungano wa mashirika yasiyo ya kiserikali ya Somalia, Nimo Hassan, amebainisha kuwa uharibifu mkubwa umetokea na ipo haja ya kuwekeza katika suluhu za kudumu za kupambana na mafuriko kadhalika kutoa tahadhari ya mapema ili kuokoa maisha ya Wasomali. Takwimu rasmi zinaashiria kuwa wahudumu wa dharura wamewafikia kiasi ya watu laki Nane na Elfu Ishirini (820,000) na kuwapa usaidizi wa kuokoa maisha ila mahitaji bado yanaongezeka kwasababu ya mafuriko. Kamishna wa mamlaka ya udhibiti wa hali ya dharura nchini Somalia Mahamud Moalim anasema hatua ya muhimu kwa sasa ni kuwaokoa walionasa kwenye mafuriko na kuwapa msaada wa haraka wa kibinadamu. Duru zinaeleza kuwa zahma hiyo inatokea wakati ambapo mamilioni ya raia wa Somalia wanakabiliana na njaa na utapiamlo huku watoto kiasi ya milioni 1.5 walio na umri wa chini ya miaka 5 huenda wakatatizwa na utapiamlo sugu katika kipindi cha agosti 2023 na Julai 2024. Mpango wa usaidizi wa dharura kwa Somalia kwa mwaka huu wa 2023 unahitaji dola bilioni 2.6 kukimu mahitaji ya watu milioni 7.6. 
12/1/20232 minutes, 3 seconds
Episode Artwork

Methali: "Mwenye kelele hana maneno"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MWENYE KELELE HANA MANENO. 
11/30/20230
Episode Artwork

Methali: "Mwenye kelele hana maneno"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MWENYE KELELE HANA MANENO. 
11/30/20230
Episode Artwork

30 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 ukiwa umefunguliwa rasmi hii leo huko Dubai, utasikia ujumbe wa Ashraf Nyorano Mugenyi mwenye umri wa miaka 80 mkazi wa Hoima nchini Uganda. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwema za ukanda wa Gaza, mabadiliko ya tabianchi na Malaria, na tunakuletea uchambuzi wa methali MWENYE KELELE HANA MANENO.  Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 umefungua pazia rasmi mjini Dubai katika Falme za nchi za Kiarabu kwa kuwaleta Pamoja wajumbe zaidi ya 60,000 kuangalia jinsi ya kuongeza hatua, fursa ya nyenzo za kujenga mnepo ikiwemo makubaliano ya kuanzishwa mfuko wa hasara na uharibifu ambayo yamepitishwa kwenye mkutano huo na pia kutumia ubunifu kudhibiti janga hilo. Tukisalia ma mabadiliko ya tabianchi ripoti mpya iliyotolewa leo kuhusu hali ya hewa duniani na shirika la utabiri wa hali ya hewa duniani WMO imethibitisha kwamba mwaka 2023 utavinja rekosi ya kuwa mwaka wenye joto Zaidi katika historia huku shirikika hilo likionya kuhusu mwenendo unaoashiria kutokea kwa mafuriko zaidi, moto wa nyika, kuyeyuka kwa barafuna joto la kupindukia katika siku zijazo.Na Shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO limesema katikia ripoti yake mpya iliyotolewa leo kwamba licha ya hatua kubwa zilizopigwa katika kupanua wigo wa kupata vyandarua vya mbu vyenye dawa pamoja dawa za kusaidia kuzuia malaria kwa watoto na kina mama wajawazito, watu wengi wamekuwa wakiugua malaria. Kwa mujibu wa shirika hilo mwaka 2022 kulikuwa na wagonjwa wa malaria milioni 249 duniani kote ikiwa ni wagonja milioni 16 zaidi ya ilivyokuwa kabla ya janga la COVID-19.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MWENYE KELELE HANA MANENO. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/30/20230
Episode Artwork

30 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 ukiwa umefunguliwa rasmi hii leo huko Dubai, utasikia ujumbe wa Ashraf Nyorano Mugenyi mwenye umri wa miaka 80 mkazi wa Hoima nchini Uganda. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwema za ukanda wa Gaza, mabadiliko ya tabianchi na Malaria, na tunakuletea uchambuzi wa methali MWENYE KELELE HANA MANENO.  Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa mabadiliko ya tabianchi COP28 umefungua pazia rasmi mjini Dubai katika Falme za nchi za Kiarabu kwa kuwaleta Pamoja wajumbe zaidi ya 60,000 kuangalia jinsi ya kuongeza hatua, fursa ya nyenzo za kujenga mnepo ikiwemo makubaliano ya kuanzishwa mfuko wa hasara na uharibifu ambayo yamepitishwa kwenye mkutano huo na pia kutumia ubunifu kudhibiti janga hilo. Tukisalia ma mabadiliko ya tabianchi ripoti mpya iliyotolewa leo kuhusu hali ya hewa duniani na shirika la utabiri wa hali ya hewa duniani WMO imethibitisha kwamba mwaka 2023 utavinja rekosi ya kuwa mwaka wenye joto Zaidi katika historia huku shirikika hilo likionya kuhusu mwenendo unaoashiria kutokea kwa mafuriko zaidi, moto wa nyika, kuyeyuka kwa barafuna joto la kupindukia katika siku zijazo.Na Shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO limesema katikia ripoti yake mpya iliyotolewa leo kwamba licha ya hatua kubwa zilizopigwa katika kupanua wigo wa kupata vyandarua vya mbu vyenye dawa pamoja dawa za kusaidia kuzuia malaria kwa watoto na kina mama wajawazito, watu wengi wamekuwa wakiugua malaria. Kwa mujibu wa shirika hilo mwaka 2022 kulikuwa na wagonjwa wa malaria milioni 249 duniani kote ikiwa ni wagonja milioni 16 zaidi ya ilivyokuwa kabla ya janga la COVID-19.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MWENYE KELELE HANA MANENO. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/30/202312 minutes, 20 seconds
Episode Artwork

Simulizi: Jina langu ni Selemani lakini nilikuwa naitwa Selina

Wakati kila kona ya dunia kwa sasa ikiadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, harakati hizo miaka ya 1987 hazikuwa rahisi kueleweka ndani ya baadhi ya jamii kwani mila na destuli ambazo nyingine zilijikita katika mfumo dume ndizo zilizokuwa zimetamalaki. Lakini wanaharakati walitumia mbinu mbalimbali hata kubadili majina ili waweze kufanya kazi ya kubadilisha mitazamo ndani ya jamii. Mwandishi wa habari nguli Selemani Mkufya kutoka nchini Tanzania anatusimulia alivyofanya kazi na chama cha waandishi wa habari wanawake -TAMWA ambapo huko alikuwa akiitwa Selina badala ya Selemani.  
11/29/20230
Episode Artwork

Simulizi: Jina langu ni Selemani lakini nilikuwa naitwa Selina

Wakati kila kona ya dunia kwa sasa ikiadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia, harakati hizo miaka ya 1987 hazikuwa rahisi kueleweka ndani ya baadhi ya jamii kwani mila na destuli ambazo nyingine zilijikita katika mfumo dume ndizo zilizokuwa zimetamalaki. Lakini wanaharakati walitumia mbinu mbalimbali hata kubadili majina ili waweze kufanya kazi ya kubadilisha mitazamo ndani ya jamii. Mwandishi wa habari nguli Selemani Mkufya kutoka nchini Tanzania anatusimulia alivyofanya kazi na chama cha waandishi wa habari wanawake -TAMWA ambapo huko alikuwa akiitwa Selina badala ya Selemani.  
11/29/20233 minutes, 18 seconds
Episode Artwork

Tunaadhimisha siku hii nyakati za kiza kwa watu wa Palestina - Guterres

Umoja wa Mataifa leo umeadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, katika nyakati ambazo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameziita mojawapo ya nyakati za kiza katika historia ya watu wa Palestina na hivyo akasisitiza mshikamano zaidi na kutafuta suluhu ya kudumu. Bwana Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii ya kimataifa ya mshikamano na watu wa Palestina, kwa njia ya maandishi amesema zaidi ya yote yanayoendelea, hii ni siku ya kuthibitisha mshikamano wa kimataifa na watu wa Palestina na haki yao ya kuishi kwa amani na utu. Guterres ameendelea kusisitiza suluhisho la Serikali mbili, kwa msingi wa maazimio ya Umoja wa Mataifa na sheria za kimataifa, ili Israeli na Palestina ziishi kwa pamoja kwa amani na usalama na mji wa Jerusalem uwe mji mkuu wa Mataifa yote mawili. “Umoja wa Mataifa hautayumba katika kujitolea kwake kwa watu wa Palestina,” anahitimisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa akihimiza kuwa leo na kila siku, ulimwengu usimame katika mshikamano na matarajio ya wananchi wa Palestina kufikia haki zao zisizoweza kupokonywa na kujenga mustakbali wa amani, haki, usalama na utu kwa wote. Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA, amesema, "Mshikamano wa kimataifa tunaoueleza leo unathibitisha kwamba hitaji la haki za Wakimbizi wa Kipalestina kama ilivyoainishwa katika maazimio ya Umoja wa Mataifa, ni muhimu zaidi sasa kuliko hapo awali." Kwa hiyo anatoa wito kwa ulimwengu kushirikiana kuelekea, “haki na amani kwa Wakimbizi wa Kipalestina, ambao hawahitaji msaada tu, bali suluhisho la haki na la kudumu." Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku hii ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, kwa Umoja wa Mataifa yamefanyika katika makao makuu jijini New York, Marekani, Geneva Uswisi, Vienna Austria na Nairobi Kenya. Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina huadhimishwa na Umoja wa Mataifa kila tarehe 29 Novemba kila mwaka, kwa mujibu wa mamlaka za Baraza Kuu katika maazimio 32/40 B ya 2 Desemba 1977, na 34/65 D ya 12 Desemba 1979 na maazimio yaliyofuata yaliyopitishwa chini ya kipengele cha ajenda "Suala la Palestina." Tarehe 29 Novemba ilichaguliwa kwa sababu ya maana na umuhimu wake kwa watu wa Palestina. Siku hiyo ya 1947, Baraza Kuu lilipitisha azimio namba 181 (II), ambalo lilikuja kuitwa Azimio la Kugawanyika. Azimio hilo lilitoa fursa ya kuanzishwa huko Palestina "Nchi ya Kiyahudi" na "Nchi ya Kiarabu", na Jerusalem kama mji mkuu wa pamoja chini ya utawala maalum wa kimataifa. Kati ya Mataifa mawili yaliyopitishwa kuundwa chini ya azimio hili, ni moja tu, Israeli, ambalo limeundwa hadi sasa. 
11/29/20230
Episode Artwork

Tunaadhimisha siku hii nyakati za kiza kwa watu wa Palestina - Guterres

Umoja wa Mataifa leo umeadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, katika nyakati ambazo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameziita mojawapo ya nyakati za kiza katika historia ya watu wa Palestina na hivyo akasisitiza mshikamano zaidi na kutafuta suluhu ya kudumu. Bwana Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii ya kimataifa ya mshikamano na watu wa Palestina, kwa njia ya maandishi amesema zaidi ya yote yanayoendelea, hii ni siku ya kuthibitisha mshikamano wa kimataifa na watu wa Palestina na haki yao ya kuishi kwa amani na utu. Guterres ameendelea kusisitiza suluhisho la Serikali mbili, kwa msingi wa maazimio ya Umoja wa Mataifa na sheria za kimataifa, ili Israeli na Palestina ziishi kwa pamoja kwa amani na usalama na mji wa Jerusalem uwe mji mkuu wa Mataifa yote mawili. “Umoja wa Mataifa hautayumba katika kujitolea kwake kwa watu wa Palestina,” anahitimisha Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa akihimiza kuwa leo na kila siku, ulimwengu usimame katika mshikamano na matarajio ya wananchi wa Palestina kufikia haki zao zisizoweza kupokonywa na kujenga mustakbali wa amani, haki, usalama na utu kwa wote. Kwa upande wake Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA, amesema, "Mshikamano wa kimataifa tunaoueleza leo unathibitisha kwamba hitaji la haki za Wakimbizi wa Kipalestina kama ilivyoainishwa katika maazimio ya Umoja wa Mataifa, ni muhimu zaidi sasa kuliko hapo awali." Kwa hiyo anatoa wito kwa ulimwengu kushirikiana kuelekea, “haki na amani kwa Wakimbizi wa Kipalestina, ambao hawahitaji msaada tu, bali suluhisho la haki na la kudumu." Maadhimisho ya mwaka huu ya Siku hii ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, kwa Umoja wa Mataifa yamefanyika katika makao makuu jijini New York, Marekani, Geneva Uswisi, Vienna Austria na Nairobi Kenya. Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina huadhimishwa na Umoja wa Mataifa kila tarehe 29 Novemba kila mwaka, kwa mujibu wa mamlaka za Baraza Kuu katika maazimio 32/40 B ya 2 Desemba 1977, na 34/65 D ya 12 Desemba 1979 na maazimio yaliyofuata yaliyopitishwa chini ya kipengele cha ajenda "Suala la Palestina." Tarehe 29 Novemba ilichaguliwa kwa sababu ya maana na umuhimu wake kwa watu wa Palestina. Siku hiyo ya 1947, Baraza Kuu lilipitisha azimio namba 181 (II), ambalo lilikuja kuitwa Azimio la Kugawanyika. Azimio hilo lilitoa fursa ya kuanzishwa huko Palestina "Nchi ya Kiyahudi" na "Nchi ya Kiarabu", na Jerusalem kama mji mkuu wa pamoja chini ya utawala maalum wa kimataifa. Kati ya Mataifa mawili yaliyopitishwa kuundwa chini ya azimio hili, ni moja tu, Israeli, ambalo limeundwa hadi sasa. 
11/29/20231 minute, 47 seconds
Episode Artwork

29 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya kimataifa ya mshikamano na watu wa Palestina na siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.  Makala tunakupeleka nchini na mashinanini nchini Tanzania, kulikoni?  Umoja wa Mataifa leo umeadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, katika nyakati ambazo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameziita mojawapo ya nyakati za kiza kwa watu wa Palestina na hivyo akasisitiza mshikamano zaidi na kutafuta suluhu ya kudumu.. Wakati dunia ikiendelea na maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza November 25 na zitafikia ukingoni December 10,2023, juhudi za kukabiliana na makovu yatokanayo na vitendo vya ukatili, unyanyasaji  na ubaguzi wa kijinsia zimeanza kuzaa matunda kwa wanawake kujua na kutambua haki zao za msingi. Angela Muhindo ni mkazi wa Wilaya ya kasese nchini Uganda,ni miongoni mwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na licha ya mikikimikiki aliyokutana nayo  amefanikiwa kufungua ukurasa mpya na sasa anawatetea wanawake wengine baada ya kupata mafunzo kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya Wanawake UN Women.Katika makala harakati za kuhakikisha kuna usawa kijinsia zinahitaji mikakati mbalimbali na mmoja kati ya mikakati iliyotumiwa na Chama cha waandishi wa Habari wanawake nchini Tanzani TAMWA ilikuwa ni kufanya kazi na waandishi wanaume na wakawapa majina ya kike.Na mashinani tutaelekea nchini Tanzania kusikia ujumbe kutoka kwa kijana mwanaharakati wa mazingira na mnufaika wa mafunzo ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/29/20230
Episode Artwork

29 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya kimataifa ya mshikamano na watu wa Palestina na siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia.  Makala tunakupeleka nchini na mashinanini nchini Tanzania, kulikoni?  Umoja wa Mataifa leo umeadhimisha Siku ya Kimataifa ya Mshikamano na Watu wa Palestina, katika nyakati ambazo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ameziita mojawapo ya nyakati za kiza kwa watu wa Palestina na hivyo akasisitiza mshikamano zaidi na kutafuta suluhu ya kudumu.. Wakati dunia ikiendelea na maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza November 25 na zitafikia ukingoni December 10,2023, juhudi za kukabiliana na makovu yatokanayo na vitendo vya ukatili, unyanyasaji  na ubaguzi wa kijinsia zimeanza kuzaa matunda kwa wanawake kujua na kutambua haki zao za msingi. Angela Muhindo ni mkazi wa Wilaya ya kasese nchini Uganda,ni miongoni mwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na licha ya mikikimikiki aliyokutana nayo  amefanikiwa kufungua ukurasa mpya na sasa anawatetea wanawake wengine baada ya kupata mafunzo kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya Wanawake UN Women.Katika makala harakati za kuhakikisha kuna usawa kijinsia zinahitaji mikakati mbalimbali na mmoja kati ya mikakati iliyotumiwa na Chama cha waandishi wa Habari wanawake nchini Tanzani TAMWA ilikuwa ni kufanya kazi na waandishi wanaume na wakawapa majina ya kike.Na mashinani tutaelekea nchini Tanzania kusikia ujumbe kutoka kwa kijana mwanaharakati wa mazingira na mnufaika wa mafunzo ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/29/202310 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

Simulizi ya Angela Muhindo - Nimejikomboa nataka kila anayekatiliwa kujikomboa pia

Wakati dunia ikiendelea na maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza November 25 na zitafikia ukingoni December 10,2023, juhudi za kukabiliana na makovu yatokanayo na vitendo vya ukatili, unyanyasaji  na ubaguzi wa kijinsia zimeanzakuzaa matunda kwa wanawake kujua na kutambua haki zao za msingi. Angela Muhindo ni mkazi wa Wilaya ya kasese nchini Uganda,ni miongoni mwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na licha ya mikikimikiki aliyokutana nayo  amefanikiwa kufungua ukurasa mpya na sasa anawatetea wanawake wengine baada ya kupata mafunzo kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya Wanawake  UN Women.Angela ambaye baada ya kukatiliwa sasa amekuwa mchagizaji mkubwa wa kupambana na ukatili dhidi ya wanawake, anasema, "Wanawake wana nguvu kidogo, lakini kama wewe ni mlemavu uko katika hatari zaidi ya kukatiliwa."Ulimwenguni kote wanawake na wasichana wenye ulemavu wana uwezekano zaidi ya mara mbili ya wanawake wengine kukumbwa na ukatili wa kijinsia, Angela anaeleza jinsi mambo yalivyo badilika, “Baada ya mama kufariki nilirithi ardhi yake lakini wajomba zangu walijaribu kuichukua kwa nguvu, kwani wameamini sina haki, bila ardhi, huna nyumba, chakula, na kipato huna hivyo wanaume watakutumia vibaya.”Angela anaongeza kwamba, “Nilipata mafunzo ya haki za wanawake, haki za walemavu na haki ya ardhi, nilijifunza mimi ni sawa na kila mtu, naweza kumiliki ardhi kama mtu mwingine yeyote, hivyo nilianza mchakato wa kuidai, haikuwa rahisi lakini hatimaye ikawekwa jina langu. Ninakuwa sauti kwa wasio na sauti ili kuwazuia wasipate kile ninachotaka kupitia, natumai wengine watasimamia haki zao kama nilivyofanya, nina ardhi yangu, ardhi hii ndio kila kitu nina nyumba inanipatia chakula na kipato.”Angela baada ya kujikomboa sasa amekuwa mkombozi kwa wanawake wengine. zaidi ya watu 300,000 nchini Uganda wamehudhuria programu za jumuiya kuhusu haki za wanawake tangu 2009, huku wakiungwa mkono na mpango wa uangalizi kupitia UN Women, chombo cha Umoja wa Mataifa kinachopambania usawa wa kijinsia.
11/29/20230
Episode Artwork

Simulizi ya Angela Muhindo - Nimejikomboa nataka kila anayekatiliwa kujikomboa pia

Wakati dunia ikiendelea na maadhimisho ya siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza November 25 na zitafikia ukingoni December 10,2023, juhudi za kukabiliana na makovu yatokanayo na vitendo vya ukatili, unyanyasaji  na ubaguzi wa kijinsia zimeanzakuzaa matunda kwa wanawake kujua na kutambua haki zao za msingi. Angela Muhindo ni mkazi wa Wilaya ya kasese nchini Uganda,ni miongoni mwa waathirika wa ukatili wa kijinsia na licha ya mikikimikiki aliyokutana nayo  amefanikiwa kufungua ukurasa mpya na sasa anawatetea wanawake wengine baada ya kupata mafunzo kutoka Shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya Wanawake  UN Women.Angela ambaye baada ya kukatiliwa sasa amekuwa mchagizaji mkubwa wa kupambana na ukatili dhidi ya wanawake, anasema, "Wanawake wana nguvu kidogo, lakini kama wewe ni mlemavu uko katika hatari zaidi ya kukatiliwa."Ulimwenguni kote wanawake na wasichana wenye ulemavu wana uwezekano zaidi ya mara mbili ya wanawake wengine kukumbwa na ukatili wa kijinsia, Angela anaeleza jinsi mambo yalivyo badilika, “Baada ya mama kufariki nilirithi ardhi yake lakini wajomba zangu walijaribu kuichukua kwa nguvu, kwani wameamini sina haki, bila ardhi, huna nyumba, chakula, na kipato huna hivyo wanaume watakutumia vibaya.”Angela anaongeza kwamba, “Nilipata mafunzo ya haki za wanawake, haki za walemavu na haki ya ardhi, nilijifunza mimi ni sawa na kila mtu, naweza kumiliki ardhi kama mtu mwingine yeyote, hivyo nilianza mchakato wa kuidai, haikuwa rahisi lakini hatimaye ikawekwa jina langu. Ninakuwa sauti kwa wasio na sauti ili kuwazuia wasipate kile ninachotaka kupitia, natumai wengine watasimamia haki zao kama nilivyofanya, nina ardhi yangu, ardhi hii ndio kila kitu nina nyumba inanipatia chakula na kipato.”Angela baada ya kujikomboa sasa amekuwa mkombozi kwa wanawake wengine. zaidi ya watu 300,000 nchini Uganda wamehudhuria programu za jumuiya kuhusu haki za wanawake tangu 2009, huku wakiungwa mkono na mpango wa uangalizi kupitia UN Women, chombo cha Umoja wa Mataifa kinachopambania usawa wa kijinsia.
11/29/20232 minutes, 25 seconds
Episode Artwork

28 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo hivi sasa dunia inaadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza tarehe 25 Novemba na zinaendelea mpaka tarehe 10 Desemba ikienda sambamba na Kampeni ya UNGANISHA au UNITE iliyoanzishwa mwaka 2008. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani. Mkimbizi wa zamani  na mwandishi wa habari Abdullahi Mire kutangazwa mshindi wa kimataifa wa tuzo ya Nansen ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kuwa kinara wa haki ya elimu kwa wote. Kupitia mradi wake ulioko kambi ya wakimbizi ya Dadaab kaskazini-mashariki mwa Kenya, Mire amefanikiwa kuzindua maktaba iliyo na vitabu laki moja vinavyosomwa na watoto walio ukimbizini. Kwingineko huko Ukanda wa Gaza, ikiwa ni siku ya tano ya sitisho la mapigano msemaij wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF James Elder ambaye ametembelea eneo hilo amesema ameshuhudia hofu waliyo nayo madaktari ya milipuko ya magonjwa kama vile kipindupindu na magonjwa ya njia ya hewa. Taka hazijakusanywa muda mrefu kwenye makazi ya wakimbizi na wagonjwa hawana uwezo wa kufikia huduma.Na kuelekea siku ya Ukimwi duniani tarehe Mosi mwezi ujao wa Desemba, shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili Ukimwi, UNAIDS limetoa ripoti yake leo inayoainisha nafasi muhimu ya jamii mashinani katika kutokomeza Ukimwi ifikapo mwaka 2030. Kwa mantiki hiyo imezitaka serikali kutumia nguvu ya jamii kwenye vita dhidi ya Ukimwi.Na mashinani tutaelekea jijini Geneva, nchini Uswsi, kusikia ujumbe kutoka kwa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa, la Uhamiaji, IOM kuhusu mapambano dhidi ya ukatili sagini kijinsia. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/28/20230
Episode Artwork

28 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo hivi sasa dunia inaadhimisha siku 16 za kupinga ukatili wa kijinsia zilizoanza tarehe 25 Novemba na zinaendelea mpaka tarehe 10 Desemba ikienda sambamba na Kampeni ya UNGANISHA au UNITE iliyoanzishwa mwaka 2008. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani. Mkimbizi wa zamani  na mwandishi wa habari Abdullahi Mire kutangazwa mshindi wa kimataifa wa tuzo ya Nansen ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR kwa kuwa kinara wa haki ya elimu kwa wote. Kupitia mradi wake ulioko kambi ya wakimbizi ya Dadaab kaskazini-mashariki mwa Kenya, Mire amefanikiwa kuzindua maktaba iliyo na vitabu laki moja vinavyosomwa na watoto walio ukimbizini. Kwingineko huko Ukanda wa Gaza, ikiwa ni siku ya tano ya sitisho la mapigano msemaij wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF James Elder ambaye ametembelea eneo hilo amesema ameshuhudia hofu waliyo nayo madaktari ya milipuko ya magonjwa kama vile kipindupindu na magonjwa ya njia ya hewa. Taka hazijakusanywa muda mrefu kwenye makazi ya wakimbizi na wagonjwa hawana uwezo wa kufikia huduma.Na kuelekea siku ya Ukimwi duniani tarehe Mosi mwezi ujao wa Desemba, shirika la Umoja wa Mataifa la kukabili Ukimwi, UNAIDS limetoa ripoti yake leo inayoainisha nafasi muhimu ya jamii mashinani katika kutokomeza Ukimwi ifikapo mwaka 2030. Kwa mantiki hiyo imezitaka serikali kutumia nguvu ya jamii kwenye vita dhidi ya Ukimwi.Na mashinani tutaelekea jijini Geneva, nchini Uswsi, kusikia ujumbe kutoka kwa mkurugenzi mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa, la Uhamiaji, IOM kuhusu mapambano dhidi ya ukatili sagini kijinsia. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/28/202314 minutes, 25 seconds
Episode Artwork

Misaada tunapata lakini tunachohitaji zaidi ni amani- Mkimbizi wa ndani DRC

Hivi karibuni tulinukuu mashirika ya Umoja wa Mataifa, lile la kuhudumia wakimbizi UNHCR na lile la kuhudumia watoto UNICEF yakielezea wasiwasi wao mkubwa juu ya kushamiri hivi karibuni kwa mzozo wa kibinadamu mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC. Mapigano makali kati ya jeshi la serikali na vikundi vilivyojihami katika muda wa wiki sita tu yamesababisha watu 450,000 kukimbia makwao kutoka maeneo ya Rutshuru na Masisi katika jimbo la Kivu Kaskazini. Evarist Mapesa wa Idhaa hii ameamua kufuatilia hao waliong’olewa kwenye makazi yao kusikia kile walichopitia na madhila gani yanawakumba. Ukisikia mhusika wakisema mumwezi anamaanisha mwezi, mnane ni nane na saa kenda ni saa tisa. Kwako Evarist.
11/27/20230
Episode Artwork

Misaada tunapata lakini tunachohitaji zaidi ni amani- Mkimbizi wa ndani DRC

Hivi karibuni tulinukuu mashirika ya Umoja wa Mataifa, lile la kuhudumia wakimbizi UNHCR na lile la kuhudumia watoto UNICEF yakielezea wasiwasi wao mkubwa juu ya kushamiri hivi karibuni kwa mzozo wa kibinadamu mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo DRC. Mapigano makali kati ya jeshi la serikali na vikundi vilivyojihami katika muda wa wiki sita tu yamesababisha watu 450,000 kukimbia makwao kutoka maeneo ya Rutshuru na Masisi katika jimbo la Kivu Kaskazini. Evarist Mapesa wa Idhaa hii ameamua kufuatilia hao waliong’olewa kwenye makazi yao kusikia kile walichopitia na madhila gani yanawakumba. Ukisikia mhusika wakisema mumwezi anamaanisha mwezi, mnane ni nane na saa kenda ni saa tisa. Kwako Evarist.
11/27/20233 minutes, 19 seconds
Episode Artwork

COP28 ihakikishe inamulika jinsi ya kupunguza vifo vitokanavyo na janga la tabianchi- WHO

Kuelekea mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai, Falme za kiarabu tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO, limesema washiriki wanapaswa waelewe kuwa suala la afya ndilo linapaswa kuchochea majadiliano wakati huu ambapo janga la tabianchi linazidi kushamiri duniani kote. Dkt, María Neira ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Afya ya Umma na Mazingira, WHO ameiambia Idhaa ya Umoja wa Mataifa jijini Geneva, Uswisi ya kwamba. “wajumbe wanapaswa kuelewa kuwa hawajadili tu punguzo la kiwango cha utoaji wa hewa chafuzi kila mwaka, bali wanajadili pia idadi ya wagonjwa wa pumu, idadi ya wagonjwa wa njia ya hewa, idadi ya wagonjwa wa saratani ya mapafu, idadi ya wagonjwa wa magonjwa yanayohusiana na kukabiliana na hewa chafu au madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Wanahitaji kuelewa wanajadili afya yetu vile vile.” Dkt. Neira amesema pamoja na hilo, wanataka washiriki pia waelewe kuwa iwapo watachukua hatua sahihi, mathalani kushughulikia visababishi vya mabadiliko ya tabianchi kwa kuwa na miji isiyo na uchafuzi, nishati safi na endelevu, hatua hizo zitakuwa na manufaa kwa afya ya kila mtu. Ndipo akatolea mfano iwapo hatua sahihi za kukabili tabianchi zikichukuliwa na matunda yatakayopatikana ifikapo mwaka 2030,  “iwapo tunaangalia afya ya umma, ningependa kupunguza kabisa vifo vya watoto wachanga vinavyosababishwa na uchafuzi wa hewa, ambavyo ni watoto milioni 7 hufia tumboni mwa mama zao. Kwa hiyo tukiongeza upatikanaji wa nishati safi, yaani kwa kuwa tu na hewa safi, tunaweza kupunguza vifo milioni 5 kila mwaka.”  Kwa mujibu wa WHO madhara ya mabadiliko ya tabianchi yamekuwa makubwa zaidi kwa nchi za Afrika zilizo kusini mwa jangwa la Sahara, halikadhalika nchi za Kusini-Mashariki mwa Asia na pia nchi za visiwa vidogo. Katika mkutano huo wa COP28 kwa mara ya kwanza kutakuwa na Siku ya Afya ambapo washiriki watajikita zaidi kujadili jinsi tabianchi inarudisha nyuma mafanikio yaliyopatikana kwenye sekta ya afya. 
11/27/20230
Episode Artwork

COP28 ihakikishe inamulika jinsi ya kupunguza vifo vitokanavyo na janga la tabianchi- WHO

Kuelekea mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai, Falme za kiarabu tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO, limesema washiriki wanapaswa waelewe kuwa suala la afya ndilo linapaswa kuchochea majadiliano wakati huu ambapo janga la tabianchi linazidi kushamiri duniani kote. Dkt, María Neira ambaye ni Mkurugenzi wa Idara ya Afya ya Umma na Mazingira, WHO ameiambia Idhaa ya Umoja wa Mataifa jijini Geneva, Uswisi ya kwamba. “wajumbe wanapaswa kuelewa kuwa hawajadili tu punguzo la kiwango cha utoaji wa hewa chafuzi kila mwaka, bali wanajadili pia idadi ya wagonjwa wa pumu, idadi ya wagonjwa wa njia ya hewa, idadi ya wagonjwa wa saratani ya mapafu, idadi ya wagonjwa wa magonjwa yanayohusiana na kukabiliana na hewa chafu au madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Wanahitaji kuelewa wanajadili afya yetu vile vile.” Dkt. Neira amesema pamoja na hilo, wanataka washiriki pia waelewe kuwa iwapo watachukua hatua sahihi, mathalani kushughulikia visababishi vya mabadiliko ya tabianchi kwa kuwa na miji isiyo na uchafuzi, nishati safi na endelevu, hatua hizo zitakuwa na manufaa kwa afya ya kila mtu. Ndipo akatolea mfano iwapo hatua sahihi za kukabili tabianchi zikichukuliwa na matunda yatakayopatikana ifikapo mwaka 2030,  “iwapo tunaangalia afya ya umma, ningependa kupunguza kabisa vifo vya watoto wachanga vinavyosababishwa na uchafuzi wa hewa, ambavyo ni watoto milioni 7 hufia tumboni mwa mama zao. Kwa hiyo tukiongeza upatikanaji wa nishati safi, yaani kwa kuwa tu na hewa safi, tunaweza kupunguza vifo milioni 5 kila mwaka.”  Kwa mujibu wa WHO madhara ya mabadiliko ya tabianchi yamekuwa makubwa zaidi kwa nchi za Afrika zilizo kusini mwa jangwa la Sahara, halikadhalika nchi za Kusini-Mashariki mwa Asia na pia nchi za visiwa vidogo. Katika mkutano huo wa COP28 kwa mara ya kwanza kutakuwa na Siku ya Afya ambapo washiriki watajikita zaidi kujadili jinsi tabianchi inarudisha nyuma mafanikio yaliyopatikana kwenye sekta ya afya. 
11/27/20232 minutes, 23 seconds
Episode Artwork

Heko waliofanikisha sitisho la mapigano Gaza - Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amezipongeza serikali za Qatar, Misri na Marekani pamoja na kutambua jukumu muhimu la kamati ya Kimataifa ya chama cha msalaba mwekudu kwa juhudi zao za kuhakikisha mapigano yanasitishwa kwa muda, mateka na wafungwa wanaachiwa pamoja na kuingiza misaada huko Ukanda wa Gaza. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Flora NduchaMapigano ya wiki saba huko Gaza na Israel yameleta hali mbaya sana ambayo imeshangaza ulimwengu. Lakini kwa muda wa siku nne sasa, Mapigano hayo yamesitishwa, Mateka wa Israel na mataifa mengine ya kigeni wanaoshikiliwa na Hamas tangu tarehe 7 Oktoba wameanza kuachiliwa na wafungwa wa Kipalestina wanafunguliwa kutoka jela za Israel.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kupitia Msemaji wake Stéphane Dujarric hii leo hapa jijini New York Marekani amewapongeza wahusika wote walioshiriki kufanikisha hayo yanayoendelea kutokea.  Umoja wa Mataifa pia umeongeza uingizaji misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza na misaada mingine imetumwa eneo la kaskazini mwa Gaza ambalo kwa wiki kadhaa wananchi waliokosa misaada kutokana na mapigano makali yaliyoendelea katika eneo hilo.Hata hivyo Katibu Mkuu Guterres amesema misaada hiyo haitoshi kukidhi mahitaji ya wananchi milioni 1.7 wenye uhitaji na kusema mahitaji ya kibinadamu kila uchao yanazidi kuongezeka.Ametaka mazungumzo yaliyokuwa chachu ya makubaliano hayo lazima yaendelee, na kufikia usitishaji kamili wa mapigano kwa sababu za kibinadamu, kwa manufaa ya watu wa Gaza, Israel na eneo zima.Katibu Mkuu kwa mara nyingine ametoa wito kwa mateka waliosalia kuachiwa mara moja bila masharti yoyote.Amehitimisha taarifa yake kwa kuyahimiza Mataifa yote kutumia ushawishi wao kumaliza mzozo huu mbaya na kuunga mkono hatua zisizoweza kutenguliwa kuelekea mustakabali pekee endelevu wa eneo hilo ambao ni suluhisho la kuwa na serikali mbili, na Israeli na Palestina kuishi bega kwa bega, kwa amani na usalama.Wakati huo huo wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa hii leo wametoa wito wa kufanyika uchunguzi wa haraka, wa uwazi na huru kuhusu tuhuma za uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu, unaotekelezwa nchini Israel na katika eneo linalokaliwa la Palestina kuanzia tarehe 7 Oktoba mwaka huu wa 2023 na baada ya hapo.Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa huko Geneva Uswisi imesema wataalamu hao wamezitaka pande zote katika mzozo unaoendelea huko Mashariki ya Kati kuwalinda raia na kuzingatia wajibu wao chini ya sheria za kimataifa.
11/27/20230
Episode Artwork

Heko waliofanikisha sitisho la mapigano Gaza - Guterres

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amezipongeza serikali za Qatar, Misri na Marekani pamoja na kutambua jukumu muhimu la kamati ya Kimataifa ya chama cha msalaba mwekudu kwa juhudi zao za kuhakikisha mapigano yanasitishwa kwa muda, mateka na wafungwa wanaachiwa pamoja na kuingiza misaada huko Ukanda wa Gaza. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Flora NduchaMapigano ya wiki saba huko Gaza na Israel yameleta hali mbaya sana ambayo imeshangaza ulimwengu. Lakini kwa muda wa siku nne sasa, Mapigano hayo yamesitishwa, Mateka wa Israel na mataifa mengine ya kigeni wanaoshikiliwa na Hamas tangu tarehe 7 Oktoba wameanza kuachiliwa na wafungwa wa Kipalestina wanafunguliwa kutoka jela za Israel.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kupitia Msemaji wake Stéphane Dujarric hii leo hapa jijini New York Marekani amewapongeza wahusika wote walioshiriki kufanikisha hayo yanayoendelea kutokea.  Umoja wa Mataifa pia umeongeza uingizaji misaada ya kibinadamu katika Ukanda wa Gaza na misaada mingine imetumwa eneo la kaskazini mwa Gaza ambalo kwa wiki kadhaa wananchi waliokosa misaada kutokana na mapigano makali yaliyoendelea katika eneo hilo.Hata hivyo Katibu Mkuu Guterres amesema misaada hiyo haitoshi kukidhi mahitaji ya wananchi milioni 1.7 wenye uhitaji na kusema mahitaji ya kibinadamu kila uchao yanazidi kuongezeka.Ametaka mazungumzo yaliyokuwa chachu ya makubaliano hayo lazima yaendelee, na kufikia usitishaji kamili wa mapigano kwa sababu za kibinadamu, kwa manufaa ya watu wa Gaza, Israel na eneo zima.Katibu Mkuu kwa mara nyingine ametoa wito kwa mateka waliosalia kuachiwa mara moja bila masharti yoyote.Amehitimisha taarifa yake kwa kuyahimiza Mataifa yote kutumia ushawishi wao kumaliza mzozo huu mbaya na kuunga mkono hatua zisizoweza kutenguliwa kuelekea mustakabali pekee endelevu wa eneo hilo ambao ni suluhisho la kuwa na serikali mbili, na Israeli na Palestina kuishi bega kwa bega, kwa amani na usalama.Wakati huo huo wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa hii leo wametoa wito wa kufanyika uchunguzi wa haraka, wa uwazi na huru kuhusu tuhuma za uhalifu wa kivita na uhalifu dhidi ya binadamu, unaotekelezwa nchini Israel na katika eneo linalokaliwa la Palestina kuanzia tarehe 7 Oktoba mwaka huu wa 2023 na baada ya hapo.Taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa huko Geneva Uswisi imesema wataalamu hao wamezitaka pande zote katika mzozo unaoendelea huko Mashariki ya Kati kuwalinda raia na kuzingatia wajibu wao chini ya sheria za kimataifa.
11/27/20232 minutes, 40 seconds
Episode Artwork

27 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Leah Mushi anamulika Gaza, siku ya nne ya sitisho la mapigano; kisha kauli ya shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO kulekea COP28. Makala ni kauli ya muathirika wa mapigano huko Mashariki mwa DRC na mashinani mnufaika wa kilimo endelevu kutoka Kenya.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amezipongeza serikali za Qatar, Misri na Marekani pamoja na kutambua jukumu muhimu la kamati ya Kimataifa ya chama cha msalaba mwekudu kwa juhudi zao za kuhakikisha mapigano yanasitishwa kwa muda, mateka na wafungwa wanaachiwa pamoja na kuingiza misaada huko Ukanda wa Gaza.Kuelekea mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai, Falme za kiarabu tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO, limesema washiriki wanapaswa waelewe kuwa suala la afya ndilo linapaswa kuchochea majadiliano wakati huu ambapo janga la tabianchi linazidi kushamiri duniani kote.Makala: Evarist Mapesa wa Idhaa hii anafuatilia madhila wanayopitia watu 450,000 waliofurushwa makwao katika kipindi cha wiki sita zilizopita huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kutokana na mapigano kati ya jeshi la serikali na vikundi vilivyojiham.Mashinani:Leo nampa fursa Hannah Karanja, mkulima mnufaika wa mpango wa kilimo endelevu kinachohusisha utandazaji wa majani makavu kama njia ya kuepusha matumizi ya mbolea zenye kemikali, mradi unaofanikishwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP.
11/27/20230
Episode Artwork

27 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Leah Mushi anamulika Gaza, siku ya nne ya sitisho la mapigano; kisha kauli ya shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO kulekea COP28. Makala ni kauli ya muathirika wa mapigano huko Mashariki mwa DRC na mashinani mnufaika wa kilimo endelevu kutoka Kenya.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amezipongeza serikali za Qatar, Misri na Marekani pamoja na kutambua jukumu muhimu la kamati ya Kimataifa ya chama cha msalaba mwekudu kwa juhudi zao za kuhakikisha mapigano yanasitishwa kwa muda, mateka na wafungwa wanaachiwa pamoja na kuingiza misaada huko Ukanda wa Gaza.Kuelekea mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai, Falme za kiarabu tarehe 30 mwezi huu wa Novemba, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO, limesema washiriki wanapaswa waelewe kuwa suala la afya ndilo linapaswa kuchochea majadiliano wakati huu ambapo janga la tabianchi linazidi kushamiri duniani kote.Makala: Evarist Mapesa wa Idhaa hii anafuatilia madhila wanayopitia watu 450,000 waliofurushwa makwao katika kipindi cha wiki sita zilizopita huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kutokana na mapigano kati ya jeshi la serikali na vikundi vilivyojiham.Mashinani:Leo nampa fursa Hannah Karanja, mkulima mnufaika wa mpango wa kilimo endelevu kinachohusisha utandazaji wa majani makavu kama njia ya kuepusha matumizi ya mbolea zenye kemikali, mradi unaofanikishwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP.
11/27/202311 minutes, 57 seconds
Episode Artwork

Mradi wa kupunguza matumizi ya dawa katika ufugaji kuku wa nyama kuanza mwakani – FAO Tanzania

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) nchini Tanzania linakusudia kutekeleza mradi wa kuhamasisha wafugaji kupunguza matumizi ya dawa, mathalani za viuavijiumbemaradhi katika ufugaji wa kuku wa nyama nchini humo. John Kabambala wa redio washirika wetu KidsTime FM anatujuza zaidi kupitia makala hii.
11/24/20230
Episode Artwork

Mradi wa kupunguza matumizi ya dawa katika ufugaji kuku wa nyama kuanza mwakani – FAO Tanzania

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) nchini Tanzania linakusudia kutekeleza mradi wa kuhamasisha wafugaji kupunguza matumizi ya dawa, mathalani za viuavijiumbemaradhi katika ufugaji wa kuku wa nyama nchini humo. John Kabambala wa redio washirika wetu KidsTime FM anatujuza zaidi kupitia makala hii.
11/24/20234 minutes, 2 seconds
Episode Artwork

Guterres aonya kwamba kifanyikacho Antarctica sasa hakisalii tena huko kinasambaa

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye yuko ziarani katika eneo la ncha ya kusini mwa dunia, Antarctica amesema eneo hilo limekuwa likijulikana kama eneo lenye manufaa makubwa lakini lililosahaulika, lakini sasa limeamshwa na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Kauli hiyo imekuwa na mashiko kwa miongo kadhaa kwa msingi kwamba eneo la ncha ya kusini mwa dunia liko mbali na wengi, lakini sasa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akiwa katika ziara ya siku tatu kwenye eneo hilo amejionea akiwa ameambatana na Rais Gabriel Boric wa Chile jinsi kile kinachofanyika maelfu ya maili kinaathiri eneo hilo, na halikadhalika kifanyikacho eneo hilo hakisalii tena eneo hilo kama ambavyo awali watu walidhania. Ametembelea kisiwa cha Kopaitic ambacho ni makazi ya ndege wa baharini aina ya Kiwi na kuona ni kwa jinsi gani mabadiliko ya tabianchi yameathiri eneo hilo. Mathalani nishati kisukuku ambayo ni mafuta yatokanayo na upasuaji na uchomaji wa miamba! Katibu Mkuu amesema uchafuzi utokanao na shughuli hiyo husababisha joto kwenye sayari ya dunia, vivyo hivyo Antarctica.  Kielelezo ni ongezeko la joto kwenye baharí kusini mwa dunia ambalo limechochea mkondo joto baharini, El Nino unaosababisha mvua, mafuriko na joto kupindukia.  Sasa kwa viongozi na washiriki wa mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai mambo matatu yazingatiwe: Mosi, wachukue hatua wahakikishe kiwango cha joto duniani hakizidi nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi; Pili, walinde binadamu dhidi ya zahma ya tabianchi na tatu waondokane na nishati kisukuku.  Guterres amesema tusiache matumaini yote ya sayari endelevu yayoyome.  Baadaye leo akiwa na Rais Boric watatembelea kituo cha Frei huko huko Antarctica na kesho Jumamosi atatembelea kituo cha wanasayansi cha Profesa Julio Escudero kupata taarifa kutoka kwa wanasayansi. Atarejea New York, Jumapili. 
11/24/20230
Episode Artwork

Guterres aonya kwamba kifanyikacho Antarctica sasa hakisalii tena huko kinasambaa

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye yuko ziarani katika eneo la ncha ya kusini mwa dunia, Antarctica amesema eneo hilo limekuwa likijulikana kama eneo lenye manufaa makubwa lakini lililosahaulika, lakini sasa limeamshwa na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Kauli hiyo imekuwa na mashiko kwa miongo kadhaa kwa msingi kwamba eneo la ncha ya kusini mwa dunia liko mbali na wengi, lakini sasa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akiwa katika ziara ya siku tatu kwenye eneo hilo amejionea akiwa ameambatana na Rais Gabriel Boric wa Chile jinsi kile kinachofanyika maelfu ya maili kinaathiri eneo hilo, na halikadhalika kifanyikacho eneo hilo hakisalii tena eneo hilo kama ambavyo awali watu walidhania. Ametembelea kisiwa cha Kopaitic ambacho ni makazi ya ndege wa baharini aina ya Kiwi na kuona ni kwa jinsi gani mabadiliko ya tabianchi yameathiri eneo hilo. Mathalani nishati kisukuku ambayo ni mafuta yatokanayo na upasuaji na uchomaji wa miamba! Katibu Mkuu amesema uchafuzi utokanao na shughuli hiyo husababisha joto kwenye sayari ya dunia, vivyo hivyo Antarctica.  Kielelezo ni ongezeko la joto kwenye baharí kusini mwa dunia ambalo limechochea mkondo joto baharini, El Nino unaosababisha mvua, mafuriko na joto kupindukia.  Sasa kwa viongozi na washiriki wa mkutano wa 28 wa nchi wanachama wa mkataba wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 huko Dubai mambo matatu yazingatiwe: Mosi, wachukue hatua wahakikishe kiwango cha joto duniani hakizidi nyuzijoto 1.5 katika kipimo cha Selsiyasi; Pili, walinde binadamu dhidi ya zahma ya tabianchi na tatu waondokane na nishati kisukuku.  Guterres amesema tusiache matumaini yote ya sayari endelevu yayoyome.  Baadaye leo akiwa na Rais Boric watatembelea kituo cha Frei huko huko Antarctica na kesho Jumamosi atatembelea kituo cha wanasayansi cha Profesa Julio Escudero kupata taarifa kutoka kwa wanasayansi. Atarejea New York, Jumapili. 
11/24/20232 minutes, 2 seconds
Episode Artwork

24 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia amani na usalama katika ukanda wa Gaza na msaada wa kibinadamu nchini Chad. Makala tunakupeleka nchini Tanzania, na mashinani tunamulika Ibara ya 13 ya Tamko la Haki za Binadamu.  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye yuko ziarani katika eneo la ncha ya kusini mwa dunia, Antarctica amesema eneo hilo limekuwa likijulikana kama eneo lenye manufaa makubwa lakini lililosahaulika, lakini sasa limeamshwa na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Chad ni mwenyeji wa wakimbizi zaidi ya milioni ambao sasa umekuwa mgogoro mkubwa zaidi wa wakimbizi na unaokuwa kwa kasi barani Afrika kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hilo linasema na vita inayoendelea katika nchi jirani ya Sudan imeongeza shinikizo la rasilimali na mahitaji ya kibinadamu kwani maelfu kwa maelfu ya watu zaidi wanavuka mpaka na kusaka usalama Chad.Katika makala John Kabambala wa redio washirika wetu KidsTime FM ya Morogogo Tanzania anatujuza kuhusu Mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) Tanzania unaokusudia kuhamasisha wafugaji wa kuku kupunguza matumizi ya dawa, mathalani za viuavijiumbemaradhi wakati wa ufugaji wa kuku wa nyama nchini humo.Na mashinani leo katika mfululizo wetu wa uchambuzi wa Ibara za Tamko la Haki za Binadamu kuelekea Siku ya Haki za Binadamu itakayoadhimishwa hapo Desemba 10 leo tunamulika Ibara ya 13. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/24/20230
Episode Artwork

24 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia amani na usalama katika ukanda wa Gaza na msaada wa kibinadamu nchini Chad. Makala tunakupeleka nchini Tanzania, na mashinani tunamulika Ibara ya 13 ya Tamko la Haki za Binadamu.  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye yuko ziarani katika eneo la ncha ya kusini mwa dunia, Antarctica amesema eneo hilo limekuwa likijulikana kama eneo lenye manufaa makubwa lakini lililosahaulika, lakini sasa limeamshwa na madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Chad ni mwenyeji wa wakimbizi zaidi ya milioni ambao sasa umekuwa mgogoro mkubwa zaidi wa wakimbizi na unaokuwa kwa kasi barani Afrika kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hilo linasema na vita inayoendelea katika nchi jirani ya Sudan imeongeza shinikizo la rasilimali na mahitaji ya kibinadamu kwani maelfu kwa maelfu ya watu zaidi wanavuka mpaka na kusaka usalama Chad.Katika makala John Kabambala wa redio washirika wetu KidsTime FM ya Morogogo Tanzania anatujuza kuhusu Mradi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) Tanzania unaokusudia kuhamasisha wafugaji wa kuku kupunguza matumizi ya dawa, mathalani za viuavijiumbemaradhi wakati wa ufugaji wa kuku wa nyama nchini humo.Na mashinani leo katika mfululizo wetu wa uchambuzi wa Ibara za Tamko la Haki za Binadamu kuelekea Siku ya Haki za Binadamu itakayoadhimishwa hapo Desemba 10 leo tunamulika Ibara ya 13. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/24/202313 minutes
Episode Artwork

WFP inasema Chad imewakirimu wakimbizi kwa kila kitu lakini sasa imeishiwa inahitaji msaada

Chad ni mwenyeji wa wakimbizi zaidi ya milioni ambao sasa umekuwa mgogoro mkubwa zaidi wa wakimbizi na unaokuwa kwa kasi barani Afrika kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hilo linasema na vita inayoendelea katika nchi jirani ya Sudan imeongeza shinikizo la rasilimali na mahitaji ya kibinadamu kwani maelfu kwa maelfu ya watu zaidi wanavuka mpaka na kusaka usalama Chad. Katika kituo cha wakimbizi  cha Adre mpakani  mwa Chad hekaheka ni nyingi kwani wakimbizi wanamiminika kwa idadi kubwa wakiwa na virago vyao wanakimbia vita inayoendelea Sudan, na miongoni mwao ni Roukaya Yacoub mama wa watoto saba aliyelazimika kukusanya kile alichoweza na wanawe na kuchanja mbuga baada ya mumewe kuawa katika shambulio lilitokea Ardamata.Sasa yuko kambini hapa lakini jinamizi la shambulio hilo linaendelea kumuandama,“Walitushambulia kwa siku tatu mfululizo, ilikuwa mbaya sana, walikwenda mlango kwa mlango wakiwakusanya wanaume wakiwatoa nje na kuwaua. Walimwita baba watoto wangu atoke nje na kisha wakampiga risasi na kumuua. Walichukua kila kitu tulichokuwa nacho na sasa nimesalia mkavu sina chochote cha kuwasaidia wanangu. Hatukuwa na chaguo linguine bali kukimbilia Chad.”Kwa mujibu wa WFP ongezeko hili la wakimbizi limezidisha shinikizo la mahitaji ya kibinadamu kama chakula inachokigawa ambacho ndio tegemeo pekee la wakimbizi hawa na sasa hakitoshelezi tena kwani idadi ya watu inaongezeka kila uchao, rasilimali zinakwisha na kuyaacha mashirika ya misaada ya kibinadamu yakihaha na kukosa la kufanya.Changamoto za wakimbizi hawa pia zinajumuisha masuala ya kiafya ikiwemo utapiamlo kwa watoto, majeruhi na magonjwa mengine ambayo baada ya vipimo wanahitaji msaada. Pierre Honnorat ni mkurugenzi wa WFP nchini Chad anasema,“Wachad wamegawana na wakimbizi kila walichokuwa nacho sasa hawana tena cha kugawana. Wao wenyewe wanahitaji msaada, hivyo tunahitaji kuwasaidia wakimbizi wote 600,000 waliokuja, wakimbizi wa Chad wanaorejea lakini pia sasa tunahitaji kuwasaidia Wachad wanaohifadhi wakimbizi ambao nao wanahaha kama walivyo waliowasili toka Sudan.”WFP inasema zaidi ya watu nusu milioni wamevuka mpaka tangu Aprili wakiwemo wakimbizi 45,000 na watu 80,000 raia wa Chad wanaorejea na idadi ya wanaoingia Chad inatarajiwa kufikia watu 600,000 ifikapo mwisho wa mwaka huu.
11/24/20230
Episode Artwork

WFP inasema Chad imewakirimu wakimbizi kwa kila kitu lakini sasa imeishiwa inahitaji msaada

Chad ni mwenyeji wa wakimbizi zaidi ya milioni ambao sasa umekuwa mgogoro mkubwa zaidi wa wakimbizi na unaokuwa kwa kasi barani Afrika kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hilo linasema na vita inayoendelea katika nchi jirani ya Sudan imeongeza shinikizo la rasilimali na mahitaji ya kibinadamu kwani maelfu kwa maelfu ya watu zaidi wanavuka mpaka na kusaka usalama Chad. Katika kituo cha wakimbizi  cha Adre mpakani  mwa Chad hekaheka ni nyingi kwani wakimbizi wanamiminika kwa idadi kubwa wakiwa na virago vyao wanakimbia vita inayoendelea Sudan, na miongoni mwao ni Roukaya Yacoub mama wa watoto saba aliyelazimika kukusanya kile alichoweza na wanawe na kuchanja mbuga baada ya mumewe kuawa katika shambulio lilitokea Ardamata.Sasa yuko kambini hapa lakini jinamizi la shambulio hilo linaendelea kumuandama,“Walitushambulia kwa siku tatu mfululizo, ilikuwa mbaya sana, walikwenda mlango kwa mlango wakiwakusanya wanaume wakiwatoa nje na kuwaua. Walimwita baba watoto wangu atoke nje na kisha wakampiga risasi na kumuua. Walichukua kila kitu tulichokuwa nacho na sasa nimesalia mkavu sina chochote cha kuwasaidia wanangu. Hatukuwa na chaguo linguine bali kukimbilia Chad.”Kwa mujibu wa WFP ongezeko hili la wakimbizi limezidisha shinikizo la mahitaji ya kibinadamu kama chakula inachokigawa ambacho ndio tegemeo pekee la wakimbizi hawa na sasa hakitoshelezi tena kwani idadi ya watu inaongezeka kila uchao, rasilimali zinakwisha na kuyaacha mashirika ya misaada ya kibinadamu yakihaha na kukosa la kufanya.Changamoto za wakimbizi hawa pia zinajumuisha masuala ya kiafya ikiwemo utapiamlo kwa watoto, majeruhi na magonjwa mengine ambayo baada ya vipimo wanahitaji msaada. Pierre Honnorat ni mkurugenzi wa WFP nchini Chad anasema,“Wachad wamegawana na wakimbizi kila walichokuwa nacho sasa hawana tena cha kugawana. Wao wenyewe wanahitaji msaada, hivyo tunahitaji kuwasaidia wakimbizi wote 600,000 waliokuja, wakimbizi wa Chad wanaorejea lakini pia sasa tunahitaji kuwasaidia Wachad wanaohifadhi wakimbizi ambao nao wanahaha kama walivyo waliowasili toka Sudan.”WFP inasema zaidi ya watu nusu milioni wamevuka mpaka tangu Aprili wakiwemo wakimbizi 45,000 na watu 80,000 raia wa Chad wanaorejea na idadi ya wanaoingia Chad inatarajiwa kufikia watu 600,000 ifikapo mwisho wa mwaka huu.
11/24/20233 minutes, 4 seconds
Episode Artwork

Waepushe watoto wachanga na bidhaa za viwandani – WHO/UNICEF

Kwa mujibu wa mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la Afya Ulimwenguni (WHO) na la Kuhudumia Watoto (UNICEF), tabia za ulishaji wa vyakula visivyo salama kiafya kwa watoto wadogo na wachanga lazima ziepukwe kwasababu zinachangia kuongezeka uzito usio salama kiafya, na vyakula hivyo vinaweza kuchukua nafasi ya vyakula vyenye virutubishi muhimu kwa watoto. Matumizi ya vyakula na vinywaji vitamu kwa watoto wachanga na watoto wadogo huongeza uwezekano wa kuharibika kwa meno na tatizo la kiribatumbo kwa watoto.  Kiujumla matumizi ya vyakula visivyo salama kiafya inamaanisha vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi na mafuta yasiyo salama kiafya. Edisoni Tumaini Anatory wa redio washirika wetu Karagwe FM ya wilayani Karagwe, mkoani Kagera Magharibi mwa Tanzania ametuandalia makala hii akiangazia mamlaka za afya kwa umma katika hiyo zinavyotoa wito kuhamasisha wananchi kuchukua hatua za kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza hususani kwa watoto wadogo.
11/22/20230
Episode Artwork

Waepushe watoto wachanga na bidhaa za viwandani – WHO/UNICEF

Kwa mujibu wa mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la Afya Ulimwenguni (WHO) na la Kuhudumia Watoto (UNICEF), tabia za ulishaji wa vyakula visivyo salama kiafya kwa watoto wadogo na wachanga lazima ziepukwe kwasababu zinachangia kuongezeka uzito usio salama kiafya, na vyakula hivyo vinaweza kuchukua nafasi ya vyakula vyenye virutubishi muhimu kwa watoto. Matumizi ya vyakula na vinywaji vitamu kwa watoto wachanga na watoto wadogo huongeza uwezekano wa kuharibika kwa meno na tatizo la kiribatumbo kwa watoto.  Kiujumla matumizi ya vyakula visivyo salama kiafya inamaanisha vyakula vyenye sukari nyingi, chumvi na mafuta yasiyo salama kiafya. Edisoni Tumaini Anatory wa redio washirika wetu Karagwe FM ya wilayani Karagwe, mkoani Kagera Magharibi mwa Tanzania ametuandalia makala hii akiangazia mamlaka za afya kwa umma katika hiyo zinavyotoa wito kuhamasisha wananchi kuchukua hatua za kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza hususani kwa watoto wadogo.
11/22/20233 minutes, 37 seconds
Episode Artwork

Ngoma za kitamaduni kuleta jamii pamoja Sudan Kusini - UNMISS

Katika kukuza utangamano ndani ya jamii yenye makabila tofauti ambayo hapo awali yalikuwa na misuguano Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwakushirikiana na wizara ya Utamaduni ya Sudan Kusini imefanya huko katika jimbo la Equatoria Magharibi. Ni sauti za ngoma, marimba, filimbi , vuvuzela na mirindimo mbalimbali ikisikika katika mji wa Yambio ulioko jimboni Equatoria Magharibi hapa Sudan Kusini, mamia ya wananchi wengine wakiwa wamevalia vibwebwe viunoni na mavazi ya asili wakicheza kwa pamoja kufurahia utajiri wao wa utafauti wa makabila. Afisa wa masuala ya kiraia wa UNMISS Emmanuel Dukundane anasema makabila tisa yamekutanishwa hapa, “Shughuli hii ni kwa ajili ya kuonesha tofauti zetu, utofauti wetu kwenye masuala ya utamaduni na lengo ni sote tuwe na furaha. Na kupitia furaha hiyo tunaweza kukuza mshikamano wa kijamii, tunaweza kufahamiana zaidi, kuthaminiana zaidi, na kusahau changamoto zetu za zamani.” Na ama hakika wananchi hapa wamefurahi na hawataki kabisa kukumbuka ya kale kwani yanaumiza kama anavyoeleza Mama Hellen Mading mkazi wa Yambio, "Wakati tunapokuwa na migogoro sisi wanawawake na watoto ndio tunateseka. kwakweli tunahitaji amani, acha tuishi kwa amani kila siku. Tunataka watoto wetu wakue katika mazingira mazuri ili wapate elimu na waje kuwa viongozi wetu wa baadae.” Tamasha hili limeandaliwa na UNMISS wakishirikiana na wizara ya utamaduni, vijana na michezo na kijana James Amabele anasema walikuwa wakisubiri tukio hili kwa hamu, “Matukio kama haya ndio yataleta amani miongoni mwa wanajamii na Sudan Kusini kwa ujumla. Hili ndilo tulikuwa tukilitamani litokee, lazima tuwe na umoja, na ikiwa kila kitu kitaenda vizuri, basi amani itatawala. Hii ndio amani yenyewe. Tulikuwa tukililia amani na hapa tupo katika umoja na amani; makabila yote yameungana.”Kwa UNMISS, hii ni hatua moja kuelekea kujenga amani ya kudumu na endelevu miongoni mwa jamii ambazo zimekumbwa na mgogoro, mmoja baada ya mwingine katika taifa lote la Sudan Kusini.
11/22/20230
Episode Artwork

Ngoma za kitamaduni kuleta jamii pamoja Sudan Kusini - UNMISS

Katika kukuza utangamano ndani ya jamii yenye makabila tofauti ambayo hapo awali yalikuwa na misuguano Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwakushirikiana na wizara ya Utamaduni ya Sudan Kusini imefanya huko katika jimbo la Equatoria Magharibi. Ni sauti za ngoma, marimba, filimbi , vuvuzela na mirindimo mbalimbali ikisikika katika mji wa Yambio ulioko jimboni Equatoria Magharibi hapa Sudan Kusini, mamia ya wananchi wengine wakiwa wamevalia vibwebwe viunoni na mavazi ya asili wakicheza kwa pamoja kufurahia utajiri wao wa utafauti wa makabila. Afisa wa masuala ya kiraia wa UNMISS Emmanuel Dukundane anasema makabila tisa yamekutanishwa hapa, “Shughuli hii ni kwa ajili ya kuonesha tofauti zetu, utofauti wetu kwenye masuala ya utamaduni na lengo ni sote tuwe na furaha. Na kupitia furaha hiyo tunaweza kukuza mshikamano wa kijamii, tunaweza kufahamiana zaidi, kuthaminiana zaidi, na kusahau changamoto zetu za zamani.” Na ama hakika wananchi hapa wamefurahi na hawataki kabisa kukumbuka ya kale kwani yanaumiza kama anavyoeleza Mama Hellen Mading mkazi wa Yambio, "Wakati tunapokuwa na migogoro sisi wanawawake na watoto ndio tunateseka. kwakweli tunahitaji amani, acha tuishi kwa amani kila siku. Tunataka watoto wetu wakue katika mazingira mazuri ili wapate elimu na waje kuwa viongozi wetu wa baadae.” Tamasha hili limeandaliwa na UNMISS wakishirikiana na wizara ya utamaduni, vijana na michezo na kijana James Amabele anasema walikuwa wakisubiri tukio hili kwa hamu, “Matukio kama haya ndio yataleta amani miongoni mwa wanajamii na Sudan Kusini kwa ujumla. Hili ndilo tulikuwa tukilitamani litokee, lazima tuwe na umoja, na ikiwa kila kitu kitaenda vizuri, basi amani itatawala. Hii ndio amani yenyewe. Tulikuwa tukililia amani na hapa tupo katika umoja na amani; makabila yote yameungana.”Kwa UNMISS, hii ni hatua moja kuelekea kujenga amani ya kudumu na endelevu miongoni mwa jamii ambazo zimekumbwa na mgogoro, mmoja baada ya mwingine katika taifa lote la Sudan Kusini.
11/22/20232 minutes, 26 seconds
Episode Artwork

22 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia tunaangazia mizozo katika ukanda wa Gaza na hali ya mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7. Pia tunamulika amani nchini Sudan Kusini. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani Ufalme wa Tonga katika bahari ya Pasifiki, kulikoni?  Muafaka uliofikiwa jana jioni wa kuwaachilia mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7 umekaribishwa na      Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye amesema Umoja huo uko tayari kutumia hatua hiyo njema kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Katika kukuza utangamano ndani ya jamii yenye makabila tofauti ambayo hapo awali yalikuwa na misuguano Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwakushirikiana na wizara ya Utamaduni ya Sudan Kusini imefanya huko katika jimbo la Equatoria Magharibi.Katika makala Edisoni Tumaini Anatory wa redio washirika wetu Karagwe FM ya wilayani Karagwe, mkoani Kagera Magharibi mwa Tanzania ameangazia elimu ya lishe kwa watoto dhidi ya bidhaa zenye sukari akizingatia wito wa mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la Afya Ulimwenguni (WHO) na la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwamba tabia za ulishaji wa vyakula visivyo salama kiafya kwa watoto wadogo na wachanga lazima ziepukwe katika kuhamasisha wananchi kuchukua hatua za kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza.Na mashinani tutaelekea katika Ufalme wa Tonga, katika bahari ya Pasifiki kusikia ni kwa jinsi gani wavuvi wameweza kuhimili majanga ya mabadiliko ya tabianchi. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/22/20230
Episode Artwork

22 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia tunaangazia mizozo katika ukanda wa Gaza na hali ya mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7. Pia tunamulika amani nchini Sudan Kusini. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani Ufalme wa Tonga katika bahari ya Pasifiki, kulikoni?  Muafaka uliofikiwa jana jioni wa kuwaachilia mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7 umekaribishwa na      Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye amesema Umoja huo uko tayari kutumia hatua hiyo njema kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Katika kukuza utangamano ndani ya jamii yenye makabila tofauti ambayo hapo awali yalikuwa na misuguano Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwakushirikiana na wizara ya Utamaduni ya Sudan Kusini imefanya huko katika jimbo la Equatoria Magharibi.Katika makala Edisoni Tumaini Anatory wa redio washirika wetu Karagwe FM ya wilayani Karagwe, mkoani Kagera Magharibi mwa Tanzania ameangazia elimu ya lishe kwa watoto dhidi ya bidhaa zenye sukari akizingatia wito wa mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa lile la Afya Ulimwenguni (WHO) na la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwamba tabia za ulishaji wa vyakula visivyo salama kiafya kwa watoto wadogo na wachanga lazima ziepukwe katika kuhamasisha wananchi kuchukua hatua za kudhibiti magonjwa yasiyo ya kuambukiza.Na mashinani tutaelekea katika Ufalme wa Tonga, katika bahari ya Pasifiki kusikia ni kwa jinsi gani wavuvi wameweza kuhimili majanga ya mabadiliko ya tabianchi. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/22/202311 minutes, 24 seconds
Episode Artwork

Muafaka wa usitishaji mapigano na kuachilia mateka Gaza umefikiwa, UN yakaribisha

Muafaka uliofikiwa jana jioni wa kuwaachilia mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7 umekaribishwa na  Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye amesema Umoja huo uko tayari kutumia hatua hiyo njema kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Kwa hakika Assumpta muafaka huo ni habari njema ambayo imepokelewa kwa mikoni miwili na mashirika karibu yote ya Umoja wa Mataifa na wahudumu wa kibinadamu huku Katibu Mkuu Guterres kupitia taarifa yake iliyotolewa leo akisema“Ni hatua muhimu kuelekea kunakostahili na Umoja wa Mataifa utasaidia kwa kila hali kufanikisha hilo lakini mengi zaidi yanahitajika kufanywa.”Tor Wennesland ambaye ni mratibu maalum wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya mchakato wa amani wa Mashariki ya Kati ameunga mkono kauli hiyo ya Guterres akikaribisha usitishaji huo wa mapigano Gaza wa saa 96 au siku nne.Amesisitiza kwamba“Usitishaji maiugano huo lazima utumiwe kikamilifu kuwezesha kuachiliwa kwa mateka na kushughulikia mahitaji makubwa ya Wapalestina Gaza”Na wadau wote wa misaada ya kibinadamu wamesema wako tayari kufanya kila wawezalo kutumia fursa hiyo kusaidia.Baadhi ya mashirika ya Umoja wa Mataifa yametumia fursa hiyo kurejea wito wao mfano lile la afya duniani WHO limetaka fursa ya ukufikia wenye uhitaji lazima ihakikishwe bila vikwazo Ukanda wa Gaza ili kuongeza msaada wa kibinadamu likisisitiza kuwa “Hatuwezi kuendelea kutoa matone tu ya msaada wakati mahitaji yaliyopo ni bahari.”La kuratibu misaada ya kibinadamu OCHA limesema muafaka huu umeleta matumaini kwa raia wa Gaza likiamini sasa idadi ya malori ya msaada wa mahitaji muhimu ikiwemo mafuta itaongezeka.Habari hii jjema hata hivyo imekuja kukiwa na hofu kubwa ya njaa hasa Kaskazini mwa Gaza kwa mujibu wa shirika la chakula na kilimo FAO, lakini pia mashambulizi dhidi ya raia na miundombinu yao kama hospitali yakiendelea kusababisha vifo na uharibifu.Nalo Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema tangu kuanza kwa machafuko ya sasa watu 191 wanaopata hifadhi katika vituo vyake wameuawa na wengine 798 kujeruhiwa huku shule mbili za UNRWA zikisambaratishwa kabisa na milipuko. Na jana tu limesema shambulio kwenye hospitali ya Al-Awda Kaskazini mwa Gaza limekatili maisha ya watu 4 wakiwemo madaktari 3 na kumjeruhi muuguzi.
11/22/20230
Episode Artwork

Muafaka wa usitishaji mapigano na kuachilia mateka Gaza umefikiwa, UN yakaribisha

Muafaka uliofikiwa jana jioni wa kuwaachilia mateka waliochukuliwa wakati wa shambulizi la Hamas huko Israel Kusini Oktoba 7 umekaribishwa na  Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ambaye amesema Umoja huo uko tayari kutumia hatua hiyo njema kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Kwa hakika Assumpta muafaka huo ni habari njema ambayo imepokelewa kwa mikoni miwili na mashirika karibu yote ya Umoja wa Mataifa na wahudumu wa kibinadamu huku Katibu Mkuu Guterres kupitia taarifa yake iliyotolewa leo akisema“Ni hatua muhimu kuelekea kunakostahili na Umoja wa Mataifa utasaidia kwa kila hali kufanikisha hilo lakini mengi zaidi yanahitajika kufanywa.”Tor Wennesland ambaye ni mratibu maalum wa Umoja wa Mataifa kwa ajili ya mchakato wa amani wa Mashariki ya Kati ameunga mkono kauli hiyo ya Guterres akikaribisha usitishaji huo wa mapigano Gaza wa saa 96 au siku nne.Amesisitiza kwamba“Usitishaji maiugano huo lazima utumiwe kikamilifu kuwezesha kuachiliwa kwa mateka na kushughulikia mahitaji makubwa ya Wapalestina Gaza”Na wadau wote wa misaada ya kibinadamu wamesema wako tayari kufanya kila wawezalo kutumia fursa hiyo kusaidia.Baadhi ya mashirika ya Umoja wa Mataifa yametumia fursa hiyo kurejea wito wao mfano lile la afya duniani WHO limetaka fursa ya ukufikia wenye uhitaji lazima ihakikishwe bila vikwazo Ukanda wa Gaza ili kuongeza msaada wa kibinadamu likisisitiza kuwa “Hatuwezi kuendelea kutoa matone tu ya msaada wakati mahitaji yaliyopo ni bahari.”La kuratibu misaada ya kibinadamu OCHA limesema muafaka huu umeleta matumaini kwa raia wa Gaza likiamini sasa idadi ya malori ya msaada wa mahitaji muhimu ikiwemo mafuta itaongezeka.Habari hii jjema hata hivyo imekuja kukiwa na hofu kubwa ya njaa hasa Kaskazini mwa Gaza kwa mujibu wa shirika la chakula na kilimo FAO, lakini pia mashambulizi dhidi ya raia na miundombinu yao kama hospitali yakiendelea kusababisha vifo na uharibifu.Nalo Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limesema tangu kuanza kwa machafuko ya sasa watu 191 wanaopata hifadhi katika vituo vyake wameuawa na wengine 798 kujeruhiwa huku shule mbili za UNRWA zikisambaratishwa kabisa na milipuko. Na jana tu limesema shambulio kwenye hospitali ya Al-Awda Kaskazini mwa Gaza limekatili maisha ya watu 4 wakiwemo madaktari 3 na kumjeruhi muuguzi.
11/22/20232 minutes, 25 seconds
Episode Artwork

21 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mada kwa kina ambapo mkutano wa tatu kati ya mitano wa kamati ya kimataifa ya majadiliano baina ya nchi kuhusu uchafuzi wa taka za plastiki INC-3 umekunja jamvi mwishoni mwa wiki jijini Nairobi Kenya, hii ikiwa ni wiki moja tu kabla ya kuanza kwa mkutano wa COP28 utakaofanyika huko Dubai katika Falme za nchi za Kiarabu. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Tunaanzia Ukanda wa Gaza, Mashariki ya Kati ambako mapigano yakiendelea hii leo ikiwa ni siku ya 45 tangu kuanza kwa mzozo eneo hilo kati ya Israeli na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO linasema kila siku watoto takribani 160 wanauawa, ikimaanisha mtoto mmoja kila baada ya dakika 10. WHO inasema wakati huo huo watoto 180 wanazaliwa kila siku eneo hilo na zaidi ya 20 wanahitaji huduma mahsusi ambazo kwa sasa ni changamoto kubwa. Tukisalia Gaza, msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF James Elder akizungumza na waandishi wa  habari huko Geneva, Uswisi hii leo amesema ukosefu wa maji kwenye eneo hilo  unatishia usalama wa watoto. Amegusia pia mateka watoto wanaoshikiliwa na Hamas akisema, “lazima waachiliwe huru. Inachukiza kufikiria kuhusu hofu yao; machungu ya familia zao. Hii lazima ikome.”Na kuelekea mkutano wa mabadiliko ya tabianchi huko Falme za kiarabu mwishoni mwa mwezi huu, mashirika ya Umoja wa Mataifa yanasema wanawake wajawazito, watoto wachanga na watoto wanakabiliwa na hatari kubwa za kiafya kutokana na majanga ya mabadiliko tabianchi hivyo hatua za kukabili tabianchi zisiwaengue.Leo ni siku ya uvuvi duniani na hivyo katika mashinani tutamsikia mchakato wa mazao ya uvuvi kutoka Ziwa Tanganyika nchini Tanzania. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/21/20230
Episode Artwork

21 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mada kwa kina ambapo mkutano wa tatu kati ya mitano wa kamati ya kimataifa ya majadiliano baina ya nchi kuhusu uchafuzi wa taka za plastiki INC-3 umekunja jamvi mwishoni mwa wiki jijini Nairobi Kenya, hii ikiwa ni wiki moja tu kabla ya kuanza kwa mkutano wa COP28 utakaofanyika huko Dubai katika Falme za nchi za Kiarabu. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.Tunaanzia Ukanda wa Gaza, Mashariki ya Kati ambako mapigano yakiendelea hii leo ikiwa ni siku ya 45 tangu kuanza kwa mzozo eneo hilo kati ya Israeli na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas, shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni, WHO linasema kila siku watoto takribani 160 wanauawa, ikimaanisha mtoto mmoja kila baada ya dakika 10. WHO inasema wakati huo huo watoto 180 wanazaliwa kila siku eneo hilo na zaidi ya 20 wanahitaji huduma mahsusi ambazo kwa sasa ni changamoto kubwa. Tukisalia Gaza, msemaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF James Elder akizungumza na waandishi wa  habari huko Geneva, Uswisi hii leo amesema ukosefu wa maji kwenye eneo hilo  unatishia usalama wa watoto. Amegusia pia mateka watoto wanaoshikiliwa na Hamas akisema, “lazima waachiliwe huru. Inachukiza kufikiria kuhusu hofu yao; machungu ya familia zao. Hii lazima ikome.”Na kuelekea mkutano wa mabadiliko ya tabianchi huko Falme za kiarabu mwishoni mwa mwezi huu, mashirika ya Umoja wa Mataifa yanasema wanawake wajawazito, watoto wachanga na watoto wanakabiliwa na hatari kubwa za kiafya kutokana na majanga ya mabadiliko tabianchi hivyo hatua za kukabili tabianchi zisiwaengue.Leo ni siku ya uvuvi duniani na hivyo katika mashinani tutamsikia mchakato wa mazao ya uvuvi kutoka Ziwa Tanganyika nchini Tanzania. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/21/202311 minutes, 4 seconds
Episode Artwork

Mataifa yaongeze kasi ya mabadiliko katika kuhakikisha upatikanaji wa choo safi na salama

Wakati hapo jana Novemba 19 dunia imeadhimisha Siku ya choo Duniani. maudhui yaliyobeba siku hiyo ni ‘Kuongeza kasi ya mabadiliko’. Kampeni hii inazingatia athari za janga la usafi wa mazingira ambalo huwa chanzo cha magonjwa mengi hasa ya kuambukiza. Kwa mujibu wa takwimu za shirika la afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO watu bilioni 3.6 karibu nusu ya watu wote duniani hawana huduma za msingi za usafi na milioni 494 miongoni mwao wanajisaidia haja kubwa katika maeneo ya wazi kwa kukosa huduma ya choo wengi wakiwa ni kutoka katika nchi masikini. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili amezungumza na baadhi ya wakazi wa eneo la Ngong, Kaunti ya Kajiado, nchini Kenya kuhusu changamoto za choo katika eneo hilo unangana naye..
11/20/20230
Episode Artwork

Mataifa yaongeze kasi ya mabadiliko katika kuhakikisha upatikanaji wa choo safi na salama

Wakati hapo jana Novemba 19 dunia imeadhimisha Siku ya choo Duniani. maudhui yaliyobeba siku hiyo ni ‘Kuongeza kasi ya mabadiliko’. Kampeni hii inazingatia athari za janga la usafi wa mazingira ambalo huwa chanzo cha magonjwa mengi hasa ya kuambukiza. Kwa mujibu wa takwimu za shirika la afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO watu bilioni 3.6 karibu nusu ya watu wote duniani hawana huduma za msingi za usafi na milioni 494 miongoni mwao wanajisaidia haja kubwa katika maeneo ya wazi kwa kukosa huduma ya choo wengi wakiwa ni kutoka katika nchi masikini. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili amezungumza na baadhi ya wakazi wa eneo la Ngong, Kaunti ya Kajiado, nchini Kenya kuhusu changamoto za choo katika eneo hilo unangana naye..
11/20/20234 minutes, 33 seconds
Episode Artwork

Mataifa lazima yaende mbali zaidi kuliko ahadi za sasa kutokomeza uzalishaji wa Hewa Chafuzi - UNEP

Wakati joto la ulimwengu na uzalishaji wa hewa chafuzi vikivunja rekodi katika mwaka huu wa 2023, Ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) ya Pengo la Uzalishaji hewa chafuzi iliyotolewa leo Novemba 20 mjini Nairobi Kenya imeeleza kwamba imegundua kuwa ahadi za sasa chini ya Mkataba wa Paris zinaweka ulimwengu kwenye mstari wa ongezeko la joto la nyuzi joto 2.5 hadi 2.9 za Selsiasi zaidi ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda katika karne hii. Ripoti hii iliyotolewa kuelekea mkutano wa tabianchi wa mwaka 2023 unaotarajiwa kufanyika huko Dubai, Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu, inaashiria hitaji la dharura la kuongezeka kwa hatua za kukabiliana na tabianchi kwani rekodi ya viwango vya juu vya joto ilivunjwa na kufikia kiwango kipya mwaka huu lakini wakati huo huo kwa mara nyingine tena ulimwengu umeshindwa kupunguza uzalishaji wa chafuzi.  Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP Inger Anderson akisisitiza kuchukua hatua mpya za kudhibiti mwenendo mbaya wa ulimwengu anasema, "Hakuna mtu au uchumi uliosalia kwenye sayari bila kuathiriwa na mabadiliko ya tabianchi, hivyo tunahitaji kuacha kuweka rekodi zisizohitajika kuhusu uzalishaji wa hewa chafuzi, joto la juu duniani na hali mbaya ya hewa.” Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake alioutoa akiwa New York, Marekani amesema yote haya ni kushindwa kwa uongozi duniani, usaliti kwa wanyonge, na fursa kubwa iliyopotea. Guterres anasisitiza uelekeo wa nishati ya jadidifu akisema, “Tunajua bado inawezekana kufanya kikomo cha nyuzi joto 1.5 za Selsiasi kuwa ukweli. Na tunajua jinsi ya kufika huko - tuna ramani kutoka Shirika la Kimataifa la Nishati na Jopo la serikali (duniani) kuhusu mabadiliko ya tabianchi IPCC. Inahitajika kung'oa mzizi wenye sumu wa janga la tabianchi: nishati ya mafuta ya kisukuku.”  Kiongozi huyu wa Umoja wa Mataifa anawataka viongozi kuimarisha juhudi zao kwa kiasi kikubwa sasa, wakiwa na matamanio ya juu, hatua za juu na kuweka rekodi za juu za upunguzaji wa hewa ukaa. “Awamu inayofuata ya mipango ya kitaifa ya tabianchi itakuwa muhimu.” Anasema Guterres na kuongeza kuwa, “Mipango hii lazima iungwe mkono na fedha, teknolojia, usaidizi na ushirikiano ili kuifanya iwezekane. Kazi ya viongozi katika COP28 ni kuhakikisha hilo linafanyika.” Hadi mwanzoni mwa Oktoba mwaka huu, siku 86 zilirekodiwa kuwa na joto ya zaidi ya nyuzi joto 1.5 za Selsiasi juu ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda. Septemba ulikuwa mwezi wa joto zaidi kuwahi kurekodiwa, ukiwa na wastani wa halijoto duniani nyuzi 1.8 za selsiasi juu ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda. Ripoti hiyo imegundua kuwa uzalishaji wa hewa chafuzi duniani (GHG) umeongezeka kwa asilimia 1.2 kutoka 2021 hadi 2022 hadi kufikia rekodi mpya ya Gigatonnes 57.4 ya ‘Carbon Dioxide Equivalent’ (GtCO2e). Uzalishaji wa GHG kote katika nchi za G20 uliongezeka kwa asilimia 1.2 mwaka wa 2022. Mitindo ya utoaji wa hewa chafuzi inaonesha mifumo ya kimataifa ya ukosefu wa usawa. Kwa sababu ya mienendo hii inayotia wasiwasi na juhudi zisizotosheleza za kupunguza hali hiyo, dunia iko kwenye mwelekeo wa kupanda kwa joto zaidi ya malengo ya tabianchi yaliyokubaliwa katika karne hii. Ripoti hii inatoa wito kwa mataifa yote kuwasilisha mabadiliko ya maendeleo ya viwango vya chini vya hewa ukaa kwa kuzingatia mabadiliko ya nishati. Makaa ya mawe, mafuta na gesi inayochimbwa katika kipindi chote cha uzalishaji kwenye migodi vinaweza kuzalisha zaidi ya mara 3.5 ya bajeti ya hewa ukaa inayopatikana ili kupunguza ongezeko la joto hadi nyuzi joto 1.5 za Selsiasi, na karibu bajeti yote iliyopo kwa nyzi joto 2 za Selsiasi. Nchi zilizo na uwezo na wajibu mkubwa wa uzalishaji wa hewa chafuzi - hasa nchi zenye mapato ya juu na zinazotoa hewa chafuzi nyingi miongoni mwa G20 - zitahitajika kuchukua hatua kabambe zaidi na za haraka na kutoa usaidizi wa kifedha na kiufundi kwa mataifa yanayoendelea. Kwa vile nchi…
11/20/20230
Episode Artwork

Mataifa lazima yaende mbali zaidi kuliko ahadi za sasa kutokomeza uzalishaji wa Hewa Chafuzi - UNEP

Wakati joto la ulimwengu na uzalishaji wa hewa chafuzi vikivunja rekodi katika mwaka huu wa 2023, Ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) ya Pengo la Uzalishaji hewa chafuzi iliyotolewa leo Novemba 20 mjini Nairobi Kenya imeeleza kwamba imegundua kuwa ahadi za sasa chini ya Mkataba wa Paris zinaweka ulimwengu kwenye mstari wa ongezeko la joto la nyuzi joto 2.5 hadi 2.9 za Selsiasi zaidi ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda katika karne hii. Ripoti hii iliyotolewa kuelekea mkutano wa tabianchi wa mwaka 2023 unaotarajiwa kufanyika huko Dubai, Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu, inaashiria hitaji la dharura la kuongezeka kwa hatua za kukabiliana na tabianchi kwani rekodi ya viwango vya juu vya joto ilivunjwa na kufikia kiwango kipya mwaka huu lakini wakati huo huo kwa mara nyingine tena ulimwengu umeshindwa kupunguza uzalishaji wa chafuzi.  Mkurugenzi Mtendaji wa UNEP Inger Anderson akisisitiza kuchukua hatua mpya za kudhibiti mwenendo mbaya wa ulimwengu anasema, "Hakuna mtu au uchumi uliosalia kwenye sayari bila kuathiriwa na mabadiliko ya tabianchi, hivyo tunahitaji kuacha kuweka rekodi zisizohitajika kuhusu uzalishaji wa hewa chafuzi, joto la juu duniani na hali mbaya ya hewa.” Kwa upande wake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake alioutoa akiwa New York, Marekani amesema yote haya ni kushindwa kwa uongozi duniani, usaliti kwa wanyonge, na fursa kubwa iliyopotea. Guterres anasisitiza uelekeo wa nishati ya jadidifu akisema, “Tunajua bado inawezekana kufanya kikomo cha nyuzi joto 1.5 za Selsiasi kuwa ukweli. Na tunajua jinsi ya kufika huko - tuna ramani kutoka Shirika la Kimataifa la Nishati na Jopo la serikali (duniani) kuhusu mabadiliko ya tabianchi IPCC. Inahitajika kung'oa mzizi wenye sumu wa janga la tabianchi: nishati ya mafuta ya kisukuku.”  Kiongozi huyu wa Umoja wa Mataifa anawataka viongozi kuimarisha juhudi zao kwa kiasi kikubwa sasa, wakiwa na matamanio ya juu, hatua za juu na kuweka rekodi za juu za upunguzaji wa hewa ukaa. “Awamu inayofuata ya mipango ya kitaifa ya tabianchi itakuwa muhimu.” Anasema Guterres na kuongeza kuwa, “Mipango hii lazima iungwe mkono na fedha, teknolojia, usaidizi na ushirikiano ili kuifanya iwezekane. Kazi ya viongozi katika COP28 ni kuhakikisha hilo linafanyika.” Hadi mwanzoni mwa Oktoba mwaka huu, siku 86 zilirekodiwa kuwa na joto ya zaidi ya nyuzi joto 1.5 za Selsiasi juu ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda. Septemba ulikuwa mwezi wa joto zaidi kuwahi kurekodiwa, ukiwa na wastani wa halijoto duniani nyuzi 1.8 za selsiasi juu ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda. Ripoti hiyo imegundua kuwa uzalishaji wa hewa chafuzi duniani (GHG) umeongezeka kwa asilimia 1.2 kutoka 2021 hadi 2022 hadi kufikia rekodi mpya ya Gigatonnes 57.4 ya ‘Carbon Dioxide Equivalent’ (GtCO2e). Uzalishaji wa GHG kote katika nchi za G20 uliongezeka kwa asilimia 1.2 mwaka wa 2022. Mitindo ya utoaji wa hewa chafuzi inaonesha mifumo ya kimataifa ya ukosefu wa usawa. Kwa sababu ya mienendo hii inayotia wasiwasi na juhudi zisizotosheleza za kupunguza hali hiyo, dunia iko kwenye mwelekeo wa kupanda kwa joto zaidi ya malengo ya tabianchi yaliyokubaliwa katika karne hii. Ripoti hii inatoa wito kwa mataifa yote kuwasilisha mabadiliko ya maendeleo ya viwango vya chini vya hewa ukaa kwa kuzingatia mabadiliko ya nishati. Makaa ya mawe, mafuta na gesi inayochimbwa katika kipindi chote cha uzalishaji kwenye migodi vinaweza kuzalisha zaidi ya mara 3.5 ya bajeti ya hewa ukaa inayopatikana ili kupunguza ongezeko la joto hadi nyuzi joto 1.5 za Selsiasi, na karibu bajeti yote iliyopo kwa nyzi joto 2 za Selsiasi. Nchi zilizo na uwezo na wajibu mkubwa wa uzalishaji wa hewa chafuzi - hasa nchi zenye mapato ya juu na zinazotoa hewa chafuzi nyingi miongoni mwa G20 - zitahitajika kuchukua hatua kabambe zaidi na za haraka na kutoa usaidizi wa kifedha na kiufundi kwa mataifa yanayoendelea. Kwa vile nchi…
11/20/20232 minutes, 12 seconds
Episode Artwork

20 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mazingira na hali ya joto, na pia mzozo katika ukanda wa Gaza. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani tunasalia hapa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kulikoni?. Wakati joto la ulimwengu na uzalishaji wa hewa chafuzi vikivunja rekodi katika mwaka huu wa 2023, Ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) ya Pengo la Uzalishaji hewa chafuzi iliyotolewa leo Novemba 20 mjini Nairobi Kenya imeeleza kwamba imegundua kuwa ahadi za sasa chini ya Mkataba wa Paris zinaweka ulimwengu kwenye mstari wa ongezeko la joto la nyuzi joto 2.5 hadi 2.9 za Selsiasi zaidi ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda katika karne hii. Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati umesambaratisha kabisa mfumo wa chakula Gaza limeonya shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, likisisitiza wakati huu ambapo ni asilimia 10 tu ya bidhaa muhimu za chakula ndizo zinazoingia Gaza tangu kuanza kwa mzozo huo Oktoba 7. Hali ni mbaya na imesababisha njaa kwa karibu wate wote wa eneo hilo na tegemeo lao pekee lililobaki ni msaada wa chakula kutoka WFP.Makala leo tunaangazia umuhimu wa choo wakati hapo jana Novemba 19 dunia imeadhimisha Siku ya choo Duniani. Maudhui yaliyobeba siku hiyo ni ‘Kuongeza kasi ya mabadiliko’. Kampeni hii inazingatia athari za janga la usafi wa mazingira ambalo huwa chanzo cha magonjwa mengi hasa ya kuambukiza. Kwa mujibu wa takwimu za shirika la afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO watu bilioni 3.6 karibu nusu ya watu wote duniani hawana huduma za msingi za usafi na milioni 494 miongoni mwao wanajisaidia haja kubwa katika maeneo ya wazi kwa kukosa huduma ya choo wengi wakiwa ni kutoka katika nchi masikini. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili amezungumza na baadhi ya wakazi wa eneo la Ngong, Kaunti ya Kajiado, nchini Kenya.Katika mashinani tutasikia ujumbe uliotolewa na mshindi wa tuzo ya polisi mwanamke wa mwaka wa Umoja wa Mataifa. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/20/20230
Episode Artwork

20 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mazingira na hali ya joto, na pia mzozo katika ukanda wa Gaza. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani tunasalia hapa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kulikoni?. Wakati joto la ulimwengu na uzalishaji wa hewa chafuzi vikivunja rekodi katika mwaka huu wa 2023, Ripoti mpya ya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira (UNEP) ya Pengo la Uzalishaji hewa chafuzi iliyotolewa leo Novemba 20 mjini Nairobi Kenya imeeleza kwamba imegundua kuwa ahadi za sasa chini ya Mkataba wa Paris zinaweka ulimwengu kwenye mstari wa ongezeko la joto la nyuzi joto 2.5 hadi 2.9 za Selsiasi zaidi ya viwango vya kabla ya kuanza kwa viwanda katika karne hii. Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati umesambaratisha kabisa mfumo wa chakula Gaza limeonya shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, likisisitiza wakati huu ambapo ni asilimia 10 tu ya bidhaa muhimu za chakula ndizo zinazoingia Gaza tangu kuanza kwa mzozo huo Oktoba 7. Hali ni mbaya na imesababisha njaa kwa karibu wate wote wa eneo hilo na tegemeo lao pekee lililobaki ni msaada wa chakula kutoka WFP.Makala leo tunaangazia umuhimu wa choo wakati hapo jana Novemba 19 dunia imeadhimisha Siku ya choo Duniani. Maudhui yaliyobeba siku hiyo ni ‘Kuongeza kasi ya mabadiliko’. Kampeni hii inazingatia athari za janga la usafi wa mazingira ambalo huwa chanzo cha magonjwa mengi hasa ya kuambukiza. Kwa mujibu wa takwimu za shirika la afya la Umoja wa Mataifa Duniani WHO watu bilioni 3.6 karibu nusu ya watu wote duniani hawana huduma za msingi za usafi na milioni 494 miongoni mwao wanajisaidia haja kubwa katika maeneo ya wazi kwa kukosa huduma ya choo wengi wakiwa ni kutoka katika nchi masikini. Pamela Awuori wa Idhaa hii ya Kiswahili amezungumza na baadhi ya wakazi wa eneo la Ngong, Kaunti ya Kajiado, nchini Kenya.Katika mashinani tutasikia ujumbe uliotolewa na mshindi wa tuzo ya polisi mwanamke wa mwaka wa Umoja wa Mataifa. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/20/202313 minutes, 24 seconds
Episode Artwork

WFP yaonya mfumo wa chakula Gaza umesambaratika kabisa

Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati umesambaratisha kabisa mfumo wa chakula Gaza limeonya shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, likisisitiza wakati huu ambapo ni asilimia 10 tu ya bidhaa muhimu za chakula ndizo zinazoingia Gaza tangu kuanza kwa mzozo huo Oktoba 7. Hali ni mbaya na imesababisha njaa kwa karibu wate wote wa eneo hilo na tegemeo lao pekee lililobaki ni msaada wa chakula kutoka WFP. Watoto wakicheza nje ya majengo ya shule ya umma ya GV  katika eneo la Deir El Balah Gaza, kana kwamba hakuna kinachoendelea, wakifurahia utoto wao na kidogo kusahau vita iliyowalazimu kuwa wakimbizi wa ndani katika shule hii iliyogeuzwa makazi ya muda.Inakadiriwa kwamba watu takriban 6,000 wanapata hifadhi katika kila shule kama hii.Hapa mlo ni changamoto, Nattss……Wanawake kwa wanaume wanapika na kujaribu kuoka mikate ambayo ndio chakula kikuu Gaza kwenye majiko ya kuni na mkaa kwani hawana gesi wala umeme. Shifa Al Masri ni mama na mmoja wa wakimbizi wa ndani hapa anasema “Watoto wananjaa na kiu na wote wanaharisha kutapika na kukohoa, hakuna chakula wala matibabu”Kabla ya machafuko ya sasa watu hawa walikuwa walila wawzavyo na kujipatia mahitaji katika maduka ya chakula yanayoendeshwa na WFP lakini sasa maduka haya yamesalia matupu bila chochote.Ni asilimia 25 tu ya maduka yote ya WFP Gaza ndio yaliyosalia wazi na mengine yote yamefunga mlango kwa kuishiwa chakula na yaliyowazi chakula kidogo kilichopo gharama haishikiki hali ambayo imewalazimu watu kula mlo mmoja tu kwa siku.Alaa Younis Mohamed Al-Helw hakuwa na jinsi bali kukimbia na familia yake hadi kwenye makazi haya ambapo sasa analala chini katika nyumba iliyofurika watu 30. Kaja dukani kuangalia mahitaji , lahaula kambulia patupu anatoa wito,“Kama unavyoona tumekuja katika duka hili hakuna chochote tangu asubuhi tumezunguka maduka yote hakuna kitu. Wajuzeni watu ili dunia isikie tuna njaa, tuna njaa tunataka kula, Kuna watoto na mke wangu ana ugonjwa wa moyo anahitaji kula na hakuna hata kipande cha mkate cha kumpa.”Mkate chakula kikuu cha Wapalestina sasa umeadimika kupita kiasi, matumaini yao yote yako kwa WFP. Samer Abdeljaber ni mkurugenzi wa WFP eneo la Palestina,“Watu wanalala njaa. Gaza, watu wanaishi kwa mlo mmoja tu kwa siku ikiwa wana bahati. Uhaba wa mafuta na kutokuwa na mawasiliano kunalemaza operesheni zetu huko Gaza. Ukosefu wa mafuta umekilazimu kiwanda cha mwisho cha kuoka mikate cha WFP kufungwa na pia kinu cha mwisho cha kusagisha unga wa ngano. Hata mkate ambao ni msingi wa kila mlo wa Wapalestina, sasa umeadimika.”Pamoja na changamoto zote hizo WFP imeendelea kuwahakikisha mlo hata kama ni mmoja tu watu hawa, inagawa tende na samaki wa makopo kila siku kwa watu karibu 800,000 wanaohifadhiwa katika shule za shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA na jamii zinazowazunguka.
11/20/20230
Episode Artwork

WFP yaonya mfumo wa chakula Gaza umesambaratika kabisa

Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati umesambaratisha kabisa mfumo wa chakula Gaza limeonya shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, likisisitiza wakati huu ambapo ni asilimia 10 tu ya bidhaa muhimu za chakula ndizo zinazoingia Gaza tangu kuanza kwa mzozo huo Oktoba 7. Hali ni mbaya na imesababisha njaa kwa karibu wate wote wa eneo hilo na tegemeo lao pekee lililobaki ni msaada wa chakula kutoka WFP. Watoto wakicheza nje ya majengo ya shule ya umma ya GV  katika eneo la Deir El Balah Gaza, kana kwamba hakuna kinachoendelea, wakifurahia utoto wao na kidogo kusahau vita iliyowalazimu kuwa wakimbizi wa ndani katika shule hii iliyogeuzwa makazi ya muda.Inakadiriwa kwamba watu takriban 6,000 wanapata hifadhi katika kila shule kama hii.Hapa mlo ni changamoto, Nattss……Wanawake kwa wanaume wanapika na kujaribu kuoka mikate ambayo ndio chakula kikuu Gaza kwenye majiko ya kuni na mkaa kwani hawana gesi wala umeme. Shifa Al Masri ni mama na mmoja wa wakimbizi wa ndani hapa anasema “Watoto wananjaa na kiu na wote wanaharisha kutapika na kukohoa, hakuna chakula wala matibabu”Kabla ya machafuko ya sasa watu hawa walikuwa walila wawzavyo na kujipatia mahitaji katika maduka ya chakula yanayoendeshwa na WFP lakini sasa maduka haya yamesalia matupu bila chochote.Ni asilimia 25 tu ya maduka yote ya WFP Gaza ndio yaliyosalia wazi na mengine yote yamefunga mlango kwa kuishiwa chakula na yaliyowazi chakula kidogo kilichopo gharama haishikiki hali ambayo imewalazimu watu kula mlo mmoja tu kwa siku.Alaa Younis Mohamed Al-Helw hakuwa na jinsi bali kukimbia na familia yake hadi kwenye makazi haya ambapo sasa analala chini katika nyumba iliyofurika watu 30. Kaja dukani kuangalia mahitaji , lahaula kambulia patupu anatoa wito,“Kama unavyoona tumekuja katika duka hili hakuna chochote tangu asubuhi tumezunguka maduka yote hakuna kitu. Wajuzeni watu ili dunia isikie tuna njaa, tuna njaa tunataka kula, Kuna watoto na mke wangu ana ugonjwa wa moyo anahitaji kula na hakuna hata kipande cha mkate cha kumpa.”Mkate chakula kikuu cha Wapalestina sasa umeadimika kupita kiasi, matumaini yao yote yako kwa WFP. Samer Abdeljaber ni mkurugenzi wa WFP eneo la Palestina,“Watu wanalala njaa. Gaza, watu wanaishi kwa mlo mmoja tu kwa siku ikiwa wana bahati. Uhaba wa mafuta na kutokuwa na mawasiliano kunalemaza operesheni zetu huko Gaza. Ukosefu wa mafuta umekilazimu kiwanda cha mwisho cha kuoka mikate cha WFP kufungwa na pia kinu cha mwisho cha kusagisha unga wa ngano. Hata mkate ambao ni msingi wa kila mlo wa Wapalestina, sasa umeadimika.”Pamoja na changamoto zote hizo WFP imeendelea kuwahakikisha mlo hata kama ni mmoja tu watu hawa, inagawa tende na samaki wa makopo kila siku kwa watu karibu 800,000 wanaohifadhiwa katika shule za shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA na jamii zinazowazunguka.
11/20/20233 minutes, 42 seconds
Episode Artwork

Juhudi za pamoja zimesaidia kudhibiti kipindupindu Zanzibar: WHO

Mtazamo wa kujumuisha sekta mbalimbali na kuishirikisha kikamilifu jamii imekuwa chachu kubwa ya kudhibiti milipuko ya ugonjwa wa kipindupindu iliyokuwa ikikiandama kisiwa cha Zanzibar kwa muda mrefu limesema shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO. Mtazamo huo ambao unaunganisha kampeni za uelimishaji kwa jamii kupitia ufadhili wa muungano wa chanjo duniani GAVI na msaada wa wadau mbalimbali likiwemo shirika la WHO imekisaidia kisiwa hicho kutokuwa na mgonjwa hata mmoja wa kipindupindu katika miaka mitano iliyopita. Ungana na Flora Nducha kwa makala hii kwa kina.
11/17/20230
Episode Artwork

Juhudi za pamoja zimesaidia kudhibiti kipindupindu Zanzibar: WHO

Mtazamo wa kujumuisha sekta mbalimbali na kuishirikisha kikamilifu jamii imekuwa chachu kubwa ya kudhibiti milipuko ya ugonjwa wa kipindupindu iliyokuwa ikikiandama kisiwa cha Zanzibar kwa muda mrefu limesema shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO. Mtazamo huo ambao unaunganisha kampeni za uelimishaji kwa jamii kupitia ufadhili wa muungano wa chanjo duniani GAVI na msaada wa wadau mbalimbali likiwemo shirika la WHO imekisaidia kisiwa hicho kutokuwa na mgonjwa hata mmoja wa kipindupindu katika miaka mitano iliyopita. Ungana na Flora Nducha kwa makala hii kwa kina.
11/17/20233 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa unasimama na Afrika kutatua janga la tabianchi – Joyce Msuya

Ijumaa wiki ijayo yaani tarehe 24 vitaanzaa vikao vya awali kuelekea COP 28 ambao ni Mkutano wa  mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika Dubai huko Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu kuanzia tarehe 30.Kuelekea mkutano huu, Naibu wa Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA, Joyce Msuya ameutumia mwezi huu kufanya ziara katika nchi nne za kusini na mashariki mwa Afrika ambako amesisitiza dhamira ya Umoja wa Mataifa ya kusimama na watu na Serikali za ukanda huo wakati janga la tabianchi linafanya mahitaji ya kibinadamu kuwa ya juu zaidi."Na nitamalizia kwa kusema jumuiya ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa, ikiwa ni pamoja na NGOs, NGOs za kitaifa na kimataifa, tumejitolea kikamilifu kuendelea kuunga mkono na kukamilisha juhudi za mamlaka zinazojaribu kuokoa maisha, na pia tutaendelea kufanya kazi na wadau wetu wa maendeleo katika mnepo.”Alipokuwa nchini Msumbiji, nchi ya kwanza katika ziara yake kabla ya Kwenda Tanzania, Kenya na Botswana, Bi Msuya alijionea jinsi athari ya pamoja ya vimbunga, migogoro na mabadiliko ya tabianchi yameweka zaidi ya watu milioni 2 katika mahitaji makubwa ya  kibinadamu."Nimejawa na matumaini kwa sababu ya ujasiri wa watu niliokutana nao, watoto ambao nimecheza nao, wataalamu wa tiba ambao nimezungumza nao na maafisa wa kibinadamu wa wilaya ambao wanajitoa sana."
11/17/20230
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa unasimama na Afrika kutatua janga la tabianchi – Joyce Msuya

Ijumaa wiki ijayo yaani tarehe 24 vitaanzaa vikao vya awali kuelekea COP 28 ambao ni Mkutano wa  mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika Dubai huko Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu kuanzia tarehe 30.Kuelekea mkutano huu, Naibu wa Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA, Joyce Msuya ameutumia mwezi huu kufanya ziara katika nchi nne za kusini na mashariki mwa Afrika ambako amesisitiza dhamira ya Umoja wa Mataifa ya kusimama na watu na Serikali za ukanda huo wakati janga la tabianchi linafanya mahitaji ya kibinadamu kuwa ya juu zaidi."Na nitamalizia kwa kusema jumuiya ya kibinadamu, Umoja wa Mataifa, ikiwa ni pamoja na NGOs, NGOs za kitaifa na kimataifa, tumejitolea kikamilifu kuendelea kuunga mkono na kukamilisha juhudi za mamlaka zinazojaribu kuokoa maisha, na pia tutaendelea kufanya kazi na wadau wetu wa maendeleo katika mnepo.”Alipokuwa nchini Msumbiji, nchi ya kwanza katika ziara yake kabla ya Kwenda Tanzania, Kenya na Botswana, Bi Msuya alijionea jinsi athari ya pamoja ya vimbunga, migogoro na mabadiliko ya tabianchi yameweka zaidi ya watu milioni 2 katika mahitaji makubwa ya  kibinadamu."Nimejawa na matumaini kwa sababu ya ujasiri wa watu niliokutana nao, watoto ambao nimecheza nao, wataalamu wa tiba ambao nimezungumza nao na maafisa wa kibinadamu wa wilaya ambao wanajitoa sana."
11/17/20231 minute, 33 seconds
Episode Artwork

17 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mzozo katika ukanda wa Gaza na mabadiliko ya tabianchi barani Afrika. Makala na mashinani tunakupeleka viziwani Zanzibar nchini Tanzania, kulikoni?. Wakati mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea na wananchi walioko Gaza wakiwa katika siku ya nne bila mawasiliano kutokana na ukosefu wa mafuta, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki ya maji salama ya kunywa na usafi ameionya Israel kuwa kuwanyima wananchi maji ni ukiukaji wa haki za binadamu kwani wanatumia maji kama silaha ya vita. Ijumaa wiki ijayo yaani tarehe 24 vitaanzaa vikao vya awali kuelekea COP 28 ambao ni Mkutano wa  mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika Dubai huko Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu kuanzia tarehe 30.Makala inatupeleka Zanzibar Tanzania ambako juhudi kubwa zilizofanywa na serikali na wadau mbalimbali likiwemo shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limesaidia kupambana na kukomesha milipuko ya kipindupindu ya mara kwa mara, kupunguza athari zake vikiwemo vifo na kuelimisha jamii jinsi ya kuzuia milipuko hiyo.Katika mashinani tunakuletea ujumbe kutoka shujaa mwenye umri wa miaka 9 kutoka Visiwani Zanzibar anayeoongoza katika utunzaji wa mazingira kwa kutumia sauti yake kuhamasisha hatua kwa mustakabali endelevu.” Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/17/20230
Episode Artwork

17 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mzozo katika ukanda wa Gaza na mabadiliko ya tabianchi barani Afrika. Makala na mashinani tunakupeleka viziwani Zanzibar nchini Tanzania, kulikoni?. Wakati mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea na wananchi walioko Gaza wakiwa katika siku ya nne bila mawasiliano kutokana na ukosefu wa mafuta, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki ya maji salama ya kunywa na usafi ameionya Israel kuwa kuwanyima wananchi maji ni ukiukaji wa haki za binadamu kwani wanatumia maji kama silaha ya vita. Ijumaa wiki ijayo yaani tarehe 24 vitaanzaa vikao vya awali kuelekea COP 28 ambao ni Mkutano wa  mabadiliko ya tabianchi utakaofanyika Dubai huko Falme za Kiarabu mwishoni mwa mwezi huu kuanzia tarehe 30.Makala inatupeleka Zanzibar Tanzania ambako juhudi kubwa zilizofanywa na serikali na wadau mbalimbali likiwemo shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limesaidia kupambana na kukomesha milipuko ya kipindupindu ya mara kwa mara, kupunguza athari zake vikiwemo vifo na kuelimisha jamii jinsi ya kuzuia milipuko hiyo.Katika mashinani tunakuletea ujumbe kutoka shujaa mwenye umri wa miaka 9 kutoka Visiwani Zanzibar anayeoongoza katika utunzaji wa mazingira kwa kutumia sauti yake kuhamasisha hatua kwa mustakabali endelevu.” Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/17/202311 minutes, 34 seconds
Episode Artwork

Israeli yaonywa Maji na mafuta yasitumike kama silaha za vita

Wakati mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea na wananchi walioko Gaza wakiwa katika siku ya nne bila mawasiliano kutokana na ukosefu wa mafuta, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki ya maji salama ya kunywa na usafi ameionya Israel kuwa kuwanyima wananchi maji ni ukiukaji wa haki za binadamu kwani wanatumia maji kama silaha ya vita. Mwakilishi huyo maalum wa Umoja wa Mataifa Pedro Arrojo- Agudo ameionya Israel hii leo kuwa inapaswa kuruhusu maji safi na mafuta kuingia Gaza ili kuwezesha mtandao wa usambazi wa maji na mitambo ya kuondoa chumvi kwenye maji ifanyekazi mapema kabla ya kuchelewa.Katika taarifa yake iliyotolewa leo huko Geneva Uswisi na Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa Agudo ameseme “Nataka kuikumbusha Israel kwamba kuzuia vifaa vinavyohitajika kwa ajili ya maji salama kuingia Ukanda wa Gaza kunakiuka sheria za kimataifa za kibinadamu na haki za binadamu. Athari zitakazo jitokeza kwenye afya ya umma haziwezi kufikirika na zinaweza kusababisha vifo vya raia zaidi ya idadi kubwa ya vifo vilivyotokana na mashambulizi ya Gaza.”Mtaalamu huyo amenukuu kifungu cha 7 cha Mkataba wa Roma kinachohusu kuwanyima raia hali zinazowawezesha kuishi kuwa kunachukuliwa kuwa ni uhalifu dhidi ya ubinadamu nakusema “Maafa haya ya kivita yanaweza kuzuilika na Israel lazima izuie, Israel lazima iache kutumia maji kama silaha ya vita.”Kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA asilimia 70 ya wananchi wa Gaza wanakunywa maji machafu na yenye chumvi na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka iwapo Israel itaendelea kuzuia mafuta kuingia Gaza. UNRWA pia imeeeleza kuwa visima 60 vya kusukuma maji taka huko kusini mwa Gaza pamoja na mitambo ya kuondoa maji chumvi huko Rafah navyo havifanyi kazi suala ambalo limeelezwa kuwa ni hatari kwani linaweza kusababisha milipuko ya magonjwa.Mbali na suala la Maji UNRWA hii leo kupitia mtandao wa kijamii wa X imeeleza kuwa “Watu walioko Ukanda wa Gaza usiku wa jana wametengwa kabisa na ulimwengu kwa sababu ya kukatika kwa mawasiliano kutokana na kutokuwepo kwa mafuta.”Nako huko Ukingo wa Magharibi katika eneo la Palestina linalokaliwa na Israel, Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni WHO, limeripoti kuwa na wasiwasi kutokana na kuongezeka kwa mashambulizi ya vituo vya afya ambapo tangu tarehe 07 Oktoba mpaka sasa kumekuwa na mashambulizi 170.WHO imeeleza hii leo huko Jenin Ukingo wa Magharibi wahudumu wa afya 6 waliokuwa wakitoka katika hospitali ya Ibn Sina walipekuliwa na kuzuiliwa na magari matatu ya kubeba wagonjwa nayo pia yalipekuliwa. Shirika hilo limekumbusha kuwa wahudumu wa afya sio walengwa katika mizozo na kwamba wanapaswa kulindwa wao navituo vya afya. 
11/17/20230
Episode Artwork

Israeli yaonywa Maji na mafuta yasitumike kama silaha za vita

Wakati mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea na wananchi walioko Gaza wakiwa katika siku ya nne bila mawasiliano kutokana na ukosefu wa mafuta, mwakilishi maalum wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki ya maji salama ya kunywa na usafi ameionya Israel kuwa kuwanyima wananchi maji ni ukiukaji wa haki za binadamu kwani wanatumia maji kama silaha ya vita. Mwakilishi huyo maalum wa Umoja wa Mataifa Pedro Arrojo- Agudo ameionya Israel hii leo kuwa inapaswa kuruhusu maji safi na mafuta kuingia Gaza ili kuwezesha mtandao wa usambazi wa maji na mitambo ya kuondoa chumvi kwenye maji ifanyekazi mapema kabla ya kuchelewa.Katika taarifa yake iliyotolewa leo huko Geneva Uswisi na Ofisi ya Haki za Binadamu ya Umoja wa Mataifa Agudo ameseme “Nataka kuikumbusha Israel kwamba kuzuia vifaa vinavyohitajika kwa ajili ya maji salama kuingia Ukanda wa Gaza kunakiuka sheria za kimataifa za kibinadamu na haki za binadamu. Athari zitakazo jitokeza kwenye afya ya umma haziwezi kufikirika na zinaweza kusababisha vifo vya raia zaidi ya idadi kubwa ya vifo vilivyotokana na mashambulizi ya Gaza.”Mtaalamu huyo amenukuu kifungu cha 7 cha Mkataba wa Roma kinachohusu kuwanyima raia hali zinazowawezesha kuishi kuwa kunachukuliwa kuwa ni uhalifu dhidi ya ubinadamu nakusema “Maafa haya ya kivita yanaweza kuzuilika na Israel lazima izuie, Israel lazima iache kutumia maji kama silaha ya vita.”Kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA asilimia 70 ya wananchi wa Gaza wanakunywa maji machafu na yenye chumvi na idadi hiyo inatarajiwa kuongezeka iwapo Israel itaendelea kuzuia mafuta kuingia Gaza. UNRWA pia imeeeleza kuwa visima 60 vya kusukuma maji taka huko kusini mwa Gaza pamoja na mitambo ya kuondoa maji chumvi huko Rafah navyo havifanyi kazi suala ambalo limeelezwa kuwa ni hatari kwani linaweza kusababisha milipuko ya magonjwa.Mbali na suala la Maji UNRWA hii leo kupitia mtandao wa kijamii wa X imeeleza kuwa “Watu walioko Ukanda wa Gaza usiku wa jana wametengwa kabisa na ulimwengu kwa sababu ya kukatika kwa mawasiliano kutokana na kutokuwepo kwa mafuta.”Nako huko Ukingo wa Magharibi katika eneo la Palestina linalokaliwa na Israel, Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni WHO, limeripoti kuwa na wasiwasi kutokana na kuongezeka kwa mashambulizi ya vituo vya afya ambapo tangu tarehe 07 Oktoba mpaka sasa kumekuwa na mashambulizi 170.WHO imeeleza hii leo huko Jenin Ukingo wa Magharibi wahudumu wa afya 6 waliokuwa wakitoka katika hospitali ya Ibn Sina walipekuliwa na kuzuiliwa na magari matatu ya kubeba wagonjwa nayo pia yalipekuliwa. Shirika hilo limekumbusha kuwa wahudumu wa afya sio walengwa katika mizozo na kwamba wanapaswa kulindwa wao navituo vya afya. 
11/17/20232 minutes, 58 seconds
Episode Artwork

Methali: Ukilima Pantosha utavuna pankwisha

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalam wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali, “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha.” Karibu!
11/16/20230
Episode Artwork

Methali: Ukilima Pantosha utavuna pankwisha

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalam wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali, “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha.” Karibu!
11/16/20231 minute, 6 seconds
Episode Artwork

16 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo ulimwengu ukijiandaa kuadhimisha siku 16 za harakati kukabiliana na ukatili wa kijinsia katika jamii zinazoendeshwa na Umoja wa Mataifa, baadhi ya sehemu duniani zimeanza kulipa suala Hilo uzito mkubwa ikiwemo Kenya. Kwa ushirikiano wa Shirika la Umoja wa mataifa la masuala ya wanawake UN Women na mengine yasiyo ya kiserikali, Kaunti ya Kakamega nchini nchini humo imefanikiwa kuzindua mpango maalum wa kuwapa waathirika wa ukatili wa kijinsia huduma za mahakamani pasi na malipo. UN Women imewashika mkono baadhi ya walioathirika kwa kuwapa bidhaa za matumizi na pia mtaji kuwawezesha kuanza biashara baada ya kuondoka kwenye vituo salama na vya Staha. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo kutoka Gaza, Ethiopia n aza WHO kuhusu matumizi ya tumbaku. Katika kujifunza Kiswahili leo tunabisha hodi Chuo Kikuu cha Zetech Limuru nchini Kenya kuchambuliwa maana ya Methali “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha”. Kamishina Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) Philippe Lazzarini kupitia ukurasa wake wa X ameandika "Kila siku ni siku ya huzuni kwa Umoja wa Mataifa na UNRWA, na kwamba anasikitika kuthibitisha kwamba wenzake 103 wameuawa Gaza tangu 7 Oktoba. Naye Tom White, Mkurugenzi wa UNRWA Gaza pia kupitia X ameandika kukosekana kwa mafuta inamaanisha ukosefu wa maji ya kunywa na kusababisha ongezeko la asilimia 40 la ugonjwa wa kuhara kwa watu wanaojihifadhi katika shule. Wakati ho huo Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk akisisitiza kuwa njia ya kisiasa inahitajika kuitoa Gaza kwenye janga la kibinadamu. Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO), leo limezindua rasmi kampeni ya "Acha uwongo" ikiwa ni hatua muhimu ya kuwalinda vijana dhidi ya sekta ya tumbaku na bidhaa zao. WHO inasema Sekta ya tumbaku ina historia ndefu ya kusema uwongo kwa umma, hata kufikia kusisitiza kwamba uvutaji sigara hausababishi saratani ya mapafu. Pia sekta hiyo inaendelea kutumia njia tofauti kueneza habari potofu, ikijumuisha kupitia watu maarufu katika mitandao ya kijamii, kufadhili matukio, na hata kufadhili wanasayansi na utafiti wenye upendeleo.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limesema linafufua mfumo wake ulioboreshwa wa operesheni nchini Ethiopia, hatua kubwa ambayo itaanza kuwafikia watu milioni 3.2 kwa msaada wa chakula kwa mara ya kwanza tangu Juni 2023. Msaada wa chakula wa WFP ulisitishwa nchini kote Ethiopia kufuatia ripoti za uporaji wa misaada.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalam wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha.” Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/16/20230
Episode Artwork

16 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo ulimwengu ukijiandaa kuadhimisha siku 16 za harakati kukabiliana na ukatili wa kijinsia katika jamii zinazoendeshwa na Umoja wa Mataifa, baadhi ya sehemu duniani zimeanza kulipa suala Hilo uzito mkubwa ikiwemo Kenya. Kwa ushirikiano wa Shirika la Umoja wa mataifa la masuala ya wanawake UN Women na mengine yasiyo ya kiserikali, Kaunti ya Kakamega nchini nchini humo imefanikiwa kuzindua mpango maalum wa kuwapa waathirika wa ukatili wa kijinsia huduma za mahakamani pasi na malipo. UN Women imewashika mkono baadhi ya walioathirika kwa kuwapa bidhaa za matumizi na pia mtaji kuwawezesha kuanza biashara baada ya kuondoka kwenye vituo salama na vya Staha. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo kutoka Gaza, Ethiopia n aza WHO kuhusu matumizi ya tumbaku. Katika kujifunza Kiswahili leo tunabisha hodi Chuo Kikuu cha Zetech Limuru nchini Kenya kuchambuliwa maana ya Methali “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha”. Kamishina Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa Kipalestina (UNRWA) Philippe Lazzarini kupitia ukurasa wake wa X ameandika "Kila siku ni siku ya huzuni kwa Umoja wa Mataifa na UNRWA, na kwamba anasikitika kuthibitisha kwamba wenzake 103 wameuawa Gaza tangu 7 Oktoba. Naye Tom White, Mkurugenzi wa UNRWA Gaza pia kupitia X ameandika kukosekana kwa mafuta inamaanisha ukosefu wa maji ya kunywa na kusababisha ongezeko la asilimia 40 la ugonjwa wa kuhara kwa watu wanaojihifadhi katika shule. Wakati ho huo Kamishina Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk akisisitiza kuwa njia ya kisiasa inahitajika kuitoa Gaza kwenye janga la kibinadamu. Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO), leo limezindua rasmi kampeni ya "Acha uwongo" ikiwa ni hatua muhimu ya kuwalinda vijana dhidi ya sekta ya tumbaku na bidhaa zao. WHO inasema Sekta ya tumbaku ina historia ndefu ya kusema uwongo kwa umma, hata kufikia kusisitiza kwamba uvutaji sigara hausababishi saratani ya mapafu. Pia sekta hiyo inaendelea kutumia njia tofauti kueneza habari potofu, ikijumuisha kupitia watu maarufu katika mitandao ya kijamii, kufadhili matukio, na hata kufadhili wanasayansi na utafiti wenye upendeleo.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) limesema linafufua mfumo wake ulioboreshwa wa operesheni nchini Ethiopia, hatua kubwa ambayo itaanza kuwafikia watu milioni 3.2 kwa msaada wa chakula kwa mara ya kwanza tangu Juni 2023. Msaada wa chakula wa WFP ulisitishwa nchini kote Ethiopia kufuatia ripoti za uporaji wa misaada.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili mtaalam wetu leo ni Nicholus Makanji mhadhiri katika chuo Kikuu cha Zetech Limuru Kenya akitufafanulia maana ya methali “Ukilima Pantosha utavuna pankwisha.” Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/16/202312 minutes, 2 seconds
Episode Artwork

Tiko: Jukwaa la kidijitali linalotumia simu ya mkononi launganisha vijana Kenya

Umoja wa Mataifa nchini Kenya, kupitia ushirikiano unaoongozwa na UNFPA, UNAIDS, WHO, na Jukwaa la Ushirikiano wa SDG, chini ya uratibu wa jumla wa Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa, kwa ushirikiano na Serikali ya Kenya, shirika la kimataifa la Triggerise, Children's Investment Fund Foundation (CIFF), and Bridges Outcomes Partnerships wanatekeleza mradi wa elimu ya afya ya uzazi kwa vijana nchini Kenya kupitia huduma ya Tiko ya shirika la Triggerise. Kiujumla huduma ya TIKO inalenga kupunguza mimba za utotoni na maambukizi ya VVU miongoni mwa wasichana wenye umri wa miaka 15 - 19Tiko ni jukwaa la kidijitali linalotumia simu ya mkononi ambalo huunganisha vijana waliobalehe kwenye vituo vya karibu vya umma na vya kibinafsi vinavyotoa huduma bila malipo. Mfumo wa Tiko unawaleta pamoja wahusika wakiwemo mitandao ya kliniki za afya, maduka ya dawa, mitandaoni, mashirika ya kijamii, na wahudumu wa afya wanaosaidia vijana katika kufanya uamuzi wao kwa huduma za afya na ustawi wanazohitaji ili kustawi. Kupitia mfumo wa kidijitali, Triggerise inaweza kufuatilia kila senti inakoenda na kutathmini matokeo yake kila siku kwa ripoti za wakati halisi na maarifa yanayotokana na takwimu.
11/15/20230
Episode Artwork

Tiko: Jukwaa la kidijitali linalotumia simu ya mkononi launganisha vijana Kenya

Umoja wa Mataifa nchini Kenya, kupitia ushirikiano unaoongozwa na UNFPA, UNAIDS, WHO, na Jukwaa la Ushirikiano wa SDG, chini ya uratibu wa jumla wa Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa, kwa ushirikiano na Serikali ya Kenya, shirika la kimataifa la Triggerise, Children's Investment Fund Foundation (CIFF), and Bridges Outcomes Partnerships wanatekeleza mradi wa elimu ya afya ya uzazi kwa vijana nchini Kenya kupitia huduma ya Tiko ya shirika la Triggerise. Kiujumla huduma ya TIKO inalenga kupunguza mimba za utotoni na maambukizi ya VVU miongoni mwa wasichana wenye umri wa miaka 15 - 19Tiko ni jukwaa la kidijitali linalotumia simu ya mkononi ambalo huunganisha vijana waliobalehe kwenye vituo vya karibu vya umma na vya kibinafsi vinavyotoa huduma bila malipo. Mfumo wa Tiko unawaleta pamoja wahusika wakiwemo mitandao ya kliniki za afya, maduka ya dawa, mitandaoni, mashirika ya kijamii, na wahudumu wa afya wanaosaidia vijana katika kufanya uamuzi wao kwa huduma za afya na ustawi wanazohitaji ili kustawi. Kupitia mfumo wa kidijitali, Triggerise inaweza kufuatilia kila senti inakoenda na kutathmini matokeo yake kila siku kwa ripoti za wakati halisi na maarifa yanayotokana na takwimu.
11/15/20234 minutes, 4 seconds
Episode Artwork

Waafghanistan wanaorejea kutoka Pakistan wanahitaji msaada - UN

Tangu katikati ya mwezi Septemba mwaka huu kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wananchi wa Afghanistan wanaorejea nchini mwao wakitokea Pakistan ambako wamelazimika kuondoka kutokana na kutokuwa na vibali vya kuishi nchini humo. Ongezeko hilo kubwa la watu limeleta changamoto kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayotoa misaada ya kibinadamu. Wengi wa wananchi hawa wanaorejea Afghanistan wanawasili wakiwa na mali kidogo kwani nyumba na mali zao zote wameziacha nchini Pakistan na sasa wanafika mpakani wakiwa hawajui waende wapi wala mustakabali wa maisha yao. Kaimu Mratibu wa masuala ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan Daniel Peter Endres, akimbatana na maafisa wengine wa mashirika ya Umoja wa Mataifa wamefanya ziara maalum jimboni Nangarhar na kuzungumza na wananchi hao. “Leo niko hapa katika eneo la Torkham mpakani na Pakistani kushuhudia maelfu ya Waafghanistan wakirejea. Wengi wa watu hawa wako katika hali mbaya sana, walisubiri siku kadhaa kabla ya kufika hapa. Nimezungumza na watu wengi, na wameniambia hawana nyumba hapa nchini Afghanistan na majira ya baridi yataanza ndani ya wiki chache zijazo.” Ujumbe unaoongozwa na Bwana Endres pia umetembelea katika kituo cha wasafiri kilichoanzishwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Kuhudumia wahamiaji IOM na la kuhudumia wakimbizi UNHCR ambapo Waafghanstani wanaorejea wamepiga kambi. Wakiwa kituoni hapo wanafanya tathmini za wanaorejea, mahitaji yao na jinsi bora ya kuwasaidia. “Watu wengi wanahitaji nyumba za kuishi. Na changamoto nikuwa mwezi uliopita kulikuwa na tetemeko kubwa la ardhi katika jimbo la Herat na mablangeti yote na vifaa vingine tulivyokuwa navyo hapa nchini Afghanistan tumevitumia kwa waathirika wa tetemeko. Hii ni changamoto tuliyonayo wakati huu katika kuwasaidia wananchi wanaorejea kutoka Pakistan na wanarejea kwa idadi kubwa. Ni muhimu sana kwanza tukipata suluhisho la muda mfupi. Watu hawa tuwape fedha taslimu, chakula na maji. Itakuwa changamoto kubwa Kwa wanawake na watoto.”Ndani ya kipindi cha miezi miwili Waafghani 327,000 wamerejea kutokea Pakistan na kati yao asilimia 45 ambao ni watu 148,000 wamewasilia kati ya tarehe mosi mpaka 11 mwezi huu wa Novemba wengi wao wakipitia katika jimbo la Nangarhar.
11/15/20230
Episode Artwork

Waafghanistan wanaorejea kutoka Pakistan wanahitaji msaada - UN

Tangu katikati ya mwezi Septemba mwaka huu kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wananchi wa Afghanistan wanaorejea nchini mwao wakitokea Pakistan ambako wamelazimika kuondoka kutokana na kutokuwa na vibali vya kuishi nchini humo. Ongezeko hilo kubwa la watu limeleta changamoto kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayotoa misaada ya kibinadamu. Wengi wa wananchi hawa wanaorejea Afghanistan wanawasili wakiwa na mali kidogo kwani nyumba na mali zao zote wameziacha nchini Pakistan na sasa wanafika mpakani wakiwa hawajui waende wapi wala mustakabali wa maisha yao. Kaimu Mratibu wa masuala ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Afghanistan Daniel Peter Endres, akimbatana na maafisa wengine wa mashirika ya Umoja wa Mataifa wamefanya ziara maalum jimboni Nangarhar na kuzungumza na wananchi hao. “Leo niko hapa katika eneo la Torkham mpakani na Pakistani kushuhudia maelfu ya Waafghanistan wakirejea. Wengi wa watu hawa wako katika hali mbaya sana, walisubiri siku kadhaa kabla ya kufika hapa. Nimezungumza na watu wengi, na wameniambia hawana nyumba hapa nchini Afghanistan na majira ya baridi yataanza ndani ya wiki chache zijazo.” Ujumbe unaoongozwa na Bwana Endres pia umetembelea katika kituo cha wasafiri kilichoanzishwa na mashirika ya Umoja wa Mataifa lile la Kuhudumia wahamiaji IOM na la kuhudumia wakimbizi UNHCR ambapo Waafghanstani wanaorejea wamepiga kambi. Wakiwa kituoni hapo wanafanya tathmini za wanaorejea, mahitaji yao na jinsi bora ya kuwasaidia. “Watu wengi wanahitaji nyumba za kuishi. Na changamoto nikuwa mwezi uliopita kulikuwa na tetemeko kubwa la ardhi katika jimbo la Herat na mablangeti yote na vifaa vingine tulivyokuwa navyo hapa nchini Afghanistan tumevitumia kwa waathirika wa tetemeko. Hii ni changamoto tuliyonayo wakati huu katika kuwasaidia wananchi wanaorejea kutoka Pakistan na wanarejea kwa idadi kubwa. Ni muhimu sana kwanza tukipata suluhisho la muda mfupi. Watu hawa tuwape fedha taslimu, chakula na maji. Itakuwa changamoto kubwa Kwa wanawake na watoto.”Ndani ya kipindi cha miezi miwili Waafghani 327,000 wamerejea kutokea Pakistan na kati yao asilimia 45 ambao ni watu 148,000 wamewasilia kati ya tarehe mosi mpaka 11 mwezi huu wa Novemba wengi wao wakipitia katika jimbo la Nangarhar.
11/15/20232 minutes, 25 seconds
Episode Artwork

15 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki za binadamu katika ukanda wa Gaza na wakimbizi wa Afghanistan wanaorejea nyumbani kutoka Pakistan. Makala tunaelekea nchini Kenya na Mashinani nchini Tanzania, kulikoni?   Umoja wa Mataifa leo umesisitiza kwa mara nyingine kwamba kinachoendelea Gaza ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu huku kukiwa na ripoti kwamba vikosi vya Israel vimevamia Hospitali ya Al-Shifa jana usiku ambako mbali ya wagonjwa kuna maelfu ya raia waliotawanywa wanapata hifadhi na umeonya kwamba hospital sio uwanja wa vita na madhila hayo kwa raia wakiwemo watoto lazima yakome kwa kutekeleza mambo 10 ya muhimu. Tangu katikati ya mwezi Septemba mwaka huu kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wananchi wa Afghanistan wanaorejea nchini mwao wakitokea Pakistan ambako wamelazimika kuondoka kutokana na kutokuwa na vibali vya kuishi nchini humo. Ongezeko hilo kubwa la watu limeleta changamoto kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayotoa misaada ya kibinadamu.Makala tunakupeleka nchini Kenya kuangazia mradi ambao unaungwa mkono na mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika la kimataifa la Triggerise linalotumia huduma ya simu inayofahamika kama Tiko kwa lengo kuu la kuunguza mimba za utotoni na maambuki ya VVU miongoni mwa wasichana wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 19. Evarist Mapesa anasimulia makala hii iliyoratibiwa na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Pamoja wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG).Mashinani tunaelekea Mkoani Kigoma-magharibi mwa Tanzania kumsikia ujumbe kutoka kwa mhudumu wa afya mkoani humo kuhusu kampeini ya chanjo ya polio awamu ya pili, lakini kwanza ni makala. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/15/20230
Episode Artwork

15 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki za binadamu katika ukanda wa Gaza na wakimbizi wa Afghanistan wanaorejea nyumbani kutoka Pakistan. Makala tunaelekea nchini Kenya na Mashinani nchini Tanzania, kulikoni?   Umoja wa Mataifa leo umesisitiza kwa mara nyingine kwamba kinachoendelea Gaza ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu huku kukiwa na ripoti kwamba vikosi vya Israel vimevamia Hospitali ya Al-Shifa jana usiku ambako mbali ya wagonjwa kuna maelfu ya raia waliotawanywa wanapata hifadhi na umeonya kwamba hospital sio uwanja wa vita na madhila hayo kwa raia wakiwemo watoto lazima yakome kwa kutekeleza mambo 10 ya muhimu. Tangu katikati ya mwezi Septemba mwaka huu kumekuwa na ongezeko kubwa la idadi ya wananchi wa Afghanistan wanaorejea nchini mwao wakitokea Pakistan ambako wamelazimika kuondoka kutokana na kutokuwa na vibali vya kuishi nchini humo. Ongezeko hilo kubwa la watu limeleta changamoto kwa mashirika ya Umoja wa Mataifa yanayotoa misaada ya kibinadamu.Makala tunakupeleka nchini Kenya kuangazia mradi ambao unaungwa mkono na mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa kupitia shirika la kimataifa la Triggerise linalotumia huduma ya simu inayofahamika kama Tiko kwa lengo kuu la kuunguza mimba za utotoni na maambuki ya VVU miongoni mwa wasichana wenye umri wa kati ya miaka 15 hadi 19. Evarist Mapesa anasimulia makala hii iliyoratibiwa na Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Pamoja wa Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDG).Mashinani tunaelekea Mkoani Kigoma-magharibi mwa Tanzania kumsikia ujumbe kutoka kwa mhudumu wa afya mkoani humo kuhusu kampeini ya chanjo ya polio awamu ya pili, lakini kwanza ni makala. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/15/202313 minutes, 37 seconds
Episode Artwork

Mambo 10 lazima yatekelezwe kuleta afueni katika ukanda wa Gaza: Griffiths

Umoja wa Mataifa leo umesisitiza kwa mara nyingine kwamba kinachoendelea Gaza ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu huku kukiwa na ripoti kwamba vikosi vya Israel vimevamia Hospitali ya Al-Shifa jana usiku ambako mbali ya wagonjwa kuna maelfu ya raia waliotawanywa wanapata hifadhi na umeonya kwamba hospital sio uwanja wa vita na madhila hayo kwa raia wakiwemo watoto lazima yakome kwa kutekeleza mambo 10 ya muhimu. Hali inaendelea kuwa janga kubwa la kibinadamu kwa watu wa Gaza kwa kumujibu wa mkuu wa masuala ya kibinadamu na msaada wa dharura wa Umoja wa Mataifa Martin Griffis ambaye kupitia tarifa yake iliyotolewa leo amesema “Wakati mauaji ya Gaza yakifikia viwango vipya vya kutisha kila siku, ulimwengu unaendelea kutazama kwa mshtuko huku hospitali zikiteketea, watoto wanaozaliwa njiti wanakufa, na watu wote wananyimwa njia za msingi za kujikimu. Hii haiwezi kuruhusiwa kuendelea.Pande zinazozozana lazima ziheshimu sheria za kimataifa za kibinadamu, zikubali kusitishwa kwa mapigano kwa minajili ya kibinadamu na kukomesha kabisa mapigano hayo.”Kwa niaba ya jumuiya ya kibinadamu anayowakilisha, Griffiths amehimiza pande zote, wale wote walio na ushawishi juu pande kinzani, na jumuiya pana ya kimataifa kufanya kila liwezalo kuunga mkono na kutekeleza mambo kumi yafuatayo;Mosi:  Kuwezesha juhudi za mashirika ya misaada kuwa na mtiririko endelevu wa misafara ya misaada na kufanya hivyo kwa njia ya usalama.Pili:  Kufungua sehemu za ziada za kuvuka kwa ajili ya misaada na malori ybiashara kuingia, ikiwa ni pamoja na Kerem Shalom.Tatu:  Kuruhusu Umoja wa Mataifa, mashirika mengine ya kibinadamu na mashirika ya umma na ya kibinafsi kupata mafuta kwa wingi wa kutosha ili kutoa misaada na kutoa huduma za msingi.Nnne:  Kuwezesha mashirika ya kibinadamu kutoa misaada kote Gaza bila vikwazo au kuingiliwa.Tano:  Kuruhusu kupanua wigo wa idadi ya makazi salama kwa watu waliohamishwa katika shule na vituo vingine vya umma kote Gaza na kuhakikisha kwamba wanasalia kuwa sehemu za usalama wakati wote wa vita.Sita: Kuboresha utaratibu wa taarifa za kibinadamu ambao ungesaidia kuwaepusha raia na miundombinu ya kiraia kutokana na uhasama na kusaidia kuwezesha ufikiaji wa kibinadamu.Saba: Kuruhusu kuweka vituo vya usambazaji wa misaada kwa raia, kulingana na mahitaji.Nane:  Kuruhusu raia kuhamia maeneo salama na kurudi kwa hiari katika makazi yao.Tisa:  Kufadhili ombi la misaada ya kibinadamu, ambalo sasa linafikia dola bilioni 1.2.Kumi: Tekeleza usitishaji mapigano wa kibinadamu ili kuruhusu huduma za msingi kuanza upya na biashara muhimu kuanza tena. Usitishaji huo wa mapigano pia ni muhimu kuwezesha utoaji wa misaada, kuruhusu kuachiliwa kwa mateka, na kutoa afueni kwa raia.Amehitimisha tarifa yake kwa kusema kwamba “Hivi ndivyo vitendo vinavyohitajika kudhibiti mauaji. Mpango huu ni wa kina, na tumedhamiria kusukuma kila hatua, lakini tunahitaji uungwaji mkono mkubwa wa kimataifa.D unia lazima ichukue hatua kabla haijachelewa.”
11/15/20230
Episode Artwork

Mambo 10 lazima yatekelezwe kuleta afueni katika ukanda wa Gaza: Griffiths

Umoja wa Mataifa leo umesisitiza kwa mara nyingine kwamba kinachoendelea Gaza ni ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu huku kukiwa na ripoti kwamba vikosi vya Israel vimevamia Hospitali ya Al-Shifa jana usiku ambako mbali ya wagonjwa kuna maelfu ya raia waliotawanywa wanapata hifadhi na umeonya kwamba hospital sio uwanja wa vita na madhila hayo kwa raia wakiwemo watoto lazima yakome kwa kutekeleza mambo 10 ya muhimu. Hali inaendelea kuwa janga kubwa la kibinadamu kwa watu wa Gaza kwa kumujibu wa mkuu wa masuala ya kibinadamu na msaada wa dharura wa Umoja wa Mataifa Martin Griffis ambaye kupitia tarifa yake iliyotolewa leo amesema “Wakati mauaji ya Gaza yakifikia viwango vipya vya kutisha kila siku, ulimwengu unaendelea kutazama kwa mshtuko huku hospitali zikiteketea, watoto wanaozaliwa njiti wanakufa, na watu wote wananyimwa njia za msingi za kujikimu. Hii haiwezi kuruhusiwa kuendelea.Pande zinazozozana lazima ziheshimu sheria za kimataifa za kibinadamu, zikubali kusitishwa kwa mapigano kwa minajili ya kibinadamu na kukomesha kabisa mapigano hayo.”Kwa niaba ya jumuiya ya kibinadamu anayowakilisha, Griffiths amehimiza pande zote, wale wote walio na ushawishi juu pande kinzani, na jumuiya pana ya kimataifa kufanya kila liwezalo kuunga mkono na kutekeleza mambo kumi yafuatayo;Mosi:  Kuwezesha juhudi za mashirika ya misaada kuwa na mtiririko endelevu wa misafara ya misaada na kufanya hivyo kwa njia ya usalama.Pili:  Kufungua sehemu za ziada za kuvuka kwa ajili ya misaada na malori ybiashara kuingia, ikiwa ni pamoja na Kerem Shalom.Tatu:  Kuruhusu Umoja wa Mataifa, mashirika mengine ya kibinadamu na mashirika ya umma na ya kibinafsi kupata mafuta kwa wingi wa kutosha ili kutoa misaada na kutoa huduma za msingi.Nnne:  Kuwezesha mashirika ya kibinadamu kutoa misaada kote Gaza bila vikwazo au kuingiliwa.Tano:  Kuruhusu kupanua wigo wa idadi ya makazi salama kwa watu waliohamishwa katika shule na vituo vingine vya umma kote Gaza na kuhakikisha kwamba wanasalia kuwa sehemu za usalama wakati wote wa vita.Sita: Kuboresha utaratibu wa taarifa za kibinadamu ambao ungesaidia kuwaepusha raia na miundombinu ya kiraia kutokana na uhasama na kusaidia kuwezesha ufikiaji wa kibinadamu.Saba: Kuruhusu kuweka vituo vya usambazaji wa misaada kwa raia, kulingana na mahitaji.Nane:  Kuruhusu raia kuhamia maeneo salama na kurudi kwa hiari katika makazi yao.Tisa:  Kufadhili ombi la misaada ya kibinadamu, ambalo sasa linafikia dola bilioni 1.2.Kumi: Tekeleza usitishaji mapigano wa kibinadamu ili kuruhusu huduma za msingi kuanza upya na biashara muhimu kuanza tena. Usitishaji huo wa mapigano pia ni muhimu kuwezesha utoaji wa misaada, kuruhusu kuachiliwa kwa mateka, na kutoa afueni kwa raia.Amehitimisha tarifa yake kwa kusema kwamba “Hivi ndivyo vitendo vinavyohitajika kudhibiti mauaji. Mpango huu ni wa kina, na tumedhamiria kusukuma kila hatua, lakini tunahitaji uungwaji mkono mkubwa wa kimataifa.D unia lazima ichukue hatua kabla haijachelewa.”
11/15/20233 minutes, 30 seconds
Episode Artwork

Mfumo wa afya Gaza umeelemewa - Mashirika

Licha ya mashambulizi dhidi ya vituo vya afya na makazi ya watu katika Ukanda wa Gaza, mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa yanaendelea kujitahidi usiku na mchana kuhakikisha watu wanapata huduma ya afya ili kuokoa maisha yao lakini ni wazi kwamba hali inazidi kuwa mbaya kila uchao. Anold Kayanda amefuatilia suala hili na kutuandalia mada hii kwa kina. 
11/14/20230
Episode Artwork

Mfumo wa afya Gaza umeelemewa - Mashirika

Licha ya mashambulizi dhidi ya vituo vya afya na makazi ya watu katika Ukanda wa Gaza, mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa yanaendelea kujitahidi usiku na mchana kuhakikisha watu wanapata huduma ya afya ili kuokoa maisha yao lakini ni wazi kwamba hali inazidi kuwa mbaya kila uchao. Anold Kayanda amefuatilia suala hili na kutuandalia mada hii kwa kina. 
11/14/20234 minutes, 2 seconds
Episode Artwork

14 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo licha ya mashambulizi dhidi ya vituo vya afya na makazi ya watu katika Ukanda wa Gaza, mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa yanaendelea kujitahidi usiku na mchana kuhakikisha watu wanapata huduma ya afya ili kuokoa maisha yao lakini ni wazi kwamba hali inazidi kuwa mbaya kila uchao. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.   Huko Gaza Mashariki ya Kati madhila kwa raia yanaendelea na leo shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limepongeza ujasiri wa juhudi za wahudumu wa afya katika hospitali ya Al-shifa  na kuelezea hofu yake kwa maelfu ya watu waliotawanywa na mgogoro unaoendelea kufuatia mvua kubwa zinazonyesha ambazo zimesababisha mafuriko na kufanya hali ya ya kibinadamu iliyokuwa mbaya kuwa mbaya zaidi. Nalo Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limeonya kuhusu ukosefu wa mafuta likisema sasa akiba yote imekwisha, malori yake hayawezi kufanya kazi na hivyo hayataweza kupokea msaada kutoka kivuko cha Rafah, nusu ya hospital zote Gaza hazifanyikazi kwa kukosa mafuta na 14 zinazoendelea kufanyakazi hazina mafuta ya kutosha na vifaa muhimu vinavyohitajika huku mawasiliano yakiendelea kuwa changamoto kubwa. Tukiendelea na madhila kwingineko nchini Sudan shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA limesema leo kwamba mlipuko mpya wa kipindupindu unaongeza shinikizo katika hali mbaya ya kibinadamu nchini humo.Na leo ni siku ya kisukari duniani  miaka 100 tangu kugunduliwa kwa ugonjwa huo shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO linasema takriban watu milioni 422 waliishi na kisukari mwaka 2014 na idadi ya wenye ugonjwa huo imeongezeka karibu mara mbili tangu mwaka 1980 kutoka asilimia 4.7 hadi asilimia 8.5. Na mashinani ikiwa leo ni Siku ya kutokomeza ugonjwa wa kisukari tutakuletea ujumbe wa WHO kuhusu matumizi ya sukari mbadala na madhara yake.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/14/20230
Episode Artwork

14 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo licha ya mashambulizi dhidi ya vituo vya afya na makazi ya watu katika Ukanda wa Gaza, mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa yanaendelea kujitahidi usiku na mchana kuhakikisha watu wanapata huduma ya afya ili kuokoa maisha yao lakini ni wazi kwamba hali inazidi kuwa mbaya kila uchao. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani.   Huko Gaza Mashariki ya Kati madhila kwa raia yanaendelea na leo shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limepongeza ujasiri wa juhudi za wahudumu wa afya katika hospitali ya Al-shifa  na kuelezea hofu yake kwa maelfu ya watu waliotawanywa na mgogoro unaoendelea kufuatia mvua kubwa zinazonyesha ambazo zimesababisha mafuriko na kufanya hali ya ya kibinadamu iliyokuwa mbaya kuwa mbaya zaidi. Nalo Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limeonya kuhusu ukosefu wa mafuta likisema sasa akiba yote imekwisha, malori yake hayawezi kufanya kazi na hivyo hayataweza kupokea msaada kutoka kivuko cha Rafah, nusu ya hospital zote Gaza hazifanyikazi kwa kukosa mafuta na 14 zinazoendelea kufanyakazi hazina mafuta ya kutosha na vifaa muhimu vinavyohitajika huku mawasiliano yakiendelea kuwa changamoto kubwa. Tukiendelea na madhila kwingineko nchini Sudan shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA limesema leo kwamba mlipuko mpya wa kipindupindu unaongeza shinikizo katika hali mbaya ya kibinadamu nchini humo.Na leo ni siku ya kisukari duniani  miaka 100 tangu kugunduliwa kwa ugonjwa huo shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO linasema takriban watu milioni 422 waliishi na kisukari mwaka 2014 na idadi ya wenye ugonjwa huo imeongezeka karibu mara mbili tangu mwaka 1980 kutoka asilimia 4.7 hadi asilimia 8.5. Na mashinani ikiwa leo ni Siku ya kutokomeza ugonjwa wa kisukari tutakuletea ujumbe wa WHO kuhusu matumizi ya sukari mbadala na madhara yake.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/14/202310 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

Huduma za afya Al-Shifa zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa rasilimali - WHO

Tangu October 7,2023 mzozo unaoendelea nchini Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas umesababisha idadi kubwa ya vifo na majeraha kwa raia na wafanyakazi zaidi ya 100 wa Umoja wa Mataifa. katika ukanda wa Gaza mashambulizi ya anga na ukosefu wa vifaa vya matibabu, chakula, maji na mafuta vimeathiri mfumo wa huduma za afya ambao tayari unakabiliwa na upungufu mkubwa wa rasilimali. Hospitali zimekuwa zikifanya kazi zaidi ya uwezo wake kutokana na ongezeko la idadi ya wagonjwa pamoja na raia waliokimbia makazi yao, utoaji wa huduma muhimu kwa mama na mtoto hadi matibabu ya magonjwa sugu umeathiriwa Vibaya.  Tuungane na Evarist Mapesa katika makala hii akiangazia mfumo wa afya.
11/13/20230
Episode Artwork

Huduma za afya Al-Shifa zinakabiliwa na upungufu mkubwa wa rasilimali - WHO

Tangu October 7,2023 mzozo unaoendelea nchini Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas umesababisha idadi kubwa ya vifo na majeraha kwa raia na wafanyakazi zaidi ya 100 wa Umoja wa Mataifa. katika ukanda wa Gaza mashambulizi ya anga na ukosefu wa vifaa vya matibabu, chakula, maji na mafuta vimeathiri mfumo wa huduma za afya ambao tayari unakabiliwa na upungufu mkubwa wa rasilimali. Hospitali zimekuwa zikifanya kazi zaidi ya uwezo wake kutokana na ongezeko la idadi ya wagonjwa pamoja na raia waliokimbia makazi yao, utoaji wa huduma muhimu kwa mama na mtoto hadi matibabu ya magonjwa sugu umeathiriwa Vibaya.  Tuungane na Evarist Mapesa katika makala hii akiangazia mfumo wa afya.
11/13/20233 minutes, 39 seconds
Episode Artwork

13 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangaia hali ya kibinadamu kwa wagonjwa na waliojeruhiwa katika hospital ya Al-Shifa Gaza, na ripoti ya UNICEF kuhusu upatikanaji wa maji safi na salama kwa watoto. Makala tunasalia huko huko Gaza na masshinani tunakupeleka nchini Nigeria, kulikoni?    Hali hatika hospitali za Gaza ni mbayá sana wagonjwa wakiendelea kupoteza maisha wakiwemo watoto njiti katika hospitali ya Al-Shifa ambayo kwa siku ya tatu mfululizo hakuna umeme huku mashambulizi ya Israel yakiongezeka, umesema Umoja wa Mataifa ambao leo unawaomboleza pia wafanyakazi wake 101 waliopoteza maisha katika mzozo huo na kusisitiza kwamba usitishwaji uhasama ni lazima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Mtoto mmoja kati ya Watoto watatu au saw ana watoto milioni 739 duniani kote - tayari wanaishi katika maeneo yaliyo na uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji, na mabadiliko ya tabianchi yanatishia kufanya hali hii kuwa mbaya zaidi, imebainisha ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF iliyotolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu kwa saa za New York, Marekani. Makala leo inaturejesha Gaza kuangazia changamoto za mfumo wa afya ambazo zinaweka rehani maisha ya mamilioni ya raia wa Gaza wakiwemo kina mama wajawazito na watoto. Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa mfumo wa afya Gaza karibu unasambaratika kabisa huku huduma muhimu za wagonjwa mahtuti, magonjwa sugu na hata za kujifungua imekuwa mtihani.Na mashinani tunakupeleka jimboni Sokoto nchini Nigeria tumsikilize Rasheeda, mama yake mtoto Nana ambaye ndani ya miezi miwili ameweza kutibiwa utapiamlo mkali ambao uligunduliwa na afisa afya wa mashinani anayefanya kazi chini ya programu zinazofadhiliwa na shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya watoto UNICEF.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/13/20230
Episode Artwork

13 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangaia hali ya kibinadamu kwa wagonjwa na waliojeruhiwa katika hospital ya Al-Shifa Gaza, na ripoti ya UNICEF kuhusu upatikanaji wa maji safi na salama kwa watoto. Makala tunasalia huko huko Gaza na masshinani tunakupeleka nchini Nigeria, kulikoni?    Hali hatika hospitali za Gaza ni mbayá sana wagonjwa wakiendelea kupoteza maisha wakiwemo watoto njiti katika hospitali ya Al-Shifa ambayo kwa siku ya tatu mfululizo hakuna umeme huku mashambulizi ya Israel yakiongezeka, umesema Umoja wa Mataifa ambao leo unawaomboleza pia wafanyakazi wake 101 waliopoteza maisha katika mzozo huo na kusisitiza kwamba usitishwaji uhasama ni lazima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Mtoto mmoja kati ya Watoto watatu au saw ana watoto milioni 739 duniani kote - tayari wanaishi katika maeneo yaliyo na uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji, na mabadiliko ya tabianchi yanatishia kufanya hali hii kuwa mbaya zaidi, imebainisha ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF iliyotolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu kwa saa za New York, Marekani. Makala leo inaturejesha Gaza kuangazia changamoto za mfumo wa afya ambazo zinaweka rehani maisha ya mamilioni ya raia wa Gaza wakiwemo kina mama wajawazito na watoto. Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa mfumo wa afya Gaza karibu unasambaratika kabisa huku huduma muhimu za wagonjwa mahtuti, magonjwa sugu na hata za kujifungua imekuwa mtihani.Na mashinani tunakupeleka jimboni Sokoto nchini Nigeria tumsikilize Rasheeda, mama yake mtoto Nana ambaye ndani ya miezi miwili ameweza kutibiwa utapiamlo mkali ambao uligunduliwa na afisa afya wa mashinani anayefanya kazi chini ya programu zinazofadhiliwa na shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya watoto UNICEF.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
11/13/202311 minutes, 19 seconds
Episode Artwork

Mtoto 1 kati ya 3 anakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji - UNICEF

Mtoto mmoja kati ya Watoto watatu au saw ana watoto milioni 739 duniani kote - tayari wanaishi katika maeneo yaliyo na uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji, na mabadiliko ya tabianchi yanatishia kufanya hali hii kuwa mbaya zaidi, imebainisha ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF iliyotolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu kwa saa za New York, Marekani. Ripoti hii iliyotolewa kabla ya mkutano wa kilele wa mabadiliko ya tabianchi wa COP28 unaoanza mwishoni mwa mwezi huu huko Falme za Kiarabu UAE, inaangazia tishio kwa watoto kutokana na mazingira magumu ya upatikanaji maji, mojawapo ya njia ambazo athari za mabadiliko ya tabianchi zinaonekana. Inatoa uchanganuzi wa athari za viwango vitatu vya uhakika wa maji duniani kote - uhaba wa maji, mazingira magumu upatikanaji wa maji, na shinikizo la maji.Ripoti hiyo, nyongeza ya ripoti nyingine ya UNICEF ya mwaka 2021 yenye jina Hatari ya Tabianchi kwa Watoto, pia inaeleza maelfu ya njia nyingine ambazo watoto hubeba mzigo mkubwa wa athari za janga la tabianchi ikiwa ni pamoja na magonjwa, uchafuzi wa hewa, na matukio mabaya ya tabianchi kama vile mafuriko na ukame. Kuanzia wakati wa kutungwa mimba hadi wanapokuwa watu wazima, afya na ukuaji wa akili za watoto, mapafu, mfumo wa kinga na kazi nyingine muhimu huathiriwa na mazingira wanayokulia. Kwa mfano, watoto wana uwezekano mkubwa wa kuteseka kutokana na uchafuzi wa hewa kuliko watu wazima. Kwa ujumla, wanapumua haraka kuliko watu wazima na ubongo wao, mapafu na viungo vingine bado vinakua."Matokeo ya mabadiliko ya tabianchi ni mabaya kwa watoto," Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF Catherine Russell anasema na kuongeza kuwa "Miili na akili zao ziko katika hatari ya kipekee kwa hewa chafuzi, lishe duni na joto kali. Sio tu kwamba ulimwengu wao unabadilika - vyanzo vya maji vikikauka na matukio ya tabianchi ya kuogofya yanakuwa yenye nguvu na ya mara kwa mara - hali kadhalika ustawi wao kwani mabadiliko ya tabianchi huathiri afya yao ya kiakili na kimwili. Watoto wanadai mabadiliko, lakini mahitaji yao mara nyingi sana yanawekwa kando.”Kulingana na matokeo ya ripoti hiyo, sehemu kubwa zaidi ya watoto wako katika maeneo ya Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini na Asia Kusini - ikimaanisha wanaishi katika maeneo yenye rasilimali chache za maji na viwango vya juu vya kutofautiana kwa msimu na mwaka, kupungua kwa maji ya ardhini au hatari ya ukame.Watoto wengi sana - milioni 436 - wanakabiliwa na mzigo maradufu wa uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji na viwango vya chini au vya chini sana vya huduma ya maji ya kunywa - inayojulikana kama mazingira magumu sana ya maji - na kuacha maisha yao, afya, na ustawi wao katika hatari. Ni mojawapo ya vichochezi muhimu vya vifo miongoni mwa watoto chini ya miaka mitano kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuilika.Ripoti hiyo inaonesha kwamba walioathirika zaidi wanaishi katika nchi za kipato cha chini na cha kati katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Asia ya Kati na Kusini, na Mashariki na Kusini-Mashariki mwa Asia. Mnamo mwaka 2022, watoto milioni 436 walikuwa wakiishi katika maeneo yanayokabiliwa na hatari kubwa ya maji. Baadhi ya nchi zilizoathiriwa zaidi ni pamoja na Niger, Jordan, Burkina Faso, Yemen, Chad, na Namibia, ambapo watoto 8 kati ya 10 wako kwenye hatari.Katika mazingira haya, uwekezaji katika huduma za maji safi ya kunywa na usafi wa mazingira ni njia muhimu ya kwanza ya ulinzi kuwalinda watoto dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi. Mabadiliko ya tabianchi pia yanasababisha kuongezeka kwa msongo wa maji - uwiano wa mahitaji ya maji hadi uwepo wa usambazaji endelevu, ripoti inaonya. Ifikapo mwaka 2050, watoto milioni 35 zaidi wanatarajiwa kukabiliwa na viwango vya juu au vya juu sana vya msongo wa maji, huku Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, na Asia Kusini kwa sasa zikikabiliwa na mabadiliko makubwa zaidi.Licha ya udhaifu wao wa kipekee, watoto wamepuuzwa au kupuuzwa kwa kiasi kikubwa katika…
11/13/20230
Episode Artwork

Mtoto 1 kati ya 3 anakabiliwa na uhaba mkubwa wa maji - UNICEF

Mtoto mmoja kati ya Watoto watatu au saw ana watoto milioni 739 duniani kote - tayari wanaishi katika maeneo yaliyo na uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji, na mabadiliko ya tabianchi yanatishia kufanya hali hii kuwa mbaya zaidi, imebainisha ripoti mpya ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF iliyotolewa usiku wa kuamkia leo Jumatatu kwa saa za New York, Marekani. Ripoti hii iliyotolewa kabla ya mkutano wa kilele wa mabadiliko ya tabianchi wa COP28 unaoanza mwishoni mwa mwezi huu huko Falme za Kiarabu UAE, inaangazia tishio kwa watoto kutokana na mazingira magumu ya upatikanaji maji, mojawapo ya njia ambazo athari za mabadiliko ya tabianchi zinaonekana. Inatoa uchanganuzi wa athari za viwango vitatu vya uhakika wa maji duniani kote - uhaba wa maji, mazingira magumu upatikanaji wa maji, na shinikizo la maji.Ripoti hiyo, nyongeza ya ripoti nyingine ya UNICEF ya mwaka 2021 yenye jina Hatari ya Tabianchi kwa Watoto, pia inaeleza maelfu ya njia nyingine ambazo watoto hubeba mzigo mkubwa wa athari za janga la tabianchi ikiwa ni pamoja na magonjwa, uchafuzi wa hewa, na matukio mabaya ya tabianchi kama vile mafuriko na ukame. Kuanzia wakati wa kutungwa mimba hadi wanapokuwa watu wazima, afya na ukuaji wa akili za watoto, mapafu, mfumo wa kinga na kazi nyingine muhimu huathiriwa na mazingira wanayokulia. Kwa mfano, watoto wana uwezekano mkubwa wa kuteseka kutokana na uchafuzi wa hewa kuliko watu wazima. Kwa ujumla, wanapumua haraka kuliko watu wazima na ubongo wao, mapafu na viungo vingine bado vinakua."Matokeo ya mabadiliko ya tabianchi ni mabaya kwa watoto," Mkurugenzi Mtendaji wa UNICEF Catherine Russell anasema na kuongeza kuwa "Miili na akili zao ziko katika hatari ya kipekee kwa hewa chafuzi, lishe duni na joto kali. Sio tu kwamba ulimwengu wao unabadilika - vyanzo vya maji vikikauka na matukio ya tabianchi ya kuogofya yanakuwa yenye nguvu na ya mara kwa mara - hali kadhalika ustawi wao kwani mabadiliko ya tabianchi huathiri afya yao ya kiakili na kimwili. Watoto wanadai mabadiliko, lakini mahitaji yao mara nyingi sana yanawekwa kando.”Kulingana na matokeo ya ripoti hiyo, sehemu kubwa zaidi ya watoto wako katika maeneo ya Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini na Asia Kusini - ikimaanisha wanaishi katika maeneo yenye rasilimali chache za maji na viwango vya juu vya kutofautiana kwa msimu na mwaka, kupungua kwa maji ya ardhini au hatari ya ukame.Watoto wengi sana - milioni 436 - wanakabiliwa na mzigo maradufu wa uhaba mkubwa au wa juu sana wa maji na viwango vya chini au vya chini sana vya huduma ya maji ya kunywa - inayojulikana kama mazingira magumu sana ya maji - na kuacha maisha yao, afya, na ustawi wao katika hatari. Ni mojawapo ya vichochezi muhimu vya vifo miongoni mwa watoto chini ya miaka mitano kutokana na magonjwa yanayoweza kuzuilika.Ripoti hiyo inaonesha kwamba walioathirika zaidi wanaishi katika nchi za kipato cha chini na cha kati katika Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara, Asia ya Kati na Kusini, na Mashariki na Kusini-Mashariki mwa Asia. Mnamo mwaka 2022, watoto milioni 436 walikuwa wakiishi katika maeneo yanayokabiliwa na hatari kubwa ya maji. Baadhi ya nchi zilizoathiriwa zaidi ni pamoja na Niger, Jordan, Burkina Faso, Yemen, Chad, na Namibia, ambapo watoto 8 kati ya 10 wako kwenye hatari.Katika mazingira haya, uwekezaji katika huduma za maji safi ya kunywa na usafi wa mazingira ni njia muhimu ya kwanza ya ulinzi kuwalinda watoto dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi. Mabadiliko ya tabianchi pia yanasababisha kuongezeka kwa msongo wa maji - uwiano wa mahitaji ya maji hadi uwepo wa usambazaji endelevu, ripoti inaonya. Ifikapo mwaka 2050, watoto milioni 35 zaidi wanatarajiwa kukabiliwa na viwango vya juu au vya juu sana vya msongo wa maji, huku Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini, na Asia Kusini kwa sasa zikikabiliwa na mabadiliko makubwa zaidi.Licha ya udhaifu wao wa kipekee, watoto wamepuuzwa au kupuuzwa kwa kiasi kikubwa katika…
11/13/20231 minute, 49 seconds
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa yaonya maisha ya watoto yanaendelea kupotea Gaza huku hali ya kukata tamaa ikitawala

Hali hatika hospitali za Gaza ni mbayá sana wagonjwa wakiendelea kupoteza maisha wakiwemo watoto njiti katika hospitali ya Al-Shifa ambayo kwa siku ya tatu mfululizo hakuna umeme huku mashambulizi ya Israel yakiongezeka, umesema Umoja wa Mataifa ambao leo unawaomboleza pia wafanyakazi wake 101 waliopoteza maisha katika mzozo huo na kusisitiza kwamba usitishwaji uhasama ni lazima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Asante Leah mashirika yote ya Umoja wa Mataifa yaliyotoa tarifa leo yamerejea wito wa kusitisha machafuko kwani hali inazidi kuwa mbaya zaidi kila uchao, lile la afya duniani WHO limesema watoto sita sita wamefariki dunia leo katika hospitali ya Al-shifa na wengine 37 njiti walilazimika kuhamishiwa katika chumba cha upasuaji mwishoni mwa wiki bila machine zao za kuwapasha joto wakati wahudumu wa afya wakihaha kupasha chumba joto kutokana na ukosefu wa umeme. Mkurugenzi mkuu wa WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus amesisitiza kwamba “Dunia haiwezi kunyamaza kimya wakati hospitali ambazo zinapaswa kuwa mahala salama zimegeuzwa kuwa vituo vya vifo, madhila na kukata tamaa” akirejea wito wa kusitisha uhasama mara moja.Hadi sasa Umoja wa Mataifa unasema zaidi ya watu 11,000 wamepoteza Maisha Gaza tangu kuanza kwa mzozo wakiwemo wafanyakazi 101 wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA ambao leo wanaombolezwa katika ofisi zote za Umoja wa Mataifa duniani kwa bendera kupepea nusu mlingoti ikiwemo hapa makao makuu jijini New York Marekani.Wakuu wa mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa wametoa kauli zao akiwemo mkuu wa shirika la kuhudumia Watoto UNICEF Cindy McCain ambaye amesema “Leo tunaungana na jumuiya ya kimataifa katika wakati wa ukimya kuwakumbuka na kuwaeznzi wafanyakazi wenzetu waliouawa huko Gaza” naye mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa Geneva Tatiana Valovaya amewashukuru wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa huko Gaza kwa kujitolea kwao akiainisha umuhimu wa kazi yao wakati huu mshikamano wa kimataifa ukiwa katika tishio kubwa.Gaza kwa mujibu wa kamishina mkuu wa UNRWA Philippe Lazzarini mashambulizi yanaendelea na leo nyumba ya wageni ya UNRWA iliyoko Rafah imeharibiwa na kombora ingawa hakuna aliyejeruhiwa.Amesema hii inadhihirisha jinsi gani sheria za kimataifa zinavyokiukwa kwa kutojali “ulinzi wa raia, miundombinu yao ikiwemo vifaa vya Umoja wa Mataifa, shule, hospitali, makambi ya wakimbizi na maeneo ya kuabudu.”
11/13/20230
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa yaonya maisha ya watoto yanaendelea kupotea Gaza huku hali ya kukata tamaa ikitawala

Hali hatika hospitali za Gaza ni mbayá sana wagonjwa wakiendelea kupoteza maisha wakiwemo watoto njiti katika hospitali ya Al-Shifa ambayo kwa siku ya tatu mfululizo hakuna umeme huku mashambulizi ya Israel yakiongezeka, umesema Umoja wa Mataifa ambao leo unawaomboleza pia wafanyakazi wake 101 waliopoteza maisha katika mzozo huo na kusisitiza kwamba usitishwaji uhasama ni lazima sasa kuliko wakati mwingine wowote. Asante Leah mashirika yote ya Umoja wa Mataifa yaliyotoa tarifa leo yamerejea wito wa kusitisha machafuko kwani hali inazidi kuwa mbaya zaidi kila uchao, lile la afya duniani WHO limesema watoto sita sita wamefariki dunia leo katika hospitali ya Al-shifa na wengine 37 njiti walilazimika kuhamishiwa katika chumba cha upasuaji mwishoni mwa wiki bila machine zao za kuwapasha joto wakati wahudumu wa afya wakihaha kupasha chumba joto kutokana na ukosefu wa umeme. Mkurugenzi mkuu wa WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus amesisitiza kwamba “Dunia haiwezi kunyamaza kimya wakati hospitali ambazo zinapaswa kuwa mahala salama zimegeuzwa kuwa vituo vya vifo, madhila na kukata tamaa” akirejea wito wa kusitisha uhasama mara moja.Hadi sasa Umoja wa Mataifa unasema zaidi ya watu 11,000 wamepoteza Maisha Gaza tangu kuanza kwa mzozo wakiwemo wafanyakazi 101 wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA ambao leo wanaombolezwa katika ofisi zote za Umoja wa Mataifa duniani kwa bendera kupepea nusu mlingoti ikiwemo hapa makao makuu jijini New York Marekani.Wakuu wa mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa wametoa kauli zao akiwemo mkuu wa shirika la kuhudumia Watoto UNICEF Cindy McCain ambaye amesema “Leo tunaungana na jumuiya ya kimataifa katika wakati wa ukimya kuwakumbuka na kuwaeznzi wafanyakazi wenzetu waliouawa huko Gaza” naye mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa Geneva Tatiana Valovaya amewashukuru wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa huko Gaza kwa kujitolea kwao akiainisha umuhimu wa kazi yao wakati huu mshikamano wa kimataifa ukiwa katika tishio kubwa.Gaza kwa mujibu wa kamishina mkuu wa UNRWA Philippe Lazzarini mashambulizi yanaendelea na leo nyumba ya wageni ya UNRWA iliyoko Rafah imeharibiwa na kombora ingawa hakuna aliyejeruhiwa.Amesema hii inadhihirisha jinsi gani sheria za kimataifa zinavyokiukwa kwa kutojali “ulinzi wa raia, miundombinu yao ikiwemo vifaa vya Umoja wa Mataifa, shule, hospitali, makambi ya wakimbizi na maeneo ya kuabudu.”
11/13/20232 minutes, 36 seconds
Episode Artwork

10 NOVEMBA 2023

Ungana na Leah Mushi kusikia haya jaridani hii leo:Hofu ya uhalifu wa vita ikitanda UN yataka jinamizi linaloghubika Gaza liishe.UNMISS yawajengea wanajeshi wa Sudan Kusini uwezo kulinda haki za watoto.UNCDF na EU katika harakati za kuwakwamua wananchi Gambia dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.Na mashinani msichana ambaye ni mkimbizi wa ndani nchini Sudan.
11/10/20230
Episode Artwork

10 NOVEMBA 2023

Ungana na Leah Mushi kusikia haya jaridani hii leo:Hofu ya uhalifu wa vita ikitanda UN yataka jinamizi linaloghubika Gaza liishe.UNMISS yawajengea wanajeshi wa Sudan Kusini uwezo kulinda haki za watoto.UNCDF na EU katika harakati za kuwakwamua wananchi Gambia dhidi ya mabadiliko ya tabianchi.Na mashinani msichana ambaye ni mkimbizi wa ndani nchini Sudan.
11/10/202313 minutes, 7 seconds
Episode Artwork

09 NOVEMBA 2023

Hii leo Jaridani Evarist Mapesa anakuletea mada kwa akina inayoangazia kazi za majumbani na utasikia kisa cha mtoto wa miaka 11 kutoka nchini Tanzania ambaye akiwa na miaka 10 alikuwa akitumikishwa pamoja na madhila mengine aliyokumbana nayo. Pia utasikia habari kwa ufupi zikiangazia masuala ya kibinadamu kwa wananchi wa Gaza na masuala ya mazingira. Na leo katika kujifunza Kiswahili utasikia ufafananuzi wa methali Umekuwa bata akili kwa watoto. Msomaji wako ni Leah Mushi.
11/9/20230
Episode Artwork

09 NOVEMBA 2023

Hii leo Jaridani Evarist Mapesa anakuletea mada kwa akina inayoangazia kazi za majumbani na utasikia kisa cha mtoto wa miaka 11 kutoka nchini Tanzania ambaye akiwa na miaka 10 alikuwa akitumikishwa pamoja na madhila mengine aliyokumbana nayo. Pia utasikia habari kwa ufupi zikiangazia masuala ya kibinadamu kwa wananchi wa Gaza na masuala ya mazingira. Na leo katika kujifunza Kiswahili utasikia ufafananuzi wa methali Umekuwa bata akili kwa watoto. Msomaji wako ni Leah Mushi.
11/9/202311 minutes, 36 seconds
Episode Artwork

Gaza hali ni tete lazima misaada zaidi ipelekwe: WFP

Hali kwa raia walioko Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati inazidi kuwa mbayá kila uchao hasa kutokana na kuendelea kwa operesheni za kijeshi za Israel za agani na ardhini zilizosababisha maelfu ya raia kuendelea kutaabika kwa kukosa mahitaji muhimu ya msingi kama chakula, maji, huduma za afya na mawasiliano limesema shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hili ni ambalo ni moja wa wasambazaji wakubwa wa chakula cha msaada sasa wanahaha kuhakikisha malori zaidi yaliyosheheni chakula na maji yanaingia Gaza kupitia mpaka pekee ulio wazi wa Rafah baina ya Gaza na Misri. Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo amefunga safari hadi Rafah kushuhudia hali halisi. Tuungane na Flora Nducha katika makala hii inayoangazia ziara hiyo. 
11/8/20230
Episode Artwork

Gaza hali ni tete lazima misaada zaidi ipelekwe: WFP

Hali kwa raia walioko Ukanda wa Gaza Mashariki ya Kati inazidi kuwa mbayá kila uchao hasa kutokana na kuendelea kwa operesheni za kijeshi za Israel za agani na ardhini zilizosababisha maelfu ya raia kuendelea kutaabika kwa kukosa mahitaji muhimu ya msingi kama chakula, maji, huduma za afya na mawasiliano limesema shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP. Shirika hili ni ambalo ni moja wa wasambazaji wakubwa wa chakula cha msaada sasa wanahaha kuhakikisha malori zaidi yaliyosheheni chakula na maji yanaingia Gaza kupitia mpaka pekee ulio wazi wa Rafah baina ya Gaza na Misri. Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo amefunga safari hadi Rafah kushuhudia hali halisi. Tuungane na Flora Nducha katika makala hii inayoangazia ziara hiyo. 
11/8/20234 minutes, 10 seconds
Episode Artwork

Harakati za kujumuisha wanawake kwenye siasa Somalia zaendelea

Catriona Laing, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia amethibitisha kuwa Umoja wa Mataifa unashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Maendeleo ya Wanawake na Haki za Binadamu nchini humo kuhakikisha kwamba sauti za wanawake zinasikika katika Baraza la Ushauri la Taifa (NCC) ambalo kwa sasa linaundwa na wanaume pekee akiwemo Rais wa shirikisho, marais wa majimbo na viongozi wengine wanaume wa ngazi ya juu ya uongozi.Aidha kiongozi mwakilishi hiyo wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia ametoa wito wa kutumia mapitio ya katiba yanayoendelea kuhamasisha kupitishwa kisheria kwa asilimia 30 ya mgawo wa wanawake katika Bunge la kitaifa, "Kuhusu asilimia 30, hii lazima iwekwe kisheria. Ni vyema kuwa na dhamira, lakini bila dhamira kisheria, tunajua kutokana na uzoefu katika nchi nyingine kwamba ni vigumu sana kusonga mbele. Nchi barani Afrika ambazo zimefanya vyema zaidi zimefanya nafasi hizi za viti maalumu kulindwa na sheria.”
11/8/20230
Episode Artwork

Harakati za kujumuisha wanawake kwenye siasa Somalia zaendelea

Catriona Laing, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia amethibitisha kuwa Umoja wa Mataifa unashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Maendeleo ya Wanawake na Haki za Binadamu nchini humo kuhakikisha kwamba sauti za wanawake zinasikika katika Baraza la Ushauri la Taifa (NCC) ambalo kwa sasa linaundwa na wanaume pekee akiwemo Rais wa shirikisho, marais wa majimbo na viongozi wengine wanaume wa ngazi ya juu ya uongozi.Aidha kiongozi mwakilishi hiyo wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia ametoa wito wa kutumia mapitio ya katiba yanayoendelea kuhamasisha kupitishwa kisheria kwa asilimia 30 ya mgawo wa wanawake katika Bunge la kitaifa, "Kuhusu asilimia 30, hii lazima iwekwe kisheria. Ni vyema kuwa na dhamira, lakini bila dhamira kisheria, tunajua kutokana na uzoefu katika nchi nyingine kwamba ni vigumu sana kusonga mbele. Nchi barani Afrika ambazo zimefanya vyema zaidi zimefanya nafasi hizi za viti maalumu kulindwa na sheria.”
11/8/20231 minute, 17 seconds
Episode Artwork

Machungu ya El Nino kuendelea hadi Aprili 2024 kaskazini na kusini mwa dunia

Tukio la mkondo joto la El Niño linalosababisha hivi sasa mvua kubwa, joto kali na ukame kwenye maeneo mbalimbali ya dunia, linatarajiwa kuendelea duniani na kuchochea ongezeko la kiwango cha joto baharini na ardhini, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa, WMO hii leo. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Taarifa ya WMO iliyotolewa leo mjini Geneva, Uswisi inaainisha kuwa El Nino ni mwenendo wa tabianchi unaoambatana na maji ya baharí kuwa ya joto kuliko kawaida kwenye maeneo ya mashariki mwa bahari ya Pasifiki na kusambaa maeneo mengine ya dunia.Hivyo WMO inasema El Nino ilishika kasi mwezi Julai hadi Agosti na kuimarika mwezi Septemba, na kuna uwezekano ikawa na matukio makubwa zaidi mwezi huu wa Novemba  hadi Januari 2024.WMO inasema kuna uwezekano wa asilimia 90 kwa El Nino kuendelea kipindi chote cha majira ya baridi kwenye eneo la kaskazini mwa dunia, halikadhalika kipindi cha majira ya joto kwa eneo la kusini mwa dunia.Katibu Mkuu wa WMO Profesa Petteri Taalas anasema kutokana na mwenendo huu, matukio ya kupindukia ya joto kali, ukame, mioto ya nyika, mvua kubwa na mafuriko vinaweza kuimarika kwenye baadhi ya maeneo na kuleta madhara makubwa.Amesema ndio maana WMO inasisitiza mpango wa Utoaji Onyo kwa Haraka kwa Wote ili kuokoa maisha na kupunguza hasara za kiuchumi.Maeneo ambayo yanadokezwa kuwa yatakuwa na mvua kubwa kutokana na El Niño, ni pamoja na Pembe ya Afrika, bonde la Parana Amerika ya Kusini.Mwaka uliotangulia na kuweka rekodi ya kuwa na joto zai kutokana na El Nino ambayo haikuwa ya kawaida ni 2016.          
11/8/20230
Episode Artwork

Machungu ya El Nino kuendelea hadi Aprili 2024 kaskazini na kusini mwa dunia

Tukio la mkondo joto la El Niño linalosababisha hivi sasa mvua kubwa, joto kali na ukame kwenye maeneo mbalimbali ya dunia, linatarajiwa kuendelea duniani na kuchochea ongezeko la kiwango cha joto baharini na ardhini, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa, WMO hii leo. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Taarifa ya WMO iliyotolewa leo mjini Geneva, Uswisi inaainisha kuwa El Nino ni mwenendo wa tabianchi unaoambatana na maji ya baharí kuwa ya joto kuliko kawaida kwenye maeneo ya mashariki mwa bahari ya Pasifiki na kusambaa maeneo mengine ya dunia.Hivyo WMO inasema El Nino ilishika kasi mwezi Julai hadi Agosti na kuimarika mwezi Septemba, na kuna uwezekano ikawa na matukio makubwa zaidi mwezi huu wa Novemba  hadi Januari 2024.WMO inasema kuna uwezekano wa asilimia 90 kwa El Nino kuendelea kipindi chote cha majira ya baridi kwenye eneo la kaskazini mwa dunia, halikadhalika kipindi cha majira ya joto kwa eneo la kusini mwa dunia.Katibu Mkuu wa WMO Profesa Petteri Taalas anasema kutokana na mwenendo huu, matukio ya kupindukia ya joto kali, ukame, mioto ya nyika, mvua kubwa na mafuriko vinaweza kuimarika kwenye baadhi ya maeneo na kuleta madhara makubwa.Amesema ndio maana WMO inasisitiza mpango wa Utoaji Onyo kwa Haraka kwa Wote ili kuokoa maisha na kupunguza hasara za kiuchumi.Maeneo ambayo yanadokezwa kuwa yatakuwa na mvua kubwa kutokana na El Niño, ni pamoja na Pembe ya Afrika, bonde la Parana Amerika ya Kusini.Mwaka uliotangulia na kuweka rekodi ya kuwa na joto zai kutokana na El Nino ambayo haikuwa ya kawaida ni 2016.          
11/8/20231 minute, 38 seconds
Episode Artwork

08 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Assumpta Massoi anamulika mwelekeo wa El Nino ya kwamba itaendelea hadi Aprili 2024,  halikadhalika madhara  yake, Somalia kulekea uchaguzi mkuu na ushiriki wa wanawake; Makala inabisha hodi Mashariki ya Kati usaidizi wa kibinadamu huko Gaza, na mashinani inabisha hodi Armenia.Tukio la mkondo joto la El Niño linalosababisha hivi sasa mvua kubwa, joto kali na ukame kwenye maeneo mbalimbali ya dunia, linatarajiwa kuendelea duniani na kuchochea ongezeko la kiwango cha joto baharini na ardhini, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa, WMO hii leo. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Catriona Laing, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia amethibitisha kuwa Umoja wa Mataifa unashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Maendeleo ya Wanawake na Haki za Binadamu nchini humo kuhakikisha kwamba sauti za wanawake zinasikika katika Baraza la Ushauri la Taifa (NCC) ambalo kwa sasa linaundwa na wanaume pekee akiwemo Rais wa shirikisho, marais wa majimbo na viongozi wengine wanaume wa ngazi ya juu ya uongozi.Makala inatupeleka Rafah kwenye mpaka wa Ukanda wa Gaza na Misri ambako Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula WFP kama yalivyo mashirika mengine ya misaada ya kibinadamu linahaha kuingiza msaada Gaza hususan chakula kwa maelfu ya watu wenye uhitaji Gaza. Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo amefunga safari hadi Rafah kushuhudia hali halisi. Tuungane na Flora Nducha katika makala hii inayoangazia alichoshuhudia.Mashinani fursa ni yake Arevik, ambaye ni mama na mkimbizi wa ndani nchini Armenia, akissema licha ya changamoto walizopitia cha muhimu yuko pamoja na familia yake.
11/8/20230
Episode Artwork

08 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Assumpta Massoi anamulika mwelekeo wa El Nino ya kwamba itaendelea hadi Aprili 2024,  halikadhalika madhara  yake, Somalia kulekea uchaguzi mkuu na ushiriki wa wanawake; Makala inabisha hodi Mashariki ya Kati usaidizi wa kibinadamu huko Gaza, na mashinani inabisha hodi Armenia.Tukio la mkondo joto la El Niño linalosababisha hivi sasa mvua kubwa, joto kali na ukame kwenye maeneo mbalimbali ya dunia, linatarajiwa kuendelea duniani na kuchochea ongezeko la kiwango cha joto baharini na ardhini, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa, WMO hii leo. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Catriona Laing, Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Somalia amethibitisha kuwa Umoja wa Mataifa unashirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu na Wizara ya Maendeleo ya Wanawake na Haki za Binadamu nchini humo kuhakikisha kwamba sauti za wanawake zinasikika katika Baraza la Ushauri la Taifa (NCC) ambalo kwa sasa linaundwa na wanaume pekee akiwemo Rais wa shirikisho, marais wa majimbo na viongozi wengine wanaume wa ngazi ya juu ya uongozi.Makala inatupeleka Rafah kwenye mpaka wa Ukanda wa Gaza na Misri ambako Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula WFP kama yalivyo mashirika mengine ya misaada ya kibinadamu linahaha kuingiza msaada Gaza hususan chakula kwa maelfu ya watu wenye uhitaji Gaza. Mkurugenzi mtendaji wa shirika hilo amefunga safari hadi Rafah kushuhudia hali halisi. Tuungane na Flora Nducha katika makala hii inayoangazia alichoshuhudia.Mashinani fursa ni yake Arevik, ambaye ni mama na mkimbizi wa ndani nchini Armenia, akissema licha ya changamoto walizopitia cha muhimu yuko pamoja na familia yake.
11/8/20239 minutes, 49 seconds
Episode Artwork

07 Novemba 2023

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Umoja wa Mataifa ulikuwa na siku tano za kuadhimisha Umoja wa Mataifa kutimiza miaka 78 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1945 huko San Fransisco nchini Marekani.  Maadhimisho yalifanyika kuanzia tarehe 23 hadi 27 Oktoba kwenye mji mkuu, Kinshasa. Byobe Malenga, mwandishi wetu katika taifa hilo la Maziwa Makuu ndio alikuwa shuhuda wetu wa nini kilifanyika.
11/7/20230
Episode Artwork

07 Novemba 2023

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, Umoja wa Mataifa ulikuwa na siku tano za kuadhimisha Umoja wa Mataifa kutimiza miaka 78 tangu kuanzishwa kwake mwaka 1945 huko San Fransisco nchini Marekani.  Maadhimisho yalifanyika kuanzia tarehe 23 hadi 27 Oktoba kwenye mji mkuu, Kinshasa. Byobe Malenga, mwandishi wetu katika taifa hilo la Maziwa Makuu ndio alikuwa shuhuda wetu wa nini kilifanyika.
11/7/202311 minutes, 45 seconds
Episode Artwork

Vijana tusiwe watazamaji bali tuchukue hatua kwa kuanza na tulicho nacho- Emmanuel

Vijana wana dhima kubwa katika kusongesha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yanayofikia ukomo mwaka 2030. Mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa kutambua nafasi hiyo ya vijana wanatumia vijana wenyewe ili wawe mabalozi wa mashirika hayo mashinani ili kupigia chepuo yale yaliyomo kwenye SDGs. Mathalani nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF lina mabalozi na miongoni mwao ni Emmanuel Cosmas Msoka yeye akijikita kwenye masuala ya usafi wa maji, usafi wa mazingira (WASH) na ubunifu. Na ndiye tunammulika leo katika makala ambapo katika mahojiano naFlora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, Emmanuel ambaye mwezi Septemba mwaka huu alishiriki vikao vya ngazi ya juu vya vijana kuhusu malengo ya maendeleo endelevu, SDGs alielezea mambo kadhaa akianza na kile alichoondoka nacho.
11/6/20230
Episode Artwork

Vijana tusiwe watazamaji bali tuchukue hatua kwa kuanza na tulicho nacho- Emmanuel

Vijana wana dhima kubwa katika kusongesha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yanayofikia ukomo mwaka 2030. Mashirika ya Umoja wa Mataifa kwa kutambua nafasi hiyo ya vijana wanatumia vijana wenyewe ili wawe mabalozi wa mashirika hayo mashinani ili kupigia chepuo yale yaliyomo kwenye SDGs. Mathalani nchini Tanzania shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF lina mabalozi na miongoni mwao ni Emmanuel Cosmas Msoka yeye akijikita kwenye masuala ya usafi wa maji, usafi wa mazingira (WASH) na ubunifu. Na ndiye tunammulika leo katika makala ambapo katika mahojiano naFlora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa, Emmanuel ambaye mwezi Septemba mwaka huu alishiriki vikao vya ngazi ya juu vya vijana kuhusu malengo ya maendeleo endelevu, SDGs alielezea mambo kadhaa akianza na kile alichoondoka nacho.
11/6/20233 minutes, 33 seconds
Episode Artwork

Kalavati 'lasogeza' huduma za afya kwa wanajamii Gambia

Nchini Gambia, Magharibi mwa bara la Afrika, kalavati au daraja dogo lililojengwa na shirika la Umoja wa Mataifa la maendeleo ya mitaji, UNCDF kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU)ili kuunganisha maeneo mawili, Pakaliba na Baro Kunda, limesogeza huduma ya afya karibu na wakazi wa maeneo hayo. Anold Kayanda na maelezo zaidiGambia vijijini, Sarata Ceesay, ili kuhudhuria uchunguzi wa baada ya kujifungua hahitaji tena kupita kwenye maji ambako mamba hupenda kukusanyika. Pia halazimiki kulipa nauli kuzunguka kilomita nne kuikwepa adha ya kupita kwenye maji ambayo hujui utaliwa na mamba au utazama maji. Shukrani kwa ujenzi wa kalavati hili jipya.Bi Ceesay, anaweza kujikinga dhidi ya hofu ya kifo cha mtoto mwingine, binti yake Awa ambaye pacha wake alishafariki akiwa kichanga kwa sababu ya changamoto hizi za huduma ya afya, “tulilazimika kuruka kutoka jiwe moja hadi jingine kuvuka mto.” Anasema.Buba Jobe, Muuguzi na Mkunga wa Afya ya Jamii, Kituo cha Afya cha Pakaliba, Gambia anathibitisha mabadiliko haya chanya,"Sasa kwa kuwa wanaweza kutembea kwa urahisi kutoka Baro Kunda hadi Pakaliba bila kulipa nauli yoyote, hiyo imefanya huduma ya afya kufikika. Wanaweza kuja wakati wowote. Kwa hivyo hiyo imeongeza mtiririko wa wagonjwa wetu katika idara ya wagonjwa wa nje.”
11/6/20230
Episode Artwork

Kalavati 'lasogeza' huduma za afya kwa wanajamii Gambia

Nchini Gambia, Magharibi mwa bara la Afrika, kalavati au daraja dogo lililojengwa na shirika la Umoja wa Mataifa la maendeleo ya mitaji, UNCDF kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU)ili kuunganisha maeneo mawili, Pakaliba na Baro Kunda, limesogeza huduma ya afya karibu na wakazi wa maeneo hayo. Anold Kayanda na maelezo zaidiGambia vijijini, Sarata Ceesay, ili kuhudhuria uchunguzi wa baada ya kujifungua hahitaji tena kupita kwenye maji ambako mamba hupenda kukusanyika. Pia halazimiki kulipa nauli kuzunguka kilomita nne kuikwepa adha ya kupita kwenye maji ambayo hujui utaliwa na mamba au utazama maji. Shukrani kwa ujenzi wa kalavati hili jipya.Bi Ceesay, anaweza kujikinga dhidi ya hofu ya kifo cha mtoto mwingine, binti yake Awa ambaye pacha wake alishafariki akiwa kichanga kwa sababu ya changamoto hizi za huduma ya afya, “tulilazimika kuruka kutoka jiwe moja hadi jingine kuvuka mto.” Anasema.Buba Jobe, Muuguzi na Mkunga wa Afya ya Jamii, Kituo cha Afya cha Pakaliba, Gambia anathibitisha mabadiliko haya chanya,"Sasa kwa kuwa wanaweza kutembea kwa urahisi kutoka Baro Kunda hadi Pakaliba bila kulipa nauli yoyote, hiyo imefanya huduma ya afya kufikika. Wanaweza kuja wakati wowote. Kwa hivyo hiyo imeongeza mtiririko wa wagonjwa wetu katika idara ya wagonjwa wa nje.”
11/6/20231 minute, 30 seconds
Episode Artwork

"Imetosha!" yasema mashirika ya kimataifa kwa kinachoendelea Gaza

Ikiwa ni siku 30 sasa tangu kuanza kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, kati ya Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas walioko katika eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu, Gaza, mashirika 18 ya Kimataifa ya misaada ya kibinadamu yametoa taarifa ya pamoja hii leo yakisema ‘imetosha’ wakitaka kusitishwa mara moja mzozo huo kwasababu za kibinadamu, mzozo ambao umegharimu maisha ya zaidi ya watu 10,000. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi.Mzozo huu alianza Oktoba 7 mwaka huu baada ya wanamgambo wa kipalestina wa Hamas kushambulia Israel, mashambulizi hayo kwa mujibu wa taarifa za Serikali ya Israel yameua takriban waisrael 1,400 huku wengine zaidi ya 200 wakitekwa nyara na Hamas.Katika kujibu mashambulizi, jeshi la Israel lilianza na operesheni ya kurusha makombora kwa njia ya anga na kisha kuongeza operesheni za kijeshi za ardhini ambazo mpaka sasa kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Palestina zimesababisha vifo vya takriban wapalestina 9,500 kati yao 3,900 ni watoto na 2,400 ni wanawake, na 88 ni wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa. Zaidi ya watu 23,000 wamejeruhiwa huku maelfu wakiwa hawajapatikana kwani wamefukiwa na vifusi vya nyumba zao ambazo zimelipuliwa na jeshi la Israel.Ufikishaji wa huduma muhimu za misaada ya kibinadamu kwa wananchi milioni 2.2 walioko Ukanda wa Gaza nazo zimekuwa zikisuasua kutokana na mapigano makali yanayoendelea hali ambayo imesababisha uhaba wa chakula, maji, vifaa tiba, mafuta kwa ajili ya kutoa huduma ya nishati hususan ya umeme kwa hospital zinazohudumia wagonjwa. Juhudi mbalimbali za kidiplomasia zimefanyika na zinaendelea kufanyika ikiwa ni pamoja na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuazimia kusitishwa kwa mapigano mara moja suala ambalo halijatekelezwa mpaka sasa.Taarifa ya Wakuu wa Kamati ya Kudumu ya Mashirika ya Kimataifa, kuhusu hali ya Israel na eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu hii leo imekuja na kauli moja tu ‘imetosha’, haikubaliki kuendelezwa kwa mauaji yakutisha huko Gaza wakati huo huo wananchi wakikosa huduma muhimu kwani hata miundombinu ya umma inashambuliwa, wakitolea mfano zaidi ya mashambulizi 100 dhidi ya huduma za afya yameripotiwa. Ndani ya kipindi cha siku 10 mawasiliano yamekatika mara 3 huko Gaza hali ambayo si tu imezuia mawasiliano ya raia walioko Gaza bali pia imeliwia vigumu Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwasaidia wakimbizi wa Kipalestina UNRWA kuwasiliana na wafanyakazi wake walioko Gaza kwa ajili ya kuratibu masuala ya usaidizi. Jeshi la Israel limelipua vyanzo vya maji safi pamoja na hifadhi za maji taka na Ofisi ya moja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu OCHA imeeleza uhaba wa maji hususan Gaza Kaskazini umezua wasiwasi mkubwa wa watu kuwa na upungufu wa maji mwilini na magonjwa yatokanayo na maji kutokana na matumizi ya maji kutoka vyanzo visivyo salama. Tayari UNRWA imeripoti kuwepo kwa wagonjwa kadhaa wenye matatizo ya kupumua, kuhara, tetekuwanga katika maeneo wanayotoa hifadhi. Taarifa hiyo ya pamoja ya mashirika hayo imerejea ombi lao kwa pande zote katika mzozo huo kuheshimu sheria za Kimataifa za kibinadamu na haki za binadamu, wametoa wito mateka wote waachiliwe bila masharti, raia na miundombinu ya umma isishambuliwe, misaada zaidi ya kibinadamu ambayo ni chakula, maji, dawa iweze kuingia kwa usalama huko Gaza kwa kiwango kinachohitajika na iwafikie wenye uhitaji hasa wanawake na watoto popote walipo. Mashirika ya UN yaliyotia saini taarifa hiyo ni WHO, UN WOMEN, UNFPA, OCHA, UNRWA, UNICEF, IOM, UNHCR, UNDP, UN-HABITAT, OHCHR, mtaalamu maalumu wa UN kuhusu wakimbizi wa ndani, na WFP mashirika yasiyo ya UN ni Care International, Save the Children, Interaction, Mercy Corp na ICVA
11/6/20230
Episode Artwork

"Imetosha!" yasema mashirika ya kimataifa kwa kinachoendelea Gaza

Ikiwa ni siku 30 sasa tangu kuanza kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, kati ya Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas walioko katika eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu, Gaza, mashirika 18 ya Kimataifa ya misaada ya kibinadamu yametoa taarifa ya pamoja hii leo yakisema ‘imetosha’ wakitaka kusitishwa mara moja mzozo huo kwasababu za kibinadamu, mzozo ambao umegharimu maisha ya zaidi ya watu 10,000. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi.Mzozo huu alianza Oktoba 7 mwaka huu baada ya wanamgambo wa kipalestina wa Hamas kushambulia Israel, mashambulizi hayo kwa mujibu wa taarifa za Serikali ya Israel yameua takriban waisrael 1,400 huku wengine zaidi ya 200 wakitekwa nyara na Hamas.Katika kujibu mashambulizi, jeshi la Israel lilianza na operesheni ya kurusha makombora kwa njia ya anga na kisha kuongeza operesheni za kijeshi za ardhini ambazo mpaka sasa kwa mujibu wa Wizara ya Afya ya Palestina zimesababisha vifo vya takriban wapalestina 9,500 kati yao 3,900 ni watoto na 2,400 ni wanawake, na 88 ni wafanyakazi wa Umoja wa Mataifa. Zaidi ya watu 23,000 wamejeruhiwa huku maelfu wakiwa hawajapatikana kwani wamefukiwa na vifusi vya nyumba zao ambazo zimelipuliwa na jeshi la Israel.Ufikishaji wa huduma muhimu za misaada ya kibinadamu kwa wananchi milioni 2.2 walioko Ukanda wa Gaza nazo zimekuwa zikisuasua kutokana na mapigano makali yanayoendelea hali ambayo imesababisha uhaba wa chakula, maji, vifaa tiba, mafuta kwa ajili ya kutoa huduma ya nishati hususan ya umeme kwa hospital zinazohudumia wagonjwa. Juhudi mbalimbali za kidiplomasia zimefanyika na zinaendelea kufanyika ikiwa ni pamoja na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kuazimia kusitishwa kwa mapigano mara moja suala ambalo halijatekelezwa mpaka sasa.Taarifa ya Wakuu wa Kamati ya Kudumu ya Mashirika ya Kimataifa, kuhusu hali ya Israel na eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu hii leo imekuja na kauli moja tu ‘imetosha’, haikubaliki kuendelezwa kwa mauaji yakutisha huko Gaza wakati huo huo wananchi wakikosa huduma muhimu kwani hata miundombinu ya umma inashambuliwa, wakitolea mfano zaidi ya mashambulizi 100 dhidi ya huduma za afya yameripotiwa. Ndani ya kipindi cha siku 10 mawasiliano yamekatika mara 3 huko Gaza hali ambayo si tu imezuia mawasiliano ya raia walioko Gaza bali pia imeliwia vigumu Shirika la Umoja wa Mataifa la kuwasaidia wakimbizi wa Kipalestina UNRWA kuwasiliana na wafanyakazi wake walioko Gaza kwa ajili ya kuratibu masuala ya usaidizi. Jeshi la Israel limelipua vyanzo vya maji safi pamoja na hifadhi za maji taka na Ofisi ya moja wa Mataifa ya Kuratibu Masuala ya Kibinadamu OCHA imeeleza uhaba wa maji hususan Gaza Kaskazini umezua wasiwasi mkubwa wa watu kuwa na upungufu wa maji mwilini na magonjwa yatokanayo na maji kutokana na matumizi ya maji kutoka vyanzo visivyo salama. Tayari UNRWA imeripoti kuwepo kwa wagonjwa kadhaa wenye matatizo ya kupumua, kuhara, tetekuwanga katika maeneo wanayotoa hifadhi. Taarifa hiyo ya pamoja ya mashirika hayo imerejea ombi lao kwa pande zote katika mzozo huo kuheshimu sheria za Kimataifa za kibinadamu na haki za binadamu, wametoa wito mateka wote waachiliwe bila masharti, raia na miundombinu ya umma isishambuliwe, misaada zaidi ya kibinadamu ambayo ni chakula, maji, dawa iweze kuingia kwa usalama huko Gaza kwa kiwango kinachohitajika na iwafikie wenye uhitaji hasa wanawake na watoto popote walipo. Mashirika ya UN yaliyotia saini taarifa hiyo ni WHO, UN WOMEN, UNFPA, OCHA, UNRWA, UNICEF, IOM, UNHCR, UNDP, UN-HABITAT, OHCHR, mtaalamu maalumu wa UN kuhusu wakimbizi wa ndani, na WFP mashirika yasiyo ya UN ni Care International, Save the Children, Interaction, Mercy Corp na ICVA
11/6/20234 minutes, 12 seconds
Episode Artwork

06 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Assumpta Massoi anaanzia Mashariki ya Kati, mapigano huko Gaza siku ya 30, "imetosha" yasema mashirika ya kimataifa, kisha anakwenda Gambia, Magharibi mwa Afrika huko kalavati limeimarisha afya. Makala ni kijana Emmanuel Cosmas Msoka akizungumza na Flora Nducha kuhusu SDGs na mashinani tunakwenda Karamoja nchini Uganda, kilimo cha kisasa kimekomboa wanawake kiuchumi na kijamii. 1. Ikiwa ni siku 30 sasa tangu kuanza kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, kati ya Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas walioko katika eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu, Gaza, mashirika 18 ya Kimataifa ya misaada ya kibinadamu yametoa taarifa ya pamoja hii leo yakisema ‘imetosha’ wakitaka kusitishwa mara moja mzozo huo kwasababu za kibinadamu, mzozo ambao umegharimu maisha ya zaidi ya watu 10,000. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi.2. Nchini Gambia, Magharibi mwa bara la Afrika, kalavati au daraja dogo lililojengwa na shirika la Umoja wa Mataifa la maendeleo ya mitaji, UNCDF kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU)ili kuunganisha maeneo mawili, Pakaliba na Baro Kunda, limesogeza huduma ya afya karibu na wakazi wa maeneo hayo. Anold Kayanda na maelezo zaidi3. Makala:  Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anazungumza na Emmanuel Cosmas Msoka mchechemuzi kijana wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF kutoka nchini Tanzania ambaye mwezi Septemba mwaka huu alishiriki vikao vya ngazi ya juu vya vijana kuhusu malengo ya maendeleo endelevu, SDGs na hapa anaelezea kile alichoondoka nacho.4. Mashinani: Fursa ni yake Rose Lydia, Mkulima na Mwenyekiti wa kundi la wanawake wakulima akisimulia ambavyo wameweza kujimudu kimaisha kutokana na mafunzo ya ukulima waliyoyapata kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP huko Karamoja, Kaskazini Mashariki mwa Uganda.
11/6/20230
Episode Artwork

06 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani Assumpta Massoi anaanzia Mashariki ya Kati, mapigano huko Gaza siku ya 30, "imetosha" yasema mashirika ya kimataifa, kisha anakwenda Gambia, Magharibi mwa Afrika huko kalavati limeimarisha afya. Makala ni kijana Emmanuel Cosmas Msoka akizungumza na Flora Nducha kuhusu SDGs na mashinani tunakwenda Karamoja nchini Uganda, kilimo cha kisasa kimekomboa wanawake kiuchumi na kijamii. 1. Ikiwa ni siku 30 sasa tangu kuanza kwa mzozo huko Mashariki ya Kati, kati ya Israel na Wanamgambo wa Kipalestina wa Hamas walioko katika eneo la Palestina linalokaliwa kwa mabavu, Gaza, mashirika 18 ya Kimataifa ya misaada ya kibinadamu yametoa taarifa ya pamoja hii leo yakisema ‘imetosha’ wakitaka kusitishwa mara moja mzozo huo kwasababu za kibinadamu, mzozo ambao umegharimu maisha ya zaidi ya watu 10,000. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Leah Mushi.2. Nchini Gambia, Magharibi mwa bara la Afrika, kalavati au daraja dogo lililojengwa na shirika la Umoja wa Mataifa la maendeleo ya mitaji, UNCDF kwa ufadhili wa Muungano wa Ulaya (EU)ili kuunganisha maeneo mawili, Pakaliba na Baro Kunda, limesogeza huduma ya afya karibu na wakazi wa maeneo hayo. Anold Kayanda na maelezo zaidi3. Makala:  Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anazungumza na Emmanuel Cosmas Msoka mchechemuzi kijana wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF kutoka nchini Tanzania ambaye mwezi Septemba mwaka huu alishiriki vikao vya ngazi ya juu vya vijana kuhusu malengo ya maendeleo endelevu, SDGs na hapa anaelezea kile alichoondoka nacho.4. Mashinani: Fursa ni yake Rose Lydia, Mkulima na Mwenyekiti wa kundi la wanawake wakulima akisimulia ambavyo wameweza kujimudu kimaisha kutokana na mafunzo ya ukulima waliyoyapata kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP huko Karamoja, Kaskazini Mashariki mwa Uganda.
11/6/202312 minutes, 59 seconds
Episode Artwork

Ibara ya 12 ya UDHR inatekelezwa Tanzania?

Na sasa tuangazie Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75. Na katika mfululizo wa vipindi vyetu vya kuelimisha umma kuhusu tamko hili kwa kuelezea Ibara kwa Ibara, ninakupeleka nchini Tanzania kwa mwanasheria na wakili Emmanuel Sosthenes kutoka shirika linalotoa msaada wa sheria kwa wanawake nchini humo, WILAC, akichambua Ibara ya 12 ya tamko hilo na jinsi inavyotekelezwa kwenye taifa hilo la Afrika Mashariki. Kwako Emmanuel.  
11/3/20230
Episode Artwork

Wanawake na wasichana wafungwa minyororo Sudan

Ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa (OHCHR) imesikitishwa sana na ripoti kwamba huko Darfur nchini Sudan wanawake na wasichana wanatekwa nyara na kushikiliwa katika mazingira ya yasiyo ya kiutu katika maeneo yanayodhibitiwa na wanamgambo waasi (RSF). Anold Kayanda na maelezo zaidi.  Msemaji wa ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa Liz Throssell (Elizabeth Throssel) hii leo Ijumaa asubuhi saa za Geneva, Uswisi akizungumza na waandishi wa Habari anasema, “habari za kuaminika kutoka kwa walionusurika, mashahidi na vyanzo vingine vinaeleza kwamba zaidi ya wanawake na wasichana 20 wametekwa, lakini idadi inaweza kuwa ni kubwa zaidi ya hiyo iliyotajwa.” Bi. Throssel anaendelea kueleza kuwa vyanzo vingine vimeripoti kuwaona wanawake na wasichana wakiwa kwenye minyororo kwenye magari ya kubebea mizigo na magari madogo. Taarifa hizi za kushtua zinakuja huku kukiwa na ongezeko la visa vya unyanyasaji wa kingono nchini humo tangu mapigano yazuke kati ya Jeshi la Sudan na Vikosi hivyo vya wanamgambo wa RSF miezi sita iliyopita. Kwa mujibu wa takwimu walizonazo, Msemaji huyo wa ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa, anasema, “takribani watu 105 wamefanyiwa ukatili wa kingono tangu mapigano hayo yalipoanza tarehe 15 Aprili 2023.” Wanawake wanatekwa, wanalazimishwa kuolewa na kushikiliwa huku watekaji wakidai kikombozi. Kufikia tarehe 2 Novemba, Ofisi ya Haki za Kibinadamu nchini humo Sudan ilikuwa imepokea ripoti za kuaminika za zaidi ya matukio 50 ya unyanyasaji wa kingono yanayohusishwa na uhasama na kuwaathiri wanawake 86, mwanamume mmoja na watoto 18. Matukio 23 kati ya hayo yalihusisha ubakaji, 26 yalikuwa ya ubakaji unaotekelezwa na watu wengi yaani genge na matatu ya kujaribu kubaka. Ofisi hiyo ya haki za binadamu imelaani vikali vitendo hivyo na kuwataka viongozi wa juu wa Jeshi la Sudan na wa Vikosi vya wanamgambo waasi wa RSF pamoja makundi mengine yenye kujihami kwa silaha ambayo yana uhusiano na pande hizi mbili kuchukua hatua za haraka kukomesha unyanyasaji wa kingono ikiwa ni pamoja na kuwaachia huru waliotekwa nyara, kuwapatia huduma ya matibabu na kisaikolojia na kuwafikisha katika mikono ya sheria wahusika wa matukio haya ya kikatili.  
11/3/20230
Episode Artwork

03 NOVEMBA 2023

Karibu kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa ambapo hii leo utasikia kutoka Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu OHCHR ambayo imesikitishwa sana na ripoti kwamba huko Darfur nchini Sudan wanawake na wasichana wanatekwa nyara na kushikiliwa katika mazingira ya yasiyo ya kiutu katika maeneo yanayodhibitiwa na wanamgambo waasi (RSF). Pia utapata ufafanuzi wa Ibara ya 12 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75. Makala utasikia utekelezaji wa SDGs nchini Tanzania na mashinani tutasalia kutoka kwa Wakimbizi wa DRC walioko nchini Tanzania. 
11/3/20230
Episode Artwork

GLAMI Tanzania yasongesha SDG 4 na SDG 5

Harakati za kuhakikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs ya Umoja wa Mataifa yanatekelezwa kwa mafanikio ifikapo ukomo wake mwaka 2030 zinaendelea katika nchi mbalimbali wanachama wa chombo hicho. Mathalani nchini Tanzania, mashirika ya kiraia yanaunga mkono hatua za serikali kufanikisha malengo hayo. Miongoni mwa mashirika hayo ni lile lisilo la kiserikali la Girls Livelihood and Mentor Initiative (GLAMI) ambalo kupitia mradi wa KISA unatekeleza kwa vitendo lengo namba 4 la Elimu Bora na namba 5 la Usawa wa Kijinsia, kwa kuwakutanisha wanafunzi wa kike 777 wa shule tatu za sekondari; Nuru, Magadini na Oshara katika Mkoa wa Kilimanjaro, kaskazini mwa nchi kutambua taaluma zao kabla ya kufikia katika elimu yao ya juu. Mwandishi wa Habari Hamad Rashid wa Redio washirika ya Mviwata FM kutoka Morogoro alihudhuria tukio hilo na kutuandalia makala hii ambapo Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la GLAMI Anande Nnko anaanza kwa kueleza umuhimu wa hii inayoitwa Siku ya Taaluma.   
11/3/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili: Ufafanuzi wa neno “INADI”.

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili  leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “INADI”. 
11/2/20230
Episode Artwork

02 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina, ambapo nchini Tanzania mradi wa Fish4ACP unaofadhiliwa na Muungano wa Ulaya na kutekelezwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo, FAO kwa kushirikiana n serikali ya Tanzania unaendelea kuleta matunda ya malengo yake ya kuanzishwa. Yaani kuongeza thamani ya mazao yanayotokana na uvuvi na kuimarisha maisha ya wavuvi na wachakataji wa mazao hayo kwa kuongeza thamani. Mradi huu unatekelezwa mikoa ya Kigoma, Katavi na Rukwa. Pi atunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo za machafuko Gaza, uhalifu unaofanyiwa waandishi wa habari na ripoti ya UNEP kuhusu Tabianchi na mazingira. Katika kujifunza Kiswahili tunakuletea ufafanuzi wa neno “INADI”.   Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA imeeleza kuwa mashambulizi za ardhini yanatotekelezwa kwa siku kadhaa sasa na Israel huko katika Ukanda wa Gaza yamezuia usafirishaji wa misaada kutoka Gaza Kusini kwenda Gaza Kaskazini hivyo wananchi walioko Gaza Kaskazini hawawezi kufikishiwa misaada ya kibinadamu wakati huu wakikabiliwa na mashambulizi ya anga na ardhini. Shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira UNEP limezindua ripoti hii leo jijini Nairobi nchini Kenya iliyoeleza maendeleo ya harakati za kuhimili mabadiliko ya tabianchi yanasuasua wakati huu ambapo yanapaswa kushika kasi ili kuendana na ongezeko la madhara ya mabadiliko ya tabianchi. Na leo ni siku ya Kimataifa ya kupinga ukwepaji sheria dhidi ya vitendo vya uhalifu wanavyofanyiwa waandishi wa habari ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amenukuu shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni, UNESCO ambalo linasema mwaka 2022 pekee, waandishi wa habari 88 waliuawa.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo ukumbi ni wake mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “INADI”.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
11/2/20230
Episode Artwork

Simulizi ya Binti Armen Gakani, Mkimbizi Kalobeyei

Migogoro ya miongo na miongo nchini Jamhuri ya kidemocrasia ya Congo, DRC imefurusha watu wengi kutoka makazi yao, wengine kubaki wakimbizi wa ndani na wengnine kukimbilia nchi Jirani. Kenya ni mojawapo wa nchi ambazo zinawahifadhi wakimbizi hao na katika Kaunti ya Turkana, tunakutana na Armen Gakani, msichana mwenye umri wa miaka 23 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, ambaye alikimbia machafuko nchini humo na sasa yeye, akiwa na mama yake na wadogo wake wawili wenye ulemavu wanaishi katika kambi ya wakimbizi ya Kalibeyei. Je, ni kwa jinsi gani wameweza kujimudu kimaisha? Tuungane na Pamela Awuori wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ili kufahamu zaidi. 
11/1/20230
Episode Artwork

01 NOVEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko Gaza na mafuriko nchini Libya. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani nchini Tanzania, kulikoni?   Umoja wa Mataifa leo umekaribisha uamuzi wa Misri wa kukubali kupokea baadhi ya wagonjwa kutoka eneo la wapalestina la Gaza linalokaliwa na Israeli, kwa ajili ya kuwapatia matibabu, huku mashirika mengine ya Umoja huo yakiendelea kuzungumzia adha inayowakabili maelfu ya watu wa Gaza wakiwemo watoto, uhaba wa mahitaji muhimu, ukosefu wa matfta, kufurika kwa makazi ya dharura na Israeli kuendelea na operesheni ya kijeshi ardhini. Mashirika ya Umoja wa Mataifa na wadau wake yakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali yanaendelea kusaidia kuwafikishia misaada watu katika maeneo ya Libya yaliyoathiriwa na mafuriko makubwa yaliyoipiga taifa hilo la Afrika Kaskazini tarehe 10 na 11 mwezi Septemba mwaka huu, hasa wakati huu msimu wa baridi Kali unapojongea. Makala leo tunaelekea Kaunti ya Turkana, nchini Kenya, ambako tunakutana msichana mwenye umri wa miaka 23 kutoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, ambaye alikimbia machafuko nchini humo na sasa yeye na mama yake na wadogo zake wawili wenye ulemavu, wanaishi katika kambi ya wakimbizi ya Kalobeyei.Mashinani tunakupeleka nchini Tanzania kusikiliza ujumbe kuhusu afya ya akili na haki za binadamu. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
11/1/20230
Episode Artwork

Waathirika wa mafuriko Libya wanaendelea kupokea msaada kutoka UN na wadau wake

Mashirika ya Umoja wa Mataifa na wadau wake yakiwemo mashirika yasiyo ya kiserikali yanaendelea kusaidia kuwafikishia misaada watu katika maeneo ya Libya yaliyoathiriwa na mafuriko makubwa yaliyoipiga taifa hilo la Afrika Kaskazini tarehe 10 na 11 mwezi Septemba mwaka huu, hasa wakati huu msimu wa baridi Kali unapojongea. Katika kipindi cha wiki sita tangu mafuriko yaliyosababishwa na kilichotambuliwa kuwa kimbunga kibaya zaidi barani Afrika, mashirika ya misaada ya kibinadamu yamewahudumia takribani watu 164,000 kwa misaada ya kibinadamu na shughuli za usaidizi zinaendelea kwa watu waliopoteza nyumba zao.Video iliyoandaliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA inaonesha mahitaji ya kipaumbele kama ukarabati wa haraka wa mitandao ya maji na maji taka, udhibiti wa taka na uondoaji salama wa uchafu yakifanyiwa kazi."Mahitaji yao makuu sasa ni kuhama kutoka kwenye makazi ya shuleni kwenda kwenye nyumba za muda au kupokea fidia ili kuanza tena maisha yao." Anasema Safina Al Mahjoud, Mwakilishi wa Shirika lisilo la kiserikali linaloitwa Kisa akiwa katika shule ya Al Um Qura huko Derna, Mashariki mwa nchi.Hali ya watu waliokusanyika katika maeneo ya pamoja baada ya kuyakimbia makazi yao bado ni tete. Takriban watu 1,750 wanaendelea kuangaliwa katika maeneo 18. Shughuli ya kuwahamisha watu hawa kwenda kwenye maeneo yenye hali nzuri itaanza ivi karibuni.Hamdi Beleid, ni mfanyakazi wa kujitolea katika Shirika la Mwezi Mwekundu la Libya, anasema, "Mimi ni mmoja wa watu walioathiriwa na janga hili. Nilipoteza wanafamilia wote. Nilipoteza nyumba yangu na chanzo cha mapato. Nilipoteza kila kitu katika maisha haya. Lakini kwa msaada wa Mungu, ninakabiliana nayo na ninaweza kuendelea na kazi yangu. Kwa sababu najua watu wanachopitia, naendelea kutoa msaada. Mungu anisaidie ili nisaidie idadi kubwa ya watu.”Kimbunga Daniel kilipoyakumba maeneo mbalimbali ya Libya, mashirika ya Umoja wa Mataifa yalitathimini kuwa takribani watu 4000 walifariki Dunia na wengine zaidi ya mara mbili ya hao hawakufahamika waliko.
11/1/20230
Episode Artwork

Wagonjwa wahamishwa Gaza kwa ajili ya matibabu Misri, UN yakaribisha

Umoja wa Mataifa leo umekaribisha uamuzi wa Misri wa kukubali kupokea baadhi ya wagonjwa kutoka Gaza kwa ajili ya matibabu, huku mashirika mengine ya Umoja huo yakiendelea kuzungumzia adha inayowakabili maelfu ya watu wa Gaza wakiwemo watoto, uhaba wa mahitaji muhimu, ukosefu wa matuta, kufurika kwa makazi ya dharura na kuendelea kwa operesheni ya ardhini ya Israel. Asante Assumpta nianze na hiyo habari njema kwa wagonjwa Gaza hususan wale walio mahtuti na waliojeruhiwa vibaya ambao sasa watakwenda kupata matibabu Misri hatua ambayo imekaribishwa na Umoja wa Mataifa akiwemo mkurugenzi mkuu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa duniani WHO Dkt. Tedross pia amesema “Tumekuwa tukifanyakazi kwa karibu na wizara ya afya ya Misri kupanga uhamishaji wa wagonjwa kwa ajili ya matibabu na tutaendelea kusaidia katika hili”Kauli yake imefuatia taarifa kwamba kivuko cha Rafah baina ya Misri na Gaza kimeruhusiwa kufunguliwa leo mahsusi kwa ajili hiyo ya kuahamisha wagonjwa ikiwa ni mara ya kwanza tangu Oktoba 7, na watakaohamishwa ni wagonjwa lakini pia raia wa kigeni na wenye uraia pacha na hicho ndio kivuko pekee ambacho hakidhibitiwi na Israel.Hata hivyo pamoja na habari hiyo njema bado madhila makubwa yanawaghubika watu wa Gaza shirika la kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA limesema kwani uhaba wa mahitaji mengine ya msingi ni mkubwa sana licha ya jana kushuhudia msafara mkubwa zaidi wa misaada wa malori 59 yakiwa na maji, chakula na dawa. Limesema changamoto kubwa zaidi hivi sasa ni mafuta kwa ajili ya kuendesha vifaa vya kuokoa maisha ambayo bado yamepigwa marufuku kuingia Gaza.Hivyo WHO na OCHA yote yamesihi kuingizwa kwa misaada zaidi Gaza ikiwemo mafuta.Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA limemulika changamoto ya makazi likisema hivi sasa zaidi ya watu milioni 1.4 wamekuwa wakimbizi wa ndani Gaza na wengine zaidi ya 689,000 wanapata hifadhi katika vituo 150 vywa UNRWA ambavyo vimejaa pomoni na kuhatarisha cangamoto zingine zikiwemo za kiafya.Mashirika hayo pia yameonya kuhusu kuendelea kwa operesheni ya ardhini ya jeshi la Israel Gaza ambapo jana kumekuwa na tarifa ya mashambulizi katika makazi ya Jabaliya Kaskazini mwa Gaza mji wenye kambi kubwa zaidi ya wakimbizi inayohifadhi watu 116,000.
11/1/20230
Episode Artwork

31 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na leo tunabisha hodi nchini Kenya ambako hivi karibuni kumefanyika mkutano kuhusu mabadiliko ya tabianchi ulioandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa ya kukabiliana na ueneaji wa hali ya jangwa UNCCD ukishirikisha wadau wengine, kukijadili ni jinsi gani ya kuzishirikisha jamii kwanza kupunguza athari na gharama zinazoletwa na hali ya jangwa na pili kuwajengea mnepo wananchi dhidi ya athari za mabadiliko ya tabianchi. Tuanluetea pia habari kwa ufupi zikiwemo za machafuko Gaza, afya nchini Sudan na ujumbe wa Katibu Mkuu wa kuhusu siku ya Miji Duniani. Mashinani tunakupeleka huko Port-au-Prince makao makuu ya taifa la Haiti, kulikoni?  1. Gaza imegeuka "makaburi" ya watoto, kwani maelfu wameuawa kufuatia mashambulizi yanayofanywa na Israel huku zaidi ya Watoto milioni moja wakikabiliwa na uhaba mkubwa wa mahitaji muhimu na maisha yao ya baadaye yakikabiliwa na kiwewe, amesema Mkuu wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu na dharura, OCHA, Martin Griffiths kupitia ukurasa wake kwenye mtandao wa X, hii leo. 2. Dkt Ni’ma Saeed Abid ambaye ni Mwakilishi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO) nchini Sudan, leo ameripoti kuwa Mfumo wa afya nchini humo umezidiwa kiasi cha kufikia hatua mbaya huku mahitaji yakiongezeka kutokana na milipuko ya magonjwa, utapiamlo, na kuongezeka kwa wagonjwa wenye magonjwa yasiyo ya kuambukiza ambao hawajatibiwa mathalani wenye kisukari, shinikizo la damu, saratani, magonjwa sugu ya kupumua na figo. Kidogo Habari njema ni kuwa WHO Sudan inajiandaa kupokea chanjo ya matone dhidi ya kipindupindu kutoka kwa ICG ambalo ni Kundi la kimataifa la kuratibu usambazaji wa chanjo nyakati za dharura linachoundwa na WHO, UNICEF na wadau wao. 3. Na ikiwa leo ni Siku ya Miji Duniani, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa siku hii ametoa wito kwamba, ‘tunapoadhimisha Siku ya Miji Duniani, tuazimie kufanya kazi pamoja kwa ajili ya maeneo ya mijini ambayo si tu ni injini za ukuaji, bali vinara wa uendelevu, mnepo, na ustawi kwa wote. Naye Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN Habitat), Maimunah Mohd Sharif akisisitiza Kaulimbiu ya mwaka huu, Kufadhili Mstakabali wa Miji Endelevu kwa wote, amesema unahitajika mfumo mpya wa ufadhili kwa ajili ya maendeleo endelevu ya miji na kwamba pia inahitajika kuwekeza katika upangaji jumuishi na kuongeza kasi ya kuyafanya makazi na nyumba kuwa haki ya binadamu.4. Mashinani tunakupeleka huko Port-au-Prince makao makuu ya taifa la Haiti kumsikia Duvernise Altema akieleza maishi wanayoishi baada ya kulazimishwa kuyahama makazi yao kutokana na mzozo unaoendelea nchini humo. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/31/20230
Episode Artwork

UNICEF na Equal Access International, wabuni mbinu za kukabiliana na changamoto katika jamii

Janga la tabianchi limesababisha kupotea kwa upatikanaji wa elimu, huduma muhimu, na ajira kwa vijana nchini Kenya. Hata hivyo Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) kwa kushirikiana na Equal Access International wamewawezesha vijana kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na kutoa ufahamu kuhusu suluhisho la kukabiliana na tatizo hilo. Evarist Mapesa wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa anatufafanulia zaidi katika Makala hii.
10/30/20230
Episode Artwork

Wanawake na wasichana wajawazito walioko Gaza wasimulia kinachowakumba

Wakati mzozo katika Ukanda wa Gaza ukizidi kuongezeka huku wananchi wakikabiliwa na changamoto nyingine lukuki ikiwemo uhaba wa chakula, maji, mafuta na vifaa vya matibabu vya kuokoa maisha, Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya watu na Afya ya Uzazi UNFPA limesema mfumo wa afya nao uko ukingoni kuanguka. Shirika hilo limezungumza na wanawake wajawazito walioko Gaza kuhusu hali mbaya wanayokabiliana nayo. Thelma mwadzaya anatujuza walichosema wanawake hao. Ukanda wa Gaza makazi ya watu milioni 2.2, wanawake 50,000 ni wajawazito hivi sasa katika eneo ambalo vita inaendelea. UNFPA imesema takriban wanawake 5,500 wanatakiwa kujifungua ndani ya siku 30 zijazo na takwimu za sasa idadi ya wanawake wanaojifungua kila siku ni 160. Wakati wanawake 840 wanaweza kuwa na changamoto wakati wa kujifungua, wengi wa wanawake walioko Gaza wamekatishwa huduma za uzazi salama, kwani hospitali, ambazo zimeelemewa na majeruhi, zinakosa mafuta ya jenereta, dawa na vifaa muhimu ikiwa ni pamoja na usimamizi wa dharura za uzazi.Hizi ndio simulizi za madhila wanayokutana nao wanawake hawa ambao hatutataja majina yao. Wakwanza anatueleza hali ilivyo “Kila mara kuna bomu, naogopa, miguu yangu inapooza, siwezi kutembea, siwezi kusogea, hasa ukizingatia nina watoto na nahitajika kukimbia kwenda kuwafuata, haya ni mateso zaidi ya changamoto zinazo tukabili kwasababu ya ardhi yetu kutwaliwa. Ninaogopa, sababu ya watoto wangu na mtoto wangu aliye tumboni ambaye hajazaliwa.”Huyu wa pili, nyumba yao ililipuliwa na mabomu yanayorushwa na Israel, anasema “Natarajia kujifungua mwezi huu, ninalala mitaani kama ulivyonikuta, hali haivumiliki hapa” Na watatu, naye amepata hifadhi katika shule zinazo endeshwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina UNRWA.“Hii ndio sehemu pekee ambayo tumeambiwa ina usalama, niña ujauzito wa miezi saba. Hali hapa inasikitisha, unaweza kuisikia hata kwenye sauti yangu. Kifua kinaniuma, niña mafua makali na niña kohoa na hakuna maji kabisa, tunajaribu kuosha vyakula lakini maji si masafi, hata maji kitone tunayofanikiwa kuyapata si masafi. Ninachotaka ni usalama, mazingira salama ya afya, suala kubwa zaidi sasa ni kusafisha vyoo na kupata vifaa vya usafi, maji ni muhimu kwetu hali ni mbaya sana kwetu.”Tayari UNFPA imetuma dawa na vifaa vya afya ya uzazi vya kuokoa maisha nchini Misri kwa ajili ya kuhifadhi na kusafirishwa kuvuka mpaka hadi Gaza. Hadi kufikia tarehe 26 Oktoba, UNFPA ilifikisha nchini Misri vifaa 3,000 vya usafi na kujihifadhi kwa ajili ya wanawake pamoja na wajawazito. 
10/30/20230
Episode Artwork

30 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia hali ya kibinadamu katika eneo linalokaliwa na wapaestina Gaza. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani nchini Ethiopia, kulikoni?Huku mzozo wa Israel na Palestina ukiwa katika wiki yake ya nne, wahudumu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa leo wameonya kuhusu shinikizo      linaloongezeka kwenye hospitali za kaskazini mwa Gaza ambako wamesalia wagonjwa na wahudumu wa afya, huku kukiwa na ripoti za kuongezeka kwa  operesheni za ardhini za jeshi la Israel. Wakati mzozo katika Ukanda wa Gaza ukizidi kuongezeka huku wananchi wakikabiliwa na changamoto nyingine lukuki ikiwemo uhaba wa chakula, maji, mafuta na vifaa vya matibabu vya kuokoa maisha, Shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya watu na Afya ya Uzazi UNFPA limesema mfumo wa afya nao uko ukingoni kuanguka. Shirika hilo limezungumza na wanawake wajawazito walioko Gaza kuhusu hali mbaya wanayokabiliana nayo. Katika makala Evarist Mapesa anakupeleka nchini Kenya ambapo mabadiliko tabianchi umesababisha kupotea kwa upatikanaji wa elimu, huduma muhimu, na ajira kwa vijana nchini Kenya, Hata hivyo Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto (UNICEF) nchini humo kwa kushirikiana na Equal Access International wanawawezesha vijana kuchukua hatua dhidi ya mabadiliko tabianchi na kutoa ufahamu kuhusu suluhisho la kukabiliana na tatizo hilo.mashinani na tutaelekea nchini Ethiopia, kushuhudia jinsi gani Umoja wa Mataifa unavyasaidia watoto kuondokana na utapiamlo uliokithiri. Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/30/20230
Episode Artwork

Wahudumu wa misaada wa UN wanasema hospitali za Gaza zimezidiwa na ziko ukingoni mwa huduma

Huku mzozo wa Israel na Palestina ukiwa katika wiki yake ya nne, wahudumu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa leo wameonya kuhusu shinikizo  linaloongezeka kwenye hospitali za kaskazini mwa Gaza ambako wamesalia wagonjwa na wahudumu wa afya, huku kukiwa na ripoti za kuongezeka kwa  operesheni za ardhini za jeshi la Israel. Asante Leah Mashirika yote ya kibinadamu ya Umoja wa Mataifa yamesisitiza wito wa misaada zaidi na usitishwaji wa uhasama kwani hali ni mbayá sana , maji yamezidi unga.Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura OCHA limesema viunga vya hospitali za Shifa na Al Quds katika mji wa Gaza na hospitali ya Indonesia kaskazini mwa Gaza, vimeshambuliwa mwishoni mwa juma na "Hii ilifuatia wito uliotolewa upya na jeshi la Israel la kuhamisha vituo hivyo mara moja."Kupitia ukurasa wake wa X mkuu wa OCHA na mratibu wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths akiwa Mashariki ya Kati amesema “Rais wa Palestina na Israel wameteseka vya kutosha.” Griffith amesema anatarajia kukutana na timu ya OCHA kwenye eneo linalokaliwa la Palestina ambayo amesema kazi yao ni ya kishujaa.Shirika hilo linasema takriban watu 117,000 waliokimbia makazi yao wanahifadhiwa katika hospitali 10 ambazo bado zinafanya kazi katika mji wa Gaza na mahali pengine kaskazini mwa Gaza, ambazo zimepokea maagizo ya kurejewa kwa wito wa kuondoka katika siku za hivi karibuni.Shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO kupitia ukurasa wake a X nalo limesema "kuhamishwa kwa hospitali nzima haiwezekani bila kuhatarisha maisha ya wagonjwa".Kwa upande wake shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu na afya ya uzazi duniani UNFPA limesema hali ni mbaya sana hasa kwa kina mama wanaojifungua kwani hivi sasa upasuaji wa wanawake kujifungua unafanywa bila ganzi huku kukiwa na uhaba mkubwa wa vifaa vya matibabu na nishati, na wakati mwingine madaktari wanabidi kuzalisha watoto njiti wa kina mama wanaofariki dunia.”Huu ni ushuhuda wa kutisha na kusikitisha kutoka kwa wafanyakazi wa Hospitali ya Shifa.UNRWA ambalo ni Shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina, lilisema licha ya changamoto zilizopo wafanyakazi wake wa misaada huko Gaza wanaendelea kufanyakazi, wakitoa msaada kwa zaidi ya watu 600,000 ambao wamesaka hifadhi katika makaazi ya UNRWA, ambayo sasa yamefurika mara tatu zaidi ya uwezo."Wafanyakazi hao ni taswira ya ubinadamu katika wakati huu wa jinamizi kubwa” limesongeza shirika hilo.Jana Jumapili shirika hilo lilifanya ibada maalum ya kumbukumbu kwa wafanyakazi wake 59 waliouawa katika mzozo huu hadi sasa na mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres alisisitiza akitoa "shukrani, mshikamano na msaada wake kamili kwa wafanyakazi wenzake hao wanaofanya kazi kuokoa maisha huko Gaza huku wakihatarisha maisha yao.Idadi ya wanaokufa inaongezeka: Hadi kufikia jana Jumapili jioni idadi ya waliofariki dunia Gaza tangu tarehe 7 Oktoba ilifika zaidi ya watu  8,000, kulingana na takwimu za wizara ya afya inayoendeshwa na Hamas huko Gaza.Kwa mujibu wa mamlaka ya Israel, Waisraeli 239 na raia wa kigeni, wakiwemo watoto 30, wamesalia mateka huko Gaza na watu 40 bado wanaripotiwa kutoweka kufuatia mashambulizi ya kigaidi ya Hamas dhidi ya Israel yaliyofanyika tarehe 7 Oktoba.OCHA imesema jana Jumapili "angalau kulikuwa na mlori 33 yaliyokuwa yamebeba maji, chakula, na vifaa vya matibabu yaliingia Gaza kupitia kivuko cha Rafah na Misri, ikiwa ni idadi kubwa zaidi yangu kuanza tena kwa msafara mdogo wa misaada tena tarehe 21 Oktoba."Wakati ongezeko hili linakaribishwa, kiasi kikubwa zaidi cha misaada kinahitajika mara kwa mara ili kuzuia kuzorota zaidi kwa hali mbaya ya kibinadamu, ikiwa ni pamoja na machafuko ya wenyewe kwa wenyewe," OCHA imesisitiza. Kabla ya shambulio la Oktoba 7 la Hamas, karibu malori 500 kwa siku yaliripotiwa kuingia Gaza.Mwishoni mwa wiki huku kukiwa na onyo…
10/30/20230
Episode Artwork

Huduma za Posta zisienguliwe kwenye uwekezaji – UPU

Uwekezaji kwenye huduma za posta hasa katika nchi zinazoendelea kama zile za barani Afrika husalia nyuma kutokana na huduma hiyo kutopatiwa kipaumbele sana katikati ya changamoto kama vile afya, elimu, chakula, mabadiliko ya tabianchi. Hali hiyo husababisha huduma za posta kukosa ufadhili unaotakiwa, amesema Mutua Muthusi Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika la posta duniani, UPU katika mahojiano yake na Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa. Bwana Muthusi anasema mizani ya huduma zinazohitajika kwa njia moja au nyingine huacha posta nyuma, licha ya kwamba huduma hiyo ilionekana umuhimu wake wakati wa janga la COVID-19. Je ni kwa vipi, na nini kifanyike kuhakikisha uwekezaji unakuwa wa kutosha na posta ichangie kwenye maendeleo endelevu zama za sasa za maendeleo ya kidijitali? Bwana Muthusi anaanza kwa kuelezea changamoto zinazokumba huduma za posta katika nchi zinazoendelea.  (H4) NB: Mahojiano haya yamefanikishwa na Kayla Redstone wa UPU. 
10/27/20230
Episode Artwork

UN: Pande husika sitisheni huhasama, janga kubwa zaidi la kibinadamu laja Gaza

Hali Mashariki ya Kati inazidi kuwa mbayá. Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa leo amezisihi pande zote katika mzozo kusitisha uhasana , huku mashirika ya misaada yakionya kuhusu janga kubwa zaidi la kibinadamu, wakati hapa Makao Makuu kikao cha 10 cha dharura kuhusu mzozo huo wa Mashariki ya Kati kikiendelea leo. Kwa hakika hali si hali kwa mujibu wa Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ambaye ameonya leo kwamba adhabu ya pamoja ni uhalifu wa vita akirejea ombi lake la pande zote katika mzozo kusikiliza wito wa amani na kusitisha mapigano hasa wakati huu idadi ya vifo ikongezeka hususan  Gaza na pia kukiwa na ripoti kwamba sasa majina ya watoto yanaandikwa kwenye mikono yako ili iwe rahisi kuwatambua endapo watauawa.Turk ameitaka Hamas kuwaachilia mara moja mateka bila masharti na kwa Israel kusitisha mara moja adhabu ya pamoja kwa Wapalestina. Pia amesisitiza kwamba kauli za kukashifu Wapalestina zinapaswa kukoma mara moja. Kwa mashirika ya kibinadu leo yote yanaonya kwamba mambo yanakuwa mabaya zaidi Gaza. Mratibu wa mwasuala ya kibinada wa Umoja wa Mataifa kwenye eneo linalokaliwa la Palestina Lynn Hastings akizungumza kutoka mjini Jerusalem amesema malori 74 ya msaada yaliyoruhusiwa kuingia Gaza tangu 21 Oktoba na mengine takriban 8 yanayotarajiwa leo hayatoshelezi mahitaji ukizingatia kwamba kabla ya mzozo wa sasa kulikuwa na malozi 450 yaliyokuwa yanaingia kila siku hivyo ameomba msaada zaidi uingine Gaza.Kwa upande wake Kamishina mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA Philippe Lazzarini amezungumzia idadi ya wanaokufa na hofu ya kuongezeka idadi hiyo kila siku kutokana na mabomu na makombora na pia kwa athari za kuzingirwa Ukanda wa Gaza. Pia ameonya juu ya kukosekana kwa mahitaji ya msingi kama maji, dawa na chakula na amesema idadi ya wafanyakazi wa shirika hilo wanaokufa inaongezeka kufikia leo ni 53.Na mashirika mengine lile la mpango wa chakula duniani WFP limesema limefanikiwa kufikisha asilimia 2 tu ya chakula kinachohitajika huku la afya la Umoja wa Mataifa WHO likisema lita 94,000 za mafuta zinahitajika kila siku kuweza kuendeleza huduma muhimu katika hospital kubwa 12 Gaza na hapa Makao Makuu Kikao cha 10 dharura cha Baraza kuu kinaendelea na kinatarajiwa kupigia kura mswada wa azimio uliowasilishwa na Jordan kuhusu usitishaji uhasama. 
10/27/20230
Episode Artwork

27 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunaangazia hali ya msaada wa kibinadamu katika eneo linalokaliwa na wapaestina Gaza, na wakimbizi wa Sudan. Makala tunamulika huduma za posta katika nchi zinazoendelea hususan barani Afrika hasa wakati huu wa maendeleo ya kidijitali na mashinani tunakupeleka nchini Kenya kusikia ni kwa jinsi gani Umoja wa Mataifa umewasaidia wakulima kuimarisha uhakika wa chakula na kujikwamua kimaisha.Hali Mashariki ya Kati inazidi kuwa mbayá. Mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa leo amezisihi pande zote katika mzozo kusitisha uhasana , huku mashirika ya misaada yakionya kuhusu janga kubwa zaidi la kibinadamu, wakati hapa Makao Makuu kikao cha 10 cha dharura kuhusu mzozo huo wa Mashariki ya Kati kikiendelea leo. Wakati maelfu ya wananchi wakikimbia machafuko nchini Sudan mashirika ya Umoja wa Mataifa nayo yana haha huku na kule kuhakikisha wanatoa usaidizi kwa wakimbizi hao. Katika makala Assumpta Massoi anazungumza na Mutua Muthusi, Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika la posta duniani, UPU kuhusu changamoto na fursa za huduma za posta katika nchi zinazoendelea hususan barani Afrika hasa wakati huu wa maendeleo ya kidijitali.Na mashinani tunakuletea ujumbe wa Everlyne Lagat kutoka Baringo Kaunti nchini Kenya, mmoja wa wakulima wadogo ambao wameweza kuondokana na hatari ya majanga ya njaa na umasikini kwa kuwa Shirika la Umoja Wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani, WFP linanunua chakula cha msaada kutoka kwao Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/27/20230
Episode Artwork

Sikuwa nataka kurejea nchini mwangu Sudan Kusini - Mkimbizi kutoka Sudan

Wakati maelfu ya wananchi wakikimbia machafuko nchini Sudan mashirika ya Umoja wa Mataifa nayo yana haha huku na kule kuhakikisha wanatoa usaidizi kwa wakimbizi hao. Tangu kuibuka kwa mzozo nchini Sudan miezi sita iliyopita, takriban watu milioni 6 wamelazimika kuyakimbia makazi yao wakisaka hifadhi katika nchi jirani zikiwemo Jamhuri ya Afrika ya Kati, Chad, Misri, Ethiopia na Sudan Kusini. Kumekuwa na idadi kubwa ya wakimbizi wa Sudan Kusini ambao walikimbilia Sudan lakini sasa wamamua kurejea katika nchi yao. Mmoja ya watu hao ni Umjuma Achol Mtu mwenye umri wa miaka 26, Mwaka 2016 alikimbia ghasia za kikatili katika kijiji chake cha Bentiu, lakini mgofor unaondelea hivi sasa Sudan umemrejesha Sudan Kusini.“Sikuwa nataka kurejea nyumbani Sudan Kusini kwa sababu ya jinsi tulivyoondoka mwaka 2016. Hali ilikuwa mbaya sana, kumbukumbu bado zinarejea akilini mwangu. Nilikuwa Bentiu vita vilipozuka. Ilitubidi kutembea kilomita 14 kutoka Bentiu hadi Gambella ili kupata usalama. Baadaye tuliishi nchini Sudan.”Ukosefu wa fedha, ufikiaji duni wa watu, na miundombinu duni vinaleta changamoto kubwa kwa mashirika ya Kimataifa kutoa misaada kwa wakimbizi kama anavyoeleza Jimmy Ogwang, Afisa wa Mashinani wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia wakimbizi UNHCR nchini Sudan Kusini.“Mvua imeanza kunyesha, sasa tuna changamoto ya barabara hasa kwa wakimbizi, wataathirika kwa sababu kutakuwa hakupitiki maana eneo hili hufurika wakati mvua inanyesha. Kwa hivyo kuna uwezekano mkubwa wa watu kukaa kwa muda mrefu hapa, na watu wakikaa kwa muda mrefu basi kutakuwa na msongamano.” Timu za UNHCR, zikiwa pamoja na wadau wengine ziko katika vituo vya kuvuka mpaka nchini Sudan Kusini kufuatilia na kuwasaidia wanaowasili hasa wakimbizi wa Sudan Kusini wanaorejea.Wameanzisha vituo kwa ajili ya wasafiri ambapo wahamiaji wapya hupewa chakula, maji na malazi katika makazi ya jumuiya huku wakiwatafutia usafiri wa kuelekea maeneo yao ya nyumbani au maeneo mengine wanayopendelea. UNHCR pia inasaidia familia kuanzisha mawasiliano na jamaa zao ndani ya Sudan Kusini ili waweze kuunganishwa tena.
10/27/20230
Episode Artwork

Methali: MTEGEMEA NUNDU HAACHI KUNONA

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MTEGEMEA NUNDU HAACHI KUNONA.
10/26/20230
Episode Artwork

26 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunakuletea mada kwa kina na leo tunabisha hodi jijini Nairobi nchini Kenya ambako wiki hii kikundi cha wanaharakati wa mazingira cha Mikoko Pamoja kutoka Pwani ya Kenya kimeibuka kidedea na kutwaa tuzo ya Umoja wa Mataifa ya “mtu mahiri wa mwaka.” Pia tunakuletea habari kwa ufupi, na katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MTEGEMEA NUNDU HAACHI KUNONA.Gaza ambako kipindi cha saa 24 cha siku ya 19 ya mapigano kati ya Israeli na kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas kimekuwa kibaya zaidi kwani watu 756 wameuawa Gaza wakiwemo watoto 344 na kufanya idadi ya waliouawa tangu Oktoba 7 kufikia 6,547 kwenye eneo hilo linalokaliwa la wapalestina, imesema Wizara ya Afya inayoongozwa na Hamas. Nalo shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni ,WHO lenyewe linawataka Hamas kutoa hakikisho la hali ya mateka wa kiisraeli wanaoshikiliwa na kundi hilo ikiwemo afya zao na iwapo wanapatiwa huduma za msingi. Hali ya sintofahamu ikiendelea Gaza, hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika kikao cha dharura cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kufuatia ombi la nchi wanachama baada ya harakati za kusaka kupitisha maazimio Baraza la Usalama kuhusu mzozo Mashariki ya Kati kugonga mwamba. Na kwingineko, hii leo huko Tbilisi, Georgia, shirika la Umoja wa Mataifa la mazingira, UNEP na Mfuko wa Tabianchi duniani, GCF wametangaza mradi wa dola milioni 19 utakaotekelezwa mkoani Kigoma nchini Tanzania kwa ajili ya kurejesha mazingira na kujengea mnepo wenyeji na wakimbizi. Mradi utatekelezwa kwa ushirikiano na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR nchini Tanzania.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali MTEGEMEA NUNDU HAACHI KUNONA.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/26/20230
Episode Artwork

UN Women: Mzozo wa Mashariki ya Kati ni jinamizi kwa wanawake na wasichana

Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati baina ya kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas na Israel kwa siku 18 sasa umesababisha jinamizi kubwa kwa maelfu ya wanawake na wasichana limesema shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya wanawake UN Women.Milio ya makombora na risasi vimekuwa vikitawala Gaza, watu kwa maelfu wakipoteza maisha na wengine kulazimika kuwa wakimbizi wa ndani. Akizungumza na Idhaa ya Kiarabu ya Umoja wa Mataifa Sarah Hendriks naibu mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya wanawake UN Women Sara Hendricks amesema miongoni mwa waathirika wakubwa ni wanawake na wasichana na ni kutoka pande zote za mzozo.Amesema  hali ni mbayá "Kwa kweli huu ni wakati wa giza na mgumu sana. Ni mzozo mkubwa tofauti na wowote ambao eneo hili limewahi kushuhudia katika miongo kadhaa. Tunasikitishwa sana na athari zake kwa maisha ya wanawake na wasichana. Ni wazi kwamba wengi sana tayari wamepoteza maisha au wapendwa wao.” Sara amesema ili kuepusha madhila zaidi kwa wasichana na wanawake hawa UN Women iko msatari wa mbele kuwasaidia kwa kila hali na pia “Wito wa UN women umekuwa ni kuhakikisha ulinzi kwa wanawake na wasichan Israel na eneo linalokaliwa la Palestina na kuhakikisha vita vinasitishwa mara moja kwa sababu za kibinadamu. Kuendelea kwa machafuko haya na athari zake kutaleta hatari za kijinsia kwa wanawake kwenye Ukanda wa Gaza.”Amezitaja hatari hizo kuwa ni pamoja na idadi kubwa ya vifo, ongezeko la wajane, hofu ya ukatili wa kijinsia  na kaya nyingi kuendeshwa na wanawake pekee .Sara amesema suluhu pekee ni Amani”Kinachohitajika ni usitishwaji haráka uhasama kwa minajili ya amasuala ya kinidamu, fursa ya bila vikwazo kuingiza misaada ya kibinadamu ikijumuisha mahitaji ya msingi kwa kila kaya, kwa kila maisha chakula, maji, vifaa vya nyumbani na hususani mafuta, ni muhimu kwa Maisha ya wanawake na wasichana kwenye Ukanda wa Gaza.”Amesisitiza kuwa kinachowakabili wanawake na wasicha hawa lazima kiwe kitovu cha suluhu“Ni muhimu sana kwa kipaumbele cha wanawake na wasichana wakati hali hii ikiendelea kieleweke vyema, na ndio sababu UN Women imetoa muhtasari unaotathimini haraka hali ya kijinsia katika mzozo wa sasa.”Afisa huyo wa UN Women amesema kwa muda mrefu kumekuwa na wanawake wanaharakati Gaza ambao kazi yao kubwa ilikuwa ni kusaidia masuala ya kibinadamu kwa wanawake wenzao lakini sasa ukurasa umepinduliwa “Mambo yamebadilika kwa wanawake ambao walikuwa wanaharakati wa kuchagiza hatua za kibinadamu kwa misingi ya kijinsia kwani sasa wamejikuta ni walengwa wa hatua hizo za kibinadamu .” Licha ya changamoto zinazoendelea kwa wanawake hao wa Mashariki ya Kati Sarah ameahidi kwamba UN women haitowapa kisogo wanawake hao “Tutaendelea kusalia hapokusikiliza sauti za wanawake na wasichana, kusikiliza mtazamo wao na kuuwasilisha kwenye jumuiya ya kimataifa ili mahitaji yao yapewe kipaumbele hata wakati suluhu ya mzozo mzima ikiwa inashughulikiwa.”
10/25/20230
Episode Artwork

UN Women: Mzozo wa Mashariki ya Kati ni jinamizi kwa wanawake na wasichana

Mzozo unaoendelea Mashariki ya Kati baina ya kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas na Israel kwa siku 18 sasa umesababisha jinamizi kubwa kwa maelfu ya wanawake na wasichana limesema shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya wanawake UN Women.Milio ya makombora na risasi vimekuwa vikitawala Gaza, watu kwa maelfu wakipoteza maisha na wengine kulazimika kuwa wakimbizi wa ndani. Akizungumza na Idhaa ya Kiarabu ya Umoja wa Mataifa Sarah Hendriks naibu mkurugenzi mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya wanawake UN Women Sara Hendricks amesema miongoni mwa waathirika wakubwa ni wanawake na wasichana na ni kutoka pande zote za mzozo.Amesema  hali ni mbayá "Kwa kweli huu ni wakati wa giza na mgumu sana. Ni mzozo mkubwa tofauti na wowote ambao eneo hili limewahi kushuhudia katika miongo kadhaa. Tunasikitishwa sana na athari zake kwa maisha ya wanawake na wasichana. Ni wazi kwamba wengi sana tayari wamepoteza maisha au wapendwa wao.” Sara amesema ili kuepusha madhila zaidi kwa wasichana na wanawake hawa UN Women iko msatari wa mbele kuwasaidia kwa kila hali na pia “Wito wa UN women umekuwa ni kuhakikisha ulinzi kwa wanawake na wasichan Israel na eneo linalokaliwa la Palestina na kuhakikisha vita vinasitishwa mara moja kwa sababu za kibinadamu. Kuendelea kwa machafuko haya na athari zake kutaleta hatari za kijinsia kwa wanawake kwenye Ukanda wa Gaza.”Amezitaja hatari hizo kuwa ni pamoja na idadi kubwa ya vifo, ongezeko la wajane, hofu ya ukatili wa kijinsia  na kaya nyingi kuendeshwa na wanawake pekee .Sara amesema suluhu pekee ni Amani”Kinachohitajika ni usitishwaji haráka uhasama kwa minajili ya amasuala ya kinidamu, fursa ya bila vikwazo kuingiza misaada ya kibinadamu ikijumuisha mahitaji ya msingi kwa kila kaya, kwa kila maisha chakula, maji, vifaa vya nyumbani na hususani mafuta, ni muhimu kwa Maisha ya wanawake na wasichana kwenye Ukanda wa Gaza.”Amesisitiza kuwa kinachowakabili wanawake na wasicha hawa lazima kiwe kitovu cha suluhu“Ni muhimu sana kwa kipaumbele cha wanawake na wasichana wakati hali hii ikiendelea kieleweke vyema, na ndio sababu UN Women imetoa muhtasari unaotathimini haraka hali ya kijinsia katika mzozo wa sasa.”Afisa huyo wa UN Women amesema kwa muda mrefu kumekuwa na wanawake wanaharakati Gaza ambao kazi yao kubwa ilikuwa ni kusaidia masuala ya kibinadamu kwa wanawake wenzao lakini sasa ukurasa umepinduliwa “Mambo yamebadilika kwa wanawake ambao walikuwa wanaharakati wa kuchagiza hatua za kibinadamu kwa misingi ya kijinsia kwani sasa wamejikuta ni walengwa wa hatua hizo za kibinadamu .” Licha ya changamoto zinazoendelea kwa wanawake hao wa Mashariki ya Kati Sarah ameahidi kwamba UN women haitowapa kisogo wanawake hao “Tutaendelea kusalia hapokusikiliza sauti za wanawake na wasichana, kusikiliza mtazamo wao na kuuwasilisha kwenye jumuiya ya kimataifa ili mahitaji yao yapewe kipaumbele hata wakati suluhu ya mzozo mzima ikiwa inashughulikiwa.”
10/25/20230
Episode Artwork

Guterres: Mzozo wa Mashariki ya Kati sipendelei upande wowote

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres hii leo amezungumza na waandishi wa Habari hapa kwenye makao makuu ya Umoja huo muda mfupi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake na amani na usalama. Asante Assumpta, Katibu Mkuu Guterres amezungumza na waandishi wa habari asubuhi ya leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani ambapo jambo la kwanza alilosema pindi alipofika mbele ya vyombo vya habari ni kuwa ……. Ameshtushwa na taarifa za upotoshaji za baadhi ya kauli alizozitoa hapo jana Katika mkutano wa Baraza la Usalama uliojadili kuhusu mzozo unaoendelea huko mashariki ya kati. Guterres amesema taarifa hizo za upotoshaji zinaonesha kana kwamba alikuwa akihalalisha vitendo vya kigaidi vilivyo fanywa na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas.Guterres amesema “Huu ni uongo, na ilikuwa kinyume chake. “amenukuu taarifa yake akisema…. “Nimelaani bila shaka, vitendo vya kutisha na visivyo na kifani vya Oktoba 7 vya Hamas nchini Israel. Hakuna kinachoweza kuhalalisha mauaji ya makusudi, kujeruhi na kutekwa nyara raia au kurusha roketi kuwalenga raia.”Katika tarifa  yake ya jana pia amesema alizungumzia malalamiko ya WaPalestina na ananukuu alichosem…. “Lakini malalamiko ya watu wa Palestina hayawezi kuhalalisha mashambulizi ya kutisha ya Hamas na kisha niliendelea na namna nilivyoingilia mgogoro huo nikimaanisha misimamo yangu yote juu ya nyanja zote za mzozo wa Mashariki ya Kati.” Guterres amehitimisha taarifa yake hiyo fupi ya dakika moja akisema “Ninaamini nilihitajika kuweka kumbukumbu sawa, hasa kwa heshima ya waathiriwa na familia zao.”
10/25/20230
Episode Artwork

Guterres: Mzozo wa Mashariki ya Kati sipendelei upande wowote

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres hii leo amezungumza na waandishi wa Habari hapa kwenye makao makuu ya Umoja huo muda mfupi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake na amani na usalama. Asante Assumpta, Katibu Mkuu Guterres amezungumza na waandishi wa habari asubuhi ya leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani ambapo jambo la kwanza alilosema pindi alipofika mbele ya vyombo vya habari ni kuwa ……. Ameshtushwa na taarifa za upotoshaji za baadhi ya kauli alizozitoa hapo jana Katika mkutano wa Baraza la Usalama uliojadili kuhusu mzozo unaoendelea huko mashariki ya kati. Guterres amesema taarifa hizo za upotoshaji zinaonesha kana kwamba alikuwa akihalalisha vitendo vya kigaidi vilivyo fanywa na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas.Guterres amesema “Huu ni uongo, na ilikuwa kinyume chake. “amenukuu taarifa yake akisema…. “Nimelaani bila shaka, vitendo vya kutisha na visivyo na kifani vya Oktoba 7 vya Hamas nchini Israel. Hakuna kinachoweza kuhalalisha mauaji ya makusudi, kujeruhi na kutekwa nyara raia au kurusha roketi kuwalenga raia.”Katika tarifa  yake ya jana pia amesema alizungumzia malalamiko ya WaPalestina na ananukuu alichosem…. “Lakini malalamiko ya watu wa Palestina hayawezi kuhalalisha mashambulizi ya kutisha ya Hamas na kisha niliendelea na namna nilivyoingilia mgogoro huo nikimaanisha misimamo yangu yote juu ya nyanja zote za mzozo wa Mashariki ya Kati.” Guterres amehitimisha taarifa yake hiyo fupi ya dakika moja akisema “Ninaamini nilihitajika kuweka kumbukumbu sawa, hasa kwa heshima ya waathiriwa na familia zao.”
10/25/20230
Episode Artwork

25 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati, na kazi za walinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, kulikoni?Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres hii leo amezungumza na waandishi wa Habari hapa kwenye makao makuu ya Umoja huo muda mfupi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake na amani na usalama. Mwezi huu wa Oktoba ikiwa ni miaka 23 tangu kupitishwa kwa azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake katika harakati za amani na usalama ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kusikia jinsi ujumuishaji wa wanawake walinda amani kwenye kikosi cha India kinachohudumu kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo (MONUSCO) kumeleta matumaini kwa wanawake. Na katika makala Flora Nducha anatupeleka Ukanda wa Gaza huko Mashariki ya Kati ambako kunaendelea mzozo baina ya kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas na Israel na anamulika jinsi mzozo huo unavyowaathiri wanawake na wasichana.Mashinani tunamsikiliza mkazi mmoja kutoka mji wa Sange, jimboni Kivu Kusini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC akielezea ni kwa jinsi gani uwepo kwa walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Pakistani wanaohudumu kwenye ujumbe wa umoja huo wa kulinda amani nchini humo MONUSCO ulivyosaidia kuleta amani katika eneo hilo. Akisema Absence anamaanisha kutokuweko.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/25/20230
Episode Artwork

25 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati, na kazi za walinda amani wa Umoja wa Mataifa nchini DRC, kulikoni?Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres hii leo amezungumza na waandishi wa Habari hapa kwenye makao makuu ya Umoja huo muda mfupi kabla ya kuanza kwa kikao cha Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake na amani na usalama. Mwezi huu wa Oktoba ikiwa ni miaka 23 tangu kupitishwa kwa azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake katika harakati za amani na usalama ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kusikia jinsi ujumuishaji wa wanawake walinda amani kwenye kikosi cha India kinachohudumu kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo (MONUSCO) kumeleta matumaini kwa wanawake. Na katika makala Flora Nducha anatupeleka Ukanda wa Gaza huko Mashariki ya Kati ambako kunaendelea mzozo baina ya kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas na Israel na anamulika jinsi mzozo huo unavyowaathiri wanawake na wasichana.Mashinani tunamsikiliza mkazi mmoja kutoka mji wa Sange, jimboni Kivu Kusini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC akielezea ni kwa jinsi gani uwepo kwa walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Pakistani wanaohudumu kwenye ujumbe wa umoja huo wa kulinda amani nchini humo MONUSCO ulivyosaidia kuleta amani katika eneo hilo. Akisema Absence anamaanisha kutokuweko.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/25/20230
Episode Artwork

Wanawake kwenye INDIBAT-1 waleta matumaini kwa wanawake Nchini DRC

Mwezi huu wa Oktoba ikiwa ni miaka 23 tangu kupitishwa kwa azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake katika harakati za amani na usalama ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kusikia jinsi ujumuishaji wa wanawake walinda amani kwenye kikosi cha India kinachohudumu kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo (MONUSCO) kumeleta matumaini kwa wanawake. Sauti hiyo ya Meja Rhandika. Yeye ni Kiongozi la kikosi cha wanawake ndani ya INDIBAT-1 [INDIBAT WAN] ambacho ni kikosi cha India ndani ya MONUSCO kinachohudumu eneo la Rwindi  huko Rutshuru jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC. Anasema kupelekwa kufanya kazi kwenye eneo jipya mara nyingi kuna changamoto. Lakini pindi unaposhirikiana na wenyeji inakuwa ni rahisi. Kupitia video ya MONUSCO, Meja Virendra Rathore Mkuu wa INDIBAT-1 anasema walipofika Rwindi baada ya muda, ilibainika kuwa baadhi ya masuala kadhaa ya jamii zilizoathiriwa na mapigano yanayoendelea kwenye eneo hilo, hususan wanawake yalikuwa hayajashughulikiwa. Uwepo wa kikundi cha walinda amani wanawake ndani kikosi hicho ukawa ni jawabu, kama asemavyo Meja Rhandika Kamanda wa kikosi cha wanawake INDIBAT-1. “Katika siku chache zilizopita, timu yangu imekutana na wanajamii hususan viongozi wa wanawake kujadili masuala hasa hofu kuhusu usalama na tumeimarisha juhudi zetu kuwapatia hakikisho la usalama kwa wanawake. Tumefanya doria kadhaa kwenye eneo kudhihirisha uwepo wa wanawake walinda amani na ilionekana kwamba wanawake waliweze kujieleza dhahiri kuhusu matatizo yao. “ Mmoja wa wanawake viongozi kwenye eneo la Kibirizi  hapa Rutshuru akaelezea furaha yake. “Sasa mimi nafurahi kuona mama msimamizi wa MONUSCO ambaye tutakuwa tunampatia malalamiko yetu hapa. Na tunakuwa na matumaini kwamba kadri tutaendelea kuhusiana naye tunaweza kupata majawabu ya shida zinazotukabili. Tunashukuru.” Na ndipo Meja Rhandika anatamatisha kwa kusema ,"Watu wa DRC wametukaribisha vema,  na kuelezea shukrani yao kwa MONUSCO kwa kuleta walinda amani wanawake kwenye eneo hili. "Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mapigano mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, hususan jimboni Kivu Kaskazini yamefurusha watu 410,000 tangu mwanzo wa mwaka huu wa 2023. 
10/25/20230
Episode Artwork

Wanawake kwenye INDIBAT-1 waleta matumaini kwa wanawake Nchini DRC

Mwezi huu wa Oktoba ikiwa ni miaka 23 tangu kupitishwa kwa azimio namba 1325 la Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa kuhusu wanawake katika harakati za amani na usalama ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kusikia jinsi ujumuishaji wa wanawake walinda amani kwenye kikosi cha India kinachohudumu kwenye ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo (MONUSCO) kumeleta matumaini kwa wanawake. Sauti hiyo ya Meja Rhandika. Yeye ni Kiongozi la kikosi cha wanawake ndani ya INDIBAT-1 [INDIBAT WAN] ambacho ni kikosi cha India ndani ya MONUSCO kinachohudumu eneo la Rwindi  huko Rutshuru jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC. Anasema kupelekwa kufanya kazi kwenye eneo jipya mara nyingi kuna changamoto. Lakini pindi unaposhirikiana na wenyeji inakuwa ni rahisi. Kupitia video ya MONUSCO, Meja Virendra Rathore Mkuu wa INDIBAT-1 anasema walipofika Rwindi baada ya muda, ilibainika kuwa baadhi ya masuala kadhaa ya jamii zilizoathiriwa na mapigano yanayoendelea kwenye eneo hilo, hususan wanawake yalikuwa hayajashughulikiwa. Uwepo wa kikundi cha walinda amani wanawake ndani kikosi hicho ukawa ni jawabu, kama asemavyo Meja Rhandika Kamanda wa kikosi cha wanawake INDIBAT-1. “Katika siku chache zilizopita, timu yangu imekutana na wanajamii hususan viongozi wa wanawake kujadili masuala hasa hofu kuhusu usalama na tumeimarisha juhudi zetu kuwapatia hakikisho la usalama kwa wanawake. Tumefanya doria kadhaa kwenye eneo kudhihirisha uwepo wa wanawake walinda amani na ilionekana kwamba wanawake waliweze kujieleza dhahiri kuhusu matatizo yao. “ Mmoja wa wanawake viongozi kwenye eneo la Kibirizi  hapa Rutshuru akaelezea furaha yake. “Sasa mimi nafurahi kuona mama msimamizi wa MONUSCO ambaye tutakuwa tunampatia malalamiko yetu hapa. Na tunakuwa na matumaini kwamba kadri tutaendelea kuhusiana naye tunaweza kupata majawabu ya shida zinazotukabili. Tunashukuru.” Na ndipo Meja Rhandika anatamatisha kwa kusema ,"Watu wa DRC wametukaribisha vema,  na kuelezea shukrani yao kwa MONUSCO kwa kuleta walinda amani wanawake kwenye eneo hili. "Kwa mujibu wa Umoja wa Mataifa, mapigano mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, hususan jimboni Kivu Kaskazini yamefurusha watu 410,000 tangu mwanzo wa mwaka huu wa 2023. 
10/25/20230
Episode Artwork

24 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo leo ni siku ya Umoja wa Mataifa, chombo kilichoanzishwa mwaka 1945 baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia ikiwa na wanachama waanzilishi 51, bara la Afrika likiwa na nchi nne tu ambazo ni Misri, Liberia, Ethiopia na Afrika Kusini enzi hizo ikijulikana kama Muungano wa Afrika Kusini. Kwa mujibu wa Chata iliyoanzisha chombo hicho, lengo ni kuendeleza amani na usalama duniani, kusongesha uhusiano wa kirafiki baina ya nchi, kufanikisha ushirikiano wa kimataifa na kuwa kitovu cha kuratibu vitendo vya mataifa. Dkt. Kaanaeli Kaale, Mhadhiri Msaidizi katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino, SAUT nchini Tanzania, na pia Mtaalamu wa Mawasiliano ya Kimataifa anaeleza iwapo malengo ya kuanzishwa bado yana mantiki. Pia tunakuletea habari kwa ufupi, na mashinani ambapo tunasikiliza ujumbe wa Katibu Mkuu kuhusu siku ya UN.Ni siku ya 17 ya kuendelea mzozo wa karibuni baina ya Israel na kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas huko Mashariki ya Kati Masharikika ya Umoja wa Mataifa yameendelea na kilio cha kuongeza misaada zaidi kuingia Gaza kwani iliyowasili hadi sasa haikidhi mahitaji.Leo ni siku ya Umoja wa Mataifa inaadhimishwa kumbukumbu ya kuanza kutumika kwa chata iliyoanzisha Umoja huo mwaka 1945. Katika ujumbe wake wa siku hii Clementine Nkweta-Salami naibu mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan na kaimu mratibu mkazi na wa masuala ya kibinadamu amesema “Mwaka huu tunaadhimisha siku hii wakati Sudan ikikabiliwa na moja ya mgogoro  wa kibinadamu unaokuwa kwa kasi ukiambatana na mahitaji makubwa. Mapigano yamegeuza mgogoro huo kuwa janga kubwa. Zaidi ya watu milioni 5.6 wamefurushwa makwao, milioni 25 wanahitaji msaada, zaidi ya wanawake na wasichana milioni 4.2 wako katika hatari ya ukajtili wa kijinsia na mtoto 1 kati ya 3 hana fursa ya kwenda shule. Na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF limesema theluthi mbili ya watoto wakimbizi nchini Armenia wameandikiswa katika mifumo ya kitaifa ya shule mwezi mmoja baada ya watoto 21, 000 wenye umri wa kwenda shule kukimbia makwao. UNICEF imesema sasa juhudi ni kuhakikisha watoto walioasalia 1 kati ya 3 ambao hawahudhurii shule wanapata fursa hiyo.Na katika mashinani tunasalia katika siku ya Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa chombo hicho anazungumzia nafasi ya kila mtu katika kusongesha malengo ya Umoja wa Mataifa.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/24/20230
Episode Artwork

24 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo leo ni siku ya Umoja wa Mataifa, chombo kilichoanzishwa mwaka 1945 baada ya Vita Kuu ya Pili ya Dunia ikiwa na wanachama waanzilishi 51, bara la Afrika likiwa na nchi nne tu ambazo ni Misri, Liberia, Ethiopia na Afrika Kusini enzi hizo ikijulikana kama Muungano wa Afrika Kusini. Kwa mujibu wa Chata iliyoanzisha chombo hicho, lengo ni kuendeleza amani na usalama duniani, kusongesha uhusiano wa kirafiki baina ya nchi, kufanikisha ushirikiano wa kimataifa na kuwa kitovu cha kuratibu vitendo vya mataifa. Dkt. Kaanaeli Kaale, Mhadhiri Msaidizi katika Chuo Kikuu cha Mtakatifu Augustino, SAUT nchini Tanzania, na pia Mtaalamu wa Mawasiliano ya Kimataifa anaeleza iwapo malengo ya kuanzishwa bado yana mantiki. Pia tunakuletea habari kwa ufupi, na mashinani ambapo tunasikiliza ujumbe wa Katibu Mkuu kuhusu siku ya UN.Ni siku ya 17 ya kuendelea mzozo wa karibuni baina ya Israel na kundi la wanamgambo wa Kipalestina la Hamas huko Mashariki ya Kati Masharikika ya Umoja wa Mataifa yameendelea na kilio cha kuongeza misaada zaidi kuingia Gaza kwani iliyowasili hadi sasa haikidhi mahitaji.Leo ni siku ya Umoja wa Mataifa inaadhimishwa kumbukumbu ya kuanza kutumika kwa chata iliyoanzisha Umoja huo mwaka 1945. Katika ujumbe wake wa siku hii Clementine Nkweta-Salami naibu mwakilishi wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan na kaimu mratibu mkazi na wa masuala ya kibinadamu amesema “Mwaka huu tunaadhimisha siku hii wakati Sudan ikikabiliwa na moja ya mgogoro  wa kibinadamu unaokuwa kwa kasi ukiambatana na mahitaji makubwa. Mapigano yamegeuza mgogoro huo kuwa janga kubwa. Zaidi ya watu milioni 5.6 wamefurushwa makwao, milioni 25 wanahitaji msaada, zaidi ya wanawake na wasichana milioni 4.2 wako katika hatari ya ukajtili wa kijinsia na mtoto 1 kati ya 3 hana fursa ya kwenda shule. Na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF limesema theluthi mbili ya watoto wakimbizi nchini Armenia wameandikiswa katika mifumo ya kitaifa ya shule mwezi mmoja baada ya watoto 21, 000 wenye umri wa kwenda shule kukimbia makwao. UNICEF imesema sasa juhudi ni kuhakikisha watoto walioasalia 1 kati ya 3 ambao hawahudhurii shule wanapata fursa hiyo.Na katika mashinani tunasalia katika siku ya Umoja wa Mataifa, Antonio Guterres, Katibu Mkuu wa chombo hicho anazungumzia nafasi ya kila mtu katika kusongesha malengo ya Umoja wa Mataifa.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/24/20230
Episode Artwork

Mshtakiwa ana haki ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa na hatia – Ibara 11

“Kila mtu aliyehukumiwa kwa kosa la adhabu ana haki ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa ana hatia kwa mujibu wa sheria katika kesi ya hadhara ambapo amekuwa na dhamana zote zinazohitajika kwa ajili ya utetezi wake, na Hakuna mtu atakayepatikana na hatia ya kosa lolote la adhabu kwa sababu ya kitendo au kutotenda jambo ambalo halikuwa ni kosa la adhabu, chini ya sheria ya kitaifa au kimataifa, wakati lilipotendwa, wala haitatolewa adhabu kubwa kuliko ile ambayo ilitumika wakati kosa la adhabu lilipotendwa.” Linasema tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, na Je Ibara hii ina maanisha nini ? na inatekelezwa? Ili kupata majibu hayo Pamela Awuori wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Wakili Fridah Jausiku wa mahakama kuu ya Kenya anayeanza kwa kufafanua haki za mshtakiwa nchini humo....
10/23/20230
Episode Artwork

Mshtakiwa ana haki ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa na hatia – Ibara 11

“Kila mtu aliyehukumiwa kwa kosa la adhabu ana haki ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa ana hatia kwa mujibu wa sheria katika kesi ya hadhara ambapo amekuwa na dhamana zote zinazohitajika kwa ajili ya utetezi wake, na Hakuna mtu atakayepatikana na hatia ya kosa lolote la adhabu kwa sababu ya kitendo au kutotenda jambo ambalo halikuwa ni kosa la adhabu, chini ya sheria ya kitaifa au kimataifa, wakati lilipotendwa, wala haitatolewa adhabu kubwa kuliko ile ambayo ilitumika wakati kosa la adhabu lilipotendwa.” Linasema tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, na Je Ibara hii ina maanisha nini ? na inatekelezwa? Ili kupata majibu hayo Pamela Awuori wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Wakili Fridah Jausiku wa mahakama kuu ya Kenya anayeanza kwa kufafanua haki za mshtakiwa nchini humo....
10/23/20230
Episode Artwork

23 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati na tetemeko la ardhi nchini Afghanistan. Makala tuanakupeleka nchini Kenya na mashinani nchini Tanzania, kulikoni?Wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu wamesihi wanasheria wanaoishauri serikali ya Israeli inayoendelea na mashambulizi dhidi ya wanamgambo wa kipalestina Hamas huko Ukanda wa Gaza, wakatae kuidhinisha kisheria vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita. Kulikoni?Nchi ya Afghanistan hivi karibuni imekumbwa na matetemeko makubwa ya ardhi na kusababisha watu kupoteza maisha pamoja na uharibifu mkubwa. Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP linasema hadi kufikia Oktoba 14, zaidi ya watu 19,250 waliathirika na matetemeko katika jimbo la Herat. Makala tunaendelea na mwendelezo wa chambuzi wa tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, leo tunabisha hodi nchini Kenya ambapo Pamela Awuori wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Fridah Jausiku, Wakili wa Mahakama Kuu ya Kenya, kufafanua Ibara ya 11 ya tamko hilo inayotaka kila mtu aliyehukumiwa kwa kosa la adhabu kupatiwa haki yake ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa na hatia.Na katika mashinani tutaelekea nchini Tanzania kufuatilia ni kwa vipi huduma za afya kwa wote zinahakikishwa husuani za magonjwa yasiyoambukizwa.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
10/23/20230
Episode Artwork

23 OKTOBA 2023

Hii leojaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati na tetemeko la ardhi nchini Afghanistan. Makala tuanakupeleka nchini Kenya na mashinani nchini Tanzania, kulikoni?Wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu wamesihi wanasheria wanaoishauri serikali ya Israeli inayoendelea na mashambulizi dhidi ya wanamgambo wa kipalestina Hamas huko Ukanda wa Gaza, wakatae kuidhinisha kisheria vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita. Kulikoni?Nchi ya Afghanistan hivi karibuni imekumbwa na matetemeko makubwa ya ardhi na kusababisha watu kupoteza maisha pamoja na uharibifu mkubwa. Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP linasema hadi kufikia Oktoba 14, zaidi ya watu 19,250 waliathirika na matetemeko katika jimbo la Herat. Makala tunaendelea na mwendelezo wa chambuzi wa tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, leo tunabisha hodi nchini Kenya ambapo Pamela Awuori wa idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Fridah Jausiku, Wakili wa Mahakama Kuu ya Kenya, kufafanua Ibara ya 11 ya tamko hilo inayotaka kila mtu aliyehukumiwa kwa kosa la adhabu kupatiwa haki yake ya kuhesabiwa kuwa hana hatia hadi athibitishwe kuwa na hatia.Na katika mashinani tutaelekea nchini Tanzania kufuatilia ni kwa vipi huduma za afya kwa wote zinahakikishwa husuani za magonjwa yasiyoambukizwa.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
10/23/20230
Episode Artwork

UNDP inahaha kuwasaidia waathirika wa matetemeko ya ardhi Afghanistan

Nchi ya Afghanistan hivi karibuni imekumbwa na matetemeko makubwa ya ardhi na kusababisha watu kupoteza maisha pamoja na uharibifu mkubwa. Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP linasema hadi kufikia Oktoba 14, zaidi ya watu 19,250 waliathirika na matetemeko katika jimbo la Herat. Video ya Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP inaanza kwa kuonesha taswira kutoka angani ambapo ni eneo kubwa la wazi likionekana kama makazi ya watu, lakini video hiyo ikiendelea, taswira inabadilika ardhini si nyumba tena bali vifusi kimejirundika pamoja na maghofu. Haya ni madhara ya matetemeko ya ardhi kadhaa katika jimbo hili la Herat ambapo takribani watu 20,000 wameathirika, asilimia 90 kati yao wakiwa ni wanawake na watoto. Manusura wanajaribu kuokoteza chochote kile kinachoweza kupatikana baada ya tetemeko, wengine wakiokote sinia, wengine spika na wengine wakiondoka na vifurushi kwenye viroba kwani ndivyo walivyoweza kupata. Kamera inamuonesha bibi huyu aitwaye Reza Gul akiangalia mabaki ya iliyokuwa nyumba yake, machozi yakimtoka, anasimulia hali ilivyokuwa, “Ilikuwa saa 11 alfajiri. Sote tulikuwa tumeketi pamoja tunakunywa chai. Nilitoka nje ya nyumba ili kuangalia kondoo. Ghafla, nikasikia mngurumo wa sauti na nikaanguka chini. Mkwe wangu mmoja alikimbia nje wakati paa likiporomoka. Mkwe wangu mwingine na watu wengine wote wa familia yangu walikuwa bado ndani”.Mwingine ni Bi. Mahzada, akiwa anapanga baadhi ya vitu vyake nje ya iliyokuwa nyumba yake sasa ni kifusi, anasema, “Hakuna kitu ndugu, tuko gizani, hakuna kitu. Hatuna taa, hatuna nyumba, hatuna maisha, tumekuwa watu wa kutanga-tanga. Tuko hai lakini tuko gizani, hatuna taa, hatuna nishati ya umeme wa jua na tunaishi gizani.”Mwakilishi mkazi wa UNDP nchini Afghanistan Stephen Rodrigues akiwa ameambatana na maafisa wengine wametembelea jimboni Herat na kuzungumza na wananchi walioathirika. “Tumewaona wanawake na watoto wengi wakiishi kwenye mahema, na hiyo ndiyo hali ya kijiji hiki hivi sasa, na vijiji vingine vingi kama hivi katika eneo lote la Herat. Watu wanauhitaji sana wa makazi kwani msimu wa baridi unakuja”.UNDP imetangaza kutenga dola milioni 1.5 kama hatua ya awali ya kusaidia juhudi za haraka za misaada na mipango ya kuokoa maisha. Pamoja na mambo mengine fedha hizo zitasaidia katika ujenzi wa nyumba mpya na nishati mbadala kwa jamii zilizoathiriwa na matetemeko ya ardhi.
10/23/20230
Episode Artwork

UNDP inahaha kuwasaidia waathirika wa matetemeko ya ardhi Afghanistan

Nchi ya Afghanistan hivi karibuni imekumbwa na matetemeko makubwa ya ardhi na kusababisha watu kupoteza maisha pamoja na uharibifu mkubwa. Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP linasema hadi kufikia Oktoba 14, zaidi ya watu 19,250 waliathirika na matetemeko katika jimbo la Herat. Video ya Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa maendeleo UNDP inaanza kwa kuonesha taswira kutoka angani ambapo ni eneo kubwa la wazi likionekana kama makazi ya watu, lakini video hiyo ikiendelea, taswira inabadilika ardhini si nyumba tena bali vifusi kimejirundika pamoja na maghofu. Haya ni madhara ya matetemeko ya ardhi kadhaa katika jimbo hili la Herat ambapo takribani watu 20,000 wameathirika, asilimia 90 kati yao wakiwa ni wanawake na watoto. Manusura wanajaribu kuokoteza chochote kile kinachoweza kupatikana baada ya tetemeko, wengine wakiokote sinia, wengine spika na wengine wakiondoka na vifurushi kwenye viroba kwani ndivyo walivyoweza kupata. Kamera inamuonesha bibi huyu aitwaye Reza Gul akiangalia mabaki ya iliyokuwa nyumba yake, machozi yakimtoka, anasimulia hali ilivyokuwa, “Ilikuwa saa 11 alfajiri. Sote tulikuwa tumeketi pamoja tunakunywa chai. Nilitoka nje ya nyumba ili kuangalia kondoo. Ghafla, nikasikia mngurumo wa sauti na nikaanguka chini. Mkwe wangu mmoja alikimbia nje wakati paa likiporomoka. Mkwe wangu mwingine na watu wengine wote wa familia yangu walikuwa bado ndani”.Mwingine ni Bi. Mahzada, akiwa anapanga baadhi ya vitu vyake nje ya iliyokuwa nyumba yake sasa ni kifusi, anasema, “Hakuna kitu ndugu, tuko gizani, hakuna kitu. Hatuna taa, hatuna nyumba, hatuna maisha, tumekuwa watu wa kutanga-tanga. Tuko hai lakini tuko gizani, hatuna taa, hatuna nishati ya umeme wa jua na tunaishi gizani.”Mwakilishi mkazi wa UNDP nchini Afghanistan Stephen Rodrigues akiwa ameambatana na maafisa wengine wametembelea jimboni Herat na kuzungumza na wananchi walioathirika. “Tumewaona wanawake na watoto wengi wakiishi kwenye mahema, na hiyo ndiyo hali ya kijiji hiki hivi sasa, na vijiji vingine vingi kama hivi katika eneo lote la Herat. Watu wanauhitaji sana wa makazi kwani msimu wa baridi unakuja”.UNDP imetangaza kutenga dola milioni 1.5 kama hatua ya awali ya kusaidia juhudi za haraka za misaada na mipango ya kuokoa maisha. Pamoja na mambo mengine fedha hizo zitasaidia katika ujenzi wa nyumba mpya na nishati mbadala kwa jamii zilizoathiriwa na matetemeko ya ardhi.
10/23/20230
Episode Artwork

UN: Wanasheria mnaoshauri Israeli muwe makini na ushauri wenu

Wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu wamesihi wanasheria wanaoishauri serikali ya Israeli inayoendelea na mashambulizi dhidi ya wanamgambo wa kipalestina Hamas huko Ukanda wa Gaza, wakatae kuidhinisha kisheria vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita. Msingi wa kauli ya wataalamu hao ni kwamba tangu tarehe 7 mwezi huu wa Oktoba wanamgambo wa Hamas waliposhambulia Israeli, jeshi la ulinzi la Israeli, IDF limekuwa likiripotiwa kuwa linajipanga kuanza uvamizi wa ardhini baada ya kutekeleza mashambulizi ya angani huko Kaskazini mwa Gaza yaliyosababisha vifo vya wapalestina zaidi ya 3,400 na majeruhi 12,000 wakiwemo watoto.  Uvamizi huo wa ardhini inaelezwa ni kulipiza kisasi cha mashambulizi yaliyofanywa na Hamas na wanamgambo wengine wa kipalestina nchini Israeli na kuua raia, halikadhalika  kuteka na kushikilia wengine mateka hadi leo hii.  Wataalamu hao kupitia taarifa yao waliyoitoa hii leo mjini Geneva, Uswisi wanasema bila shaka vitendo vya Hamas dhidi ya raia wa Israeli vilikuwa mauaji.  Lakini sasa mashambulizi ya Israeli yamekuwa yakielekezwa kwenye maeneo yenye makazi ya watu wengi, yakiharibu makazi, hospitali, masoko huku ikizidi kuweka vizuizi na kuzingira Gaza, imekata usambazaji wa vyakula, maji, umeme na mafuta.  Sasa wataalamu wanasema kadri ambavyo Israeli inajibu kitendo cha Hamas na kuendesha operesheni zake Gaza, wanasheria wote wanaoshauri kijeshi serikali ya Israeli lazima wabainishe na wasake ushauri ambao utaepusha vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita.  Wamesema wanasheria wana wajibu kwa mujibu wa kazi yao kukataa kuidhinisha kisheria vitendo vya kihalifu, vitendo ambavyo vitakiuka sheria ya kimataifa.  Ifahamike kuwa sheria ya kimataifa pamoja na mambo mengine inataka pande kinzani kulinda raia kwenye mapigano na kuepuka kushambulia miundombinu ya kiraia kama vile mifumo ya maji, hospitali na shule.  
10/23/20230
Episode Artwork

UN: Wanasheria mnaoshauri Israeli muwe makini na ushauri wenu

Wataalamu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu wamesihi wanasheria wanaoishauri serikali ya Israeli inayoendelea na mashambulizi dhidi ya wanamgambo wa kipalestina Hamas huko Ukanda wa Gaza, wakatae kuidhinisha kisheria vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita. Msingi wa kauli ya wataalamu hao ni kwamba tangu tarehe 7 mwezi huu wa Oktoba wanamgambo wa Hamas waliposhambulia Israeli, jeshi la ulinzi la Israeli, IDF limekuwa likiripotiwa kuwa linajipanga kuanza uvamizi wa ardhini baada ya kutekeleza mashambulizi ya angani huko Kaskazini mwa Gaza yaliyosababisha vifo vya wapalestina zaidi ya 3,400 na majeruhi 12,000 wakiwemo watoto.  Uvamizi huo wa ardhini inaelezwa ni kulipiza kisasi cha mashambulizi yaliyofanywa na Hamas na wanamgambo wengine wa kipalestina nchini Israeli na kuua raia, halikadhalika  kuteka na kushikilia wengine mateka hadi leo hii.  Wataalamu hao kupitia taarifa yao waliyoitoa hii leo mjini Geneva, Uswisi wanasema bila shaka vitendo vya Hamas dhidi ya raia wa Israeli vilikuwa mauaji.  Lakini sasa mashambulizi ya Israeli yamekuwa yakielekezwa kwenye maeneo yenye makazi ya watu wengi, yakiharibu makazi, hospitali, masoko huku ikizidi kuweka vizuizi na kuzingira Gaza, imekata usambazaji wa vyakula, maji, umeme na mafuta.  Sasa wataalamu wanasema kadri ambavyo Israeli inajibu kitendo cha Hamas na kuendesha operesheni zake Gaza, wanasheria wote wanaoshauri kijeshi serikali ya Israeli lazima wabainishe na wasake ushauri ambao utaepusha vitendo ambavyo vinaweza kuwa uhalifu wa kivita.  Wamesema wanasheria wana wajibu kwa mujibu wa kazi yao kukataa kuidhinisha kisheria vitendo vya kihalifu, vitendo ambavyo vitakiuka sheria ya kimataifa.  Ifahamike kuwa sheria ya kimataifa pamoja na mambo mengine inataka pande kinzani kulinda raia kwenye mapigano na kuepuka kushambulia miundombinu ya kiraia kama vile mifumo ya maji, hospitali na shule.  
10/23/20230
Episode Artwork

Makala: Je akili mnemba AI ni faida au athari katika sekta ya filamu?

Hii leo makala inamulika Akili Mnemba au AI ambayo imebadili fani mbali mbali ikiwemo ya sanaa. Ni kwa kutambua umuhimu wa suala hili shirika la umoja wa mataifa la elimu, sayansi na utamaduni, UNESCO limeandaa mjadala maalum kuhusu akili mnemba kwenye sekta ya filamu unaoendelea huko Paris Ufaransa. Ajenda inajikita ni manufaa na changamoto kwa sekta ya sanaa ukizingatia maadili  na ubunifu. Yvonne Muinde mchanganya picha za filamu ni msanii aliyebobea kwenye sekta ya ubunifu na dijitali na mshiriki wa mjadala huo wa UNESCO ulioanza jana. Mwandishi wetu wa Nairobi Thelma Mwadzaya alimtembelea ofisini kwake mjini Nairobi na kuandaa makala hii.
10/20/20230
Episode Artwork

Makala: Je akili mnemba AI ni faida au athari katika sekta ya filamu?

Hii leo makala inamulika Akili Mnemba au AI ambayo imebadili fani mbali mbali ikiwemo ya sanaa. Ni kwa kutambua umuhimu wa suala hili shirika la umoja wa mataifa la elimu, sayansi na utamaduni, UNESCO limeandaa mjadala maalum kuhusu akili mnemba kwenye sekta ya filamu unaoendelea huko Paris Ufaransa. Ajenda inajikita ni manufaa na changamoto kwa sekta ya sanaa ukizingatia maadili  na ubunifu. Yvonne Muinde mchanganya picha za filamu ni msanii aliyebobea kwenye sekta ya ubunifu na dijitali na mshiriki wa mjadala huo wa UNESCO ulioanza jana. Mwandishi wetu wa Nairobi Thelma Mwadzaya alimtembelea ofisini kwake mjini Nairobi na kuandaa makala hii.
10/20/20230
Episode Artwork

Mazungumzo yanaendelea kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi kabla ya misaada kuingia Gaza

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliyeko nchini Misri leo ametembelea mpaka wa Rafah, kivuko pekee cha kuingia na kutoka Ukanda wa Gaza, ambako hivi sasa kuna mashambulizi yanaendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas na kusema hivi sasa wanaendelea na mazungumzo kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi vya masharti yaliyowekwa na Israel kabla ya kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Ukanda wa Gaza. Ni vigumu uwepo hapa na usivunjike moyo, ndivyo Katibu Mkuu Guterres alivyowaeleza wanahabari walioko mji wa mpakani wa Rafah ambako msururu wa malori ya misaada ya kibinadamu unasubiri kuingia Gaza ambako takriban watu milioni 2 wanasubiri kwa udi na uvumba Msaada huo kwani hawana maji, chakula, dawa wala umeme huku wakiendelea kukabiliwa na mashambulizi kwa takriban wiki mbili sasa.Ingawa Marekani, Israel na Misri zote zimeeleza kuwa mpaka huo utafunguliwa lakini hilo bado halijatendeka na Guterres anasema.“Matangazo haya yalitolewa kwa masharti na vikwazo vingine. Na kwa hivyo sasa tupo tukishirikisha wahusika wa pande zote kikikamilifu, tunashirikiana kikamilifu na Misri, na Israel, na Marekani ili kuhakikisha tunaweza kufafanua masharti hayo, na tunaweza kupunguza vizuizi hivyo ili malori haya yaweze kuelekea kwa haraka iwezekanavyo mahali yanapohitajika.”Guterres amesema kinachohitaji si tu misaada hiyo iweze kufika haraka lakini pia zoezi hilo liwe endelevu kwani mzozo unaoendelea Gaza si wa kawaida.“Kwa bahati mbaya, hii sio operesheni ya kawaida ya kibinadamu. Ni operesheni katika eneo la vita na ndiyo sababu nimetoa wito wa kusitishwa kwa mapigano ya kibinadamu, sio kwamba ninaona kuwa usitishaji mapigano wa kibinadamu ni sharti la utoaji wa misaada ya kibinadamu lakini hatutaki kuwaadhibu watu wa Gaza mara mbili. Kwanza kwa sababu ya vita na pili kwa sababu ya ukosefu wa misaada ya kibinadamu. Lakini ni wazi kwamba usitishaji mapigano wa kibinadamu utafanya mambo kuwa rahisi zaidi na salama zaidi kwa kila mtu.”Pamoja na kuishukuru nchi ya Misri na shirika la kimataifa la hilal nyekundu kwa kuendelea kushughulikia suala hili kwa karibu, Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amehitimisha mkutano wake na wanahabari kwa kusema anatumai ipo siku Israel na Palestina wataishi kwa amani.“Natumai kwamba kutakuwa na mustakabali na matumaini kwamba siku moja kutakuwa na amani na suluhisho la Serikali mbili, huku Wapalestina na Waisraeli wakiishi kwa amani katika Mataifa mawili, upande mmoja hadi mwingine.”
10/20/20230
Episode Artwork

Mazungumzo yanaendelea kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi kabla ya misaada kuingia Gaza

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliyeko nchini Misri leo ametembelea mpaka wa Rafah, kivuko pekee cha kuingia na kutoka Ukanda wa Gaza, ambako hivi sasa kuna mashambulizi yanaendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas na kusema hivi sasa wanaendelea na mazungumzo kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi vya masharti yaliyowekwa na Israel kabla ya kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Ukanda wa Gaza. Ni vigumu uwepo hapa na usivunjike moyo, ndivyo Katibu Mkuu Guterres alivyowaeleza wanahabari walioko mji wa mpakani wa Rafah ambako msururu wa malori ya misaada ya kibinadamu unasubiri kuingia Gaza ambako takriban watu milioni 2 wanasubiri kwa udi na uvumba Msaada huo kwani hawana maji, chakula, dawa wala umeme huku wakiendelea kukabiliwa na mashambulizi kwa takriban wiki mbili sasa.Ingawa Marekani, Israel na Misri zote zimeeleza kuwa mpaka huo utafunguliwa lakini hilo bado halijatendeka na Guterres anasema.“Matangazo haya yalitolewa kwa masharti na vikwazo vingine. Na kwa hivyo sasa tupo tukishirikisha wahusika wa pande zote kikikamilifu, tunashirikiana kikamilifu na Misri, na Israel, na Marekani ili kuhakikisha tunaweza kufafanua masharti hayo, na tunaweza kupunguza vizuizi hivyo ili malori haya yaweze kuelekea kwa haraka iwezekanavyo mahali yanapohitajika.”Guterres amesema kinachohitaji si tu misaada hiyo iweze kufika haraka lakini pia zoezi hilo liwe endelevu kwani mzozo unaoendelea Gaza si wa kawaida.“Kwa bahati mbaya, hii sio operesheni ya kawaida ya kibinadamu. Ni operesheni katika eneo la vita na ndiyo sababu nimetoa wito wa kusitishwa kwa mapigano ya kibinadamu, sio kwamba ninaona kuwa usitishaji mapigano wa kibinadamu ni sharti la utoaji wa misaada ya kibinadamu lakini hatutaki kuwaadhibu watu wa Gaza mara mbili. Kwanza kwa sababu ya vita na pili kwa sababu ya ukosefu wa misaada ya kibinadamu. Lakini ni wazi kwamba usitishaji mapigano wa kibinadamu utafanya mambo kuwa rahisi zaidi na salama zaidi kwa kila mtu.”Pamoja na kuishukuru nchi ya Misri na shirika la kimataifa la hilal nyekundu kwa kuendelea kushughulikia suala hili kwa karibu, Mkuu huyo wa Umoja wa Mataifa amehitimisha mkutano wake na wanahabari kwa kusema anatumai ipo siku Israel na Palestina wataishi kwa amani.“Natumai kwamba kutakuwa na mustakabali na matumaini kwamba siku moja kutakuwa na amani na suluhisho la Serikali mbili, huku Wapalestina na Waisraeli wakiishi kwa amani katika Mataifa mawili, upande mmoja hadi mwingine.”
10/20/20230
Episode Artwork

20 AGOSTI 2023

Hii leojaridani tunaangazia ziara ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa mashariki ya kati na kilichojiri hapa makao makuu baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huko kugonga mwamba. Makala tunaangazia akili mnemba katika filamu na mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina na utamsikia ujumbe wa mfanyakazi wa Umoja wa Mataifa kuhusu machungu wanayopitia wanawake na wasichana katika eneo hilo.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliyeko nchini Misri leo ametembelea mpaka wa Rafah, kivuko pekee cha kuingia na kutoka Ukanda wa Gaza, ambako hivi sasa kuna mashambulizi yanaendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas na kusema hivi sasa wanaendelea na mazungumzo kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi vya masharti yaliyowekwa na Israel kabla ya kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Ukanda wa Gaza.Mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea kati ya Israeli na kundi la wanamgambo wa kipalestina, Hamas, hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye jukumu la kusimamia amani na usalama liko njiapanda baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huo kugonga mwamba! Makala leo inamulika Akili mnemba ambayo imebadili fani ya sanaa na utamaduni kwa njia ambazo hazikutarajiwa na mabadiliko hayo ni ya muda mrefu. Na kwa kutambua umuhimu wa suala hili shirika la umoja wa mataifa la elimu, sayansi na utamaduni, UNESCO limeandaa mjadala maalum kuhusu akili mnemba kwenye sekta ya filamu. Ajenda inajikita kwenye manufaa na changamoto zitakazokumba sekta za utamaduni na sanaa ukizingatia maadili na ubunifu. Yvonne Muinde mchanganya picha za filamu ni msanii aliyebobea kwenye sekta ya ubunifu na dijitali na mshiriki wa mjadala huo wa UNESCO ulioanza jana.Na katika mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina na utamsikia ujumbe wa mfanyakazi wa Umoja wa Mataifa kuhusu machungu wanayopitia wanawake na wasichana katika eneo hilo.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/20/20230
Episode Artwork

20 AGOSTI 2023

Hii leojaridani tunaangazia ziara ya Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa mashariki ya kati na kilichojiri hapa makao makuu baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huko kugonga mwamba. Makala tunaangazia akili mnemba katika filamu na mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina na utamsikia ujumbe wa mfanyakazi wa Umoja wa Mataifa kuhusu machungu wanayopitia wanawake na wasichana katika eneo hilo.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres aliyeko nchini Misri leo ametembelea mpaka wa Rafah, kivuko pekee cha kuingia na kutoka Ukanda wa Gaza, ambako hivi sasa kuna mashambulizi yanaendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina wa Hamas na kusema hivi sasa wanaendelea na mazungumzo kupata ufafanuzi wa vikwazo na vizuizi vya masharti yaliyowekwa na Israel kabla ya kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Ukanda wa Gaza.Mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea kati ya Israeli na kundi la wanamgambo wa kipalestina, Hamas, hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye jukumu la kusimamia amani na usalama liko njiapanda baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huo kugonga mwamba! Makala leo inamulika Akili mnemba ambayo imebadili fani ya sanaa na utamaduni kwa njia ambazo hazikutarajiwa na mabadiliko hayo ni ya muda mrefu. Na kwa kutambua umuhimu wa suala hili shirika la umoja wa mataifa la elimu, sayansi na utamaduni, UNESCO limeandaa mjadala maalum kuhusu akili mnemba kwenye sekta ya filamu. Ajenda inajikita kwenye manufaa na changamoto zitakazokumba sekta za utamaduni na sanaa ukizingatia maadili na ubunifu. Yvonne Muinde mchanganya picha za filamu ni msanii aliyebobea kwenye sekta ya ubunifu na dijitali na mshiriki wa mjadala huo wa UNESCO ulioanza jana.Na katika mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina na utamsikia ujumbe wa mfanyakazi wa Umoja wa Mataifa kuhusu machungu wanayopitia wanawake na wasichana katika eneo hilo.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/20/20230
Episode Artwork

Fahamu nini kinaweza kufuatia pindi maazimio yanagonga mwamba Baraza la Usalama la UN

Mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea kati ya Israeli na kundi la wanamgambo wa kipalestina, Hamas, hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye jukumu la kusimamia amani na usalama liko njiapanda baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huo kugonga mwamba! Marekani ikitumia kura turufu. Sasa nini kinafuatia? Rasimu mpya au kikao cha dharura cha Baraza Kuu? Bila shaka Assumpta! Ikumbukwe kuwa mzozo wa sasa huko Mashariki ya Kati alianza tarehe 7 mwezi huu wa Oktoba kwa Hamas kurusha makombora Israel.Hali hiyo ikatinga kwenye rada za Baraza la Usalama lenye wanachama 15, watano wakiwa wa kudumu, Baraza lenye wajibu wa kusimamia amani na usalama duniani. Rasimu mbili ziliandaliwa zote zikiwa na lengo la pamoja na mambo mengine sitisho la mapitano na kupatikana kwa njia ya kupitisha misaada ya kibinadamu. Ya kwanza ikiwasilishwa na Urusi haikupata kura za kutosha kuweza kupitishwa, ya pili iliyowasilishwa na Brazili, ilipigiwa kura turufu na Marekani. Marekani, China, Urusi, Ufaransa na Uingereza zina ujumbe wa kudumu Barazani hivyo zina kura turufu au veto ambayo ikitumika rasimu haipiti hata ikipata kura tisa ambazo zinahitajika azimio kupita. Kura turufu ilipatiwa wajumbe hao wa kudumu punde tu baada ya Baraza kuanzishwa mwishoni mwa vita kuu ya pili ya dunia. Hadi sasa harakati za kupanua wigo wa umiliki wa kura hiyo zimegonga mwamba. Lakini wajumbe wa Baraza wanaweza pia kumaliza tofauti zao kwenye lugha ya rasimu na kisha kuwasilisha rasimu nyingine Barazani ili ipigiwe kura. Hiyo itakuwa heri!! Nafasi ya Baraza Kuu Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa nalo lina nafasi yake ambapo kwa ombi la nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, Rais wa Baraza hilo Kuu anaweza kuitisha kikao rasmi ndani ya siku 10 tangu mjumbe mmoja au zaidi atumie kura tufuru kuzuia azimio.  Na kumbuka Marekani ilitumia turufu yake kuzuia rasimu ya azimio juu ya mzozo wa Israel na Palestina, hivyo Baraza lina hadi tarehe Mosi mwezi ujao wa Novemba kuitisha kikao hicho. Hatua nyingine pia inayoweza kufuatia ni kwa nchi wanachama kumuomba Rais wa Baraza Kuu kuitisha mjadala kuhusu mazingira ambamo kwayo kura hiyo turufu ilitumika. Lakini ni vema kutambua kuwa Baraza hilo halikutani kwa kile ambacho aghalabu huitwa kikao maalum cha dharura juu ya suala moja. Lengo ni kutoa mapendekezo ikiwemo uwezekano wa kutumia nguvu za kijeshi, kuendeleza au kurejesha amani na usalama kwenye eneo husika. Halikadhalika kusitisha mapigano na mahitaji yafikie walio kwenye shida. Na ukiangalia ongezeko la idadi ya vifo huko Mashariki ya Kati, iwapo Rais wa Baraza ataombwa kuitisha kikao kutokana na kura ya wajumbe wowote 7 au zaidi wa Baraza la Usalama au kwa idadi kubwa ya nchi 193 wanachama wa UN, basi Rais huyo lazima aitishe kikao maalum cha dharura ndani ya saa 24. Tangu Umoja wa Mataifa uanzishwe mwaka 195 kumekuweko na vikao vya aina hiyo 11 pekee, na kati ya hivyo, vitano (5) vilihusu Mashariki ya Kati.  Kikao cha mwisho kilikuwa Februari mwaka 2022, siku 6 baada ya Urusi kuvamia Ukraine. Lakini wengine wanauliza, mkwamo ndani ya Baraza la Usalama unamaanisha Umoja wa Mataifa umefungwa mikono hauwezi kutekeleza majukumu yake? La hasha!  Kwa sasa harakati za kidiplomasia na kibinadamu zinaendelea tangu kulipuka kwa mzozo huo ambapo Katibu Mkuu na wasaidizi wake wako tayari Mashariki ya Kati, huku mashirika yakiendelea kuhakikisha misaada ya kiutu inafikia wahusika. 
10/20/20230
Episode Artwork

Fahamu nini kinaweza kufuatia pindi maazimio yanagonga mwamba Baraza la Usalama la UN

Mzozo wa Mashariki ya Kati ukiendelea kati ya Israeli na kundi la wanamgambo wa kipalestina, Hamas, hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lenye jukumu la kusimamia amani na usalama liko njiapanda baada ya rasimu mbili za maazimio kwa ajili ya kuchukua hatua kwenye mzozo huo kugonga mwamba! Marekani ikitumia kura turufu. Sasa nini kinafuatia? Rasimu mpya au kikao cha dharura cha Baraza Kuu? Bila shaka Assumpta! Ikumbukwe kuwa mzozo wa sasa huko Mashariki ya Kati alianza tarehe 7 mwezi huu wa Oktoba kwa Hamas kurusha makombora Israel.Hali hiyo ikatinga kwenye rada za Baraza la Usalama lenye wanachama 15, watano wakiwa wa kudumu, Baraza lenye wajibu wa kusimamia amani na usalama duniani. Rasimu mbili ziliandaliwa zote zikiwa na lengo la pamoja na mambo mengine sitisho la mapitano na kupatikana kwa njia ya kupitisha misaada ya kibinadamu. Ya kwanza ikiwasilishwa na Urusi haikupata kura za kutosha kuweza kupitishwa, ya pili iliyowasilishwa na Brazili, ilipigiwa kura turufu na Marekani. Marekani, China, Urusi, Ufaransa na Uingereza zina ujumbe wa kudumu Barazani hivyo zina kura turufu au veto ambayo ikitumika rasimu haipiti hata ikipata kura tisa ambazo zinahitajika azimio kupita. Kura turufu ilipatiwa wajumbe hao wa kudumu punde tu baada ya Baraza kuanzishwa mwishoni mwa vita kuu ya pili ya dunia. Hadi sasa harakati za kupanua wigo wa umiliki wa kura hiyo zimegonga mwamba. Lakini wajumbe wa Baraza wanaweza pia kumaliza tofauti zao kwenye lugha ya rasimu na kisha kuwasilisha rasimu nyingine Barazani ili ipigiwe kura. Hiyo itakuwa heri!! Nafasi ya Baraza Kuu Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa nalo lina nafasi yake ambapo kwa ombi la nchi wanachama wa Umoja wa Mataifa, Rais wa Baraza hilo Kuu anaweza kuitisha kikao rasmi ndani ya siku 10 tangu mjumbe mmoja au zaidi atumie kura tufuru kuzuia azimio.  Na kumbuka Marekani ilitumia turufu yake kuzuia rasimu ya azimio juu ya mzozo wa Israel na Palestina, hivyo Baraza lina hadi tarehe Mosi mwezi ujao wa Novemba kuitisha kikao hicho. Hatua nyingine pia inayoweza kufuatia ni kwa nchi wanachama kumuomba Rais wa Baraza Kuu kuitisha mjadala kuhusu mazingira ambamo kwayo kura hiyo turufu ilitumika. Lakini ni vema kutambua kuwa Baraza hilo halikutani kwa kile ambacho aghalabu huitwa kikao maalum cha dharura juu ya suala moja. Lengo ni kutoa mapendekezo ikiwemo uwezekano wa kutumia nguvu za kijeshi, kuendeleza au kurejesha amani na usalama kwenye eneo husika. Halikadhalika kusitisha mapigano na mahitaji yafikie walio kwenye shida. Na ukiangalia ongezeko la idadi ya vifo huko Mashariki ya Kati, iwapo Rais wa Baraza ataombwa kuitisha kikao kutokana na kura ya wajumbe wowote 7 au zaidi wa Baraza la Usalama au kwa idadi kubwa ya nchi 193 wanachama wa UN, basi Rais huyo lazima aitishe kikao maalum cha dharura ndani ya saa 24. Tangu Umoja wa Mataifa uanzishwe mwaka 195 kumekuweko na vikao vya aina hiyo 11 pekee, na kati ya hivyo, vitano (5) vilihusu Mashariki ya Kati.  Kikao cha mwisho kilikuwa Februari mwaka 2022, siku 6 baada ya Urusi kuvamia Ukraine. Lakini wengine wanauliza, mkwamo ndani ya Baraza la Usalama unamaanisha Umoja wa Mataifa umefungwa mikono hauwezi kutekeleza majukumu yake? La hasha!  Kwa sasa harakati za kidiplomasia na kibinadamu zinaendelea tangu kulipuka kwa mzozo huo ambapo Katibu Mkuu na wasaidizi wake wako tayari Mashariki ya Kati, huku mashirika yakiendelea kuhakikisha misaada ya kiutu inafikia wahusika. 
10/20/20230
Episode Artwork

Neno: KIPA MKONO”

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”. 
10/19/20230
Episode Artwork

Neno: KIPA MKONO”

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”. 
10/19/20230
Episode Artwork

19 OKTOBA 2023

Hii leo tunakuletea mada kwa kina ambapo shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO nchini Tanzania kwa ushirikiano na wadau wengine ikiwemo serikali ya Tanzania, waliamua hitimisho la maadhimisho ya siku ya chakula huko Kigoma, Magharibi mwa Tanzania, lifanyike kwenye mwalo wa Kibirizi – Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Ujiji kwa kufanya mashindano ya ngalawa, washiriki wakiwa mashujaa wa chakula kitokacho kwenye maji, ziwani Tanganyika, yaani wavuvi na wale waongezao thamani ya mazao ya ziwani kwani wote wanasongesha utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu, SDGs ya Umoja wa Mataifa likiwemo lile la kutokomeza umaskini halikadhalika njaa. Pia tunakuleta habari zifuatazo kwa ufupi na katika kujifunza Kiswahili  mtaalam wetu Onni Sigalla anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”.Kuna matumaini huko Gaza ambako wahudumu wa misaada ya kibinadamu wanaendelea kusubiri ruksa kwa hamasa kubwa kuingiza misaada ya kuokoa maisha kufuatia ripoti za makubaliano yaliyosimamiwa na Rais wa Marekani ya kuingiza Gaza malori 20 ya misaada kupitia mpaka wa Misri umesema leo Umoja wa Mataifa. Tani 3,000 za vifaa zimekuwa zikisubiri kuingia upande wa Misri wa kivuko cha Rafah tangu Jumamosi na shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa WFP limesema liko tayari kusambaza msaada huo.Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, leo limetoa wito wa ufadhili mpya na kujitolea kwa muda mrefu kwa ajili ya kusambaza mlo shuleni katika mkutano muhimu wa kimataifa unaofanyika mjini Paris Ufaransa kuhusu mlo shuleni. Na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu , sayansi na utamaduni UNESCO leo limeanza majadiliano ya ngazi ya juu mjini Paris Ufanrasa kuhusu akili mnemba au AI na sekta ya filamu. Ajenda kubwa ni kuangalia jinsi gani maendeleo ya AI yanavyoathiri sekta hiyo na jinsi sekta hiyo inavyoweza kukumbatia maendeleo hayo kupata ufanisi na manufaa.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili  mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/19/20230
Episode Artwork

19 OKTOBA 2023

Hii leo tunakuletea mada kwa kina ambapo shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO nchini Tanzania kwa ushirikiano na wadau wengine ikiwemo serikali ya Tanzania, waliamua hitimisho la maadhimisho ya siku ya chakula huko Kigoma, Magharibi mwa Tanzania, lifanyike kwenye mwalo wa Kibirizi – Halmashauri ya Wilaya ya Kigoma Ujiji kwa kufanya mashindano ya ngalawa, washiriki wakiwa mashujaa wa chakula kitokacho kwenye maji, ziwani Tanganyika, yaani wavuvi na wale waongezao thamani ya mazao ya ziwani kwani wote wanasongesha utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu, SDGs ya Umoja wa Mataifa likiwemo lile la kutokomeza umaskini halikadhalika njaa. Pia tunakuleta habari zifuatazo kwa ufupi na katika kujifunza Kiswahili  mtaalam wetu Onni Sigalla anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”.Kuna matumaini huko Gaza ambako wahudumu wa misaada ya kibinadamu wanaendelea kusubiri ruksa kwa hamasa kubwa kuingiza misaada ya kuokoa maisha kufuatia ripoti za makubaliano yaliyosimamiwa na Rais wa Marekani ya kuingiza Gaza malori 20 ya misaada kupitia mpaka wa Misri umesema leo Umoja wa Mataifa. Tani 3,000 za vifaa zimekuwa zikisubiri kuingia upande wa Misri wa kivuko cha Rafah tangu Jumamosi na shirika la mpango wa chakula la Umoja wa Mataifa WFP limesema liko tayari kusambaza msaada huo.Shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani WFP, leo limetoa wito wa ufadhili mpya na kujitolea kwa muda mrefu kwa ajili ya kusambaza mlo shuleni katika mkutano muhimu wa kimataifa unaofanyika mjini Paris Ufaransa kuhusu mlo shuleni. Na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu , sayansi na utamaduni UNESCO leo limeanza majadiliano ya ngazi ya juu mjini Paris Ufanrasa kuhusu akili mnemba au AI na sekta ya filamu. Ajenda kubwa ni kuangalia jinsi gani maendeleo ya AI yanavyoathiri sekta hiyo na jinsi sekta hiyo inavyoweza kukumbatia maendeleo hayo kupata ufanisi na manufaa.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili  mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA anafafanua maana ya neno “KIPA MKONO”.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/19/20230
Episode Artwork

Tunashukuru TANZBATT10 kwa vifaa vya shule lakini pia watusaidie majengo

Hii leo katika makala ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, kikosi cha 10, TANZBATT 10 kinachohudumu kwenye ujumbe wa UN wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO, hususan kile cha kujibu mashambulizi, FIB wamefika shule ya msingi Ushindi mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini na kutoa msaada wa vifaa vya shule wakilenga kufanikisha lengo namba 4 la malengo  ya maendeleo endelevu. SDGs hukusan kipengele kinachohusu ujumuishi. Afisa Habari wa kikosi hicho  Luteni Abubakari Muna ameandaa makala hii kutoka na ziara hiyo, ikianza na Meja Neema Neligwa mwakilishi wa Kamanda kikosi cha TANZBATT 10, Luteni Kanali John Peter Kalabaka akifafanua walengwa kwa msaada huo. 
10/18/20230
Episode Artwork

Tunashukuru TANZBATT10 kwa vifaa vya shule lakini pia watusaidie majengo

Hii leo katika makala ninakupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, kikosi cha 10, TANZBATT 10 kinachohudumu kwenye ujumbe wa UN wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO, hususan kile cha kujibu mashambulizi, FIB wamefika shule ya msingi Ushindi mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini na kutoa msaada wa vifaa vya shule wakilenga kufanikisha lengo namba 4 la malengo  ya maendeleo endelevu. SDGs hukusan kipengele kinachohusu ujumuishi. Afisa Habari wa kikosi hicho  Luteni Abubakari Muna ameandaa makala hii kutoka na ziara hiyo, ikianza na Meja Neema Neligwa mwakilishi wa Kamanda kikosi cha TANZBATT 10, Luteni Kanali John Peter Kalabaka akifafanua walengwa kwa msaada huo. 
10/18/20230
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa unaendelea kuwapatia msaada wananchi waliosalia nchini Ukraine

Uvamizi wa Urusi  nchini Ukraine umefurusha makwao mamilioni ya watu kwenda kusaka hifadhi maeneo ya mikoani na hata nchi jirani. Katika Mkoa wa Donetsk asilimia 90 ya wananchi walikimbia tu vita ilipoanza, na zaidi ya wananchi 1,000 walioamua kusalia hawana huduma za maji, umeme na gesi na Umoja wa Mataifa umekuwa ukifanya kila juhudi kuhakikisha wanapata huduma hizo muhimu.Wakazi wa Chasiv Yar mkoani Donetsk tangu kuibuka kwa vita kati ya Ukraine na Urusi wamekuwa wakiishi katika hali ya taabu na kujificha katika mahandaki chini ya nyumba zao.Mapigano yameharibu nyumba zao pamoja na miundombinu na kuwaacha wakazi zaidi ya 1,000 wakiwa katika hali ngumu.Mfanyakazi wa kujitolea aitwaye Oleksandr anasema baadhi ya walioamua kubaki katika eneo hilo wanawasaidia wananchi wenzao kwani kuna kundi kubwa la wazee wake kwa waume ambao hawataki kuondoka na wanahitaji msaada, “Kwa wakati huu, tuseme, hali si rahisi. Naweza kusema kuwa ni ngumu kwa wenyeji. Kwa nini? Hakuna umeme, gesi, taa, wala miundombinu ya kuletajoto kwenye nyumba. Ndio maana shirika letu linafanya kila liwezalo kusaidia watu kuboresha nyumba zao.”Mratibu mkazi wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Ukraine Denise Brown amefika katika mkoa huo akiwa na msafara wa 31 uliosheheni misaada ya kibinadamu kutoka kwa mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa na kugawa misaada hiyo kwa wananchi.Miongoni mwa waliopokea msaada ni Bi. Lyubove, “Tumepokea misaada ya kibinadamu leo, sijui imetoka wapi, lakini kila mtu amepata chupa tatu za maji pamoja na masanduku mawili ya bidhaa.”Pamoja na kushukuru kwa msaada huo Bi.Lyubove akatoa ombi kwa wadau wa misaada ya kibinadamu, “Kodi ya nyumba ni ghali sana kwa sasa. Watu wameanza kurejea Chasiv Yar. Ingawa ni ngumu sana na inatisha kuishi hapa lakini wanajaribu kurudi nyumbani hasa wale wenye nyumba zao binafsi zilizo ambazo zina majiko. Majira ya baridi yanakuja, na watu hawana pesa za kulipa… Pensheni ni ndogo, na hakuna mishahara.”Kiujumla kwa mwaka huu Umoja wa Mataifa na wadau wake wamefanikiwa kufikisha misaada ya kibinadamu kwa wakazi zaidi ya milioni 8.3 nchini Ukraine.
10/18/20230
Episode Artwork

Umoja wa Mataifa unaendelea kuwapatia msaada wananchi waliosalia nchini Ukraine

Uvamizi wa Urusi  nchini Ukraine umefurusha makwao mamilioni ya watu kwenda kusaka hifadhi maeneo ya mikoani na hata nchi jirani. Katika Mkoa wa Donetsk asilimia 90 ya wananchi walikimbia tu vita ilipoanza, na zaidi ya wananchi 1,000 walioamua kusalia hawana huduma za maji, umeme na gesi na Umoja wa Mataifa umekuwa ukifanya kila juhudi kuhakikisha wanapata huduma hizo muhimu.Wakazi wa Chasiv Yar mkoani Donetsk tangu kuibuka kwa vita kati ya Ukraine na Urusi wamekuwa wakiishi katika hali ya taabu na kujificha katika mahandaki chini ya nyumba zao.Mapigano yameharibu nyumba zao pamoja na miundombinu na kuwaacha wakazi zaidi ya 1,000 wakiwa katika hali ngumu.Mfanyakazi wa kujitolea aitwaye Oleksandr anasema baadhi ya walioamua kubaki katika eneo hilo wanawasaidia wananchi wenzao kwani kuna kundi kubwa la wazee wake kwa waume ambao hawataki kuondoka na wanahitaji msaada, “Kwa wakati huu, tuseme, hali si rahisi. Naweza kusema kuwa ni ngumu kwa wenyeji. Kwa nini? Hakuna umeme, gesi, taa, wala miundombinu ya kuletajoto kwenye nyumba. Ndio maana shirika letu linafanya kila liwezalo kusaidia watu kuboresha nyumba zao.”Mratibu mkazi wa misaada ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa nchini Ukraine Denise Brown amefika katika mkoa huo akiwa na msafara wa 31 uliosheheni misaada ya kibinadamu kutoka kwa mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa na kugawa misaada hiyo kwa wananchi.Miongoni mwa waliopokea msaada ni Bi. Lyubove, “Tumepokea misaada ya kibinadamu leo, sijui imetoka wapi, lakini kila mtu amepata chupa tatu za maji pamoja na masanduku mawili ya bidhaa.”Pamoja na kushukuru kwa msaada huo Bi.Lyubove akatoa ombi kwa wadau wa misaada ya kibinadamu, “Kodi ya nyumba ni ghali sana kwa sasa. Watu wameanza kurejea Chasiv Yar. Ingawa ni ngumu sana na inatisha kuishi hapa lakini wanajaribu kurudi nyumbani hasa wale wenye nyumba zao binafsi zilizo ambazo zina majiko. Majira ya baridi yanakuja, na watu hawana pesa za kulipa… Pensheni ni ndogo, na hakuna mishahara.”Kiujumla kwa mwaka huu Umoja wa Mataifa na wadau wake wamefanikiwa kufikisha misaada ya kibinadamu kwa wakazi zaidi ya milioni 8.3 nchini Ukraine.
10/18/20230
Episode Artwork

18 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia hali ya kibinadamu Gaza na ya wakimbizi wa ndani Ukraine. Makala tunakupeleka nchini DRC na mashini tuanarejea huko Gaza kusikia ushuhuda wa waathirika, salía papo hapo tafadhali!Hali Mashariki ya Kati inaendelea kuwa mbayá hasa baada ya shambulio dhidi ya Hospitali ya Al-Ahli lililokatili maisha ya zaidi ya watu 500. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelazimika kukatisha ziara yake nchini China na kuelekea Cairo Misri atakakozungumza na wadau kuhusu jinsi ya kupunguza madhila kwa waathirika wa mzozo wa Israel na Hamas huko Gaza, lakini kabla ya kuondoka ametoa wito wa kusitishwa mara moja mapigano kwa ajili ya masuala ya kibinadamu, huku mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths tayari ameshawasili Cairo ili kuhakikisha misaada ya kibinadamu inaruhusiwa kuingia Gaza.Uvamizi wa Urusi nchini Ukraine umefurusha makwao mamilioni ya watu kwenda kusaka hifadhi maeneo ya mikoani na hata nchi jirani. Katika Mkoa wa Donetsk asilimia 90 ya wananchi walikimbia tu vita ilipoanza, na zaidi ya wananchi 1,000 walioamua kusalia hawana huduma za maji, umeme na gesi na Umoja wa Mataifa umekuwa ukifanya kila juhudi kuhakikisha wanapata huduma hizo muhimu. Makala inatupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, kikosi cha 10, TANZBATT 10 kinachohudumu kwenye ujumbe wa UN wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO, hususan kile cha kujibu mashambulizi, FIB wamefika shule ya msingi Ushindi mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini na kutoa msaada wa vifaa vya shule. Afisa Habari wa kikosi hicho  Luteni Abubakari Muna ameandaa makala hii kutoka na ziara hiyo, ikianza na Meja Neema Neligwa mwakilishi wa Kamanda kikosi cha TANZBATT 10, Luteni Kanali John Peter Kalabaka akifafanua walengwa kwa msaada huo.Na mashinani tuaelekea katika ukanda wa Gaza, eneo linalokaliwa la Palestina huko Mashariki ya Kati, kusikia ushuhuda wa waathirika wa mapigano yanayoendelea kati ya wanamgambo wa Hamas wa kipalestina na jeshi la Israel      kati ya Hamas na Israeli.Mwenyeji wako ni Assumpta, karibu!
10/18/20230
Episode Artwork

18 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia hali ya kibinadamu Gaza na ya wakimbizi wa ndani Ukraine. Makala tunakupeleka nchini DRC na mashini tuanarejea huko Gaza kusikia ushuhuda wa waathirika, salía papo hapo tafadhali!Hali Mashariki ya Kati inaendelea kuwa mbayá hasa baada ya shambulio dhidi ya Hospitali ya Al-Ahli lililokatili maisha ya zaidi ya watu 500. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelazimika kukatisha ziara yake nchini China na kuelekea Cairo Misri atakakozungumza na wadau kuhusu jinsi ya kupunguza madhila kwa waathirika wa mzozo wa Israel na Hamas huko Gaza, lakini kabla ya kuondoka ametoa wito wa kusitishwa mara moja mapigano kwa ajili ya masuala ya kibinadamu, huku mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths tayari ameshawasili Cairo ili kuhakikisha misaada ya kibinadamu inaruhusiwa kuingia Gaza.Uvamizi wa Urusi nchini Ukraine umefurusha makwao mamilioni ya watu kwenda kusaka hifadhi maeneo ya mikoani na hata nchi jirani. Katika Mkoa wa Donetsk asilimia 90 ya wananchi walikimbia tu vita ilipoanza, na zaidi ya wananchi 1,000 walioamua kusalia hawana huduma za maji, umeme na gesi na Umoja wa Mataifa umekuwa ukifanya kila juhudi kuhakikisha wanapata huduma hizo muhimu. Makala inatupeleka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, kikosi cha 10, TANZBATT 10 kinachohudumu kwenye ujumbe wa UN wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO, hususan kile cha kujibu mashambulizi, FIB wamefika shule ya msingi Ushindi mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini na kutoa msaada wa vifaa vya shule. Afisa Habari wa kikosi hicho  Luteni Abubakari Muna ameandaa makala hii kutoka na ziara hiyo, ikianza na Meja Neema Neligwa mwakilishi wa Kamanda kikosi cha TANZBATT 10, Luteni Kanali John Peter Kalabaka akifafanua walengwa kwa msaada huo.Na mashinani tuaelekea katika ukanda wa Gaza, eneo linalokaliwa la Palestina huko Mashariki ya Kati, kusikia ushuhuda wa waathirika wa mapigano yanayoendelea kati ya wanamgambo wa Hamas wa kipalestina na jeshi la Israel      kati ya Hamas na Israeli.Mwenyeji wako ni Assumpta, karibu!
10/18/20230
Episode Artwork

Guterres: Mapigano lazima yasite mara moja Gaza kwa sababu za kibinadamu

Hali Mashariki ya Kati inaendelea kuwa mbayá hasa baada ya shambulio dhidi ya Hospitali ya Al-Ahli na kukatili Maisha ya zaidi ya watu 500. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelazimika kukatisha ziara yake nchini China na kuelekea Cairo Misri lakini kabla ya kuondoka ametoa wito wa kusitishwa mara moja kwa mapigano Mashariki ya kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Naye mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths ameshawasili Cairo Misri katika juhudi za kuhakikisha misaada inaruhusiwa kuingia Gaza. Akizungumza mjini Beijing China, kabla ya kuondoka kuelekea Cairo Misri hii leo Bwana Guterres hakutafuna maneno, amesema kama Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anawajibika kutoa kauli hii ili kupunguza madhila makubwa yanayowaghubika watu katika mzozo wa Masharikiya Kati Mashariki ya Kati ni "mateso makubwa ya kibinadamu"  Hivyo amesema “Natoa wito wa usitishaji mapigano haraka kwa sababu za kibinadamu ili kutoa wakati na fursa ya kutosha kusaidia kutimiza maombi yangu mawili na kupunguza mateso makubwa kwa binadamu tunayoshuhudia. Maisha ya watu wengi na hatma ya ukanda mzima viko njiapanda.”Guterres ameonya kwamba eneo mzima liko katika hatari ya janga kubwa akisisitiza umuhimu wa kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Gaza.Wakati huohuo mratibu wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths ameshawasili Cairo Misri kwa ajili ya kuhakikisha misaada hiyo ya kibinadamu ambayo iko tayari mpakani mwa Gaza inaruhusiwa kuingia ili kuokoa maisha ya watu wengi. Kupitia ukurasa wake wa X amesema “ Kutoa misaada kwa watu wa Gaza popote walipo ni suala la uhai au kifo. Kufanya hivyo kwa njia endelevu, isiyozuiliwa, na inayotabirika ni sharti la kibinadamu.”Naye Phillippe Lazzarini kamishina mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA amewaomba mawaziri wa mambo ya nje wa jumuiya ya ushirikiano wa nchi za Kiislamu OIC "kuunga mkono kwa dhati na bila masharti juhudi za kibinadamu za kuwalinda raia huko Gaza"  akisema kwani hadi sasa “Hakuna shehena hata moja ya msaada imeruhusiwa kuingia Ukanda wa Gaza tangu kuanza kwa mzozo huu kutokana na hali iliyowekwa na Israel  ya kuzingizwa. Watu wanalazimika kunywa maji ambayo hayafai kwa matumizi, kwani maji safi ya kunywa hayapatikani. Akiba ya chakula, vifaa vya usafi na dawa vinapungua kwa kasi. Tuko ukingoni mwa janga kubwa la afya na usafi wa mazingira”.Hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama limekutana kujadili mgogoro huo na huko Israel Rais wa Marekani Joe Biden amewasili na kukutana na waziri mkuu Benjamin Netanyahu ambapo ameahidi msaada wa Marekani kwa Israel na kusema ameshtushwa na kughadhibishwa na mlipuko wa jana katika hospital mjini Gaza. 
10/18/20230
Episode Artwork

Guterres: Mapigano lazima yasite mara moja Gaza kwa sababu za kibinadamu

Hali Mashariki ya Kati inaendelea kuwa mbayá hasa baada ya shambulio dhidi ya Hospitali ya Al-Ahli na kukatili Maisha ya zaidi ya watu 500. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amelazimika kukatisha ziara yake nchini China na kuelekea Cairo Misri lakini kabla ya kuondoka ametoa wito wa kusitishwa mara moja kwa mapigano Mashariki ya kwa ajili ya masuala ya kibinadamu. Naye mratibu wa masuala ya kibinadamu wa Umoja wa Mataifa Martin Griffiths ameshawasili Cairo Misri katika juhudi za kuhakikisha misaada inaruhusiwa kuingia Gaza. Akizungumza mjini Beijing China, kabla ya kuondoka kuelekea Cairo Misri hii leo Bwana Guterres hakutafuna maneno, amesema kama Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa anawajibika kutoa kauli hii ili kupunguza madhila makubwa yanayowaghubika watu katika mzozo wa Masharikiya Kati Mashariki ya Kati ni "mateso makubwa ya kibinadamu"  Hivyo amesema “Natoa wito wa usitishaji mapigano haraka kwa sababu za kibinadamu ili kutoa wakati na fursa ya kutosha kusaidia kutimiza maombi yangu mawili na kupunguza mateso makubwa kwa binadamu tunayoshuhudia. Maisha ya watu wengi na hatma ya ukanda mzima viko njiapanda.”Guterres ameonya kwamba eneo mzima liko katika hatari ya janga kubwa akisisitiza umuhimu wa kuruhusu misaada ya kibinadamu kuingia Gaza.Wakati huohuo mratibu wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths ameshawasili Cairo Misri kwa ajili ya kuhakikisha misaada hiyo ya kibinadamu ambayo iko tayari mpakani mwa Gaza inaruhusiwa kuingia ili kuokoa maisha ya watu wengi. Kupitia ukurasa wake wa X amesema “ Kutoa misaada kwa watu wa Gaza popote walipo ni suala la uhai au kifo. Kufanya hivyo kwa njia endelevu, isiyozuiliwa, na inayotabirika ni sharti la kibinadamu.”Naye Phillippe Lazzarini kamishina mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA amewaomba mawaziri wa mambo ya nje wa jumuiya ya ushirikiano wa nchi za Kiislamu OIC "kuunga mkono kwa dhati na bila masharti juhudi za kibinadamu za kuwalinda raia huko Gaza"  akisema kwani hadi sasa “Hakuna shehena hata moja ya msaada imeruhusiwa kuingia Ukanda wa Gaza tangu kuanza kwa mzozo huu kutokana na hali iliyowekwa na Israel  ya kuzingizwa. Watu wanalazimika kunywa maji ambayo hayafai kwa matumizi, kwani maji safi ya kunywa hayapatikani. Akiba ya chakula, vifaa vya usafi na dawa vinapungua kwa kasi. Tuko ukingoni mwa janga kubwa la afya na usafi wa mazingira”.Hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa Baraza la Usalama limekutana kujadili mgogoro huo na huko Israel Rais wa Marekani Joe Biden amewasili na kukutana na waziri mkuu Benjamin Netanyahu ambapo ameahidi msaada wa Marekani kwa Israel na kusema ameshtushwa na kughadhibishwa na mlipuko wa jana katika hospital mjini Gaza. 
10/18/20230
Episode Artwork

17 OKTOBA 2023

Hii leo jaridanitunakuletea mada kwa kina na ukulima wa kisasa hususani mijini umeelezwa kuchangia si tu upatikanaji wa chakula bali pia unatumia maji kidogo hivyo unapigiwa chepuo hususan wakati huu dunia ikikabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Taasisi ya Malembo Farm iliyofanya kazi nchini Tanzania na Kenya inatoa mafunzo ya kilimo cha kisasa mijini ambapo tumezungumza na wanufaika wa mafunzo hayo pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wake Lucas Elias Malembo akiwa nchini Tanzania anayeanza kwa kueleza namna wanavyoienzi kauli mbiu ya mwaka huu. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani, zinahusu nini? Salía papo hapo tafadhali!Asante Leah naazia Mashariki ya Kati ambako mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa kwa mara nyingine yameelezea wasiwasi mkubwa kuhusu hatma raia huko Gaza na Ukingo wa Magaribi yakisistiza fursa ya kufikisha misaada kwa wenye uhitaji likiwemo shirika la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA linalohifadhi wakimbizi wa ndani takribani 400,000 kati ya laki sita sasa katika vituo vyake.Katika taarifa nyingine leo UNHCR, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi limetoa tahadhari kuhusu kukithiri kwa ghasia na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika majimbo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ambazo zimesababisha wimbi jipya la watu kukimbia makazi yao, ndani na nje ya nchi. Licha ya makubaliano ya hivi karibuni ya kusitisha mapigano katika jimbo la Kivu Kaskazini, UNHCR imeripoti kuwa zaidi ya watu 90,000 katika maeneo ya Rutshuru na Masisi wamelazimika kukimbia makazi yao katika wiki za kwanza za Oktoba. Nchini Sudan kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, Takriban watu 4,000 wameuawa huku mali na miundombinu ya raia      vikiharibiwa vibaya katika vita inavyoendelea Darfur na watu wengine 8,400 wamejeruhiwa, kati ya Aprili 15 na mwisho wa Agosti, huku wengi wao wakilengwa kutokana na sababu za kikabila, hasa eneo la Darfur Magharibi.Na mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina kushuhudia jinsi ambavyo watoto na jamii zao wanavyoathirika kufuatia vita kati ya Hamas na Israeli.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/17/20230
Episode Artwork

17 OKTOBA 2023

Hii leo jaridanitunakuletea mada kwa kina na ukulima wa kisasa hususani mijini umeelezwa kuchangia si tu upatikanaji wa chakula bali pia unatumia maji kidogo hivyo unapigiwa chepuo hususan wakati huu dunia ikikabiliana na athari za mabadiliko ya tabianchi. Taasisi ya Malembo Farm iliyofanya kazi nchini Tanzania na Kenya inatoa mafunzo ya kilimo cha kisasa mijini ambapo tumezungumza na wanufaika wa mafunzo hayo pamoja na Mkurugenzi Mtendaji wake Lucas Elias Malembo akiwa nchini Tanzania anayeanza kwa kueleza namna wanavyoienzi kauli mbiu ya mwaka huu. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani, zinahusu nini? Salía papo hapo tafadhali!Asante Leah naazia Mashariki ya Kati ambako mashirika mbalimbali ya Umoja wa Mataifa kwa mara nyingine yameelezea wasiwasi mkubwa kuhusu hatma raia huko Gaza na Ukingo wa Magaribi yakisistiza fursa ya kufikisha misaada kwa wenye uhitaji likiwemo shirika la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA linalohifadhi wakimbizi wa ndani takribani 400,000 kati ya laki sita sasa katika vituo vyake.Katika taarifa nyingine leo UNHCR, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi limetoa tahadhari kuhusu kukithiri kwa ghasia na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu katika majimbo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ambazo zimesababisha wimbi jipya la watu kukimbia makazi yao, ndani na nje ya nchi. Licha ya makubaliano ya hivi karibuni ya kusitisha mapigano katika jimbo la Kivu Kaskazini, UNHCR imeripoti kuwa zaidi ya watu 90,000 katika maeneo ya Rutshuru na Masisi wamelazimika kukimbia makazi yao katika wiki za kwanza za Oktoba. Nchini Sudan kwa mujibu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, Takriban watu 4,000 wameuawa huku mali na miundombinu ya raia      vikiharibiwa vibaya katika vita inavyoendelea Darfur na watu wengine 8,400 wamejeruhiwa, kati ya Aprili 15 na mwisho wa Agosti, huku wengi wao wakilengwa kutokana na sababu za kikabila, hasa eneo la Darfur Magharibi.Na mashinani tunakupeleka katika ukanda wa Gaza nchini Palestina kushuhudia jinsi ambavyo watoto na jamii zao wanavyoathirika kufuatia vita kati ya Hamas na Israeli.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/17/20230
Episode Artwork

Asante FAO kwani sasa nimeweza kujipatia zaidi ya dola Elfu 3 kupitia kilimo cha kisasa

Wanawake wa vijijini wanatambuliwa kimataifa kupitia siku yao ya kimataifa inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 15 mwezi Oktoba. Mwaka huu maadhimisho yamefanyika maeneo mbalimbali duniani ikiwemo mkoani Kigoma, magharibi mwa Tanzania, huko Afrika Mashariki. Shirika la Umoja wa Mataifa la kilimo na chakula, FAO liliandaa tukio maalum la kutambua mchango wa wanawake hao hasa kwa kuzingatia mchango wao katika uzalishaji chakula, kwani shirika la Umoja wa Mataifa la kazi, ILO linasema wanawake ni zaidi  ya asilimia 40 ya nguvukazi kwenye sekta ya kilimo. Ingawa hivyo tija itokanayo na kilimo hicho mara nyingi huwa ni ya chini sana na ndio maana FAO nchini Tanzania kupitia Mradi wa Pamoja wa Kigoma, KJP, wameendesha miradi kama vile kilimo cha kisasa kinachohimili mabadiliko ya tabianchi, halikadhalika  ufugaji wa kisasa. Baadhi ya wanawake wanufaika wa miradi hiyo wamekuwa mashujaa wa chakula, maudhui ya siku hiyo ya mwanamke wa Kijijini. Sasa wamefanya nini? John Kabambala wa Radio Washirika Kids Time FM ya mkoani Morogoro nchini Tanzania alikuwa shuhuda wetu wa tukio hilo mkoani Kigoma. 
10/16/20230
Episode Artwork

Asante FAO kwani sasa nimeweza kujipatia zaidi ya dola Elfu 3 kupitia kilimo cha kisasa

Wanawake wa vijijini wanatambuliwa kimataifa kupitia siku yao ya kimataifa inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 15 mwezi Oktoba. Mwaka huu maadhimisho yamefanyika maeneo mbalimbali duniani ikiwemo mkoani Kigoma, magharibi mwa Tanzania, huko Afrika Mashariki. Shirika la Umoja wa Mataifa la kilimo na chakula, FAO liliandaa tukio maalum la kutambua mchango wa wanawake hao hasa kwa kuzingatia mchango wao katika uzalishaji chakula, kwani shirika la Umoja wa Mataifa la kazi, ILO linasema wanawake ni zaidi  ya asilimia 40 ya nguvukazi kwenye sekta ya kilimo. Ingawa hivyo tija itokanayo na kilimo hicho mara nyingi huwa ni ya chini sana na ndio maana FAO nchini Tanzania kupitia Mradi wa Pamoja wa Kigoma, KJP, wameendesha miradi kama vile kilimo cha kisasa kinachohimili mabadiliko ya tabianchi, halikadhalika  ufugaji wa kisasa. Baadhi ya wanawake wanufaika wa miradi hiyo wamekuwa mashujaa wa chakula, maudhui ya siku hiyo ya mwanamke wa Kijijini. Sasa wamefanya nini? John Kabambala wa Radio Washirika Kids Time FM ya mkoani Morogoro nchini Tanzania alikuwa shuhuda wetu wa tukio hilo mkoani Kigoma. 
10/16/20230
Episode Artwork

Matarajio ya OCHA ni misaada ya kibinadamu kuruhusiwa kuingia Gaza

Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths, ameeleza wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa mzozo wa kibinadamu huko Gaza, Mashariki ya Kati, kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina, Hamas, halikadhalika hatma ya mateka wa Israel, huku pia akieleza matarajio yake ya kupokea habari njema za misaada kuruhusiwa kuingia Gaza. Akihojiwa jijini Geneva nchini Uswisi hii leo, na Idhaa ya Umoja wa Mataifa, Mkuu huyo wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA amezungumzia hali inayoendelea huko Mashariki ya Kati na kutaja mambo matatu.Mosi, ametaka mateka wa Israel wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto waliochukuliwa na wapiganaji wa Hamas waachiliwe mara moja. Pili, ametaka kuheshimiwa kwa sheria za kibinadamu kwenye vita akieleza kuwa “Huwezi kuwaeleza watu wahame kutoka kwenye hatari bila ya kuwasaidia kwenda mahali wanapotaka, ambako wanataka kuwa salama na kuwapa misaada ya kibinadamu ikayofanya safari yao hiyo kuwa salama. Akifafanua suala la misaada ya kibinadamu Griffiths amesema kwa sasa hospitali hazina nishati ya kujiendeesha, na wanakabiliwa na upungufu wa misaada hivyo watu hawawezi kuhama kutoka Gaza Kaskazini Kwenda Gaza Kusini bila ya Msaada. “Suala la tatu tunahitaji misaada”, amesisitiza Griffiths akieleza kuwa wanaendelea na mazungumzo na nchi za Israel, Misri na nyinginezo huku wakitarajia kupata habari njema.“Na ninatumai kusikia habari njema asubuhi ya leo kuhusu misaada kuruhusiwa kuingia huko Gaza kupitia mpaka wa Rafah, (Ulioko nchini Misri) kusaidia watu milioni moja waliohamia eneo hulo wakitokea Kaskazini pamoja na wakazi wa eneo hilo la kusini waliokuwepo muda wote. Na kumesisitiza katika hili “sheria za vita, misaada, na kuruhusiwa kupita” lazima zizingatiwe.Mkuu huyo wa Misaada ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa ametangaza kuwa hapo kesho yeye mwenyewe ataenda Mashariki ya Kati ili kusaidia kwenye mazungumzo pamoja na kuonesha mshikamano na wafanyakazi wa misaada ya kibinadamu ambao wamesalia kuendelea kutoa usaidizi kwa watu.  Amehitimisha taarifa yake kwa kueleza kueleza kuna maisha baada ya vita.  “Ninataka kuwaacha na wazo moja la mwisho. Historia inatuambia kwamba kitendo cha vita vina athari ambazo mara nyingi hazizingatiwi wakati watu wakiingia vitani. Tumeona filamu hii kwa mara nyingi sana. Tunahitaji kuwa na wasiwasi na kuunda hali ambayo kwa sasa itaonekana kama ya kipuuzi - ambapo Waisraeli na Wapalestina wanaweza kuishi kama majirani, kama marafiki, kwa hakika, kama wanaoingiliana, ambapo hawahitaji kupeana mafunzo kupitia vita. Asante.”
10/16/20230
Episode Artwork

Matarajio ya OCHA ni misaada ya kibinadamu kuruhusiwa kuingia Gaza

Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths, ameeleza wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa mzozo wa kibinadamu huko Gaza, Mashariki ya Kati, kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina, Hamas, halikadhalika hatma ya mateka wa Israel, huku pia akieleza matarajio yake ya kupokea habari njema za misaada kuruhusiwa kuingia Gaza. Akihojiwa jijini Geneva nchini Uswisi hii leo, na Idhaa ya Umoja wa Mataifa, Mkuu huyo wa ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura, OCHA amezungumzia hali inayoendelea huko Mashariki ya Kati na kutaja mambo matatu.Mosi, ametaka mateka wa Israel wengi wao wakiwa ni wanawake na watoto waliochukuliwa na wapiganaji wa Hamas waachiliwe mara moja. Pili, ametaka kuheshimiwa kwa sheria za kibinadamu kwenye vita akieleza kuwa “Huwezi kuwaeleza watu wahame kutoka kwenye hatari bila ya kuwasaidia kwenda mahali wanapotaka, ambako wanataka kuwa salama na kuwapa misaada ya kibinadamu ikayofanya safari yao hiyo kuwa salama. Akifafanua suala la misaada ya kibinadamu Griffiths amesema kwa sasa hospitali hazina nishati ya kujiendeesha, na wanakabiliwa na upungufu wa misaada hivyo watu hawawezi kuhama kutoka Gaza Kaskazini Kwenda Gaza Kusini bila ya Msaada. “Suala la tatu tunahitaji misaada”, amesisitiza Griffiths akieleza kuwa wanaendelea na mazungumzo na nchi za Israel, Misri na nyinginezo huku wakitarajia kupata habari njema.“Na ninatumai kusikia habari njema asubuhi ya leo kuhusu misaada kuruhusiwa kuingia huko Gaza kupitia mpaka wa Rafah, (Ulioko nchini Misri) kusaidia watu milioni moja waliohamia eneo hulo wakitokea Kaskazini pamoja na wakazi wa eneo hilo la kusini waliokuwepo muda wote. Na kumesisitiza katika hili “sheria za vita, misaada, na kuruhusiwa kupita” lazima zizingatiwe.Mkuu huyo wa Misaada ya Kibinadamu wa Umoja wa Mataifa ametangaza kuwa hapo kesho yeye mwenyewe ataenda Mashariki ya Kati ili kusaidia kwenye mazungumzo pamoja na kuonesha mshikamano na wafanyakazi wa misaada ya kibinadamu ambao wamesalia kuendelea kutoa usaidizi kwa watu.  Amehitimisha taarifa yake kwa kueleza kueleza kuna maisha baada ya vita.  “Ninataka kuwaacha na wazo moja la mwisho. Historia inatuambia kwamba kitendo cha vita vina athari ambazo mara nyingi hazizingatiwi wakati watu wakiingia vitani. Tumeona filamu hii kwa mara nyingi sana. Tunahitaji kuwa na wasiwasi na kuunda hali ambayo kwa sasa itaonekana kama ya kipuuzi - ambapo Waisraeli na Wapalestina wanaweza kuishi kama majirani, kama marafiki, kwa hakika, kama wanaoingiliana, ambapo hawahitaji kupeana mafunzo kupitia vita. Asante.”
10/16/20230
Episode Artwork

16 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia msaada wa kibinadamu Gaza, na siku ya chakula duniani. Makala tunakupeleka nchini Tanzania kushuhudia jinsi ambavyo FAO nchini humo umeinua wanawake wa kijijini. Mashinani tunasalia katika siku ya chakula duniani na tutasikia ujumbe kuhusu jinsi ambavyo wahamiaji wanavyoweza kusaidiwa kuhimili madhila ya mabadiliko ya tabianchi.Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths, ameeleza wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa mzozo wa kibinadamu huko Gaza, Mashariki ya Kati, kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina, Hamas, halikadhalika hatma ya mateka wa Israel, huku pia akieleza matarajio yake ya kupokea habari njema za misaada kuruhusiwa kuingia Gaza.Leo ni siku ya chakula duniani na maadhimisho ya mwaka huu kwa mujibu wa shirika na chakula na kilimo FAO yanasherehekea moja ya rasilimali muhimu zaidi kwa maisha ya binadamu ambayo ni maji, kwani yanachukua asilimia 50 ya uso wa dunia, yanazalisha chakula na kuwezesha watu kuishi. Makala leo inatupeleka Kigoma, magharibi mwa Tanzania ambako huko mradi wa pamoja wa Kigoma, KJP unaotekelezwa na shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO nchini humo umeinua wanawake wa kijijini, na mwenyeji wetu ni John Kabambala wa Radio Washirika Kids Time FM ya Morogoro nchini Tanzania.Na mashinani leo ikiwa ni siku ya chakula duniani tutasikia ujumbe kuhusu mifumo ya kilimo na njia mbadala ya kuwezesha jamii waathirika kuhimili changamoto za mabadiliko ya tabianchi.Mwenyeji wako ni Flora, karibu !
10/16/20230
Episode Artwork

16 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia msaada wa kibinadamu Gaza, na siku ya chakula duniani. Makala tunakupeleka nchini Tanzania kushuhudia jinsi ambavyo FAO nchini humo umeinua wanawake wa kijijini. Mashinani tunasalia katika siku ya chakula duniani na tutasikia ujumbe kuhusu jinsi ambavyo wahamiaji wanavyoweza kusaidiwa kuhimili madhila ya mabadiliko ya tabianchi.Mratibu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths, ameeleza wasiwasi wake juu ya kuongezeka kwa mzozo wa kibinadamu huko Gaza, Mashariki ya Kati, kutokana na mapigano yanayoendelea kati ya Israel na wanamgambo wa kipalestina, Hamas, halikadhalika hatma ya mateka wa Israel, huku pia akieleza matarajio yake ya kupokea habari njema za misaada kuruhusiwa kuingia Gaza.Leo ni siku ya chakula duniani na maadhimisho ya mwaka huu kwa mujibu wa shirika na chakula na kilimo FAO yanasherehekea moja ya rasilimali muhimu zaidi kwa maisha ya binadamu ambayo ni maji, kwani yanachukua asilimia 50 ya uso wa dunia, yanazalisha chakula na kuwezesha watu kuishi. Makala leo inatupeleka Kigoma, magharibi mwa Tanzania ambako huko mradi wa pamoja wa Kigoma, KJP unaotekelezwa na shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO nchini humo umeinua wanawake wa kijijini, na mwenyeji wetu ni John Kabambala wa Radio Washirika Kids Time FM ya Morogoro nchini Tanzania.Na mashinani leo ikiwa ni siku ya chakula duniani tutasikia ujumbe kuhusu mifumo ya kilimo na njia mbadala ya kuwezesha jamii waathirika kuhimili changamoto za mabadiliko ya tabianchi.Mwenyeji wako ni Flora, karibu !
10/16/20230
Episode Artwork

FAO inasisitiza kwamba maji ni uhai, maji ni chakula tusimwache yeyote nyuma katika hili

Leo ni siku ya chakula duniani na maadhimisho ya mwaka huu kwa mujibu wa shirika na chakula na kilimo FAO yanasherehekea moja ya rasilimali muhimu zaidi kwa maisha ya binadamu ambayo ni maji, kwani yanachukua asilimia 50 ya uso wa dunia, yanazalisha chakula na kuwezesha watu kuishi. Maudhui ya siku ya mwaka huu ni “Maji ni uhai, maji ni chakula, usimwache yeyote nyuma”.Pamoja na kwamba maji ndio kila kitu FAO imekumbusha kwamba rasilimali hiyo haidumu milele na dunia inahitaji kuacha kuichukulia kama mazoea kwani chakula kinacholiwa duniani na jinsi kinavyozalishwa vinaathiri rasilimali ya maji.Hivyo shirika hilo limesisitiza kwamba dunia “Kwa pamoja tunaweza kuchukua hatua kwa ajili ya chakula na kuwa mabadiliko yanayohitajika, kwani maji ni msingi kwa ajili ya maisha na chakula.”Akisisitiza umuhimu huo mkurugenzi mkuu wa FAO Qu Dongyu (TAMKA KYU DONGYU) amesema, "Mgogoro wa madadiliko ya tabianchi, ongezoko la idadi ya watu, ukuaji wa miji, maendeleo ya viwanda na maendeleo ya kiuchumi na kijamii vinaongeza shinikizo katik rasilimali ya maji.”Na kuongeza kuwa theluthi moja ya watu wote duniani wanaishi bila rasilimali hiyo muhimu hivyo changamoto hizo zinaleta athari kubwa kwa uhakika wa chakula  na ametoa wito wa kugeukia sayansi, ubunifu na teknolojia kuzitatua, “Lazima tukumbatie uwezo wa sayansi, ubunifu, takwimu na teknolojia kuzalisha zaidi kwa kutumia maji kidogo ili kufanya kila tone la maji kuwa na maana. Sote tunapswa kutumia na kudhibiti maji kwa ufanisi.”Ili kuendeleza azma hiyo ametaka sekta ya kilimo inayotumia asilimia 70 ya maji duniani kufanya mabadiliko ya mifumo yake ya chakula na ndio maana leo mjini Roma Italia FAO limenaza kongamano la siku nne litakalokamilika 20 Oktaba kujadili umuhimu wa sayansi, uvumbuzi na teknolojia katika kubadili mifumo ya chakula kuwa sehemu ya suluhu ya mabadiliko ya tabianchi.Ismahane Elouafi ni mkuu wa kitengo cha sayansi ya chakula na kilimo wa FAO anasema, “Kuanzia uvumbuzi wa teknolojia hadi uvumbuzi wa kifedha, uvumbuzi wa kitaasisi, uvumbuzi wa sera, ni katika wigo mzima wa uvumbuzi, na tunatumai kwamba mjadala kati ya wadau tofauti utaleta matokeo, je tunajua nini  hadi sasa, tunaweza kuongeza nini kwa sasa na ni wapi tunapaswa kuwekeza katika siku za usoni ili kuwa na msingi bora wa sayansi na ushahidi kwa ajili ya utungaji sera na kwa ajili ya mabadiliko ya mifumo ya kilimo ya chakula.”FAO inasema kampeni ya siku ya chakula mwaka huu ni kuelimisha dunia kuhusu umuhimu wa kutumia maji kwa ufanisi kwa sababu rasilimali hiyo iko katika tishio kubwa na huu ni wakati wa kufanyakazi pamoja na kujenga mustakbali bora, na endelevu kwa wote.
10/16/20230
Episode Artwork

FAO inasisitiza kwamba maji ni uhai, maji ni chakula tusimwache yeyote nyuma katika hili

Leo ni siku ya chakula duniani na maadhimisho ya mwaka huu kwa mujibu wa shirika na chakula na kilimo FAO yanasherehekea moja ya rasilimali muhimu zaidi kwa maisha ya binadamu ambayo ni maji, kwani yanachukua asilimia 50 ya uso wa dunia, yanazalisha chakula na kuwezesha watu kuishi. Maudhui ya siku ya mwaka huu ni “Maji ni uhai, maji ni chakula, usimwache yeyote nyuma”.Pamoja na kwamba maji ndio kila kitu FAO imekumbusha kwamba rasilimali hiyo haidumu milele na dunia inahitaji kuacha kuichukulia kama mazoea kwani chakula kinacholiwa duniani na jinsi kinavyozalishwa vinaathiri rasilimali ya maji.Hivyo shirika hilo limesisitiza kwamba dunia “Kwa pamoja tunaweza kuchukua hatua kwa ajili ya chakula na kuwa mabadiliko yanayohitajika, kwani maji ni msingi kwa ajili ya maisha na chakula.”Akisisitiza umuhimu huo mkurugenzi mkuu wa FAO Qu Dongyu (TAMKA KYU DONGYU) amesema, "Mgogoro wa madadiliko ya tabianchi, ongezoko la idadi ya watu, ukuaji wa miji, maendeleo ya viwanda na maendeleo ya kiuchumi na kijamii vinaongeza shinikizo katik rasilimali ya maji.”Na kuongeza kuwa theluthi moja ya watu wote duniani wanaishi bila rasilimali hiyo muhimu hivyo changamoto hizo zinaleta athari kubwa kwa uhakika wa chakula  na ametoa wito wa kugeukia sayansi, ubunifu na teknolojia kuzitatua, “Lazima tukumbatie uwezo wa sayansi, ubunifu, takwimu na teknolojia kuzalisha zaidi kwa kutumia maji kidogo ili kufanya kila tone la maji kuwa na maana. Sote tunapswa kutumia na kudhibiti maji kwa ufanisi.”Ili kuendeleza azma hiyo ametaka sekta ya kilimo inayotumia asilimia 70 ya maji duniani kufanya mabadiliko ya mifumo yake ya chakula na ndio maana leo mjini Roma Italia FAO limenaza kongamano la siku nne litakalokamilika 20 Oktaba kujadili umuhimu wa sayansi, uvumbuzi na teknolojia katika kubadili mifumo ya chakula kuwa sehemu ya suluhu ya mabadiliko ya tabianchi.Ismahane Elouafi ni mkuu wa kitengo cha sayansi ya chakula na kilimo wa FAO anasema, “Kuanzia uvumbuzi wa teknolojia hadi uvumbuzi wa kifedha, uvumbuzi wa kitaasisi, uvumbuzi wa sera, ni katika wigo mzima wa uvumbuzi, na tunatumai kwamba mjadala kati ya wadau tofauti utaleta matokeo, je tunajua nini  hadi sasa, tunaweza kuongeza nini kwa sasa na ni wapi tunapaswa kuwekeza katika siku za usoni ili kuwa na msingi bora wa sayansi na ushahidi kwa ajili ya utungaji sera na kwa ajili ya mabadiliko ya mifumo ya kilimo ya chakula.”FAO inasema kampeni ya siku ya chakula mwaka huu ni kuelimisha dunia kuhusu umuhimu wa kutumia maji kwa ufanisi kwa sababu rasilimali hiyo iko katika tishio kubwa na huu ni wakati wa kufanyakazi pamoja na kujenga mustakbali bora, na endelevu kwa wote.
10/16/20230
Episode Artwork

Tanzania tumepiga hatua kubwa kupambana na kifua kikuu: Waziri Ummy Mwalimu

Kifua kikuu au TB ni moja ya changamoto kubwa za kiafya duniani na janga ni kubwa zaidi Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO duniani kote, TB ni sababu ya 13 inayoongoza kwa vifo na ya pili muuaji wa magonjwa ya kuambukiza baada ya COVID-19 ikiwa juu ya VVU na Ukimwi. Shirika hilo linakadiria kwamba mwaka 2021, takriban watu milioni 10.6 waliugua kifua kikuu kote duniani wakiwemo wanaume milioni sita, wanawake milioni 3.4 na watoto milioni 1.2. Na shirika hilo loimesisitiza kuwa TB iko katika nchi zote na inaathiri makundi ya umri wote ndio maana wakati wa mkutano mkuu wa Baraza Kuu mwezi septemba TB ilikuwa moja wa mada zilizojadiliwa kandoni na mjadala wa Baraza Kuu ukizitaka nchi kuchukua hatua kuutokomeza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030. Tanzania ilishiriki mkutano huo na waziri wake wa afya ummy Mwalimu alimweleza Flora Nducha wa idhaa hii ya Kiswahili hatua wanazochukua katika vita dhidi ya TB.
10/13/20230
Episode Artwork

Tanzania tumepiga hatua kubwa kupambana na kifua kikuu: Waziri Ummy Mwalimu

Kifua kikuu au TB ni moja ya changamoto kubwa za kiafya duniani na janga ni kubwa zaidi Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara. Kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO duniani kote, TB ni sababu ya 13 inayoongoza kwa vifo na ya pili muuaji wa magonjwa ya kuambukiza baada ya COVID-19 ikiwa juu ya VVU na Ukimwi. Shirika hilo linakadiria kwamba mwaka 2021, takriban watu milioni 10.6 waliugua kifua kikuu kote duniani wakiwemo wanaume milioni sita, wanawake milioni 3.4 na watoto milioni 1.2. Na shirika hilo loimesisitiza kuwa TB iko katika nchi zote na inaathiri makundi ya umri wote ndio maana wakati wa mkutano mkuu wa Baraza Kuu mwezi septemba TB ilikuwa moja wa mada zilizojadiliwa kandoni na mjadala wa Baraza Kuu ukizitaka nchi kuchukua hatua kuutokomeza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030. Tanzania ilishiriki mkutano huo na waziri wake wa afya ummy Mwalimu alimweleza Flora Nducha wa idhaa hii ya Kiswahili hatua wanazochukua katika vita dhidi ya TB.
10/13/20230
Episode Artwork

Raia katika ukanda wa Gaza hawana pa kukimbilia, milioni 1 waambiwa waondoke ndani ya saa 24: UN

Leo ni siku nyingine ambapo hali imeendelea kuwa tete na mbayá zaidi kwenye Ukanda wa Gaza, kwani Israel imetangaza watu wote wanaoishi katika eneo la Kaskazini mwa Wadi Gaza kuondoka na kwenda Kusini mwa Gaza ndani ya saa 24 na hivyo kuwaacha njiapanda maelfu kwa maelfu ya watu wanaoishi eneo hilo yamesema mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo ambayo yanahaha kuwasaidia na kuwanusuru watu hao. Umoja wa Mataifa umesema amri hiyo ya watu kuondona inawaathiri zaidi ya Wapalestina milioni moja wakiwemo watoto, wazee na wagonjwa ikiwalazimisha kuhamia kwingine wakati hawana chochote na hata usafiri, pia kukiwa na hakikisho dogo sana kwa ajili ya usalama wao wakati mashambulizi yakiendelea.Umoja wa Mataifa unasema unadhani itakuwa vigumu sana kuendesha shughuli hiyo ya kuhama bila kuleta madhara makubwa ya kibinadamu, hivyo umeto ombi la kufuta amri hiyo ili kuepuka zahma kubwa zaidi katika hali ambayo tayari ni mbayá.Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ametoa wito kwa mataifa yote kusisitiza na kuzisaidia pande kinzani katika mzozo kutekeleza utoaji mwanya wa fursa ya misaada ya kibinadamu ili kuhakikisha msaada unaohitajika haraka unawafikia wenye uhitaji.Pia ameonya kwamba katika nchi nyingi hivi sasa kumekuwa na ongezeko la chuki dhidi ya Wayahudi na kauli za chuki dhidi ya Uislam amelaani vikali hayo.Ndani ya Gaza kamisha mkuu wa shirika laumoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA Philippe Lazzarini amezitaka pande zote na wale wenye ushawishi juu ya pande hizo kukomesha madhila yanayoendelea na kuhakikisha msaada na ulinzi kwa raia wote.Amesisitiza kwamba amri iliyotangazwa na Israel kutaka zaidi ya watu milioni moja kuondoka” Hii itasababisha janga kubwa ambalo halijawahi kushuhudiwa na kuwasukuma zaidi jehanamu watu wa Gaza.”Ili kutoa msaada ipasavyo Umoja wa Mataifa unasema fedha zinahitajika ndio maana leo shirika lake la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA limezindua ombi la dola milioni 249 kwa ajili ya washirika wake wa kibinadamu 77 watakaokuwa wakihudumia mahitaji ya haraka ya watu milioni 1.26 Gaza na kwenye Ukingo wa Magharibi.Na shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa UNICEF limeonya kuhusu vifo, majeruhi na machungu wanayopitia watoto wasio na hatia katika mzozo huu , huku lile la afya duniani WHO likisema mfumo wa afya Gaza hauana uwezo tena wa kutoa huduma zinazohitajika hasa kutokana na hospital nyingi kusambaratishwa na makombora na kutokuwa na vifaa vinavyohitajika.Wito wa mashirika haya ni mmoja tu, mgogoro huu lazima ukome mara moja kunusuru maisha ya raia wa pande zote mbili. 
10/13/20230
Episode Artwork

Raia katika ukanda wa Gaza hawana pa kukimbilia, milioni 1 waambiwa waondoke ndani ya saa 24: UN

Leo ni siku nyingine ambapo hali imeendelea kuwa tete na mbayá zaidi kwenye Ukanda wa Gaza, kwani Israel imetangaza watu wote wanaoishi katika eneo la Kaskazini mwa Wadi Gaza kuondoka na kwenda Kusini mwa Gaza ndani ya saa 24 na hivyo kuwaacha njiapanda maelfu kwa maelfu ya watu wanaoishi eneo hilo yamesema mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo ambayo yanahaha kuwasaidia na kuwanusuru watu hao. Umoja wa Mataifa umesema amri hiyo ya watu kuondona inawaathiri zaidi ya Wapalestina milioni moja wakiwemo watoto, wazee na wagonjwa ikiwalazimisha kuhamia kwingine wakati hawana chochote na hata usafiri, pia kukiwa na hakikisho dogo sana kwa ajili ya usalama wao wakati mashambulizi yakiendelea.Umoja wa Mataifa unasema unadhani itakuwa vigumu sana kuendesha shughuli hiyo ya kuhama bila kuleta madhara makubwa ya kibinadamu, hivyo umeto ombi la kufuta amri hiyo ili kuepuka zahma kubwa zaidi katika hali ambayo tayari ni mbayá.Kamishina mkuu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ametoa wito kwa mataifa yote kusisitiza na kuzisaidia pande kinzani katika mzozo kutekeleza utoaji mwanya wa fursa ya misaada ya kibinadamu ili kuhakikisha msaada unaohitajika haraka unawafikia wenye uhitaji.Pia ameonya kwamba katika nchi nyingi hivi sasa kumekuwa na ongezeko la chuki dhidi ya Wayahudi na kauli za chuki dhidi ya Uislam amelaani vikali hayo.Ndani ya Gaza kamisha mkuu wa shirika laumoja wa Mataifa la msaada kwa wakimbizi wa Kipalestina UNRWA Philippe Lazzarini amezitaka pande zote na wale wenye ushawishi juu ya pande hizo kukomesha madhila yanayoendelea na kuhakikisha msaada na ulinzi kwa raia wote.Amesisitiza kwamba amri iliyotangazwa na Israel kutaka zaidi ya watu milioni moja kuondoka” Hii itasababisha janga kubwa ambalo halijawahi kushuhudiwa na kuwasukuma zaidi jehanamu watu wa Gaza.”Ili kutoa msaada ipasavyo Umoja wa Mataifa unasema fedha zinahitajika ndio maana leo shirika lake la kuratibu misaada ya kibinadamu na masuala ya dharura OCHA limezindua ombi la dola milioni 249 kwa ajili ya washirika wake wa kibinadamu 77 watakaokuwa wakihudumia mahitaji ya haraka ya watu milioni 1.26 Gaza na kwenye Ukingo wa Magharibi.Na shirika la kuhudumia watoto la Umoja wa Mataifa UNICEF limeonya kuhusu vifo, majeruhi na machungu wanayopitia watoto wasio na hatia katika mzozo huu , huku lile la afya duniani WHO likisema mfumo wa afya Gaza hauana uwezo tena wa kutoa huduma zinazohitajika hasa kutokana na hospital nyingi kusambaratishwa na makombora na kutokuwa na vifaa vinavyohitajika.Wito wa mashirika haya ni mmoja tu, mgogoro huu lazima ukome mara moja kunusuru maisha ya raia wa pande zote mbili. 
10/13/20230
Episode Artwork

13 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia athari za majanga na ujumuishwaji katika utoaji wa maonyo ya mapema, na pia machafuko mashariki ya kati.  Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani tunasalia hapa makau makuu, kulikoni?Leo ni siku nyingine ambapo hali imeendelea kuwa tete na mbayá zaidi kwenye Ukanda wa Gaza, kwani Israel imetangaza watu wote wanaoishi katika eneo la Kaskazini mwa Wadi Gaza kuondoka na kwenda Kusini mwa Gaza ndani ya saa 24 na hivyo kuwaacha njiapanda maelfu kwa maelfu ya watu wanaoishi eneo hilo yamesema mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo ambayo yanahaha kuwasaidia na kuwanusuru watu hao. Ufilipino ni mojawapo ya nchi zinazokabiliwa zaidi na hatari za majanga duniani, jimboni Samar Kaskazini, hatari kwa watoto ni kubwa zaidi ndio maana Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linafanya kazi na serikali za mtaa ili kuwashirikisha watoto na vijana katika hatua za kujiandaa na hatari pamoja na kupunguza athari za majanga. Makala leo inamulika jitihada za kupambana na ugonjwa wa kifua kikuu au TB nchini Tanzania.Kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO watu milioni 10.6 walikufa kwa TB mwaka 2021 na nchi za afrika Kusini mwa janga la Sahara ndizo zinazobeba mzigo mkubwa wa ugonjwa hu. Flora Nducha wa Idhaa akizungumza na waziri wa afya wa Tanzania Ummy Mwalimu wakati wa mkutano kuhusu kifua kuu kandoni ya mjada mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwezi Septemba alitaka kufahamu nchi hiyo inafanya nini kutokomeza TB ifikapo 2030.Na mashinani tunakuletea ujumbe kuhusu athari za majanga kwa watu wasiojiweza..Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu !
10/13/20230
Episode Artwork

13 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia athari za majanga na ujumuishwaji katika utoaji wa maonyo ya mapema, na pia machafuko mashariki ya kati.  Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani tunasalia hapa makau makuu, kulikoni?Leo ni siku nyingine ambapo hali imeendelea kuwa tete na mbayá zaidi kwenye Ukanda wa Gaza, kwani Israel imetangaza watu wote wanaoishi katika eneo la Kaskazini mwa Wadi Gaza kuondoka na kwenda Kusini mwa Gaza ndani ya saa 24 na hivyo kuwaacha njiapanda maelfu kwa maelfu ya watu wanaoishi eneo hilo yamesema mashirika ya Umoja wa Mataifa hii leo ambayo yanahaha kuwasaidia na kuwanusuru watu hao. Ufilipino ni mojawapo ya nchi zinazokabiliwa zaidi na hatari za majanga duniani, jimboni Samar Kaskazini, hatari kwa watoto ni kubwa zaidi ndio maana Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linafanya kazi na serikali za mtaa ili kuwashirikisha watoto na vijana katika hatua za kujiandaa na hatari pamoja na kupunguza athari za majanga. Makala leo inamulika jitihada za kupambana na ugonjwa wa kifua kikuu au TB nchini Tanzania.Kwa mujibu wa shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO watu milioni 10.6 walikufa kwa TB mwaka 2021 na nchi za afrika Kusini mwa janga la Sahara ndizo zinazobeba mzigo mkubwa wa ugonjwa hu. Flora Nducha wa Idhaa akizungumza na waziri wa afya wa Tanzania Ummy Mwalimu wakati wa mkutano kuhusu kifua kuu kandoni ya mjada mkuu wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa mwezi Septemba alitaka kufahamu nchi hiyo inafanya nini kutokomeza TB ifikapo 2030.Na mashinani tunakuletea ujumbe kuhusu athari za majanga kwa watu wasiojiweza..Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu !
10/13/20230
Episode Artwork

Tushirikishe watoto katika kujiandaa na athari za majanga unamanufaa - UNICEF

Ufilipino ni mojawapo ya nchi zinazokabiliwa zaidi na hatari za majanga duniani, jimboni Samar Kaskazini, hatari kwa watoto ni kubwa zaidi ndio maana Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linafanya kazi na serikali za mtaa ili kuwashirikisha watoto na vijana katika hatua za kujiandaa na hatari pamoja na kupunguza athari za majanga kama anavyotujuza Leah Mushi katika taarifa hii aliyotuandalia.Manispaa ya Mapanas iliyoko jimboni Samar Kaskazini nchini Ufilipino kutokana na kuathirika mara kwa mara na vimbunga pamoja na dhoruba mwaka 2014 UNICEF na Kituo cha Kukabiliana na Majanga kwa wananchi walizindua kituo cha Kupunguza Hatari za Majanga kwa Watoto- CCDRR. Gary Lavin ni Makamu Ganava wa jimbo la Samar Kaskazini anasema lengo la kituo hicho ni kuwajengea watoto na vijana uelewa kuhusu majanga na kuwashirikisha katika kusaka majawabu wakati wa majanga. “Lazima tuwalinde watoto na vijana kwa mustakabali si wa jamii yetu na jimbo letu pekee, bali taifa zima ndio maana tunatakiwa kuhakikisha wanakuwa salama wakati wa majanga na wanapewa ulinzi unaostahili.”Kituo hicho kinawafundisha hatua kwa hatua namna ya kupunguza athari za majanga kama anavyoeleza Faye Anne Bandilla Rais wa Kituo hicho ambaye pia ni kijana. Faye Anne Bandilla – Msichana “Kituo hiki kinahusishwa watoto na vijana kuanzia kwenye ngazi zote kuanzia kwenye kupanga, kwasababu kuna hatari ambazo watoto wanaziana lakini watu wazima hawazioni” Kupitia Program hiyo inayofadhiliwa na UNICEF shule pia zilifundishwa namna ya kuunganisha kujikinga na majanga kwenye mitaala yao kama anavyoeleza mwalimu Mayla Bricio. “Programu ya Kupunguza Hatari za Majanga kwa Watoto ilipokuja tulianza kuunganisha kujiandaa na majanga katika karibu masomo yote. Kwakufanya hivyo tunahakikisha kwamba kila mtoto anajua jinsi ya kujiandaa kwa ajili ya majanga.”Kupitia shirika lisilo la kiserikali la KKK watoto na vijana walihamasishwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kupunguza maafa ikiwemo upandaji miti na kuandaa ramani shirikishi 3D Mapping ambayo inaeleza waende wapi na wafanye nini majanga yanapotokea.Vijana pia wamepata nafasi katika Baraza la Manispaa, wanapaza sauti zao kueleza nini wanahitaji na hii imewezesha manispaa kutekeleza mahitaji yao na kutunga sera zenye kuzingatia mahitaji ya watoto na vijana. Jolan Baguo ni kijana mwanachama wa KKK na anasema …. “Kabla ya programu hii, majanga yalipotokea tulikuwa tunakimbilia kwenye vituo vya kujiokoa tukiwa na wasiwasi bila ya kujua tutafanya nini, lakini baada ya CCDRR hatimaye nikawa mmoja wa vijana waliowezesha kuwahamisha watu na kuwaweka maeneo salama.”Programu hii iliyowezeshwa na UNICEF imethibitisha umuhimu wa ushirikishaji wa jamii nzima kwenye kila ngazi ya maamuzi na kubwa zaidi imetengenezwa kwa namna ambayo hata uongozi wa kisiasa ukibadilika na ufadhili wa programu ukiisha bado watoto na vijana wataendelea kushiriki kwenye kufanya maamuzi kwa masuala yahusuyo maslahi yao. 
10/13/20230
Episode Artwork

Tushirikishe watoto katika kujiandaa na athari za majanga unamanufaa - UNICEF

Ufilipino ni mojawapo ya nchi zinazokabiliwa zaidi na hatari za majanga duniani, jimboni Samar Kaskazini, hatari kwa watoto ni kubwa zaidi ndio maana Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF linafanya kazi na serikali za mtaa ili kuwashirikisha watoto na vijana katika hatua za kujiandaa na hatari pamoja na kupunguza athari za majanga kama anavyotujuza Leah Mushi katika taarifa hii aliyotuandalia.Manispaa ya Mapanas iliyoko jimboni Samar Kaskazini nchini Ufilipino kutokana na kuathirika mara kwa mara na vimbunga pamoja na dhoruba mwaka 2014 UNICEF na Kituo cha Kukabiliana na Majanga kwa wananchi walizindua kituo cha Kupunguza Hatari za Majanga kwa Watoto- CCDRR. Gary Lavin ni Makamu Ganava wa jimbo la Samar Kaskazini anasema lengo la kituo hicho ni kuwajengea watoto na vijana uelewa kuhusu majanga na kuwashirikisha katika kusaka majawabu wakati wa majanga. “Lazima tuwalinde watoto na vijana kwa mustakabali si wa jamii yetu na jimbo letu pekee, bali taifa zima ndio maana tunatakiwa kuhakikisha wanakuwa salama wakati wa majanga na wanapewa ulinzi unaostahili.”Kituo hicho kinawafundisha hatua kwa hatua namna ya kupunguza athari za majanga kama anavyoeleza Faye Anne Bandilla Rais wa Kituo hicho ambaye pia ni kijana. Faye Anne Bandilla – Msichana “Kituo hiki kinahusishwa watoto na vijana kuanzia kwenye ngazi zote kuanzia kwenye kupanga, kwasababu kuna hatari ambazo watoto wanaziana lakini watu wazima hawazioni” Kupitia Program hiyo inayofadhiliwa na UNICEF shule pia zilifundishwa namna ya kuunganisha kujikinga na majanga kwenye mitaala yao kama anavyoeleza mwalimu Mayla Bricio. “Programu ya Kupunguza Hatari za Majanga kwa Watoto ilipokuja tulianza kuunganisha kujiandaa na majanga katika karibu masomo yote. Kwakufanya hivyo tunahakikisha kwamba kila mtoto anajua jinsi ya kujiandaa kwa ajili ya majanga.”Kupitia shirika lisilo la kiserikali la KKK watoto na vijana walihamasishwa kushiriki katika shughuli mbalimbali za kupunguza maafa ikiwemo upandaji miti na kuandaa ramani shirikishi 3D Mapping ambayo inaeleza waende wapi na wafanye nini majanga yanapotokea.Vijana pia wamepata nafasi katika Baraza la Manispaa, wanapaza sauti zao kueleza nini wanahitaji na hii imewezesha manispaa kutekeleza mahitaji yao na kutunga sera zenye kuzingatia mahitaji ya watoto na vijana. Jolan Baguo ni kijana mwanachama wa KKK na anasema …. “Kabla ya programu hii, majanga yalipotokea tulikuwa tunakimbilia kwenye vituo vya kujiokoa tukiwa na wasiwasi bila ya kujua tutafanya nini, lakini baada ya CCDRR hatimaye nikawa mmoja wa vijana waliowezesha kuwahamisha watu na kuwaweka maeneo salama.”Programu hii iliyowezeshwa na UNICEF imethibitisha umuhimu wa ushirikishaji wa jamii nzima kwenye kila ngazi ya maamuzi na kubwa zaidi imetengenezwa kwa namna ambayo hata uongozi wa kisiasa ukibadilika na ufadhili wa programu ukiisha bado watoto na vijana wataendelea kushiriki kwenye kufanya maamuzi kwa masuala yahusuyo maslahi yao. 
10/13/20230
Episode Artwork

METHALI: SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Jino la P Na leo katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI, KARIBU! 
10/12/20230
Episode Artwork

METHALI: SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Jino la P Na leo katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI, KARIBU! 
10/12/20230
Episode Artwork

12 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo tunaangazia moja ya miradi ya Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) unaotelelezwa katika kisiwa cha Pemba nchini Tanzania. Evarist Mapesa anatupitisha katika Bahari ya Hindi hadi visiwani humo. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na kataika kujifunza lugha ya Kiswahili leo tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI.Hii leo ikiwa ni siku ya 6 ya mapigano huko Mashriki ya Kati, kati ya Israeli na Palestina idadi ya waliouawa upande wa Palestina inatajwa kuwa ni 1,100 ihali Israeli ni 1,200, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA, likiongeza kuwa miongoni mwa waliouawa ni wafanyakazi wake 12.Tukisalia huko Gaza, shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani, WFP linasema kuna hatari ya eneo hilo kukosa chakula, maji, umeme na vifaa muhimu kutokana na ukata, hivyo usaidizi wa kifedha kwa shirika hilo unahitajika. Tayari WFP na UNRWA wamesambaza mikate, na chakula kwa wakimbizi 137,000 wanaoishi kwenye makazi ya muda, na mpango ni kufikia watu 800,000 katika eneo lote la Palestina.Na huko nchini Tanzania kuelekea siku ya chakula duniani tarehe 16 mwezi huu wa Oktoba, shirika la Umoja wa Mataifa chakula na kilimo, FAO limeanza kuelimisha watoto kuhusu lishe bora kupitia mafunzo ya mapishi, Alfonsina Paul ni miongoni mwa wanafunzi walionufaika na na ujumbe.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Jino la P Na leo katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/12/20230
Episode Artwork

12 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo tunaangazia moja ya miradi ya Mfuko wa Umoja wa Mataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) unaotelelezwa katika kisiwa cha Pemba nchini Tanzania. Evarist Mapesa anatupitisha katika Bahari ya Hindi hadi visiwani humo. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na kataika kujifunza lugha ya Kiswahili leo tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI.Hii leo ikiwa ni siku ya 6 ya mapigano huko Mashriki ya Kati, kati ya Israeli na Palestina idadi ya waliouawa upande wa Palestina inatajwa kuwa ni 1,100 ihali Israeli ni 1,200, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA, likiongeza kuwa miongoni mwa waliouawa ni wafanyakazi wake 12.Tukisalia huko Gaza, shirika la Umoja wa Mataifa la mpango wa chakula duniani, WFP linasema kuna hatari ya eneo hilo kukosa chakula, maji, umeme na vifaa muhimu kutokana na ukata, hivyo usaidizi wa kifedha kwa shirika hilo unahitajika. Tayari WFP na UNRWA wamesambaza mikate, na chakula kwa wakimbizi 137,000 wanaoishi kwenye makazi ya muda, na mpango ni kufikia watu 800,000 katika eneo lote la Palestina.Na huko nchini Tanzania kuelekea siku ya chakula duniani tarehe 16 mwezi huu wa Oktoba, shirika la Umoja wa Mataifa chakula na kilimo, FAO limeanza kuelimisha watoto kuhusu lishe bora kupitia mafunzo ya mapishi, Alfonsina Paul ni miongoni mwa wanafunzi walionufaika na na ujumbe.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Jino la P Na leo katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali methali SHIMO LA ULIMI MKONO HAUFUTIKI.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/12/20230
Episode Artwork

Usambazaji wa misaada ya chakula kwa wahitaji Gaza umeanza - WFP

Ikiwa leo ni siku ya tano ya mzozo kati ya Israeli na Palestina huko Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan, mashirika ya Umoja wa Mataifa yamepiga kambi kuhakikisha yanafikisha misaada kwa wahitaji wakati huu ambapo mapigano hayo yamefurusha takribani watu 246, 000 kutoka ukanda wa Gaza pekee. Mashirika hayo ni pamoja na lile la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP ambalo limeanza kugawa mikate, vyakula vya makopo na vingine vilivyo tayari kuliwa kwa takribani watu 100,000 waliosaka hifadhi kwenye maeneo ya hifadhi ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA huko Gaza. Lengo la UNRWA ni kwamba operesheni hii ya dharura ifikishe misaada kwa zaidi ya watu 800,000. Ikumbukwe kuwa idadi hii ni pamoja na wakimbizi wa zamani waliokuwa wanahifadhiwa na UNRWA.Mkurugenzi Mkazi wa WFP  huko Palestina Samer Abdeljaber anasema tuko hapa kwenye enep na tunafanya  kila tuwezalo kuhakikisha wahitaji waliofurushwa makwao ambao wanaishi kwenye makazi ya muda wanapata chakula na msaada wanaohitaji ili waweze kuishi. Tutaanza pia kutoka vocha za fedha ili watu waweze kununua chakula kutoka kwenye maduka yaliyo bado wazi.Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF nalo pia liko Gaza likisambaza misaada ya kiutu.WFP inasihi pande kinzani kuhakikisha njia za usambazaji chakula ziko wazi ili misaada ifikie wahitaji huku ikitoa ombi la dola milioni 17.3 ili kufanikisha operesheni zake za dharura kwa wiki nne zijazo kwani mzozo huu umelipuka wakati tayari ukata ulikuwa unalikabili na kulazimu mwezi Juni kukata misaada kwa maelfu ya familia za kipalestina zisizo na uwezo.Wakati huo huo UNRWA kupitia mtandao wa X inasema tangu Jumamosi hadi hii leo watumishi wake 9 wameuawa kwenye mashambulizi hayo huko Gaza.
10/11/20230
Episode Artwork

Usambazaji wa misaada ya chakula kwa wahitaji Gaza umeanza - WFP

Ikiwa leo ni siku ya tano ya mzozo kati ya Israeli na Palestina huko Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan, mashirika ya Umoja wa Mataifa yamepiga kambi kuhakikisha yanafikisha misaada kwa wahitaji wakati huu ambapo mapigano hayo yamefurusha takribani watu 246, 000 kutoka ukanda wa Gaza pekee. Mashirika hayo ni pamoja na lile la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP ambalo limeanza kugawa mikate, vyakula vya makopo na vingine vilivyo tayari kuliwa kwa takribani watu 100,000 waliosaka hifadhi kwenye maeneo ya hifadhi ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA huko Gaza. Lengo la UNRWA ni kwamba operesheni hii ya dharura ifikishe misaada kwa zaidi ya watu 800,000. Ikumbukwe kuwa idadi hii ni pamoja na wakimbizi wa zamani waliokuwa wanahifadhiwa na UNRWA.Mkurugenzi Mkazi wa WFP  huko Palestina Samer Abdeljaber anasema tuko hapa kwenye enep na tunafanya  kila tuwezalo kuhakikisha wahitaji waliofurushwa makwao ambao wanaishi kwenye makazi ya muda wanapata chakula na msaada wanaohitaji ili waweze kuishi. Tutaanza pia kutoka vocha za fedha ili watu waweze kununua chakula kutoka kwenye maduka yaliyo bado wazi.Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF nalo pia liko Gaza likisambaza misaada ya kiutu.WFP inasihi pande kinzani kuhakikisha njia za usambazaji chakula ziko wazi ili misaada ifikie wahitaji huku ikitoa ombi la dola milioni 17.3 ili kufanikisha operesheni zake za dharura kwa wiki nne zijazo kwani mzozo huu umelipuka wakati tayari ukata ulikuwa unalikabili na kulazimu mwezi Juni kukata misaada kwa maelfu ya familia za kipalestina zisizo na uwezo.Wakati huo huo UNRWA kupitia mtandao wa X inasema tangu Jumamosi hadi hii leo watumishi wake 9 wameuawa kwenye mashambulizi hayo huko Gaza.
10/11/20230
Episode Artwork

11 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati, na mradi wa maji Baringo nchini Kenya. Makala tunakuletea uchambuzi wa Ibara ya 10 ya tamko la haki za binadamu na mashinani tunamulika siku ya mtoto wa kike duniani inayoadhimishwa kila mwaka Oktoba 11 kila mwaka ambayo ni leo.  Ikiwa leo ni siku ya tano ya mzozo kati ya Israeli na Palestina huko Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan, mashirika ya Umoja wa Mataifa yamepiga kambi kuhakikisha yanafikisha misaada kwa wahitaji wakati huu ambapo mapigano hayo yamefurusha takribani watu 246, 000 kutoka ukanda wa Gaza pekee..Uhakika wa upatikanaji wa maji ni moja ya majawabu ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi hususan katika maeneo yanayokabiliwa na ukame. Ni kwa kutambua hilo, huko nchini Kenya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani WFP kwa kushirikiana na serikali wamewezesha wananchi wa kaunti ya Baringo kuondokana na adha ya maji..Makala leo inaangaza Ibara ya 10 ya tamko la haki za binadamu. Je ibara hiyo inasema nini?  Na Inatekelezwa ipasavyo hasa barani Afrika? Kujibu maswali hayo Pamela Awuori wa Idhaa hii amezungumza na wakili wa mahakama kuu ya Kenya Kevin Ngetich.Katika mashinani tunamulika siku ya mtoto wa kike duniani inayoadhimishwa kila mwaka Oktoba 11 kila mwaka ambayo ni leo.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/11/20230
Episode Artwork

11 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko mashariki ya kati, na mradi wa maji Baringo nchini Kenya. Makala tunakuletea uchambuzi wa Ibara ya 10 ya tamko la haki za binadamu na mashinani tunamulika siku ya mtoto wa kike duniani inayoadhimishwa kila mwaka Oktoba 11 kila mwaka ambayo ni leo.  Ikiwa leo ni siku ya tano ya mzozo kati ya Israeli na Palestina huko Ukanda wa Gaza na Ukingo wa Magharibi mwa mto Jordan, mashirika ya Umoja wa Mataifa yamepiga kambi kuhakikisha yanafikisha misaada kwa wahitaji wakati huu ambapo mapigano hayo yamefurusha takribani watu 246, 000 kutoka ukanda wa Gaza pekee..Uhakika wa upatikanaji wa maji ni moja ya majawabu ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi hususan katika maeneo yanayokabiliwa na ukame. Ni kwa kutambua hilo, huko nchini Kenya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani WFP kwa kushirikiana na serikali wamewezesha wananchi wa kaunti ya Baringo kuondokana na adha ya maji..Makala leo inaangaza Ibara ya 10 ya tamko la haki za binadamu. Je ibara hiyo inasema nini?  Na Inatekelezwa ipasavyo hasa barani Afrika? Kujibu maswali hayo Pamela Awuori wa Idhaa hii amezungumza na wakili wa mahakama kuu ya Kenya Kevin Ngetich.Katika mashinani tunamulika siku ya mtoto wa kike duniani inayoadhimishwa kila mwaka Oktoba 11 kila mwaka ambayo ni leo.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/11/20230
Episode Artwork

Wenyeji Baringo nchini Kenya wanufaika kufuatia mradi wa maji wa WFP

Uhakika wa upatikanaji wa maji ni moja ya suluhisho za kupambana na mabadiliko ya tabianchi hususan katika maeneo yanayokabiliwa na ukame. Nchini Kenya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani WFP kwakushirikiana na serikali wamewezesha wananchi wa kaunti ya Baringo kuondokana na adha ya maji. Kwa miaka takriban 40 wananchi wa Kaunti ya Baringo nchini Kenya wamekuwa wakitaabika na uhaba wa maji kutokana na ukame unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi. Hali hiyo imewafanya wananchi hao kuwa tegemezi wa chakula kwa kwakuwa wamekosa maji ya kulisha mifugo yao na kilimo. Kutokana na adha hiyo WFP kwa kushirikiana na wadau wake na serikali ya Kenya imetekeleza mradi wa kuchimba visima mradi ambao Naibu gavana wa kaunti ya Baringo Felix Kimaiyo anasema unaenda kubadili maisha ya wananchi. “Mradi huu utakuwa muhimu sana kwa sababu unaenda kugusa maisha ya watu hawa na kuweza kupunguza maswala mengi na kuhakikisha kuwa eneo hili kuna uhakika wa upatikanaji wa chakula”Naam, na WFP mpaka sasa imefanikisha kuchimba visima 74 na vingine 22 vikiendelea kuchimvwa. Na mabadiliko yanaonekana kwani mifugo imepata maji, kilimo cha umwagiliaji kinaendelea na matumizi mengine ya majumbani pamoja na shuleni kama anavyothibitisha Lilian Ruto Mkazi wa Kijiji cha Kapkut ambaye pia ni mkulima wa mbogamboga wa kikundi cha kina mama wa Eitui. “Mahali tulikuwa tunatoa maji kulikuwa mbali sana na ilikuwa inatuchukua muda ili uweze kufikisha maji nyumbani ndio uende kuendelea na kazi zako za nyumbani. Kwahiyo tunashukuru sana kwasababu maji yamefika.“ Bi.Ruto anasema sasa hawategemeai tena chakula cha msaada kwani wanaweza kulima wenyewe na lishe za watoto wao zimeimarika.  “Sasa kwasababu tumepata maji tunajua sasa tuta tengeneza bustani tupande vyakula vyenye lishe ili kuhakikisha watoto wetu wanapata lishe bora.”WFP inafanya kazi kwa karibu na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa ikiwemo UNICEF, UNEP, FAO na IFAD kuhamasisha matumizi bora ya maji kwa afya, uhakika wa upatikanaji wa chakula na ustawi bora wa maisha yao. 
10/11/20230
Episode Artwork

Wenyeji Baringo nchini Kenya wanufaika kufuatia mradi wa maji wa WFP

Uhakika wa upatikanaji wa maji ni moja ya suluhisho za kupambana na mabadiliko ya tabianchi hususan katika maeneo yanayokabiliwa na ukame. Nchini Kenya Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani WFP kwakushirikiana na serikali wamewezesha wananchi wa kaunti ya Baringo kuondokana na adha ya maji. Kwa miaka takriban 40 wananchi wa Kaunti ya Baringo nchini Kenya wamekuwa wakitaabika na uhaba wa maji kutokana na ukame unaosababishwa na mabadiliko ya tabianchi. Hali hiyo imewafanya wananchi hao kuwa tegemezi wa chakula kwa kwakuwa wamekosa maji ya kulisha mifugo yao na kilimo. Kutokana na adha hiyo WFP kwa kushirikiana na wadau wake na serikali ya Kenya imetekeleza mradi wa kuchimba visima mradi ambao Naibu gavana wa kaunti ya Baringo Felix Kimaiyo anasema unaenda kubadili maisha ya wananchi. “Mradi huu utakuwa muhimu sana kwa sababu unaenda kugusa maisha ya watu hawa na kuweza kupunguza maswala mengi na kuhakikisha kuwa eneo hili kuna uhakika wa upatikanaji wa chakula”Naam, na WFP mpaka sasa imefanikisha kuchimba visima 74 na vingine 22 vikiendelea kuchimvwa. Na mabadiliko yanaonekana kwani mifugo imepata maji, kilimo cha umwagiliaji kinaendelea na matumizi mengine ya majumbani pamoja na shuleni kama anavyothibitisha Lilian Ruto Mkazi wa Kijiji cha Kapkut ambaye pia ni mkulima wa mbogamboga wa kikundi cha kina mama wa Eitui. “Mahali tulikuwa tunatoa maji kulikuwa mbali sana na ilikuwa inatuchukua muda ili uweze kufikisha maji nyumbani ndio uende kuendelea na kazi zako za nyumbani. Kwahiyo tunashukuru sana kwasababu maji yamefika.“ Bi.Ruto anasema sasa hawategemeai tena chakula cha msaada kwani wanaweza kulima wenyewe na lishe za watoto wao zimeimarika.  “Sasa kwasababu tumepata maji tunajua sasa tuta tengeneza bustani tupande vyakula vyenye lishe ili kuhakikisha watoto wetu wanapata lishe bora.”WFP inafanya kazi kwa karibu na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa ikiwemo UNICEF, UNEP, FAO na IFAD kuhamasisha matumizi bora ya maji kwa afya, uhakika wa upatikanaji wa chakula na ustawi bora wa maisha yao. 
10/11/20230
Episode Artwork

10 OKTOBA 2023

Ungana na Leah Mushi kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa ambapo hii leo ikiwa ni siku ya Kimataifa ya Afya ya Akili Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO limehimiza serikali na jamii kuhakikisha wanalinda haki za wale wanao ugua afya ya akili na pia kulinda jamii isiathirike na hatari za afya ya akili. Pia utasikia habari kwa ufupi zikijikita katika vita inayoendelea mashariki ya kati na kuna ujumbe uliotolewa na mashirika matano ya Umoja wa Mataifa. Mashinani hii leo tunakupeleka nchini Sudan kuona mradi wa maji safi na salama ulivyowanufaisha wananchi wana Puntland. 
10/10/20230
Episode Artwork

10 OKTOBA 2023

Ungana na Leah Mushi kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa ambapo hii leo ikiwa ni siku ya Kimataifa ya Afya ya Akili Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO limehimiza serikali na jamii kuhakikisha wanalinda haki za wale wanao ugua afya ya akili na pia kulinda jamii isiathirike na hatari za afya ya akili. Pia utasikia habari kwa ufupi zikijikita katika vita inayoendelea mashariki ya kati na kuna ujumbe uliotolewa na mashirika matano ya Umoja wa Mataifa. Mashinani hii leo tunakupeleka nchini Sudan kuona mradi wa maji safi na salama ulivyowanufaisha wananchi wana Puntland. 
10/10/20230
Episode Artwork

UPU na harakati za kusaidia nchini kusongesha posta za kidijitali

Leo ni siku  ya posta duniani ambapo maudhui ni Pamoja kwa kuaminiana:Ushirikiano kwa mustakabali salama na uliounganika. Lengo la maudhui hay ani kuchagiza serikali na huduma zao za posta kusaidia maendeleo ya posta ya kidijitali ambayo itaboresha mtandao wa kale wa posta ulioendelezwa karne na karne, ukihitaji kwa kiasi kikubwa mtoa huduma na mhudumiwa kuonana uso kwa uso, jambo ambalo sasa kwa kiasi kikubwa limebadilika, huduma za posta mtandao zikichukua fursa. Shirika la Umoja wa Mataifa la Posta, UPU linataka ofisi za posta zichochee uchumi wa kidijitali. Katika kufahamu UPU inafanya nini kusongesha hilo Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika hilo, Mutua Muthusi anazungumza na Evarist Mapesa wa Idhaa hii na anaanza kwa kuelezea hali ya huduma ya posta hususan katika nchi zinazoendelea au maskini katika zama za sasa za maendeleo ya kidijitali. Mahojiano haya yamefanikishwa na Kayla Redstone wa UPU. 
10/9/20230
Episode Artwork

UPU na harakati za kusaidia nchini kusongesha posta za kidijitali

Leo ni siku  ya posta duniani ambapo maudhui ni Pamoja kwa kuaminiana:Ushirikiano kwa mustakabali salama na uliounganika. Lengo la maudhui hay ani kuchagiza serikali na huduma zao za posta kusaidia maendeleo ya posta ya kidijitali ambayo itaboresha mtandao wa kale wa posta ulioendelezwa karne na karne, ukihitaji kwa kiasi kikubwa mtoa huduma na mhudumiwa kuonana uso kwa uso, jambo ambalo sasa kwa kiasi kikubwa limebadilika, huduma za posta mtandao zikichukua fursa. Shirika la Umoja wa Mataifa la Posta, UPU linataka ofisi za posta zichochee uchumi wa kidijitali. Katika kufahamu UPU inafanya nini kusongesha hilo Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika hilo, Mutua Muthusi anazungumza na Evarist Mapesa wa Idhaa hii na anaanza kwa kuelezea hali ya huduma ya posta hususan katika nchi zinazoendelea au maskini katika zama za sasa za maendeleo ya kidijitali. Mahojiano haya yamefanikishwa na Kayla Redstone wa UPU. 
10/9/20230
Episode Artwork

Mashirika ya kibinadamu nayo yanahitaji msaada ili kusaidia wakimbizi wa Armenia

Mashirika ya kibinadamu nayo yanahitaji msaada ili kusaidia wakimbizi wa Armenia Ili kuhakikisha mahitaji ya muda mfupi, kati na ya muda mrefu yanatimizwa, mashirika ya kibinadamu yanaendelea kuhaha kutafuta ufadhili wa haraka ili kuongeza msaada kwa zaidi ya wakimbizi 100,000 nchini Armenia waliokimbia eneo la Karabhak kufuatia kuongezeka kwa uhasama mwezi Septemba. Anold Kayanda na maelezo zaidi.(Taarifa ya Anold Kayanda)Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) linaeleza kuwa takribani wakimbizi 100,000 waliwasili Armenia ndani ya muda wa chini ya wiki moja kufuatia kuongezeka kwa uhasama unaoendelea kwenye eneo la Karabakh linalogombaniwa na Armenia na Azerbaijan huko barani Asia.UNHCR inasema miongoni mwa wakimbizi wapya waliowasili, ni watoto wapatao 30,000 na watu wengi wenye uhitaji ikiwa ni pamoja na wazee, wanawake wajawazito, watu wenye ulemavu na wengine wenye magonjwa ya kudumu. Zaidi ya nusu ya wakimbizi ni wanawake na wasichana.Huyu ni Vika, mmoja wa wakimbizi anasema, (Sauti ya Vika) – Evarist/sauti ya kike“Hali yetu hapa si ya uhakika. Huko, nilikuwa nikifanya kazi shuleni, nilikuwa muuguzi pale. Kila kitu kilikuwa kikienda sawa, tulikuwa tukiishi na wazazi wangu baada ya kifo cha mume wangu. Lakini hapa, hatuna chochote, hatuna kazi, hakuna kitu, hata nguo. Wasamaria wema wanaleta vitu sasa, hivi au vile, kutoka hapa na pale… la sivyo hatuna kitu, binti yangu hana nguo nyingine, hana chochote cha kuvaa kumpa joto.”UNHCR inaisaidia Serikali ya Armenia kwa vifaa vya kiufundi, kama aina mbalimbali za kompyuta ili kurahisisha usajili na imetoa msaada wa vitu muhimu kama vitanda vya kukunja na magodoro kwa ajili ya wakimbizi, huku misaada muhimu zaidi ikiwa njiani.Tags: Armenia, UNHCR, Karabhak
10/9/20230
Episode Artwork

Mashirika ya kibinadamu nayo yanahitaji msaada ili kusaidia wakimbizi wa Armenia

Mashirika ya kibinadamu nayo yanahitaji msaada ili kusaidia wakimbizi wa Armenia Ili kuhakikisha mahitaji ya muda mfupi, kati na ya muda mrefu yanatimizwa, mashirika ya kibinadamu yanaendelea kuhaha kutafuta ufadhili wa haraka ili kuongeza msaada kwa zaidi ya wakimbizi 100,000 nchini Armenia waliokimbia eneo la Karabhak kufuatia kuongezeka kwa uhasama mwezi Septemba. Anold Kayanda na maelezo zaidi.(Taarifa ya Anold Kayanda)Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi (UNHCR) linaeleza kuwa takribani wakimbizi 100,000 waliwasili Armenia ndani ya muda wa chini ya wiki moja kufuatia kuongezeka kwa uhasama unaoendelea kwenye eneo la Karabakh linalogombaniwa na Armenia na Azerbaijan huko barani Asia.UNHCR inasema miongoni mwa wakimbizi wapya waliowasili, ni watoto wapatao 30,000 na watu wengi wenye uhitaji ikiwa ni pamoja na wazee, wanawake wajawazito, watu wenye ulemavu na wengine wenye magonjwa ya kudumu. Zaidi ya nusu ya wakimbizi ni wanawake na wasichana.Huyu ni Vika, mmoja wa wakimbizi anasema, (Sauti ya Vika) – Evarist/sauti ya kike“Hali yetu hapa si ya uhakika. Huko, nilikuwa nikifanya kazi shuleni, nilikuwa muuguzi pale. Kila kitu kilikuwa kikienda sawa, tulikuwa tukiishi na wazazi wangu baada ya kifo cha mume wangu. Lakini hapa, hatuna chochote, hatuna kazi, hakuna kitu, hata nguo. Wasamaria wema wanaleta vitu sasa, hivi au vile, kutoka hapa na pale… la sivyo hatuna kitu, binti yangu hana nguo nyingine, hana chochote cha kuvaa kumpa joto.”UNHCR inaisaidia Serikali ya Armenia kwa vifaa vya kiufundi, kama aina mbalimbali za kompyuta ili kurahisisha usajili na imetoa msaada wa vitu muhimu kama vitanda vya kukunja na magodoro kwa ajili ya wakimbizi, huku misaada muhimu zaidi ikiwa njiani.Tags: Armenia, UNHCR, Karabhak
10/9/20230
Episode Artwork

Mashariki ya Kati bado hali si shwari, UNHCR yapaza sauti

Mashariki ya Kati bado hali si shwari, UNHCR yapaza sauti Mapigano huko Mashariki ya Kati yakiingia siku ya tatu kati ya Israel na wapalestina, huko Geneva, hii leo wajumbe wa mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za binadamu wamesimama kwa dakika moja kuwakumbuka mamia ya watu waliopoteza maisha katika mapigano hayo yaliyoanza baada ya wanamgambo wa Hamas kurusha makombora kuelekea upande wa Israel. Assumpta Massoi na maelezo zaidi. (Taarifa ya Assumpta Massoi) Nats.. Ni katika ukumbi wa Baraza la Umoja wa Mataifa la haki za binadamu, jijini Geneva, Uswisi kunakoendelea mkutano wa 54 wa Baraza hilo ambako mwenyekiti alitaka wajumbe kusimama kwa dakika moja kukumbuka waliopoteza maisha kwenye mapigano hayo yanayoendelea huko Mashariki ya Kati, kati ya wanamgambo wa Hamas kutoka Palestina na jeshi la Israel. Takwimu kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA zinasema hadi sasa watu 370 wakiwemo watoto 20 wameuawa huku zaidi ya 2,200 wamejeruhiwa upande Palestina ihali kwa Israel waliouawa ni takribani 650. Kamishna Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR Filippo Grandi amenukuliwa hii leo huko Geneva, Uswisi akisema shirika hilo linakabiliwa na moja ya nyakati ngumu zaidi katika historia yake ya miaka 70. Amesema watu milioni 110 ni wakimbizi duniani kote na ukata ndio umekumba zaidi UNHCR. Bwana Grandi amesema picha za kutisha na kusikitisha za mashambulizi yaliyofanywa na wanamgambo wa Hamas dhidi ya raia wa Israel zimegubika skrini za televisheni kwa saa 48. Mkuu huyo wa UNHCR amesema “tunashuhudia vita nyingine Mashariki ya Kati, vita ambayo bila shaka itasababisha machungu zaidi kwa raia, pande zote za Israel na Palestina, na kuhatarisha kuleta ukosefu mkubwa wa utulivu kwenye ukanda huo ambao tayari umegubikwa na mvutano.” Bwana Grandi amesema iwapo hatua hazitachukuliwa haraka kudhibiti, kuna hatari mzozo huo ukasambaa na kudumaza amani duniani. Jana Jumapili, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana kwa faragha kujadili mapigano hayo Mashariki ya Kati huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alitoa taarifa Jumamosi akilaani mashambulizi hayo ya Hamas dhidi ya Israel huku akitaka diplomasia itumike kumaliza mzozo huo. TAGS: Amani na Usalama Additional: Amani na Usalama News: Israel, Palestina, Hamas Region: Mashariki ya Kati UN/Partner: UNRWA, UNHCR 
10/9/20230
Episode Artwork

Mashariki ya Kati bado hali si shwari, UNHCR yapaza sauti

Mashariki ya Kati bado hali si shwari, UNHCR yapaza sauti Mapigano huko Mashariki ya Kati yakiingia siku ya tatu kati ya Israel na wapalestina, huko Geneva, hii leo wajumbe wa mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za binadamu wamesimama kwa dakika moja kuwakumbuka mamia ya watu waliopoteza maisha katika mapigano hayo yaliyoanza baada ya wanamgambo wa Hamas kurusha makombora kuelekea upande wa Israel. Assumpta Massoi na maelezo zaidi. (Taarifa ya Assumpta Massoi) Nats.. Ni katika ukumbi wa Baraza la Umoja wa Mataifa la haki za binadamu, jijini Geneva, Uswisi kunakoendelea mkutano wa 54 wa Baraza hilo ambako mwenyekiti alitaka wajumbe kusimama kwa dakika moja kukumbuka waliopoteza maisha kwenye mapigano hayo yanayoendelea huko Mashariki ya Kati, kati ya wanamgambo wa Hamas kutoka Palestina na jeshi la Israel. Takwimu kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi wa kipalestina, UNRWA zinasema hadi sasa watu 370 wakiwemo watoto 20 wameuawa huku zaidi ya 2,200 wamejeruhiwa upande Palestina ihali kwa Israel waliouawa ni takribani 650. Kamishna Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR Filippo Grandi amenukuliwa hii leo huko Geneva, Uswisi akisema shirika hilo linakabiliwa na moja ya nyakati ngumu zaidi katika historia yake ya miaka 70. Amesema watu milioni 110 ni wakimbizi duniani kote na ukata ndio umekumba zaidi UNHCR. Bwana Grandi amesema picha za kutisha na kusikitisha za mashambulizi yaliyofanywa na wanamgambo wa Hamas dhidi ya raia wa Israel zimegubika skrini za televisheni kwa saa 48. Mkuu huyo wa UNHCR amesema “tunashuhudia vita nyingine Mashariki ya Kati, vita ambayo bila shaka itasababisha machungu zaidi kwa raia, pande zote za Israel na Palestina, na kuhatarisha kuleta ukosefu mkubwa wa utulivu kwenye ukanda huo ambao tayari umegubikwa na mvutano.” Bwana Grandi amesema iwapo hatua hazitachukuliwa haraka kudhibiti, kuna hatari mzozo huo ukasambaa na kudumaza amani duniani. Jana Jumapili, Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa lilikutana kwa faragha kujadili mapigano hayo Mashariki ya Kati huku Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alitoa taarifa Jumamosi akilaani mashambulizi hayo ya Hamas dhidi ya Israel huku akitaka diplomasia itumike kumaliza mzozo huo. TAGS: Amani na Usalama Additional: Amani na Usalama News: Israel, Palestina, Hamas Region: Mashariki ya Kati UN/Partner: UNRWA, UNHCR 
10/9/20230
Episode Artwork

09 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani Leah Mushi anamulika Mashariki ya Kati, Ulaya, siku ya posta duniani na mashinani anaelekea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kumsikia mnufaika wa mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP.1. Mapigano huko Mashariki ya Kati yakiingia siku ya tatu kati ya Israel na wapalestina, huko Geneva, hii leo wajumbe wa mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za binadamu wamesimama kwa dakika moja kuwakumbuka mamia ya watu waliopoteza maisha katika mapigano hayo yaliyoanza baada ya wanamgambo wa Hamas kurusha makombora kuelekea upande wa Israel.2. Ili kuhakikisha mahitaji ya muda mfupi, kati na ya muda mrefu yanatimizwa, mashirika ya kibinadamu yanaendelea kuhaha kutafuta ufadhili wa haraka ili kuongeza msaada kwa zaidi ya wakimbizi 100,000 nchini Armenia waliokimbia eneo la Karabhak kufuatia kuongezeka kwa uhasama mwezi Septemba.3. Makala ni siku ya Posta Duniani ambapo Evarist Mapesa wa Idhaa hii ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la Posta, UPU Mutua Muthusi anaelezea nafasi ya maendeleo ya kidijitali katika kusongesha huduma za posta. 4. Mashinani ni mnufaika wa msaada wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani, WFP nchini DR Congo.
10/9/20230
Episode Artwork

09 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani Leah Mushi anamulika Mashariki ya Kati, Ulaya, siku ya posta duniani na mashinani anaelekea Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kumsikia mnufaika wa mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP.1. Mapigano huko Mashariki ya Kati yakiingia siku ya tatu kati ya Israel na wapalestina, huko Geneva, hii leo wajumbe wa mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa la Haki za binadamu wamesimama kwa dakika moja kuwakumbuka mamia ya watu waliopoteza maisha katika mapigano hayo yaliyoanza baada ya wanamgambo wa Hamas kurusha makombora kuelekea upande wa Israel.2. Ili kuhakikisha mahitaji ya muda mfupi, kati na ya muda mrefu yanatimizwa, mashirika ya kibinadamu yanaendelea kuhaha kutafuta ufadhili wa haraka ili kuongeza msaada kwa zaidi ya wakimbizi 100,000 nchini Armenia waliokimbia eneo la Karabhak kufuatia kuongezeka kwa uhasama mwezi Septemba.3. Makala ni siku ya Posta Duniani ambapo Evarist Mapesa wa Idhaa hii ya Umoja wa Mataifa amezungumza na Mkurugenzi wa Maendeleo ya Ushirikiano kutoka shirika la Umoja wa Mataifa la Posta, UPU Mutua Muthusi anaelezea nafasi ya maendeleo ya kidijitali katika kusongesha huduma za posta. 4. Mashinani ni mnufaika wa msaada wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani, WFP nchini DR Congo.
10/9/20230
Episode Artwork

Madarasa yajengwa Sofala, Msumbiji kuhimili majanga ya asili ikiwemo vimbunga

Hii leo Umoja wa Mataifa umetoa ripoti ya kwanza ya uchambuzi wa aina yake kuhusu matukio ya watoto kulazimika kukimbia makwao kutokana na majanga yasababishwayo na hali ya hewa ikisema zaidi ya watoto milioni 43 walijikuta wakimbizi wa ndani kwenye nchi 44 katika kipindi cha miaka sita iliyopita, ikitafsiri kuwa ni watoto 20,000 kila siku.Makadirio ya ripoti hiyo ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, yanaonesha kuwa kufurika kwa mito pekee kutafurusha watoto milioni 96 katika miaka 30 ijayo.Kwa kutambua hilo, mafuriko yaliyosababishwa na kimbunga Idai nchini Msumbiji mwaka 2019  tayari yamekuwa somo na hatua zimechukuliwa, hatua ambazo zinaweza kuwa somo pia kwa maeneo mengine. Je ni hatua zipi hizo? Ungana na Assumpta Massoi kwenye makala hii iliyofanikishwa na UNICEF.
10/6/20230
Episode Artwork

Madarasa yajengwa Sofala, Msumbiji kuhimili majanga ya asili ikiwemo vimbunga

Hii leo Umoja wa Mataifa umetoa ripoti ya kwanza ya uchambuzi wa aina yake kuhusu matukio ya watoto kulazimika kukimbia makwao kutokana na majanga yasababishwayo na hali ya hewa ikisema zaidi ya watoto milioni 43 walijikuta wakimbizi wa ndani kwenye nchi 44 katika kipindi cha miaka sita iliyopita, ikitafsiri kuwa ni watoto 20,000 kila siku.Makadirio ya ripoti hiyo ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, yanaonesha kuwa kufurika kwa mito pekee kutafurusha watoto milioni 96 katika miaka 30 ijayo.Kwa kutambua hilo, mafuriko yaliyosababishwa na kimbunga Idai nchini Msumbiji mwaka 2019  tayari yamekuwa somo na hatua zimechukuliwa, hatua ambazo zinaweza kuwa somo pia kwa maeneo mengine. Je ni hatua zipi hizo? Ungana na Assumpta Massoi kwenye makala hii iliyofanikishwa na UNICEF.
10/6/20230
Episode Artwork

Tuzo ya amani ya Nobel yaenda kwa mfungwa Iran, UN yasifu wanawake wa Iran kwa kuongoza vuguvugu

Kamati ya tuzo ya amani ya Nobel mwaka huu imemtunuku mfungwa mwanaharakati wa masuala ya haki za binadamu wa Iran Narges Mohammadi na Umoja wa Mataifa umepongeza uamuzi huo. Flora Nducha na taarifa zaidiBaada ya kutangazwa tu leo ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa OHCHR imesema “ Kumpatia tuzo Narges Mohammadi mwanaharakati shupavu wa haki za binadamu ambaye hivi sasa anatumikia kifongo cha miaka 16 kwenye gereza la Evin mjini Tehran nchini Iran  kunasisitiza ijasiri na dhamira waliyonayo wanawake wa Iran.”Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis msemaji wa ofisi hiyo ya haki za binadamu Liz Throssell amesema “ Nadhani kilicho bayan ani kwamba wanawake wa Iran wamekuwa chanzo cha hamasa ulimwenguni . Tumeshuhudia ujasiri na kujizatiti kwao katika wakati wa ukiukwaji wa haki, vitisho, machafuko na watu kuswekwa vizuizini. Na ujasiri huu na kujizatiti huku ni kwa hali ya juu, kwani wamekuwa wakibughudhwa kwa kile wanachovaa au kutovaa, wanabanwa kisheria, kijamii na kiuchumi kwa hatua zinazochukuliwa dhidi yao.”Naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameongeza sauti yake akisema “Narges kupewa tuzo hiyo ni kumbusho muhimu kwamba haki za wanawake na wasichana zinakabiliwa na changamoto kubwa ikiwemo kupitia kushitakiwa kwa wanawake watetezi wa haki za binadamu nchini Iran na kwingineko.Na hivyo “ Tuzo hiyo ya Amani ya Nobel ni “Utambuzi wa wanawake wote ambao wanapambana kwa ajili ya haki za binadamu huku wakihatarisha uhuru wao, afya zao n ahata Maisha yao.”Narges amefanyakazi kwa miaka mingi kama muandishi wa habari  na pia ni mwandishi wa vitabu na pia naibu mkurugenzi wa shirika la kiraia la Defenders of Human rights Center lililoko mjini Tehran.MweZi mei mwaka huu alipata tuzo ya siku ya Uhuru wa vyombo vya habari inayotolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu sayansi na utamaduni UNESCO 
10/6/20230
Episode Artwork

Tuzo ya amani ya Nobel yaenda kwa mfungwa Iran, UN yasifu wanawake wa Iran kwa kuongoza vuguvugu

Kamati ya tuzo ya amani ya Nobel mwaka huu imemtunuku mfungwa mwanaharakati wa masuala ya haki za binadamu wa Iran Narges Mohammadi na Umoja wa Mataifa umepongeza uamuzi huo. Flora Nducha na taarifa zaidiBaada ya kutangazwa tu leo ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa OHCHR imesema “ Kumpatia tuzo Narges Mohammadi mwanaharakati shupavu wa haki za binadamu ambaye hivi sasa anatumikia kifongo cha miaka 16 kwenye gereza la Evin mjini Tehran nchini Iran  kunasisitiza ijasiri na dhamira waliyonayo wanawake wa Iran.”Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva Uswis msemaji wa ofisi hiyo ya haki za binadamu Liz Throssell amesema “ Nadhani kilicho bayan ani kwamba wanawake wa Iran wamekuwa chanzo cha hamasa ulimwenguni . Tumeshuhudia ujasiri na kujizatiti kwao katika wakati wa ukiukwaji wa haki, vitisho, machafuko na watu kuswekwa vizuizini. Na ujasiri huu na kujizatiti huku ni kwa hali ya juu, kwani wamekuwa wakibughudhwa kwa kile wanachovaa au kutovaa, wanabanwa kisheria, kijamii na kiuchumi kwa hatua zinazochukuliwa dhidi yao.”Naye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameongeza sauti yake akisema “Narges kupewa tuzo hiyo ni kumbusho muhimu kwamba haki za wanawake na wasichana zinakabiliwa na changamoto kubwa ikiwemo kupitia kushitakiwa kwa wanawake watetezi wa haki za binadamu nchini Iran na kwingineko.Na hivyo “ Tuzo hiyo ya Amani ya Nobel ni “Utambuzi wa wanawake wote ambao wanapambana kwa ajili ya haki za binadamu huku wakihatarisha uhuru wao, afya zao n ahata Maisha yao.”Narges amefanyakazi kwa miaka mingi kama muandishi wa habari  na pia ni mwandishi wa vitabu na pia naibu mkurugenzi wa shirika la kiraia la Defenders of Human rights Center lililoko mjini Tehran.MweZi mei mwaka huu alipata tuzo ya siku ya Uhuru wa vyombo vya habari inayotolewa na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu sayansi na utamaduni UNESCO 
10/6/20230
Episode Artwork

Mtoto kuzaliwa njiti humtia hatarini kukumbwa na kifo, hatua zichukuliwe- WHO

Inakadiriwa watoto milioni 13.4 njiti (wanaozaliwa kabla ya wiki 37 za ujauzito) walizaliwa mwaka 2020 idadi hii ikiwa ni takriban mtoto 1 kati ya 10 na wengi wa watoto hao ni kutoka Ukanda wa jangwa la Sahara na Asia ya Kusini imesema ripoti iliyochapishwa leo kwenye jarida la masuala ya afya la Lancet. Leah Mushi na maelezo zaidi.Ripoti hiyo inafuatia utafiti uliofanywa na shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kwakushirikiana na lile la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF pamoja na Chuo kikuu cha London kitivo cha usafi na dawa za kitropiki (London School of Hygiene and Tropical Medicine.)Mkurugenzi wa WHO idara ya masuala ya watoto wachanga, watoto, afya za barubaru na wazee Dkt. Anshu Banerjee amesema kwa kuwa watoto kuzaliwa kabla ya muda ni sababu kubwa ya vifo vya watoto wachanga suala hili linapaswa kushughulikiwa kwa udharura.“Idadi hii inaonesha uhitaji wa uwekezaji wa maana ili kuweza kusaidia familia na watoto wao pamoja na kuweka mkazo katika katika kuhakikisha kuna upatikanaji wa huduma bora za afya kabla na wakati wa ujauzito.”Sababu za kujifungua mtoto njitiHatari za afya ya uzazi, kama vile mimba za utotoni, maambukizi, lishe duni, na hali ya kutokwa na damu wakati wa ujauzito ni sababu zinazo husishwa na mama mjamzito kujifungua mtoto njiti.Upatikanaji wa huduma bora wakati wa ujauzito ni suala muhimu kwani linawezesha kufanya utambuzi na udhibiti wa matatizo wakati wa ujauzito, kuhakikisha kuna uhesabuji sahihi wa ujauzito kwakuazia wakati mimba upo ndogo kupitia uchunguzi wa kutumia ultrasound na pale inapohitajika kuchelewesha mwanamke kupata uchungu wa kujifungua itawezekana kupitia matibabu yaliyo idhinishwaAthari za kuzaliwa njitiTaarifa ya WHO iliyotolewa leo kutoka huko Jijini Geneva Uswisi imebainisha kuwa mbali na suala la watoto kupoteza maisha, watoto njiti wanakabiliwa na ukuwaji wenye changamoto ikiwemo kupata magonjwa makubwa, ulemavu na ukuaji kwa kuchelewa na hata wakiwa wakiwa watu wazima wanaweza kupata magonjwa sugu kama kisurari na magonjwa ya moto.“Watoto njiti wapo hatarini sana kupata matatizo ya afya yanayo hatarisha maisha na wanahitaji uangalizi maalum” amesema Dr. BanerjeeMatokeo ya utafitiUtafiti huo Makadirio ya kwenye karatasi, ya Kitaifa, kikanda na kimataifa ya watoto njiti kwa mwaka wa 2020, yenye muelekeo kuanzia mwaka 2010: uchambuzi wa kiutaratibu,umeonesha kuna utofauti baina ya kanda na mataifa.Asilimia 65 ya watoto njiti waliozaliwa mwaka 2020 walitokea…
10/6/20230
Episode Artwork

Mtoto kuzaliwa njiti humtia hatarini kukumbwa na kifo, hatua zichukuliwe- WHO

Inakadiriwa watoto milioni 13.4 njiti (wanaozaliwa kabla ya wiki 37 za ujauzito) walizaliwa mwaka 2020 idadi hii ikiwa ni takriban mtoto 1 kati ya 10 na wengi wa watoto hao ni kutoka Ukanda wa jangwa la Sahara na Asia ya Kusini imesema ripoti iliyochapishwa leo kwenye jarida la masuala ya afya la Lancet. Leah Mushi na maelezo zaidi.Ripoti hiyo inafuatia utafiti uliofanywa na shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kwakushirikiana na lile la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF pamoja na Chuo kikuu cha London kitivo cha usafi na dawa za kitropiki (London School of Hygiene and Tropical Medicine.)Mkurugenzi wa WHO idara ya masuala ya watoto wachanga, watoto, afya za barubaru na wazee Dkt. Anshu Banerjee amesema kwa kuwa watoto kuzaliwa kabla ya muda ni sababu kubwa ya vifo vya watoto wachanga suala hili linapaswa kushughulikiwa kwa udharura.“Idadi hii inaonesha uhitaji wa uwekezaji wa maana ili kuweza kusaidia familia na watoto wao pamoja na kuweka mkazo katika katika kuhakikisha kuna upatikanaji wa huduma bora za afya kabla na wakati wa ujauzito.”Sababu za kujifungua mtoto njitiHatari za afya ya uzazi, kama vile mimba za utotoni, maambukizi, lishe duni, na hali ya kutokwa na damu wakati wa ujauzito ni sababu zinazo husishwa na mama mjamzito kujifungua mtoto njiti.Upatikanaji wa huduma bora wakati wa ujauzito ni suala muhimu kwani linawezesha kufanya utambuzi na udhibiti wa matatizo wakati wa ujauzito, kuhakikisha kuna uhesabuji sahihi wa ujauzito kwakuazia wakati mimba upo ndogo kupitia uchunguzi wa kutumia ultrasound na pale inapohitajika kuchelewesha mwanamke kupata uchungu wa kujifungua itawezekana kupitia matibabu yaliyo idhinishwaAthari za kuzaliwa njitiTaarifa ya WHO iliyotolewa leo kutoka huko Jijini Geneva Uswisi imebainisha kuwa mbali na suala la watoto kupoteza maisha, watoto njiti wanakabiliwa na ukuwaji wenye changamoto ikiwemo kupata magonjwa makubwa, ulemavu na ukuaji kwa kuchelewa na hata wakiwa wakiwa watu wazima wanaweza kupata magonjwa sugu kama kisurari na magonjwa ya moto.“Watoto njiti wapo hatarini sana kupata matatizo ya afya yanayo hatarisha maisha na wanahitaji uangalizi maalum” amesema Dr. BanerjeeMatokeo ya utafitiUtafiti huo Makadirio ya kwenye karatasi, ya Kitaifa, kikanda na kimataifa ya watoto njiti kwa mwaka wa 2020, yenye muelekeo kuanzia mwaka 2010: uchambuzi wa kiutaratibu,umeonesha kuna utofauti baina ya kanda na mataifa.Asilimia 65 ya watoto njiti waliozaliwa mwaka 2020 walitokea…
10/6/20230
Episode Artwork

06 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani mwenyeji wako ni Anold Kayanda akimulika pamoja na mambo mengine mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Mabadiliko ya Tabianchi, vijana na siasa pamoja na majiko sanifu.1.Kamati ya tuzo ya amani ya Nobel mwaka huu imemtunuku mfungwa mwanaharakati wa masuala ya haki za binadamu wa Iran Narges Mohammadi na Umoja wa Mataifa umepongeza uamuzi huo2. Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwa kushirikiana na Umoja wa wanafunzi wa nchini humo wanaendesha midahalo ya wanafunzi lengo likiwa ni kuchagiza vijana waweze kushiriki kikamilifu katika masuala ya siasa kuelekea uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo unaotarajiwa kufanyika mwezi Desemba 2024.3. Makala inakupeleka Msumbiji ambako huko UNICEF imejenga majengo ya shule yanayoweza kuhimili mvua kubwa na mafuriko.4 .Mashinani ni mfinyanzi mkimbizi kutoka DRC akijiinua si  yeye peke yake bali pia jamii kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya.
10/6/20230
Episode Artwork

06 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani mwenyeji wako ni Anold Kayanda akimulika pamoja na mambo mengine mshindi wa Tuzo ya Amani ya Nobel, Mabadiliko ya Tabianchi, vijana na siasa pamoja na majiko sanifu.1.Kamati ya tuzo ya amani ya Nobel mwaka huu imemtunuku mfungwa mwanaharakati wa masuala ya haki za binadamu wa Iran Narges Mohammadi na Umoja wa Mataifa umepongeza uamuzi huo2. Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini UNMISS kwa kushirikiana na Umoja wa wanafunzi wa nchini humo wanaendesha midahalo ya wanafunzi lengo likiwa ni kuchagiza vijana waweze kushiriki kikamilifu katika masuala ya siasa kuelekea uchaguzi Mkuu wa nchi hiyo unaotarajiwa kufanyika mwezi Desemba 2024.3. Makala inakupeleka Msumbiji ambako huko UNICEF imejenga majengo ya shule yanayoweza kuhimili mvua kubwa na mafuriko.4 .Mashinani ni mfinyanzi mkimbizi kutoka DRC akijiinua si  yeye peke yake bali pia jamii kwenye kambi ya wakimbizi ya Kakuma nchini Kenya.
10/6/20230
Episode Artwork

Mwalimu binafsi aanzisha maktaba inayosaidia watoto katika maeneo duni Kenya

Siku ya walimu duniani huadhimishwa tarehe 5 Oktoba kila mwaka.Mada kuu kwa mwaka huu ni walimu tunaohitaji kwa elimu tunayoitaka. Kenya imepiga hatua kwenye sekta ya elimu kwa kuzindua mfumo unaojikita katika kukuza vipaji na uwezo wa mwanafunzi, CBC,ila uhaba wa walimu ni kikwazo cha utekelezaji. Baadhi ya walimu wa kujitegeme wamechukua hatua mikononi mwao na kuanzisha maktaba za binafsi ili kuwapa watoto nafasi ya kusoma nje ya mazingira ya shule.Maktaba ya Little Voice Deep Within iko mtaani Kariobangi South jijini Nairobi katikati ya makaazi ya umma.Hii ndiyo taswira unayokumbana nayo unapowasili.Watoto wanacheza nje au kusoma vitabu wakiwa ndani.Kila siku ina ratiba yake ima ni kusoma, sanaa au kujifunza kutumia kompyuta .Eric Odhiambo ni mwalimu wa kujitegemea na muasisi wa maktaba binafsi ya Little Voice Deep Within na anaamini kuwa kila mtoto ana haki ya kupata elimu mujarab nje ya mazingira ya shule kwani,”Watoto wa mtaani hawana maktaba.Unakuta mtoto anafikiria tu kutazama vibonzo kwenye televisheni hakuna kingine cha kufanya.Hakuna kituo ambapo mtoto anaweza kupitisha muda au kusoma na kufanya kitu fulani.Niliona ni bora kuwaletea maktaba karibu ili mtoto akitaka kusoma au ambaye hajui kusoma anapata msaada.”Kusoma vitabu ni njia mujarab ya kuepusha utunduMaktaba hii ina vitabu vya lugha na mada tofauti mahsusi kwa watoto wa kila rika.Siku ya walimu duniani huadhimishwa tarehe 5 Oktoba kila mwaka na mada kuu mwaka huu ni walimu tunaowahitaji kwa elimu tunayoitaka.Kwa mujibu wa takwimu za shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi na utamaduni,UNESCO, walimu milioni 44 bado wanahitajika ili kutimiza lengo la kusambaza elimu ya msingi na sekondari kwa wote ifikapo 2030.Walimu wana mchango muhimu kwenye maisha ya wanafunzi na ni sawa na walezi. Evelyne Wambui ni mzazi na binti yake Joy anapata mafunzo kwenye kituo cha Little Voice Deep Within , anakiri kwa mba mwanawe amebadilika na kwa sasa,”Mwanzo wa mwaka mwalimu aliwaandikia vile vitabu vinavyohitajika kununuliwa. Mimi kama mzazi niliweza kununua vitabu vinne....hivyo vyengine vilinunuliwa na viko huko Vinamsaidia. Akipewa kazi ya ziada ya nyumbani.Yeye ana vitabu vya msingi vya Kiswahili, Hesabu na Sayansi.Vingine anavipata huku.”Watoto hujifunza pia vitu vingine kama kufuma mitandio na vitambaa wanapokuja kwenye kituo hiki.Kadhalika wanapata ujuzi wa kuchora kulingana na uwezo na umri wao.Ili kuiongeza kasi ya kutimiza lengo la 4 la maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa,SDGs ya elimu bora,UNESCO inashirikiana na mataifa hasa ya eneo la Afrika kusini mwa jangwa la Sahara na kusini mwa Asia ili kuimarisha sera zinazowahusu na kuunga mkono mifumo ya kutoa mafunzo kwa walimu.Susan Muthoni ni mwalimu wa hiari kwenye kituo hiki cha watoto na anawafunza kufuma vitambaa na mitandio kwa upande wake anaamini kuwa masomo ya kutengeza bidhaa kwa mikono yana umuhimu mkubwa katika maisha ya usoni lakini,”Kwanza ni kuwa na walimu wanaowaelewa watoto.Kwenye shule kama hizi za umma,unapata kuwa kama mtoto wako huwa wa kwanza ataendelea hivyo na kama huwa wa mwisho anaendelea kuvuta mkia. Kwahiyo upo umuhimu wa kuwa na njia maalum ya kuwasomesha hawa watoto...kuwe na walimu wa kuwasomesha masomo mengine.Ukiona mtoto haelewi masomo ya kuandika anaweza kupata ujuzi wa kazi za mikono.”UNESCO,shirika la lazi la Umoja wa Mataifa ILO,shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF na Education International ndiyo mashirika yanayosimamia siku ya walimu duniani na dhamira ni kuzishajiisha serikali na mashirika ya kijamii kuipa fani ya ualimu sifa nzuri zaidi ili kuwavutia wengi kujiunga hasa vijana.UNESCO imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa haki ya elimu inakuwa mchango muhimu kwenye misingi ya haki za binadamu na kulinda amani.Hata hivyo,kwa mujibu wa UNESCO nadharia hii itatimia iwapo walimu wanaungwa mkono kuwafunza…
10/5/20230
Episode Artwork

Mwalimu binafsi aanzisha maktaba inayosaidia watoto katika maeneo duni Kenya

Siku ya walimu duniani huadhimishwa tarehe 5 Oktoba kila mwaka.Mada kuu kwa mwaka huu ni walimu tunaohitaji kwa elimu tunayoitaka. Kenya imepiga hatua kwenye sekta ya elimu kwa kuzindua mfumo unaojikita katika kukuza vipaji na uwezo wa mwanafunzi, CBC,ila uhaba wa walimu ni kikwazo cha utekelezaji. Baadhi ya walimu wa kujitegeme wamechukua hatua mikononi mwao na kuanzisha maktaba za binafsi ili kuwapa watoto nafasi ya kusoma nje ya mazingira ya shule.Maktaba ya Little Voice Deep Within iko mtaani Kariobangi South jijini Nairobi katikati ya makaazi ya umma.Hii ndiyo taswira unayokumbana nayo unapowasili.Watoto wanacheza nje au kusoma vitabu wakiwa ndani.Kila siku ina ratiba yake ima ni kusoma, sanaa au kujifunza kutumia kompyuta .Eric Odhiambo ni mwalimu wa kujitegemea na muasisi wa maktaba binafsi ya Little Voice Deep Within na anaamini kuwa kila mtoto ana haki ya kupata elimu mujarab nje ya mazingira ya shule kwani,”Watoto wa mtaani hawana maktaba.Unakuta mtoto anafikiria tu kutazama vibonzo kwenye televisheni hakuna kingine cha kufanya.Hakuna kituo ambapo mtoto anaweza kupitisha muda au kusoma na kufanya kitu fulani.Niliona ni bora kuwaletea maktaba karibu ili mtoto akitaka kusoma au ambaye hajui kusoma anapata msaada.”Kusoma vitabu ni njia mujarab ya kuepusha utunduMaktaba hii ina vitabu vya lugha na mada tofauti mahsusi kwa watoto wa kila rika.Siku ya walimu duniani huadhimishwa tarehe 5 Oktoba kila mwaka na mada kuu mwaka huu ni walimu tunaowahitaji kwa elimu tunayoitaka.Kwa mujibu wa takwimu za shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu na Sayansi na utamaduni,UNESCO, walimu milioni 44 bado wanahitajika ili kutimiza lengo la kusambaza elimu ya msingi na sekondari kwa wote ifikapo 2030.Walimu wana mchango muhimu kwenye maisha ya wanafunzi na ni sawa na walezi. Evelyne Wambui ni mzazi na binti yake Joy anapata mafunzo kwenye kituo cha Little Voice Deep Within , anakiri kwa mba mwanawe amebadilika na kwa sasa,”Mwanzo wa mwaka mwalimu aliwaandikia vile vitabu vinavyohitajika kununuliwa. Mimi kama mzazi niliweza kununua vitabu vinne....hivyo vyengine vilinunuliwa na viko huko Vinamsaidia. Akipewa kazi ya ziada ya nyumbani.Yeye ana vitabu vya msingi vya Kiswahili, Hesabu na Sayansi.Vingine anavipata huku.”Watoto hujifunza pia vitu vingine kama kufuma mitandio na vitambaa wanapokuja kwenye kituo hiki.Kadhalika wanapata ujuzi wa kuchora kulingana na uwezo na umri wao.Ili kuiongeza kasi ya kutimiza lengo la 4 la maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa,SDGs ya elimu bora,UNESCO inashirikiana na mataifa hasa ya eneo la Afrika kusini mwa jangwa la Sahara na kusini mwa Asia ili kuimarisha sera zinazowahusu na kuunga mkono mifumo ya kutoa mafunzo kwa walimu.Susan Muthoni ni mwalimu wa hiari kwenye kituo hiki cha watoto na anawafunza kufuma vitambaa na mitandio kwa upande wake anaamini kuwa masomo ya kutengeza bidhaa kwa mikono yana umuhimu mkubwa katika maisha ya usoni lakini,”Kwanza ni kuwa na walimu wanaowaelewa watoto.Kwenye shule kama hizi za umma,unapata kuwa kama mtoto wako huwa wa kwanza ataendelea hivyo na kama huwa wa mwisho anaendelea kuvuta mkia. Kwahiyo upo umuhimu wa kuwa na njia maalum ya kuwasomesha hawa watoto...kuwe na walimu wa kuwasomesha masomo mengine.Ukiona mtoto haelewi masomo ya kuandika anaweza kupata ujuzi wa kazi za mikono.”UNESCO,shirika la lazi la Umoja wa Mataifa ILO,shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto UNICEF na Education International ndiyo mashirika yanayosimamia siku ya walimu duniani na dhamira ni kuzishajiisha serikali na mashirika ya kijamii kuipa fani ya ualimu sifa nzuri zaidi ili kuwavutia wengi kujiunga hasa vijana.UNESCO imekuwa mstari wa mbele kuhakikisha kuwa haki ya elimu inakuwa mchango muhimu kwenye misingi ya haki za binadamu na kulinda amani.Hata hivyo,kwa mujibu wa UNESCO nadharia hii itatimia iwapo walimu wanaungwa mkono kuwafunza…
10/5/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili - "KUMBITI"

Katika jifunze Kiswahili hii leo tunabisha hodi kwenye Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania BAKITA  Je wajua maana ya neno “KUMBITI”? Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua. 
10/5/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili - "KUMBITI"

Katika jifunze Kiswahili hii leo tunabisha hodi kwenye Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania BAKITA  Je wajua maana ya neno “KUMBITI”? Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania , BAKITA anafafanua. 
10/5/20230
Episode Artwork

05 OKTOBA 2023

Mwandishi wetu wa Kenya Thelma Mwadzaya ametembelea maktaba ya Little Voice Deep iliyoko jijini Nairobi kujionea jinsi gani kupitia waalimu walioko inavyochangia kuhakikisha watoto wanapata elimu wanayoitaka na kusongesha lengo namba 4 la malengo ya maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa linalohusu elimu bora.
10/5/20230
Episode Artwork

05 OKTOBA 2023

Mwandishi wetu wa Kenya Thelma Mwadzaya ametembelea maktaba ya Little Voice Deep iliyoko jijini Nairobi kujionea jinsi gani kupitia waalimu walioko inavyochangia kuhakikisha watoto wanapata elimu wanayoitaka na kusongesha lengo namba 4 la malengo ya maendeleo endelevu ya Umoja wa Mataifa linalohusu elimu bora.
10/5/20230
Episode Artwork

Uchumi wa dunia uko njiapanda: UNCTAD

Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa UNCTAD, imezindua leo ripoti yake kuu ya Biashara na Maendeleo ya mwaka 2023 ambayo inachunguza kuimarika kwa uchumi wa dunia na kutoa utabiri wa kinachotarajiwa. Ripoti inaeleza hatua za kisera zinazopaswa kuchukuliwa ili kulinda uchumi wa dunia kutokana na matatizo ya kimfumo ya siku zijazo. Hii ni ripoti ambayo hutolewa kila mwaka ikitathimini mwenendo wa ukuaji wa uchumi kote duniani, changamoto zinazojitokeza na nini kifanyike ili kuhakikisha uchumi unaendelea kukua na kuepusha athari kubwa kwa nchi lakini pia kwa Dunia nzima.Ripoti hiyo iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi safari hii imeonya kwamba uchumi wa Dunia unadorora na kuna tofauti kubwa za ukuaji wa uchumi huo miongoni mwa nchi na kanda duniani. Inasema “Ukuaji wa uchumi wa dunia unatarajiwa kupungua kutoka asilimia 3 mwaka jana hadi asilimmia 2.4 mwaka huu huku kukiwa na dalili chache za kuimarika tena mwaka ujao.”Hivyo imeweka bayana kwamba “Uchumi wa dunia uko katika njia panda.”Ripoti hiyo ya UNCTAD imeendelea kueleza kwamba “Njia tofauti za ukuaji uchumi, kuongezeka kwa ukosefu wa usawa, kukua kwa hali ya kujikita na masoko na mzigo wa madeni vinahatarisha mustakabali wake wa uchumi wa dunia.” Mathalani ripoti imesema wakati nchi zilizoendelea kama Marekani, Uchina na nyinginezo za Ulaya zikijaribu kujikwamua kiuchumi kutokana na athari za janga la COVID-19 katika nchi zinazoendelea mchanganyiko wa viwango vya riba vinavyoongezeka, kudhoofika kwa sarafu zao na ukuaji duni wa mauzo ya nje vinabana nafasi ya kifedha inayohitajika kwa serikali kutoa huduma muhimu, na kubadilisha mzigo unaokua wa huduma ya madeni kuwa changamoto ya maendeleo inayojitokeza.Takriban watu bilioni 3.3  karibu nusu ya binadamu wote duniani sasa wanaishi katika nchi ambazo hutumia zaidi fecha kwa ajili ya malipo yenye riba ya madeni kuliko katika huduma za elimu au afya.Na nchi ambazo zimeathirika zaidi ni nchi zinazoendelea zenye kipato cha chini au ambazo zilianza kupata masoko ya mitaji ya kimataifa baada ya msukosuko wa kifedha duniani.Kwa mantiki hiyo UNCTAD inatoa wito wa “Kutaka mageuzi ya kitaasisi katika usimamizi wa fedha duniani, sera za kiutendaji zaidi za kukabiliana na mfumuko wa bei, ukosefu wa usawa, madeni katika nchi na uangalizi thabiti wa masoko muhimu ili kufikia uthabiti wa kifedha, kuongeza uwekezaji wenye tija na kuunda nafasi bora za kazi.
10/4/20230
Episode Artwork

Uchumi wa dunia uko njiapanda: UNCTAD

Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa UNCTAD, imezindua leo ripoti yake kuu ya Biashara na Maendeleo ya mwaka 2023 ambayo inachunguza kuimarika kwa uchumi wa dunia na kutoa utabiri wa kinachotarajiwa. Ripoti inaeleza hatua za kisera zinazopaswa kuchukuliwa ili kulinda uchumi wa dunia kutokana na matatizo ya kimfumo ya siku zijazo. Hii ni ripoti ambayo hutolewa kila mwaka ikitathimini mwenendo wa ukuaji wa uchumi kote duniani, changamoto zinazojitokeza na nini kifanyike ili kuhakikisha uchumi unaendelea kukua na kuepusha athari kubwa kwa nchi lakini pia kwa Dunia nzima.Ripoti hiyo iliyotolewa leo mjini Geneva Uswisi safari hii imeonya kwamba uchumi wa Dunia unadorora na kuna tofauti kubwa za ukuaji wa uchumi huo miongoni mwa nchi na kanda duniani. Inasema “Ukuaji wa uchumi wa dunia unatarajiwa kupungua kutoka asilimia 3 mwaka jana hadi asilimmia 2.4 mwaka huu huku kukiwa na dalili chache za kuimarika tena mwaka ujao.”Hivyo imeweka bayana kwamba “Uchumi wa dunia uko katika njia panda.”Ripoti hiyo ya UNCTAD imeendelea kueleza kwamba “Njia tofauti za ukuaji uchumi, kuongezeka kwa ukosefu wa usawa, kukua kwa hali ya kujikita na masoko na mzigo wa madeni vinahatarisha mustakabali wake wa uchumi wa dunia.” Mathalani ripoti imesema wakati nchi zilizoendelea kama Marekani, Uchina na nyinginezo za Ulaya zikijaribu kujikwamua kiuchumi kutokana na athari za janga la COVID-19 katika nchi zinazoendelea mchanganyiko wa viwango vya riba vinavyoongezeka, kudhoofika kwa sarafu zao na ukuaji duni wa mauzo ya nje vinabana nafasi ya kifedha inayohitajika kwa serikali kutoa huduma muhimu, na kubadilisha mzigo unaokua wa huduma ya madeni kuwa changamoto ya maendeleo inayojitokeza.Takriban watu bilioni 3.3  karibu nusu ya binadamu wote duniani sasa wanaishi katika nchi ambazo hutumia zaidi fecha kwa ajili ya malipo yenye riba ya madeni kuliko katika huduma za elimu au afya.Na nchi ambazo zimeathirika zaidi ni nchi zinazoendelea zenye kipato cha chini au ambazo zilianza kupata masoko ya mitaji ya kimataifa baada ya msukosuko wa kifedha duniani.Kwa mantiki hiyo UNCTAD inatoa wito wa “Kutaka mageuzi ya kitaasisi katika usimamizi wa fedha duniani, sera za kiutendaji zaidi za kukabiliana na mfumuko wa bei, ukosefu wa usawa, madeni katika nchi na uangalizi thabiti wa masoko muhimu ili kufikia uthabiti wa kifedha, kuongeza uwekezaji wenye tija na kuunda nafasi bora za kazi.
10/4/20230
Episode Artwork

04 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia ripoti ya UNCTAD na elimu kwa watoto wote. Makala tunarejelea uchambuzi wa ibara ya 10 ya Tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa. Mashinani tunakupeleka nchini DRC, kulikoni? Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa UNCTAD, imezindua leo ripoti yake kuu ya Biashara na Maendeleo ya mwaka 2023 ambayo inachunguza kuimarika kwa uchumi wa dunia na kutoa utabiri wa kinachotarajiwa. Ripoti inaeleza hatua za kisera zinazopaswa kuchukuliwa ili kulinda uchumi wa dunia kutokana na matatizo ya kimfumo ya siku zijazo.Katika kuhakikisha hakuna mtoto yeyote anayeachwa nyuma kupata elimu Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF linatekeleza mradi wa kutoa mafunzo kwa walimu nchini Ghana na tayari wanafunzi 37,000 wamenufaika na mafunzo waliopewa walimu wao. Leah Mushi anatuletea taarifa ya Mwalimu Sam mnufaika wa mafunzo yanayofadhiliwa na UNICEF.Katika mwendelezo wa uchambuzi wa tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, leo tunaangazia ibara ya 10 ambayo inasema kwamba “Kila mtu mwenye kesi ana haki ya kusikilizwa kwa haki katika mahakama iliyo wazi kwa umma, yenye kujitegemea, huru na isiyo na upendeleo. Ili kufahamu zaidi kuhusu Ibara hii niliwahi kuzungumza na Dkt. Elifuraha Laltaika, Mhadhiri Mwandamizi wa sheria kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini Makumira nchini Tanzania na alianza kwa kuelezea historia ya ibara hiyo.Katika mashinani Kivu Kusini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kushuhudia jinsi masomo ya kujua kusoma na kuandika inavyoelimisha wananchi kuendesha biashara zao.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/4/20230
Episode Artwork

04 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia ripoti ya UNCTAD na elimu kwa watoto wote. Makala tunarejelea uchambuzi wa ibara ya 10 ya Tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa. Mashinani tunakupeleka nchini DRC, kulikoni? Kamati ya biashara na maendeleo ya Umoja wa Mataifa UNCTAD, imezindua leo ripoti yake kuu ya Biashara na Maendeleo ya mwaka 2023 ambayo inachunguza kuimarika kwa uchumi wa dunia na kutoa utabiri wa kinachotarajiwa. Ripoti inaeleza hatua za kisera zinazopaswa kuchukuliwa ili kulinda uchumi wa dunia kutokana na matatizo ya kimfumo ya siku zijazo.Katika kuhakikisha hakuna mtoto yeyote anayeachwa nyuma kupata elimu Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF linatekeleza mradi wa kutoa mafunzo kwa walimu nchini Ghana na tayari wanafunzi 37,000 wamenufaika na mafunzo waliopewa walimu wao. Leah Mushi anatuletea taarifa ya Mwalimu Sam mnufaika wa mafunzo yanayofadhiliwa na UNICEF.Katika mwendelezo wa uchambuzi wa tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, leo tunaangazia ibara ya 10 ambayo inasema kwamba “Kila mtu mwenye kesi ana haki ya kusikilizwa kwa haki katika mahakama iliyo wazi kwa umma, yenye kujitegemea, huru na isiyo na upendeleo. Ili kufahamu zaidi kuhusu Ibara hii niliwahi kuzungumza na Dkt. Elifuraha Laltaika, Mhadhiri Mwandamizi wa sheria kutoka Chuo Kikuu cha Tumaini Makumira nchini Tanzania na alianza kwa kuelezea historia ya ibara hiyo.Katika mashinani Kivu Kusini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kushuhudia jinsi masomo ya kujua kusoma na kuandika inavyoelimisha wananchi kuendesha biashara zao.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
10/4/20230
Episode Artwork

UNICEF yafanikisha mbinu bunifu za ufundishaji na zimeongeza uelewa wa wanafunzi Ghana

Katika kuhakikisha hakuna mtoto yeyote anayeachwa nyuma kupata elimu Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF linatekeleza mradi wa kutoa mafunzo kwa walimu nchini Ghana na tayari wanafunzi 37,000 wamenufaika na mafunzo waliopewa walimu wao. Leah Mushi anatuletea taarifa ya Mwalimu Sam mnufaika wa mafunzo yanayofadhiliwa na UNICEF.Video ya UNICEF inaanza kwa kumuonesha mwalimu Sam anaendesha baiskeli akielekea shuleniWalimu Sam anasema yeye ana falsafa yake ya ufundishaji,  “Ukitaka kupanga kwa mwaka mmoja utapanda mpunga, kwa muongo mmoja utapanda miti lakini ukitaka kupanga kwa maisha yote unachotakiwa kufanya ni kuelimisha watu na hiyo ndio falsafa yangu kama mwalimu.” Mwalimu Sam anasema katika kila darasa uelewa wa watoto unatofautiana ndio maana huwaweka katika makundi tofauti. “Nawapa kila kikundi zoezi fulani kutokana na uwezo wao wa kujifunza, na natenga muda wangu ili kuhakikisha nafikia kila kikundi ili kufikia kiwango fulani, na kila mtu ataweza kuelewa nafundisha nini.”Na manufaa yameonekana kwani, “Darasani kwangu asilimia 80 mpaka 90 wanaweza kusoma vizuri kutokana na mbinu ninayotumia kuwafundisha.” Na huu ndio ushauri wa mwalimu Sam kwako.“Ukitaka kufanya jambo lolote kwenye maisha inakubidi ufanye msingi kwenye kila somo ili kupata uelewa mpana wa kukuwezesha kukabiliana na changamoto unazokumbana nazo kwenye maisha.”
10/4/20230
Episode Artwork

UNICEF yafanikisha mbinu bunifu za ufundishaji na zimeongeza uelewa wa wanafunzi Ghana

Katika kuhakikisha hakuna mtoto yeyote anayeachwa nyuma kupata elimu Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF linatekeleza mradi wa kutoa mafunzo kwa walimu nchini Ghana na tayari wanafunzi 37,000 wamenufaika na mafunzo waliopewa walimu wao. Leah Mushi anatuletea taarifa ya Mwalimu Sam mnufaika wa mafunzo yanayofadhiliwa na UNICEF.Video ya UNICEF inaanza kwa kumuonesha mwalimu Sam anaendesha baiskeli akielekea shuleniWalimu Sam anasema yeye ana falsafa yake ya ufundishaji,  “Ukitaka kupanga kwa mwaka mmoja utapanda mpunga, kwa muongo mmoja utapanda miti lakini ukitaka kupanga kwa maisha yote unachotakiwa kufanya ni kuelimisha watu na hiyo ndio falsafa yangu kama mwalimu.” Mwalimu Sam anasema katika kila darasa uelewa wa watoto unatofautiana ndio maana huwaweka katika makundi tofauti. “Nawapa kila kikundi zoezi fulani kutokana na uwezo wao wa kujifunza, na natenga muda wangu ili kuhakikisha nafikia kila kikundi ili kufikia kiwango fulani, na kila mtu ataweza kuelewa nafundisha nini.”Na manufaa yameonekana kwani, “Darasani kwangu asilimia 80 mpaka 90 wanaweza kusoma vizuri kutokana na mbinu ninayotumia kuwafundisha.” Na huu ndio ushauri wa mwalimu Sam kwako.“Ukitaka kufanya jambo lolote kwenye maisha inakubidi ufanye msingi kwenye kila somo ili kupata uelewa mpana wa kukuwezesha kukabiliana na changamoto unazokumbana nazo kwenye maisha.”
10/4/20230
Episode Artwork

03 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na inatupeleka Kibokoni, Kaunti ya Kilifi nchini Kenya ambako mabwawa ya samaki yamebadili kabisa maisha ya wavuvi wa eneo hilo walioathirika na mabadiliko ya tabianchi yaliyosabisha samaki kutoweka baharini na kuwakatisha tamaa ya Maisha. Lakini sasa kupitia mradi wa ufugaji samaki ulio chini ya mwamvuli wa Umoja Self-Help Group jamii hiyo ina mabwawa 17 ya samaki yanayozalisha samaki aina ya milkfish, kamba, kaa, sandfish, rabbitfish na perege au tilapia. Mshiani tanakuletea ujumbe kusu afya ya uzazi na uswa wa kijinsia. Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) leo limeonya kwamba hali ya njaa inaibuka kwenye mpaka kati ya Sudan Kusini na Sudan huku familia zinazokimbia mapigano nchini Sudan zikiendelea kuvuka mpaka kila siku. Takwimu mpya zilizokusanywa na WFP zinaonesha kuwa kati ya karibu watu 300,000 ambao wamewasili Sudan Kusini katika miezi mitano iliyopita, mtoto mmoja kati ya watano ana utapiamlo na asilimia 90 ya familia wanasema wanakaa siku nyingi bila kula.Leo imetimia miaka 10 kamili tangu ajali ya meli iliyokuwa imebeba wahamiaji zaidi ya 500 kutoka Libya barani Afrika kuelekea nchini Italia ilipozama kwenye eneo la Lampedusa.  Katika taarifa ya pamoja ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji, Amy E. Pope, na Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi,(UNHCR) Filippo Grandi wamesema tukio hilo baya lilipotokea dunia iliahidi, “isitokee tena” lakini hilo halijatekelezeka.  Mwaka huu pekee kufikia jana Oktoba pili tayari watu 2,517 wameshahesabiwa kuwa wamefariki dunia au kupotea katika bahari ya Mediterania.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) limesema leo kuwa Armenia inakabiliwa na changamoto za kiafya kutokana na wimbi la wakimbizi ambalo halijawahi kushuhudiwa. Lakini wakati huo huo mashirika ya Umoja wa Mataifa kama la Afya ya Uzazi na Idadi ya watu duniani UNFPA limepeleka vifaa vya afya ya uzazi na la Kuhudumia Watoto UNICEF limeanzisha eneo salama huko Goris, kusini mwa Armenia.Katika mashinani Dk. Natalia Kanem, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu na afya ya uzazi UNFPA anatoa ujumbe kuhusu upatikanaji wa afya Uzazi kwa wote, na usawa wa kijinsia.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
10/3/20230
Episode Artwork

03 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na inatupeleka Kibokoni, Kaunti ya Kilifi nchini Kenya ambako mabwawa ya samaki yamebadili kabisa maisha ya wavuvi wa eneo hilo walioathirika na mabadiliko ya tabianchi yaliyosabisha samaki kutoweka baharini na kuwakatisha tamaa ya Maisha. Lakini sasa kupitia mradi wa ufugaji samaki ulio chini ya mwamvuli wa Umoja Self-Help Group jamii hiyo ina mabwawa 17 ya samaki yanayozalisha samaki aina ya milkfish, kamba, kaa, sandfish, rabbitfish na perege au tilapia. Mshiani tanakuletea ujumbe kusu afya ya uzazi na uswa wa kijinsia. Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) leo limeonya kwamba hali ya njaa inaibuka kwenye mpaka kati ya Sudan Kusini na Sudan huku familia zinazokimbia mapigano nchini Sudan zikiendelea kuvuka mpaka kila siku. Takwimu mpya zilizokusanywa na WFP zinaonesha kuwa kati ya karibu watu 300,000 ambao wamewasili Sudan Kusini katika miezi mitano iliyopita, mtoto mmoja kati ya watano ana utapiamlo na asilimia 90 ya familia wanasema wanakaa siku nyingi bila kula.Leo imetimia miaka 10 kamili tangu ajali ya meli iliyokuwa imebeba wahamiaji zaidi ya 500 kutoka Libya barani Afrika kuelekea nchini Italia ilipozama kwenye eneo la Lampedusa.  Katika taarifa ya pamoja ya Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji, Amy E. Pope, na Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi,(UNHCR) Filippo Grandi wamesema tukio hilo baya lilipotokea dunia iliahidi, “isitokee tena” lakini hilo halijatekelezeka.  Mwaka huu pekee kufikia jana Oktoba pili tayari watu 2,517 wameshahesabiwa kuwa wamefariki dunia au kupotea katika bahari ya Mediterania.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) limesema leo kuwa Armenia inakabiliwa na changamoto za kiafya kutokana na wimbi la wakimbizi ambalo halijawahi kushuhudiwa. Lakini wakati huo huo mashirika ya Umoja wa Mataifa kama la Afya ya Uzazi na Idadi ya watu duniani UNFPA limepeleka vifaa vya afya ya uzazi na la Kuhudumia Watoto UNICEF limeanzisha eneo salama huko Goris, kusini mwa Armenia.Katika mashinani Dk. Natalia Kanem, Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu na afya ya uzazi UNFPA anatoa ujumbe kuhusu upatikanaji wa afya Uzazi kwa wote, na usawa wa kijinsia.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
10/3/20230
Episode Artwork

02 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya kimataifa ya makazi, na simulizi ya wakimbizi wa Armania kutoka Karabakh. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani nchini Kenya, kulikoniMipango ya jamii kudhibiti taka katika maeneo yao inaunga mkono uundaji wa mzunguko wa uchumi, anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake mahususi kwa ajili ya Siku ya leo ya Kimataifa ya Makazi na anaongeza kuwa “juhudi za umma za kupanua maeneo safi ya kijani yanasaidia kupoza maeneo ya mijini nyakati za mawimbi ya joto.”Nchini Armenia, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, linahaha kusaidia wakimbizi wanaoendelea kumiminika nchini humo kutoka eneo la Karabakh linalogombewa kati ya Armenia na Azerbaijan ambako sasa idadi ya wakimbizi waliowasili katika kipindi kisichozidi wiki moja ni zaidi ya laki moja na wako taabani.Makala makala inatupeleka Kenya ambako Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa, Nairobi Kenya UNIS amezungumza na mmoja wa wazee wastaafu wa Umoja wa Mataifa katika maadhimisho maalum yaliyofanyika leo kuadhimisha siku ya wazee duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka Oktoba Mosi.Katika mashinani Benedicto Kapaya, mfanyakazi wa kujitolea kutoka Tanzania ambaye ameitikia wito wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni, WHO wa kuhamasisha wenyeji wa vijiji vya Muzee na Kalakala kuhakikisha watoto wote wamepatiwa chanjo ya polio katika kampeni ya chanjo inayoendelea nchini humo.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/2/20230
Episode Artwork

02 OKTOBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya kimataifa ya makazi, na simulizi ya wakimbizi wa Armania kutoka Karabakh. Makala tunakupeleka nchini Tanzania na mashinani nchini Kenya, kulikoniMipango ya jamii kudhibiti taka katika maeneo yao inaunga mkono uundaji wa mzunguko wa uchumi, anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake mahususi kwa ajili ya Siku ya leo ya Kimataifa ya Makazi na anaongeza kuwa “juhudi za umma za kupanua maeneo safi ya kijani yanasaidia kupoza maeneo ya mijini nyakati za mawimbi ya joto.”Nchini Armenia, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, linahaha kusaidia wakimbizi wanaoendelea kumiminika nchini humo kutoka eneo la Karabakh linalogombewa kati ya Armenia na Azerbaijan ambako sasa idadi ya wakimbizi waliowasili katika kipindi kisichozidi wiki moja ni zaidi ya laki moja na wako taabani.Makala makala inatupeleka Kenya ambako Stella Vuzo afisa habari wa kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa, Nairobi Kenya UNIS amezungumza na mmoja wa wazee wastaafu wa Umoja wa Mataifa katika maadhimisho maalum yaliyofanyika leo kuadhimisha siku ya wazee duniani ambayo huadhimishwa kila mwaka Oktoba Mosi.Katika mashinani Benedicto Kapaya, mfanyakazi wa kujitolea kutoka Tanzania ambaye ameitikia wito wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni, WHO wa kuhamasisha wenyeji wa vijiji vya Muzee na Kalakala kuhakikisha watoto wote wamepatiwa chanjo ya polio katika kampeni ya chanjo inayoendelea nchini humo.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
10/2/20230
Episode Artwork

Wakimbizi kutoka Kabarakh wasimulia yaliyowasibu

Nchini Armenia, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, linahaha kusaidia wakimbizi wanaoendelea kumiminika nchini humo kutoka eneo la Karabakh linalogombewa kati ya Armenia na Azerbaijan ambako sasa idadi ya wakimbizi waliowasili katika kipindi kisichozidi wiki moja ni zaidi ya laki moja na wako taabani.Tuko eneo la Goris, jimboni Syunik kusini mwa Armenia, taifa hili la Ulaya Mashariki, wakimbizi wake kwa waume, vijana na watoto wakiwasili kutoka Karabakh, magari yamesheheni virago vyao. Marine mmoja wa wakimbizi hao anasema, “leo tunakwenda Yerevan kusajiliwa na kupata pahala pa kuishi, tuko wanne, Nahitaji kumhudumia binti yangu mdogo.” Mkimbizi mwingine anakumbuka safari yao akisema “ilikuwa ngumu sana, tulikuwa barabarani kwa saa kati ya 26 hadi 29. Kulikuwa na msururu mrefu wa magari, ilikuwa vigumu sana kufika hapa. Mama yangu ni mgonwa, na kaka yangu ana watoto na wajukuu.” Serikali ya Armenia kwa msaada wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR) na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa na mashirika yakiraia imebeba jukumu la kuwalinda na kusaidia wakimbizi. “Niko hapa mji wa Goris ambako zaidi ya wakimbizi 100,000 wamewasili hapa Armenia, baada ya kutumia siku kadhaa njiani. Wamewasili hapa wamechoka, wameacha kila kitu chao nyumbani. Watu wanahitaji msaada wa dharura. UNHCR imekuweko kwenye eneo hili  mapema kuwapatia wahitaji misaada ya dharura, vitanda na magodoro. Tunayo malori ambayo yatawasili na kuendelea kutoa msaada kwa wale wenye uhitaji zaidi.” 
10/2/20230
Episode Artwork

Wakimbizi kutoka Kabarakh wasimulia yaliyowasibu

Nchini Armenia, shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR, linahaha kusaidia wakimbizi wanaoendelea kumiminika nchini humo kutoka eneo la Karabakh linalogombewa kati ya Armenia na Azerbaijan ambako sasa idadi ya wakimbizi waliowasili katika kipindi kisichozidi wiki moja ni zaidi ya laki moja na wako taabani.Tuko eneo la Goris, jimboni Syunik kusini mwa Armenia, taifa hili la Ulaya Mashariki, wakimbizi wake kwa waume, vijana na watoto wakiwasili kutoka Karabakh, magari yamesheheni virago vyao. Marine mmoja wa wakimbizi hao anasema, “leo tunakwenda Yerevan kusajiliwa na kupata pahala pa kuishi, tuko wanne, Nahitaji kumhudumia binti yangu mdogo.” Mkimbizi mwingine anakumbuka safari yao akisema “ilikuwa ngumu sana, tulikuwa barabarani kwa saa kati ya 26 hadi 29. Kulikuwa na msururu mrefu wa magari, ilikuwa vigumu sana kufika hapa. Mama yangu ni mgonwa, na kaka yangu ana watoto na wajukuu.” Serikali ya Armenia kwa msaada wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR) na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa na mashirika yakiraia imebeba jukumu la kuwalinda na kusaidia wakimbizi. “Niko hapa mji wa Goris ambako zaidi ya wakimbizi 100,000 wamewasili hapa Armenia, baada ya kutumia siku kadhaa njiani. Wamewasili hapa wamechoka, wameacha kila kitu chao nyumbani. Watu wanahitaji msaada wa dharura. UNHCR imekuweko kwenye eneo hili  mapema kuwapatia wahitaji misaada ya dharura, vitanda na magodoro. Tunayo malori ambayo yatawasili na kuendelea kutoa msaada kwa wale wenye uhitaji zaidi.” 
10/2/20230
Episode Artwork

Viongozi wa UN wanasema safisha mji wako ili kuunga mkono mzunuko wa uchumi

Mipango ya jamii kudhibiti taka katika maeneo yao inaunga mkono uundaji wa mzunguko wa uchumi, anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake mahususi kwa ajili ya Siku ya leo ya Kimataifa ya Makazi na anaongeza kuwa “juhudi za umma za kupanua maeneo safi ya kijani yanasaidia kupoza maeneo ya mijini nyakati za mawimbi ya joto.”Naye Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN Habitat), Maimunah Mohamed Sharif anasisitiza kauli hiyo ya Guterres akisema, “Safisha mji wako. Ondoa uchafu wako. Safisha mitaro. Ufanye mji wako kuwa msafi wa kijani. Hiki ndicho ninataka. Kubadilisha tabia. Usitupe taka kwenye mitaro. Unapokuwa na mvua kunafurika, unalaumu mabadiliko ya tabianchi. Ninafurahi kwamba hapa Kenya kumezuiliwa mifuko ya plastiki kwenye maduka lakini ukiangalia nje bado kuna mifuko ya plastiki kwenye mitaro. Kwa hiyo ninafiriki hicho ndicho mtu binafsi anaweza kufanya kama yeye.”Siku ya Kimataifa ya Makazi ya mwaka huu 2024 inaangazia 'Uchumi Mijini Wenye Mnepo’ na uwezekano wa miji kuwa vichochezi vya ukuaji jumuishi, wa kijani na endelevu.
10/2/20230
Episode Artwork

Viongozi wa UN wanasema safisha mji wako ili kuunga mkono mzunuko wa uchumi

Mipango ya jamii kudhibiti taka katika maeneo yao inaunga mkono uundaji wa mzunguko wa uchumi, anasema Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres katika ujumbe wake mahususi kwa ajili ya Siku ya leo ya Kimataifa ya Makazi na anaongeza kuwa “juhudi za umma za kupanua maeneo safi ya kijani yanasaidia kupoza maeneo ya mijini nyakati za mawimbi ya joto.”Naye Mkurugenzi Mtendaji wa shirika la Umoja wa Mataifa la Makazi Duniani (UN Habitat), Maimunah Mohamed Sharif anasisitiza kauli hiyo ya Guterres akisema, “Safisha mji wako. Ondoa uchafu wako. Safisha mitaro. Ufanye mji wako kuwa msafi wa kijani. Hiki ndicho ninataka. Kubadilisha tabia. Usitupe taka kwenye mitaro. Unapokuwa na mvua kunafurika, unalaumu mabadiliko ya tabianchi. Ninafurahi kwamba hapa Kenya kumezuiliwa mifuko ya plastiki kwenye maduka lakini ukiangalia nje bado kuna mifuko ya plastiki kwenye mitaro. Kwa hiyo ninafiriki hicho ndicho mtu binafsi anaweza kufanya kama yeye.”Siku ya Kimataifa ya Makazi ya mwaka huu 2024 inaangazia 'Uchumi Mijini Wenye Mnepo’ na uwezekano wa miji kuwa vichochezi vya ukuaji jumuishi, wa kijani na endelevu.
10/2/20230
Episode Artwork

Simulizi ya kijana mkimbizi Gad Harindimana Mnyarwanda nchini Uganda - FAO inavyofungua uwezo

Makala inatupeleka nchini Uganda kumsikiliza Gad Harindimana, kijana mkimbizi kutoka Rwanda anayeishi katika makazi ya wakimbizi Nakivale mnufaika wa programu ya Huduma za Ajira Vijijini inayoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kazi Duniani, ILO kupitia shirika lisilo la kiserikali la AVSI Foundation. Gad Harindimana amepata kazi ya ufundi pikipiki baada ya kukamilisha programu ya Huduma hizo. Anasimulia kwa lugha ya Kinyakole inayotafsiriwa na Anold Kayanda. 
9/29/20230
Episode Artwork

Simulizi ya kijana mkimbizi Gad Harindimana Mnyarwanda nchini Uganda - FAO inavyofungua uwezo

Makala inatupeleka nchini Uganda kumsikiliza Gad Harindimana, kijana mkimbizi kutoka Rwanda anayeishi katika makazi ya wakimbizi Nakivale mnufaika wa programu ya Huduma za Ajira Vijijini inayoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kazi Duniani, ILO kupitia shirika lisilo la kiserikali la AVSI Foundation. Gad Harindimana amepata kazi ya ufundi pikipiki baada ya kukamilisha programu ya Huduma hizo. Anasimulia kwa lugha ya Kinyakole inayotafsiriwa na Anold Kayanda. 
9/29/20230
Episode Artwork

FAO waeleza kwa nini kuzuia upotevu na utupaji wa chakula ni muhimu na jukumu la kila mtu

Katika siku ya kimataifa ya uhamasishaji kuhusu uelewa wa Upotevu na utupaji wa chakula, shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO linataka kila mtu atambue ni kwanini kuzuia na kupumguza upotevu na utupaji wa chakula ni muhimu hasa katika kuchangia mabadiliko ya mifumo ya chakula na utimizaji wa malengo ya maendeleo endelevu SDGs. Siku yam waka huu ambayo imebeba mauadhui “Komesha upotevu na utupaji wa chakula kwa ajili ya watu na sayari” inaadhimishwa huku kati ya watu milioni 691 na 783 walikabiliwa na njaa mmwaka 2022 limesema shirika hilo.Likisisitiza jinsi hali inavyohitaji kubadilika haraka shirika hilo linasema wakati njaa na kutokuwa na uhakika wa chakula kukiendelea duniani mwaka 2022 inakadiriwa kuwa asilimia 13 ya chakula duniani ilipotea kwenye mnyororo wa thamani kuanzia baada ya kuvunwa na kabla ya kufika sokoni, na asilimia 17 nyingine ilitupwa majumbani, kwenye sehemu za utoaji huduma za chakula na kwenye masoko ya chakula.Hivyo FAO inatatoa mwito wa kuchukua hatua kwa mashirika ya umma, sekta binafsi, na kila mtu ili kupunguza upotevu na utupaji wa chakula (FLW) na kuelekea kubadilisha mifumo ya kilimo kwa ajili ya kuweza kuchangia katika mafanikio ya utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya 2030. Kwani limesema Kupunguza upotevu na utupaji wa chakula kunaweza kuwa na jukumu muhimu katika sio tu kwa mabadiliko ya mifumo ya chakula ya kilimo bali pia kwa kuongeza upatikanaji wa chakula, kuchangia uhakika wa chakula, lishe bora, na kujenga mnepo. Upunguzaji wa upotevu na utupaji wa chakula kwa mujibibu wa FAO pia hutumika kama mkakati muhimu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kwa kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi (GHGs). Kwa hivyo unaweza kusaidia nchi na biashara kuongeza hamasa ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi, huku zikihifadhi na kulinda mifumo yetu ya ikolojia na maliasili ambayo mustakabali wa chakula huitegemea.FAO inasema hivi sasa, mifumo mingi ya kilimo ya chakula duniani sio endelevu, kwani inaharibu ardhi ya kilimo, inachangia uzalishaji wa gesi chafu na upotevu wa bioanuwai na hutumia maji mengi ya ardhini. Mifumo ya chakula pia iko hatarini kwa majanga ya hali ya hewa na mishtuko mingine, kwa sababu ya athari kwa mazingira.
9/29/20230
Episode Artwork

FAO waeleza kwa nini kuzuia upotevu na utupaji wa chakula ni muhimu na jukumu la kila mtu

Katika siku ya kimataifa ya uhamasishaji kuhusu uelewa wa Upotevu na utupaji wa chakula, shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO linataka kila mtu atambue ni kwanini kuzuia na kupumguza upotevu na utupaji wa chakula ni muhimu hasa katika kuchangia mabadiliko ya mifumo ya chakula na utimizaji wa malengo ya maendeleo endelevu SDGs. Siku yam waka huu ambayo imebeba mauadhui “Komesha upotevu na utupaji wa chakula kwa ajili ya watu na sayari” inaadhimishwa huku kati ya watu milioni 691 na 783 walikabiliwa na njaa mmwaka 2022 limesema shirika hilo.Likisisitiza jinsi hali inavyohitaji kubadilika haraka shirika hilo linasema wakati njaa na kutokuwa na uhakika wa chakula kukiendelea duniani mwaka 2022 inakadiriwa kuwa asilimia 13 ya chakula duniani ilipotea kwenye mnyororo wa thamani kuanzia baada ya kuvunwa na kabla ya kufika sokoni, na asilimia 17 nyingine ilitupwa majumbani, kwenye sehemu za utoaji huduma za chakula na kwenye masoko ya chakula.Hivyo FAO inatatoa mwito wa kuchukua hatua kwa mashirika ya umma, sekta binafsi, na kila mtu ili kupunguza upotevu na utupaji wa chakula (FLW) na kuelekea kubadilisha mifumo ya kilimo kwa ajili ya kuweza kuchangia katika mafanikio ya utekelezaji wa ajenda ya maendeleo ya 2030. Kwani limesema Kupunguza upotevu na utupaji wa chakula kunaweza kuwa na jukumu muhimu katika sio tu kwa mabadiliko ya mifumo ya chakula ya kilimo bali pia kwa kuongeza upatikanaji wa chakula, kuchangia uhakika wa chakula, lishe bora, na kujenga mnepo. Upunguzaji wa upotevu na utupaji wa chakula kwa mujibibu wa FAO pia hutumika kama mkakati muhimu dhidi ya mabadiliko ya tabianchi kwa kupunguza uzalishaji wa gesi chafuzi (GHGs). Kwa hivyo unaweza kusaidia nchi na biashara kuongeza hamasa ya kupambana na mabadiliko ya tabianchi, huku zikihifadhi na kulinda mifumo yetu ya ikolojia na maliasili ambayo mustakabali wa chakula huitegemea.FAO inasema hivi sasa, mifumo mingi ya kilimo ya chakula duniani sio endelevu, kwani inaharibu ardhi ya kilimo, inachangia uzalishaji wa gesi chafu na upotevu wa bioanuwai na hutumia maji mengi ya ardhini. Mifumo ya chakula pia iko hatarini kwa majanga ya hali ya hewa na mishtuko mingine, kwa sababu ya athari kwa mazingira.
9/29/20230
Episode Artwork

29 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia utupaji wa chakula, na uchaguzi ujao nchini Sudan Kusini. Makala tunakupeleka nchini Uganda na mashinani nchini DRC, kulikoni?.Hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, Baraza la Usalama limejadili hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambapo awali Naibu Mkuu wa ofisi ya Umoja huo kuhusu misaada ya kiutu Joyce Msuya anataja changamoto zinazokumba taifa hilo.Wakati nchi ya Sudan Kusini ikijiandaa kushiriki katika uchaguzi mkuu kwa mara ya kwanza kabisa tangu ipate uhuru, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS unaendesha makongamano na vyama vya siasa nchini humo.Makala inatupeleka nchini Uganda kumsikiliza Gad Harindimana, kijana mkimbizi kutoka Rwanda anayeishi katika makazi ya wakimbizi Nakivale mnufaika wa programu ya Huduma za Ajira Vijijini inayoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kazi Duniani, ILO kupitia shirika lisilo la kiserikali la AVSI Foundation. Harindimana anasimulia kwa lugha ya Kinyakole inayotafsiriwa na Anold Kayanda.Katika mashinani tutammsikia mwanamke ambaye aliweza kujifungua salama, na bila malipo, kwa usaidizi wa wakunga katika kliniki tembezi inayohifadhiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ya Uzazi na Idadi ya watu, UNFPA katika kambi ya wakimbizi wa ndani mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC.Mwenyeji wako ni Assumpta, karibu!
9/29/20230
Episode Artwork

29 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia utupaji wa chakula, na uchaguzi ujao nchini Sudan Kusini. Makala tunakupeleka nchini Uganda na mashinani nchini DRC, kulikoni?.Hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, Baraza la Usalama limejadili hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambapo awali Naibu Mkuu wa ofisi ya Umoja huo kuhusu misaada ya kiutu Joyce Msuya anataja changamoto zinazokumba taifa hilo.Wakati nchi ya Sudan Kusini ikijiandaa kushiriki katika uchaguzi mkuu kwa mara ya kwanza kabisa tangu ipate uhuru, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS unaendesha makongamano na vyama vya siasa nchini humo.Makala inatupeleka nchini Uganda kumsikiliza Gad Harindimana, kijana mkimbizi kutoka Rwanda anayeishi katika makazi ya wakimbizi Nakivale mnufaika wa programu ya Huduma za Ajira Vijijini inayoungwa mkono na Shirika la Umoja wa Mataifa la Kazi Duniani, ILO kupitia shirika lisilo la kiserikali la AVSI Foundation. Harindimana anasimulia kwa lugha ya Kinyakole inayotafsiriwa na Anold Kayanda.Katika mashinani tutammsikia mwanamke ambaye aliweza kujifungua salama, na bila malipo, kwa usaidizi wa wakunga katika kliniki tembezi inayohifadhiwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ya Uzazi na Idadi ya watu, UNFPA katika kambi ya wakimbizi wa ndani mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Kongo, DRC.Mwenyeji wako ni Assumpta, karibu!
9/29/20230
Episode Artwork

UNMISS wataka wanasiasa Sudan Kusini wapatie wanachi elimu ya kisiasa

Wakati nchi ya Sudan Kusini ikijiandaa kushiriki katika uchaguzi mkuu kwa mara ya kwanza kabisa tangu ipate uhuru, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS unaendesha makongamano na vyama vya siasa nchini humo. Ikiwa imesalia miezi 15 mpaka uchaguzi ufanyike hapo Desemba 2024 UNMISS wanasema lengo la kuandaa makongamano hayo nikujenga utamaduni wa kuwa na mazungumzo thabiti, kutatua changamoto zinazowakabili kuhusu utawala bora na kujenga kuaminiana miongoni mwa wanasiasa na jamii wanazozitumikia. Akiwa katika moja ya majukwaa huyo katika mji mkuu wa Juba Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini ambaye pia ni Mkuu wa UNMISS, Nicholas Haysom aliwaambia washiriki kuwa, “Uchaguzi hauwezi kufanyika ikiwa hakuna makubaliano ya masuala ya kiufundi. Hisia za uharaka walizonazo jumuiya ya kimataifa kuhusu uchaguzi hazisaidii. Udharura unawahusu Wasudan Kusini — wananchi, na hasa vyama vya siasa, ndiyo maana tutawaomba nyinyi kufanya kazi na kutusaidia sisi katika kuunda na kuelewa asili ya chaguzi mnazotaka kufanya ili na sisi tuweze kuhamasisha kupatikana kwa misaada kwa ajili ya mambo hayo.”Si wanasiasa pekee wanaohudhuria makongamano hayo bali pia wasomi ambao wamehimiza umuhimu wa kuwa na ushiriki mkubwa wa umma katika michakato ya amani, pamoja vyama vya siasa kuwa na ushindani imara kama anavyoeleza Adwak Nyaba, “Vyama vya siasa vinapaswa kuhimiza elimu ya kisiasa ili kuongeza ufahamu wa kijamii na ufahamu wa kisiasa wa wananchi. Ni kutokana na kuwepo kwa ufahamu wa kisiasa na watu wanaozingatia siasa kunakowezesha uwepo wa serikali za kidemokrasia. Ikiwa watu hawana ufahamu kabisa wa kisiasa, huwezi kuzungumzia utawala wa kidemokrasia, au huwezi kuzungumzia demokrasia.”Wanasiasa wamehimizwa kufikia makubaliano ya masuala muhimu haswa kuhusu uanzishwaji wa taasisi muhimu ambazo ni Baraza la Vyama vya Siasa, Tume ya Kitaifa ya Marekebisho ya Katiba na Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi.
9/29/20230
Episode Artwork

UNMISS wataka wanasiasa Sudan Kusini wapatie wanachi elimu ya kisiasa

Wakati nchi ya Sudan Kusini ikijiandaa kushiriki katika uchaguzi mkuu kwa mara ya kwanza kabisa tangu ipate uhuru, Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini humo UNMISS unaendesha makongamano na vyama vya siasa nchini humo. Ikiwa imesalia miezi 15 mpaka uchaguzi ufanyike hapo Desemba 2024 UNMISS wanasema lengo la kuandaa makongamano hayo nikujenga utamaduni wa kuwa na mazungumzo thabiti, kutatua changamoto zinazowakabili kuhusu utawala bora na kujenga kuaminiana miongoni mwa wanasiasa na jamii wanazozitumikia. Akiwa katika moja ya majukwaa huyo katika mji mkuu wa Juba Mwakilishi maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini ambaye pia ni Mkuu wa UNMISS, Nicholas Haysom aliwaambia washiriki kuwa, “Uchaguzi hauwezi kufanyika ikiwa hakuna makubaliano ya masuala ya kiufundi. Hisia za uharaka walizonazo jumuiya ya kimataifa kuhusu uchaguzi hazisaidii. Udharura unawahusu Wasudan Kusini — wananchi, na hasa vyama vya siasa, ndiyo maana tutawaomba nyinyi kufanya kazi na kutusaidia sisi katika kuunda na kuelewa asili ya chaguzi mnazotaka kufanya ili na sisi tuweze kuhamasisha kupatikana kwa misaada kwa ajili ya mambo hayo.”Si wanasiasa pekee wanaohudhuria makongamano hayo bali pia wasomi ambao wamehimiza umuhimu wa kuwa na ushiriki mkubwa wa umma katika michakato ya amani, pamoja vyama vya siasa kuwa na ushindani imara kama anavyoeleza Adwak Nyaba, “Vyama vya siasa vinapaswa kuhimiza elimu ya kisiasa ili kuongeza ufahamu wa kijamii na ufahamu wa kisiasa wa wananchi. Ni kutokana na kuwepo kwa ufahamu wa kisiasa na watu wanaozingatia siasa kunakowezesha uwepo wa serikali za kidemokrasia. Ikiwa watu hawana ufahamu kabisa wa kisiasa, huwezi kuzungumzia utawala wa kidemokrasia, au huwezi kuzungumzia demokrasia.”Wanasiasa wamehimizwa kufikia makubaliano ya masuala muhimu haswa kuhusu uanzishwaji wa taasisi muhimu ambazo ni Baraza la Vyama vya Siasa, Tume ya Kitaifa ya Marekebisho ya Katiba na Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi.
9/29/20230
Episode Artwork

Methali: Umekuwa Jeta Hubanduki!

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Umekuwa Jeta Hubanduki! 
9/28/20230
Episode Artwork

Methali: Umekuwa Jeta Hubanduki!

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali Umekuwa Jeta Hubanduki! 
9/28/20230
Episode Artwork

28 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO nchini Tanzania kwa kushirikiana na wadau wake wamewezesha hatua ya upimaji wa udongo katika wilaya sita ambako mradi wa kulinda na kuhifadhi baiyonuai unatekelezwa. Kazi hiyo imefanywa na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine - SUA, na sasa utafiti huo umekamilika, Je umebaini nini? John Kabambala wa redio washirika KidsTime ya Morogoro-Tanzania amehudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo ya vipimo vya udongo. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo za ulinzi wa amani, haki za binadamu na ubaguzi wa rangi. Na katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali “UMEKUWA JETA HUBANDUKI”.Hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, Baraza la Usalama limejadili hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambapo awali Naibu Mkuu wa ofisi ya Umoja huo kuhusu misaada ya kiutu Joyce Msuya anataja changamoto zinazokumba taifa hilo.Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu Volker Türk, ametoa wito wa ujumbe wa kimataifa wa kusaidia polisi wa kitaifa nchini Haiti kutokomeza mzunguko wa ghasia uliojikita kwenye ngazi zote za jamii na kuchochea janga la ukosefu wa usalama na haki za binadamu.Na mfumo wa kibaguzi dhidi ya wamarekani weusi wenye asili ya Afrika umepenyezwa hadi kwenye utendaji wa jeshi la polisi na mfumo wa mahakama nchini Marekani na hivyo lazima marekebisho ya haraka yafanywe ili kuondokana na madhila yanayokumba wananchi hao, imesema ripoti mpya ya wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali “Umekuwa Jeta Hubanduki!”.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/28/20230
Episode Artwork

28 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO nchini Tanzania kwa kushirikiana na wadau wake wamewezesha hatua ya upimaji wa udongo katika wilaya sita ambako mradi wa kulinda na kuhifadhi baiyonuai unatekelezwa. Kazi hiyo imefanywa na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine - SUA, na sasa utafiti huo umekamilika, Je umebaini nini? John Kabambala wa redio washirika KidsTime ya Morogoro-Tanzania amehudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo ya vipimo vya udongo. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo za ulinzi wa amani, haki za binadamu na ubaguzi wa rangi. Na katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali “UMEKUWA JETA HUBANDUKI”.Hii leo kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani, Baraza la Usalama limejadili hali ya kibinadamu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambapo awali Naibu Mkuu wa ofisi ya Umoja huo kuhusu misaada ya kiutu Joyce Msuya anataja changamoto zinazokumba taifa hilo.Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu Volker Türk, ametoa wito wa ujumbe wa kimataifa wa kusaidia polisi wa kitaifa nchini Haiti kutokomeza mzunguko wa ghasia uliojikita kwenye ngazi zote za jamii na kuchochea janga la ukosefu wa usalama na haki za binadamu.Na mfumo wa kibaguzi dhidi ya wamarekani weusi wenye asili ya Afrika umepenyezwa hadi kwenye utendaji wa jeshi la polisi na mfumo wa mahakama nchini Marekani na hivyo lazima marekebisho ya haraka yafanywe ili kuondokana na madhila yanayokumba wananchi hao, imesema ripoti mpya ya wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na hii leo Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali “Umekuwa Jeta Hubanduki!”.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/28/20230
Episode Artwork

Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine na FAO Tanzania wapima udongo katika wilaya 6 Tanzania

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO nchini Tanzania kwa kushirikiana na wadau wake wamewezesha hatua ya upimaji wa udongo katika wilaya sita ambako mradi wa kulinda na kuhifadhi baiyonuai unatekelezwa. Kazi hiyo imefanywa na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine - SUA, na sasa utafiti huo umekamilika, Je umebaini nini? John Kabambala wa redio washirika KidsTime ya Morogoro-Tanzania amehudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo ya vipimo vya udongo.
9/28/20230
Episode Artwork

Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine na FAO Tanzania wapima udongo katika wilaya 6 Tanzania

Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO nchini Tanzania kwa kushirikiana na wadau wake wamewezesha hatua ya upimaji wa udongo katika wilaya sita ambako mradi wa kulinda na kuhifadhi baiyonuai unatekelezwa. Kazi hiyo imefanywa na Chuo Kikuu cha Kilimo Sokoine - SUA, na sasa utafiti huo umekamilika, Je umebaini nini? John Kabambala wa redio washirika KidsTime ya Morogoro-Tanzania amehudhuria uzinduzi wa ripoti hiyo ya vipimo vya udongo.
9/28/20230
Episode Artwork

27 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tuanaangazia usafirishaji baharini, na ulinzi wa amani. Makala tunakupeleka mjini Roma na mashinani tutasalia hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kuikoni?Usafirishaji baharini unapaswa kuangaliwa upya ili kupunguza hewa ya ukaa au kaboni inayochafua mazingira, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo na Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara duniani, UNCTAD.Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA, Jenerali Humphrey Nyone amewataka walinda amani kutoka Tanzania wanaohudumu nchini humo chini ya MINUSCA kuendelea na moyo wa uchapa kazi huku wakizingatia kuepuka unyanyasaji na unyonyaji wa kingono.Katika makala Evarist Mapesa anayetuletea makala kutoka nchini Thailand ikiangazia mradi unaotekelezwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO wakusaidia wafanyabiashara kupunguza upotevu na utupaji wa chakula.Mashinani tunasalia katika ajenda 2030 ya malengo ya maendeleo endelevu kusikia ujumbe wa Orlando Bloom, Balozi Mwema wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/27/20230
Episode Artwork

27 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tuanaangazia usafirishaji baharini, na ulinzi wa amani. Makala tunakupeleka mjini Roma na mashinani tutasalia hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa, kuikoni?Usafirishaji baharini unapaswa kuangaliwa upya ili kupunguza hewa ya ukaa au kaboni inayochafua mazingira, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo na Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara duniani, UNCTAD.Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA, Jenerali Humphrey Nyone amewataka walinda amani kutoka Tanzania wanaohudumu nchini humo chini ya MINUSCA kuendelea na moyo wa uchapa kazi huku wakizingatia kuepuka unyanyasaji na unyonyaji wa kingono.Katika makala Evarist Mapesa anayetuletea makala kutoka nchini Thailand ikiangazia mradi unaotekelezwa na Shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo FAO wakusaidia wafanyabiashara kupunguza upotevu na utupaji wa chakula.Mashinani tunasalia katika ajenda 2030 ya malengo ya maendeleo endelevu kusikia ujumbe wa Orlando Bloom, Balozi Mwema wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Watoto, UNICEF.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/27/20230
Episode Artwork

Mradi wa FAO wa kupunguza upotevu wa chakula wazaa matunda nchini Thailand

Kupunguza upotevu wa chakula na taka kuna jukumu muhimu katika kubadilisha mifumo ya kilimo na chakula.Ajenda ya 2030 ya Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa SDGs inataka kupunguza nusu ya upotevu wa chakula duniani kwa kila mtu katika viwango vya rejareja na walaji wa mwisho na pia inapigia chepuo kuimarisha minyororo ya uzalishaji na usambazaji wa chakula.Nchini Thailand shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na kilimo FAO linatekeleza mradi wa kuwapatia ujuzi wafanyabiashara wadogo na wa kati ili waweze kupunguza upotevu na uharibifu wa chakula na pia kuongeza thamani ya mazao yao na hatimaye kujipatia kipato zaidi. Tuungane na Evarist Mapesa katika Makala hii akitujuza ziadi kuhusu mradi huo. 
9/27/20230
Episode Artwork

Mradi wa FAO wa kupunguza upotevu wa chakula wazaa matunda nchini Thailand

Kupunguza upotevu wa chakula na taka kuna jukumu muhimu katika kubadilisha mifumo ya kilimo na chakula.Ajenda ya 2030 ya Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Umoja wa Mataifa SDGs inataka kupunguza nusu ya upotevu wa chakula duniani kwa kila mtu katika viwango vya rejareja na walaji wa mwisho na pia inapigia chepuo kuimarisha minyororo ya uzalishaji na usambazaji wa chakula.Nchini Thailand shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na kilimo FAO linatekeleza mradi wa kuwapatia ujuzi wafanyabiashara wadogo na wa kati ili waweze kupunguza upotevu na uharibifu wa chakula na pia kuongeza thamani ya mazao yao na hatimaye kujipatia kipato zaidi. Tuungane na Evarist Mapesa katika Makala hii akitujuza ziadi kuhusu mradi huo. 
9/27/20230
Episode Artwork

UNCTAD: Hatua za kijasiri zahitajika kukabili hewa ya ukaa kwenye usafiri baharini

Usafirishaji baharini unapaswa kuangaliwa upya ili kupunguza hewa ya ukaa au kaboni inayochafua mazingira, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo na Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara duniani, UNCTAD. Ikipatiwa jina Usafiri wa Baharini mwaka 2030, ripoti inahimiza hatua za kijasiri na ushirikiano wa mfumo mzima kwa kuzingatia umuhimu wake duniani lakini vile vile uchafuzi wake wa mazingira sababu kuu ikiwa vyombo hivyo vya usafiri maji kuwa kuukuu.  Mkurugenzi wa UNCTAD anayehusika na teknolojia Shamika N. Sirimanne anasema, “Usafiri wa baharini ni tegemeo kuu la uchumi wa dunia ukibeba asilimia 80 ya biashara yote. Sekta hii muhimu inachangia asilimia 3 ya hewa chafuzi zinazotolewa duniani. Na kadri biashara kupitia usafiri wa baharíni unakua, vivyo utoaji wa hewa chafuzi ambao umeongezeka kwa asilimia 20 muongo mmoja uliopita.”  Sasa jawabu ni nini?  “Tunahitaji hatua za kijasiri duniani za kupunguza utoaji wa hewa ya ukaa wakati wa usafirishaji baharini. Na ili kuhakikisha mpito wenye haki na sawia katika kuelekea nishati salama ni lazima tushirikishe wadau wote kwenye sekta ya usafiri majini. UNCTAD tunatoa wito mifumo ya udhibiti ya kimataifa itumike kwa meli zote bila kujali ni ya nchi gani au inamilikiwa na nani.”  UNCTAD inasisitiza mfumo wa ushirikiano mpana zaidi, uingiliaji kati haraka kuchukua hatua na uwekezaji thabiti kwenye teknolojia za usafirishaji zisizochafua mazingira, halikadhalika ununuzi wa vyombo vipya vya usafiri  baharini. 
9/27/20230
Episode Artwork

UNCTAD: Hatua za kijasiri zahitajika kukabili hewa ya ukaa kwenye usafiri baharini

Usafirishaji baharini unapaswa kuangaliwa upya ili kupunguza hewa ya ukaa au kaboni inayochafua mazingira, imesema ripoti mpya iliyotolewa leo na Kamati ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo ya Biashara duniani, UNCTAD. Ikipatiwa jina Usafiri wa Baharini mwaka 2030, ripoti inahimiza hatua za kijasiri na ushirikiano wa mfumo mzima kwa kuzingatia umuhimu wake duniani lakini vile vile uchafuzi wake wa mazingira sababu kuu ikiwa vyombo hivyo vya usafiri maji kuwa kuukuu.  Mkurugenzi wa UNCTAD anayehusika na teknolojia Shamika N. Sirimanne anasema, “Usafiri wa baharini ni tegemeo kuu la uchumi wa dunia ukibeba asilimia 80 ya biashara yote. Sekta hii muhimu inachangia asilimia 3 ya hewa chafuzi zinazotolewa duniani. Na kadri biashara kupitia usafiri wa baharíni unakua, vivyo utoaji wa hewa chafuzi ambao umeongezeka kwa asilimia 20 muongo mmoja uliopita.”  Sasa jawabu ni nini?  “Tunahitaji hatua za kijasiri duniani za kupunguza utoaji wa hewa ya ukaa wakati wa usafirishaji baharini. Na ili kuhakikisha mpito wenye haki na sawia katika kuelekea nishati salama ni lazima tushirikishe wadau wote kwenye sekta ya usafiri majini. UNCTAD tunatoa wito mifumo ya udhibiti ya kimataifa itumike kwa meli zote bila kujali ni ya nchi gani au inamilikiwa na nani.”  UNCTAD inasisitiza mfumo wa ushirikiano mpana zaidi, uingiliaji kati haraka kuchukua hatua na uwekezaji thabiti kwenye teknolojia za usafirishaji zisizochafua mazingira, halikadhalika ununuzi wa vyombo vipya vya usafiri  baharini. 
9/27/20230
Episode Artwork

Mkuu wa MINUSCA kwa TANBAT6 - Zingatieni uhusiano mwema na raia

Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA, Jenerali Humphrey Nyone amewataka walinda amani kutoka Tanzania wanaohudumu nchini humo chini ya MINUSCA kuendelea na moyo wa uchapa kazi huku wakizingatia kuepuka unyanyasaji na unyonyaji wa kingono. Akitokea katika makao makuu ya MINUSCA yaliyoko kwenye mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, Bangui (tamka Bongii) takribani kilometa 292 magharibi mwa Mambéré-Kadéï, Jenerali Humphray Nyone ametua katika uwanja wa ndege wa mjini wa Berberati na baadaye akiambatana na wanadhimu wa kijeshi akazungumza na askari wa Kikosi cha 6 cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, TANBAT6 wanaohudumu chini ya MINUSCA, "Askari mila na desturi yake ni nidhamu na kufuata maelekezo. Hapa mlipo nimempata taarifa kutoka kwa kamanda Kikosi hiki Luteni Kanali Ramadhani Shaaban Ramadhani jinsi mnavyo jituma katika utendaji kazi wenu nimefurahi sana kusikia hivyo. Aidha hii ni kweli kwamba kikosi hiki kinasaidia kikundi changu vyema katika kutekeleza na kukamilisha jukumu la MINUSCA hapa Jamhuri ya Afrika ya Kati ninawasihi kuendelea hivyo bila kusahau kuzidi kuepuka suala zima la unyanyasaji wa kingono. Asante sana."Naye Kamanda wa TABAT6 Luteni Kanali Ramadhani Shaaban Ramadhani amesema amepokea na kuahidi kudumisha aliyoelekezwa katika katika utendaji wa kikosi hicho cha walinda amani kutoka Tanzania.
9/27/20230
Episode Artwork

Mkuu wa MINUSCA kwa TANBAT6 - Zingatieni uhusiano mwema na raia

Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA, Jenerali Humphrey Nyone amewataka walinda amani kutoka Tanzania wanaohudumu nchini humo chini ya MINUSCA kuendelea na moyo wa uchapa kazi huku wakizingatia kuepuka unyanyasaji na unyonyaji wa kingono. Akitokea katika makao makuu ya MINUSCA yaliyoko kwenye mji mkuu wa Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, Bangui (tamka Bongii) takribani kilometa 292 magharibi mwa Mambéré-Kadéï, Jenerali Humphray Nyone ametua katika uwanja wa ndege wa mjini wa Berberati na baadaye akiambatana na wanadhimu wa kijeshi akazungumza na askari wa Kikosi cha 6 cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, TANBAT6 wanaohudumu chini ya MINUSCA, "Askari mila na desturi yake ni nidhamu na kufuata maelekezo. Hapa mlipo nimempata taarifa kutoka kwa kamanda Kikosi hiki Luteni Kanali Ramadhani Shaaban Ramadhani jinsi mnavyo jituma katika utendaji kazi wenu nimefurahi sana kusikia hivyo. Aidha hii ni kweli kwamba kikosi hiki kinasaidia kikundi changu vyema katika kutekeleza na kukamilisha jukumu la MINUSCA hapa Jamhuri ya Afrika ya Kati ninawasihi kuendelea hivyo bila kusahau kuzidi kuepuka suala zima la unyanyasaji wa kingono. Asante sana."Naye Kamanda wa TABAT6 Luteni Kanali Ramadhani Shaaban Ramadhani amesema amepokea na kuahidi kudumisha aliyoelekezwa katika katika utendaji wa kikosi hicho cha walinda amani kutoka Tanzania.
9/27/20230
Episode Artwork

MONUSCO na ufanikishaji wa uchaguzi mkuu wa 2023 DRC

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, (MONUSCO) unashiriki katika maandalizi ya uchaguzi mkuu nchini humo unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu ambapo tayari umeshasaidia usafirishaji wa nyaraka za uchaguzi, halikadhalika mafunzo kwa polisi wa kitaifa ili uchaguzi huo uwe huru na ufanyike kwa amani.Ikumbukwe kuwa wiki iliyopita, Rais wa DRC Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akihutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani alithibitisha kuwa uchaguzi mkuu wa rais, wabunge, magavana na madiwani utafanyika kama ilivyopangwa na Tume Huru ya Uchaguzi nchini humo, CENI tayari imeshaanza kuchapisha majina ya wagombea.Tumesafirisha nyaraka nyeti za CENIAkizungumza George Musubao wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC, Msemaji wa MONUSCO mjini Beni-Lubero Bwana Jean Tobie Okala amesema “CENI  inatuambia inabidi zifanyike kwa hali ya usalama na amani. Jambo la kwanza ni kuungwa mkono kwa CENI. Nakujulisha kwamba tangu Januari 2023 MONUSCO imesafirisha maelfu ya tani za shehena nyeti sana za uchaguzi ambazo ni za CENI na ambazo zimewezesha shughuli za kurekodi na kuandikisha wapiga.”
9/26/20230
Episode Artwork

MONUSCO na ufanikishaji wa uchaguzi mkuu wa 2023 DRC

Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, (MONUSCO) unashiriki katika maandalizi ya uchaguzi mkuu nchini humo unaotarajiwa kufanyika mwishoni mwa mwaka huu ambapo tayari umeshasaidia usafirishaji wa nyaraka za uchaguzi, halikadhalika mafunzo kwa polisi wa kitaifa ili uchaguzi huo uwe huru na ufanyike kwa amani.Ikumbukwe kuwa wiki iliyopita, Rais wa DRC Félix Antoine Tshisekedi Tshilombo akihutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani alithibitisha kuwa uchaguzi mkuu wa rais, wabunge, magavana na madiwani utafanyika kama ilivyopangwa na Tume Huru ya Uchaguzi nchini humo, CENI tayari imeshaanza kuchapisha majina ya wagombea.Tumesafirisha nyaraka nyeti za CENIAkizungumza George Musubao wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa mjini Beni, jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC, Msemaji wa MONUSCO mjini Beni-Lubero Bwana Jean Tobie Okala amesema “CENI  inatuambia inabidi zifanyike kwa hali ya usalama na amani. Jambo la kwanza ni kuungwa mkono kwa CENI. Nakujulisha kwamba tangu Januari 2023 MONUSCO imesafirisha maelfu ya tani za shehena nyeti sana za uchaguzi ambazo ni za CENI na ambazo zimewezesha shughuli za kurekodi na kuandikisha wapiga.”
9/26/20230
Episode Artwork

26 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC Félix-Antoine Tshisekedi Tshilombo alihutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza  Kuu la Umoja wa Mataifa na kutangaza kuwa uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika nchini humo mwishoni mwa mwaka huu, utafanyika kama ilivyopangwa. Alisema tayari Tume Huru ya Uchaguzi nchini DRC, CENI [SENI] imeshachapisha majina ya wagombea na michakato mingine inaendelea. Kufuatia kauli hiyo, mwandishi wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa nchini humo, George Musubao amezungumza na msemaji wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani DRC, MONUSCO ofisi ya Beni-Lubero jimboni Kivu Kaskazini Tobi Okala, kufahamu MONUSCO inafanya nini kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uhuru na amani. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani, baki nasi!Hii leo Mjadala Mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa umekunja jamvi ambapo viongozi na wawakilishi kutoka nchi 15 wamehutubia wakiwemo kutoka India, Zambia na Morocco. Mjadala huo umefungwa na Rais wa Baraza Kuu Balozi Dennis Francis.Siku ya Kimataifa ya Kutokomeza Kabisa Silaha za Nyuklia inatukumbusha kwamba wakati ujao wenye amani unategemea kukomeshwa kwa tishio la nyuklia, ndivyo António Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa alivyouanza ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 26 Septemba. Kwa msingi huo Guterres anatoa wito mataifa yenye silaha za nyuklia yaongoze kwa kutimiza wajibu wao wa kupokonya silaha, na kujitolea kamwe kutotumia silaha za nyuklia kwa hali yoyote.Na Leo, ili kusaidia kulinda afya ya Watoto, Shirika la Umoja wa Matafa la Afya Ulimwenguni limetoa machapisho mawili mapya, “Uhuru dhidi ya tumbaku na nikotini: mwongozo kwa shule,” na “zana za shule zisizo na nikotini na tumbaku.” Lengo la machapisho hayo ni kuzuia hali ambayo inazidi kuenea ya matumizi ya sigara hasa za kielektroniki kwa vijana hasa wanafunzi.Katika mashinani Samuel Eto’o Rais wa shirikisho la soka Cameroon anasema mchezaji atamulika mbinu za kuepusha soka kutumika kusafirisha kiharamu binadamu.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/26/20230
Episode Artwork

26 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo hivi karibuni Rais wa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC Félix-Antoine Tshisekedi Tshilombo alihutubia mjadala mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza  Kuu la Umoja wa Mataifa na kutangaza kuwa uchaguzi mkuu uliopangwa kufanyika nchini humo mwishoni mwa mwaka huu, utafanyika kama ilivyopangwa. Alisema tayari Tume Huru ya Uchaguzi nchini DRC, CENI [SENI] imeshachapisha majina ya wagombea na michakato mingine inaendelea. Kufuatia kauli hiyo, mwandishi wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa nchini humo, George Musubao amezungumza na msemaji wa ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani DRC, MONUSCO ofisi ya Beni-Lubero jimboni Kivu Kaskazini Tobi Okala, kufahamu MONUSCO inafanya nini kuhakikisha uchaguzi unafanyika kwa uhuru na amani. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na mashinani, baki nasi!Hii leo Mjadala Mkuu wa mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa umekunja jamvi ambapo viongozi na wawakilishi kutoka nchi 15 wamehutubia wakiwemo kutoka India, Zambia na Morocco. Mjadala huo umefungwa na Rais wa Baraza Kuu Balozi Dennis Francis.Siku ya Kimataifa ya Kutokomeza Kabisa Silaha za Nyuklia inatukumbusha kwamba wakati ujao wenye amani unategemea kukomeshwa kwa tishio la nyuklia, ndivyo António Guterres, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa alivyouanza ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii inayoadhimishwa kila mwaka tarehe 26 Septemba. Kwa msingi huo Guterres anatoa wito mataifa yenye silaha za nyuklia yaongoze kwa kutimiza wajibu wao wa kupokonya silaha, na kujitolea kamwe kutotumia silaha za nyuklia kwa hali yoyote.Na Leo, ili kusaidia kulinda afya ya Watoto, Shirika la Umoja wa Matafa la Afya Ulimwenguni limetoa machapisho mawili mapya, “Uhuru dhidi ya tumbaku na nikotini: mwongozo kwa shule,” na “zana za shule zisizo na nikotini na tumbaku.” Lengo la machapisho hayo ni kuzuia hali ambayo inazidi kuenea ya matumizi ya sigara hasa za kielektroniki kwa vijana hasa wanafunzi.Katika mashinani Samuel Eto’o Rais wa shirikisho la soka Cameroon anasema mchezaji atamulika mbinu za kuepusha soka kutumika kusafirisha kiharamu binadamu.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/26/20230
Episode Artwork

Tuna imani Tanzania tutafikia lengo la huduma za afya kwa yote 2030: Waziri Ummy

Tanzania taifa lililo Afrika Mashariki limesema limejipanga vyema katika kutekeleza azimio la kuchukua hatua kuhusu huduma za afya kwa wote lililoidhinishwa kwa kauli moja mwishoni mwa juma na nchi zote wanachama wa Umoja wa Mataifa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Waziri wa afya wa Tanzania Ummy Mwalimu alikuwa miongoni mwa waliohudhuria na ameketi chini na Flora Nducha wa Idhaa hii na kumfafanulia mikakati yao ya kutekeleza azimio hilo.
9/25/20230
Episode Artwork

Tuna imani Tanzania tutafikia lengo la huduma za afya kwa wote 2030: Waziri Ummy

Tanzania taifa lililo Afrika Mashariki limesema limejipanga vyema katika kutekeleza azimio la kuchukua hatua kuhusu huduma za afya kwa wote lililoidhinishwa kwa kauli moja mwishoni mwa juma na nchi zote wanachama wa Umoja wa Mataifa hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Waziri wa afya wa Tanzania Ummy Mwalimu alikuwa miongoni mwa waliohudhuria na ameketi chini na Flora Nducha wa Idhaa hii na kumfafanulia mikakati yao ya kutekeleza azimio hilo.
9/25/20230
Episode Artwork

Vitendo vya kikatili vya Urusi nchini Ukraine vinasikitisha - Tume ya UN

Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchunguzi kuhusu Ukraine imeripoti leo kwa Baraza la Haki za Kibinadamu kwamba kuna ushahidi kuwa wanajeshi wa Urusi wanaendelea wanafanya uhalifu wa kivita nchini Ukraine.Katika taarifa yao waliyoiwasilisha leo katika ofisi za Umoja wa Mataifa jijini Geneva, Uswisi, Tume hiyo ya Huru ya Kimataifa ya Umoja wa Mataifa imeeleza kinagaubaga kwamba wanajeshi wa Urusi wanafanya mashambulizi haramu ya kutumia silaha za milipuko, mateso, unyanyasaji wa kingono na kijinsia, na mashambulizi dhidi ya miundombinu ya nishati.Wakati wa uwasilishaji kwa Baraza la Haki za Kibinadamu, Tume imeripoti kwamba imerekodi mashambulizi ya silaha za milipuko kwenye majengo ya makazi, kituo cha matibabu kinachofanya kazi, kituo cha reli, mgahawa, maduka na maghala ya biashara. Mashambulizi haya yalisababisha vifo vya raia, uharibifu wa miundombinu muhimu, na kukatizwa kwa huduma muhimu.Taarifa iliyosambazwa kwa vyombo vya Habari imeeleza kuwa Tume inachunguza sababu ya uvunjaji wa bwawa la Nova Kakhovka na athari zake kwa raia.Wakati huo huo Tume imeeleza kuwa uchunguzi wake huko Kherson na Zaporizhzhia unaonesha matumizi makubwa na yaliyoratibiwa ya utesaji yanayotekelezwa na vikosi vya jeshi la Urusi dhidi ya watu wanaoshutumiwa kuwa watoa habari wa vikosi vya jeshi la Ukraine. Katika matukio fulani, mateso yalifanywa kwa ukatili kiasi kwamba yalisababisha kifo.Mtu mmoja ambaye  aliteswa kwa kupigwa na mshtuko wa umeme aliiambia tume kwamba kila wakati alipojibu kwamba hajui wala hakumbuki jambo Fulani, walimpiga shoti za umeme na hajui hali hiyo ilidumu kwa muda gani kwani kwake aliona ni kama milele.  Katika eneo la Kherson, askari wa Urusi waliwabaka na kufanya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake wa umri wa kuanzia miaka 19 hadi 83, Tume iligundua. Mara kwa mara, wanafamilia waliwekwa katika chumba cha karibu na hivyo kulazimika kusikia ukiukaji unaofanyika.Tume imeendelea kuchunguza hali za kibinafsi za uhamisho wa madai ya kuhamishwa  watoto wa Ukraine bila usimamizi wowote na kuwapeleka Urusi. Tume pia ina wasiwasi kuhusu madai ya mauaji ya kimbari nchini Ukraine. Kwa mfano, baadhi ya matamshi yanayosambazwa katika Urusi na vyombo vingine vya habari yanaweza kujumuisha uchochezi wa mauaji ya kimbari. Tume inaendelea na uchunguzi wake kuhusu masuala hayo.Tume inasisitiza wasiwasi wake mkubwa juu ya ukubwa na uzito wa ukiukaji ambao umefanywa nchini Ukraine na vikosi vya kijeshi vya Urusi na inasisitiza haja ya uwajibikaji. Pia inakumbuka hitaji la mamlaka ya Ukraine kuchunguza kwa haraka na kwa kina visa vichache vya ukiukaji wa sheria uliofanywa na vikosi vyao wenyewe. Taarifa hii mpya ya Tume kwa Baraza la Haki za Kibinadamu ni mwendelezo wa ripoti zake za awali, ikijumuisha Waraka wake wenye matokeo ya uchunguzi wa kina, iliyotolewa tarehe 29 Agosti 2023.Tangu kuanzishwa kwake, Tume imesafiri zaidi ya mara kumi Kwenda Ukraine. Wakati wa uchunguzi wake, wanachama na wachunguzi wake walikutana na mamlaka za serikali, mashirika ya kimataifa, mashirika ya kiraia, na wadau wengine husika.Tume Huru ya Kimataifa ya Uchunguzi ya Umoja wa Mataifa kuhusu Ukraine ni chombo huru kilichopewa mamlaka na Baraza la Haki za Kibinadamu la Umoja wa Mataifa, pamoja na mambo mengine, kuchunguza ukiukwaji wote wa haki za binadamu na ukiukwaji wa sheria za kimataifa za kibinadamu, na uhalifu unaohusiana nao katika muktadha wa uchokozi dhidi ya Ukraine unaofanywa na Shirikisho la Urusi. Tume itawasilisha ripoti za shughuli zake kwa Baraza Kuu mwezi Oktoba mwaka huu 2023, na kwa Baraza la Haki za Kibinadamu la Umoja wa Mataifa mnamo Machi mwaka kesho 2024. 
9/25/20230
Episode Artwork

Vitendo vya kikatili vya Urusi nchini Ukraine vinasikitisha - Tume ya UN

Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchunguzi kuhusu Ukraine imeripoti leo kwa Baraza la Haki za Kibinadamu kwamba kuna ushahidi kuwa wanajeshi wa Urusi wanaendelea wanafanya uhalifu wa kivita nchini Ukraine.Katika taarifa yao waliyoiwasilisha leo katika ofisi za Umoja wa Mataifa jijini Geneva, Uswisi, Tume hiyo ya Huru ya Kimataifa ya Umoja wa Mataifa imeeleza kinagaubaga kwamba wanajeshi wa Urusi wanafanya mashambulizi haramu ya kutumia silaha za milipuko, mateso, unyanyasaji wa kingono na kijinsia, na mashambulizi dhidi ya miundombinu ya nishati.Wakati wa uwasilishaji kwa Baraza la Haki za Kibinadamu, Tume imeripoti kwamba imerekodi mashambulizi ya silaha za milipuko kwenye majengo ya makazi, kituo cha matibabu kinachofanya kazi, kituo cha reli, mgahawa, maduka na maghala ya biashara. Mashambulizi haya yalisababisha vifo vya raia, uharibifu wa miundombinu muhimu, na kukatizwa kwa huduma muhimu.Taarifa iliyosambazwa kwa vyombo vya Habari imeeleza kuwa Tume inachunguza sababu ya uvunjaji wa bwawa la Nova Kakhovka na athari zake kwa raia.Wakati huo huo Tume imeeleza kuwa uchunguzi wake huko Kherson na Zaporizhzhia unaonesha matumizi makubwa na yaliyoratibiwa ya utesaji yanayotekelezwa na vikosi vya jeshi la Urusi dhidi ya watu wanaoshutumiwa kuwa watoa habari wa vikosi vya jeshi la Ukraine. Katika matukio fulani, mateso yalifanywa kwa ukatili kiasi kwamba yalisababisha kifo.Mtu mmoja ambaye  aliteswa kwa kupigwa na mshtuko wa umeme aliiambia tume kwamba kila wakati alipojibu kwamba hajui wala hakumbuki jambo Fulani, walimpiga shoti za umeme na hajui hali hiyo ilidumu kwa muda gani kwani kwake aliona ni kama milele.  Katika eneo la Kherson, askari wa Urusi waliwabaka na kufanya ukatili wa kijinsia dhidi ya wanawake wa umri wa kuanzia miaka 19 hadi 83, Tume iligundua. Mara kwa mara, wanafamilia waliwekwa katika chumba cha karibu na hivyo kulazimika kusikia ukiukaji unaofanyika.Tume imeendelea kuchunguza hali za kibinafsi za uhamisho wa madai ya kuhamishwa  watoto wa Ukraine bila usimamizi wowote na kuwapeleka Urusi. Tume pia ina wasiwasi kuhusu madai ya mauaji ya kimbari nchini Ukraine. Kwa mfano, baadhi ya matamshi yanayosambazwa katika Urusi na vyombo vingine vya habari yanaweza kujumuisha uchochezi wa mauaji ya kimbari. Tume inaendelea na uchunguzi wake kuhusu masuala hayo.Tume inasisitiza wasiwasi wake mkubwa juu ya ukubwa na uzito wa ukiukaji ambao umefanywa nchini Ukraine na vikosi vya kijeshi vya Urusi na inasisitiza haja ya uwajibikaji. Pia inakumbuka hitaji la mamlaka ya Ukraine kuchunguza kwa haraka na kwa kina visa vichache vya ukiukaji wa sheria uliofanywa na vikosi vyao wenyewe. Taarifa hii mpya ya Tume kwa Baraza la Haki za Kibinadamu ni mwendelezo wa ripoti zake za awali, ikijumuisha Waraka wake wenye matokeo ya uchunguzi wa kina, iliyotolewa tarehe 29 Agosti 2023.Tangu kuanzishwa kwake, Tume imesafiri zaidi ya mara kumi Kwenda Ukraine. Wakati wa uchunguzi wake, wanachama na wachunguzi wake walikutana na mamlaka za serikali, mashirika ya kimataifa, mashirika ya kiraia, na wadau wengine husika.Tume Huru ya Kimataifa ya Uchunguzi ya Umoja wa Mataifa kuhusu Ukraine ni chombo huru kilichopewa mamlaka na Baraza la Haki za Kibinadamu la Umoja wa Mataifa, pamoja na mambo mengine, kuchunguza ukiukwaji wote wa haki za binadamu na ukiukwaji wa sheria za kimataifa za kibinadamu, na uhalifu unaohusiana nao katika muktadha wa uchokozi dhidi ya Ukraine unaofanywa na Shirikisho la Urusi. Tume itawasilisha ripoti za shughuli zake kwa Baraza Kuu mwezi Oktoba mwaka huu 2023, na kwa Baraza la Haki za Kibinadamu la Umoja wa Mataifa mnamo Machi mwaka kesho 2024. 
9/25/20230
Episode Artwork

25 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko nchini Ukraine na mkutano wa kimataifa huko Rome kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa wanyama. Makala tunasalia hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa na mashinani tunakupeleka nchini Poland, kulikoni?Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchunguzi kuhusu Ukraine imeripoti leo kwa Baraza la Haki za Kibinadamu kwamba kuna ushahidi unaoendelea kuwa wanajeshi wa Urusi wanafanya uhalifu wa kivita nchini Ukraine.Mkutano wa kwanza kabisa wa kimataifa kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa Wanyama umeanza hii leo kwenye makao makuu ya shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO lengo likiwa ni kusaka mbinu za kuwezesha ufugaji huo uwe na mnepo zaidi, usiharibu mazingira na uchangie katika maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii, halikadhalika sayari yenye afya.Katika makala Waziri wa Afya wa Tanzania Ummy Mwalimu aliketi chini na Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili kuzungumzia mikakati ya nchi hiyo katika kulitekeleza azimio la Umoja wa Mataifa la kuchukua hatua kuhusu huduma za afya kwa wote ifikapo mwaka 2030.Mashinani tunakupeleka nchini Poland kusikia jinsi ambavyo wakimbizi wa Ukraine walivyoshindwa kuendelea na matibabu ya kifua kikuu baada ya kulazimika kukimbia makwao.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
9/25/20230
Episode Artwork

25 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia machafuko nchini Ukraine na mkutano wa kimataifa huko Rome kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa wanyama. Makala tunasalia hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa na mashinani tunakupeleka nchini Poland, kulikoni?Tume ya Umoja wa Mataifa ya Uchunguzi kuhusu Ukraine imeripoti leo kwa Baraza la Haki za Kibinadamu kwamba kuna ushahidi unaoendelea kuwa wanajeshi wa Urusi wanafanya uhalifu wa kivita nchini Ukraine.Mkutano wa kwanza kabisa wa kimataifa kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa Wanyama umeanza hii leo kwenye makao makuu ya shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO lengo likiwa ni kusaka mbinu za kuwezesha ufugaji huo uwe na mnepo zaidi, usiharibu mazingira na uchangie katika maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii, halikadhalika sayari yenye afya.Katika makala Waziri wa Afya wa Tanzania Ummy Mwalimu aliketi chini na Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili kuzungumzia mikakati ya nchi hiyo katika kulitekeleza azimio la Umoja wa Mataifa la kuchukua hatua kuhusu huduma za afya kwa wote ifikapo mwaka 2030.Mashinani tunakupeleka nchini Poland kusikia jinsi ambavyo wakimbizi wa Ukraine walivyoshindwa kuendelea na matibabu ya kifua kikuu baada ya kulazimika kukimbia makwao.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
9/25/20230
Episode Artwork

FAO: Ufugaji endelevu unaonufaisha jamii bila kuharibu mazingira wamulikwa huko Roma, Italia

Mkutano wa kwanza kabisa wa kimataifa kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa Wanyama umeanza hii leo kwenye makao makuu ya shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO lengo likiwa ni kusaka mbinu za kuwezesha ufugaji huo uwe na mnepo zaidi, usiharibu mazingira na uchangie katika maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii, halikadhalika sayari yenye afya. Mkutano huo wa siku tatu unaleta pamoja wawakilishi wanachama wa FAO, mashirika yanayohusika n uzalishaji wa mazao yatokanayo na mifugo, watafiti, wanazuoni, mashirika ya maendeleo, mashirika ya kiraia na sekta binafsi ambapo watapata fursa kujadili mbinu bunifu na za ugunduzi ili hatimye sekta ya mifugo iweze kuzalisha mazao yenye lishe bora zaidi, gharama nafuu huku ikichangia kidogo katika uchafuzi wa mazingira. Thanawat Tiensin, Mkurugenzi wa Kitengo cha FAO kinachohusika na Uzalishaji wa Mifugo na Afya anafafanua maana ya ufugaji endelevu wa Wanyama. "Ufugaji endelevu unahusisha mwenendo unaolenga kukidhi mahitaji ya kufuga wanyama kwa ajili ya chakula huku ukipunguza uharibifu wa mazingira. Ufugaji endelevu unasongesha uwepo wa mifumo ya kilimo cha mazao ya chakula, hulinda maliasili, huboresha mnepo wa kiuchumi na huchangia kwenye mustakabali endelevu na wenye mnepo zaidi.” Wakati huu ambapo mahitaji ya mazao yatokanayo na mifugo duniani yakitarajiwa kuongezeka kwa asilimia 20 ifikapo mwaka 2050, nyama, mayai na bidhaa za maziwa zitakuwa dhima muhimu katika kuhakikisha uhakika wa upatikanaji wa chakula na mlo wenye afya na endelevu. Bwana Tiensin anaelezea zaidi jukumu la mkutano. "Ili kuzalisha mifugo huku unapunguza madhara, kwanza lazima tujitike katika mifumo fanisi ya ufugaji. Hii inajumuisha kubadili na kutumia vema chakula cha mifugo, kupunguza utupaji wa chakula hicho, matumizi mazuri ya virutubisho, kupunguza umomonyoaji wa udongo na vyanzo vya maji, kupunguza utoaji wa hewa chafuzi na kupunguza uharibifu wa mazingira. Halikadhalika, kupatia kipaumbele mifumo ya kilimo na ufugaji wa kisasa unaokidhi tabianchi.” Na zaidi ya yote, "Mkutano huu wa kimataifa utatoa fursa ya kuangazia tafiti na ujumbe muhimu, na kuchangia katika mazungumzo ya dunia kuhusu ufugaji endelevu na nafasi yake katika kuhimili na kukabili mabadiliko ya tabianchi. Kwa ujumla mkutano huu una dhima muhimu katika kusongesha ajenda ya ufugaji endelevu na kuendeleza mbinu zote ambazo zinashughulikia masuala ya kimazingira, kijamii na kiuchumi ya mifumo ya ufugaji.” Mambo yanayomulikwa ni pamoja na chakula na afya ya mifugo, lishe ya binadamu, matumizi ya teknolojia, na nafasi ya mifugo katika kuwezesha wafugaji wadogo kuendesha maisha yao na pia uhusiano kati ya ufugaji na uendelevu wa mazingira, uchumi na jamii. 
9/25/20230
Episode Artwork

FAO: Ufugaji endelevu unaonufaisha jamii bila kuharibu mazingira wamulikwa huko Roma, Italia

Mkutano wa kwanza kabisa wa kimataifa kuhusu marekebisho ya mfumo wa ufugaji wa Wanyama umeanza hii leo kwenye makao makuu ya shirika la Umoja wa Mataifa la chakula na kilimo, FAO lengo likiwa ni kusaka mbinu za kuwezesha ufugaji huo uwe na mnepo zaidi, usiharibu mazingira na uchangie katika maendeleo endelevu ya kiuchumi na kijamii, halikadhalika sayari yenye afya. Mkutano huo wa siku tatu unaleta pamoja wawakilishi wanachama wa FAO, mashirika yanayohusika n uzalishaji wa mazao yatokanayo na mifugo, watafiti, wanazuoni, mashirika ya maendeleo, mashirika ya kiraia na sekta binafsi ambapo watapata fursa kujadili mbinu bunifu na za ugunduzi ili hatimye sekta ya mifugo iweze kuzalisha mazao yenye lishe bora zaidi, gharama nafuu huku ikichangia kidogo katika uchafuzi wa mazingira. Thanawat Tiensin, Mkurugenzi wa Kitengo cha FAO kinachohusika na Uzalishaji wa Mifugo na Afya anafafanua maana ya ufugaji endelevu wa Wanyama. "Ufugaji endelevu unahusisha mwenendo unaolenga kukidhi mahitaji ya kufuga wanyama kwa ajili ya chakula huku ukipunguza uharibifu wa mazingira. Ufugaji endelevu unasongesha uwepo wa mifumo ya kilimo cha mazao ya chakula, hulinda maliasili, huboresha mnepo wa kiuchumi na huchangia kwenye mustakabali endelevu na wenye mnepo zaidi.” Wakati huu ambapo mahitaji ya mazao yatokanayo na mifugo duniani yakitarajiwa kuongezeka kwa asilimia 20 ifikapo mwaka 2050, nyama, mayai na bidhaa za maziwa zitakuwa dhima muhimu katika kuhakikisha uhakika wa upatikanaji wa chakula na mlo wenye afya na endelevu. Bwana Tiensin anaelezea zaidi jukumu la mkutano. "Ili kuzalisha mifugo huku unapunguza madhara, kwanza lazima tujitike katika mifumo fanisi ya ufugaji. Hii inajumuisha kubadili na kutumia vema chakula cha mifugo, kupunguza utupaji wa chakula hicho, matumizi mazuri ya virutubisho, kupunguza umomonyoaji wa udongo na vyanzo vya maji, kupunguza utoaji wa hewa chafuzi na kupunguza uharibifu wa mazingira. Halikadhalika, kupatia kipaumbele mifumo ya kilimo na ufugaji wa kisasa unaokidhi tabianchi.” Na zaidi ya yote, "Mkutano huu wa kimataifa utatoa fursa ya kuangazia tafiti na ujumbe muhimu, na kuchangia katika mazungumzo ya dunia kuhusu ufugaji endelevu na nafasi yake katika kuhimili na kukabili mabadiliko ya tabianchi. Kwa ujumla mkutano huu una dhima muhimu katika kusongesha ajenda ya ufugaji endelevu na kuendeleza mbinu zote ambazo zinashughulikia masuala ya kimazingira, kijamii na kiuchumi ya mifumo ya ufugaji.” Mambo yanayomulikwa ni pamoja na chakula na afya ya mifugo, lishe ya binadamu, matumizi ya teknolojia, na nafasi ya mifugo katika kuwezesha wafugaji wadogo kuendesha maisha yao na pia uhusiano kati ya ufugaji na uendelevu wa mazingira, uchumi na jamii. 
9/25/20230
Episode Artwork

Msukumo dhidi ya TB ufanane na ule wa COVID-19- Waziri Wafula

Mkutano wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mapambano dhidi ya Kifua Kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo dunia itashikamana na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19. Waziri Wafula alizungumza na Flora Nducha wa Idhaa  hii ya Umoja wa Mataifa.
9/22/20230
Episode Artwork

Msukumo dhidi ya TB ufanane na ule wa COVID-19- Waziri Wafula

Mkutano wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mapambano dhidi ya Kifua Kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo dunia itashikamana na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19. Waziri Wafula alizungumza na Flora Nducha wa Idhaa  hii ya Umoja wa Mataifa.
9/22/20230
Episode Artwork

Kliniki tembezi nchini Tanzania yasaidia kudhibiti ugonjwa wa Kifua Kikuu

Hii leo hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York Marekani, wakuu wa nchi na serikali wamekutana katika mkutano wa pili wa ngazi za juu wa Umoja wa Mataifa  kutathmini mwelekeo wa Kifua Kikuu au TB kufuatia azimio la kisiasa la mwaka 2018 ambalo pamoja na mambo mengine linalenga kutokomeza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.  Mkutano huo ni muhimu katika kukabiliana na vikwazo ikiwemo hatua za dharura za kutengeneza na kusambaza aina mpya ya chanjo dhidi ya Kifua Kikuu, huku ikibebwa na maudhui ya “kusongesha sayansi, ufadhili na ugunduzi na faida zake, kumaliza haraka kifua kikuu duniani kwa kuhakikisha kupata kwa usawa huduma za kinga, tiba na malezi.” Licha ya changamoto ya kudhibiti ugonjwa huo, tayari matunda yanaonekana ikiwemo huko Kanda ya Ziwa nchini Tanzania ambako kliniki tembezi zinafikia wagonjwa kule waliko.  Evarist Mapesa wa Idhaa hii amezungumza na Dokta Abdallah Keresa kutoka kitengo cha Kliniki ya Kifua Kikuu na Virusi vya Ukimwi (VVU) Hospitali ya Rufaa ya Bugando mkoani Mwanza nchini Tanzania ambapo pamoja na kueleza mafanikio ya kudhibiti TB, anaanza kwa kueleza umhimu wa mkutano huu.  
9/22/20230
Episode Artwork

Kliniki tembezi nchini Tanzania yasaidia kudhibiti ugonjwa wa Kifua Kikuu

Hii leo hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York Marekani, wakuu wa nchi na serikali wamekutana katika mkutano wa pili wa ngazi za juu wa Umoja wa Mataifa  kutathmini mwelekeo wa Kifua Kikuu au TB kufuatia azimio la kisiasa la mwaka 2018 ambalo pamoja na mambo mengine linalenga kutokomeza ugonjwa huo ifikapo mwaka 2030.  Mkutano huo ni muhimu katika kukabiliana na vikwazo ikiwemo hatua za dharura za kutengeneza na kusambaza aina mpya ya chanjo dhidi ya Kifua Kikuu, huku ikibebwa na maudhui ya “kusongesha sayansi, ufadhili na ugunduzi na faida zake, kumaliza haraka kifua kikuu duniani kwa kuhakikisha kupata kwa usawa huduma za kinga, tiba na malezi.” Licha ya changamoto ya kudhibiti ugonjwa huo, tayari matunda yanaonekana ikiwemo huko Kanda ya Ziwa nchini Tanzania ambako kliniki tembezi zinafikia wagonjwa kule waliko.  Evarist Mapesa wa Idhaa hii amezungumza na Dokta Abdallah Keresa kutoka kitengo cha Kliniki ya Kifua Kikuu na Virusi vya Ukimwi (VVU) Hospitali ya Rufaa ya Bugando mkoani Mwanza nchini Tanzania ambapo pamoja na kueleza mafanikio ya kudhibiti TB, anaanza kwa kueleza umhimu wa mkutano huu.  
9/22/20230
Episode Artwork

22 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazi ugonjwa wa kifua kikuu na haki za wanawake nchini Iran. Makala na mashinani tunasalia hapa hapa makao makuu wa Umoja wa Mataifa, kulikoni?Mkutano wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mapambano dhidi ya Kifua Kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo dunia itashikamana na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19.Hatua ya Bunge la Iran kupitisha mswada mpya utakaowabana zaidi wanawake kuhusu uhuru wa miili yao na pia uvaaji wao hususani vazi la Hijab imepokelewa kwa masikitiko makubwa  na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu, OHCHR.Katika makala hii leo hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa kunafanyika mkutano wa pili wa ngazi ya juu kutathmini azimio la kisiasa la mwaka 2018 kuhusu kutokomeza ugonjwa wa Kifua Kikuu ifikapo mwaka 2030. Evarist Mapesa wa Idhaa hii amezungumza na Dokta Abdallah Keresa kutoka kitengo cha Kliniki ya Kifua Kikuu na Virusi vya Ukimwi (VVU) Hospitali ya Rufaa ya Bugando mkoani Mwanza nchini Tanzania ambapo pamoja na kueleza mafanikio ya kudhibiti TB, anaanza kwa kueleza umhimu wa mkutano huu.Mashinani tutasalia hapa Makao Makuu kupata ujumbe wa Rais wa Guinea kwa viongozi wa Dunia.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/22/20230
Episode Artwork

22 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazi ugonjwa wa kifua kikuu na haki za wanawake nchini Iran. Makala na mashinani tunasalia hapa hapa makao makuu wa Umoja wa Mataifa, kulikoni?Mkutano wa ngazi ya juu wa Umoja wa Mataifa kuhusu mapambano dhidi ya Kifua Kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo dunia itashikamana na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19.Hatua ya Bunge la Iran kupitisha mswada mpya utakaowabana zaidi wanawake kuhusu uhuru wa miili yao na pia uvaaji wao hususani vazi la Hijab imepokelewa kwa masikitiko makubwa  na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu, OHCHR.Katika makala hii leo hapa makao makuu ya Umoja wa Mataifa kunafanyika mkutano wa pili wa ngazi ya juu kutathmini azimio la kisiasa la mwaka 2018 kuhusu kutokomeza ugonjwa wa Kifua Kikuu ifikapo mwaka 2030. Evarist Mapesa wa Idhaa hii amezungumza na Dokta Abdallah Keresa kutoka kitengo cha Kliniki ya Kifua Kikuu na Virusi vya Ukimwi (VVU) Hospitali ya Rufaa ya Bugando mkoani Mwanza nchini Tanzania ambapo pamoja na kueleza mafanikio ya kudhibiti TB, anaanza kwa kueleza umhimu wa mkutano huu.Mashinani tutasalia hapa Makao Makuu kupata ujumbe wa Rais wa Guinea kwa viongozi wa Dunia.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/22/20230
Episode Artwork

OHCHR: Mswada Hijabu na ‘usafi’ kwa wanawake wa Iran unasikitisha

Hatua ya Bunge la Iran kupitisha mswada mpya utakaowabana zaidi wanawake kuhusu uhuru wa miili yao na pia uvaaji wao hususani vazi la Hijab imepokelewa kwa masikitiko makubwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu, OHCHR. Tunasikitika sana Bunge la Iran kupitisha Mswada mpya wa Usafi na Hijabu ambao unaongeza kwa kiasi kikubwa vifungo vya jela na faini ya kuwakandamiza wanawake na wasichana ambao hawatatii kanuni za lazima za uvaaji, imesema Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu kupitia kwa Msemaji wake Ravina Shamdasani alipozunguza na waandishi wa Habari jijini Geneva, Uswisi.  Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu, Volker Türk, ametuma ujumbe kwamba mswada huu wa kikatili unaopeperushwa waziwazi mbele ya uso wa sheria za kimataifa lazima usitishwe. Wale wanaopuuza kanuni kali ya mavazi ya Kiislamu ya kufunika kichwa na mavazi yanayoitwa ya heshima wako hatarini kukumbwa na kifungo cha hadi miaka 10 jela, kuchapwa viboko pamoja na kutozwa faini ya hadi rial za Iran milioni 360 sawa na takribani dola za kimarekani 8,522.  Kwa hatua mswada huu ulipofikia, kinachosubiriwa ni kupitishwa na Baraza la Uongozi linaloundwa na wazee 12 walioidhinishwa kikatiba ambao wana nguvu na ushawishi mkubwa katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Chini ya sheria ya awali, kosa kama hilo lilibeba kifungo cha hadi miezi miwili jela, au faini ya hadi rial 500,000 za Iran sawa na takribani dola 11.84 za kimarekani. 
9/22/20230
Episode Artwork

OHCHR: Mswada Hijabu na ‘usafi’ kwa wanawake wa Iran unasikitisha

Hatua ya Bunge la Iran kupitisha mswada mpya utakaowabana zaidi wanawake kuhusu uhuru wa miili yao na pia uvaaji wao hususani vazi la Hijab imepokelewa kwa masikitiko makubwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya haki za binadamu, OHCHR. Tunasikitika sana Bunge la Iran kupitisha Mswada mpya wa Usafi na Hijabu ambao unaongeza kwa kiasi kikubwa vifungo vya jela na faini ya kuwakandamiza wanawake na wasichana ambao hawatatii kanuni za lazima za uvaaji, imesema Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu kupitia kwa Msemaji wake Ravina Shamdasani alipozunguza na waandishi wa Habari jijini Geneva, Uswisi.  Kamishna Mkuu wa Haki za Kibinadamu, Volker Türk, ametuma ujumbe kwamba mswada huu wa kikatili unaopeperushwa waziwazi mbele ya uso wa sheria za kimataifa lazima usitishwe. Wale wanaopuuza kanuni kali ya mavazi ya Kiislamu ya kufunika kichwa na mavazi yanayoitwa ya heshima wako hatarini kukumbwa na kifungo cha hadi miaka 10 jela, kuchapwa viboko pamoja na kutozwa faini ya hadi rial za Iran milioni 360 sawa na takribani dola za kimarekani 8,522.  Kwa hatua mswada huu ulipofikia, kinachosubiriwa ni kupitishwa na Baraza la Uongozi linaloundwa na wazee 12 walioidhinishwa kikatiba ambao wana nguvu na ushawishi mkubwa katika Jamhuri ya Kiislamu ya Iran. Chini ya sheria ya awali, kosa kama hilo lilibeba kifungo cha hadi miezi miwili jela, au faini ya hadi rial 500,000 za Iran sawa na takribani dola 11.84 za kimarekani. 
9/22/20230
Episode Artwork

Waziri wa Afya Kenya atoa wito kwa wadau kutengeneza chanjo ya TB

Mkutano wa ngazi ya juu kuhusu mapambano dhidi ya kifua kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo Dunia itashikama na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19.Akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa Waziri Wafula amesema “Najiuliza, mbona sisi watu wote, kwanza wafadhili na wale wazalishaji wa hizo dawa na vifaa, mbona tusifikirie lile jambo moja ambalo tunastahili kufanya ili kumaliza ugonjwa wa TB?” Akifafanua zaidi Waziri huyo amesema jambo la muhimu ni kupata kinga ili watu wasipata ugonjwa wa TB kwakuwa kwa kiasi kikubwa wanaoambukizwa ni watu walio katika maeneo duni. “Kulikuwa na COVID-19, muda mfupi tu kumekuwa na chanjo na sasa watu tunatembea kwa uhuru kabisa na watu wanatangamana, pale mwanzo COVID-19 ilikuwa imefanya watu hawatembeleani. Ninauhakika kwamba tukiweka fedha kwenye sayansi, kufanya utafiti na maendeleo tutapata chanjo ya hii TB ama pia tupate tiba ya mara moja.”Waziri huyo wa Afya kutoka nchini Kenya amesema pamoja na taifa hilo kutibu ugonjwa wa TB bure kwa wananchi wake lakini changamoto wanayokutana nayo ni uhaba wa vifaa tiba katika baadhi ya hospitali na kutoa wito kwa wafanyabiashara kupunguza bei za vifaa tiba hivyo ili waweze kusambaza katika hospital zote nchini Kenya.  Kuhusu namna watakavyotekeleza Azimio la kisiasa kuhusu Afya kwa wote nchini Kenya ambayo wanaiita “Afya Mashinani” Waziri Wafula amesema Kenya imejipanga kutekeleza katika vipengele vifuu vinne ambavyo ni: kuhakikisha kuna dawa na vifaa tiba, kuhakikisha kuna watoa huduma katika vituo vya afya, matumizi ya teknolojia kufikisha afya mashinani na ufadhili wa afya kupitia bima ya afya ya taifa.
9/22/20230
Episode Artwork

Waziri wa Afya Kenya atoa wito kwa wadau kutengeneza chanjo ya TB

Mkutano wa ngazi ya juu kuhusu mapambano dhidi ya kifua kikuu au TB ukifanyika leo hapa katika Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani, Waziri wa Afya wa Kenya Susan Nakhumicha Wafula amesema kutokomeza TB ifikapo mwaka 2030 inawezekana endapo Dunia itashikama na kuweka msokumo mkubwa kwa ugonjwa huo kama ilivyofanya wakati wa mlipuko wa janga la COVID-19.Akihojiwa na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa Waziri Wafula amesema “Najiuliza, mbona sisi watu wote, kwanza wafadhili na wale wazalishaji wa hizo dawa na vifaa, mbona tusifikirie lile jambo moja ambalo tunastahili kufanya ili kumaliza ugonjwa wa TB?” Akifafanua zaidi Waziri huyo amesema jambo la muhimu ni kupata kinga ili watu wasipata ugonjwa wa TB kwakuwa kwa kiasi kikubwa wanaoambukizwa ni watu walio katika maeneo duni. “Kulikuwa na COVID-19, muda mfupi tu kumekuwa na chanjo na sasa watu tunatembea kwa uhuru kabisa na watu wanatangamana, pale mwanzo COVID-19 ilikuwa imefanya watu hawatembeleani. Ninauhakika kwamba tukiweka fedha kwenye sayansi, kufanya utafiti na maendeleo tutapata chanjo ya hii TB ama pia tupate tiba ya mara moja.”Waziri huyo wa Afya kutoka nchini Kenya amesema pamoja na taifa hilo kutibu ugonjwa wa TB bure kwa wananchi wake lakini changamoto wanayokutana nayo ni uhaba wa vifaa tiba katika baadhi ya hospitali na kutoa wito kwa wafanyabiashara kupunguza bei za vifaa tiba hivyo ili waweze kusambaza katika hospital zote nchini Kenya.  Kuhusu namna watakavyotekeleza Azimio la kisiasa kuhusu Afya kwa wote nchini Kenya ambayo wanaiita “Afya Mashinani” Waziri Wafula amesema Kenya imejipanga kutekeleza katika vipengele vifuu vinne ambavyo ni: kuhakikisha kuna dawa na vifaa tiba, kuhakikisha kuna watoa huduma katika vituo vya afya, matumizi ya teknolojia kufikisha afya mashinani na ufadhili wa afya kupitia bima ya afya ya taifa.
9/22/20230
Episode Artwork

Tunaelimisha wanafunzi na vijana kuhusu mabadiliko ya tabianchi - Madina Jubilate Kimaro

Wiki hii hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika mkutano wa tathmini ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs kuona wapi nchi wanachama, kampuni, watu binafsi wamefikia kusongesha maendeleo hayo yanayofikia ukomo mwka 2030. Vijana nao walikuwa na siku zao mbili za kuelezea wanafanya nini kule waliko na wanataka nini kifanyike kusongesha malengo hayo likiwemo namba 13 la tabianchi. Miongoni mwa vijana walioshiriki ni Madina Jubilate Kimaro, Balozi wa Mazingira wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto duniani, UNICEF nchini Tanzania. Flora Nducha wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alizungumza naye kufahamu masuala kadhaa ikiwemo nini anafanya kuhakikisha mazingira yanasalia salama.
9/21/20230
Episode Artwork

Tunaelimisha wanafunzi na vijana kuhusu mabadiliko ya tabianchi - Madina Jubilate Kimaro

Wiki hii hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika mkutano wa tathmini ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs kuona wapi nchi wanachama, kampuni, watu binafsi wamefikia kusongesha maendeleo hayo yanayofikia ukomo mwka 2030. Vijana nao walikuwa na siku zao mbili za kuelezea wanafanya nini kule waliko na wanataka nini kifanyike kusongesha malengo hayo likiwemo namba 13 la tabianchi. Miongoni mwa vijana walioshiriki ni Madina Jubilate Kimaro, Balozi wa Mazingira wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto duniani, UNICEF nchini Tanzania. Flora Nducha wa Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa alizungumza naye kufahamu masuala kadhaa ikiwemo nini anafanya kuhakikisha mazingira yanasalia salama.
9/21/20230
Episode Artwork

Methali: "Mshale mzuri haukai ziakani"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mshale mzuri haukai ziakani.”
9/21/20230
Episode Artwork

Methali: "Mshale mzuri haukai ziakani"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mshale mzuri haukai ziakani.”
9/21/20230
Episode Artwork

21 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo wiki hii hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika mkutano wa tathmini ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs kuona wapi nchi wanachama, kampuni, watu binafsi wamefikia kusongesha maendeleo hayo yanayofikia ukomo mwka 2030. Vijana nao walikuwa na siku zao mbili za kuelezea wanafanya nini kule waliko na wanataka nini kifanyike kusongesha malengo hayo likiwemo namba 13 la tabianchi. Miongoni mwa vijana walioshiriki ni Madina Jubilate Kimaro, Balozi wa Mazingira wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto duniani, UNICEF nchini Tanzania. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiangazia Afya, amani na yanayoendelea katika UNGA78. Katika kujifinza lugha ya Kiswahili Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mshale mzuri haukai ziakani.”. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/21/20230
Episode Artwork

21 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo wiki hii hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa kumefanyika mkutano wa tathmini ya malengo ya maendeleo endelevu SDGs kuona wapi nchi wanachama, kampuni, watu binafsi wamefikia kusongesha maendeleo hayo yanayofikia ukomo mwka 2030. Vijana nao walikuwa na siku zao mbili za kuelezea wanafanya nini kule waliko na wanataka nini kifanyike kusongesha malengo hayo likiwemo namba 13 la tabianchi. Miongoni mwa vijana walioshiriki ni Madina Jubilate Kimaro, Balozi wa Mazingira wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto duniani, UNICEF nchini Tanzania. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiangazia Afya, amani na yanayoendelea katika UNGA78. Katika kujifinza lugha ya Kiswahili Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Mshale mzuri haukai ziakani.”. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/21/20230
Episode Artwork

Guterres: Tumieni vizuri Mjadala wa ngazi ya juu wa Baraza Kuu kuhusu ufadhili wa maendeleo

Viongozi wa ulimengu wanaohudhuria Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wamefanya Mjadala wa Ngazi ya Juu kujadili ufadhili kwa ajili ya maendeleo ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amewasihi kuitumia fursa ya majadiliano haya ili kufanya marekebisho katika mfumo wa ufadhili duniani. Evarist Mapesa na taarifa zaidi.“Waheshimiwa, Mabibi na mabwana…Katika masuala yote tutakayojadili wiki hii, ufadhili unaweza kuwa muhimu zaidi.” Ndivyo alivyoanza hotuba yake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres mbele ya viongozi wa ulimwengu kwa lengo la kutafuta suluhisho la ufadhili wa maendeleo unaosuasua duniani. Akitumia mfano wa nishati isukumavyo mitambo, Guterres amesema kwa sababu ufadhili wa maendeleo ndio nishati inayosukuma maendeleo kwenye Ajenda ya mwaka 2030 na Mkataba wa Paris. Leo, nishati hiyo inaisha na injini ya maendeleo endelevu inadumaa, inakwama, na inarudi nyuma.Bwana Guterres ameweka wazi kuwa kuna mgawanyiko mkubwa na unaokua kati ya nchi ambazo zinaweza kupata ufadhili kwa masharti yanayokubalika na zile ambazo haziwezi na zinaachwa nyuma zaidi akitoa mfano mchungu kwamba nchini zinazoendelea zinakabiliwa na gharama za kukopa hadi mara nane zaidi ya nchi zilizoendelea – kitu ambacho amekiita mtego wa madeni na hapo akatoa wito,“Ninakuombeni mtumie mjadala huu wa ngazi ya juu kama jukwaa la ushirikiano wenye kujenga, kwa kuzingatia suluhisho za ufadhili za kiubunifu na vitendo ambazo zinaweza kuendelezwa katika miezi na miaka ijayo.”
9/20/20230
Episode Artwork

Guterres: Tumieni vizuri Mjadala wa ngazi ya juu wa Baraza Kuu kuhusu ufadhili wa maendeleo

Viongozi wa ulimengu wanaohudhuria Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wamefanya Mjadala wa Ngazi ya Juu kujadili ufadhili kwa ajili ya maendeleo ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa amewasihi kuitumia fursa ya majadiliano haya ili kufanya marekebisho katika mfumo wa ufadhili duniani. Evarist Mapesa na taarifa zaidi.“Waheshimiwa, Mabibi na mabwana…Katika masuala yote tutakayojadili wiki hii, ufadhili unaweza kuwa muhimu zaidi.” Ndivyo alivyoanza hotuba yake Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres mbele ya viongozi wa ulimwengu kwa lengo la kutafuta suluhisho la ufadhili wa maendeleo unaosuasua duniani. Akitumia mfano wa nishati isukumavyo mitambo, Guterres amesema kwa sababu ufadhili wa maendeleo ndio nishati inayosukuma maendeleo kwenye Ajenda ya mwaka 2030 na Mkataba wa Paris. Leo, nishati hiyo inaisha na injini ya maendeleo endelevu inadumaa, inakwama, na inarudi nyuma.Bwana Guterres ameweka wazi kuwa kuna mgawanyiko mkubwa na unaokua kati ya nchi ambazo zinaweza kupata ufadhili kwa masharti yanayokubalika na zile ambazo haziwezi na zinaachwa nyuma zaidi akitoa mfano mchungu kwamba nchini zinazoendelea zinakabiliwa na gharama za kukopa hadi mara nane zaidi ya nchi zilizoendelea – kitu ambacho amekiita mtego wa madeni na hapo akatoa wito,“Ninakuombeni mtumie mjadala huu wa ngazi ya juu kama jukwaa la ushirikiano wenye kujenga, kwa kuzingatia suluhisho za ufadhili za kiubunifu na vitendo ambazo zinaweza kuendelezwa katika miezi na miaka ijayo.”
9/20/20230
Episode Artwork

20 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea maoni kuhusu matumizi ya lugha ya kiswahili kutokwa kwa viongozi wanaoshiriki UNGA78, na yaliyojiri hapa makao makuu katika mjadala kuhusu malengo ya maendeleo endelevu. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani tunasalia hapa makao makuu, kulikoni?  Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt. Peter Mathuki ambaye yuko hapa New York, Marekani kushiriki vikao vya ngazi ya juu vya Umoja wa Mataifa amesema ili kuongeza ushawishi na kukuza lugha ya Kiswahili duniani ambayo sasa inatambulika kimataifa, ni vyema viongozi wa jumuiya hiyo wakawa mfano kwa kuhutubia kwa lugha hiyo mathalani kwenye mjadala mkuu wa Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.Viongozi wa ulimwengu wanaohudhuria Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wamekuwa na Mjadala wa Ngazi ya Juu kujadili ufadhili kwa ajili ya maendeleo hususan katika kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs, ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amewasihi kuitumia fursa ya majadiliano hayo ili kurekebisha mfumo wa ufadhili duniani.   Na katika makala wakati hapa Makao Makuu hii leo kukifanyika mkutano wa ngazi ya juu kuhusu tabianchi na jinsi ya kudhibiti athari zake, wakazi wa Kibokoni kaunti ya Kilifi nchini Kenya, wamechukua hatua kwani baada ya kuathirika wamejijengea mnepo na kuendelea kujikimu kimaisha kwa kuanzisha mradi wa ufugaji wa samaki kwenye mabwawa.Mashinani inaturejesha hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mjadala wa Baraza Kuu kunafanyika mkutano kuhusu hali ya Sudan. Naibu msaidizi wa Katibu Mkuu wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Joyce Msuya anasema kwa upande wa kibinadamu hali ni tete. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/20/20230
Episode Artwork

20 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea maoni kuhusu matumizi ya lugha ya kiswahili kutokwa kwa viongozi wanaoshiriki UNGA78, na yaliyojiri hapa makao makuu katika mjadala kuhusu malengo ya maendeleo endelevu. Makala tunakupeleka nchini Kenya na mashinani tunasalia hapa makao makuu, kulikoni?  Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt. Peter Mathuki ambaye yuko hapa New York, Marekani kushiriki vikao vya ngazi ya juu vya Umoja wa Mataifa amesema ili kuongeza ushawishi na kukuza lugha ya Kiswahili duniani ambayo sasa inatambulika kimataifa, ni vyema viongozi wa jumuiya hiyo wakawa mfano kwa kuhutubia kwa lugha hiyo mathalani kwenye mjadala mkuu wa Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.Viongozi wa ulimwengu wanaohudhuria Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa wamekuwa na Mjadala wa Ngazi ya Juu kujadili ufadhili kwa ajili ya maendeleo hususan katika kufanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs, ambapo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amewasihi kuitumia fursa ya majadiliano hayo ili kurekebisha mfumo wa ufadhili duniani.   Na katika makala wakati hapa Makao Makuu hii leo kukifanyika mkutano wa ngazi ya juu kuhusu tabianchi na jinsi ya kudhibiti athari zake, wakazi wa Kibokoni kaunti ya Kilifi nchini Kenya, wamechukua hatua kwani baada ya kuathirika wamejijengea mnepo na kuendelea kujikimu kimaisha kwa kuanzisha mradi wa ufugaji wa samaki kwenye mabwawa.Mashinani inaturejesha hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mjadala wa Baraza Kuu kunafanyika mkutano kuhusu hali ya Sudan. Naibu msaidizi wa Katibu Mkuu wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Joyce Msuya anasema kwa upande wa kibinadamu hali ni tete. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/20/20230
Episode Artwork

Mradi wa ufugaji wa Samaki umenikombia mimi na familia yangu: Michael Chiwayi

Mkutano wa ngazi ya juu kuhusu mabadiliko ya tabianchi unafanyika leo kwenye makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mjadala mkuu wa Baraza Kuu , UNGA78 lengo likiwa kuzihamasisha nchi wanachana kuchukua hatua zaidi kuzinusuru nchi zinazobeba mzigo mkubwa wa athari za janga hilo. Eneo la Kibokoni kaunti ya Kilifi nchini Kenya ni moja ya maeneo ya wavuvi yaliyoathirika na mabadiliko ya tabianchi na kuwalazimu wavufi kutafuta mbinu mbadala ya kuweza kujikimu kimaisha.  Na ndipo chini ya mwamvuli wa shirika lisilo la kiserikali la Umoja Self-Help Group likiwa na wanachama 40 wakaanzisha mabwa 17 ya ufugaji wa Samaki aina ya milkfish, dagaa kamba, kaa, sandfish, rabbitfish na tilapia wa baharini. Mradi huu unaihakikisha jamii uzalishaji, kuwainua kiuchumi  na kuwajengea mnepo. Tuungane Flora Nducha na mmoja wa wanaufaika wa mradi huo katika makala hii iliyofanikishwa na kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS, Nairobi Kenya.
9/20/20230
Episode Artwork

Mradi wa ufugaji wa Samaki umenikombia mimi na familia yangu: Michael Chiwayi

Mkutano wa ngazi ya juu kuhusu mabadiliko ya tabianchi unafanyika leo kwenye makao Makuu ya Umoja wa Mataifa kandoni mwa mjadala mkuu wa Baraza Kuu , UNGA78 lengo likiwa kuzihamasisha nchi wanachana kuchukua hatua zaidi kuzinusuru nchi zinazobeba mzigo mkubwa wa athari za janga hilo. Eneo la Kibokoni kaunti ya Kilifi nchini Kenya ni moja ya maeneo ya wavuvi yaliyoathirika na mabadiliko ya tabianchi na kuwalazimu wavufi kutafuta mbinu mbadala ya kuweza kujikimu kimaisha.  Na ndipo chini ya mwamvuli wa shirika lisilo la kiserikali la Umoja Self-Help Group likiwa na wanachama 40 wakaanzisha mabwa 17 ya ufugaji wa Samaki aina ya milkfish, dagaa kamba, kaa, sandfish, rabbitfish na tilapia wa baharini. Mradi huu unaihakikisha jamii uzalishaji, kuwainua kiuchumi  na kuwajengea mnepo. Tuungane Flora Nducha na mmoja wa wanaufaika wa mradi huo katika makala hii iliyofanikishwa na kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS, Nairobi Kenya.
9/20/20230
Episode Artwork

Tuzungumze Kiswahili kwenye UNGA78 - Viongozi wa EAC

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt. Peter Mathuki amesema ili kuongeza ushawishi na kukuza lugha ya Kiswahili duniani ni vyema viongozi wa jumuiya wakazungumza lugha hiyo wakiwa katika mikutano mikubwa duniani akitolea mfano mjadala Mkuu wa Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.  “Katika vikao vyetu vya jumuiya (EAC) tumewaomba marais pia wakija vikao kama hivi (UNGA78) wazungumze kwa lugha ya Kiswahili ndio sasa wananchi waanze kuwasikia wanasema nini lakini pia itakuwa mchango wao kuendelea kusukuma lugha ya Kiswahili iweze kwenda mbele kama lugha zingine.” Amesema Dkt. Mathuki katika mahojiano yake na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa Dkt. Mathuki amesema tayari jumuiya hiyo imeanza kutekeleza mambo mbalimbali ya kusongesha lugha hiyo kimataifa. “Katika kikao cha baraza la mawaziri cha 43 kilichofanyika mwezi Machi mwaka huu 2023 tumekubaliana mambo yote tunayofanya katika jumuiya ya Afrika Mashariki lazima yawe kwa lugha ya Kiswahili na kiingereza. Tumeanza kutafuta wataalamu watusaidie kutafrisi nyaraka zote tunazofanya na ujumbe wowote tunaotoa lazima pia uwe kwa lugha ya Kiswahili.” Ili kusongesha zaidi lugha hiyo amesema wameanza mchakato wa kuanzisha vituo vya Kiswahili kwenye kila balozi za nchi wanachama ughaibuni ili kuvutia wageni pia watake kujifunza lugha hiyo adhimu. Amlipoulizwa inakuwaje viongozi wengi wa kisiasa wanaposimama katika majukwaa ya kimataifa wanazungumza kwa kingereza Dkt Mathuki alisema hiyo ni kutokana na uzoefu wao wakuwa wanazungumza lugha ya kigeni lakini kuna juhudi zinafanyika akitolea “mfano nchini Uganda, katika baraza la mawaziri mafunzo ya lugha ya Kiswahili ni lazima.” 
9/20/20230
Episode Artwork

Tuzungumze Kiswahili kwenye UNGA78 - Viongozi wa EAC

Katibu Mkuu wa Jumuiya ya Afrika Mashariki Dkt. Peter Mathuki amesema ili kuongeza ushawishi na kukuza lugha ya Kiswahili duniani ni vyema viongozi wa jumuiya wakazungumza lugha hiyo wakiwa katika mikutano mikubwa duniani akitolea mfano mjadala Mkuu wa Mkutano wa 78 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.  “Katika vikao vyetu vya jumuiya (EAC) tumewaomba marais pia wakija vikao kama hivi (UNGA78) wazungumze kwa lugha ya Kiswahili ndio sasa wananchi waanze kuwasikia wanasema nini lakini pia itakuwa mchango wao kuendelea kusukuma lugha ya Kiswahili iweze kwenda mbele kama lugha zingine.” Amesema Dkt. Mathuki katika mahojiano yake na Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa Dkt. Mathuki amesema tayari jumuiya hiyo imeanza kutekeleza mambo mbalimbali ya kusongesha lugha hiyo kimataifa. “Katika kikao cha baraza la mawaziri cha 43 kilichofanyika mwezi Machi mwaka huu 2023 tumekubaliana mambo yote tunayofanya katika jumuiya ya Afrika Mashariki lazima yawe kwa lugha ya Kiswahili na kiingereza. Tumeanza kutafuta wataalamu watusaidie kutafrisi nyaraka zote tunazofanya na ujumbe wowote tunaotoa lazima pia uwe kwa lugha ya Kiswahili.” Ili kusongesha zaidi lugha hiyo amesema wameanza mchakato wa kuanzisha vituo vya Kiswahili kwenye kila balozi za nchi wanachama ughaibuni ili kuvutia wageni pia watake kujifunza lugha hiyo adhimu. Amlipoulizwa inakuwaje viongozi wengi wa kisiasa wanaposimama katika majukwaa ya kimataifa wanazungumza kwa kingereza Dkt Mathuki alisema hiyo ni kutokana na uzoefu wao wakuwa wanazungumza lugha ya kigeni lakini kuna juhudi zinafanyika akitolea “mfano nchini Uganda, katika baraza la mawaziri mafunzo ya lugha ya Kiswahili ni lazima.” 
9/20/20230
Episode Artwork

19 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Leo ni siku ya pili na ya mwisho wa mkutano kuhusu malengo ya maendeleo endelevu SDGs lakini leo pia ndio pazia la mjadala Mkuu wa 78, UNGA78 limefunguliwa na pamoja na na hotuba za viongozi pia kutakuwa na mikutano itakayo jadili hali za ulinzi na usalama katika mataifa mbalimbali na hapo kesho kutakuwa na mkutano wa ngazi ya juu kuhusu Sudan. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na nashinani ikimulika hotuba za viongozi katika Baraza Kuu na kazi za vijana katika utekelezaji wa DGs.  Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030.   Makala nampisha Thelma Mwadzaya na makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs.Kama kawaida Rais wa kwanza kuhutubia ni wa Brazil akifuatiwa na Marekani. Pia Rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine yuko hapa akiwa miongoni mwa wanaoutubia leo. Aidha ratiba inaonesha kwa leo siku ya ufunguzi marais kutoka bara la Afrika watakaohutubia ni Rais wa Afrika Kusini, Msumbiji, Nigeria, Senegal. Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC wanaonekana kwenye ratiba ya kesho.Mashinani tunasalia hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York kusikia jinsi ambavyo vijana wanavyochangia katika mchakato wa kusongesha ajenda ya malengo ya malengo endelevu. Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/19/20230
Episode Artwork

19 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Leo ni siku ya pili na ya mwisho wa mkutano kuhusu malengo ya maendeleo endelevu SDGs lakini leo pia ndio pazia la mjadala Mkuu wa 78, UNGA78 limefunguliwa na pamoja na na hotuba za viongozi pia kutakuwa na mikutano itakayo jadili hali za ulinzi na usalama katika mataifa mbalimbali na hapo kesho kutakuwa na mkutano wa ngazi ya juu kuhusu Sudan. Pia tunakuletea habari kwa ufupi na nashinani ikimulika hotuba za viongozi katika Baraza Kuu na kazi za vijana katika utekelezaji wa DGs.  Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030.   Makala nampisha Thelma Mwadzaya na makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs.Kama kawaida Rais wa kwanza kuhutubia ni wa Brazil akifuatiwa na Marekani. Pia Rais Volodymyr Zelenskyy wa Ukraine yuko hapa akiwa miongoni mwa wanaoutubia leo. Aidha ratiba inaonesha kwa leo siku ya ufunguzi marais kutoka bara la Afrika watakaohutubia ni Rais wa Afrika Kusini, Msumbiji, Nigeria, Senegal. Rwanda na Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC wanaonekana kwenye ratiba ya kesho.Mashinani tunasalia hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York kusikia jinsi ambavyo vijana wanavyochangia katika mchakato wa kusongesha ajenda ya malengo ya malengo endelevu. Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/19/20230
Episode Artwork

UNICEF: Apu ya OKY na hedhi salama yasongesha SDG 3

Shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, limezindua apu maalum ya wasichana kufuatilia maelezo wakati wa hedhi. Apu hiyo ni mahsusi kwa wasichana wa mataifa yanayoinukia na yaliyo masikini. Apu hii inaleta matumaini wakati huu ambapo viongozi wa dunia wanakutana New York, Marekani kutathmini maendeleo ya malengo ya maendeleo endelevu, SDGs. Thelma Mwadzaya amefuatilia na kutuletea makala kuhusu apu hiyo, iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF.  
9/18/20230
Episode Artwork

UNICEF: Apu ya OKY na hedhi salama yasongesha SDG 3

Shirika la umoja wa mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, limezindua apu maalum ya wasichana kufuatilia maelezo wakati wa hedhi. Apu hiyo ni mahsusi kwa wasichana wa mataifa yanayoinukia na yaliyo masikini. Apu hii inaleta matumaini wakati huu ambapo viongozi wa dunia wanakutana New York, Marekani kutathmini maendeleo ya malengo ya maendeleo endelevu, SDGs. Thelma Mwadzaya amefuatilia na kutuletea makala kuhusu apu hiyo, iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF.  
9/18/20230
Episode Artwork

Guterres: Badala ya kutomwacha yeyote nyuma tunahatarisha kuyaacha malengo ya SDGs nyuma

Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Muda wa kuchukua hatua ni sasa kuhakikisha tunayaokoa malengo ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanasuasua na kuwa kwenye hatari kubwa ya kutotimizwa amesema leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akizungumza katika ufunguzi wa jukwaa hilo hapa kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa chini ya mwamvuli wa Kikao cha 78 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.Katibu Mkuu amesema ahadi iliyotolewa na viongozi wa Dunia miaka 8 iliyopita kwa watu ya kuwa na Dunia yenye afya, maendeleo na fursa kwa wote inakwenda mrama na hadi sasa ni asilimia 15 pekee ya malengo 17 yaliyopitishwa ndio yako kwenye msitari unaotakiwa  menggine yanarudi nyuma na mengi yanajikongoja.Viongozi wa Dunia waliafikiana na kupitisha malengo hayo 17 mwaka 2015  wakiahidi kutomwacha yeyote nyuma.Malengo hayo yanajumuisha kutokomeza umasikini, kutokomeza njaa, kuhakikisha fursa ya upatikanaji wa maji safi na usafi lakini pamoja na kutoa elimu bora kwa wote na fursa za muda mrefu za kusoma. Kila lengo kuu lina vipengele vyake na jumla ya ni asilimia 15 pekee ya malengo hayo na vipengele vyake ndio viko kwenye msitari unaotakiwa.vipengele vya malengo hayo ni 169, lakini Katibu Mkuu ameonya kwamba ni malengo mengi yako nje ya msitari.Hivyo amesisitiza kuwa azimio la kisiasa ndio dawa mujarabu wa kusongesha mbele utimizaji na ufikiaji wa malengo hayo ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufika ukomo wake mwaka 2030.Azimio hilo linajumuisha “ahadi ya kufadhli kwa nchi zinazoendelea ili kusongesha malengo hayo  na msaada mkubwa wa kuunga mkono mapendekezo yake kwa ajili ya SDGs angalu dola bilioni 500 kila mwaka , na pia mkakati wa upunguzaji wa madeni.Azimio hilo pia linatoa wito wa kubadili mtindo wa biashara wa benki za maendeleo za kimataifa ili kutoa fedha za kibinafsi kwa viwango vya riba nafuu zaidi kwa nchi zinazoendelea, na kuunga mkono mageuzi ya usanifu wa fedha wa kimataifa ambao ameuita umepitwa na wakati, haufanyi kazi vizuri na sio wa haki.
9/18/20230
Episode Artwork

Guterres: Badala ya kutomwacha yeyote nyuma tunahatarisha kuyaacha malengo ya SDGs nyuma

Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Muda wa kuchukua hatua ni sasa kuhakikisha tunayaokoa malengo ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanasuasua na kuwa kwenye hatari kubwa ya kutotimizwa amesema leo Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres akizungumza katika ufunguzi wa jukwaa hilo hapa kwenye Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa chini ya mwamvuli wa Kikao cha 78 cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa au UNGA78.Katibu Mkuu amesema ahadi iliyotolewa na viongozi wa Dunia miaka 8 iliyopita kwa watu ya kuwa na Dunia yenye afya, maendeleo na fursa kwa wote inakwenda mrama na hadi sasa ni asilimia 15 pekee ya malengo 17 yaliyopitishwa ndio yako kwenye msitari unaotakiwa  menggine yanarudi nyuma na mengi yanajikongoja.Viongozi wa Dunia waliafikiana na kupitisha malengo hayo 17 mwaka 2015  wakiahidi kutomwacha yeyote nyuma.Malengo hayo yanajumuisha kutokomeza umasikini, kutokomeza njaa, kuhakikisha fursa ya upatikanaji wa maji safi na usafi lakini pamoja na kutoa elimu bora kwa wote na fursa za muda mrefu za kusoma. Kila lengo kuu lina vipengele vyake na jumla ya ni asilimia 15 pekee ya malengo hayo na vipengele vyake ndio viko kwenye msitari unaotakiwa.vipengele vya malengo hayo ni 169, lakini Katibu Mkuu ameonya kwamba ni malengo mengi yako nje ya msitari.Hivyo amesisitiza kuwa azimio la kisiasa ndio dawa mujarabu wa kusongesha mbele utimizaji na ufikiaji wa malengo hayo ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufika ukomo wake mwaka 2030.Azimio hilo linajumuisha “ahadi ya kufadhli kwa nchi zinazoendelea ili kusongesha malengo hayo  na msaada mkubwa wa kuunga mkono mapendekezo yake kwa ajili ya SDGs angalu dola bilioni 500 kila mwaka , na pia mkakati wa upunguzaji wa madeni.Azimio hilo pia linatoa wito wa kubadili mtindo wa biashara wa benki za maendeleo za kimataifa ili kutoa fedha za kibinafsi kwa viwango vya riba nafuu zaidi kwa nchi zinazoendelea, na kuunga mkono mageuzi ya usanifu wa fedha wa kimataifa ambao ameuita umepitwa na wakati, haufanyi kazi vizuri na sio wa haki.
9/18/20230
Episode Artwork

Mazao ya asili yaliyo puuzwa yatasaidia kutokomeza njaa

Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030Wadau wa Maendeleo wamejaa hapa katika makao Makuu hakika na rangi za malengo 17 zikiwa zimetaradadi kila kona kuanzia nje mpaka ndani ya Baraza Kuu, mwaka huu wakija na maudhui yasemayo, Kujenga upya kuaminiana na kuchochea mshikamano wa dunia.Mikutano ya SDGs imekuwa na ubunifu tofauti mwaka baada ya mwaka, na mwaka huu katika eneo la wazi baada tu ya kuingia makao makuu kuna milango midogo 17 inayoonesha malengo 17 na kila mlango una mchechemuzi na umeandikwa namna anavyopambana kutekeleza lengo.Mlango namba mbili ni kutokomeza njaa, na ukifungua mlango unakutana na Pierre Thiam raia wa Senegali na mpishi mwenye makazi yake hapa jijini New York Marekani, yeye anaamini kuwa dunia inaweza kutokomeza njaa iwapo itageukia katika mazao ambayo hayatumiwi sana na yamekuwa yakipuuzwa.Thiam alihojiwa na mwenzangu Florence Westergard wa Idhaa ya Kifaransa ya Umoja wa Mataifa na anasema,“Kwa hiyo kupambana na njaa kutanza kwa kubadili mifumo yetu ya chakula na kurejea katika aina ya kilimo kinachosaidia wakulima wadogo na mazao yao ambayo hayatumiki, na kutafuta njia za kuongeza thamani katika mazao hayo na kuyafanya yaweze kupatikana masokoni.”Thiam yeye ananena na anatenda kwani anahamasisha zao la Forno ambalo linapatikana maeneo mengi ya ukanda wa Sahel. Ukanda ambao nchi nyingi zinatakabiliwa na uhaba wa chakula.Kwakweli Flora mara baada ya kumsikia mchechemuzi huyu nami nikakumbuka kule kwetu Kilimanjaro Tanzania tumehamasika kula ndizi lakini kuna mazao kama viazi vikuu ambavyo ndio hayo yanayoelezwa kuwa yamepuuzwa na tunapaswa kurejea kwayo. 
9/18/20230
Episode Artwork

Mazao ya asili yaliyo puuzwa yatasaidia kutokomeza njaa

Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030Wadau wa Maendeleo wamejaa hapa katika makao Makuu hakika na rangi za malengo 17 zikiwa zimetaradadi kila kona kuanzia nje mpaka ndani ya Baraza Kuu, mwaka huu wakija na maudhui yasemayo, Kujenga upya kuaminiana na kuchochea mshikamano wa dunia.Mikutano ya SDGs imekuwa na ubunifu tofauti mwaka baada ya mwaka, na mwaka huu katika eneo la wazi baada tu ya kuingia makao makuu kuna milango midogo 17 inayoonesha malengo 17 na kila mlango una mchechemuzi na umeandikwa namna anavyopambana kutekeleza lengo.Mlango namba mbili ni kutokomeza njaa, na ukifungua mlango unakutana na Pierre Thiam raia wa Senegali na mpishi mwenye makazi yake hapa jijini New York Marekani, yeye anaamini kuwa dunia inaweza kutokomeza njaa iwapo itageukia katika mazao ambayo hayatumiwi sana na yamekuwa yakipuuzwa.Thiam alihojiwa na mwenzangu Florence Westergard wa Idhaa ya Kifaransa ya Umoja wa Mataifa na anasema,“Kwa hiyo kupambana na njaa kutanza kwa kubadili mifumo yetu ya chakula na kurejea katika aina ya kilimo kinachosaidia wakulima wadogo na mazao yao ambayo hayatumiki, na kutafuta njia za kuongeza thamani katika mazao hayo na kuyafanya yaweze kupatikana masokoni.”Thiam yeye ananena na anatenda kwani anahamasisha zao la Forno ambalo linapatikana maeneo mengi ya ukanda wa Sahel. Ukanda ambao nchi nyingi zinatakabiliwa na uhaba wa chakula.Kwakweli Flora mara baada ya kumsikia mchechemuzi huyu nami nikakumbuka kule kwetu Kilimanjaro Tanzania tumehamasika kula ndizi lakini kuna mazao kama viazi vikuu ambavyo ndio hayo yanayoelezwa kuwa yamepuuzwa na tunapaswa kurejea kwayo. 
9/18/20230
Episode Artwork

18 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tuanaangazia malengo ya maendeleo endelevu na tutasalia hapa makao makuu ya umoja wa Mataifa kwenye Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo hayo.Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030.   Katika makala Thelma Mwadzaya amefuatilia na kukuletea makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs.Mashinani tunasalia hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani kusikia kile ambacho vijana wanataka kifanyike ili malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yaweze kufanikiwa, lakini kwanza ni makala nampisha Thelma Mwadzaya na makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/18/20230
Episode Artwork

18 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tuanaangazia malengo ya maendeleo endelevu na tutasalia hapa makao makuu ya umoja wa Mataifa kwenye Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo hayo.Jukwaa la siku mbili la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya maendeleo endelevu SDGs, limefungua pazia leo kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York Marekani. Lengo kubwa la jukwaa hilo ni kuja na azimio la kisiasa la kuhakikissha wanayanusuru malengo hayo ambayo mengi yanakwenda mrama kwani ni asilimia 15 pekee kwa mujibu wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ndio yametimizwa huku ikiwa imesalia chini ya miaka 7 kufikia mwaka 2030 ukomo wa utimizaji wa malengo hayo.Tarehe 17 na 18 Septemba yani leo na kesho hapa katika makao Makuu viongozi wanakutana kuangalia vipi wametekeleza malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs ambayo yanatarajiwa kufikia kilele mwaka 2030.   Katika makala Thelma Mwadzaya amefuatilia na kukuletea makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs.Mashinani tunasalia hapa Makao Makuu ya Umoja wa Mataifa New York, Marekani kusikia kile ambacho vijana wanataka kifanyike ili malengo ya maendeleo endelevu, SDGs yaweze kufanikiwa, lakini kwanza ni makala nampisha Thelma Mwadzaya na makala kuhusu apu iliyoandaliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF iitwayo oKy ya kuwezesha wasichana kufuatilia hedhi, moja ya vipengele vya SDGs. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/18/20230
Episode Artwork

Tunakumbatia wito wa kupambana na mabadiliko ya tabianchi kwa vitendo - Vijana Bongoyo Tanzania

Wakati macho na masikio ya Dunia yakielekezwa hapa New York Marekani kwenye mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa utakaoanza Jumatatu wiki ijayo kujadili mada mbalimbali ikiwemo hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi , tunaelekea Tanzania ambako katika pitapita zake, Flora Nducha alipokuwa jijini Dar es Salaama alikutana na mmoja wa vijana wajasiriamali kwenye kisiwa cha Bongoyo waliokumbatia wito wa kupambana na jinamizi la mabadiliko ya tabianchi, akamweleza  Flora kuwa mbali ya kujipatia kipato kutokana na utalii endelevu ana jukumu kubwa pamoja na baadhi ya vijana wenzie la kulinda msitu wa Bongoyo na matumbawe ya Kisiwa hicho kilicho katika Bahari ya Hindi. Tusikilize mahojiano na kijana huyo anayeanza kwa kujitambulisha.
9/15/20230
Episode Artwork

Tunakumbatia wito wa kupambana na mabadiliko ya tabianchi kwa vitendo - Vijana Bongoyo Tanzania

Wakati macho na masikio ya Dunia yakielekezwa hapa New York Marekani kwenye mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa utakaoanza Jumatatu wiki ijayo kujadili mada mbalimbali ikiwemo hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi , tunaelekea Tanzania ambako katika pitapita zake, Flora Nducha alipokuwa jijini Dar es Salaama alikutana na mmoja wa vijana wajasiriamali kwenye kisiwa cha Bongoyo waliokumbatia wito wa kupambana na jinamizi la mabadiliko ya tabianchi, akamweleza  Flora kuwa mbali ya kujipatia kipato kutokana na utalii endelevu ana jukumu kubwa pamoja na baadhi ya vijana wenzie la kulinda msitu wa Bongoyo na matumbawe ya Kisiwa hicho kilicho katika Bahari ya Hindi. Tusikilize mahojiano na kijana huyo anayeanza kwa kujitambulisha.
9/15/20230
Episode Artwork

WHO: Msizike marehemu wa majanga kwenye makaburi ya halaiki

Kunapotokea majanga au vita na kusababisha watu wengi kupoteza maisha kunakuwa na hofu kuhusu miili ya marehemu kuwa inaweza kusababisha mlipuko wa magonjwa hivyo baadhi ya jamii kwa kutokuwa na taarifa sahihi hujikuta wakizika miili hiyo katika makaburi ya halaiki ili kuepuka mlipuko wa magonjwa lakini shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO linasema hiyo si sahihi. Kuzika marehemu ni ibada, ni heshima na kubwa zaidi husaidia wafiwa kuponya nafsi zao kwa kufunga ukurasa wa mpendwa wao wakibaki na matumaini kuwa wamempumzisha katika nyumba yake ya milele. Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa leo na WHO pamoja na shirika la chama cha Msalaba mwekundu ICRC na Mwezi mwekundu IFRC imeeleza kuwa miili ya watu ambao wamekufa kutokana na majeraha, katika majanga ya asili au vita kamwe haileti hatari ya kiafya kwa jamii. Hii ni kwa sababu watu hao ambao wamekufa kutokana na kiwewe, kuzama au moto hawahifadhi katika miili yao  vinavyosababisha magonjwa ambayo yatahitaji jamii kuchukua tahadhari za kawaida.Dkt. Kazunobu Kojima ni Afisa Tiba wa ulinzi na usalama wa katika Mpango wa Dharura wa Afya wa WHO na ametoa ombi kwa mamlaka zote duniani. “Tunahimiza mamlaka katika jamii zilizoguswa na msiba kutoharakisha mazishi ya halaiki au kuchoma maiti. Usimamizi wenye heshima ni muhimu kwa familia na jamii, na katika maeneo yaliyo na migogoro, mara nyingi, ni sehemu muhimu ya kukomesha haraka mapigano.”WHO imeeleza kuwa eneo ambalo kuna magonjwa kama Ebola, Marburg au kipindupindu, au wakati maafa mengine yanapotokea katika eneo lenye magonjwa hayo ya kuambukiza hapo ni vyema kuzika marehemu haraka kwani magonjwa ya mlipuko yanaweza kutokea.Naye Mkuu wa kitengo cha uchunguzi wa ICRC Pierre Guyomarch amesema “Imani kwamba maiti yoyote itasababisha magonjwa ya mlipuko haiungwi mkono na ushahidi wowote” na kutoa wito kwa wanao elimisha jamii kuzingatia utoaji taarifa sahihi.“Tumekuwa tukiona ripoti nyingi za vyombo vya habari na hata wataalamu wakikosea katika kushughulikia suala hili, ukweli ni kwamba wale wanaookoka kwenye matukio kama msiba wa asili wana uwezekano mkubwa wa kueneza magonjwa kuliko maiti.” Amesema Guyomarch. Mashirika hayo kwa pamoja yamehimiza jamii kupatiwa zana na taarifa sahihi ili kupunguza hofu na ili waweze kudhibiti na kuhifadhi maiti kwa usalama na heshima. Na wale wanaohusika katika kushughulikia majanga wanapaswa kufuata kanuni zilizowekwa za usimamizi wa maiti, kwa manufaa ya jamii yote, na watoe msaada zaidi kama inahitajika.
9/15/20230
Episode Artwork

WHO: Msizike marehemu wa majanga kwenye makaburi ya halaiki

Kunapotokea majanga au vita na kusababisha watu wengi kupoteza maisha kunakuwa na hofu kuhusu miili ya marehemu kuwa inaweza kusababisha mlipuko wa magonjwa hivyo baadhi ya jamii kwa kutokuwa na taarifa sahihi hujikuta wakizika miili hiyo katika makaburi ya halaiki ili kuepuka mlipuko wa magonjwa lakini shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO linasema hiyo si sahihi. Kuzika marehemu ni ibada, ni heshima na kubwa zaidi husaidia wafiwa kuponya nafsi zao kwa kufunga ukurasa wa mpendwa wao wakibaki na matumaini kuwa wamempumzisha katika nyumba yake ya milele. Katika taarifa ya pamoja iliyotolewa leo na WHO pamoja na shirika la chama cha Msalaba mwekundu ICRC na Mwezi mwekundu IFRC imeeleza kuwa miili ya watu ambao wamekufa kutokana na majeraha, katika majanga ya asili au vita kamwe haileti hatari ya kiafya kwa jamii. Hii ni kwa sababu watu hao ambao wamekufa kutokana na kiwewe, kuzama au moto hawahifadhi katika miili yao  vinavyosababisha magonjwa ambayo yatahitaji jamii kuchukua tahadhari za kawaida.Dkt. Kazunobu Kojima ni Afisa Tiba wa ulinzi na usalama wa katika Mpango wa Dharura wa Afya wa WHO na ametoa ombi kwa mamlaka zote duniani. “Tunahimiza mamlaka katika jamii zilizoguswa na msiba kutoharakisha mazishi ya halaiki au kuchoma maiti. Usimamizi wenye heshima ni muhimu kwa familia na jamii, na katika maeneo yaliyo na migogoro, mara nyingi, ni sehemu muhimu ya kukomesha haraka mapigano.”WHO imeeleza kuwa eneo ambalo kuna magonjwa kama Ebola, Marburg au kipindupindu, au wakati maafa mengine yanapotokea katika eneo lenye magonjwa hayo ya kuambukiza hapo ni vyema kuzika marehemu haraka kwani magonjwa ya mlipuko yanaweza kutokea.Naye Mkuu wa kitengo cha uchunguzi wa ICRC Pierre Guyomarch amesema “Imani kwamba maiti yoyote itasababisha magonjwa ya mlipuko haiungwi mkono na ushahidi wowote” na kutoa wito kwa wanao elimisha jamii kuzingatia utoaji taarifa sahihi.“Tumekuwa tukiona ripoti nyingi za vyombo vya habari na hata wataalamu wakikosea katika kushughulikia suala hili, ukweli ni kwamba wale wanaookoka kwenye matukio kama msiba wa asili wana uwezekano mkubwa wa kueneza magonjwa kuliko maiti.” Amesema Guyomarch. Mashirika hayo kwa pamoja yamehimiza jamii kupatiwa zana na taarifa sahihi ili kupunguza hofu na ili waweze kudhibiti na kuhifadhi maiti kwa usalama na heshima. Na wale wanaohusika katika kushughulikia majanga wanapaswa kufuata kanuni zilizowekwa za usimamizi wa maiti, kwa manufaa ya jamii yote, na watoe msaada zaidi kama inahitajika.
9/15/20230
Episode Artwork

15 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea habari kuhusu magonjwa ya mlipuko baada ya majanga, na makaburi ya wafalme wa Uganda. Makala tunakupeleka nchini Tanzania kusikia matarajio wa wananchi tukielekea mkutano wa UNGA78 na mashinani tutasalia hapa hapa Makao Makuu  kusikia ujumbe kuhusu kikao cha ngazi ya juu cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika juma lijalo.  Kunapotokea majanga au vita na kusababisha watu wengi kupoteza maisha kunakuwa na hofu kuhusu miili ya marehemu kuwa inaweza kusababisha mlipuko wa magonjwa hivyo baadhi ya jamii kwakutokuwa na taarifa sahihi hujikuta wakizika miili hiyo katika makaburi ya halaiki ili kuepuka mlipuko wa magonjwa lakini shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO linasema hiyo si sahihi.Baada ya kunusurika kwa moto na hatimaye kuwekwa kwenye orodha ya maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini kuharibika, makaburi ya wafalme wa Buganda huko Kasubi nchini Uganda sasa yako salama na yameondolewa kwenye orodha hiyo baada ya ukarabati uliofanywa na Uganda kwa usaidizi wa Umoja wa Mataifa na wadau.   Katika makala na wakati macho na masikio ya Dunia yakielekezwa New York Marekani kwenye mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa utakaoanza Jumatatu ijayo kujadili mada mbalimbali ikiwemo hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na tunaelekea Tanzania.Mashinani tutasalia hapa makao Makuu  kusikia ujumbe wa Mwakilishi wa kudumu wa Marekani kwenye Umoja wa Mataifa Balozi Linda Thomas-Greenfield kuhusu kikao cha ngazi ya juu cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika juma lijalo. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/15/20230
Episode Artwork

15 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea habari kuhusu magonjwa ya mlipuko baada ya majanga, na makaburi ya wafalme wa Uganda. Makala tunakupeleka nchini Tanzania kusikia matarajio wa wananchi tukielekea mkutano wa UNGA78 na mashinani tutasalia hapa hapa Makao Makuu  kusikia ujumbe kuhusu kikao cha ngazi ya juu cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika juma lijalo.  Kunapotokea majanga au vita na kusababisha watu wengi kupoteza maisha kunakuwa na hofu kuhusu miili ya marehemu kuwa inaweza kusababisha mlipuko wa magonjwa hivyo baadhi ya jamii kwakutokuwa na taarifa sahihi hujikuta wakizika miili hiyo katika makaburi ya halaiki ili kuepuka mlipuko wa magonjwa lakini shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO linasema hiyo si sahihi.Baada ya kunusurika kwa moto na hatimaye kuwekwa kwenye orodha ya maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini kuharibika, makaburi ya wafalme wa Buganda huko Kasubi nchini Uganda sasa yako salama na yameondolewa kwenye orodha hiyo baada ya ukarabati uliofanywa na Uganda kwa usaidizi wa Umoja wa Mataifa na wadau.   Katika makala na wakati macho na masikio ya Dunia yakielekezwa New York Marekani kwenye mkutano wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa utakaoanza Jumatatu ijayo kujadili mada mbalimbali ikiwemo hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi na tunaelekea Tanzania.Mashinani tutasalia hapa makao Makuu  kusikia ujumbe wa Mwakilishi wa kudumu wa Marekani kwenye Umoja wa Mataifa Balozi Linda Thomas-Greenfield kuhusu kikao cha ngazi ya juu cha Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa kitakachofanyika juma lijalo. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/15/20230
Episode Artwork

UNESCO imeondoa makaburi ya wafalme wa Buganda kwenye orodha, kulikoni?

Baada ya kunusurika kwa moto na hatimaye kuwekwa kwenye orodha ya maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini kuharibika, makaburi ya wafalme wa Buganda huko Kasubi nchini Uganda sasa yako salama na yameondolewa kwenye orodha hiyo baada ya ukarabati uliofanywa na Uganda kwa usaidizi wa Umoja wa Mataifa na wadau. Mwaka 2010 moto mkubwa uliharibu kwa kiasi kikubwa Makaburi ya Wafalme wa Buganda kwenye vilima vya wilaya ya Kampala nchini Uganda, hali iliyosababisha Umoja wa Mataifa kuingilia kati kwa kuwa makaburi hayo yaliorodheshwa mwaka 2001 na shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni kuwa eneo la urithi wa dunia.   Lazare Eleoundou Assomo Mkurugenzi wa Kituo cha UNESCO cha Maeneo ya Urithi wa Dunia akizungumza akiwa kwenye eneo hilo anasema, ni siku ya kihistoria. Kamati ya Urithi wa Dunia imeondoa makaburi ya Kasubi kutoka orodha ya maeneo yaliyo hatarini. Miezi michache iliyopita nilitembelea eneo hili, na niliweza kuona kazi nzuri na ya kina iliyofanywa na wanajamii na watu wa Uganda. Napenda kumpongeza kila mtu kwa kazi hii kubwa.  Hongereni sana nyote.”   Makaburi hayo yako kwenye eneo la ukubwa wa ekari 30 na kwa kiasi kikubwa eneo hilo ni shamba ambalo kilimo chake hutumia mbinu za kiasili. Ujenzi wake umetumia vitu vya asili kama miti, nyasi na matete.  Eneo la kati ni kasri ya zamani ya wafalme Kabaka wa Buganda iliyojengwa mwaka 1882 na kugeuzwa kuwa makaburi mwaka 1884.  Wanajamii ndio waliokuwa kitovu cha mafanikio ya ukarabati wa makaburi hayo kwa ushirikiano na serikali na wataalamu ambapo walifanikisha ujenzi mpya wa Muzibu Azaala Mpanga ambalo ndilo jengo kuu lenye makaburi, na urejeshaji wa Bujjabukala, ambayo ni nyumba ya muangalizi na uwekaji wa mfumo wa kisasa wa kutoa onyo la kuzima moto. Mradi huo ulihusisha pia mafunzo kwa wazima moto kutoka eneo hilo ili kuzuia janga kama la 2010 lisitokee tena. Kikao cha 45 cha Kamati ya UNESCO ya maeneo ya urithi wa dunia kinafanyika huko Riyadhi, Saudi Arabia kuanzia tarehe 10 hadi 25 mwezi huu ambako pamoja na mambo mengine kinatathmini uhifadhi wa maeneo ya urithi wa dunia. Bofyahapakutambua maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini. 
9/15/20230
Episode Artwork

UNESCO imeondoa makaburi ya wafalme wa Buganda kwenye orodha, kulikoni?

Baada ya kunusurika kwa moto na hatimaye kuwekwa kwenye orodha ya maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini kuharibika, makaburi ya wafalme wa Buganda huko Kasubi nchini Uganda sasa yako salama na yameondolewa kwenye orodha hiyo baada ya ukarabati uliofanywa na Uganda kwa usaidizi wa Umoja wa Mataifa na wadau. Mwaka 2010 moto mkubwa uliharibu kwa kiasi kikubwa Makaburi ya Wafalme wa Buganda kwenye vilima vya wilaya ya Kampala nchini Uganda, hali iliyosababisha Umoja wa Mataifa kuingilia kati kwa kuwa makaburi hayo yaliorodheshwa mwaka 2001 na shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu, Sayansi na Utamaduni kuwa eneo la urithi wa dunia.   Lazare Eleoundou Assomo Mkurugenzi wa Kituo cha UNESCO cha Maeneo ya Urithi wa Dunia akizungumza akiwa kwenye eneo hilo anasema, ni siku ya kihistoria. Kamati ya Urithi wa Dunia imeondoa makaburi ya Kasubi kutoka orodha ya maeneo yaliyo hatarini. Miezi michache iliyopita nilitembelea eneo hili, na niliweza kuona kazi nzuri na ya kina iliyofanywa na wanajamii na watu wa Uganda. Napenda kumpongeza kila mtu kwa kazi hii kubwa.  Hongereni sana nyote.”   Makaburi hayo yako kwenye eneo la ukubwa wa ekari 30 na kwa kiasi kikubwa eneo hilo ni shamba ambalo kilimo chake hutumia mbinu za kiasili. Ujenzi wake umetumia vitu vya asili kama miti, nyasi na matete.  Eneo la kati ni kasri ya zamani ya wafalme Kabaka wa Buganda iliyojengwa mwaka 1882 na kugeuzwa kuwa makaburi mwaka 1884.  Wanajamii ndio waliokuwa kitovu cha mafanikio ya ukarabati wa makaburi hayo kwa ushirikiano na serikali na wataalamu ambapo walifanikisha ujenzi mpya wa Muzibu Azaala Mpanga ambalo ndilo jengo kuu lenye makaburi, na urejeshaji wa Bujjabukala, ambayo ni nyumba ya muangalizi na uwekaji wa mfumo wa kisasa wa kutoa onyo la kuzima moto. Mradi huo ulihusisha pia mafunzo kwa wazima moto kutoka eneo hilo ili kuzuia janga kama la 2010 lisitokee tena. Kikao cha 45 cha Kamati ya UNESCO ya maeneo ya urithi wa dunia kinafanyika huko Riyadhi, Saudi Arabia kuanzia tarehe 10 hadi 25 mwezi huu ambako pamoja na mambo mengine kinatathmini uhifadhi wa maeneo ya urithi wa dunia. Bofyahapakutambua maeneo ya urithi wa dunia yaliyo hatarini. 
9/15/20230
Episode Artwork

Mradi wa "Football for the Goals" kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu Rwanda - UN Rwanda

Umoja wa Mataifa umekuwa ukipigia chepuo mbinu mbali mbali halali za kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu, SDGs, na miongoni mwa mbinu hizo ni mpira wa miguu, soka, wengine wakisema kabumbu au kandanda! Sasa wenyewe wabobezi au manguli wa soka wameitikia wito na Umoja wa Mataifa hususan nchini Rwanda ukaitikia Naam!!! Je nini kinafanyika? Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ameketi na Mkuu wa Ofisi ya Mratibu Mkazi wa UN, Rwanda Josephine Marealle-Ulimwengu na anafafanua kitendawili hicho.
9/14/20230
Episode Artwork

Mradi wa "Football for the Goals" kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu Rwanda - UN Rwanda

Umoja wa Mataifa umekuwa ukipigia chepuo mbinu mbali mbali halali za kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu, SDGs, na miongoni mwa mbinu hizo ni mpira wa miguu, soka, wengine wakisema kabumbu au kandanda! Sasa wenyewe wabobezi au manguli wa soka wameitikia wito na Umoja wa Mataifa hususan nchini Rwanda ukaitikia Naam!!! Je nini kinafanyika? Assumpta Massoi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ameketi na Mkuu wa Ofisi ya Mratibu Mkazi wa UN, Rwanda Josephine Marealle-Ulimwengu na anafafanua kitendawili hicho.
9/14/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili - "Nyamba"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA akieleza maana ya neno “NYAMBA”.
9/14/20230
Episode Artwork

Jifunze Kiswahili - "Nyamba"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa nchini Tanzania, BAKITA akieleza maana ya neno “NYAMBA”.
9/14/20230
Episode Artwork

14 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Umoja wa Mataifa umekuwa ukipigia chepuo mbinu mbali mbali halali za kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu, SDGs, na miongoni mwa mbinu hizo ni mpira wa miguu, soka, wengine wakisema kabumbu au kandanda na tunabisha hodi nchini Rwanda kushuhudia jinzi ambavyo wameitikia.  Pia tunakuletea habari kwa ufupi kuhusu ombi la msaada kusaidia waathirika Libya, utabiri wa hali ya hewa na usalama wa afya ya mgonjwa. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili  tuankuletea ufafanuzi wa neno “NYAMBA”.  Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths amesema kufuatia zahma kubwa ya mafuriko yaliyoikumba Libya na kuathiri maelfu kwa maelfu ya waltu leo ametoa dola milioni 10 kutoka kwenye mfuko wa dharura wa Umoja wa Mataifa CERF huku ombi la msaada zaidi likitarajiwa kwa lengo la kufikisha msaada unaohitajika haraka kwa waathirika na kuwaepushia janga zaidi la kiafya.Ripoti mpya iliyotolewa leo na mashirika mbalimbali na kuratibiwa na shirika la Umoja wa Mataifa la utabiri wa hali ya hewa duniani WMO imesema wakati dunia imeshafikia nusu ya muda wa utimizaji wa ajenda ya maendeleo ya 2030, sayansi iko bayana kwamba lengo la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi linakwenda kombo, hali ambayo inaathiri juhudi za kimataifa za kupambana na njaa, umasikini, afya, kuboresha fursa za upatikanaji wa maji na nishati na maeneo mengine ya malengo ya maendeleo endelevu SDG’s , kwani hadi sasa ni asilimia 15 pekee ya malengo hayo 17 ndio yakk kwenye mstari unaotakiwa.   Na shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limehitimisha mkutano wa kimataifa kuhusu ushirikishwaji na usalama wa afya ya mgonjwa kwa makubaliano ya mkataba wa kwanza kabisa wa haki za usalama wa mgonjwa ambao unabainisha haki za msingi za wagonjwa wote katika muktadha wa usalama wa huduma za afya na unataka kusaidia serikali na wadau wengine wa sekta ya afya kuhakikisha kwamba sauti za wagonjwa zinasikika na haki yao ya kupata huduma salama za afya inalindwa.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili  nampisha mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA akieleza maana ya neno “NYAMBA”. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/14/20230
Episode Artwork

14 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Umoja wa Mataifa umekuwa ukipigia chepuo mbinu mbali mbali halali za kufanikisha malengo 17 ya maendeleo endelevu, SDGs, na miongoni mwa mbinu hizo ni mpira wa miguu, soka, wengine wakisema kabumbu au kandanda na tunabisha hodi nchini Rwanda kushuhudia jinzi ambavyo wameitikia.  Pia tunakuletea habari kwa ufupi kuhusu ombi la msaada kusaidia waathirika Libya, utabiri wa hali ya hewa na usalama wa afya ya mgonjwa. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili  tuankuletea ufafanuzi wa neno “NYAMBA”.  Mkuu wa Umoja wa Mataifa wa masuala ya kibinadamu na misaada ya dharura Martin Griffiths amesema kufuatia zahma kubwa ya mafuriko yaliyoikumba Libya na kuathiri maelfu kwa maelfu ya waltu leo ametoa dola milioni 10 kutoka kwenye mfuko wa dharura wa Umoja wa Mataifa CERF huku ombi la msaada zaidi likitarajiwa kwa lengo la kufikisha msaada unaohitajika haraka kwa waathirika na kuwaepushia janga zaidi la kiafya.Ripoti mpya iliyotolewa leo na mashirika mbalimbali na kuratibiwa na shirika la Umoja wa Mataifa la utabiri wa hali ya hewa duniani WMO imesema wakati dunia imeshafikia nusu ya muda wa utimizaji wa ajenda ya maendeleo ya 2030, sayansi iko bayana kwamba lengo la kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi linakwenda kombo, hali ambayo inaathiri juhudi za kimataifa za kupambana na njaa, umasikini, afya, kuboresha fursa za upatikanaji wa maji na nishati na maeneo mengine ya malengo ya maendeleo endelevu SDG’s , kwani hadi sasa ni asilimia 15 pekee ya malengo hayo 17 ndio yakk kwenye mstari unaotakiwa.   Na shirika la afya la Umoja wa Mataifa WHO limehitimisha mkutano wa kimataifa kuhusu ushirikishwaji na usalama wa afya ya mgonjwa kwa makubaliano ya mkataba wa kwanza kabisa wa haki za usalama wa mgonjwa ambao unabainisha haki za msingi za wagonjwa wote katika muktadha wa usalama wa huduma za afya na unataka kusaidia serikali na wadau wengine wa sekta ya afya kuhakikisha kwamba sauti za wagonjwa zinasikika na haki yao ya kupata huduma salama za afya inalindwa.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili  nampisha mtaalam wetu Onni Sigalla, Mhariri mwandamizi wa Baraza la Kiswahili la Taifa  nchini Tanzania, BAKITA akieleza maana ya neno “NYAMBA”. Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/14/20230
Episode Artwork

Mradi wa stadi za maisha waleta manufaa kwa wanafunzi wa kike Tanzania

Shirika la Campaign for Female Education au CAMFED kwa kushirikiana na wizara za Elimu Sayansi na Teknolojia na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa nchini Tanzania wanatekeleza mradi wakutoa elimu ya stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike katika shule za sekondari za serikali lengo likiwa ni kuboresha stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike na kuwapa fursa zaidi za elimu na ujifunzaji.Mradi huo unaotekeleza lengo namba 4 na namba 5 la Malengo ya Maendeleo endelevu SDGs yanayohimiza elimu bora na usawa wa kijinsia mtawalia umeanza kuzaa matunda kama anavyotujuza John Kabambala wa redio washirika KidsTime FM nchini Tanzania. 
9/13/20230
Episode Artwork

Mradi wa stadi za maisha waleta manufaa kwa wanafunzi wa kike Tanzania

Shirika la Campaign for Female Education au CAMFED kwa kushirikiana na wizara za Elimu Sayansi na Teknolojia na Ofisi ya Rais, Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa nchini Tanzania wanatekeleza mradi wakutoa elimu ya stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike katika shule za sekondari za serikali lengo likiwa ni kuboresha stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike na kuwapa fursa zaidi za elimu na ujifunzaji.Mradi huo unaotekeleza lengo namba 4 na namba 5 la Malengo ya Maendeleo endelevu SDGs yanayohimiza elimu bora na usawa wa kijinsia mtawalia umeanza kuzaa matunda kama anavyotujuza John Kabambala wa redio washirika KidsTime FM nchini Tanzania. 
9/13/20230
Episode Artwork

Mwanafunzi Malawi: Asante UNICEF, sasa kuoga si tatizo tena

Nchini Malawi, hofu ya wanafunzi wa kike kunuka wakati wakiwa kwenye hedhi kutokana na uhaba wa maji shuleni kwao imepatiwa jawabu baada ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, kufunga kisima cha maji kinachotumia nishati ya sola kuvuta maji kutoka ardhini. Noria Kanyama, mwanafunzi huyu wa shule moja ya msingi wilaya ya Chikwawa, mkoa wa Kusini nchini Malawi akikumbuka siku ambayo mafuriko yalikumba eneo lao. Anasema ililazimu wakimbilie maeneo ya mwinuko ambako ndiko aliko hivi sasa. Anasema, hapa ndipo tulalapo, mimi, mama yangu na wadogo zangu watatu. Pahala penyewe ni chumba kimoja na kidogo. Vimbunga ikiwemo Idai na Fredy vilisambaratisha miundombinu ya maji kwenye eneo lao.Kwa hiyo kando ya zahma ya malazi, ni zahma ya maji, akisema walitembea mwendo mrefu kwenda kuteka maji mtoni ambapo walitumia saa moja kwenda na kurudi. Maji yenyewe anasema hayakuwa masafi na si salama na watu wengine waliugua kuhara kwa kunywa maji hayo. Lakini zaidi ya yote, “Ninapokuwa kwenye hedhi, wavulana shuleni huwa wanatucheka. Wanasema wasichana wananuka, wako kwenye hedhi. Hii inatufanya tusiende shuleni, tunabakia nyumbani hadi tumalize hedhi. Hii inatuacha nyuma kwa sababu wenzetu wanaendelea na masomo wakati sisi tuko nyumbani.” UNICEF kwa kutambua zahma hii imejenga kisima cha maji kinachotumia nishati ya sola kusukuma maji kutoka ardhini, kisima kinachohudumia watoto 504 na familia zao. Sasa Noria mwenye umri wa miaka 14 anasema, “Ujio wa kisima hiki umebadili maisha yangu mno. Kuoga si tatizo, halikadhalika maji ya kunywa. Magonjwa nayo yametoweka. Tunapenda kuwashukuru wale waliotuletea hii huduma ya maji. Kinachonifurahisha zaidi mama yangu ananiruhusu niende shuleni. Ndoto yangu ni kuwa daktari.” 
9/13/20230
Episode Artwork

13 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea habari kutoka UNICEF na Benki ya Dunia. Makala tunamulika lengo namba nne na tano la malengo ya maendeleo endelevu SDGs ya Umoja wa Mataifa yanazungumzia upatikanaji wa elimu bora kwa wote na usawa wa kijinsia na mashinani tunakupeleka nchini Sudan, kulikoni?Ripoti mpya iliyotolewa leo kwa pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF na Benki ya Dunia inasema zaidi ya watoto milioni 333 duniani kote wanaishi katika ufukara, huku kudorora kwa uchumi kulikochangiwa na janga la COVID-19 kwa miaka mitatu kukichochea zaidi janga hilo.Nchini Malawi, hofu ya wanafunzi wa kike kunuka wakati wakiwa kwenye hedhi kutokana na uhaba wa maji shuleni kwao imepatiwa jawabu baada ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF, kufunga kisima cha maji kinachotumia nishati ya sola kuvuta maji kutoka ardhini.   Makala tunamulika lengo namba nne na tano la malengo ya maendeleo endelevu SDGs ya Umoja wa Mataifa yanazungumzia upatikanaji wa elimu bora kwa wote na usawa wa kijinsia ambapo serikali zinahimizwa kushirikiana na wadau kuhakikisha yote yanatimia ifikapo mwaka 2030 na nchini Tanzania shirika la CAMFED linatekeleza malengo hayo katika mradi wa kutoa elimi ya Stadi za maisha kwa wanafunzi wa kike wa shule za serikali za sekondari na tayari faida zimeanza kuonekana.Na mashinani tutakupeleka nchini Sudan ambapo licha ya migogoro ambayo imesababisha watu wengi nchini humo kukimbia makazi yao, wahudumu wa afya wanaendelea kutoa huduma kwa wananchi.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/13/20230
Episode Artwork

UNICEF/Benki ya Dunia: Watoto milioni 333 duniani kote wanaishi katika ufukara

Ripoti mpya iliyotolewa leo kwa pamoja na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF na Benki ya Dunia inasema zaidi ya watoto milioni 333 duniani kote wanaishi katika ufukara, huku kudorora kwa uchumi kulikochangiwa na janga la COVID-19 kwa miaka mitatu kukichochea zaidi janga hilo. Kwa mujibu wa ripoti hiyo “Mwenendo wa kimataifa wa umaskini wa kifedha wa mtoto kulingana na mistari ya kimataifa ya umaskini” iliyotolewa mjini New York na Washington mtoto 1 kati ya 6 kote duniani anaishi kwa chini dola 2 na senti 15 kwa siku ikiwa imepungua kutoka watoto milioni 383 hadi milioni 333 sawa na asilimia 13 kati ya mwaka 2013 na 2022.Ripoti imesema athari za kiuchumi za janga la COVID-19 zimechangia kupotea kwa miaka mitatu ya kupiga hatua za kiuchumi na kuwaacha watoto milioni 30 zaidi kusalia katika umasikini ambao waliotarajiwa kuondolewa kwenye jinamizi hilo.Tathimini hii iliyotolewa kuelekea mjadala wa Baraza Kuu la umoja wa Mataifa wa ngazi ya juu wiki ijayo ambao pamoja na mambo mengine viongozi wa dunia watatthimini hatua za mchakato wa utekelezaji wa malengo ya malengo ya maendeleo endelevu SDG’s inaonya kwamba lengo la kutokomeza umasikini kwa watuto ifikapo mwaka 2030 halitotimia.Mkurugenzi mtendaji wa UNICEF Catherine Russell amesema "Miaka saba iliyopita, dunia ilitoa ahadi ya kumaliza umaskini uliokithiri kwa watoto ifikapo mwaka 2030. Tumepiga hatua, tukionyesha kwamba kwa uwekezaji na utashi sahihi, kuna uwezekano wa kuwainua mamilioni ya watoto kutoka katika hali mbaya ya maisha ya umaskini. Lakini majanga yanayoongezeka kuanzia  athari za COVID-19, migogoro, mabadiliko ya tabianchi na majanga ya kiuchumi, yamezuia maendeleo, na kuwaacha mamilioni ya watoto katika umaskini uliokithiri. Hatuwezi kuwaangusha watoto hawa sasa. Kutokomeza umaskini wa watoto ni chaguo la kisera. Juhudi lazima ziongezwe maradufu ili kuhakikisha watoto wote wanapata huduma muhimu, ikiwa ni pamoja na elimu, lishe, huduma za afya na hifadhi ya jamii, huku tukishughulikia chanzo cha umaskini uliokithiri.”Naye Luis-Felipe Lopez-Calva mkurugenzi wa kimataifa wa Benki ya Dunia wa masuala ya umaskini na usawa amesema"Dunia ambapo watoto milioni 333 wanaishi katika umaskini uliokithiri na kunyimwa sio tu mahitaji ya msingi lakini pia utu, fursa au matumaini hali hii haiwezi kuvumiliwa. Ni muhimu zaidi kuliko wakati mwingine wowote kwamba watoto wote wawe na fursa bayana ya kutoka katika umaskini  kupitia upatikanaji sawa wa elimu bora, lishe bora, afya, ulinzi wa hifadhi ya jamii, pamoja na ulinzi na usalama. Ripoti hii inapaswa kuwa kumbusho tosha kwamba hatuna muda wa kupoteza katika vita dhidi ya umaskini na ukosefu wa usawa, na kwamba watoto lazima wawe kipaumbele katika juhudi zetu.”Tathimini ya ripoti hiyo inaonyesha kuwa nchi za Afrika Kusini mwa Jangwa la Sahara ndizo zinazobeba mzigo mkubwa zaidi wa watoto masikini kwani asilimia 40 wanaishi katika ufukara, na ilichangia ongezeko kubwa la Watoto masikini katika muongo uliopita, ikipanda kutoka asilimia 54.8 mwaka 2013 hadi asilimia 71.1 mwaka 2022.Wakati huo huo, ripoti inasema maeneo mengine yote duniani yameshuhudia kupungua kwa kasi kwa viwango vya umaskini uliokithiri, isipokuwa Mashariki ya Kati na Afrika Kaskazini.
9/13/20230
Episode Artwork

12 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani leo inatupeleka nchini Kenya kupata tathmini ya wanamazingira kufuatia kumalizika kwa mkutano wa siku tatu wa viongozi wa Afrika kuhusu tabianchi, mkutano uliotamatishwa kwa kupitishwa kwa azimio la Nairobi ambalo lilikuwa na vipengele 10 vya hatua za kuchukua ikiwemo wito kwa viongozi wa dunia kutambua kuwa uwepo wa shughuli za kiuchumi zitoazo kiwango kidogo cha hewa ya ukaa, ni fursa pia ya kuchangia katika usawa na ustawi wa watu wote duniani. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwema za WHO na WMO. Mashinani tunakupeleka nchini nchini Sudan Kusini kusikia simulizi ya mkimbizi kutoka nchini Sudan.Ikiwa leo ni Siku ya Kimataifa ya Usalama wa Mgonjwa, Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa, Dkt. Tedros Ghebreyesus ameuambia Mkutano wa Kimataifa wa WHO mjini Geneva, Uswisi kuwa ushahidi unaonesha kwamba mitazamo ambayo wagonjwa na familia zao huleta husababisha huduma bora, uzoefu bora wa wagonjwa, na matokeo bora.Shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya Hewa Duniani (WMO) limeeleza kuwa maafa yaliyosababishwa na mvua kubwa kupindukia siku mbili zilizopita nchini Libya yamesisitiza haja ya kampeni ya kimataifa ya Maonyo ya Mapema kwa Wote iliyozinduliwa na Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres mapema mwaka jana.   Na Leo, Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) limezindua miongozo miwili iliyoundwa ili kuimarisha juhudi za kuzuia watu kujiua. Mmoja ni muongozo ulioboreshwa kwa ajili wataalamu wa vyombo vya habari na pili Muhtasari wa sera kuhusu vipengele vya afya vya kuyafanya majaribio ya kujiua na kujiua yasiwe jinai.Na mashinani leo Aziza Harba Idriss, mkimbizi kutoka Sudan ambaye alikimbilia nchi jirani ya Sudan Kusini kupitia njia hatarishi akisaka usalama anasimulia changamoto alizozipitia.Mwenyeji wako ni Flora Nducha, karibu!
9/12/20230
Episode Artwork

Türk: Haki ya makazi bado ni ndoto kwa wengi duniani

Mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu umeanza hii leo huko Geneva, Uswisi ambapo Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Volker Türk pamoja na mambo mengine amesisitiza suala la makazi kama moja ya haki za msingi za binadamu na haki inayopigiwa chepuo pia kwenye malengo ya maendeleo endelevu, SDGs. Mwakilishi wa kudumu wa Gambia kwenye ofisi za Umoja wa Mataifa huko Geneva, Uswisi, anaomba wajumbe kusimama kwa dakika moja kukumbuka watu waliopoteza maisha kufuatia tetemeko kubwa la ardhi lililokumba Morocco usiku wa kuamkia jumamosi. Kisha hotuba zikaanza na ulipowadia wakati wa Kamishna Mkuu Volker Türk, yeye amemulika masuala mbali mbali ikiwemo mahitaji na haki za watu kuishi kwenye mazingira bora ya maisha, makazi na kupata chakula na huduma za afya wakati wowote wanapohitaji, hivyo vyote vikisalia ndoto kwa wengi. Bwana Türk  amesema “lakini katika nchi nyingi, makazi, mathalani yanaonekana kama bidhaa ya uwekezaji kulingana na mahitaji ya soko: mchezo wa soko la fedha badala ya kuwa haki ya msingi. Janga la kuweko kwa makazi yenye unafuu linabinya vipato vya familia, linaongeza kasi ya ukosefu usawa, linadhuru afya ya watoto, linafanya vijana wawe hohehahe, na kuchochea zaidi janga la watu kutokuwa na makazi. Janga hili limesambaa pia katika nchi zilizoendelea.” Bwana Türk  amesema anaangazia zaidi janga la watu kukosa makazi au pahala pa kuishi kwa sababu suala hilo ndio msingi wa mkataba wa kijami. Amesema nchini Marekani, zadi ya watu 500,000 hawakuwa na makazi mwezi Januari mwaka 2022, kwa mujibu wa takwimu rasmi, ambapo asilimia 40 kati yao hao ni watu wenye asili ya Afrika, ambao ni asilimia 12 ya wanachi wote wa Marekani. Bwana Türk amekumbusha kuwa kutokomeza ukosefu wa makazi na kuhakikisha upatikanaj wa makazi nafuu vimejumuishwa kwenye malengo ya maendleeo endelevu na pia ni haki ya msingi wa binadamu.  Ametoa wito kwa nchi zote hususan zilizoendelea kuelekeza rasilimali ili kukidhi haki hiyo kwa mujibu wa sheria za kimataifa. 
9/11/20230
Episode Artwork

Mradi wa UNCDF Tanzania wawezesha kaya kuondakana na nishati hatarishi ya kupikia

Nchini Tanzania kuna kaya nyingi ambazo zinatumia mkaa, kuni na mafuta ya taa kama tegemeo kuu la mapishi ya nyumbani, nishati ambazo si rafiki sio tu kwa mazingira bali pia afya ya mamilioni ya binadamu. Lakini sasa kuna mabadiliko,wakati huu ambapo Umoja wa Mataifa unapigia chepuo nishati jadidifu na salama; wakati huu ambapo pia wakuu wa nchi watakutana jijini New York, Marekani kutathmini hatua zipi zimechukuliwa kubadili mwelekeo wa mabadiliko ya tabianchi. Shukrani kwa mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa la maendeleo ya mitaji, UNCDF uitwao COOK FUND unaofadhiliwa na Muungano wa Ulaya. Mradi huu unalenga kuchangia katika ahadi za Tanzania katika kukabili athari za mabadiliko ya tabianchi kwa kuongeza idadi ya watu wanaopata nishati safi ya kupikia hadi asilimia 80 ifikapo mwishoni mwa mwaka huu wa 2023. Evarist Mapesa anafafanua kwenye makala hii.. 
9/11/20230
Episode Artwork

11 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki ya makazi na mkutano wa G20.  Makala na mashinani tunakupeleka nchini Tanzania, kulikoni?Mkutano wa 54 wa Baraza la Umoja wa Mataifa kuhusu haki za binadamu umeanza hii leo huko Geneva, Uswisi ambapo Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu kwenye Umoja wa Mataifa Volker Türk pamoja na mambo mengine amesisitiza suala la makazi kama moja ya haki za msingi za binadamu na haki inayopigiwa chepuo pia kwenye malengo ya maendeleo endelevu, SDGs.Mkutano wa kila mwaka wa Kundi la Nchi 20 zenye Maendeleo Makubwa ya Kiuchumi Duniani (G20) umehitimishwa jana katika mji mkuu wa India New Delhi huku Umoja wa Mataifa ukiwa umekaribisha kupitishwa kwa Azimio la Viongozi wa Kundi hilo kukubali kujumuisha Muungano  wa Afrika (AU) kama mwanachama wake mpya wa kudumu.   Katika makala Evarist Mapesa kutoka Tanzania amefuatilia mradi wa shirika la Umoja wa Mataifa unaoleta majawabu ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi nchini Tanzania kwa kuwezesha kaya kutumia nishati jadidifu katika kupikia.Na mashinani tunasalia nchini Tanzania kusikia ni kwa jinzi gani mashirika wanasaidia wasichana waathririka wa mimba za utotoni kurejea shuleni na hatimaye kufikia ndoto zao.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
9/11/20230
Episode Artwork

African Union kukubaliwa katika G20 ni taswira ya kuongezeka kwa umuhimu wa Afrika kimataifa - Guterres

Mkutano wa kila mwaka wa Kundi la Nchi 20 zenye Maendeleo Makubwa ya Kiuchumi Duniani (G20) umehitimishwa jana katika mji mkuu wa India New Delhi huku Umoja wa Mataifa ukiwa umekaribisha kupitishwa kwa Azimio la Viongozi wa Kundi hilo kukubali kujumuisha Muungano  wa Afrika (AU) kama mwanachama wake mpya wa kudumu. "Hii ni taswira ya kuongezeka kwa ushawishi na umuhimu wa Afrika katika hatua ya kimataifa," alieleza Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres alisema kupitia Msemaji wake mara tu baada ya uamuzi huo wa G20 kuujumuisha muungano wa Afrika kama mwanachama wake wa kudumu na akaongeza kuwa, "Wakati sehemu kubwa ya usanifu wa kimataifa uliopo ulipojengwa, sehemu kubwa ya Afŕika ilikuwa bado inatawaliwa na ukoloni na haikuwa na fuŕsa ya kusikilizwa sauti zao. Hii ni hatua nyingine ya kurekebisha usawa huo." Baadhi ya viongozi wa Afrika haraka baada ya uamuzi huo walijitokeza kuonesha furaha yao ambapo kwa upande wake Rais wa Afrika Kusini Cyril Ramaphosa ambaye pia alihuduria mkutano huo aliandika katika ukurasa wake wa mtandao wa X akisema, "Tuna furaha kwamba G20 imekubali AU kama mwanachama wa G20. Mabadiliko ya tabianchi, uharibifu wa mazingira, matumizi yasiyo endelevu na uzalishaji na uhaba wa rasilimali ni changamoto zinazoweza kutatuliwa kwa pamoja na kwa mshikamano mkubwa." Naye Rais wa Kenya William Ruto akitumia pia ukurasa wake wa X aliandika, "Kenya inakaribisha kuongezwa katika G20 Muungano wa Afrika - bara linalokua kwa kasi zaidi duniani. Hii itaongeza sauti ya Afrika, kuonekana, na ushawishi katika jukwaa la kimataifa na kutoa jukwaa la kuendeleza maslahi ya pamoja ya watu wetu. Hii inaendana kikamilifu na maazimio ya Mkutano wa Afrika kuhusu Tabianchi uliokamilika hivi karibuni.” Katika Mkutano wa G20, chini ya Kauli Mbiu “Dunia Moja, Familia Moja, Mstakabali Mmoja,” masuala muhimu kama vile uhakika wa chakula, tabianchi na nishati, maendeleo, afya na digitali yalijadiliwa. 
9/11/20230
Episode Artwork

Dola Bil 360 zinahitajika kwa mwaka ili kufikia usawa wa kijinsia 2030

Takwimu mpya zilizokusanywa na mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa zimeonesha kuwa kuna haja ya uwekezaji wa ziada wa dola bilioni 360 kwa mwaka ili kufikia usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake ifikapo 2030. Hapo jana mchana kwa saa za New York Marekani shirika la Umoja wa Mataifa la UN WOMEN linalohusika na masuala ya wanawake na UNDESA ambayo ni Idara ya Umoja wa Mataifa ya uchumi na kijamii, walizindua ripoti yao ya kila mwaka ya Maendeleo kwenye Malengo ya Maendeleo Endelevu: Muhtasari wa jinsia 2023 inayotathimini namna malengo 17 ya maendeleo endelevu SDGs yanavyotekelezwa kwa kuzingatia usawa wa kijinsia.Utafiti wa mwaka huu ulihusisha nchi 116 pamoja na mambo mengine uliweka mkazo kwa wanawake wazee ambapo ripoti ilionesha kuwa kundi hilo ndani ya jamii linakabiliwa na viwango vikubwa si tu vya umasikini na kutokuwa na pensheni, bali pia ukatili, ikilinganishwa na wanaume wazee. Wakati huu ambapo utelekezaji wa SDGs umefika nusu ya muda uliopangwa kabla ya kufikia kilele hapo mwaka 2030, Naibu Mkurugenzi Mtendaji wa UN Women Bi. Sarah Hendriks anasema ripoti ya mwaka huu ni wito mkubwa wa kuchukua hatua. Bi. Hendriks aliongeza kuwa “ni lazima kwa pamoja na kwa dhamira ya dhati tuchukue hatua sasa kusahihisha changamoto zilizopo ili tuwe na ulimwengu ambao mwanamke na msichana wana haki sawa, fursa na uwakilishi. Ili kufikia hili, tunahitaji dhamira isiyoyumba, suluhu bunifu, na ushirikiano katika sekta zote na washikadau.”Ripoti hii imesisitiza hitaji la dharura la juhudi madhubuti za kuharakisha maendeleo kuelekea usawa wa Kihansi ifikapo mwaka 2030 na kueleza kwamba zaidi ya dola bilioni 360 kwa mwaka zinahitajika ili kufikia usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake katika malengo muhimu ya kimataifa.Pamoja kupigiwa chepuo kila kwenye majukwaa makubwa hususani ya wafanya maamuzi, pengo la kijinsia katika madaraka na nyadhifa za uongozi bado limekita mizizi, na, kwa kasi ya sasa ya maendeleo, ripoti imeeelza kizazi kijacho cha wanawake bado kitatumia wastani wa saa 2.3 zaidi kwa kila siku bila ujira wakati wakifanya kazi za nyumbani kuliko wanaume.Ripoti ya mwaka huu pia iliangazia suala la mabadiliko ya tabianchi na takwimu zilizokusanywa zimeonesha kuwa mabadiliko ya tabianchi yanaweza kusukuma hadi wanawake na wasichana milioni 158.3 katika umasikini. Idadi hiyo zaidi ya milioni 16 ikilinganishwa na wanaume na wavulana. Ripoti hiyo pia inajumuisha wito wa kuwa na mtazamo jumuishi na wa kiujumla, ushirikiano mkubwa kati ya wadau, ufadhili endelevu, na hatua za kisera kushughulikia tofauti za kijinsia na kuwawezesha wanawake na wasichana duniani kote, ikihitimisha kwamba kushindwa kuweka kipaumbele kwa usawa wa kijinsia sasa kunaweza kuhatarisha Ajenda nzima ya 2030 ya SDGs.
9/8/20230
Episode Artwork

08 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia habari za masikitiko kuhusu watototo katika migogoro nchini DRC. Pia tunamulika pengo katika usawa wa kijinsia.  Makala tunarejelea ufafanuzi wa ibara ya 9 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la haki za binadamu na mashinani tunakuletea ujumbe wa vijana kuhusu mabadiliko ya tabianchi.Ukatili dhidi ya watoto mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC umepindukia, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF nchini humo likitolea mfano watoto mapacha ambao hivi karibuni walikutwa wamefungwa mkanda wenye mabomu kiunoni ili yeyote atakayejaribu kuufungua uwezo kulipuka na kusababisha maafa.Takwimu mpya zilizokusanywa na mashirika mawili ya Umoja wa Mataifa zimeonesha kuwa kuna haja ya uwekezaji wa ziada wa dola bilioni 360 kwa mwaka ili kufikia usawa wa kijinsia na uwezeshaji wa wanawake ifikapo 2030.   Katika makala Anold Kayanda akizungumza na Jebra Kombole, Mwanasheria na Wakili kutoka TAnzania akifafanua Ibara ya 9 ya Tamko la Kimataifa la Haki za binadamu ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75 tangu lipitishwe.Na mashinani Balozi mwema wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto, UNICEF kutoka Uganda ni mmoja wa vijana ambao wanahudhuria Wiki ya Tabianchi ya Afrika nchini Kenya inayokunja jamvi hii leo, wiki iliyoambatana na Mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi, uliofunga pazia tarehe 6 mwezi huu wa Septemba nchini Kenya na anatoa ujumbe wa vijana.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/8/20230
Episode Artwork

Nchini DRC watoto wamefungwa mitego ya mikanda ya mabomu

Ukatili dhidi ya watoto mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC umepindukia, limesema shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF nchini humo likitolea mfano watoto mapacha ambao hivi karibuni walikutwa wamefungwa mkanda wenye mabomu kiunoni ili yeyote atakayejaribu kuufungua uwezo kulipuka na kusababisha maafa.Ni Grant Leaity mwakilishi wa UNICEF nchini Jamhuri ya kidemokrasia ya Congo, DRC akieleza kuwa hivi karibuni alitembelea kituo kimoja jimboni Kivu Kaskazini kinachohifadhi watoto walioachiliwa huru na vikundi vilivyojihami na kukuta watoto wawili mapacha wenye umri wa mwaka mmoja waliokuwa wametelekezwa kwenye Kijiji wakiwa na mkanda kiunoni wenye mabomu. Amewaambia waandishi wa Habari mjini Geneva USwisi hii leo kuwa kitendo hicho ni miongoni mwa ukatili dhidi ya watoto nchini DRC na kwamba ni taifa lenye matukio makubwa ya ukatili dhidi ya watoto yaliyothibitishwa na Umoja wa Mataifa. Katika kipindi cha mwaka mmoja, ongezeko la ghasia mashariki mwa DRC limesababisha ukimbizi mkubwa zaidi Afrika, watoto zaidi ya milioni 2.8 wakibeba mzigo wa janga hilo. Bwana Leity anasema niko hapa leo, natumai nitapaza sauti nisikike. Kila siku watoto wanabakwa, na wanauawa, wanatekwa, wanatumikishwa vitani na wanatumiwa na makundi yaliyojihami na tunajua ripoti tulizo nazo ni kidogo kulinganisha na matukio halisi.” Alipoulizwa nini kilitokea baada ya kubaini watoto hao, Mwakilishi huyo wa UNICEF DRC amesema “tuliwasiliana na wenzetu wataalamu wa kutegua mabomu ambao walikuja na kuweza kuondoa mtego huo wa mabomu kwa usalama.” Amesema matumizi ya vilipuzi vya kutengeneza yanazidi kuongezeka DRC. na hivyo UNICEF inatoa wito kwa hatua zichukuliwe ili kumaliza mzozo na familia zirejee nyumbani. Pamoja na ghasia ya kiwango cha juu dhidi ya watoto, Afisa huyo amesema maisha ya watoto mashariki mwa DRC yanatishiwa na milipuko ya magonjwa na utapiamlo. Takribani watoto milioni 1.2 wenye umri wa chini ya miaka mitano wanakabiliwa na utapiamlo uliokithiri kwenye eneo hilo. UNICEF inasema dunia inawaangusha watoto wa DRC kwani imewasahau, ikisema kuna matumaini lakini bado msaada unahitaji kwenye maeneo mawili. Mosi, rasilimali kuweza kukidhi mahitaji ya kibinadamu ya watoto inahitaji dola milioni 400. Pili ni utashi wa kisiasa kumaliza mzozo unaoendelea DRC na hivyo inatoa wito kwa serikali, mataifa ya Afrika na jamii ya kimataifa kushirikiana kusaka suluhisho la amani ya kudumu kwenye janga hilo ili familia zirejee nyumbani. 
9/8/20230
Episode Artwork

Methali: "Kivuli cha fimbo hakimfichi mtu jua"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali "KIVULI CHA FIMBO HAKIMFICHI MTU JUA"
9/7/20230
Episode Artwork

07 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Magavana Dkt. Wilber Ottichilo wa Kaunti ya Vihiga na Gavana wa Kaunti ya Narok, Patrick Ole Ntutu hivi karibuni walipohudhuria Jukwaa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu SDGs lijulikanalo kama HLPF hapa katika makao makuu ya Umoja wa Mataifa jijini New York, Marekani, waliketi na Flora Nducha wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ili waeleze mipango yao ya kutimiza Malengo ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu, SDGs katika majimbo yao huko nchini Kenya. Pia tunakuletea habari kwa fupi kuhusu Akili mnemba au AI, Siku ya Polisi na mkutano wa ASEAN.  Katika kujifunza lugha ya kiswahili tunakuletea maana ya methali KIVULI CHA FIMBO HAKIMFICHI MTU JUA.Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amezipongeza nchi za kusini-mashariki mwa Asia kwa mchango wake wa kujenga maelewano duniani kote wakati huu ambapo ulimwengu umegubikwa na mivutano ya kisiasa na kijiografia.Ikiwa leo ni siku ya Kimataifa ya Ushirikiano na Polisi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amewatumia salamu za pongezi polisi ulimwenguni kote kwa kujitolea kwao kuhakikisha jamii inakuwa na amani, usalama na haki. Amewakumbusha pia upolisi unaolenga katika kusaka suluhisho za kijamii husaidia zaidi kujenga uaminifu na kuboresha usalama.  Na tuhitimishe na masuala ya teknolojia, wakati muhula mpya wa masomo ukianza maeneo mengi duniani, Shirika la Umoja wa Mataifa la Elimu Sayansi na Utamaduni UNESCO limetoa muongozo wenye vipengele saba unaotaka nchi kudhibiti matumizi ya akili mnemba  au -AI mashuleni.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili Dkt Mwanahija Ali Juma, Katibu Mkuu wa Baraza la Kiswahili, Zanzibar nchini Tanzania, BAKIZA anachambua methali KIVULI CHA FIMBO HAKIMFICHI MTU JUA.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
9/7/20230
Episode Artwork

Amini Sayansi na sikilizeni sauti za watoto na vijana - Vijana katika mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi

Mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi uliokunja chamvi hii leo jijini Nairobi nchini Kenya, umeleta pamoja vijana wanaharakati wa tabianchi kutoka nchi zote barani Afrika.  Stella Vuzo wa Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS Nairobi amekutana na baadhi ya vijana hao kandoni mwa mkutano huo na wanaeleza mawazo yao na walichojifunza.
9/6/20230
Episode Artwork

Azimio la Nairobi kuhusu mabadiliko ya tabianchi lapitishwa na viongozi wa Afrika

Mkutano wa siku tatu wa viongozi wa Afrika kuhusu tabianchi umekunja jamvi hii leo huko Nairobi Kenya kwa viongozi hao kupitisha Azimio la Nairobi kuhusu mabadiliko ya tabianchi likiwa na vipengele 10 vya hatua za kuchukua ikiwemo wito kwa viongozi wa dunia kutambua kuwa uwepo wa shughuli za kiuchumi zitoazo kiwango kidogo cha hewa ya ukaa, ni fursa pia ya kuchangia katika usawa na ustawi wa watu wote duniani. Azimio hilo limepitishwa kwa kutambua mambo kadhaa ikiwemo ripoti ya IPCC ya kwamba joto linaongezeka kwa kasi kubwa barani Afrika kuliko mabara mengine na iwapo hatua hazitachukuliwa, mabadiliko ya tabianchi yatakuwa na madhara makubwa kwa uchumi wa Afrika na jamii zake, halikadhalika kukwamisha ukuaji na ustawi wa watu wake.  Hivyo azimio hilo linakaribisha wadau wa maendeleo kutoka pande zote usaidizi wao wa kiufundi na kifedha kwa Afrika ili kusongesha matumizi endelevu ya maliasili zilizomo kwenye bara hilo ili kutoa kiwango kidogo cha hewa ya ukaa na hivyo kuchangia katika upunguzaji wa hewa hiyo duniani.   Halikadhalika linataka hatua za kina dhidi ya janga la madeni ili kuepusha nchi kutumbukia kwenye mtego wa kushindwa kulipa na badala yake kuwekwe mfumo unaokidhi mahitaij ya nchi zinazoendelea katika kupata fedha za maendeleo na hatua kwa tabianchi.  Azimio linapendekeza kuanzishwa kwa mfumo mpya wa ufadhili unaokidhi mahitaji ya Afrika, ikiwemo marekebisho ya mfumo wa madeni na msamaha kupitia kuanzishwa kwa Chata ya kimataifa ya ufadhili kwa tabianchi kupitia Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa ifikapo mwaka 2025.  Pamoja na kuamua kuwa Azimio hili litakuwa msingi wa msimamo wa mchakato wa Afrika kwa tabianchi kuelekea mkutano wa 28 wa mabadiliko ya tabianchi, COP28 baadaye mwaka huu, azimio hilo pia limeitaka Kamisheniya Muunganowa Afrika kuandaa mpango wa utekelezaji na kufanya Mabadiliko ya Tabianchi kuwa maudhumi ya Muungano wa Afrika kwa mwaka 2025 au 2026.  Mkutano huo wa siku tatu umemazilika leo lakini Wiki ya Tabianchi Afrika iliyoanza tarehe 4 itamalizika tarehe 8 mwezi huu wa Septemba. 
9/6/20230
Episode Artwork

06 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia Mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi nchini Kenya leo hii ikifunga pazia. Pia tunamulika kazi za walinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR. Makala na mashinani tunasalia nchini Kenya katika mkutano wa Afrika kuhusu kukuletea ujumbe wa vijana.Mkutano wa siku tatu wa viongozi wa Afrika kuhusu tabianchi umekunja jamvi hii leo huko Nairobi Kenya kwa viongozi hao kupitisha Azimio la Nairobi kuhusu mabadiliko ya tabianchi likiwa na vipengele 10 vya hatua za kuchukua ikiwemo wito kwa viongozi wa dunia kutambua kuwa uwepo wa shughuli za kiuchumi zitoazo kiwango kidogo cha hewa ya ukaa, ni fursa pia ya kuchangia katika usawa na ustawi wa watu wote duniani. Walinda amani wa Tanzania wanaohudumu chini ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati MINUSCA wametoa misaada mbalimbali kwa jamii wanazo zilinda.   Katika Makala Stella Vuzo wa Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS Nairobi anawapa fursa vijana wengine waliohudhuria mkutano huo uliofikia tamati leo kueleza mawazo yao na walichojifunza.Na katika mashinani Mohammed Abbas, Mwanaharakati wa mazingira kutoka Tanzania ambaye pia ni mmjoa wa vijana waliohudhuria Mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi anatoa ujumbe wake akizungumza na Kituo hicho hicho cha Habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS Nairobi kandoni mwa mkutano huo.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
9/6/20230
Episode Artwork

Walinda amani kutoka Tanzania TANBAT 6 wafanya usafi na kutoa msaada wa vifaa tiba CAR

Walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutokaTanzania wanaohudumu chini ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, MINUSCA wametoa misaada mbalimbali kwa jamii wanazolinda kama moja ya sehemu ya kuimarisha utangamano na maelewano kati yao na jamii wanayoilinda. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Kapten Mwijage Inyoma.  Taarifa ya Kapten Mwijage Inyoma  Wanajeshi wa TANBAT 6 ambacho ni Kikosi cha sita cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania wamefanya usafi na kukabidhi baadhi ya vifaa tiba Kwa Mganga Mkuu wa hospitali ya Mkoa wa Mambéré-Kadéï ikiwa ni namna mojawapo ya kusherehekea kilele cha maadhimisho ya kumbukumbu ya miaka 59 ya kuundwa Kwa Jeshi la Ulinzi la wananchi Tanzania JWTZ, ambalo limekuwa mstari wa mbele kuchangia kwenye ulinzi wa amani wa Umoja wa Mataifa.  Bi. Atheo Mathible ni Mkuu wa hospitali hiyo. “Nawapongeza walinda Amani wa jeshi laTanzania kwa jeshi lao kutimiza miaka 59 Kwa kweli si kazi ndogo toka mwaka 1964 mpaka sasa likiwa imara, lakini pia tunawashukuru kutumia maadhimisho hayo kusaidia jamii Kwa kufanya usafi eneo la hospitali yetu”  Akihitimisha maadhimisho hayo Mkuu wa kikosi TANBAT6 Luten kanali Ramadhani Shaaban Ramadhani anasema, “Ujumbe wangu kwa wanajeshi wenzangu hasa wanaohudumu katika Jamhuri ya Afrika ya Kati kufanya kazi kwa bidhii na weledi wa hali ya juu ili kuweza kufikia lengo kuu la MINUSCA ambalo ni amani ya kudumu” 
9/6/20230
Episode Artwork

05 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mada kwa kina ikimulika Siku ya kimataifa ya hisani  au kuwaonea huruma wagonjwa na maskini. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo yanayojiri katika mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi nchini Kenya na ujumbe wa Rais wa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Csaba Kőrösi akitamatisha awamu yake hii leo. Katika mashinani tunakupeleka nchini DRC, kulikoni?Mkutano wa Afrika kuhusu tabianchi ukiingia siku ya pili hii leo huko Nairobi, Kenya, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema bara la Afrika lina asilimia 30 ya akiba ya madini ambayo ni muhimu katika kuzalisha nishati jadidifu na teknolojia zinazotoa kiwango kidogo cha hewa ya ukaa, rasilimali ambazo zinaweza kuifanya Afrika kuwa kitovu cha nishati jadidifu duniani iwapo zitatumika kiuendelevu na kwa haki.Tukisalia kwenye mkutano huo, mmoja wa washiriki ni Dkt. Victor Yamo kutoka shirika la World Animal Protection la kulinda haki za wanyama na anasisitizia umuhimu wa kuwa na mifumo endelevu ya ufugaji.   Na Rais wa mkutano wa 77 wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Csaba Kőrösi ametamatisha awamu yake hii leo kwa kuwaeleza wajumbe kuwa mivutano ya kisiasa katu  haiwezi kuisha duniani, lakini mivutano hiyo ipatiwe suluhu si kwa mmoja kushinda na mwingine kupoteza bali kwa kuridhiana kupitia maazimio yanayopitishwa na Baraza hilo.Na mashinani tutakupeleka nchini Jamhuri ya Kiemokrasia ya Congo, DRC ambapo mizozo na ongezeko la idadi ya watu wanaokimbia makazi yao mashariki mwa nchi hiyo linawafanya watoto kuingia katika janga kubwa la kipindupindu kuwahi tokea tangu mwaka 2017”.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
9/5/20230
Episode Artwork

Ndoto za kuwa daktari au Mwalimu Mkuu kwa watoto hawa zitatimia?

Ijapokuwa ni wakimbizi wa ndani na wanaishi kwenye kituo cha kuhifadhi wakimbizi wa ndani cha Bushagara, mjini Goma, jimboni Kivu Kaskazini, mtoto Irene anataka kuwa daktari, na Christelle anataka kuwa Mwalimu Mkuu. Ingawa hivyo, elimu bado ni changamoto kubwa kwa watoto milioni 2.4 wakimbizi wa ndani nchini DRC hususan majimbo ya Kivu Kaskazini, Ituri na Kivu Kusini ambao wanahitaji elimu kwa haraka. Hoja ni iwapo ndoto zao hizo zitatimia au ndio zitapeperushwa na vita inayoendelea nchini mwao na kuwafurusha kila uchao? Assumpta Massoi kupitia Makala hii iliyoandaliwa na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya dharura anakuletea simulizi za watoto hao wakiwa Bushagara. 
9/1/20230
Episode Artwork

Nchini Kenya mkutano wa Mabadiliko ya tabianchi utaanza Septemba 4

Viongozi wa Afrika wanatarajiwa kukutana jijini Nairobi, kenya wiki ijayo kwa ajili ya mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi ambako watajadili njia mbalimbali za kupunguza utoaji wa gesi chafuzi huku wakija na mbinu za kukabiliana na athari za hali ya hewa. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Thelma Mwadzaya. Taarifa ya Thelma Mwadzaya akiwa jijini Nairobi inafafanua zaidi.Mkutano huo unaoanza tarehe 04 mpaka 6 Septemba mwaka huu unawaleta pamoja watunga sera, viongozi wafanyabiashara na wanaharakati wa mazingira kutoka kila pembe ya bara la Afrika. Mratibu Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Kenya Stephen Jackson akizungumzia mkutano huo ulioandaliwa na Umoja wa Mataifa kwa kushirikiana na Muungano wa Afrika na Serikali ya Kenya anaeleza sababu za mkutano huo kufanyikia nchini Kenya. “Kenya ipo mstari wa mbele katika kuathirika na changamoto ya Mabadiliko ya Tabia Nchi, Kenya ipo hatua ya mbele katika kupendekeza suluhu. Hii ni sawa kwa bara la Afrika. Afrika ndilo bara litakalotupa suluhu kuhusiana na tatizo hili la Mabadiliko ya Tabia Nchi. Afrika ina pafu la pili la dunia katika msitu mkubwa nchini Congo wenye hulka ya kuwa na mvua za mara kwa mara.  Afrika inautajiri mkubwa wa dunia wa rasilimali za nishati jadidifu. Kenya, ninapofanyia kazi, tayari ipo katika ngazi kubwa ya kutumia asilimia 93 ya nishati ya umeme unozalishwa na nishati jadidifu. Afrika ina sehemu kubwa ya ardhi asilia yenye uwezo wa kuilisha dunia. Kwa sababu hizi zote, Afrika ndiyo mahala panapofaa kupatia suluhu kuhusiana na janga la Mabadiliko ya Tabia Nchi. Na Kenya ni miongoni mwa nchi zinazoongoza kubadili mitizamo.“Mratibu Mkaazi huyu anaeleza pamoja na kuwa na suluhu lakini Afrika inahitaji ufadhili wa kifedha, “Tunahitaji uwezeshwaji wa kifedha wenye masharti nafuu ili kuliwezesha bara la Afrika kutatua janga la Mabadiliko ya Tabia Nchi linalolikabili bara hili ili pia tutatue tatizo la dunia nzima. Hivi sasa hakuna fedha na ambapo fedha zikikosekana gharama zinakuwa ni za juu sana. Hivyo maono ya Rais Ruto kuhusu Kilele cha Mkutano huu na maono ya Umoja wa Afrika kuhusiana na bara hili kuhusu Mkutano huu wa Bara la Afrika ni kwenda mbali zaidi ya kuangalia ajenda ya upotevu na uharibifu na agenda kuhusiana na uwezeshwaji ili kukabiliana na janga hili la mabadiliko ya `tabia nchi. Ajenda ambazo bado zinabaki kuwa ni za umuhimu sana na na kuangalia ni jinsi gani tutashirikiana kuchanga fedha nyingi kwa Pamoja ili kuleta suluhu za kudumu za afrika katika soko la dunia.”Mkutano huu umeundwa rasmi ili kuongeza kasi ya ushawisi kabla ya viongozi hao kushiriki katika Mkutano wa Umoja wa Mataifa wa Mabadiliko ya Tabianchi COP28 huko Dubai baadae mwaka huu.
9/1/20230
Episode Artwork

01 SEPTEMBA 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mabadiliko ya tabianchi na malelengo ya maendeleo endelevu kupitia mchezo wa mpira wa miguu. Makala tutaelekea nchini DRC kusikia simulizi ya wakimbizi na mashinani tunakupeleka nchini Tanzania kusikia ni kwa vipi wanawake wameweza kufanya kazi zao na kunyonyesha watoto wao ipasavyo.Viongozi wa Afrika wanatarajiwa kukutana jijini Nairobi, kenya wiki ijayo kwa ajili ya mkutano wa Mabadiliko ya Tabianchi ambako watajadili njia mbalimbali za kupunguza utoaji wa gesi chafuzi huku wakija na mbinu za kukabiliana na athari za hali ya hewa.Mwaka jana 2022 mwezi Julai, katika siku ya kwanza ya Michuano ya Mpira wa Miguu ya Wanawake Barani Ulaya chini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani humo (UEFA Women's EURO 2022), Umoja wa Mataifa uliitumia siku hiyo kuzindua mradi wa ‘Football for the Goals’ yaani Mpira wa Miguu kwa ajili ya Malengo ukiwa ni mpango mpya wa Umoja wa Mataifa ambao unatoa jukwaa kwa jumuiya ya soka duniani kujihusisha na kuhamasisha Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs). Nchi ziliitikia na mradi huo unaendelea duniani kote.   Makala tunakupeleka nchiniJamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC kusikiliza simulizi ya watoto wawili wakimbiziwa ndani juu ya kile wanachopitia sasa, ndotoyao na watamanicho kukipata hivi sasa. Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi katikamakala hii iliyofanikishwa na Ofisi ya Umojawa Mataifa ya uratibu wa misaada ya dharura, OCHA nchini DRC.Na mashinani hivi karibuni katika maadhimisho ya wiki wa unyonyeshaji mtoto maziwa ya mama, Umoja wa Mataifa ulithirihirisha kwamba kunyonyesha si tu jukumu la mama pekee, bali ni jukumu la kila mmoja wetu kuhakikisha tunaheshimu jitihada za mama kunyonyesha kwa amani, na Lilian Nyachama, mfanyakazi wa kuchuna majani chai kutoka Tanzania anatoa shuhuda.”.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
9/1/20230
Episode Artwork

Global Youth Forum  na UNIS Nairobi watekeleza mradi wa ‘Football for the Goals’ kwa vitendo

Mwaka jana 2022 mwezi Julai, katika siku ya kwanza ya Michuano ya Mpira wa Miguu ya Wanawake Barani Ulaya chini ya Shirikisho la Mpira wa Miguu Barani humo (UEFA Women's EURO 2022), Umoja wa Mataifa uliitumia siku hiyo kuzindua mradi wa ‘Football for the Goals’ yaani Mpira wa Miguu kwa ajili ya Malengo ukiwa ni mpango mpya wa Umoja wa Mataifa ambao unatoa jukwaa kwa jumuiya ya soka duniani kujihusisha na kuhamasisha Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs). Nchi ziliitikia na mradi huo unaendelea duniani kote.  Peter Omondi kutoka shirika la vijana la Global Youth Forum nchini Kenya ni mmoja wa vijana ambao mapema mwezi huu kwa kushirikiana na Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa, UNIS Nairobi waliandaa mechi ya mpira wa miguu iliyohusisha zaidi ya vijana 100 katika Kaunti ya Siaya ili kusongesha Malengo ya Maendeleo Endelevu.   Omondi Peter akihojiwa na Kituo cha habari cha Umoja wa Mataifa Nairobi Kenya anaeleza ushiriki wao katika mradi huu akisema, “Kulingana na ripoti, mambo ya Malengo ya Maendeleo Endelevu yanafaa yazingatiwe kila mahali kuhakikisha kila mtu katika ulimwengu anajumuika katika kuendeleza hii miradi ya SDGs.” “Huu mradi (Mpira wa Miguu kwa ajili ya Malengo) ,” Kijana huyo kutoka shirika la vijana la Global Youth Forum nchini Kenya anaendelea kueleza, “inahakikisha kujumuisha wachezaji wote katika michezo ya mpira, kuwa pamoja, na kuunganisha vijana wote, wazee na akina mama kuja pamoja.” Omondi Akieleza kitu kilichomfurahisha anasema ni watu kuja pamoja na hii michezo kuandaliwa katika miji iliyoko ndani au pembezoni na hivyo watu wa vijijini kushiriki katika mazungumzo ya Malengo ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu. “Kama kijana ningependa kuhamasisha vijana wenzangu pale nyumbani na katika maeneo ya ndani kwenye jamii waendelee kujumuika kwa ajili ya SDGs. Hiyo yote itahakikisha kwamba hakuna aliyeachwa nyuma katika haya mazungumzo ya Malengo ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo Endelevu.” Anahitimisha kijana Omondi Peter.  
9/1/20230
Episode Artwork

Methali: “Lakesho huonekana leo ila la jana halipingi la leo.”

Hii leo katika kujifunza Lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “La kesho huonekana leo ila la jana halipingi la leo.”
8/31/20230
Episode Artwork

31 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo mradi wa msaada wa maendeleo ya biashara ndogo-ndogo na za kati wa Benki ya Dunia, unaoendeshwa na mshirika wake, shirika la Umoja wa Mataifa la masuala ya wanawake, UN Women, unaaminika kuleta manufaa mengi katika maeneo ya mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo Siku ya Kimataifa ya Watu wa Asili ya Afrika na afya nchini Yemen. Katika kujifunza Lugha ya Kiswahili, Dkt. Josephat Gitonga anafafanua maana ya methali “Lakesho huonekana leo ila la jana halipingi la leo.”Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa ajili ya Siku ya Kimataifa ya Watu wa Asili ya Afrika inayoadhimishwa leo amehimiza Mataifa kuchukua hatua madhubuti, kwa ushirikishwaji kamili wa watu wa asili ya Afrika na jamii zao, kukabiliana na aina za zamani na mpya za ubaguzi wa rangi; na kuondoa ubaguzi wa rangi wa kimuundo na kitaasisi uliokita mizizi na kupaza sauti bila kuchoka dhidi ya mawazo yote ya ubora wa rangi  ili kukomboa jamii zote kutoka kwenye balaa la ubaguzi wa rangi.”   Wakati huo huo, Mshauri Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu kupinga ubaguzi pahala pa kazi, Mojankunyane Gumbi akizungumza kuhusu siku hii ya Kimataifa ya Watu wa Asili ya Afrika amesema Timu ya kupinga Ubaguzi inapenda kutambua michango ya waafrika walioko ughaibuni.   Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Duniani (WHO) limeeleza leo wasiwasi wake kuhusu kuongezeka kwa maambukizi ya ugonjwa wa surua na rubela miongoni mwa watoto nchini Yemen. Hadi kufikia tarehe 31 mwei jana, Julai, mwaka huu, idadi ya wanaoshukiwa kuwa na surua na rubela nchini Yemen imefikia karibu watu 34,300 na vifo 413, ikilinganishwa na wagonjwa 27,000 na vifo 220 vilivyohusishwa na magonjwa hayo mwaka 2022.Katika kujifunza Lugha ya Kiswahili, mchambuzi wetu Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Lakesho huonekana leo ila la jana halipingi la leo.”.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/31/20230
Episode Artwork

Watoto Kakuma wafikishiwa msaada wa kuwanusuru na utapiamlo

Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya watoto UNICEF nchini Kenya linatekeleza mradi wa matibabu kwa watoto wenye utapiamlo, mradi ambao umeanza kuzaa matunda kwani afya za watoto zimeanza kuimarika. Leah Mushi na taarifa zaidi.Sabina Naboi mwenye umri wa miaka 28 mama wa watoto watatu, alizaliwa ndani ya kambi ya Kakuma iliyoko katika kaunti ya Turkana nchini Kenya.Misimu sita mfululizo ya ukame uliochochewa na mabadiliko ya tabianchi umekuwa na athari hasi hususan kwenye suala la lishe kwa watu wengi katika kaunti hii ya Turkana na mmoja wao ni Sabina ambaye mtoto wake mwenye umri chini ya miaka mitano alipata utapiamlo.Changamoto alizopitia SabinaSabina anasema,“sisi tunategemea chakula hiki cha msaada wa wakimbizi ambacho tunakipata mara moja kwa mwezi na huwa hatuwezi kufika nacho mwisho wa mwezi mwingine. Wakati nimejifungua binti yangu analia alikuwa sawa lakini alipofika miezi sita akaanza kuumwaumwa mara kuharisha yani afya yake haikuwa sawa. Nilikuwa nampeleka hospitali anapewa dawa lakini mtoto alikuwa anakonda sana.”Mtoto wa Sabina aligundulika kuwa na utapiamlo na hivyo akapewa lishe maalum kwa ajili ya watoto wenye utapiamlo.Vicent Opinya ni meneja wa programu ya afya katika kambi ya Kakuma anasema, “tunahudumia takribani watu 246,000 ambapo wahudumu wetu wa afya wanawapatia matibabu ya chakula maalum kilicho tayari kwa ajili ya kutibu watoto walio na utapiamlo mkali bila shida nyingine yoyote katika vituo vyetu vya wagonjwa wanje.”Mgao wa fedha taslimu, lishe na huduma ya matibabuChini ya ufadhili wa Muungano wa Ulaya UNICEF na wadau wake wanatoa lishe, msaada wa fedha taslimu na matibabu kwa watoto wenye upatiamlo waliochini ya umri wa miaka mitano kwa wakazi wa Kalobeyei pamoja na Kambi ya wakimbizi ya Kakuma. Kwa sasa watoto zaidi ya 22,000 wamefikiwa na misaada hiyo ya kuokoa maisha.Susan Jobando ni Afisa afya wa UNICEF nchini Kenya na anasema mbali na kusaidia serikali ya Kaunti ya kakuma katika masuala ya afya kwa watoto pia wanawajengea uwezo wahudumu wa afya na kuimarisha mfumo wa afya na kuhakikisha kuna mnyororo thabiti wa usambazaji matibabu ya utapiamlo kuweza kumfikia kila mtoto mwenye uhitaji.’Tukiwa na wadau kama ECHO tunaweza kuwafikia watoto wengi zaidi sio tu kama mkakati wa matibabu bali pia ni mkakati wa kujikinga ili waweze kukabiliana vyema na athari za mabadiliko ya tabianchi.”Tabasamu sasa kwa SabinaSasa Sabina ana furaha kwa kuwa mtoto wake ameanza kupata nafuu na anasema, “vile ninaona afya yake iko sawa hata mimi hufurahi. Na ninaamini mwezi ujao mwili wake utarudi kama zamani (atanenepa) na utaendelea kuongezeka mpaka atoke kwenye hiyo programu ( ya kula chakula cha watoto wenye utapiamlo) na aende kwenye programu nyingine . Kila mama anataka mtoto wake awe na afya nzuri, awe na mwili mzuri.”
8/30/20230
Episode Artwork

Msaada kutoka TANZBATT 10 umenusuru wagonjwa wanaokabiliwa na njaa

Mgeni njoo mwenyeji apone ni methali iliyodhihirisha huko eneo la Mbau jimboni Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC baada ya walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania kikosi cha 10, TANZBATT 10 walipotembelea hospitali ya La Grace kutoa msaada si tu wa chakula bali pia dawa. Walinda amani hawa wanahudumu kwenye kikosi cha kujibu mashambulizi, FIB cha ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO. Mwenyeji wetu ni Afisa Habari wa TANZBATT 10, Luteni Abubakari Muna ambapo katika makala hii Meja Neema Neligwa mwakilishi wa Kamanda kikosi cha TANZBATT 10, Luteni Kanali John Peter Kalabaka anaanza kwa kufafanua kilichojiri kwenye ziara hiyo.
8/30/20230
Episode Artwork

Wataalamu wa haki waongeza sauti kwenye suala la utoweshwaji wa watu

Wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa na wa kanda mbalimbali ikiwemo Afrika na Asia wameyasihi mataifa yote kutoa haki kwa waathirika wa utoweshwaji wa watu, ikiwa ni pamoja na mtu yeyote ambaye amepata madhara kama matokeo ya moja kwa moja ya utoweshwaji wa watu. Anold Kayanda na maelezo zaidi. "Kuhakikisha haki ya waathiriwa kunahitaji kuchukua hatua zote muhimu ili kufichua ukweli," wataalam hao wamesema katika taarifa walioitoa jana mjini Geneva, Uswisi kuelekea leo ambayo ni Siku ya Kimataifa ya Waathiriwa wa Kutoweshwa kwa watu.  Wataalamu hao wanasema kwamba kuhakikisha upatikanaji wa kutosha wa haki na uwajibikaji ipasavyo kwa wahalifu katika ngazi zote za mnyororo mzima wa amri ni muhimu ili kuwasilisha ujumbe mzito kwamba kutowesha watu ni uhalifu chini ya sheria ya kimataifa ya haki za binadamu, hairuhusiwi au kuvumiliwa. Kwa mujibu wa Azimio la Ulinzi wa Watu Wote dhidi ya Kutoweshwa kwa Watu, lililotangazwa na Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa katika azimio lake la 47/133 la tarehe 18 Desemba 1992 kutoweshwa ni pindi "Watu wanakamatwa, kuwekwa kizuizini au kutekwa nyara bila hiari yao au kunyimwa uhuru wao kwa njia nyingine na maafisa wa matawi au ngazi mbalimbali za Serikali, au na makundi yaliyopangwa au watu binafsi kwa niaba ya, au kwa msaada, moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja, ridhaa au kukubaliana na Serikali, ikifuatiwa na kukataa kufichua hatima au mahali walipo watu waliokamatwa au kukataa kukiri kunyimwa uhuru wao, jambo ambalo linawaweka watu hao nje ya ulinzi wa sheria." Wataalamu wa haki za binadamu wanasema "Katika mapambano yao ya kila siku ya haki, waathiriwa mara nyingi wanakabiliwa na vitisho, kisasi na unyanyapaa. Hili lazima likomeshwe, na waathiriwa lazima wapate msaada wa kisheria bila malipo ili kuhakikisha kuwa hali yao ya kifedha haiwazuii kutafuta haki na upatikanaji wa haki lazima usiwe wa kinadharia tu bali uhakikishwe kivitendo kupitia hatua madhubuti zinazokuza na kuthamini kikamilifu ushiriki wa kweli na wa maana wa waathiriwa na wawakilishi wao katika mchakato wote."  
8/30/20230
Episode Artwork

30 AGOSTI 2023

Karibu kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa ambapo miongoni mwa utakayoyasikia ni pamoja na Wataalamu wa haki za binadamu wa Umoja wa Mataifa na wa kanda mbalimbali ikiwemo Afrika na Asia wameyasihi mataifa yote kutoa haki kwa waathirika wa utoweshwaji wa watu, ikiwa ni pamoja na mtu yeyote ambaye amepata madhara kama matokeo ya moja kwa moja ya utoweshwaji wa watu. Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na masuala ya watoto UNICEF nchini Kenya linatekeleza mradi wa matibabu kwa watoto wenye utapiamlo ambao umeanza kuzaa matunda kwa afya za watoto kuimarika. Makala hii leo inatoka Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako huko walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania, kikosi cha 10 wanaohudumu kwenye ujumbe wa kulinda amani nchini humo, MONUSCO wametembelea wagonjwa katika hospitali ya La Grace iliyoko Mbau jimboni Kivu Kaskazini. Na katika mashinani ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya watu kutoweshwa tunakwenda SriLanka kusikia changamoto anazopitia Jeyatheepa Ponniyamoorthi ambaye mumewe alitoweshwa mwaka 2009 na kumuacha na mtoto wao wa kiume mwenye umri wa mwaka mmoja na nusu na sasa mtoto huyo ana umri wa miaka 14.
8/30/20230
Episode Artwork

29 AGOSTI 2023

Karibu kusikiliza jarida la Umoja wa Mataifa ambapo leo tunamulika kilimo cha parachini na jinsi kinavyo changia kutekeleza malengo ya Umoja wa Mataifa ya Maendeleo endelevu hususan la kutokomeza umaskini. Pia utasikia habari kwa ufupi kuhusu matumizi ya silaha za nyuklia, hali ya usalama nchini Niger na haki za binadamu nchini Ethiopia. Mashinani hii leo utamsikilia Luteni Kanali Kevin Byabato, Msemaji wa kikosi cha Umoja wa Mataifa cha kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, MONUSCO akieleza jinsi ushirikiano kati ya MONUSCO na jeshi la serikali FARDC umezaa matunda kwani katika siku 15 za hivi karibuni waliweza kuzuia mashambulizi matano toka kwa waasi wa ADF jimboni Ituri na Kivu Kaskazini.
8/29/20230
Episode Artwork

Walinda amani wanaondoka Mali lakini Umoja wa Mataifa unabakia

Baada ya kuweko nchini Mali kwa muongo mmoja, ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani na kuweka utulivu nchini humo umeanza kufunga virago. Hii ni baada ya mamlaka nchini humo kutaka ujumbe huo uondoke, ombi ambalo liliridhiwa na Baraza la Usalama la Umoja wa Mataifa. Sasa MINUSMA inatakiwa iwe imeondoka ifikapo tarehe 31 mwezi Agosti mwaka huu. Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Mali, El-Ghassim Wane ambaye pia ni Mkuu wa MINUSMA amezungumza na Jerome Bernard wa Idhaa ya Kifaransa ya Umoja wa Mataifa, mazungmzo ambayo ndio msingi wa makala hii inayoletwa kwako na Assumpta Massoi.
8/28/20230
Episode Artwork

Botswana: Mkutano wa 73 wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya WHO waanza Gaborone

Mkutano wa Sabini na tatu wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) umeanza hii leo katika mji mkuu wa Botswana, Gaborone huku tukio hilo likishuhudia pia Maabara ya Kitaifa ya Marejeleo ya Virusi vya Ukimwi (VVU) ya Botswana ikipewa hadhi ya kuwa Kituo Kishiriki cha Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) cha kufuatilia Ubora. Mkutano huu utakaoendelea hadi tarehe Mosi ya mwezi ujao Septemba unawakutanisha Mawaziri wa afya wa Afrika na wawakilishi wa serikali pamoja na wadau wengine wa sekta ya afya kutoka kote barani Afrika ili kujadili na kukubaliana kuhusu hatua muhimu za kushughulikia changamoto za afya za kanda ya Afrika, kuendeleza na kukuza afya bora na ustawi wa watu. Na kuhusu Maabara ya Kitaifa ya Botswana kuwa Kituo Kishiriki cha Ubora cha WHO, Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus  akizungumza asubuhi ya leo ya Botswana baada ya yeye na Rais Dkt Mokgweetsi Eric Keabetswe Masisi wa Botswana kutia saini makubaliano amesema,"WHO inajivunia kuhesabu maabara hii kama Kituo cha Kushirikiana na inatarajia kufanya kazi pamoja kwa karibu zaidi katika kutoa msaada na huduma zinazohitajika kwa watu wanaoishi na VVU." Kwa upande wake Rais Masisi wa Botswana amesema kuteuliwa kwa maabara hii kama Kituo Kishiriki cha Ubora cha WHO kunaipa nchi ya Botswana imani kwamba wako kwenye njia sahihi ya kufikia lengo la WHO la mwaka 2030 la kudhibiti Virusi Vya Ukimwi (VVU).  Wengine walioko nchini Botswana kuhudhuria Mkutano huo unaofanyika kwa njia ya ana kwa ana na mtandaoni ni Mkurugenzi wa WHO kanda ya Afrika Dkt. Matshidiso Moeti ambaye kabla ya kuhitimishwa kwa mkutano huu, anatarajiwa kutoa taarifa kuhusu hali ya afya barani Afrika. 
8/28/20230
Episode Artwork

Baada ya uchaguzi mkuu Zimbabwe Guterres aomba amani

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amesema anafuatilia kwa karibu kinachoendelea kwenye mchakati wa uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Zimbabwe tarehe 23 mwezi huu wa Agosti. Taarifa iliyotolewa Jumapili jioni na ofisi ya msemaji wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa inasema Katibu Mkuu Guterres katika ufuatiliaji wa kinachoendelea nchini humo, hofu yake kubwa ni ripoti za kukamatwa kwa waangalizi wa uchaguzi, vitisho dhidi ya wapiga kura, vitisho vya ghasia, halikadhalika manyanyaso na matumizi ya nguvu.  Hofu ya Guterres inakuja wakati ambapo tayari vyombo vya habari vinaripoti kuwa Rais wa sasa Rais wa sasa Emmerson Mnangagwa ameibuka na ushindi kwenye kinyang’anyiro cha urais kilichokuwa kinawaniwa na wagombea 11.  Katibu Mkuu ametoa wito kwa viongozi wa kisiasa na wafuasi wao kuepuka aina yoyote ya ghasia au kuchochea ghasia, na badala yake wahakikishe haki za binadamu na utawala wa sheria vinaheshimiwa.    Ametoa wito pia kwa washiriki wote kwenye siasa kutatua mizozano yoyote ile kupitia njia za kisheria na taasisi zilizowekwa kwa ajili hiyo.  Bwana Guterres amezitaka taasisi husika zitatue migogoro yoyote itakayoibuka kwa njia ya haki, uwazi na haraka ili kuhakikisha matokeo ya uchaguzi huo yanaakisi utashi wa wananchi wa Zimbabwe.  Vyombo vya habari vinaripoti kuwa wagombea kutoka upinzani wamekataa matokeo ya uchaguzi yaliyompatia ushindi Rais Mnangagwa kwa asilimia 52.6, matokeo yaliyotangazwa Jumamosi na Tume ya Uchaguzi nchini Zimbabwe.  Bwana Mnangagwa aliingia madarakani kufuatia uchaguzi wa mwaka 2018. 
8/28/20230
Episode Artwork

28 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani jaridani tunaangazia hali ya usalama nchini Zimbabwe baada ya uchaguzi na masuala ya afya nchini Botswana. Makala tunakupeleka nchini Mali na mashinani nchini Rwanda, kulikoni?Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amesema anafuatilia kwa karibu kinachoendelea kwenye mchakati wa uchaguzi mkuu uliofanyika nchini Zimbabwe tarehe 23 mwezi huu wa AgostiMkutano wa Sabini na tatu wa Kamati ya Kanda ya Afrika ya Shirika la Afya la Umoja wa Mataifa (WHO) umeanza hii leo katika mji mkuu wa Botswana, Gaborone huku tukio hilo likishuhudia pia Maabara ya Kitaifa ya Marejeleo ya Virusi vya Ukimwi (VVU) ya Botswana ikipewa hadhi ya kuwa Kituo Kishiriki cha Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) cha kufuatilia Ubora. Katika makala Assumpta Massoi anamulika harakati za Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Mali, MINUSMA kuwa umeondoka nchini humo ifikapo tarehe 31 mwezi Desemba mwaka huu kufuatia ombi la mamlaka nchini Mali.Mashinani tunakupeleka nchini Rwanda kusikia ni kwa jinsi gani wazazi wameweza kutokomeza udumavu na kuhakikisha afya njema kwa watoto wao.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/28/20230
Episode Artwork

Wakati wa mafuriko nilipoteza mtoto, na sasa sina uhakika nitakayejifungua ataishi- Mkazi Pakistani

Mwaka mmoja tangu mafuriko ya kihistoria yakumbe Pakistani, na hali ya dharura nchini humo kutangazwa, mamilioni ya watoto bado wanaendelea kuhitaji misaada ya dharura huku operesheni za ukarabati zikisalia kukumbwa na ukata kwani fedha zinazotakiwa hazijapatikana. Hii leo katika Makala Assumpta Massoi anakupeleka Pakistani kusikia waathirika na kumbukumbu za hali ilivyokuwa, shaka na shuku zao hivi sasa na nini Umoja wa Mataifa unafanya kuleta angalau ahueni. 
8/25/20230
Episode Artwork

Griffiths: Vita na njaa vinaweza kusambaratisha Sudan

Vita inayoendelea nchini Sudan inachochea dharura kubwa ya kibinadamu ambapo vita na njaa, magonjwa na watu kufurushwa makwao vilivyofuatia sasa  inatishia ‘kutafuna’ nchi nzima, amesema Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA, Martin Griffiths. Taarifa iliyotolewa na OCHA hii leo jijini New York, Marekani imemnukuu mkuu wa ofisi hiyo Martin Griffiths akisema kuwa mapigano makali yaliyoanzia mji mkuu wa Sudan, Khartoum na jimbo la Darfur katikati ya mwezi Aprili mwaka huu yamesambaa hadi Kordofan. Amesema katika mji mkuu wa jimbo la Kordofan Kusini, Kadugli hifadhi ya vyakula imekwisha kwa kuwa mapigano na vizuizi njiani vinasababisha wahudumu wa misaada washindwe kufikia wenye njaa. Huko El Fula, mji mkuu wa jimbo la Kordofan Magharibi, ofisi za watoa misaada zimevamiwa na misaada imeporwa. Bwana Griffiths amesema hofu yake sasa ni usalama wa raia kwenye jimbo la Al Jazira wakati huu ambapo mzozo huo unasogelea eneo hilo tegemewa kwa uzalishaji wa chakula Sudan. Mkuu huyo wa OCHA amesema kadri mapigano yanavyoendelea, vivyo hivyo madhara yanayongezeka. Mamia ya maelfu ya watoto wana utapiamlo uliokithiri na wako hatarini kufa iwapo hawatapata tiba. Magonywa ya kuambukizwa kwa vimelea kama vile Malaria, Kifaduro, Kidingapopo yanasambaa nchi nzima na yanatishia uhai kwa wale wenye waliodhoofishwa tayari na utapiamlo. Wagongwa hao hawawezi kupata matibabu kwani mapigano yamesambaratisha mfumo wa afya. Bwana Griffiths amesema vita ya muda mrefu itapoteza kizazi cha watoto kwani mamilioni hawaendi shuleni, na watakumbwa na kiwewe na kusalia na kovu la vita katika maisha yao. Amesema ripoti za kwamba watoto wanatumika pia kwenye mapigaon ni za kuchukiza. Mkuu huyo wa OCHA ametaka pande kinzani kuweka mbele maslahi ya wananchi Sudan badala ya uroho wao wa madaraka, watoa misaada wapatiwe ruhusa ya kufikisha mahitaji na zaidi ya yote jamii ya kimataifa ipatie janga la Sudan udharura unaohitajika. 
8/25/20230
Episode Artwork

25 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani jaridani tunaangazia haki za binadamu nchini Sudan na utaifa wa Wapemba nchini Kenya. Makala tunakupeleka nchini Pakistan na mashinani nchini Tanzania, kulikoni?Vita inayoendelea nchini Sudan inachochea dharura kubwa ya kibinadamu ambapo vita na njaa, magonjwa na watu kufurushwa makwao vilivyofuatia sasa inatishia ‘kutafuna’ nchi nzima, amesema Mkuu wa Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya kibinadamu, OCHA, Martin GriffithsMwishoni mwa mwezi uliopita Rais wa Kenya William Ruto akiwa Kilifi mashariki mwa Kenya alitangaza kutambulika rasmi kwa jamii ya Wapemba ambao kwa miaka mingi waliishi nchini humo wakikosa hadhi ya utaifa kwa kuwa vizazi vyao vya nyuma vilitoka nje ya Kenya. Makala tunakwenda Pakistani ambako leo ni mwaka mmoja tangu mafuriko makubwa yaliyozua zahma nchini humo.Mashinani tunakupeleka nchini Tanzania kushuhudia jinsi ambavyo ukulima wa mboga mboga  na matunda unavyosaidia wanawake kupatia jamii zao mapato thabiti na kuwapeleka watoto wao shuleni.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/25/20230
Episode Artwork

Mdau wa UNHCR Haki center, moja ya mashirika yaliyosaidia Wapemba kutambulika rasmi Kenya

Mwishoni mwa mwezi uliopita Rais wa Kenya William Ruto akiwa Kilifi mashariki mwa Kenya alitangaza kutambulika rasmi kwa jamii ya Wapemba ambao kwa miaka mingi waliishi nchini humo wakikosa hadhi ya utaifa kwa kuwa vizazi vyao vya nyuma vilitoka nje ya Kenya. Nyuma ya mafanikio haya zimekuwepo harakati za muda mrefu za kuitafuta haki hiyo zikifanywa na wananchi na mashirika yasiyo ya kiserikali. Moja ya mashirika hayo ni Haki Center ambalo ni mdau wa shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR) katika eneo la pwani na kaskazinimashariki mwa Kenya.  Barke Hamisi kutoka jamii ya wapemba anatambua mchango wa shirika hili na anakumbuka hali ilivyokuwa kabla ya hatua ya juzi ya kutambulika,“Mimi nimezaliwa hapa watamu na nikalelewa hapa watamu na pia nilisoma shule ya msingi watamu. Nilikuwa najumuika vizuri na jamii zingine lakini shida ilikuwa ni mtu anakwambia wewe ni mpemba. Sasa mtu akikuambia wewe ni mpemba, hiyo ni kama mtu amekudunga mkuki. Unakosa morali (ari).” Na ni kwa vipi basi shirika la Haki Center lilichangia harakati hizi? Barke anaeleza, “Haki Center ilikuwa na mchango mkubwa katika utetezi wetu kwa sababu walituwezesha sana kutojificha tena kupigania haki yetu kupitia msaada wao, ndipo tuliposhirikiana na wabunge na kutoka kwenye mazungumzo na majadiliano tuliyokuwa nayo pamoja nao tuliandika ombi.”  
8/25/20230
Episode Artwork

Methali - Mnywa Maji kwa Mkono Mmoja Kiu yake I pale pale

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania anachambua methali, "Mnywa Maji kwa Mkono Mmoja Kiu yake I pale pale."
8/24/20230
Episode Artwork

Wanawake wapatiwe nafasi katika sayansi na teknolojia, watasongesha agenda 2030- Mwanaisha Ulenge

Ikiwa imesalia takribani miaka 6 ushehe kufika mwaka 2030 muda ambao ulimwengu ulijiwekea lengo la kuwa umetimiza Malengo ya Maendeleo Endelevu (SDGs), mapema mwaka huu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa akiamini wanawake wanasayansi wana uwezo wa kuchangia haraka katika maendeleo ya ulimwengu, alieleza namna kuwanyima fursa za sayansi wanawake kunarudisha maendeleo nyuma na hivyo akashauri wanawake wanasayansi wapewe nafasi kuanzia darasani, maabara na katika vyumba vya maamuzi.Mwanaisha Ulenge ni Mwanamke Mwanasayansi Mhandisi, Mbunge nchini Tanzania vilevile Mjumbe wa Shirikisho la Mabunge Duniani (IPU) na hivi karibuni akiwa katika ziara ya kikazi hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa nilipata fursa ya kujadiliana naye kuhusu nafasi ya mwanamke katika sayansi na teknolojia.
8/24/20230
Episode Artwork

24 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na Mwanaisha Ulenge ni Mwanamke Mwanasayansi Mhandisi, Mbunge nchini Tanzania vilevile Mjumbe wa Shirikisho la Mabunge Duniani (IPU) na hivi karibuni akiwa katika ziara ya kikazi hapa kwenye makao makuu ya Umoja wa Mataifa Anold Kayanda alipata fursa ya kujadiliana naye kuhusu nafasi ya mwanamke katika sayansi na teknolojia. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo ziara za Katibu Mkuu wa umoja wa Mataifa nchini Afrika Kusini, kazi za umoja wa mataifa nchini Sudan na hali ya kibinadamu ya wakimbizi wa Rohingya baada ya miaka 6 ya kukimbia makazi yao nchini Myanmar. Katika kujifunza Kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania anachambua methali “Mnywa Maji kwa Mkono Mmoja Kiu yake I pale pale”Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amehutubia mkutano wa viongozi kundi la Brazil, Urusi, India, China na Afrika Kusini au BRICS  huko Johannesburg Afrika Kusini na kusema katika dunia ya sasa iliyogawanyika na kugubikwa na majanga hakuna mbadala mwingine wa kuwezesha kusonga mbele zaidi ya mshikamano hasa kwenye masuala lukuki ikiwemo marekebisho ya mfumo wa kimataifa wa fedha duniani.Ikiwa kesho ni miaka 6 tangu serikali ya kijeshi nchini Myanmar ianze msako wa kufurusha waislamu wa kabila la Rohingya kutoka jimbo la Rakhine nchini humo, Kamishna Mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Haki za Binadamu Volker Türk amesema jamii ya kimataifa isisahau warohingya na wale wanaowahifadhi, na zaidi ya yote juhudi za kimataifa ziongezwe maradufu ili wahusika wawajibishwe. Na shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF linaonya kuwa bila amani nchini Sudan, hatma ya watoto iko mashakani wakati huu ambapo zaidi ya watoto milioni 2 wamefurushwa makwao tangu mapigano yaanze kwenye mji mkuu Khartoum mwezi Aprili mwaka huu na sasa mapigano hayo yanaenea kwenye maeneo mapya.Katika kujifunza lugha ya Kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania anachambua methali Mnywa Maji kwa Mkono Mmoja Kiu yake I pale pale.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/24/20230
Episode Artwork

UNEP: Majitaka yawe jawabu la changamoto ya maji na tabianchi duniani

Maadhimisho ya Wiki ya Maji  yakiendelea huko Stockholm nchini Sweden, shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira duniani, (UNEP) leo limezindua ripoti yenye lengo la kugeuza majitaka kuwa jawabu la uhaba wa maji na changamoto ya tabianchi duniani.UNEP kupitia taarifa yake iliyotolewa leo Nairobi nchini Kenya inasema majitaka yanaendelea kuwa tishio la afya na mazingira yakichangia utoaji wa hewa chafuzi kama ilivyo sekta ya anga.  Hata hivyo ripoti hiyo inasema kwa kutunga será sahihi, majitaka yanaweza kuwa chanzo mbadala cha nishati kwa watu nusu bilioni duniani na kusambaza mara 10 zaidi ya maji ya baharini yanayotolewa chumvi kwa matumizi ya binadamu na wakati huo huo kuepusha zaidi ya asilimia 10 ya matumizi ya mbolea duniani. Ripoti hiyo ikipatiwa jina Majitaka. Kubadili tatizo kuwa jawabu, imeandaliwa na UNEP kwa ushirikiano na taasisi ya GRID-Arendal na Mpango wa Kimataifa kuhusu majitajika, (GWWI) na inazisihi serikali na sekta ya biashara kutumia tena na tena majitaka kama fursa ya kiuchumi, badala ya kuyageuza kuwa tatizo la kuondokana nalo. Faida za kukusanya, kusafisha na kutumia tena na tena maji hayo ni lukuki, kwa mujibu wa ripoti hiyo, ikiwemo fursa mpya za ajira na vyanzo vipya vya mapato, halikadhalika kupunguza kiwango cha majitaka yanayozalishwa. Leo hii ni asilimia 11 tu ya majitaka duniani kote ndio yanatumika ten ana tena na takribani nusu ya majitaka yasiyosafishwa yanaingia kwenye mito, maziwa na bahari. Akizungumzia ripoti hiyo, Leticia Carvalho kutoka UNEP anasema duniani kote, majitaka yana fursa kubwa lakini kwa sasa yanaachiwa yachafue mfumo anuai tunaotegemea. Tusipoteze fursa hii: ni wakati wa kutimiza ahadi ya majitaka kuwa chanzo mbadala cha maji safi, nishati na virutubisho muhimu.” 
8/23/20230
Episode Artwork

23 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia wiki ya maji na kazi ya Umoja wa mataifa katika utoaji wa huduma za maji. Makala tunakuletea uchambuzi wa Ibara ya 8 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu na mashinani tunakupeleka jijini Mbeya nchini Tanzania, kulikoni? Maadhimisho ya Wiki ya Maji  yakiendelea huko Stockholm nchini Sweden, shirika la Umoja wa Mataifa la Mazingira duniani, (UNEP) leo limezindua ripoti yenye lengo la kugeuza majitaka kuwa jawabu la uhaba wa maji na changamoto ya tabianchi dunianiTukiwa bado katika Wiki ya Maji ambayo imeanza tarehe 20 na itaendelea hadi kesho tarehe 24, TANBAT 6 ambacho ni Kikosi cha sita cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania wanaohudumu chini ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati (MINUSCA), kwa kutumia magari wametoa msaada wa maji safi na salama kwa wanawake wa vijiji vinavyokabiliwa na uhaba wa maji mjini Berberati mkoa wa Mambéré-Kadéï. Hii leo katika makala tunakuletea uchambuzi wa Ibara ya 8 ya Tamko la Umoja wa Mataifa la Haki za Binadamu. Makala hii iliyoandaliwa na Grace Kaneiya ni marejeo na ilirushwa tarehe 12 Novemba 2018. Grace Kaneiya alizungumza na Robi Chacha akiwa Afisa Kampeni usalama na Haki za binadamu Amnesty International nchini Kenya. Ibara inasema kila mtu ana haki ya kupata msaada wa kisheria na kutumia mfumo wa kisheria iwapo haki zake haziheshimiwi.Na mashinani tunakupeleka jijini Mbeya nchini Tanzania ambako ujenzi wa vyoo na vituo vya maji ambavyo ni muhimu kwa afya na ustawi wa watoto vimewezesha wanafunzi kunawa mikono na kunywa maji safi na salama.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/23/20230
Episode Artwork

Walinda amani kutoka Tanzania TANBAT6 watoa huduma ya maji kwa wanakijiji nchini CAR

Tukiwa bado katika Wiki ya Maji ambayo imeanza tarehe 20 na itaendelea hadi kesho tarehe 24, TANBAT 6 ambacho ni Kikosi cha sita cha walinda amani wa Umoja wa Mataifa kutoka Tanzania wanaohudumu chini ya ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Afrika ya Kati (MINUSCA), kwa kutumia magari wametoa msaada wa maji safi na salama kwa wanawake wa vijiji vinavyokabiliwa na uhaba wa maji mjini Berberati mkoa wa Mambéré-Kadéï. Siku ya leo ni shangwe isiyo na kifani kwa wananchi wa kijiji cha Bisa  na kijiji  cha Diforo vilichopo mkoani Mambéré-Kadéï kusini magharibi mwa Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR. Ni baada ya kikosi cha TANZBAT 6 kutoa msaada wa kuwagawia maji waliyobeba kwenye magari yao maalum hasa msaada ukiwaalenga wanawake na watoto ambao ndio waathirika wakubwa kwenye tatizo hilo.Bi. Yakele Stella mmoja wa wanawake wanufaika wa msaada huu wa maji ametoa shukrani kwa walinda amani hawa wa Umoja wa Mataifa akisema, "Mimi kama mama nimefurahi sana leo kwa msaada wa kupewa maji maana sisi akinamama tunakwenda mbali kuchota maji lakini pia maji hayo si maji salama. Lakini leo hii walinda amani hawa kutoka Tanzania wanazidi kutusaidia jamii zetu kwa kutupatia maji safi na salama."Mwingine aliyetoa shukrani kwa niaba ya wananchi wengine ni chifu wa eneo la Difolo Bwana Mamadour Soh Papy, "Tunashukuru sana kwa walinda amani kutoka Tanzania kwa jinsi walivyoamua kutupa msaada wa maji safi hapa nyumbani maana hatuna maji safi hapa kwetu. Huwa tunapata maji ya bomba mara mbili tu kwa wiki na huwa tunanunua. Watu tunakuwa wengi sana, wanasukumana mpaka kuumia. Lakini leo tunajisikia amani kupata maji bila fujo yeyote. Mungu awabariki walinda amani wa Tanzania kwa upendo wao wanaouonyesha hapa kwetu."Aidha TANBAT 6 sabamba na wiki hii ya maji, wanautumia wakati huu kusaidia jamii za hapa CAR ikiwa ni sehemu ya shughuli za kuelekea kuadhimisha miaka mitano tangu kuundwa kwa Jeshi la Wananchi wa Tanzania (JWTZ). Shughuli nyingine zinazotarajiwa kufanyika kwenye jamii katika kuelekea wiki hii ya maadhimisho ya kuundwa kwa JWTZ ni pamoja na kutoa elimu ya ujasiliamali Kwa vikundi mbalimbali na matibabu kwenye zahanati zilizopo  karibu na kikosi hicho.
8/23/20230
Episode Artwork

22 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Mapigano yanayoendelea huko Mashariki mwa Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC yakiendeshwa na vikundi vilivyojihami vya waasi yanaendelea kufurusha watu kutoka makwao, na hivyo wakimbizi hao wa ndani kushindwa kujikimu maisha yao ya kila siku. Malazi ni shida, makazi ni shida, halikadhalika chakula. Maisha yanakuwa ni changamoto kila uchao. Hali hiyo iko dhahiri kabisa jimboni Kivu Kaskazini ambako hata hivyo hatua za shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa chakula duniani, WFP kwa wakimbizi Oicha zimeleta ahueni. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo za msaada wa kibinadumu, malaria na maji. Mashinani tunakwenda Tanzania hususan mkoani Kilimanjaro.Mamilioni ya watu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) wako hatarini kukumbwa na njaa huku ufadhili ukiwa katika hali mbali ametahadharisha leo Peter Musoko ambaye ni Mkurugenzi wa Nchi wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula (WFP) nchini DRC alipozungumza leo na waandishi wa habari mjini Geneva, Uswisi. Rais wa Baraza Kuu la Umoja wa Mataifa Csaba Kőrösi amehutubia mkutano wa Wiki ya Maji huko Stockholm nchini Sweden na kutaka mabadiliko makubwa ya hatua za kufanikisha upatikanaji wa maji duniani akisema kwa kasi ya sasa muda uliosalia hautawezesha kufanikisha lengo la malengo ya maendeleo endelevu, SDGs kuhusu maji.Na Mfuko wa Kimataifa wa Kupambana na UKIMWI, Kifua Kikuu na Malaria (Global Fund) umetangaza Mbinu Mpya ya Kuongeza Upatikanaji wa Vyandarua Vizuri Zaidi ili Kuzuia Malaria. Na mashinai Anna Assey, mkulima kutoka mkoani Kilimanjaro nchini Tanzania akielezea ni kwa vipi yeye anahifadhi mbegu za kiasili wakati huu ambapo Umoja wa Mataifa unasisitiza matumizi ya mbinu za kiasili kama njia ya kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/22/20230
Episode Artwork

Lebanon - Mabomu yateguliwa na kuwezesha wamiliki kurejea kwenye ardhi baada ya kutelekeza miaka ya 1970

Huko nchini Lebanon, Mashariki ya Kati, ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo UNIFIL kwa ushirikiano na wadau wameteketeza mabomu 4,000 yaliyokuwa yametegwa kwenye eneo la ukubwa wa mita 44,000 za mraba na hivyo kuwezesha ianze kutumika tena kwa kilimo baada ya kushindikana tangu miaka ya 1970 kwa hofu ya milipuko ya mabomu.Ni katika eneo la Mess el Jebal, kusini mwa Lebanon eneo hili la ukubwa wa meta 44,000 za mraba ni kichaka lakini  salama. Wamiliki wa eneo hili wamerejea bila hofu ya kulipukiwa na mabomu na mmojawao ni Jaffar Ghadban, “Zamani miaka ya 70 mababu zetu walikuwa wanalima hapa na zao kuu kwenye eneo hili lilikuwa kunde. Jeshi la Lebanon, walinda amani wa UNIFIL  [YUNIFIL] kutoka Cambodia wamesafisha ardhi kwa kutegua mabomu.Tumekuja leo hapa kumiliki tena ardhi yetu. Mungu akipenda tutaanza kulima tena kama walivyofanya watangulizi wetu. Tutarejesha upya eneo hili liwe bora kuliko zamani.” Luteni Kanali Zang Dongjie, Mkuu wa kitengo cha uhandisi UNIFIL anasema mabomu 4,000 ya kutegwa ardhini yaliteketezwa hivyo “sasa naweza kuthibitisha kuwa eneo hili ni salama kwa kilimo.” Kazi hii iliyoendeshwa kwa ushirikiano katiya UNIFIL, ofisi ya Umoja wa Mataifa ya hatua dhidi ya mabomu, UNMAS na Kituo cha Lebanon cha hatua dhidi ya mabomu, LMAC haikuwa rahisi kwani wakati wa operesheni mteguaji mmoja wa mabomu alifariki dunia.  Julie Mayers, Mkuu wa Programu ya uteguaji mabomu, UNIFIL anatamatisha akisema baada ya miaka miwili ya kutegua mabomu kwenye maeneo 10 sasa wana furaha kwamba “kilichofanyika kina uhusiano moja kwa moja na dira ya kituo cha Lebanon cha hatua dhidi ya mabomu ya ardhini ya kuona jamii inastawi na kuondokana na tishio la vilipuzi.” 
8/21/20230
Episode Artwork

Siku ya Kimataifa ya Kuwakumbuka na Kuwaenzi Waathirika wa Ugaidi

Ikiwa leo tarehe 21 Agosti ni Siku ya Kimataifa ya Kuwakumbuka na Kuwaenzi Waathirika wa Ugaidi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii amewasihi watu wote ulimwenguni kuhakikisha kwamba wale waliofariki au kukumbwa na athari za muda mrefu za ugaidi hawasahauliki kamwe. Kama sehemu ya kuadhimisha Siku hii, Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Kukabiliana na Ugaidi (UNOCT) kupitia Kampeni ya Kumbukumbu, kwa njia mbalimbali ikiwemo mitandao ya kijamii inasambaza kumbukumbu za waathirika wa ugaidi kupitia filamu na picha ili kuwaenzi waliofariki na pia kuwapa waathirika fursa ya kutoa ya moyoni. Mmoja wao ni Nigeel Namai alikuwa na umri wa miezi 4 baba yake alipouawa katika shambulio la mwaka 1998 kwenye Ubalozi wa Marekani mjini Nairobi, Kenya. Wakati wowote Nigeel anapovaa suti, inaleta kumbukumbu na simulizi kuhusu baba yake, ambaye kila mara alikuwa nadhifu.“Kila wakati ninapovaa suti inarejesha kumbukumbu ya simulizi ambazo mama alikuwa ananisimulia kuhusu baba. Ningependa baba yangu ajivunie. Popote alipo aangalie aseme: “Oo, ingawa siwezi kuwa naye kimwili ninajivunia yeye kama mvulana mdogo na pia mwanaume mdogo.” 
8/21/20230
Episode Artwork

Mifumo madhubuti ya kuwasiliana Sierra Leone imeimarisha uthibiti wa milipuko ya magonjwa

Takriban miaka 10 iliyopita nchi kadhaa za Afrika zilikumbana na mlipuko wa ugonjwa hatari wa ebola uliogharimu maisha ya mamilioni ya watu. Moja ya nchi hizo ni Sierra Leone ambayo wakati mlipuko wa Ebola ukiikumba nchi hiyo walikuwa hawana njia bora za kuwasiliana kama taifa na kujua ukubwa wa ugonjwa huo na namna ya kudhibiti. Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO kanda ya Afrika mbali na kuisaidia nchi hiyo kupamba na Ebola lakini iliwasaidia kuweka mifumo madhubuti ya kuwasiliana nchi nzima kujua iwapo kuna mlipuko wa ugonjwa wowote. Ni kutokana na mfumo huo thabiti nchi hiyo imefanikiwa kuongoza katika utambuzi wa haraka wa milipuko ya magonjwa na kushughulikia kwa wakati. Leah Mushi anatujuza zaidi katika Makala hii. 
8/21/20230
Episode Artwork

21 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia Siku ya waathirika wa ugaidi duniani na mabomu ya kutegwa ardhini. Makala tunakupeleka nchini Siarra Leone na mashinani nchini Msumbiji, kulikoni? Ikiwa leo tarehe 21 Agosti ni Siku ya Kimataifa ya Kuwakumbuka na Kuwaenzi Waathirika wa Ugaidi, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres kupitia ujumbe wake mahususi kwa ajili ya siku hii amewasihi watu wote ulimwenguni kuhakikisha kwamba wale waliofariki au kukumbwa na athari za muda mrefu za ugaidi hawasahauliki kamwe. Huko nchini Lebanon, Mashariki ya Kati, ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini humo UNIFIL kwa ushirikiano na wadau wameteketeza mabomu 4,000 yaliyokuwa yametegwa kwenye eneo la ukubwa wa mita 44,000 za mraba na hivyo kuwezesha ianze kutumika tena kwa kilimo baada ya kushindikana tangu miaka ya 1970 kwa hofu ya milipuko ya mabomu.Katika makala Leah Mushu anatujuza namna nchi ya Sierra Leone ilivyoweza kubadilika kutoka nchi yenye ugunduzi dhaifu wa magonjwa hususan ya mlipuko mpaka kuwa nchi yenye ugunduzi thabiti na unaofanya kazi.Mashinai tunakwenda mjini Maputo nchini Msumbiji kusikia jinsi huduma ya maji ilivyoleta furaha kwa wafanyabiashara.Mwenyeji wako ni Anold Kayanda, karibu!
8/21/20230
Episode Artwork

Kutana na Nafi Aïsha Diop mtaalamu wa usalama na ubora wa chakula wa WFP DRC

Ikiwa kesho Agosti 19 ni Siku ya watoa misaada ya kibinadamu, ambapo ulimwengu unawatambua na kuwasherehekea watu wote ambao waliojitolea au wanajitolea maisha yao kusaidia wanadamu wengine walio katika changamoto, leo tunakukutanisha na Nafi Aïsha Diop mtaalamu wa usalama na ubora wa chakula wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) anayehudumu nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, (DRC). Msimulizi ni Anold Kayanda.Nafi Aïsha Diop akieleza kuhusu kazi yake hiyo katika WFP kwamba ni kuhakikisha usalama na ubora wa chakula ambacho WFP inakisambaza kwa wahitaji kuanzia shambani hadi mezani.  Anafafanua anachomaanisha anaposema usalama na ubora wa chakula kwamba chakula lazima kiwe salama kwa matumizi ya binadamu. Na kuhusu ubora ni kwamba chakula hiki inabidi kiwe na lishe ndani yake kama vitamini na madini na kwa hiyo kiwape walaji kila kitu kinachohitajika katika mlo wao. Je ni kitu gani Nafi Aïsha Diop anakipenda zaidi katika kazi yake?Anasema, "Ninachopenda zaidi kuhusu kazi yangu ni kwamba ninafanya kazi na watu tofauti, mazingira, na aina tofauti za chakula. Ninajihisi kuridhishwa hasa na matokeo kwenye mnyororo mzima wa usambazaji kwa sababu unaweza kuona wazi matokeo. Kwa mfano tunapofanya mafunzo ya usalama na ubora wa chakula kwenye ghala, hatugusi tu wafanyakazi kwenye ghala. , lakini pia tunagusa jamii zao.”    
8/18/20230
Episode Artwork

Wahisani msichoke kukirimu wenye uhitaji – Gregory Akall wa OCHA

Siku ya watoa misaada ya kibinadamu huadhimishwa kila Agosti 19, na maudhui mwaka huu ni “kwa vyovyote vile,” ikimaanisha misaada lazima iendelewe kutolewa katika mazingira yoyote yale. Gregory Akall wa Ofisa wa usaidizi wa kibinadamu katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya misaada ya binadamu na ya dharura (OCHA), anahudumu kaskazini mwa Kenya. Akiwa naye mshiriki kwenye jukumu hili anatumia mazungumzo yake na mwandishi wa Idhaa hii ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa nchini Kenya kutia shime wahisani wasichoke kwa vyovyote vile bali waendelee kunyoosha mikono yao kukirimu walio na uhitaji. Gregory anahudumu kaskazini mwa Kenya, eneo ambalo limezongwa na uhaba wa mvua, njaa na maafa ya mifugo. Hapa anaanza kufafanua jukumu la OCHA.  
8/18/20230
Episode Artwork

UNICEF DRC: Mlipuko mbaya zaidi wa kipindupindu watishia uhai wa watoto

Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto, UNICEF nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC linaonya kuwa kuimarika kwa mapigano mashariki mwa taifa hilo kumetumbukiza Watoto katika mlipuko mbaya Zaidi wa ugonjwa wa kipindupindu kuwahi kukumba taifa hilo katika kipindi cha miaka sita. George Musubao na melezo zaidi. UNICEF kupitia taarifa yake iliyotolewa leo mjini Goma, jimboni Kivu Kaskazini nchini DRC, inasema nchini kote, kumekuweko na wagonjwa 31,342 wa kipindupindu ambapo kati yao hao 230 wamekufa na hiyo ni kuanzia Januari hadi Julai mwaka huu, wengi wao wakiwa ni watoto.Jimbo lililoathirika zaidi ni Kivu Kaskazini ambako zaidi ya watoto 8,000 wenye umri wa chini ya miaka mitano waliambukizwa kipindupindu katika miezi 7 ya mwanzoni mwa mwaka huu, idadi ambayo ni mara sita zaidi ya mwaka mzima wa 2022.Idadi hiyo ni kubwa ikilinganishwa na wagonjwa 5,120 mwaka mzima wa 2022 ambako wagonjwa 1,200 walikuwa ni watoto wenye umri wa chini ya miaka 5.Hali ya sasa ni kengele ya dharura"Ukubwa wa mlipuko wa kipindupindu na kiwango cha tishio lake vinapaswa kuwa kengele ya dharura,” amesema Shameza Abdulla, Mratibu wa dharura wa UNICEF Goma, ambao ndio mji mkuu wa jimbo la Kivu Kaskazini.Amesema iwapo hatua za dharura hazitachukuliwa ndani ya miezi ijayo, kuna hatari kubwa ugonjwa huo utasambaa maeneo mengine ya nchi ambayo hayashuhudia kipindupindu kwa miaka kadhaa.Bi. Abdulla amesema kuna hatari pia kuwa kipindupindu kitaendelea kusambaa kwenye makazi ya wakimbizi wa ndani ambayo tayari yana idadi kubwa ya watu hasa Watoto walio hatarini zaidi kuambukizwa magonjwa na hatimaye kifo.Mwaka 2017 kipindupindu kilienea nchi zima ikiwemo mji mkuu wa DRC, Kinshasa na kusababisha vifo vya watu zaidi ya 1,100 kati ya wagonjwa 55,000.© UNICEF/UNI418287/NdeboVyoo vilivyojengwa na UNICEF na wadau wake katika kambi ya wakimbizi wa ndani ya Bulengo magharibi mwa mji wa Goma jimboni Kivu Kaskazini nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC.Watu 159 wanatumia choo kimoja kambini DRCUNICEF inasema kwa familia zinazoishi kwenye kambi za wakimbizi wa ndani, uhaba mkubwa wa maji na huduma za kujisafi ni changamoto kubwa.Takribani watu 300,000 wakiwemo Watoto 183,000 hawana maji ya kutosha, chini ya theluthi moja wana huduma za vyoo, ikimaanisha watu 159 wanatumia choo kimoja.Uchunguzi wa kina uliofanywa na Wizara ya Afya ya Umma DRC kati ya mwezi Mei na Juni mwaka huu kwenye kaya zenye wagonjwa wa kipindupindu jimboni Kivu Kaskazini umebaini kuwa kati ya asilimia 62 hadi 99 ya kaya hizo ni familia ambazo mwaka jana zilifurushwa makwao.Uchunguzi huo ulibaini pia familia kwenye maeneo yenye kipindupindu zina changamoto nyingine za kiafya ikiwemo utapiamlo na ukosefu wa huduma za wajawazito na chanjo.UNICEF yahitaji dola milioni 62.5 kufanikisha operesheni zakeSasa UNICEF inatoa wito wa dola milioni 62.5 ili kuimarisha harakati zake za kinga na operesheni dhidi ya kipindupindu sambamba na huduma za kujisafi kwa miezi mitano ijayo.Fedha hizo zinalenga kufanikisha huduma hizo kwa watu milioni 1.8 wakiwemo watoto milioni 1.
8/18/20230
Episode Artwork

18 AGOSTI 2023

Kipindupindu chatishia uhai wa watoto DRC, UNICEF na wadau wachukua hatua.Heshima kwa Nafi Aïsha Diop mtaalamu wa usalama na ubora wa chakula wa WFP DRC.Makala leo tunaendelea na Gregory Akall, Msaidizi wa kibinadamu nchini Kenya hususan eneo la kaskazini mwa nchi akihudumu kupitia shirika la Umoja wa Mataifa la uratibu wa misaada ya kibinadamu na dharura.Na mashinani, ili kukabiliana na tatizo la utapiamlo na uhaba wa chakula katika mkoa wa Karamoja nchini Uganda Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula Duniani WFP linatumia vijana kama mawakala wa kuleta mabadiliko katika jamii zao.
8/18/20230
Episode Artwork

Methali: "Ukubwa jalala"

Dkt. Josephat Gitonga, kutoka Kenya ambaye ni Mhadhiri katika Chuo Kikuu cha Nairobi kwenye kitivo cha tafsiri na ukalimani anatufafanulia methali isemayo “Ukubwa ni jalala.”
8/17/20230
Episode Artwork

17 AGOSTI 2023

Siku ya watoa misaada ya kibinadamu huadhimishwa tarehe 19 ya mwezi Agosti kila mwaka kwa lengo la kutambua wale waliojitolea maisha yao kusaidia walio katika changamoto.Thomas Nyambane kutoka Kenya amekuwa mratibu wa misaada ya binadamu kwa zaidi ya miongo miwili na amehudumu kwenye mazingira magumu. Anaipenda kazi yake ila changamoto ni tishio la usalama na kila anapokuwa nje anaikumbuka sana familia yake kwani anapitwa na mengi. Hata hivyo, majukumu yake katika Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya kuratibu misaada ya binadamu na ile ya dharura, UNOCHA yanampa faraja kubwa kwani anapata nafasi ya kubadili maisha ya watu walio taabani.Mwandishi wetu wa Kenya ,Thelma Mwadzaya alikutana naye mjini Nairobi alipokuwako kwa muda mfupi kabla kurejea Somalia ambako ndiko kituo chake cha kazi. Hapa Thomas anaanza kwa kusimulia ilikoanzia safari yake.
8/17/20230
Episode Artwork

Sikufahamu jinsi ya kuzungumza na mwanangu kumuepusha na mimba za utotoni - Mzazi Haiti

Hebu fikiria kutarajia kupata mtoto wakati ambapo hata hufahamu neno ujauzito lina maana gani. Hicho ndicho kilichomfika mtoto mwenye umri wa miaka 14 nchini Haiti ambaye alijikuta anapewa ujauzito na kaka wa rafiki ya kiume wa rafiki yake. Hakuwa anajitambua akakubali kumsindikiza rafiki yake na zaidi ya yote akakubali urafiki na kijana huyo mwenye umri wa miaka 16. Mama yake binti huyu naye anasema hakufahamu ni kwa jinsi gani azungumze na mtoto wake ili kumuepusha na uhusiano na wavulana kwa lengo la kumuepusha kupata ujauzito. Maji yameshamwagika hayazoleki lakini shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ya Uzazi na Idadi ya watu, UNFPA nchini Haiti linachukua hatua kutoa eliu ya viungo vya uzazi na afya ya uzazi kwa wasichana na watoto wa kike ili kuepusha maji kumwagika zaidi ilhali hayazoleki. Simulizi ya mtoto huyo na kinachofanyika kuwasaidia ndio makala yetu ya leo inayoletwa kwako na Assumpta Massoi.
8/16/20230
Episode Artwork

WFP na mradi wa kushughulikia utapiamlo na kuinua kipato nchini Kenya

Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani WFP nchini Kenya linatekeleza mradi wa Mchepuko Chanya au Positive Deviance (PD) Heart unaolenga kuwasaidia kinamama kushughulikia na kuzuia utapiamlo kwa kutumia vyakula salama na vyenye lishe ambavyo vinalimwa na wanajamii wenyewe. Evarist Mapesa na maelezo zaidi.Katika Kaunti ya Baringo mradi wa PD Heart unaotekelezwa na WFP nchini Kenya umesaidia watoto kukarabati afya zao kwa kuwapatia kinamama ujuzi wa kuweza kushughulikia utapiamlo wakiwa majumbani pamoja na kuwafundisha wazazi wote namna bora yakupika vyakula vyenye virutubisho kwakutumia viungo vinavyopatikana katika maeneo yao. Mafanikio yamepatikana tayari kwa watoto kuongezeka uzito kutoka gramu 200 hadi 800 katika muda wa siku 12 hadi 30 shuhuda wa hilo ni Irene Menjo.  “Kile kilinifanya nijiunga na PD Heart ni mtoto wangu alikuwa na uzito mdogo nikamlisha mboga za majani kwa siku 12 na naona sasa hivi mtoto wangu amepata afya.”Mradi huo pia unawaunganisha wakulima na masoko kama anavyoeleza Caroline chedu Afisa mradi wa WFP. “Kila wiki wanapeleka mboga za majani katika shule mbalimbali lengo letu linalotuongoza ni kuongeza utofauti wa mlo kwa wanafunzi wanaoenda shule” Kwa watoto wengi wa Kaunti hiyo ya Baringo wanapoenda shuleni wanakuwa hawajala kitu chochote na Mwalimu Mkuu wa shule ya msingi Maji Moto Ann Mungai anasema wanashukuru pogramu za mlo shuleni.  “Tuna bahati nzuri ya kuwa na programu ya mlo shuleni inayotolewa na serikali. Mboga za majani zilizoongezwa kwenye vyakula vya watoto ni muhimu sana mosi vinafanya kuwa kitamu na pili kuwa na muonekano mzuri, utatamani kukila kwa jinsi kinavyoonekana. Na wakinamama nao wanafuraha kwani wananufaika na mradi huu kwakupata fedha kutokana na kuuza mboga za majani na pia kwa lishe.”WFP wanasema programu hii ni mbinu ya gharama nafuu ya kupunguza utapiamlo kwani imepunguza idadi kubwa ya watoto wanaopelekwa kwenye vituo vya kusaidia wenye utapiamlo. 
8/16/20230
Episode Artwork

Ripoti ya UNCTAD - Afrika inaweza kuwa kiungo muhimu katika minyororo ya ugavi duniani

Nchi za Kiafrika zinaweza kuwa washiriki wakuu katika minyororo ya ugavi duniani kwa kutumia rasilimali zao kubwa za nyenzo zinazohitajika na sekta za teknolojia ya juu na soko lao la wateja linalokua, imesema Ripoti ya Shirika la Biashara na Maendeleo la Umoja wa Mataifa (UNCTAD) kuhusu Maendeleo ya Kiuchumi Barani Afrika mwaka 2023 iliyozinduliwa leo jijini Nairobi, Kenya. Anold Kayanda na maelezo zaidi.Afisa Mchumi Mkuu wa UNCTAD ambaye pia ameongoza katika kuandika ripoti hii, Habiba Ben Barka anasema, “Wakati majanga ya kimataifa kama Covid, vita ya Ukraine na athari zingine zinazohusiana na tabianchi ziliathiri biashara na mnyororo wa usambazaji ulimwenguni kote kampuni nyingi za kimataifa zilianza kutafuta njia za kujenga uwezo wa kukabiliana na mitikisiko ya siku zijazo. Kwa hivyo, Ripoti ya Maendeleo ya Kiuchumi ya Afrika ya mwaka 2023 inaangalia mikakati, sera, na taratibu tofauti ambazo Nchi za Afrika zinaweza kuweka ili kuunganisha baadhi ya mnyororo huo wa ugavi.” Minyororo ya ugavi inajumuisha mifumo na rasilimali zinazohitajika kuendeleza, kuzalisha na kusafirisha bidhaa na huduma kutoka kwa wasambazaji hadi kwa wateja.  Kwa upande wake Katibu Mkuu wa UNCTAD Rebeca Grynspan ananukuliwa akisema, "Huu ni wakati wa Afrika kuimarisha nafasi yake katika minyororo ya ugavi duniani huku juhudi za usambazaji bidhaa zikiendelea. Pia ni fursa kwa bara la Afrika kuimarisha viwanda vinavyoibuka, kukuza uchumi na kutengeneza ajira kwa mamilioni ya watu wake."  © Nicholas Hopkins-HallWingi wa madini na vyuma muhimu barani Afrika, zikiwemo alumini, kobalti, shaba, lithiamu na manganisi, vipengele muhimu katika tasnia zinazotumia teknolojia kubwa, vinaliweka bara hili kama kivutio kwa viwanda, kwa sababu misukosuko ya hivi karibuni iliyosababishwa na mtikisiko wa biashara, matukio ya kijiografia na kutokuwa na uhakika wa kiuchumi zinalazimisha wazalishaji kugawanya maeneo yao ya uzalishaji. Afrika pia inatoa faida kama vile ufikiaji mfupi na rahisi zaidi wa pembejeo za msingi, nguvu kazi ya vijana  inayofahamu teknolojia, na inayoweza kubadilika, na tabaka la kati linalokua na linalojulikana kwa kuendelea kuhitaji bidhaa na huduma za hali ya juu zaidi. Kuimarisha minyororo ya ugavi barani Afrika ni muhimu kwa ukuaji wa kanda Ripoti hiyo inaangazia kwamba kuunda mazingira yanayofaa kwa viwanda vinavyotumia teknolojia kubwa kutasaidia kuongeza mishahara katika bara hilo, ambayo kwa sasa imewekewa kima cha chini cha dola 220 kwa mwezi, ikilinganishwa na wastani wa dola 668 katika bara la Amerika. Ushirikiano wa kina katika minyororo ya ugavi wa kimataifa pia utaleta mseto katika uchumi wa Kiafrika, na kuongeza mnepo wao kwa majanga yajayo. Aidha ripoti inaeleza kuwa kupanua minyororo ya usambazaji wa nishati barani Afrika pia ni fursa ya kuharakisha hatua za kukabiliana na mabadiliko ya tabia nchi. Uwezo mkubwa wa nishati mbadala wa bara hili, hasa katika nishati ya jua, unaweza kusaidia kupunguza gharama za uzalishaji na kupunguza utegemezi wa vyanzo vya nishati vinavyotokana na mafuta. Afrika inahitaji uwekezaji zaidi katika nishati mbadala ili kusaidia kuziba pengo kubwa la uwekezaji na kukabiliana na vikwazo vingine kwenye utengenezaji wa paneli za miale ya jua barani humo. Hivi sasa, ni takribani asilimia 2 tu ya uwekezaji wa kimataifa katika nishati mbadala inayoenda Afrika. Ukuaji wa uwekezaji katika nishati mbadala, kama ilivyooneshwa na UNCTAD, unaweza kukuza utengenezaji wa paneli za jua barani Afrika. Kwa mfano, mwaka wa 2022, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo (DRC) ilikuwa mzalishaji mkubwa zaidi wa shaba barani Afrika, ikiwa na tani milioni 1.8 za metriki na zaidi ya uchunguzi na uchimbaji, nchi hiyo inaweza kuwa mahali pazuri pa kusafisha bidhaa za chuma kwa tasnia ya magari ya umeme. Wekeza katika miundombinu, teknolojia na ufadhili Nchi 17 za Afrika, zikiwemo Angola, Botswana, Ghana na Afrika Kusini, tayari zimetekeleza…
8/16/20230
Episode Artwork

16 AGOSTI 2023

Afrika inaweza kuwa kiungo muhimu katika minyororo ya ugavi duniani - Ripoti ya UNCTAD.Mradi wa PD wa WFP Kenya washughulikia utapiamlo na kuinua kipato cha wakulima.Sikufahamu jinsi ya kuzungumza na mwanangu kumuepusha na mimba za utotoni - Mzazi HaitiMashinani ni ushauri wa Issa Ibrahim Shauri anayefahamika kama mgonjwa wa mwisho nchini Tanzania wa  virusi vya polio aina ya 1. 
8/16/20230
Episode Artwork

15 AGOSTI 2023

Tarehe 19 mwezi huu wa Agosti siku ya ubinadamu duniani ikilenga kutambua watu wanaojitoa kwa moyo wao wote kusaidia wale walio kwenye uhitaji. Miongoni mwa watu hao ni Gregory Akall, Afisa huyu wa ubinadamu kwenye shirika la Umoja wa Mataifa la kuratibu misaada ya binadamu,UNOCHA. Eneo lake la kufanyia kazi ni kaskazini mwa Kenya ambako ukame, uhaba wa maji na njaa ni matatizo makubwa yanayowazonga wakaazi kila uchao. Gregory Akall mwenyewe ni mturkana kutoka eneo hilo la kaskazini mwa Kenya, hivyo kufanya kazi eneo hilo ni sawa na mcheza kwao. Je, kama mratibu wa misaada ya binadamu kwenye shirika la UNOCHA, siku yake huanza vipi? Hilo ndilo swali mwandishi wetu wa Kenya Thelma Mwadzaya aliloanza kumuuliza alipokutana naye mjini Nairobi, Kenya.
8/15/20230
Episode Artwork

Kamishna Susan aelezea ambacho hatosahau wakati wa huduma yake Abyei

Hii leo katika makala nakukutanisha na Kamishna Susan Kaganda, Mkuu huyu wa Utawala na Raslimali watu katika Jeshi la Polisi Tanzania ambaye aliwahi kuwa Mkuu wa  Operesheni kwenye ujumbe wa muda wa Umoja wa Mataifa wa mpito kwenye eneo la Abyei lililoko katikati ya Sudan na Sudan Kusini, UNISFA. Katika mahojiano yake na Stella Vuzo wa Kituo cha Habari cha Umoja wa Mataifa, UNIC Dar es salaam nchini Tanzania anasimulia mambo kadhaa ikiwemo hili analoanza nalo la jambo gani anakumbuka zaidi wakati akihudumu UNISFA. 
8/15/20230
Episode Artwork

Tiba asilia duniani: Takriban nusu ya nchi wanachama wa WHO wanazitambua na kuzitumia

8/14/20230
Episode Artwork

Wataalam UN: Watalibani wanazidi kukandamiza raia kinyume na madai yao

8/14/20230
Episode Artwork

14 AGOSTI 2023

Watalibani wanazidi kukandamiza raia kinyume na madai yao - Wataalam UN.Takriban nusu ya nchi wanachama wa WHO wanatambua na kutumia tiba asilia.Kwenye makala ni Suzan Kaganda, Kamishna wa Utawala na Rasilimali watu katika Jeshi la Polisi Tanzania ambaye aliwahi kuwa Mkuu wa Operesheni kwenye ujumbe wa muda wa Umoja wa Mataifa kwenye eneo la Abyei lililoko katikati ya Sudan na Sudan Kusini, UNISFA. Mashinani ni ujumbe wa mama mnufaika wa huduma za afya hususan za uzazi nchini Rwanda.
8/14/20230
Episode Artwork

Wakazi wa Darfur Magharibi hatimaye wafikishiwa chakula – WFP

Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP hatimaye limethibisha hofu yake juu ya viwango vya juu vya njaa nchini Sudan baada ya kuweza kwa mara ya kwanza kufikisha msaada wa chakula kwa wakazi wa Darfur Magharibi nchini humo tangu kuzuka kwa vita mwezi Aprili mwaka huu huku mamilioni ya watu wakiwa hawana chakula. Punde tu baada ya vita kuanza mwezi APrili mwaka huu  nchini Sudan, WFP ilitabiri kuwa njaa inaweza kuongezeka na kukumba zaidi ya watu milioni 19 katika miezi ijayo.   Eddie Rowe Mkurugenzi wa WFP nchini Sudan akizungumza na waandishi wa habari jijini Geneva Uswisi kwa njia ya video kutoka mji wa Port Sudan amesema, "sasa ikiwa ni miezi takribani minne tangu vita ianze, utabiri huo mchungu umethibitika kuwa ukweli mchungu." Amenukuu taarifa ya shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) kwamba ripoti mpya ya uhakika wa kupata chakula (IPC) imeonesha kuwa vita imetumbukiza zaidi ya watu milioni 20 kwenye njaa kali. Idadi hiyo ni sawa na asilimia 42 ya wananchi wa Sudan.  Watu milioni 6.3 kati yao hao milioni 20 wenye njaa Sudan, wako katika kiwango cha juu zaidi cha njaa, ikiwa ni hatua moja kabla ya kuwa na baa la njaa.  Licha ya changamoto ya usalama, Bwana Rowe amesema wiki iliyopita wameweza kwa mara ya kwanza kufikishia wakazi wa Darfur Magharibi msaada wa chakula kupitia mpaka wa mashariki mwa Chad, msaada ulionufaisha watu 15,400 kwenye vijiji vya Adikong, Shukri, na Jarabi.   Amesema ni matumaini yake njia hiyo itaendelea kutumika kwa ajili ya kupitishia misaada huko Geneina, mji muu wa jimbo la Darfur MAgharibi ambako miji na vijijii vimetelekezwa na waliosalia ni wanawake na watoto bila huduma za afya na miundombinu mingine muhimu.  
8/11/20230
Episode Artwork

Manusurua kutoka Gambia: Sitamani tena kuzamia kwenda ulaya

Kila mwaka maelfu ya wahamiaji kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo Afrika hujaribu kufika Ulaya wakivuka Bahari ya Mediterania wakieleza kwenda kusaka maisha bora lakini safari hiyo inaelezwa kuwa ni hatari sana kwani maelfu ya watu hufa maji au kutoweka. Ni Amadou Jobe kijana ambaye akiwa na umri wa miaka 25 alianza safari ya hatari kutoka nchini Kwake Gambia kupitia kaskazini mwa Afrika lengo likiwa Kwenda nchini Italia kusaka maisha bora kwani alikuwa akiishi katika hali ya umasikini na alitamani kuja kuisaidia familia yake iwapo angefanikiwa kufika Ulaya. Safari ya Amadou haikuwa rahisi kwa zaidi ya miaka miwili alikuwa safarini kutoka nchini mwake Gambia alienda mpaka nchi ya Mauritani, kisha Mali, akaingia Niger na mwisho nchini Libya nchi ambayo baada ya kukaa zaidi ya mwaka mmoja alifanikiwa kupata boti ambayo ndio ingetimiza ndoto yake ya Kwenda Ulaya. “Ndani ya boti yetu, kulikuwa na zaidi ya watu 100 kutoka Gambia, watu wengine niliowakuta ni Wanigeria na wengine wanatoka Liberia kiufupi kulikuwa na nchi  kutoka barani Afrika. Siku tulipojaribu kuvuka Kwenda Ulaya, boti yetu ilikuwa na matatizo na hali ya hewa pia haikuwa nzuri. Tuliona maji yakijaa ndani ya boti yetu. Kwa hivyo tuliamua kurudi kwa sababu kama tukitaka kuendelea, tungaweza wote kufamaji huko.” Bahati haikuwa yake kwani alipojaribu kusafiri awamu ya pili walikamatwa na kufingwa jela nchini Libya anasema maisha jela yalikuwa mabaya na baadae Shirika la Umoja wa Mataifa la Uhamiaji IOM liliwatembelea gerezani na kuwapa fursa ya kurejeshwa makwao na Amadou naye alirejea.“Sikuwa nataka kurudi hapa. Nilitaka kuendelea na safari yangu. Nina huzuni sana kwa sababu pesa zote nilizotumia, nilipoteza kila kitu na kuja kuanza upya kutoka sifuri. Nimetumia karibu dola 1700. Lakini hakuna la kufanya. Mahali tulipokuwa tusingeweza kwenda kokote na hauwezi kutoroka.” Marie Stella Ndiaye ni meneja program wa IOM nchini Gambia anaeleza baada ya kuwajeresha makwao hawawaachi pia wa programu za kuwasaidia.  “Tumejikita kwenye kuwatafuta na kuokOa maisha yao. Pia tunatoa usaidizi kwenye vituo vya rasilimali za wahamiaji vilivyo katika nchi ambazo wahamiaji hawa hupita wakitaka kusafiri Kwenda ulaya. Mara tu wanaporejea, IOM inatoa usaizi wa kila aina kuanzia masuala ya ushauri nasaha, ujumuishaji wa kiuchumi, ujumuishaji upya wa kijamii, lakini pia, muhimu zaidi, usaidizi wa kisaikolojia.” Mara bada ya kurejea nchini Gambia Amadou alipata ufundi stadi kutoka mashirika ya UN ambayo ni IOM na UNCDF na sasa anafanya kazi ya fundi uashi, ameoa na ana watoto wawili. Ameapa kutojaribu tena kuzamia kwenda ulaya, ataenda bara hilo kwa kupanda ndege kihalali nasi vinginevyo.  
8/11/20230
Episode Artwork

Kijana Florent: Vijana DRC tunahaha kujikwamua kiuchumi lakini usalama unatukwamisha

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC, vijana kesho wataadhimisha siku yao duniani huku kiza kinene cha ukosefu wa usalama kikiwa kimetanda mashariki mwa taifa hilo la ukanda wa Maziwa Makuu barani Afrika. Wakati Umoja wa Mataifa ukipigia chepuo vijana kushika hatamu ya kusongesha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs ikiwemo hatua kwa tabianchi, kutokomeza umaskini na ajira zenye hadhi, kwa vijana wa mashariki mwa DRC vuguvugu hilo linakumbwa na kikwazo cha usalama hata kama wawe wamepata elimu. Shuhuda wa changamoto hizo ni kijana Florent Muhindo Nambura mkazi wa Beni jimboni Kivu Kaskazini na amefunguka hali halisi ilivyo akizungumza na George Musubao, mwandishi wetu DRC. Florent anaanza kwa kuelezea kile anachofanya. 
8/11/20230
Episode Artwork

11 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia Siku ya Vijana Duniani ambayo inaadhimishwa tarehe 12 Agosti 2023 kila mwaka na tutafuatilia kazi za vijana waliorejea nyumbani Gambia kutoka Ulaya. Pia tuanaangazia msaada wa kibinadamu Sudan. Makala tunakupeleka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC na mashinani Jamhuri ya Afrika ya Kati, CAR, salía papo hapo!Shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Chakula duniani, WFP hatimaye limethibisha hofu yake juu ya viwango vya juu vya njaa nchini Sudan baada ya kuweza kwa mara ya kwanza kufikisha msaada wa chakula kwa wakazi wa Darfur Magharibi nchini humo tangu kuzuka kwa vita mwezi Aprili mwaka huu huku mamilioni ya watu wakiwa hawana chakula. Assumpta Massoi na maelezo zaidi. Kila mwaka maelfu ya wahamiaji kutoka maeneo mbalimbali ikiwemo Afrika hujaribu kufika Ulaya wakivuka Bahari ya Mediterania wakieleza kwenda kusaka maisha bora lakini safari hiyo inaelezwa kuwa ni hatari sana kwani maelfu ya watu hufa maji au kutoweka. Evarist Mapesa anatupeleka nchini Gambia kusikia simulizi wa kijana ambaye chupuchupu apoteze maisha.Hii leo katika Makala tunakwenda Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC ambako mwandishi wetu George Musubao amezungumza na kijana Florent Muhindo Nambura mkazi wa Beni jimboni Kivu Kaskazini ikiwa ni kuelekea maadhimisho ya siku ya vijana duniani tarehe 12 mwezi huu wa Agosti. Florent anaanza kwa kuelezea kile afanyacho.Mashinai tunakupeleka katika kambi ya wakimbizi ya Birau nchini CAR, ambako kijana mkimbizi kutoka Sudan hajafa moyo na anatarajia kutimiza ndoto zake na zile za watoto wakibizi walioko kambini humo.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/11/20230
Episode Artwork

Methali: "Mchakacho ujao haulengwi jiwe."

Katika kujifunza lugha ya kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania anachambua methali "Mchakacho ujao haulengwi jiwe."
8/10/20230
Episode Artwork

10 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ikimulika kazi ya vijana katika kusongesha malengo ya maendeleao endeleu na tunaelekea huko mkoani Mwanza kaskazini Magharibi mwa Tanzania ambapo kijana Mbunifu Kelvin Paul amekuwa akibuni vifaa mbalimbali vya kiteknolojia ili kufanikisha lengo namba 4 linalozungumzia Elimu kwa wote ifikapo Mwaka 2030. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo kutoka nchini Chad, Niger na Ethiopia. Katika kujifunza Kiswahili  tunapata uchambuzi wa methali “Mchakacho ujao haulengwi jiwe.” Huku duru za habari zikiripoti kuwa Rais wa Niger Mohamed Bazoum na familia yake wanashikiliwa na walinzi wa Rais bila huduma kama umeme, dawa chakula na maji, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres ameeleza kusikitishwa na hali hiyo na kutaka wanaomshikilia wamwachilie huru bila  masharti. Kamisheni ya kimataifa ya wataalamu wa haki za binadamu kuhusu Ethiopia leo imesema ina wasiwasi mkubwa kuhusu ripoti ya kudorora kwa hali ya usalama kwenye ukanda wa kaskazini-magharibi mwa Ethiopia hususan jimbo la Amhara ambako huko Baraza la Mawaziri lilitangaza hali ya dharura tarehe 4 mwezi huu kinyume na katiba ya nchi.Na nchini Chad, zaidi ya watu 50 waliokimbia machafuko nchini Sudan wamepata hifadhi kwenye nyumba ya Fatna Hamid, jambo linalofanywa na raia wengi wa Chad wakati huu ambapo zaidi ya wakimbizi 320,000 wameingia mashariki mwa Chad tangu mapigano yaanze Sudan mwezi April mwaka huu. Fatna anasema, “Wengi wananifahamu tangu zamani na baadhi ni wagonjwa hawana mtu wa kuwahudumia. Wanahitaji msaada kwa sababu hawana chochote.”Na katika kujifunza kiswahili Dkt. Mwanahija Ali Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania anachambua methali Mchakacho ujao haulengwi jiwe.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/10/20230
Episode Artwork

Vijana wa jamii ya asili tuna nafasi kubwa kusongesha jamii zetu

Katika kuadhimisha siku ya kimataifa ya jamii ya watu wa asili hii leo, ambayo maudhui yake yanalenga vijana na nafasi yao katika kusongesha tamaduni na ufahamu wa jamii hizo Idhaa ya Kiswahili ya Umoja wa Mataifa ilibisha hodi nchini Kenya, Mashariki mwa Afrika ambako kuna vijana wa jamii ya asili wanachukua hatua. Lengo ni kufahamu nafasi yao hivi sasa na nini wanafanya kuona mustakabali wao unaimarika. Vijana hao Virginia Sintanai wa jamii ya Ilchamus na pia mwanachama wa Mtandao wa vijana wa jamii ya asili nchini Kenya (KIYN). Mwingine ni Bernard Loolasho wa jamii ya Yiaku kutoka mpango wa hifadhi ya jamii ya Laikipia kaskazini, (LANCCI). Tunaanza na Virginia. 
8/9/20230
Episode Artwork

09 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia siku ya watu wa asili ambapo umoja wa mataifa umepongeza vijana wa jamii hizo kwa kazi zao za kusongesha malengo ya maendeleo endelevu.  Pia tunakupeleka nchini Rwanda na Kenya, kulikoni?Hii leo ni siku ya jamii ya watu wa asili duniani ambapo maudhui ni vijana, ikisherehekea vijana wa jamii ya asili na dhima yao katika kuleta mabadiliko na kuumba mustakabali wa dunia. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametoa ujumbe wake. Wakati dunia ikiwa na maono mbalimbali juu ya ukuaji wa mtandao wa intaneti na namna unavyoweza kuwasaidia, Mwakilishi Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Rwanda Ozzonia Ojielo amesema ni vyema maono hayo kuhakikisha hakuna mtu anaachwa nyuma.Makala tunakupeleka Kenya kupata ujumbe kutoka kwa vijana wa jamii ya asili ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya jamii ya asili ikimulika zaidi vijana.Na katika mashinani Hapo baadaye ni mashinani na ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya watu wa asili tutakuletea ujumbe kuhusu haki za wasichana na wanawake, hususan wanaolelewa katika jamii za watu wa asili.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu sana!
8/9/20230
Episode Artwork

Wananchi wakipatiwa elimu ya kidigital watakuza maendeleo ya Taifa

Wakati dunia ikiwa na maono mbalimbali juu ya ukuaji wa mtandao wa intaneti na namna unavyoweza kuwasaidia, Mwakilishi Mkaazi wa Umoja wa Mataifa nchini Rwanda Ozzonia Ojielo amesema ni vyema maono hayo kuhakikisha hakuna mtu anaachwa nyuma.  Ni Mwakilishi Mkaazi wa UN nchini Rwanda akizungumza katika jukwaa la kujadili utawala wa mtandao lililofanyika huko nchini Rwanda likikutanisha wadau wa masuala ya mtandao ili kuangalia namna bora ya kuhakikisha jamii nzima inanufaika na maendeleo ya kiteknolojia yanayoletwa na huduma ya mtandao. Katika hotuba yake Ojielo amesema, “Ahadi yetu ya kumjumuisha kila mtu inaanza kwa kuhakikisha kuna upatikanaji sawa wa mtandao kote nchini Rwanda kuanzia mijini mpaka vijijini. Kuunganishwa na mtandao haipaswi kuwa fursa bali haki ya msingi inayopatikana kwa wote.” Mkuu huyo wa UN nchini Rwanda amesema pamoja na kufikishiwa huduma ya mtandao lakini pia wananchi wapatiwe elimu.“Kwa kukuza elimu ya kidigitali, tutawawezesha watu binafsi kuchangamkia fursa katika elimu, ujasiriamali, na ushiriki wa kiraia, hatimaye hivi vyote vitasaidia kuendeleza maendeleo ya taifa letu.” Katika hotuba yake hiyo pia ameipongeza serikali ya Rwanda kwa kupitisha sheria ya kulinda taarifa za watumia mitandao ya mwaka 2021 pamoja na sera ya kitaifa ya Akili Mnemba au AI ya mwaka 2022 na kusema juhudi hizo zinaonesha nia ya dhati ya serikali ya Rwanda ya kuendelea kidijitali, kibunifu na kuwalinda wananchi wake. 
8/9/20230
Episode Artwork

UN wawapongeza vijana wa jamii ya asili kwa kutokubali ukandamizaji wa jamii zao

Hii leo ni siku ya jamii ya watu wa asili duniani ambapo maudhui ni vijana, ikisherehekea vijana wa jamii ya asili na dhima yao katika kuleta mabadiliko na kuumba mustakabali wa dunia. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ametoa ujumbe wake. Katika ujumbe wake wa siku hii iadhimishwayo tarehe 9 mwezi Agosti ya kila mwaka, Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres anasema duniani kote watu wa jamii ya asili wanakabiliwa na changamoto, ardhi na rasilimali zao zikitishiwa haki zao zikikandamizwa na changamoto yao ya kila uchao ya kuenguliwa na kutengwa. Hata hivyo amesema vijana wa jamii ya asili wanapambana kupinga vitisho hivyo kwa kuchukua hatua. Katibu Mkuu amesema wao ni viongozi wa vuguvugu la hatua kwa tabianchi duniani. Ni wachechemuzi wa haki, wanafurahia tamaduni zao, wanasongesha haki za binadamu na kuhamasisha uelewa wa watu kuhusu historia ya watu wa jamii ya asili na masuala yao duniani kote. Kama hiyo haitoshi, Bwana Guterres amesema vijana hao wanajifunza kutoka kwa wazee wao, wakihakikisha tamaduni za watu jamii ya asili, busara na utambulisho wao vinasonga mbele badala ya kutoweka. Ufahamu wa watu wa jamii ya asili na tamaduni zao zimejikita mizizi katika maendeleo endelevu na vinaweza kusaidia kutatua changamoto nyingi za pamoja. Ni kwa sababu hiyo Katibu Mkuu anasema ni muhimu vijana wa jamii ya asili, wote wake kwa waume, wavulana na wasichana washiriki katika upitisha wa maamuzi. Bwana Guterres amesema chaguo lifanyikalo leo litaamua dunia ya kesho hivyo ametaka kila mtu apatie msisitizo  ahadi yake ya kuhakikisha haki za mtu mmoja mmoja na za kijamii kwa watu wa asili na wakati huo huo kusaidia ushiriki wao katika mijalada dunian ina upitishaji wa maamuzi. Ametamatisha ujumbe wake akisma kwa pamoja hebu tujenge mustakabli bora kwa sisi sote. 
8/9/20230
Episode Artwork

Watoto wanaonyonyeshwa maziwa ya mama wana afya bora - UNICEF Kenya

Wiki ya unyonyeshaji mtoto maziwa ya mama duniani, imehitimishwa Agosti 7, au jana Jumatatu, wiki iliyosheheni matukio ya kuonesha hatua za kuhakikisha watoto wanapozaliwa wananyonyeshwa maziwa ya mama kwa faida sio tu ya mtoto bali pia mama. Nchini Kenya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF na Wizara ya Afya, walikuwa na tukio la aina hiyo na shuhuda wetu alikuwa mwandishi wetu nchini Kenya, Thelma Mwadzaya.
8/8/20230
Episode Artwork

08 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kinaambapo wiki ya unyonyeshaji mtoto maziwa ya mama duniani, imehitimishwa Agosti 7, au jana Jumatatu, wiki iliyosheheni matukio ya kuonesha hatua za kuhakikisha watoto wanapozaliwa wananyonyeshwa maziwa ya mama kwa faida sio tu ya mtoto bali pia mama. Nchini Kenya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia watoto UNICEF na Wizara ya Afya, walikuwa na tukio la aina hiyo na shuhuda wetu alikuwa mwandishi wetu nchini Kenya. Mashinani tutakupeleka kijijini Mauratou nchini Fiji kushuhudia jinsi wakulima wanawake wanavyoweza kukabiliana na tatizo la kupanda kwa bei ya chakula na bidhaa zingine. Wakati idadi ya watu wanaokimbia machafuko nchini Sudan ikifikia milioni 4, Shirika la Umoja wa Mataifa linalojihusisha na masuala ya wakimbizi UNHCR limesema lina wasiwasi mkubwa kuhusu kuzorota kwa afya za wakimbizi hao ikiwa ni pamoja na wale wanaoishi katika kambi za wakimbizi. Tukisalia na vita vya Sudan, nalo shirika la Afya la Umoja wa Mataifa WHO limeeleza kukabiliwa na uhaba wa vifaa tiba pamoja na huduma za maji na umeme katika maeneo yaliyoathirika na vita.Na katika pwani ya Lampedusa nchini Italia Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya watoto UNICEF limesikitishwa na ajali nyingine ya meli katika bahari hiyo ya Mediterania.Na katika mashinani wanawake wakulima nchini Fiji, kufuatia mafunzo yanoyotolewa na Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo duniani, IFAD wameweza kubadilisha bidhaa zinazotoka nje kama vile unga na aina zinazozalishwa nyumbani.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/8/20230
Episode Artwork

OCHA: Maisha ya kila siku nchini Sudan ni jinamizi

Mkuu wa kitengo cha Operesheni na Uchechemuzi kwenye Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na masuala ya kibinadamu na kuratibu masuala ya dharura OCHA Edem Wosornu amesema maisha ya kila siku ya wananchi nchini Sudan yamegubikwa na sintofahamu kutokana na vita inayoendelea hivyo amesihi pande husika kukomesha mapigano na wakati huo huo wahisani waongeze ufadhili wa kibinadamu. Akihojiwa na Idhaa ya kiarabu ya Umoja wa Mataifa Bi. Wosornu ambaye alikuwa ziarani nchini humo hivi karibuni, amesema hali ya sintofahamu imekumba wananchi akitolea mfano Hawaa, mama, bibi na mfanyabiashara ambaye alikuwa mchuuzi nje kidogo ya mji mkuu wa Sudan Khartoum ambaye sasa tangu vita ianze hawezi kujikimu bali anategemea malipo kidogo ya fedha kila mwezi ili anunue dawa za kujitibu kisukari. Na kwa watoa misaada ya dharura nao hali ni mbayá,  “Na niliwauliza maisha yako vipi kwa mtu wa kawaida mjini Khartoum? Na wakasema ni kama jinamizi kwa sababu hufahamu kama upande wowote ule utakukamata na kukuweka ndani. Hufahamu iwapo utatoweshwa. Lakini wanaendelea na maisha kwa sababu wameazimia kuliko wakati wowote ule kusambaza misaada ya kiutu.” Afisa huyo wa OCHA ametoa wito kwa wahisani wengine zaidi wajitokeza kuchangia ili kufanikisha mahitaji ya wananchi wa Sudan huku akipeleka ujumbe kwa pande kinzani ambazo ni jeshi la serikali, (SAF) na wanamgambo waasi wa kikundi cha Rapid Support Forces (RSF), “Ujumbe wangu kwa pande kinzani ni ujumbe ambao wasudan wamenieleza nilipotembelea Sudan. Acheni vita. Acheni mapigano ma tuacheni turejee majumbani mwetu na tuishi maisha yetu.” 
8/7/20230
Episode Artwork

Mauritius waelekeza mbinu wanazotumia kutokomeza uvutaji wa tumbaku nchini mwao

Mwishoni mwa mwezi Julai mwaka huu shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya Afya WHO walitoa ripoti ya 9 kuhusu janga la uvutaji tumbaku na kueleza kuwa mafanikio yameanza kuonekana kwa nchi wanachama kutekeleza sera ya kulinda umma kutoathirika na uvutaji wa sigara unaofanywa na mtu mwingine ambapo zaidi ya watu bilioni 5.6 wamenufaika na sera hiyo ulimwenguni kote. Nchi ya Mauritius ilipongezwa kwa kuwa nchi pekee iliyotekeleza vyema sera zote sita za kupambana na athari za tumbaku. Je waliwezaje? Tuungane na Hapinness Palangyo wa redio washirika akitusomea makala hii iliyoandaliwa hapa studio. 
8/7/20230
Episode Artwork

07 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia mizozo Sudan na ukulima wa mboga mboga nchini Benin. Makala tunakupeleka nchini Mauritius na mashinani nchini Kenya, kulikoni?  Mkuu wa kitengo cha Operesheni na Uchechemuzi kwenye Ofisi ya Umoja wa Mataifa inayohusika na masuala ya kibinadamu na kuratibu masuala ya dharura OCHA Edem Wosornu amesema maisha ya kila siku ya wananchi nchini Sudan yamegubikwa na sintofahamu kutokana na vita inayoendelea hivyo amesihi pande husika kukomesha mapigano na wakati huo huo wahisani waongeze ufadhili wa kibinadamu. Nchini Benin, mradi unaofadhiliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji, UNCDF umewezesha vijana waliokuwa wanazurura wakati wa msimu wa mwambo nchini humo kuweza kuendelea na shughuli za kilimo kutokana na mradi huo kuwapatia pampu za kusukuma maji ya umwagiliaji kwa kutumia nishati ya sola.Makala tuankupeleka nchini Mauritius ambapo hivi karibuni imepongezwa kwa kuwa nchini ya kwanza Barani Afrika kupunguza kwa kiasi kikumbwa athari za matumizi ya tumbaku kwa umma.Na katika mashinani tutakupeleka nchini Kenya kusikia ujumbe wa mwanaharakati wa mazingira na tabianchi kuhusu vijana wa vijijini na jukumu lao muhimu katika kukabiliana na ukosefu wa chakula na mabadiliko ya tabianchi.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/7/20230
Episode Artwork

Mradi wa maji unaotumia sola Benin waepusha vijana na uzururaji wakati wa mwambo

Nchini Benin, mradi unaofadhiliwa na shirika la Umoja wa Mataifa la Mfuko wa Maendeleo ya Mitaji, UNCDF umewezesha vijana waliokuwa wanazurura wakati wa msimu wa mwambo nchini humo kuweza kuendelea na shughuli za kilimo kutokana na mradi huo kuwapatia pampu za kusukuma maji ya umwagiliaji kwa kutumia nishati ya sola. Ni Issotina Nala huyo kijana mkulima wa mboga mboga mwenye umri wa miaka 32 akizungumza kwa furaha juu ya manufaa ya pampu inayotumia nishati ya jua au sola na mfumo wa umwagiliaji maji uliofanikihswa na UNCDF hapa Kijiji cha Wekete jimbo la Ouake, kaskazini magharibi mwa Benin, huko Afrika Magharibi.  “Ndio, inaleta tofauti kubwa sasa na kwa siku za usoni, kwa kuwa hatutakosa kipato. Kwa sababu mimi nina wake wawili na Watoto. Kwa pampu hii Watoto wangu wataweza Kwenda shuleni, na familia yangu itakuwa na ahueni.” Cossova Nanako, Mkuu wa Programu za UNCDF Benin anasema suala kwamba kuna uhaba wa maji kutokana na mabadiliko ya tabianchi tunabaini kuwa vijana wengi wanakuwa hawana cha kufanya msimu wa ukame kuanzia mwezi Oktoba hadi Aprili.  Bwana Nala akiwa kwenye bustani yake ya mboga anakiri.. “Hakuna maji kuanzia Oktoba hadi Machi kwa hiyo tunabakia nyumbani. Na unaweza kufanya nini bila maji? Ukiwa na bustani ya mboga unapaswa kuwepo bustani kila wakati.” UNCDF inasema hali hiyo inalazimu vijana kuondoka vijijini na kuelekea mijini kutafuta vibarua lakini kupitia mradi huu uitwalo LoCAL wa kuwezesha wakazi kuhimili mabadiliko ya tabiachi nchi sasa kuna nuru na Bwana Nala anasema,  “Sasa na mfumo huu wa umwagiliaji, hakuna tena kupumzika na tutakuwa na muda wa kufanya kazi wakati wowote.” UNCDF inasema sasa wakulima wanaweza kulima misimu yote hata wakati wa ukame na hivyo kuwa na uhakika sio tu wa chakula bali pia kipato kwa ajili ya familia zao. 
8/7/20230
Episode Artwork

Amina J. Mohammed ziarani Amazon: Nimesikia maombi yenu na tutapaza sauti

Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed anaendele ana ziara yake ya siku tano nchini Brazil ambapo siku ya Alhamisi Agosti 3, 2023 alizuru jamii ya watu wa asili ya Mapuera kwenye ukanda wa Amazon jimboni Para ambako huko alipata fursa ya kuzungumza na wanajamii hao na kusikia maombi yao, ziara ambayo anafanya kufuatilia utekelezaji wa malengo ya maendeleo endelevu, SDGs kuelekea mkutano wa viongozi kuhusu SDGs mwezi Septemba mwaka huu. Thelma Mwadzaya anatusimulia kilichojiri. 
8/4/20230
Episode Artwork

Türk asikitishwa baada ya ofisi ya UN ya Haki za Binadamu Uganda yafungwa

Kamishna mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Haki za Binadamu  UN Volker Türk, hii leo ameelezea masikitiko yake makubwa kufuatia kufungwa kwa ofisi yake nchini Uganda kufuatia uamuzi wa serikali hiyo kutotia saini mkataba wa kuendelea kuweko kwa ofisi hiyo nchini humo. Taarifa iliyotolewa leo huko Geneva, Uswisi na Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu (OHCHR) imesema tayari ofisi ndogo za Gulu na Maroto zilifungwa tarehe 30 Juni na 31 Julai mtawalia, huku ofisi kuu ya jijini Kampala ikifungwa kesho Jumamosi Agosti 5. Bwana Türk  amesema “nasikitika ofisi yetu Uganda inafungwa baada ya kuweko nchini humo kwa miaka 18, ambapo tuliweza kushirikiana na mashirika ya kiraia, watu kutoka pande mbalimbali nchini Uganda pamoja na taasisi za serikali kusongesha na kulinda haki za binaamu za waganda wote.” Amesema tangu kuanzishwa kwa ofisi hiyo mwaka 2005 wameshirikiana na serikali na wadau kwenye masuala kama vile kujumuisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs kwenye mipango ya kitaifa na kushauri juu ya kuoanisha sheria za nchi na sheria za kimataifa za haki za binadamu. Hata hivyo amesema licha ya maendeleo makubwa yaliyopatikana kwenye haki za binadamu Uganda bado kuna changamoto kubwa za haki za binadmau, akitaja hususan hofu juu ya haki za binadamu kuelekea uchaguzi mkuu wa Uganda mwaka 2026 ambako watetezi wa haki, wawakilishi wa mashirika ya kiraia na waandishi wa habari wanafanya kazi katika mazingira magumu. Bwana Türk ameonya juu ya uwezekano wa kudorora kwa ahadi za Uganda kwenye mikataba ya kimataifa ya haki za binadamu iliyoridhia, ikiwemo kupitishwa kwa sheria dhidi ya ushoga ambayo tayari imekuwa na madhara kwa waganda. Kamishna huyo Mkuu wa Haki za Binadamu ameisihi serikali ya Uganda ihakikishe kuwa taasisi ya kitaifa ya haki za binadamu inafanya kazi kwa ufanisi, kwa uhuru kama chombo chenye jukumu la kusimamia haki nchini humo. Amesema kwa upande wake, Ofisi ya Umoja wa Mataifa ya Haki za Binadamu inasalia kuendelea kushughulikia haki za binadamu Uganda kwa mujibu wa mamlaka ya kimataifa. 
8/4/20230
Episode Artwork

04 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia haki za binadamu na Akili Mnemba au ‘Artificial Intelligence’.  Makala tunakupeleka nchini Brazil na mashinani tutasikia ujumbe wa kijana kutoka Tanzania, salía papo hapo!  Kamishna mkuu wa Umoja wa Mataifa kuhusu Haki za Binadamu UN Volker Türk, hii leo ameelezea masikitiko yake makubwa kufuatia kufungwa kwa ofisi yake nchini Uganda kufuatia uamuzi wa serikali hiyo kutotia saini mkataba wa kuendelea kuweko kwa ofisi hiyo nchini humo. Hatimaye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ametimiza ahadi yake ya kuunda Bodi ya Umoja wa Mataifa ya Ushauri wa Kisayansi wakati huu ambapo teknolojia ya Akili Mnemba au ‘Artificial Intelligence’ imeshaanza kugonganisha vichwa vya watu kuhusu nafasi yake katika maendeleo duniani.Katika makala Naibu Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Amina J. Mohammed akiwa ziarani nchini Brazil amewahakikishia watu wa jamii ya asili ya Mapuera kwenye jimbo la Pará nchini humo kwamba amesikia kilio chao na zaidi ya yote Umoja wa Mataifa utahakikisha sauti zao zinasikilizwa kwani wanachodai ni haki zao za msingi.Na katika mashinani na ikiwa tunaelekea siku ya vijana duniani nampisha tutasikia ujumbe wa kijana Najma Mohamed kutoka Tanzania ambaye ni bingwa wa haki za watoto kupitia Shirika la Umoja wa Mataifa wa Kuhudumia watoto UNICEF.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/4/20230
Episode Artwork

António Guterres aunda Bodi ya Ushauri wa Kisayansi

Hatimaye Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres ametimiza ahadi yake ya kuunda Bodi ya Umoja wa Mataifa ya Ushauri wa Kisayansi wakati huu ambapo teknolojia ya Akili Mnemba au ‘Artificial Intelligence’ imeshaanza kugonganisha vichwa vya watu kuhusu nafasi yake katika maendeleo duniani. Kwa mujibu wa Katibu Mkuu Guterres Bodi hii mpya aliyoiunda ni kwa ajili ya kuwashauri viongozi wa Umoja wa Mataifa kuhusu mafanikio katika sayansi na teknolojia na jinsi ya kutumia manufaa ya maendeleo haya na kupunguza hatari zinazoweza kutokea. Bwana Guterres anaamini maendeleo ya kisayansi na kiteknolojia yanaweza kuunga mkono juhudi za kufikia Malengo ya Maendeleo Endelevu  lakini pia yanaleta wasiwasi wa kimaadili, kisheria na kisiasa, wasiwasi ambao unahitaji ufumbuzi wa kimataifa.  Bodi ya Umoja wa Mataifa ya Ushauri wa Kisayansi ambayo Bwana Guterres anaamini pia kuwa itaimarisha jukumu la Umoja wa Mataifa kama chanzo cha kuaminika cha data na ushahidi wa kisayansi itajumuisha kundi la Maprofesa wanasayansi saba mashuhuri duniani. Maprofesa hao ni Profesa Yoshua Bengio, Profesa Sandra Díaz, Profesa Saleemul Huq, Profesa Fei-Fei Li, Profesa Alan Lightman, Profesa Thuli Madonsela, na Profesa Thomas C. Südhof. Pia kundi jingine ni Wanasayansi Wakuu wa mashirika tofauti ya Umoja wa Mataifa, Mkuu wa Chuo Kikuu cha Umoja wa Mataifa, na Mjumbe wa Katibu Mkuu kuhusu Teknolojia. Mmoja wa wanaounda Bodi hiyo, Profesa Yoshua Bengio, Mkurugenzi wa Kisayansi wa Taasisi ya Mila - Quebec AI ambaye pia ni Mkufunzi katika Chuo Kikuu cha Montréal anatoa ahadi akisema, “Uamuzi wa Katibu Mkuu wa kuanzisha Bodi ya Ushauri wa Kisayansi unasisitiza kujitolea bila kuyumba kwa viongozi wa Umoja wa Mataifa kwa kanuni za mbinu za kisayansi. Ninatazamia kumuunga mkono Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa katika kupaza sauti kwa ajili ya sera zinazotegemea sayansi na kufanya uamuzi.”  Kupitia juhudi zao za ushirikiano, Bodi na Mtandao wake utawaunga mkono viongozi wa Umoja wa Mataifa katika kutazamia, kuzoea, na kutumia maendeleo ya hivi karibuni ya kisayansi katika kazi yao kwa watu, sayari na ustawi. Bodi itafanya kazi kama kitovu cha mtandao wa mitandao ya kisayansi. Lengo ni kuwa na muunganiko bora kati ya jumuiya ya kisayansi na kufanya uamuzi katika Umoja wa Mataifa. Kwa upande wake Bi. Ismahane Elouafi, Mwanasayansi Mkuu katika Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo anasema, "Kwa kuhakikisha kwamba sera na programu za Umoja wa Mataifa zimeanzishwa kwa msingi wa ushahidi na utaalamu bora wa kisayansi uliopo, Bodi itachukua jukumu muhimu katika kutatua matatizo changamano ya kimaadili, kijamii na kisiasa yanayowasilishwa na maendeleo ya haraka ya kisayansi na kiteknolojia."  Ikumbukwe mwezi Julai mwaka huu, kwa mara ya kwanza Baraza la Usalama lilikuwa na mjadala mahususi kuhusu Akili Mnemba na mstakabali wake katika amani na usalama duniani na kabla yake, Katibu Mkuu Antonio Guterres kupitia moja ya matamko yake ya kisera ya Ajenda Yetu ya Pamoja, alitoa ahadi ambayo imetimia kwa kuunda Bodi hii ya kumshauri katika masuala ya kisayansi.  
8/4/20230
Episode Artwork

03 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina na tunakupeleka nchini DRC ambako MONUSCO, ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kulinda amani nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, DRC uko kwenye mchakato wa kuondoka nchini humo na kukabidhi jukumu la ulinzi na usalama kwa serikali. Pia tunakuletea habari kwa ufupi kutoka UNITAMS, FAO na nchini Haiti. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili na nitakupeleka kwake Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili Zanzibar, BAKIZA nchini Tanzania, salía papo hapo tafadhali!  Ujumbe wa Umoja wa Mataifa wa kusimamia kipindi cha mpito nchini Sudan, (UNITAMS) umesema una wasiwasi mkubwa kuhusu athari kubwa kwa raia katika eneo la Darfur kutokana na mapigano kati ya Vikosi vya Msaada wa Haraka (RSF) vinavyoungwa mkono na wanamgambo wa Kiarabu dhidi ya Vikosi vya Wanajeshi wa Sudan (SAF). Ripoti zinaonesha kuwa raia wanazuiwa kuondoka kwenda maeneo salama.Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo (FAO) limetahadharisha kuhusu kuongezeka kwa janga la chakula nchini Sudan. Kulingana na tathimini ya hivi karibuni ya hali ya uhakika wa chakula (IPC), zaidi ya watu milioni 20.3, wanaowakilisha zaidi ya asilimia 42 ya watu wote nchini humo wanakabiliwa na viwango vya juu vya uhaba wa chakula (IPC ngazi ya 3 au zaidi) kati ya Julai na Septemba mwaka huu 2023.Mtaalamu Maalumu wa Umoja wa Mataifa kuhusu uhuru wa majaji na wanasheria Margaret Satterthwaite leo ameelezea wasiwasi wake mkubwa kuhusu shambulio la kikatili lililomlenga Jaji wa nchini Haiti Haiti Wilner Morin, ambaye gari lake lilipigwa risasi katika mji mkuu wa Port-au-Prince miezi michache iliyopita. Morin ni jaji wa Mahakama ya Mwanzo ya Port-au-Prince, ambaye anachunguza kesi kadhaa za ufisadi zenye hadhi ya juu.Na katika kujifunza lugha ya Kiswahili nampisha Dkt. Mwanahija Ally Juma Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA akitufafanualia maana ya neno “NDEKWA”.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/3/20230
Episode Artwork

Jifunze Lugha ya Kiswahili: Neno "NDEKWA"

Katika kujifunza lugha ya Kiswahili leo Dkt. Mwanahija Ally Juma, Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA anatufafanualia maana ya neno “NDEKWA”.
8/3/20230
Episode Artwork

Maji ya kisima hiki ni jawabu kwa afya na kipato – Mwananchi Sudan Kusini

Kwa siku tatu, viongozi wakuu wa mashirika ya Umoja wa Mataifa, lile la Mpango wa Chakula (WFP), Chakula na Kilimo (FAO) na Mfuko wa Maendeleo ya Kilimo duniani, IFAD walikuwemo nchini Sudan Kusini kuona ni kwa jinsi gani miradi wanayotekeleza kwa pamoja ya kujenga mnepo na kuhakikisha lishe ya uhakika na bora imeleta mabadiliko. Wakazi wa Apada Boma jimboni Bahr el Ghazal Kaskazini nchini humo walikuwa taswira ya manufaa ya miradi hiyo ambayo wakuu hao walikagua kama inavyofafanua Makala hii iliyoandaliwa na Assumpta Massoi. 
8/2/20230
Episode Artwork

02 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia hali ya usalama nchini Sudan Kusini na mradi wa maji nchini Rwanda. Makala tunasalia huko huko Sudan Kusini na Mashinani tunakupeleka nchini Zimbabwe, kulikoni?  Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ambaye pia ni Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS), Nicholas Haysom ametahadharisha kwamba muda unazidi kuyoyoma kuelekea Sudan Kusini kufanya uchaguzi mkuu unaotarajiwa mwezi Desemba mwaka ujao wa 2024 lakini bado masuala muhimu ya kuufanya uchaguzi huo uende kama ulivyopangwa bila kuchelewa hayajakamilika.Balozi mwema wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto UNICEF Vanessa Nakate amefanya ziara nchini Rwanda kujionea namna mradi wa pampu ya kuvutia maji inayotumia nishati ya umeme wa jua au Sola ilivyoleta manufaa kwa wanawake na wasichana barubaru 11,000 waliokuwa wakitembea umbali mrefu kusaka hmaji.Katika makala Assumpta Massoi anafuatilia ziara ya wakuu wa mashirika matatu ya Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini.Na tunakupeleka nchini Zimbabwe ambako vijana wameweza sio tu kijikwamua kiuchumi na kuondokana na umaskini bali pia kuhifadhi mazingira na tutasikia kutoka kwa mmoja wao.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/2/20230
Episode Artwork

Nicholas Haysom: Hatua inahitajika sasa kwa ajili ya uchaguzi kwa wakati na wa huru na haki nchini Sudan Kusini

Mwakilishi Maalum wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa ambaye pia ni Mkuu wa Ujumbe wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini (UNMISS), Nicholas Haysom ametahadharisha kwamba muda unazidi kuyoyoma kuelekea Sudan Kusini kufanya uchaguzi mkuu unaotarajiwa mwezi Desemba mwaka ujao wa 2024 lakini bado masuala muhimu ya kuufanya uchaguzi huo uende kama ulivyopangwa bila kuchelewa hayajakamilika."Ikiwa imesalia miezi 17 tu kwenye ratiba ya kuelekea uchaguzi wa mwaka 2024, narudia kile nilichokisema katika mkutano wa awali na waandishi wa habari, kwamba mwaka 2023 ni mwaka wa 'kutengeneza au kuvunja'," amesema Bwana Haysom mapema leo Agosti pili alipozungumza na vyombo vya Habari mjini Juba ambao ni mji mkuu wa nchi hiyo changa zaidi duniani.    Ghasia miongoni mwa jamii za Sudan Kusini zinaendelea kuongezeka pamoja na shinikizo la kuongezeka kwa ufinyu wa rasilimali huku maelfu ya watu wakiendelea kuingia nchini humo wakikimbia mapigano katika nchi jirani ya Sudan.  Kwa mujibu wa Bwana Haysom, miongoni mwa hatua muhimu ambazo inabidi zichukuliwe ni pamoja na hitaji la kuunda upya vyombo vitatu muhimu, ambavyo ni, Tume ya Kitaifa ya Marekebisho ya Katiba, Tume ya Kitaifa ya Uchaguzi, na Baraza la Vyama vya Kisiasa; kukamilisha mipango ya mpito ya usalama; kuendeleza mchakato wa kudumu wa kutengeneza katiba; na kuunda nafasi za kiraia na kisiasa ambapo kila raia ana uhuru wa kujadili na kujihusisha na uchaguzi wa kisiasa na kikatiba bila woga.  "Kufanya uchaguzi tu hakutoshi - uaminifu, uwazi na ushirikishwaji wa mchakato ndio unaoleta uhalali. Hii ni pamoja na kwamba vyama vya siasa lazima viweze kujiandikisha na kufanya kampeni kwa uhuru; asasi ya kiraia kwa ajili ya elimu ya uraia na kuwa waangalizi wa mchakato. Inajumuisha vyombo vya habari vinavyoweza kuripoti kuhusu mchakato huo na kutoa nafasi kwa sauti na maoni mbalimbali kwa wapiga kura kufanya uamuzi sahihi,” amesema Mwakilishi huyo wa Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa nchini Sudan Kusini.  Aidha Bwana Haysom amesisitiza kuwa UNMISS itaendelea kuiunga mkono Sudan Kusini katika michakato ya uchaguzi na uundaji wa katiba kwa kushirikiana na wadau wa kikanda kama vile Muungano wa Afrika (AU) na mamlaka ya pamoja ya kitaifa kwa ajili ya maendeleo kwenye eneo la Pembe ya Afrika (IGAD).  
8/2/20230
Episode Artwork

Vanessa Nakate: Matumizi ya nishati safi yanasaidia wasichana kusalia shuleni

Balozi mwema wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohudumia watoto UNICEF Vanessa Nakate amefanya ziara nchini Rwanda kujionea namna mradi wa pampu ya kuvutia maji inayotumia nishati ya umeme wa jua au Sola ilivyoleta manufaa kwa wanawake na wasichana barubaru 11,000 waliokuwa wakitembea umbali mrefu kusaka hmaji. Ni Vanessa Nakate Balozi mwema wa UNICEF, raia wa Uganda ambaye pia ni mwanaharakati wa mabadiliko ya tabianchi akiwa Nyagashankara nchini Rwanda alikokwenda kutembelea mradi wa maji ambao hapo awali ulikuwa ukitumia mafuta ya diseli lakini saa unatumia nishati safi ya Sola. Akiwa kijijini hapo Vanessa alikutana na mabinti wawili Adele na Graciela ambao kabla ya mradi huu walikuwa wakitembea umbali mrefu kusaka maji …… na anaeleza kuwa,  “Ilikuwa hatari kwao, tunajua kuwa kwa uwiano, wasichana na wanawake wanaathirika pakubwa na majanga ya tabianchi, kwa hiyo ni muhimu sana kuelewa kuwa tunavyopamba kupata haki kutokana na athari za mabadilko ya tabianchi ni kuwa pia tunapambana kwa haki ya kijinsia.”Vanessa anaikumbusha jamii kuwa wasichana hawana changamoto moja tu ndani ya jamii, utakuja binti ambaye anaathirika na mabadiliko ya tabianchi, huyo huyo anaweza kuacha shule au kukosa masomo hivyo kuleta majawabu mtambuka kunasaidia kutatua changamoto nyingi ndani ya jamii. “Kuwa na mashine ya kuvuta maji inayotumia umeme wa Sola ambao unawarahisishia kupata maji sio tu unasaidia kuhakikisha wasichana wanasalia shuleni lakini pia inawasaidia kuwa na maono ya dunia bora zaidi. “Vanessa anahitimisha kwa kueleza kuwa ili kuhakikisha wanajamii wengi zaidi wananufaika na miradi kama hii ya maji lazima kuwepo na miradi mingi kama hii na hilo litawezekana iwapo watapata uwezeshaji wa kifedha na rasilimani nyingine nah apo wasichana wengi watakuwa wamehakikishiwa kuendelea kusalia shuleni. 
8/2/20230
Episode Artwork

01 AGOSTI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo mradi wa serikali ya DRC na UN Women wajengea uwezo wajasiriamali Goma. Pia tunakuletea habari kwa ufupi kutoka IFAD, FAO, WHO na UNICEF ikiwa ni pamoja na Tamko la Haki za binadamu. Mashinani tunakupeleka nchini Sudan, kulikoni? Ikiwa leo ni mwanzo wa Wiki ya Kimataifa ya Unyonyeshaji Maziwa ya Mama kwa mtoto, kaulimbiu ikiwa, "Tufanye unyonyeshaji kazini, ufanye kazi" Mashirika ya Umoja wa Mataifa la kuhudumia Watoto (UNICEF) na la Afya Ulimwenginu (WHO) wanasisitiza haja ya usaidizi mkubwa wa unyonyeshaji katika sehemu zote za kazi ili kuendeleza na kuboresha maendeleo katika viwango vya unyonyeshaji duniani kote huku ushauri wao ukijumuisha likizo ya uzazi yenye malipo ikiwezekana kwa muda wa miezi sita au zaidi baada ya kujifungua.Wakuu wa mashirika matatu ya Umoja wa Mataifa, lile la Chakula na Kilimo (FAO), Mfuko wa Kimataifa wa Maendeleo ya Kilimo (IFAD) na la Mpango wa Chakula Duniani (WFP) wameonya leo walipokuwa wakihitimisha ziara ya siku tatu nchini Sudan Kusini kuwa madhara ya kutochukua hatua katika kushughulikia majanga tata ya chakula, tabianchi na ukosefu wa usalama nchini humo yatajitokeza katika kupoteza maisha, ustawi na mustakabali wa mamilioni ya watu katika taifa hilo changa duniani.Na tukiendelea na ufafanuzi wa tamko la haki za binadamu la Umoja wa Mataifa ambalo mwaka huu linatimiza miaka 75, Mwanasheria wa Haki za Binadamu nchini Tanzania, Wakili Jebra Kambole anafafanua ibara ya 6 ya tamko hilo.Na mashinani tutamsikia Mkuu wa Operesheni wa Shirika la Umoja wa Mataifa linalohusika na masuala ya kibinadamu pamoja na kuratibu masuala ya dharura OCHA aliyetembelea kambi za wakimbizi wa ndani nchini Sudan.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
8/1/20230
Episode Artwork

Je unafahamu kuwa kuna fursa ya ufadhili katika nishati safi na salama Tanzania?

Kwa mujibu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la mfuko wa maendeleo ya mitaji UNCDF wakizingatia Utafiti wa Bajeti ya Kaya Tanzania Bara (2017/18), upatikanaji wa nishati safi na teknolojia ya kupikia ni asilimia 17.1 tu ya wakazi wa mijini na asilimia 2 ya wakazi wa vijijini. Kuongezeka kwa mahitaji ya nishati ya kuni kunatokana na ukuaji wa haraka wa miji, bei ya juu, na upatikanaji mdogo wa nishati mbadala. Ili kuondokana na changamoto hizi, Programu ya CookFund ambayo inatekelezwa chini ya UNCDF kwa kushirikiana na Wizara ya Nishati nchini Tanzania, ina nia kuongeza idadi ya watu kwa kutumia suluhu endelevu za nishati safi ya kupikia katika maeneo ya mijini. Tayari awamu ya kwanza ya ufadhili imeenda kwa makampuni 16 kama anavyosimulia Anold Kayanda katika makala hii. 
7/31/20230
Episode Artwork

Sera za MPOWER zaepusha watu kuvutishwa sigara bila ridhaa yao- WHO

Miaka 15 baada ya Shirika la Umoja wa Mataifa la afya duniani, WHO kuanzisha sera ya kulinda umma kutoathirika na uvutaji wa sigara unaofanywa na mtu mwingine, zaidi ya watu bilioni 5.6 wamenufaika na sera hiyo ulimwenguni kote, imesema ripoti mpya ya shirika hilo iliyotolewa leo. Tupate taarifa zaidi kutoka kwa Assumpta Massoi. Idadi hiyo ni sawa na kusema kuwa asilimia 71 ya watu ulimwengu kose sasa wamelindwa na athari ambazo wangeweza kuzipata kutokana na mtu mwingine kuvuta sigara karibu yake. Na iwapo kusingekuwa na sera hizo zaidi ya watu milioni 300 wangekuwa wametumbukia katika uvutaji moshi wa sigara bila wao kuvuta wenyewe.  Akizindua ripoti hiyo ya  9  ya janga la uvutaji tumbaku ulimwengu hii leo jijini Geneva Uswisi, Mkurugenzi Mkuu wa WHO Dkt. Tedros Ghebreyesus amesema mikakati 6 iliyopendekezwa kuwa sera imeanza kuleta mafanikio ambapo watu 7 kati ya 10 ulimwenguni wanalindwa na angalau Sera moja.  Dkt. Tedros amesema “takwimu hizi zinaonesha japo ni polepole lakini kwa hakika, watu wengi zaidi wanalindwa dhidi ya madhara ya tumbaku kwa kutumia sera za utendaji bora za WHO zilizotungwa kwa msingi wa ushahidi.”  Sera hizo ziitwazo MPOWER zinataka serikali kuweka mikakati sita ya kudhibiti tumbaku ambayo ni  Mosi; Fuatilia sera za matumizi na uzuiaji wa tumbaku, Pili; kuweka kinga ya kulinda watu dhidi ya moshi wa tumbaku, Tatu; kutoa usaidizi wa wale wanaotaka kuacha matumizi ya tumbaku; Nne,kuelimisha watu kuhusu hatari za tumbaku, Tano; kuweka marufuku ya utangazaji, ukuzaji na udhamini wa bidhaa za tumbaku na sita; kuongeza ushuru kwa bidhaa za tumbaku. Nchi za Brazil na Uturuki zilifanikiwa kutekeleza sera hizo kwa viwango vya juu na leo Mkuu huyo wa WHO amezipongeza nchi ya Mauritius kwa kuwa nchi ya kwanza barani Afrika, na Uholanzi kwa kuwa ya kwanza katika Muungano wa Ulaya kutekeleza mpango kamili wa sera hizo za kudhibiti matumizi ya tumbaku.  WHO pia imeeleza ipo tayari kuunga mkono nchi zote kufuata mfano wao na kuwalinda watu wao kutokana na janga hili baya. 
7/31/20230
Episode Artwork

Mradi wa "Njoo shuleni" nchini Kenya warejesha matumaini kwa familia

Elimu ni moja ya nyenzo zenye nguvu zaidi za kuleta mabadiliko kwa watu binafsi na jamii na ndio maana katika miongo miwili iliyopita, serikali ya Kenya imefanya mageuzi mengi ili elimu ya msingi iwe bure na ya lazima kwa watoto wote walio katika umri wa kwenda shule. Hata hivyo, watoto wengi bado hawako shuleni kutokana na umaskini, miundombinu duni, kutelekezwa na wazazi na matatizo ya kiafya hasa katika maeneo masikini. Sasa shirika la Umoja la kuhudumia watoto UNICEF limeamua kuingilia kati kwa kushirikiana na wadau kusaidia. Flora Nducha na maelezo zaidi.Katika Kaunti ya Dandora jijini Nairobi ambako wakazi wengi ni walala hoi, watoto kwenda shule ni mtihani unaoanzia kwa wazazi kama Wambui Kahiga mama wa Octavia mtoto mwenye umri wa miaka 10.Wambui anasema, “shida zangu kubwa sasa hivi ni chakula, mavazi , kulipa gharama za shule na ghara za kulipia nyumba. Kibarua ninachopata wakati huu ni cha kufua nguo na hakiaminiki kuna wakati napata na kuna wakati nakosa. Najihisi vibaya kwani ingekuwa mapenzi yangu , Octavia angekuwa alianza shule kitambo.”Kwa mujibu wa UNICEF umasikini ndio sababu kubwa inayowafanya wazazi kushindwa kuwapeleka watoto shule na sasa shirika hilo linashirikiana na wakfu wa Elimisha mtoto (EAC) na wanaendesha programu ya elimu zaidi ya yote kupitia mradi wa “Njoo shuleni” ili kuwafikia watoto wote kama Octavia na kuhakikisha wanapata haki ya elimu.Elizabeth Waitha ni afisa elimu wa UNICEF Kenya anasema “mara tunapobaini watoto ambao hawana fursa ya elimu, tunawasajili na tunaweza kuwasaidia na vifaa vya shule ambavyo vinapunguza mzigo kwa wazazi kuweza kuwasaidia watoto wao kwa ajili ya kusoma”.Na hii inaleta faja na matumaini kwa watoto na wazazi kama kwa mama wa Octavia akisema, “Octavia yuko shuleni , na sasa ambavyo anasoma naona maisha yake yatabadilika , yatakuwa maziri hata mimi atakuja kuniinua.”Kwa UNICEF “Elimu ni haki ya msingi ya binadamu na kila mtoto anapaswa na anahitaji fursa ya kupata elimu na uelimishaji mkubwa unahitajika kuhakikisha kwamba kila mtoto anasoma.”Kulingana na takwimu za Educate A Child (EAC) kuna watoto milioni 1.3 wa umri wa kati ya miaka 6 hadi 13 ambao hawasomi nchini Kenya.Mradi huu unafadhiliwa na mfuko kwa ajili ya maendeleo wa serikali ya Qatar na unatekelezwa katika kaunti 16 nchini Kenya ambazo ni Baringo, Bungoma, Garissa, Isiolo, Kajiado, Kilifi, Kwale, Mandera, Marsabit, Narok, Samburu, Tana River, Turkana, Wajir, West Pokot, na katika makazi yasiyo rasmi ya jijini Nairobi.
7/31/20230
Episode Artwork

31 JULAI 2023

Hii leo jaridani mwenyeji wako ni Leah Mushi akimulika masuala ya afya hususan mafanikio ya será za kudhibiti uvutaji sigara na tumbaku; elimu kwa watoto waliokosa fursa huko Kenya; nishati salama nchini Tanzania na ujumbe wa Romeo George mwanaharakati wa SDGs.Miaka 15 baada ya Shirika la Umoja wa Mataifa la afya duniani, WHO kuanzisha sera ya kulinda umma kutoathirika na uvutaji wa sigara unaofanywa na mtu mwingine, zaidi ya watu bilioni 5.6 wamenufaika na sera hiyo ulimwenguni kote, imesema ripoti mpya ya shirika hilo iliyotolewa leo.Nchini Kenya, UNICEF na wadau wameibuka na mradi wa kusaidia watoto waliokosa fursa ya elimu kurejea tena shuleni.Makala: Mradi wa COOKFUND unaoendeshwa na shirika la Umoja wa Mataifa la mfuko wa mitaji ya maendeleo, UNCDF nchini Tanzania wasongesha nishati safi na salama.Mashinani: Romeo George ajulikanye kama RJ, Mwigizaji na mwanaharakati wa malengo ya maendeleo endelevu nchini Tanzania anayehudumu chini ya Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi, UNHCR akitaka wakimbizi wapatiwe fursa sawa katika ufanikishwaji wa malengo hayo.
7/31/20230
Episode Artwork

Kutoka Dodoma Tanzania Bara hadi Paje, Zanzibar kukabiliana na  umaskini

Moja ya malengo ya Umoja wa Mataifa kuhusu maendeleo endelevu, SDGs ni kutokomeza umaskini ifikapo mwaka 2030. Ikiwa imesalia miaka 7 kabla ya kufikia ukomo, nchi, jamii na kila mtu mmoja mmoja anachukua hatua kutokomeza umaskini hasa kuanzia ngazi ya familia. Umaskini unasababisha watu washindwe sio tu kupata mlo bali pia kupeleka watoto wao shuleni kupata elimu bora. Nchini Tanzania,  hususan visiwani Zanzibar katika mkoa wa Kusini Unguja Assumpta Massoi katika pita ya hapa na pale alikutana na mwananchi mmoja ambaye ameamua kuvuka baharí ya Hindi kutoka Bara  hadi visiwani kukabiliana na umaskini. Ungana naye basi Assumpta Massoi katika makala hii. 
7/28/20230
Episode Artwork

Hali si swari Burkina Faso msirejeshe wakimbizi wake: UNHCR

Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR, leo limetoa mwongozo mpya juu ya ulinzi wa watu wanaokimbia Burkina Faso, na wito wa haraka kwa mataifa yote kuacha kuwarudisha kwa nguvu watu wote wanaotoka katika ukanda huo ulioathiriwa zaidi na mgogoro unaoendelea nchini humo na badala yake kuwaruhusu raia wanaokimbia Burkina Faso kuingia katika mipaka yao. Huku hali ya usalama nchini Burkina Faso ikiendelea kuzorota, UNHCR imesema ina wasiwasi mkubwa kutokana na kuenea kwa hali ya ukosefu wa usalama na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu unaofanywa dhidi ya raia.Ukwiukwaji huo ni pamoja na mauaji, kutoweshwa kwa lazima, mateso na utekaji nyara. Akizungumza na waandishi wa habari mjini Geneva uswis hii leo Elizabeth Tan, mkurugenzi wa ulinzi wa kimataifa wa UNHCR amesema: “Katika matukio kadhaa, raia wamekuwa wakilengwa na kuuawa, na hivyo kusababisha vifo vingi vya raia na watu kutawanywa. Watoto pia wanakabiliwa na ukiukwaji mkubwa wa haki za binadamu, kama vile kuajiriwa kwa nguvu vitani na makundi yenye silaha, ajira ya watoto, pamoja na aina nyingine za unyanyasaji, ukatili, unyonyaji na unyanyasaji wa kijinsia."Ameongeza kuwa asilimia kubwa ya watu wanaotawanywa ni watoto, shule nyingi zimelazimika kufungwa na takriban asilimia 82 ya wasichana wanakabiliwa na ukatili wa kijinsia, lakini pia mamilioni wanahitaji msaada.Anasema "Takriban watu milioni 4.7 kote nchini wanahitaji msaada wa kibinadamu, na ikiwa ni zaidi ya asilimia 20 ya wakazi wote wa nchi hiyo."Kwa mujibu wa UNHCR vita na machafuko pia vimesambaratisha mioundombinu na kuathiri huduma za serikali na taasisi ikiwemo katika maeneo yaliyoathirika na vita na hali ni mbayá zaidi kwa watu wanaoishi katika miji ambayo makundi yenye itikadi Kali yanazuia watu ikiwemo idadi kubwa ya wakimbizi wa ndani.Hadi kufikia Juni mwaka huu wa 2023, zaidi ya watu 67,000 kutoka Burkina Faso wamesaka hifadhi katika nchi jirani kama vile Mali, Niger, Ivory Coast, Togo, Benin na Ghana, huku zaidi ya watu milioni 2 wakiwa wakimbizi wa ndani katika nchi yao, na kuufanya mzozo huo kuwa moja ya mizozo mibaya zaidi yawakimbizi wa ndani katika bara la Afrika.
7/28/20230
Episode Artwork

28 JULAI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia afya na hali ya usalama na msaada wa kibinadamu nchini Burkina Faso. Makala tnamulika harakati za kufanikisha SDGs na mashinani tunakupeleka nchini Kenya, kulikoni? Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi UNHCR, leo limetoa mwongozo mpya juu ya ulinzi wa watu wanaokimbia Burkina Faso, na wito wa haraka kwa mataifa yote kuacha kuwarudisha kwa nguvu watu wote wanaotoka katika ukanda huo ulioathiriwa zaidi na mgogoro unaoendelea nchini humo na badala yake kuwaruhusu raia wanaokimbia Burkina Faso kuingia katika mipaka yao.Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus kupitia ujumbe wake kwa Siku ya Kimataifa ya Homa ya Ini inayoadhimishwa kila Julai 28, amesema kwa kuwa wanadamu tunaishi mara moja na tuna ini moja, WHO imejitolea kushirikiana na nchi zote na wadau wote ili kutimiza maono ya pamoja ya kutokomeza virusi vya homa ya ini ifikapo 2030.Katika makala Assumpta Massoi anaangazia harakati za kufanikisha malengo ya Umoja wa Mataifa ya maendeleo endelevu, SDGs hususan kutokomeza umaskini na kujiinua kiuchumi.Na mashinani tutaelekea kaunti ya Turkana nchini Kenya kusikia ni kwa jinsi gani ukame umeathiri utoaji wa huduma za afya ya uzazi kwa wanawake na wasichana.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
7/28/20230
Episode Artwork

Dkt. Tedros - Tunaishi mara moja na tuna ini moja, tutokomeze Homa ya Ini

Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya Ulimwenguni (WHO) Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus kupitia ujumbe wake kwa Siku ya Kimataifa ya Homa ya Ini inayoadhimishwa kila Julai 28, amesema kwa kuwa wanadamu tunaishi mara moja na tuna ini moja, WHO imejitolea kushirikiana na nchi zote na wadau wote ili kutimiza maono ya pamoja ya kutokomeza virusi vya homa ya ini ifikapo 2030.  “Kila mwaka, homa ya ini inayosababishwa na virusi inaua zaidi ya watu milioni moja, na zaidi ya watu milioni tatu wapya wanaambukizwa. Tunajua namba hizi ni za chini ya makadirio. Mamilioni ya watu ulimwenguni kote wana homa ya ini ambayo haijatambuliwa na ambayo haijatibiwa. Mara nyingi, ugonjwa huendelea bila kutambuliwa mpaka dalili zinakuwa mbaya.” Hata hivyo Dkt. Tedros anaeleza habari njema akisema, “Sasa tuna zana bora zaidi za kuzuia, kutambua na kutibu homa ya ini. Duniani kote, WHO inaunga mkono nchi kupanua matumizi ya zana hizo, ili kutokomeza homa ya ini na kuokoa maisha.” Anayoyasema Mkuu huyu wa WHO tayari yameanza kuzaa matunda katika baadhi ya nchi. Mathalani barani Afrika, wizara ya Afya ya Uganda, kwa msaada wa kiufundi kutoka WHO, ilibuni mkakati wa kudhibiti homa ya ini ya B, ikijumuisha uhamasishaji wa umma, upimaji na matibabu nchini kote. Hadi kufikia sasa watu milioni 4 wamefanyiwa uchunguzi wa ugonjwa huo na  zaidi ya asilimia 30 ya watu walioambukizwa homa ya ini ya B wanafahamu hali zao na wanaweza kupata huduma za matibabu ya kina, ikiwa ni pamoja na dawa za bure. Tags: Homa ya Ini, Virusi vya Homa ya Ini, Hepatitis, Dkt. Tedros Adhanom Ghebreyesus, Siku za UN 
7/28/20230
Episode Artwork

27 JULAI 2023

Hii leo jaridani tunakuletea mada kwa kina ambapo Jacqueline Woiso, Mkurugenzi Mwendeshaji wa Multichoice Tanzania anafafanua ni malengo yapi ya Maendeleo Endelevu yaliyoipa Multichoice Tanzania Ushindi wa Tuzo ya UN Global Compact. Pia tunakuletea habari kwa ufupi zikiwemo ripoti ya hali ya hewa, jaribio la kutaka kutwaa madaraka kijeshi nchini Niger na uhifadhi wa bioanuwai barani Afrika. Katika kujifunza lugha ya Kiswahili tunakuletea maana ya neno “NDOFYA". Kufuatia ripoti iliyotolewa leo na Shirika la Umoja wa Mataifa la Hali ya hewa WMO kwa kushirikiana na lile la Kamisheni ya Muungano wa Ulaya ambayo imethibitisha kuwa mwezi huu wa Julai utavunja rekodi ya dunia ya kuwa na joto kali ulimwenguni kote,  Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa Antonio Guterres amesema takwimu hizi mpya ni uthibitisho kuwa ubinadamu umeketi katika kiti cha moto na kwamba lazima hatua zichukuliwe haraka.Tukitoka Marekani tuelekee Geneva Uswisi ambako Kamishna Mkuu wa Haki za Binadamu wa Umoja wa Mataifa Volker Türk ameshtushwa, amehuzunishwa na kulaani vikali jaribio la kutaka kutwaa madaraka kijeshi nchini Niger lililofanyika hapo jana.Na Shirika la Umoja wa Mataifa la Chakula na Kilimo FAO limekaribisha mchango wa zaidi ya dola milioni 27 uliotolewa na Muungano wa Ulaya kwa ajili ya utekelezaji wa miradi ya uhifadhi wa bioanuwai barani Afrika.Na Leo katika kujifunza lugha ya Kiswahili nampisha Dkt. Mwanahija Ally Juma Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA akitufafanualia maana ya neno “NDOFYA".Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
7/27/20230
Episode Artwork

Je wajua maana ya neno "NDOFYA?" - Dkt. Mwanahija Ally Juma

Leo katika kujifunza lugha ya Kiswahili nampisha Dkt. Mwanahija Ally Juma Katibu Mtendaji wa Baraza la Kiswahili la Zanzibar, BAKIZA akitufafanualia maana ya neno “NDOFYA".
7/27/20230
Episode Artwork

Kutana na Timu ya Taifa ya Kandanda ya Wanawake ya Afghanistan - Wakimbizi katika Michezo

“Tunajaribu kuleta michezo na nguvu zake katika mazingira magumu sana ya watu wasiojiweza. Mchezo ni mzuri kwa kuwapa watu matumaini ya siku zijazo.” Anasema Filippo Grandi, Kamishna Mkuu wa Shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi (UNHCR) akirejelea Timu ya mpira wa miguu ya wanawake wakimbizi wanaoishi nchini Australia baada ya kuokoa maisha yao yaliyokuwa hatarini nchini mwao Afghanistan. Anold Kayanda anasimulia zaidi. 
7/26/20230
Episode Artwork

Hospitali Sudan zaomba usaidizi

Vita nchini Sudan ambayo sasa imedumu kwa zaidi ya siku 100 imeshuhudia zaidi ya watu milioni 3 wakiyakimbaia makazi yao kwenda kusaka hifadhi katika miji mingine pamoja na nchi Jirani. Video ya shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu na afya ya uzazi UNFPA inaanza kwa kuonesha chupa cha upasuaji ambako mjamzito amefanyiwa upasuaji na kujifungua salama huko katika mji Port Sudan jimboni Red Sea mashariki mwa nchi ya Sudan.Hapo awali, hospitali hiyo ilikuwa ikipokea wajawazito 300 mpaka 450 wanaojifungua kwa njia ya kawaida na wale wanaohitaji upasuaji walikuwa takriban 300 kwa mwezi. Daktari Randa Osman ni Mkurugenzi Mtendaji wa hospitali hiyo ya Wazazi ya Port Sudan anasema “Idadi ya sasa ni kubwa zaidi kwa sababu ya ongezeko la watu wanaokimbilia katika jimbo hili.” Dokta Randa anaendelea kwa kusema wajawazito na watoto wachanga wanakabiliwa na ufikiaji finyu wa huduma muhimu za afya. “Hospitali hii ya kujifungulia ndio pekee iliyopo katika mji huu na inatoa huduma za dharura za uzazi, uangalizi baada ya kujifungua na upasuaji. Hospitali imekuwa ikipokea idadi kubwa ya wagonjwa na mzigo wa kazi umeongezeka mara mbili. Watendaji wetu wanafanya kazi bila kuchoka kuwahudumia wakimbizi wanaokaa katika makazi ya muda ya wakimbizi.” Daktari huyu anahitimisha kwa kueleza kile wanachohitaji? “Tunahitaji vifaa tiba zaidi kwakuwa idadi ya wagonjwa ni zaidi ya mara mbili. Na pia tunahitaji kuongeza juhudi ili kukabiliana na hitaji hili kubwa linalozidi kuongezeka.”Shirika la Umoja wa Mataifa la idadi ya watu na afya ya uzazi UNFPA linafanya kila juhudi kwa kushirikiana na mashirika mengine ya Umoja wa Mataifa na wadau kuhakikisha wanawasaidia watu wote wenye uhitaji.
7/26/20230
Episode Artwork

UNESCO inasema teknolojia itumike kwa manufaa ya mwanadamu na sio kuwa mbadala wake: Ripoti

Ripoti mpya iliyotolewa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu , sayansi na utamaduni UNESCO kuhusu ufuatiliaji wa teknolojia katika elimu GEM 2023 imetaka mifumo ya elimu kote duniani siku zote kuhakikisha kwamba matakwa ya wanaojifunza yanakuwa katika kitovu cha teknolojia na kwamba teknolojia zitumike kusaidia elimu inayotokana na mwingiliano wa binadamu badala ya kulenga kuwa mbadala wake. Ripoti hiyo mwaka 2023 ya GEM inashughulikia matumizi ya teknolojia katika elimu duniani kote kupitia muktadha wa umuhimu, usawa, uthabiti na uendelevu.UNESCO inasema teknolojia inabadilika haraka kuliko inavyowezekana kutathminiwa na bidhaa za teknolojia ya elimu hubadilika kila baada ya miezi 36, kwa wastani huku ushahidi mkubwa ukitoka katika nchi tajiri zaidi.Mathalani ripoti inasema “Nchini Uingereza, asilimia 7 ya makampuni ya teknolojia ya elimu yalikuwa yamefanya majaribio yaliyodhibitiwa bila mpangilio, na asilimia 12 yalikuwa yametumia uthibitishaji wa watu wengine. Pia utafiti uliofanywa kwa walimu na wasimamizi katika majimbo 17 ya Marekani ulmeonyesha kuwa ni asilimia 11 tu waliomba tathimini ya ushahidi kabla ya kupitishwa.Katika miaka 20 iliyopita, wanafunzi, waelimishaji na taasisi wamepitisha na kukumbatia kwa kiasi kikubwa zana za teknolojia ya kidijitali.Audrey Azoulay, mkurugenzi mkuu wa UNESCO anaonya kwamba  "Mapinduzi ya kidijitali yana uwezo usiopimika lakini, kama vile onyo ambavyo limekuwa likitolewa kuhusu jinsi yanavyopaswa kudhibitiwa katika jamii, tahadhari sawa lazima izingatiwe jinsi mapinduzi hayo yanavyotumiwa katika elimu. Matumizi yake lazima yawe kwa ajili ya uzoefu ulioimarishwa wa kujifunza na kwa ajili ya ustawi wa wanafunzi na walimu, si kwa madhara kwao. Matakwa ya mwanafunzi yawe kipaumbele cha kwanza na yawasaidie walimu. Kuunganishwa mtandaoni sio mbadala wa mwingiliano wa wanadamu.”Azoulay amesisitiza kuwa “Kutumia teknolojia kunaweza kuboresha baadhi ya aina za kujifunza katika baadhi ya miktadha. Ripoti hiyo inataja ushahidi unaoonyesha kuwa manufaa ya kujifunza hutoweka ikiwa teknolojia itatumiwa kupita kiasi au kutokuwepo kwa mwalimu aliyehitimu. Kwa mfano, kusambaza kompyuta kwa wanafunzi hakuboreshi hali ya kujifunza ikiwa walimu hawatahusika katika tajriba ya ufundishaji. Simu za rununu shuleni pia zimeonekana kuwa kero katika kujifunza, lakini ni chini ya robo ya nchi tu ndizo zimepiga marufuku matumizi ya simu hizo shuleni.”Duniani kote ripoti imesema idadi ya watu wanaotumia mtandao wa intaneti imeongezeka kutoka asilimia 16 mwaka 2005 hadi asilimia 66 mwaka 2022.
7/26/20230
Episode Artwork

26 JULAI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia ripoti ya UNESCO kuhusu teknolojia na pia afya ya wanawake wajawazito nchini Sudan. Makala tunakupeleka nchini Australia na mashinani Roma nchini Italia, kulikoni? Ripoti mpya iliyotolewa leo na shirika la Umoja wa Mataifa la elimu , sayansi na utamaduni UNESCO kuhusu ufuatiliaji wa teknolojia katika elimu GEM 2023 imetaka mifumo ya elimu kote duniani siku zote kuhakikisha kwamba matakwa ya wanaojifunza yanakuwa katika kitovu cha teknolojia na kwamba teknolojia zitumike kusaidia elimu inayotokana na mwingiliano wa binadamu badala ya kulenga kuwa mbadala wake.Vita nchini Sudan ambayo sasa imedumu kwa zaidi ya siku 100 imeshuhudia zaidi ya watu milioni 3 wakiyakimbaia makazi yao kwenda kusaka hifadhi katika miji mingine pamoja na nchi Jirani.Makala tunaangazia Timu ya taifa ya mpira wa miguu ya wanawake ambao wako ukimbizini Australia baada ya kuukimbia utawala wa Taliban nchini mwao Afghanistan.Na katika mashinani ikiwa mkutano wa viongozi kuhusu mifumo ya upatikanaji wa chakula unakunja jamvi leo huko Roma nchini Italia tutasikia ujumbe unaotaka jumuiya ya kimataifa kubuni njia mpya za kukabiliana na changamoto za ukosefu wa chakula.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
7/26/20230
Episode Artwork

25 JULAI 2023

Hii leo jaridani mada kwa kina ambapo wakimbizi kutoka nchini Rwanda na Burundi wanaopata hifadhi katika nchi Jirani ya Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo DRC, wamepata matumaini mapya ya maisha baada ya shirika la Umoja wa Mataifa la kuhudumia wakimbizi UNHCR na shirika lisilo la kiserikali ya AIDES kuwawezesha kuanzisha mradi wa kazi za Sanaa ambao unawasidia kujikimu kimaisha pamoja na familia zao. Ashinani tutaelekea Bahari ya Shamu au Red Sea, kulikoni? Hatimaye operesheni kubwa imeanza leo huko Yemen ya kupakua mapipa ya mafuta ghafi kutoka meli ya FSO Safer iliyoanza kuoza kwenda meli ya  Nautica au Yemen katika pwani  ya bahari ya Shamu.Ikiwa leo ni siku ya kimataifa ya kuzuia watu kuzama majini, shirika la Umoja wa MAtaifa la chakula na kilimo, FAO limesema linatumia siku hii kushirikiana na shirika la Umoja wa Mataifa la afya ulimwenguni WHO kuelimisha umma juu ya kuzama majini hasa katika sekta ya uvuvi.Nchini Sudan Kusini, shirika la Umoja wa Mataifa la Idadi ya Watu na Afya ya Uzazi, UNFPA linaendesha semina kuhusu ukatili wa kijinsia na kingono ili kusaidia manusura ambao wanakabiliwa na vitendo hivyo wakati wakirejea nyumbani kutokana na mapigano yanayoendelea nchini Sudan.Mashinani tutamsikia Mkuu wa shirika la Umoja wa Mataifa la Mpango wa Maendeleo, UNEP hatua iliyoanza asubuhi ya leo kwa saa za Yemen ya kuhamisha mafuta yaliyokuwa yanahatarisha usalama kwenye Bahari ya Shamu au Red Sea.Mwenyeji wako ni Leah Mushi, karibu!
7/25/20230
Episode Artwork

WD2023 imeonesha kuwa wanawake tunachukua hatua mashinani - Martha Wanza

Mkutano wa kimataifa wa Women Deliver 2023 (WD2023) au wanawake wanatekeleza umekunja jamvi mwishoni mwa wiki mjini Kigali nchini Rwanda baada ya kuwaleta pamoja washiriki 6,000 ana kwa ana na wengine zaidi ya 200,000 mtandaoni. Lengo kuu la mkutano huo mkubwa kabisa uliozanza Julai 17 hadi 20 na kubeba kaulimbiu “Nafasi, mshikamano na suluhu” lilijikita katika ujumuishwaji ili kusongesha usawa endelevu wa kijinsia kwa kuhusisha sekta mbalimbali. Wadau wakiwemo wakuu wa nchi na serikali na mashirika ya Umoja wa Mataifa likiwemo linalohusika na masuala ya wanawake UN-Women na la idadi ya watu na afya ya uzazi UNFPA walikuwa mstari wa mbele katika mkutano huo Martha Wanza alikuwa miongoni mwa washiriki kutoka Kenya , anafanyakazi na shirika lijulikanalo kama Jumuiya ya wanawake vijana Wakristo nchini humo YWCA. Amezungumza na Eugene Uwimana Afisa uratibu msaidizi wa maendeleo, mawasiliano na mipango katika ofisi ya Mratibu Mkazi wa Umoja wa Mataifa  nchini Rwanda , maswali yake ynarejewa studio na Flora Nducha na Martha akianza kwa kumfafanulia kuhusu shirika lao
7/24/20230
Episode Artwork

Wanawake tuache uoga, tujiamini - Mwanaisha Ulenge

Jukwaa la Umoja wa Mataifa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo ya maendeleo endelevu HLPF limekunja jamvi mwishoni mwa wiki iliyopita kwenye Makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York Marekani baada ya siku 10 za tathimini ya utekelezaji wa malengo hayo au SDGs. Mhandisi Mwanaisha Ulenge ambaye ni Mbunge katika Bunge la Tanzania na pia Mjumbe wa Bunge la Dunia IPU, mmoja wa walioshiriki Jukwaa hilo la Umoja wa Mataifa la Ngazi ya juu la kisiasa kuhusu SDGs, akihojiwa na Anold Kayanda wa Idhaa hii ya Umoja wa Mataifa hapa  jijini New York, Marekani ametoa wito kwa wanawake ulimwenguni kote kwamba wao pia wanapaswa kuwa na mchango katika kuleta usawa wa kijinsia kwanza kwa wao wenyewe kutojiwekea mipaka.  Lakini kwanza Mwanaisha Ulenge anaanza kwa kueleza ushiriki wa wabunge katika jukwaa hili la HLPF akisema, “Kikao hiki ambacho tumeshiriki hapa katika Umoja wa Mataifa (New York, Marekani) ni kikao ambacho kinaangazia namna ambavyo Bunge la Tanzania limeweza kuisimamia serikali katika utekelezaji wa Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs. Ndilo lilikuwa lengo kubwa kama Bunge kuangalia ni namna gani ambavyo serikali imeweza kutekeleza. Kwa hiyo serikali pia wameleta watu wao wamewasilisha lakini na Bunge sisi tumewasilisha namna ambavyo tumeisimamia serikali katika kutekeleza Malengo ya Maendeleo Endelevu ya Dunia.” Na kwa kuwa yeye ni mbunge mwanamke na wakati huo huo bado kuna changamoto kwa wanawake kuzifikia nafasi hizo za kushiriki katika ngazi za maamuzi, Mhandisi Mwanaisha Ulenge ana ujumbe kwa wasichana na wanawake kote ulimwenguni kuhusu mchango wao kufanikisha kuondoa pengo la usawa wa kijinsia. “Hakika usawa wa jinsia ni sehemu ya yale Malengo 17 ya Maendeleo Endelevu.” Anasema Mwanaisha akiongeza, “Kwa hiyo mimi niwaambie wanawake kwamba tuna uwezo sawa wa kuweza kuhudumu na kuweza kufanya makubwa kama jinsia nyingine. Mahali popote pale mwanamke ukiweka dhamira ya dhati kabisa katika kulifanya jambo kwa dhamira kubwa na pana inawezekana.  Anahitimisha kwa kusema, “Tusijiwekee mipaka na wala tusiwe na woga.” 
7/24/20230
Episode Artwork

Guterres ataja mambo matatu ya kufanikisha mifumo bora ya chakula duniani

Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amezungumza kwenye mkutano wa viongozi kuhusu Mifumo ya Upatikanaji wa Chakula huko Roma, Italia hii leo akisema bado inastaajabisha kuwa katika dunia yenye utajiri bado kuna watu hawana chakula au wanakufa njaa, huku akipendekeza mambo makuu matatu ya kuzingatia ili kurekebisha mifumo hiyo. Assumpta Massoi na maelezo zaidiKatika hotuba yake ya kurasa 6, Katibu Mkuu amechambua ni kwa jinsi gani mifumo ya chakula duniani kuanzia shambani hadi mezani imesambaratika na kusababisha zaidi ya watu bilioni tatu wakose mlo wenye lishe, huku zaidi ya bilioni mbili wakiwa matipwatipwa na zaidi ya milioni 780 hawana chakula.Guterres amesema “bila ufadhili na msamaha wa madeni, nchi zinazoendelea zinahaha kuwekeza kwenye mifumo ya chakula itakayowezesha kufikishia wananchi wao lishe wanayohitaji kwa Maisha yenye afya. Kwingineko uzalishaji, ufungishaji na ulaji usio endelevu wa chakula unazidisha  janga la tabianchi na kuzalisha theluthi moja ya hewa chafuzi, unatumia asilimia 70 ya maji na kupoteza bayonuai.”Ameenda mbali kuelezea jinsi hatua ya Urusi kujiondoa kwenye makubaliano ya kusafirisha nafaka na mbolea kupitia Bahari Nyeusi kumesababisha bei za vyakula kupanda na hivyo kuisihi Urusi kurejea kwenye makubaliano hayo.Ameieleza hadhira ya mkutano huo ulioandaliwa na Italia kuwa licha ya changamoto kwenye mifumo ya chakula, kuna nuru katika kuiboresha kwani tayari nchi zinaitikia wito wa mwaka 2021 wa kuboresha mifumo ya chakula.Nchi 100 zimewasilisha ripoti zao za jinsi ambavyo zinatunga sera na kujumuisha katika mipango ya kitaifa hatua za kuimarisha mifumo hiyo.Hata hivyo ili dunia iwe na mifumo bora na endelevu ya kuzalisha na kusambaza chakula na itakayofanikisha malengo ya maendeleo endelevu, SDGs, Katibu Mkuu amependekeza mambo makuu matatu.Mosi; uwekezaji wa kiwango kikubwa kwenye mifumo ya chakula endelevu, yenye uwiano, afya na mnepo. Pili; serikali na sekta binafsi zishirikiane kujenga mifumo ya chakula itakayojali watu badala ya faida na tatu; kuhakikisha mifumo ya chakula haiharibu mazingira ya sayari dunia.
7/24/20230
Episode Artwork

24 JULAI 2023

Hii leo jaridani mwenyeji wako ni Leah Mushi akimulika mkutano wa mifumo ya chakula ulioanza leo Roma, Italia; Kauli ya mshiriki kutoka Tanzania kwenye mkutano uliomalizika hivi karibuni hapa makao makuu ya UN; Makala anabisha hodi Rwanda ilhali mashinani anakupeleka Tunisia.1. Katibu Mkuu wa Umoja wa Mataifa António Guterres amezungumza kwenye mkutano wa viongozi kuhusu Mifumo ya Upatikanaji wa Chakula huko Roma, Italia hii leo akisema bado inastaajabisha kuwa katika dunia yenye utajiri bado kuna watu hawana chakula au wanakufa njaa, huku akipendekeza mambo makuu matatu ya kuzingatia ili kurekebisha mifumo hiyo.2. Mwanaisha Ulenge ambaye ni Mbunge katika Bunge la Tanzania na pia Mjumbe wa Bunge la Dunia IPU, mmoja wa walioshiriki Jukwaa la Umoja wa Mataifa la Ngazi ya juu la kisiasa kuhusu Malengo ya Maendeleo Endelevu, SDGs, lililokamilika wiki iliyopita akihojiwa na Anold Kayanda wa Idhaa hii ya Umoja wa Mataifa hapa jijini New York, Marekani ametoa wito kwa wanawake ulimwenguni kote kwamba wao pia wanapaswa kuwa na mchango katika kuleta usawa wa kijinsia kwanza kwa wao wenyewe kutojiwekea mipaka.3. Makala: Leo inatupeleka mjini Kigali Rwanda ambako mwishoni mwa wiki umekamilika mkutano wa kimataifa wa Women Deliver 2023 (WD2023) au wanawake wanatekeleza. Mkutano ulijikita na suala la ujumuishwaji ili kusongesha usawa endelevu wa kijinsia. Ulihudhuriwa na washiriki zaidi ya 200,000 mtandaoni na ana kwa ana, miongoni mwao ni Martha Wanza kutoka Kenya, anayefanyakazi na shirika la Jumuiya ya wanawake vijana Wakristo nchini humo YWCA.4. Mashinani: Jinsi mkopo na mafunzo kutoka mfuko wa Umoja wa Mataifa wa maendeleo ya kilimo, IFAD umemuinua kiuchumi Hayet Aouida nchini Tunisia.
7/24/20230
Episode Artwork

Asante UNMAS kwa kutegua bomu lililotishia uhai wetu- Wananchi Kididiwe, DRC

Nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo - DRC, Shirika la Umoja wa Mataifa la kutegua Mabomu ya ardhini (UNMAS) Jumanne Julai 18 mwaka huu wa 2023  lilitegua bomu lenye uzito wa kilo 250 lililogunduliwa wiki iliyopita na wakulima katika eneo la Kididiwe, wilayani Beni. Jimboni Kivu Kaskazini. Wakazi wanaonesha furaha yao kwa Umoja wa Mataifa kwa kutegua bomu hilo linalosababisha vifo.  Mwandishi wetu wa nchini DRC, George Musubao amefuatilia na kuandaa makala hii. 
7/21/20230
Episode Artwork

WHO: Nusu ya watu duniani hatarini kuugua Dengue

Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO limesema takriban nusu ya idadi ya watu ulimwenguni hivi sasa wapo hatarini kuungua ugonjwa wa Dengue huku ikikadiriwa kila mwaka watu kati ya milioni 100 mpaka 400 wanapata maambukizi. Dengue ni ugonjwa unaoenezwa na mbu aina ya Aedes. Ugonjwa huo hutokea zaidi katika nchi zenye hali ya hewa ya kitropiki na ya joto. Mkuu wa Kitengo kinachohusika na magonjwa ya Kitropiki yasiyopewa kipaumbele ambaye pia ni mratibu wa mpango wa magonjwa ya Dengue na Arbovirus katika shirika la Afya ulimwenguni WHO Dkt. Raman Velayudhan, akizungumza na waandishi wa habari hii leo jijini Geneva Uswisi amesema ugonjwa huu wa Dengue “Umeongezeka kwa kasi duniani kote katika miongo ya hivi karibuni, huku idadi ya wagonjwa wanaoripotiwa WHO wakiongezeka kutoka nusu milioni mwaka 2000 hadi zaidi ya milioni 4.2 mwaka 2022. Hiyo ni takriban mara 8 zaidi katika miongo miwili.”Ugonjwa wa Dengue, ambao pia huitwa homa ya mfupa, ni maambukizi ya kawaida ya virusi ambayo huenea kutoka kwa mbu hadi kwa binadamu. Watu wengi walio na ugonjwa huu hawana dalili na hupata nafuu baada ya wiki 1 mpaka 2. Hata hivyo Dkt. Velayudhan amesema “Kwa wengine hupata dalili za kawaida ikiwemo homa kali, maumivu ya kichwa, maumivu ya mwili, kichefuchefu na vipele. Iwapo mtu ataugua na kupona na kisha kuugua kwa mara ya pili ana uwezekano mkubwa kupata dalili za dengue kali.”Watu ambao hupata Dengue kali wanahitaji kupatiwa matibabu hospitalini kwani wakichelewa wanaweza kupoteza maisha.Ingawa hakuna matibabu kamili ya ugonjwa huu mpaka sasa , wale wanaogundulika hupatiwa dawa za kupunguza joto na maumivu ya mwili. Watu wanaweza kupunguza hatari ya kupata dengue kwa kuepuka kuumwa na mbu, hasa mchana.Wakati takriban asilimia 70 ya wagonjwa wengi wakiripotiwa kutoka Barani Asia, Ukanda wq Jangwa la Sahara idadi kubwa ya wagonjwa wameripotiwa kutoka nchini Sudan ambapo kulikuwa na wagonjwa 8239 na vifo 45 tangu Julai 2022. Katika wiki za hivi karibuni WHO imepokea ripoti za uwepo wa wagonjwa wa dengue nchini Misri.WHO imezitaka wizara za Afya kuchukua hatua kwani wakati kuna milipuko, dengue inaweza kuchukua rasilimali za thamani kutoka kwenye mfumo wa afya, na kuongeza mzigo zaidi kwa taifa.
7/21/20230
Episode Artwork

21 JULAI 2023

Hii leo jaridani tunaangazia Afya na malengo ya maendeleo endelevu. Makala tunakupeleka nchini DRC na mashinani nchini Rwanda, kulikoni? Shirika la Umoja wa Mataifa la Afya ulimwenguni WHO limesema takriban nusu ya idadi ya watu ulimwenguni hivi sasa wapo hatarini kuungua ugonjwa wa Dengue huku ikikadiriwa kila mwaka watu kati ya milioni 100 mpaka 400 wanapata maambukizi..Jukwaa la Umoja wa Mataifa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo ya maendeleo endelevu HLPF limekunja jamvi jana hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York Marekani baada ya siku 10 za tathimini ya utekelezaji wa malengo hayo au SDGs. Waakilishi wa nchi na serikali, wanazuoni, mashirika ya Umoja wa Mataifa, wanaharakati na vijana ni miongoni mwa waliohudhuria. Kenya haikubaki nyuma katika jukwaa hilo.Makala inatupeleka nchini Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo - DRC, ambapo Shirika la Umoja wa Mataifa la kutegua Mabomu ya ardhini (UNMAS) Jumanne Julai 18 mwaka huu wa 2023 lilitegua bomu lenye uzito wa kilo 250 lililogunduliwa wiki iliyopita na wakulima katika eneo la Kididiwe, wilayani Beni. Jimboni Kivu Kaskazini. Wakazi wanaonesha furaha yao kwa Umoja wa Mataifa kwa kutegua bomu hilo linalosababisha vifo.  .Mashinani tutaelekea nchini Rwanda kusikia ni kwa jinsi gani programu ya remedial ambayo imewafikia watoto zaidi ya 10,000 katika shule 200 na vituo 10 vya vijana imeboresha masomo kwa wanafunzi.Mwenyeji wako ni Assumpta Massoi, karibu!
7/21/20230
Episode Artwork

Susan Mang’eni: Serikali imesikia kilio chenu Wakenya ina mikakati chonde chonde kuweni na subira

Jukwaa la Umoja wa Mataifa la ngazi ya juu la kisiasa kuhusu malengo ya maendeleo endelevu HLPF limekunja jamvi jana hapa Makao makuu ya Umoja wa Mataifa New York Marekani baada ya siku 10 za tathimini ya utekelezaji wa malengo hayo au SDGs. Waakilishi wa nchi na serikali, wanazuoni, mashirika ya Umoja wa Mataifa, wanaharakati na vijana ni miongoni mwa waliohudhuria. Kenya haikubaki nyuma katika jukwaa hilo.  Susan Auma Mang’eni katibu mkuu wa wizara ya ushirika na biashara ndogondogo wa Kenya alibeba bendera yataifa hilo miongoni mwa waliowasilisha tarifa katika mkutano wa vijana kandoni mwa jukwaa hilo amenieleza kuwa  moja ya changamoto kubwa ya utekelezaji wa malengo hayo hasa kwa nchi zinazoendelea kama Kenya ni ufadhili ulioahidiwa na mataifa tajiri ya G20 ambao bado haujatolewa kwa nchi zinazoendelea, “Zikitusaidia sasa tutaweza kuweka mikakati ambayo inatakikana ili tuweze kupunguza hali ngumu ya Maisha na kando ya hapo katika kuangalia masuala ya mabadiliko ya tabianchi tumejitoa ndio maana kuanzia tarehe 4 hadi tarehe 6 mwezi ujao tutakuwa na kongamano kubwa sana la Afrika la kuweza kuangazia mambo ya hatua dhidi ya mabadiliko ya tabianchi tukijiandaa kwenye kwenye kongamano la COP28.”Susan amekiri kwamba changamoto za hali ngumu ya maisha zinazochangiwa na sababu lukuki ikiwemo mabadiliko ya tabia nchi, na vita inayoendelea baina ya Urusi na Ukraine hususa kwa Kenya zimechochea hali ya uchumi hasa mifukoni mwa watu kuwa mbayá zaidi wengi wakishindwa kumudu Maisha ya kila siku na kuzusha maandamano, hata hivyo amesema serikali imesikia kilio chao na inajitahidi kuleta afueni amewasihi Wakenya kuwa na subirá, “Ningependa kuwaambia Wakenya kwamba serikali ina mikakati tulieni, tufanye bidii , tupange pamoja hali itakuwa nzuri, tukiendelea kwenda kufanya maandamano ambayo ni maharibifu katika hiyo hali watu wanapoteza maisha, watu wanaumia hata askari pia wanaumia tuanendelea kufanya hii hali iwe hata ghali kiasi. Ugali hauko barabarani, ugali uko mashambani kwetu , ugali uko kwenye bidii yetu ya biashara ndogondogo. Niwaomba Wakenya kwamba msikubali kupelekwa barabarani bila msimamo kwa sababu hizo changamoto sio za Kenya peke yake.”Mapema wiki hii ofisi ya haki za binadamu ya Umoja wa Mataifa ilitoa tarifa ikisema inatiwa hofu na maandamano yanayoendelea Kenya baada ya watu 23 kuuawa katika maandamano hayo huku ikivisihi vyombo vya ulinzi na usalama kutotumia nguvu kupita kiasi dhidi ya waandamanaji kwani kuandamana ni haki yao ya msingi ya kiraia.
7/21/20230